Sarafina - Mtunzi Nyemo Chilongani

Sarafina - Mtunzi Nyemo Chilongani

SEHEMU YA 18...

Catherine alishangaa lakini ndiyo ulikuwa msimamo wa msichana huyo, hakutaka kutoa mimba na alikuwa tayari kuona akizaa na kumtunza mtoto wake. Wakaondoka na kurudi chuo, huko, maisha yaliendelea, hakuacha kumpigia simu David, mwanaume huyo hakuwa akipokea na wakati mwingine alihisi kama anasumbuliwa na hivyo kuizima simu hiyo.
Sarafina aliendelea kuumia moyoni mwake lakini hakuwa na jinsi. Alipokuwa akimuona Richard alijishtukia, wakati mwingine alikuwa akijificha kwani mwanaume huyo ndiye aliyeonyesha kuwa na shida naye kwa hali na mali japokuwa alionekana kuwa masikini wa kutupwa.
Baada ya miezi kadhaa, kila mtu akajua kwamba alikuwa na mimba, muonekano wake ukawatia hofu wanachuo wote. Uongozi ukamuita na kuzungumza naye, hakubisha, akawaambia kwamba kweli alikuwa na mimba hivyo kufukuzwa chuoni.

Hakuwa na pa kwenda zaidi ya nyumbani kwao. Ingekuwa rahisi kwenda nyumbani kwa kina David kama tu wangekuwa pamoja lakini kwa kuwa alikuwa amekataliwa na mwanaume huyo, hakuwa na jinsi zaidi ya kujipanga kurudi jijini Mwanza.

Ndani ya basi mawazo yake yalikuwa kwa wazazi wake, hakujua wangemfanya nini baada ya kugundua kwamba alikuwa mjauzito. Walitumia kiasi cha fedha kwa ajili yake, walikopa kuhakikisha anapata elimu bora lakini mwisho wa siku alikuwa akiwapelekea mimba nyumbani.

Alipofika Mwanza, kabla ya kwenda nyumbani akatafuta saluni, akatoa blichi na kiduku kisha kujiweka kama msichana wa kawaida asiyekuwa na tatizo lolote lile. Alipofika nyumbani, wazazi wake walishangaa, hakikuwa kipindi cha likizo lakini alikuwa amerudi, alirudi kufanya nini?

“Una mimba?” aliuliza mama yake huku akimwangalia kwa mshtuko, aliligundua hilo baada ya kuona mabadiliko makubwa.
“Ndiyo mama! Naomba unisamehe!” alisema mama yake.

“Yeleuwiiiiiiii….una mimba!” alisema mama yake kwa kupayuka.
Hakuzungumza kitu zaidi ya kupiga kelele, akamwambia kwamba hiyo ilikuwa kesi kubwa na alitakiwa kumsubiri baba yake. Sarafina akabaki akitetemeka, alimfahamu baba yake, alikuwa mwanaume mkorofi ambaye hakuwa na masihara hata kidogo.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 19...

Alibaki nyumbani hapo akilia tu, alimsubiri baba yake, wakati mwingine alijisemea kwamba ilikuwa ni lazima kufukuzwa lakini wakati mwingine aliamini kwamba baba yake asingeweza kumfukuza kwa kuwa alikuwa mtoto wake.
Ilipofika saa kumi na mbili jioni, Mzee Butati akafika nyumbani hapo, kwanza alishangaa kumkuta sarafina, hicho hakikuwa kipindi cha likizo sasa ilikuwaje binti huyo awe nyumbani hapo.

Akamsalimia na kwenda chumbani, huko, mkewe akamwambia kilichokuwa kimetokea.
Maneno hayo yalimtia hasira, hakuamini kama kweli mtoto wake kipenzi, Sarafina alirudi nyumbani hapo akiwa na mimba. Alikumbuka mkopo waliokuwa wakikopa kwa ajili ya msichana huyo, alikumbuka maumivu aliyokuwa akiyapata kufanya kazi ili kulipa mikopo aliyokuwa akichukua kwa ajili ya binti yake, leo hii, pamoja na tabu zote, alirudi nyumbani akiwa na mimba.

“Unasemaje?” alimuuliza mkewe kana kwamba hakujua alichoambiwa.
“Amekuja na mimba. Huyo hapo na tumbo lake,” alisema mkewe.

Mzee Butati akatoka chumbani na kuelekea sebuleni, alionekana kama mbogo, alikuwa na hasira mno, hakutaka kuzungumza kitu chochote kile, akamshika mkono Sarafina na kutoka naye nje kwani aliamini kwamba kama angempiga basi angeweza kusababisha matatizo kwa mtoto.

“Umekuja kufanya nini na mimba yako?” aliuliza Mzee Butati huku akimwangalia sarafina.
“Nisamehe baba!” alisema Sarafina huku akilia kwa uchungu, tayari majirani waliokuwa ndani ya nyumba zao wakatoka nje na kuangalia kilichokuwa kikiendelea.

“Ninasema hivi! Ondoka nyumbani kwangu, sitaki kukuona, yaani kuanzia leo wewe siyo mtoto wangu! Ondoka nyumbani kwanguuuuuu…” alisema Mzee Butati kwa hasira kiasi kwamba mpaka akawa anatetemeka.

Sarafina aliogopa, aliwahi kumuona baba yake akiwa kwenye hasira lakini siku hiyo alionekana kuwa tofauti, alionekana kuwa na hasira kuliko siku zote. Akaondoka huku akilia, katika mfuko wa sketi yake alikuwa na kiasi cha shilini laki moja tu, hakujua maisha yangekuwaje na kiasi hicho cha fedha.

je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 20...

Giza likaanza kuingia, akaondoka nyumbani hapo huku akilia. Wazazi wake walimfukuza, hakuamini kama angeweza kupokelewa na watu wengine, mawazo yaliyomjia kichwani mwake ni kurudi Dar es Salaam.

Usiku wa siku hiyo akachukua chumba gesti na siku iliyofuata akapanda ndani ya basi na kuanza safari ya kurudi Dar. Moyo wake ulikuwa na huzuni kubwa, hakujua ni wapi alitakiwa kuelekea, aliwaza kwenda nyumbani kwa kina david lakini hakuamini kama mwanaume huyo angeweza kumpokea, alijua kabisa kwamba angemfukuza kwa kuwa tayari alimpa hela ya kutoa mimba lakini hakufanya hivyo.

Siku hiyo usiku gari likaingia Ubungo jijini Dar, akateremka na kwenda katika Mtaa wa tandale na kuchukua chumba katika gesti moja na kutulia humo. Usiku mzima hakulala, kichwa chake kilikuwa na mawazo tele, alikuwa na ndoto za kuwa mtu mwenye heshima hapo baadaye lakini ndoto yake hiyo ikafutika kama upepo, mimba aliyokuwa nayo ikayaharibu maisha yake.

Usiku huo ulikuwa mgumu kupata usingizi, alikuwa akiyafikiria maisha yake, aliharibu hivyo ilikuwa ni lazima kufikiria namna ambavyo angeishi na mimba yake mpaka kujifungua salama.
“Nitafanya kila kitu kumtunza mtoto wangu!” alisema.

Asubuhi ilipofika, akatoka ndani ya chumba kile, akaanza kuelekea katika sehemu mbalimbali, hasa migahawa akitafuta kazi. Hakutamani kuishi maisha ya kumtegemea mtu mwingine, alitaka kuishi kwa kujitegemea yeye mwenyewe.
Alizunguka katika migahawa yote Tandale japo apate kazi, hakupata kazi, akaelekea Mwananyamala napo mambo yalikuwa magumu. Siku hiyo ilikuwa ni siku ya kuzunguka kila kona, akakosa kazi, mpaka inafika saa moja usiku, alikuwa amechoka, mfukoni alikuuwa na shilingi elfu kumi na tano tu na hakuwa amekula.

Akaelekea katika mgahawa mmoja na kula, alipomaliza, akaondoka na kuelekea mitaani. Hakuwa na sehemu ya kulala, alipopaona kufaa ilikuwa ni kwenye nyumba moja ya kawaida ambayo ilikuwa na kigiza fulani huku kukiwa na kibaraza, hapo ndipo palionekana kuwa sehemu sahihi ya yeye kulala

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 21...

Akatafuta maboksi, akayakosa hivyo kutafuta viroba vya gunia, akavipata, havikuwa visafi, hakujali, akavitandika na kulala kwani hakuwa na jinsi.
Kutoka katika uzuri wa ajabu,
kupapatikiwa na wanaume wengi mpaka kufikia hatua ya kulala mtaani, tena juu ya viroba ilikuwa ni hatua moja kubwa kushuka chini. Usiku huo akayafikiria maisha yake kwa ujumla, jinsi alivyokuwa akipapatikiwa na wanaume wengi, jinsi alivyokuwa akipendwa kila sehemu.

Mtu ambaye alimjia kichwani mwake mara nyingi hakuwa mwingine bali Richard. Akamfikiria sana mwanaume huyo, jinsi alivyokuwa akimpenda, aliamini kwamba kama angepata mimba ya mwanaume huyo asingeweza kumfukuza japokuwa alikuwa masikini.

Akajuta, akalia sana, akaumia lakini hilo halikuweza kubadilisha maisha yake. Pale alipokuwa, akapata kazi kubwa ya kufukuza mbu waliokuwa wakimuuma, baridi lilimpiga lakini hakujali, akaingia katika maisha ya mitaani, alikuwa na kazi kubwa ya kuendelea kuishi katika maisha hayo. Hakujua angeishi kwa kipindi gani, hakujua kama angeishi mpaka kifo chake, hakuwa na jinsi, alikubaliana na maisha hayo yaliyosababishwa na uzuri wake wa sura na umbo lake matata.

Wakati akiwa na mawazo lukuki, akapitiwa na usingizi, akalala na kuamshwa na adhana iliyokuwa ikiadhiniwa alfajiri, akaamka, hakulala tena, alikaa na ilipofika saa moja asubuhi, akaanza kuzunguka huku na kule kutafuta kazi.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 22...

Hakuchagua kazi, alitaka yoyote ambayo ingeyafanya maisha yake kuwa na afueni. Alizunguka na kuzunguka, mfukoni alikuwa na kumi na moja, alikula na kuendelea kuzungumza, jua likamchoma lakini hakujali, mpaka inafika saa moja usiku, hakupata kazi, akabakiwa na kiasi kidogo zaidi cha fedha na ilipofika majira ya saa tano usiku, akarudi katika nyumba ileile, akaweka viroba vyake na kulala huku akiwa hoi. Kila alipoyatathmini maisha yake ya baadaye, aliiona dhiki kubwa ikimsogelea.

**** Baada ya saa kadhaa ndege ikaanza kuingia katika uwanja wa ndege jijini Mwanza, Richard akateremka na kuanza kuelekea katika jengo la uwanja huo. Hakutaka kuzungumza na mtu yeyote, kitu pekee kilichokuwa kichwani mwake wakati huo kilikuwa ni msichana Sarafina ambaye katika kipindi hicho aliamini kwamba alikuwa nyumbani kwao.

Akatoka ndani ya jengo la uwanja huo, alipofika nje akachukua teksi ambayo ilimpeleka mpaka katika Hoteli ya Tausi na kutulia hapo. Siku hiyo hakutaka kuzunguka, kwa kuwa ilikuwa ni jioni, akafanya mambo mengine huku akipanga siku inayofuatia ndiyo ya kwenda nyumbani kwa kina Sarafina kumuona kwa kuamini kwamba kama angefanya hivyo basi msichana huyo angeweza kukubaliana naye kwamba alikuwa akimpenda kwa moyo wa dhati.

“Hakuniamini! Sasa nitataka aniamini niliposema kwamba ninampenda,” alisema Richard.
Alishindwa kuuficha moyo wake, ulikuwa kwenye mapenzi ya dhati, alimpenda sana Sarafina zaidi ya msichana yeyote yule, hakujali kuhusu mimba aliyokuwa nayo, alichokuwa akikiangalia ni jinsi moyo wake ulivyokuwa ukimpenda.

Usiku huo akalala na ilipofika asubuhi, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kwenda katika Mtaa wa Mabatini kwa lengo la kuonana na Sarafina aliyekuwa ameelekea huko kutokea Dar es Salaam.
Hakuwa akipafahamu lakini kwa kuwa aliulizia sana, akapelekwa mpaka katika mtaa huo na alipoulizia jina la sarafina, ilikuwa rahisi kupelekwa huko. Hakuchukua dakika nyingi akafika, hali aliyoikuta nyumbani hapo haikumvutia kabisa.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 23...

Aliwakuta wazazi wote wawili wakiwa wamekaa nje, kwa jinsi walivyoonekana, walikuwa na hasira kupita kawaida. Hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea mahali hapo, hakujua kama Sarafina alikuwepo ndani au la.

Aliwasalimia na kusimama kiheshima, akawaambia kilichokuwa kimewaleta. Mzee Butati akasimama kwa hasira, akili yake ilimwambia kwamba mwanaume aliyesimama mbele ya macho yao ndiye aliyempa ujauzito binti yao kwani hata lafudhi yake ilisikika kama mtu aliyetokea Dar.

“Wewe ndiye uliyempa mimba binti yangu?” aliuliza mzee Butati huku akionekana kuwa na hasira, palepale alipokaa, akachukua panga lililokuwa pembeni yake.

“Mzee! Nimekuja tuzungumze kwanza!”
“Niambie kama wewe ndiye uliyempa mimba mtoto wangu?” aliuliza mzee Butati kwa hasira, tayari watu waliokuwa pembeni wakasogea kwani hali ilivyoonekana mahali hapo, ilikuwa ni lazima mzee Butati afanye jambo.
Richard aliogopa, alitetemeka, kwa jinsi alivyomwangalia mzee yule, aliziona hasira zake usoni mwake, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka, kwa lile panga alilokuwa nalo mkononi mwake akahisi kabisa kwamba mzee huyo angeweza kumfanyia jambo baya.

Hakukimbia, alitulia huku akimwangalia mzee huyo machoni, alijaribu kumwambia ukweli kwamba yeye hakuhusika, alimfahamu sana Sarafina lakini ukweli ni kwamba hakuwahi kupendwa na msichana huyo mrembo.

Mzee Butati akatulia, akahisi kwamba kijana huyo alikuwa na mambo mengi ya kumwambia hivyo kumpunguza hasira zake na kumruhusu kukaa chini na kusikiliza ni kitu gani kijana huyo alitaka kumwambia.

Richard hakutaka kuficha, alitaka kuwa mkweli kwa kila kitu, alichoamini ni kwamba msichana huyo alikuwa ndani ya nyumba hiyo na kitu ambacho kingemfanya kuwa na amani ni kuwaambia wazee hao ukweli juu ya kile kilichokuwa kimetokea.

Akaanza kuwahadithia kilichokuwa kimetokea jijini Dar. Hakutaka kuwaficha kwa kitu chochote kile, aliwaambia jinsi alivyokuwa na malengo na binti yao, alivyodhamiria kuwa naye na mwisho wa siku kumuoa lakini msichana huyo alikataa.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 24...

Wazazi wa Sarafina walikuwa kimya wakimwangalia Richard, alizungumza kwa kujiamini, aliwaambia wazazi hao jinsi alivyokuwa, alikuwa mtoto wa bilionea mkubwa nchini Tanzania na lengo lake kubwa la kutaka kuwa na Sarafina ni kumzalia watoto, kujenga familia na kumsaidia yeye na familia yake.

Mzee Butati alivyosikia hivyo, akapiga hatua fupifupi kurudi nyuma, akaliweka panga chini kisha kushika mikono yake kichwani. Alichanganyikiwa, alikuwa kwenye umasikini mkubwa sana lakini mwisho wa siku, alimfukuza binti yake, kwa maana hiyo msaada ambao alitakiwa kuupata asingeweza kuupata.

“Mke wangu! Tumefanya makosa,” alisema mzee Butati huku akimwangalia mke wake, uso wake tu ulionyesha kujuta kwa kile alichokuwa amekifanya.
Huo haukuwa muda wa majuto, ulikuwa ni muda wa kukubaliana kwa kile kilichokuwa kimetokea, walimwambia Richard ukweli kwamba walimfukukuza Sarafina siku iliyopita, na mpaka muda huo hawakujua binti huyo alikuwa wapi.

Richard alishangaa, hakuamini kama Tanzania bado kungekuwa na wazazi wenye roho kama hiyo, alinyong’onyea, moyo wake ukaingiwa na hasira, katika vitu ambavyo hakuwa akivipenda ni kuona msichana aliyekuwa akimpenda akipata shida. Hakuzungumza kitu, akaondoka mahali hapo.

Kilichofuata kilikuwa ni kuzunguka kila kona jijini Mwanza, alijua kwamba angebahatika kumuona msichana huyo mjini. Alifanya kazi hiyo ya kuzunguka kwa siku tatu lakini hakufanikiwa, akaamua kurudi jijini Dar ambapo hakukaa sana, baada ya wiki mbili, akaondoka na kuelekea nchini Marekani kusoma katika Chuo cha Mississippi kilichokuwa katika jiji hilohilo.

**** Maisha ya Sarafina hayakubadilika, bado yalikuwa kwenye msoto mkubwa, hakuwa na pa kulala, aliendelea kulala katika vibaraza vya nyumba mbalimbali. Usiku, baridi lilimpiga, mbu walimuuma lakini hakuwa na cha kufanya.
Alikwishakwenda kwa marafiki zake kuomba msaada, kwa Catherine, alifukuzwa kama mbwa, alipomfuata rafiki yake mwingine, Matilda, hakumfungulia mlango, kwa kifupi hakutaka kabisa kuonana naye.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 25...

Mrembo yule, aliyewatikisa wanaume akaanza kufifia, urembo wake aliokuwa akiringia ukaanza kupotea, figa yake kali ikaanza kondoka, Sarafina alilia mno, aliyajutia maisha yake, tamaa ya kupenda pesa leo hii ilimfanya kuishi katika maisha aliyokuwa akiishi.

Mchana wanaume walipokuwa wakimuona walimmendea, walihisi kwamba alikuwa msichana aliyekuwa akiishi nyumba fulani na usiku ulipoingia, walishangaa kumuona akiwa analala mitaani, tena katika vibaraza vya nyumba.

Hawakumuelewa msichana huyo, wanaume hawakutaka kumfuata, alikuwa mzuri lakini kila mmoja alimuogopa kwa kuhisi kwamba alikuwa ofisa wa Usalama wa Taifa ambaye alifika Tandale kwa ajili ya kuchunguza kitu fulani.

Uoga wa wanaume hao ukamfanya kupata nafuu, hakusumbuliwa, hakubakwa, aliendelea kuishi maisha hayohayo huku asubuhi akiamka na kwenda kutafuta kazi ya kuwahudumia wateja katika migahawa mbalimbali.
Baada ya kuzunguka sana, hatimaye akafika katika Baa ya Las vegas iliyokuwa hapohapo Tandale. Alikwenda hapo kwa lengo moja la kutafuta kazi. Hakutamani kuwa mfanyakazi wa baa lakini kwa hatua aliyokuwa amefikia, hakuwa na jinsi, alikuwa radhi kuifanya kazi hiyo na mwisho wa siku apate hela ya kula.

“Hapa kazi ipo! Upo tayari kuuza baa?” aliuliza mwanaume mmoja huku akimwangalia Sarafina kwa macho ya matamanio.
“Nipo tayari mzee wangu!”

“Sawa. Mshahara utakuwa elfu thelathini kwa mwezi!” alisema mwanaume huyo.
“Elfu thelathini?” aliuliza Sarafina, hakuamini kama kungekuwa na kazi yenye mshahara mdogo kama huo.
“Ndiyo! Unaona mdogo?” aliuliza mzee huyo huku akianza kubadilika.

“Hapana! Ni mkubwa na ndiyo maana nimeshangaa,” alisema Sarafina, japokuwa ilikuwa ni kazi ya kuuza baa lakini hakutaka kuiacha.

Akaanza kazi katika baa hiyo, walevi walipokuwa wakifika mahali hapo, walipenda sana kuhudumiwa na Sarafina kwa kuwa alikuwa msichana mrembo na msafi. Kila wakati alipenda kutabasamu japokuwa moyoni mwake kulikuwa na maumivu makali mno.
 
SEHEMU YA 26...

Kama ilivyokuwa kwa wahudumu wengine, hata yeye alikuwa akishikwashikwa, kila alipobeba chupa ya pombe na kupeleka katika meza za wateja, huko alishikwa makalio na hata wakati mwingine kusifiwa kwa uzuri aliokuwa nao.
“Unajua wewe dada mzuri sana,” alisema jamaa mmoja huku akimwangalia Sarafina.
“Ahsante!”
“Unakunywa pombe?”
“Hapana!”
“Daah! Unakosa ladha moja matata sana duniani! Pole. Hivi unaweza kunipa namba yako ya simu?’ aliuliza jamaa huyo.
“Sina simu!”

“Basi nikupe yangu moja ili tuwasiliane!” alisema mwanaume huyo.
“Huwa sijui kutumia simu!”
“Nitakufundisha!”
“Hapana! Usijali! Unataka Safari na nini?” aliuliza Sarafina.
Hakupumzika, kila siku alikuwa akisumbuliwa na wanaume hao, walimsfia kutokana na uzuri aliokuwa nao. Ni kama wanaume waliambiana kwani baada ya siku kadhaa wanaanza kujaa hapo baa na kila mmoja alitaka kuhudumiwa na Sarafina.

“Mimi namtaka yule dada mweupe ndiyo anihudumie,” alisema jamaa mmoja baada ya kufika hapo baa.
“Nani? Asnath?”
“Hapana yule mcheshi!”
“Mariamu?”

“Yule pale. Psipsiiiii…cheupe!” aliita jamaa huyo baada ya kumuona Sarafina.
Japokuwa tumbo lake lilikwishaanza kuonekana kwa mbali lakini msichana huyo alionekana kuwa kivutio kwa wateja wengi. Aliifanya kazi hiyo kwa kujitoa sana, kila mmoja alimpenda kutokana na upole wake.

Maisha yalikuwa na unafuu japokuwa yaliendelea kuwa mabaya. Hakuwa na chumba, alichangia chumba na wenzake, kama ikitokea mmoja akapata mteja, basi siku hiyo wengine wote walitakiwa kulala nje, na kama ulitaka kulala ndani basi ujue kwamba ni lazima uingiliwe na ukubali.

Hilo, kwa Sarafina lilikuwa gumu, wenzake walipokuwa wakipata wateja, alikwenda baa na kulala kwenye viti. Yalikuwa ni maisha yenye mateso mno lakini alivumilia.

Baada ya miezi miwili tumbo lake likaanza kuonekana, watu wakagundua kwamba alikuwa na mimba, wanaume waliokuwa wakimuona mrembo wakaanza kuondoka. Mimba iliharibu kila kitu lakini kwa Sarafina hakutaka kujali, hakuitoa mimba yake kwa kuwa alimuonea huruma mtoto aliyekuwa tumboni mwake, hivyo kubaki na mimba wala hakuona kama kulikuwa na tatizo.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 27...

Miezi ikasonga, ilipofikisha miezi sita, meneja wa baa hiyo akaamua kumfukuza Sarafina kazi. Msichana huyo akakimbilia mitaani, kulekule alipokuwa akiishi zamani. Hakuwa na fedha za kutosha kupanga chumba bali alianza upya kulala mitaani kama kawaida yake.

Mbu walimng’ata, alipigwa na baridi kali lakini hakujali, ndiyo kwanza aliendelea kufanya mambo yake, asubuhi anaamka na kuzurura kuombaomba mitaani na jioni anarudi kwenye kibaraza kulala.
**** “Nesi….nesi fungua mlango!” alisikika mwanaume mmoja akipiga kelele, saa ilionyesha ni saa saba usiku.
“Kuna nini jamani?”

“Huyu dada! Analalamika tumbo! Nadhani anataka kujifungua,” alisema jamaa huyo aliyekuwa na wenzake wawili.
Sarafina alikuwa akipiga kelele, alilishika tumbo lake, miezi tisa ilikatika na sasa alisikia uchungu wa kutaka kujifungua.

Usiku huo alikuwa kwenye wakati mgumu, alikuwa akilia huku akiomba msaada, wanaume hao waliokuwa wakipita njiani ndiyo waliomfuata na kumsaidia.
Walimpeleka katika Hospitali ya Halmashauri ya Tandale, kwa kuwa alitaka kujifungua, wakamchukulia usafiri na kutakiwa kupelekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mwananyamala. Njiani ilikuwa tabu tupu, msichana huyo alikuwa akipiga kelele za kutaka kujifungua.

“Damu! Jamani damu!” alisema jamaa mmoja, tayari aliona damu zikianza kumtoka Sarafina sehemu za siri.
“Kaka ongeza mwendo! Kama kanyaga moto,” alisema mwanaume mmoja.
“Nakufa! Nakufa! Nisaidieni nakufa!” alisema Sarafina huku akisikia maumivu makali chini ya kitovu.

*** “Nesi…nesi…sogeza machela…” alisema jamaa mmoja kwa sauti kubwa iliyowakurupusha manesi waliokuwa nje.
Hawakutaka kupoteza muda, haraka sana wakachukua moja ya machela zilizokuwa nje na kuwasogezea watu wale kisha kumuweka Sarafina na kuanza kuisukuma kuelekea ndani.

Damu hazikukoma, alionekana kuwa kwenye hatua za mwisho kujifungua. Wakampeleka katika chumba cha kujifunguliwa kilichoandikwa Labour mlangoni na kumlaza kitandani.

Ilikuwa ni lazima wafanye haraka sana kwani kama wangechelewa walihofia kuyapoteza maisha ya mama na mtoto. Ndani ya dakika moja tu, tayari walikuwa wakimtoa mtoto kutoka katika mfuko wa uzazi wa Sarafina.
Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 28...

“Sukuma…sukumaaaa…” alisema daktari aliyekuwa ndani ya chumba hicho.
“Naumiaaaaa…siweziiiiii…” alisema Sarafina huku akipiga kelele.
Hawakutaka kukubali, tayari mtoto alianza kuonekana, kitendo cha kukubaliana naye kwamba hawezi kusukuma kulimaanisha kwamba mtoto angekufa na hata yeye maisha yake yangekuwa hatarini.

Wakaanza kumpiga vibao mapajani na mashavuni kwa kumtaka kusukuma zaidi. Alijitahidi, alisukuma kwa nguvu zote, kichwa cha mtoto kikaanza kutoka, hakukoma, aliendelea kusukuma zaidi na zaidi na baada ya dakika chache, mtoto akatoka na nesi kumkata kitovu.

Sarafina akawa hoi, hakuamini kama alijifungua salama, akataka kujua ni mtoto wa jinsia gani alikuwa amejifungua, alikuwa mtoto wa kike, mzuri. Akapewa na kumuweka kifuani mwake kwa ajili ya kuchukua harufu yake.

Uso wake ukawa na tabasamu pana, alipomaliza kumuweka kifuani kwa dakika moja, manesi wakamchukua na kwenda kumuogesha kisha kumletea. Sarafina hakutakiwa kuondoka, walimtaka kubaki hospitalini hapo kwa siku mbili kwani hali yake haikuwa nzuri kama watu wengine walivyokuwa wakijifungua.

Hospitalini hapo, hakuwa na ndugu, hakujua ni kwa namna angeweza kuishi na mtoto wake baada ya kutoka hospitalini hapo. Aliendelea kuwa mahali hapo huku vyakula vya wagonjwa vilivyokuwa vikiandaliwa na uongozi wa hospitali hiyo ndivyo alivyokuwa akila kila siku.

Kichwa kilimuuma, alikuwa na mawazo tele, aliyafikiria maisha yake, yalikuwa ni ya kuumiza sana na hakujua ni kwa jinsi gani angeweza kuishi kama ilivyokuwa zamani. Alivyokuwa peke yake tu alikuwa na maisha ya tabu, vipi kama angekuwa akiishi na mtoto wake.

Kwenye kufikiria sana, ndipo akakumbuka kwamba zamani alipokuwa akipita katika mitaa ya kitajiri ya Masaki na Mikocheni kulikuwa na nyumba nyingi za matajiri ambazo hazikuwa zimemaliziwa na ndani kulikuwa na familia za mafundi waliokuwa wakiishi.

Hukoo ndipo alipotaka kwenda kuanza maisha mapya, hakujua kama angepokelewa na familia za mafunid hao au la. Siku aliyoruhusiwa, akamchukua mtoto wake aliyempa jina la Malaika na kuanza kwenda naye huko.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 29...

Hakuwa na pesa, hakukuwa na kitu chochote zaidi ya mtoto wake tu. Safari ya kwenda Mikocheni ikaanza mara moja. Ilimchosha, ilikuwa ni safari yenye kuchosha lakini alipambana njiani mpaka kufika huko akiwa hoi.

Alisimama mbele ya jumba moja kubwa na la kifahari, halikuwa limemaliziwa, lilizungushiwa ukuta na alipoangalia kwa ndani, aliona kukiwa kumeanikwa nguo na kugundua kwamba humo ndani kulikuwa na moja ya familia za mafundi waliokuwa wakiishi.

Akaingia huku akiwa na mtoto wake, hakuogopa, aliufuata mlango ambao ulizibwa kwa khanga na kuingia ndani. Macho yake yakatua kwa watu watatu, mwanamke mmoja, mwanaume na mtoto wao.

“Hodi!” alipiga hodi huku tayari akiwa ndani ya nyumba ile.
Watu wale wakaamka na kumwangalia Sarafina. Walishtuka! Hawakumfahamu mwanamke huyo na hawakujua alifuata nini. Wakakaa kitako kwa lengo la kumsikiliza shida zake.

Sarafina hakutaka kuwaficha, alikuwa mahali hapo kwa kuwa alihitaji sana msaada hivyo kuwaambia watu hao kwamba alikuwa masikini hivyo alihitaji msaada. Kwa kumwangalia tu ilionyesha dhahiri alikuwa masikini wa kutupwa, alikonda sana, macho yaliingia ndani, maziwa yake yalilala na hata nguo alizokuwa amezivaa zilionyesha ni kwa jinsi gani alikuwa masikini.

“Huyu ni nani?” mwanamke alimuuliza mumewe kwa sauti ya chini, japokuwa Sarafina aliwahadithia historia ya maisha yake lakini bado walitaka kujua zaidi.

“Sijui! Tumsaidie kweli au?” aliuliza mwanaume huyo, walikuwa wakiteta kwa sauti za kunoing’ona.
“Labda! Haina jinsi, ila tumebakiza miezi sita tu ya kuishi hapa, itakuwaje?” aliuliza mke.

“Haina jinsi! Japokuwa sisi ni masikini, haina jinsi, tumsaidie hata masikini mwenzetu,” alinong’ona mwanaume huyo.
Hawakuwa na kitu chochote kile, walikuwa wakiishi ndani ya nyumba hiyo kwa mwaka wa pili. Hayo ndiyo yalikuwa maisha yao, wakati nyumba za matajiri zilivyokuwa zikijengwa, waliomba hifadhi, walikuwa wakipewa, kwa kifupi maisha yao yalikuwa ya kuhamahama.

je, nini kiliendelea?
 
SEHEMU YA 30...

Wakaishi na Sarafina nyumbani hapo, hakukuwa na maisha mazuri hata kidogo, sakafu ilikuwa ni ya mchanga, madirisha hayakuwekewa nyavu wala kioo, yaliwekewa khanga kwa ajili ya kuzuia wadudu kuingia humo ndani.

Malaika alikuwa msumbufu, mara kwa mara alikuwa mtoto wa kulia, alisumbua sana lakini Sarafina hakuonekana kukasirika hata mara moja. Huyo alikuwa mtoto wake, aliyemzaa yeye mwenyewe, alimpenda zaidi ya kitu chochote kile.
Siku zikaendelea kukatika. Mtu aliyekuwa akitegemewa nyumbani hapo alikuwa mzee Hamidu, mwanaume aliyekuwa akiishi na mkewe. Yeye ndiye aliyekuwa akitafuta pesa ya matumizi kwa kwenda kwenye kazi zake za ujenzi na kufanya mishemishe yake nyingine.

Miezi iliendelea kukatika huku mtoto Malaika akiendelea kukua pamoja na mtoto wa wasamaria wema hao aliyeitwa Saleh aliyekuwa na miaka mitatu. Maisha hayakuwa rahisi hata mara moja, wakati mwingine walilazimika kulala na njaa hasa pale walipokuwa wakikosa chakula.

Baada ya kutimiza miezi mitano tangu aishi mahali hapo Aisha akaanza kujisikia hali ya tofauti mwilini mwake. Uchovu ukamuanza na muda mwingi alikuwa akisikia maumivu katika maziwa yake.
Alijishangaa, hakuwahi kuwa katika hali hiyo hata siku moja, alikuwa na hofu kwamba inawezekana alikuwa na kifua kikuu lakini kitu kilichompa maswali mengi. Hakutaka kubaki kimya, akamshirikisha Aisha ambaye alimwambia kwamba ni lazima waende hospitali kwani inawezekana maziwa yake yalikuwa yakiisha kwa haraka.

“Naogopa!” alisema Sarafina.
“Unaogopa nini?”
“Basi tu kwani hata huku kwapani nimepata uvimbe!” alisema Sarafina.
Hilo lilimuogopesha zaidi Aisha na hivyo kumlazimisha kwenda hospitalini ili kujua ni kitu gani kilisababisha hali hiyo mwilini mwake. Wakaondoka hapo mpaka katika Hospitali ya Mwananyamala ambapo baada ya kuonana na daktari, Sarafina akaambiwa kwamba alikuwa na saratani ya matiti ambayo kwa Kiingereza iliitwa Breast Cancer).
“What?” (nini?)
“You have breast cancer,” (una saratani ya matiti) alijibu daktari.

je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 31...

Sarafina akanyamaza, akakiinamisha kichwa chake chini, machozi yakaanza kumtoka. Moyo wake ulikuwa na maumivu makali, hakuamini kama aliathirika kwa kupata ugonjwa huo.

Aisha akaanza kumbembeleza anyamaze lakini mwanamke huyo hakunyamaza, aliendelea kulia zaidi. Wakapewa dawa na kurudi nyumbani. Mimba aliyopewa na David ikaharibu kila kitu, ikayaharibu maisha yake kwa ujumla na kujikuta akipata matatizo makubwa zaidi.

Alijuta kuwa na mwanaume huyo, alimwamini kwa asilimia mia moja lakini matokeo yake mwanaume huyo akamuumiza, hakumuonea huruma hata kidogo.
Kitendo cha kuumwa ugonjwa huo, tayari aliliona kaburi mbele yake, hakuona kama angeweza kupona kwani aliwafahamu watu wengi waliowahi kuumwa ugonjwa huo, wengi walikufa na yeye mwenyewe kuwazika.

“Ninakufa,” alisema Sarafina huku akiendelea kulia.
“Hutokufa! Kuumwa si kufa!”
“Ila ninaumwa kansa!”
“Hata kama kuumwa si kufa Sarafina!” alisema Aisha.
Matumaini ya kuendelea kuishi yakafutika, aliuona mwisho wake, alichokuwa akikifikiria kilikuwa ni mtoto wake tu. Hakujua kama angekufa mtoto huo angekuwa mgeni wa nani. Kila alipokuwa akimwangalia Malaika, moyo wake ulikuwa kwenye maumivu mazito.

“Who will love my baby?” (nani atampenda mtoto wangu?) alijiuliza, kila alipomwangalia Malaika, alikosa nguvu kabisa.
Kuanzia siku hiyo maisha yake hayakuwa kama yalivyokuwa kipindi cha nyuma, yakabadilika na mwezi wa sita ulipoingia, mwenye nyumba akafika na kuwaambia kwamba alitaka kuendeleza ujenzi wa nyumba yake na hivyo walitakiwa kuondoka haraka iwezekanavyo.

“Nyie mnakwenda wapi?” aliuliza Sarafina.
“Hatujajua! Ila tutaishi popote pale! Na wewe?” aliuliza Aisha.
“Sijajua! Ila nitakwenda mtaani, nitaishi hivyohivyo na mtoto wangu!” alisema Sarafina.

Hakutaka kubaki mahali hapo, siku hiyohiyo akaondoka kuelekea mitaani. Hakuwa na pa kwenda, kwa Dar es Salaam hakuwa na ndugu yeyote yule, marafiki zake hawakumtaka tena.
Sarafina hakuwa mrembo tena, alisinyaa, mwili ulikwisha na kwa jinsi alivyoonekana alionekana kama bibi aliyekaribia kufa.

Maisha ya mitaani yakaanza, akaanza kuombaomba fedha ya chakula. Mtoto wake alimsumbua, ili anyonye, alitakiwa kula chakula cha kutosha.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 32...

Alipokuwa akipita mitaani, watu walimuonea huruma, hawakujua historia ya maisha yake, walimsaidia kwa kuwa alionekana kuwa mwanamke aliyehitaji sana msaada.

Hakuwa na pesa za kununua dawa, kansa aliyokuwa nayo ikaendelea kusambaa, ikatoka katika maziwa na kusambaa katika kifua chake. Akaanza kukohoa, mwili ulipata tabu lakini alivumilia.

Hakuacha kumuomba Mungu, alijua kwamba asingepona lakini alimwambia Mungu kwamba amchukue wakati mtoto wake amefikisha hata miaka saba, kipindi ambacho angekuwa na uwezo wa kufanya kitu chochote kile.

Akayarudia maisha ya kulala vibarazani, usiku aliumwa na mbu, alipigwa na baridi lakini hakuwa na jinsi. Kila alipokuwa akilala, alihakikisha Malaika anamfunika vizuri kabisa. Si kila mtu aliyependa Sarafina alale kibarazani kwake, wakati mwingine alikuwa akifukuzwa kama mbwa, aliondoka na kwenda kulala katika kibaraza cha nyumba nyingine.

“Nyamaza mwanangu! Nyamaza Malaika!” alisema Sarafina huku akimwangalia mtoto wake aliyekuwa akilia.
Usiku wa siku hiyo ulionekana kuwa tofauti! Malaika alikuwa akilia kupita kawaida, alionekana kuwa na tatizo, ilimuogopesha mno Sarafina na kuhisi kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa maisha ya mtoto wake.

Mwili wake ulichemka mno, aliogopa, alipomwangalia machoni, mboni nyeusi haikuwa ikionekana, alikuwa akitetemeka mno huku aking’atang’ata ulimi wake kwa fisi zake zisizokuwa na meno.

“Mungu wangu! Malaika! Kuna nini mpenzi?” aliuliza Sarafina.
Aliuona mwisho wa mtoto wake, aliona kabisa kwamba alikuwa akienda kufa. Alikuwa tayari kushuhudia kila kitu maishani mwake lakini si kushuhudia mtoto wake akifariki dunia.

Akainuka pale kibarazani alipokuwa, hakutaka kubaki mahali hapo, akambeba na kuanza kuondoka. Alikuwa Magomeni Mapipa, kuelekea katika Hospitali ya Mwananyamala ilikuwa mbali sana lakini hakuwa na jinsi, hakuwa na nauli, ilikuwa ni saa nane usiku, kama hakuwa na nauli, alitakiwa kukimbia kuelekea hospitalini huko.

Hali ya Malaika iliendelea kubadilika, kila alipopiga hatua ndivyo hali yake ilivyozidi kuwa mbaya. Sarafina alilia, kilio chake hakikubadilisha kitu! Malaika aliendelea kuwa vilevile.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 33...

“Please my baby! Don’t go! Please don’t leave me,” (tafadhali mtoto wangu! Usiondoke! Usiniache!) alisema Sarafina huku akilia.
Alikuwa akikimbia, alifika Magomeni Morocco huku hali ya mtoto wake ikiwa mbaya kabisa. Aliendelea kugongagonga fizi zake huku akionekana kuwa kwenye hatua za mwisho kabisa za kuishi. Angefanya nini kama mtoto wake, Malaika angekufa? Angelia vipi? Angemlaumu Mungu kiasi gani?

“Mungu! Nina kansa! Najua nitakufa! Ila naomba uniachie mtoto wangu! Mungu! Nisikie kilio changu, naomba uniachie mtoto wangu! Mungu! Niue mimi, nipo tayari kufa hata sasa hivi, niue Mungu, niue Mungu, nipo tayari kufa hata sasa hivi ila naomba uniachie mtoto wangu! Ni mdogo mno, sijajua ataishi vipi baada ya mimi kufa, ila nipo tayari kufa kwa ajili ya mtoto wangu! Niue Mungu hata sasa hivi ila umuache Malaika aishi!” alisema Sarafina huku akilia.

Hakujua kama mwilini mwake alikuwa na nguo ya ndani tu. Khanga aliyokuwa nayo mwilini ilidondoka, hakujua, alikuwa akikimbia. Mwananyamala kulikuwa mbali, hakusimama, hakujua kama alikuwa na nguo ya ndani, kitu alichokuwa akikifikiria ni kumuokoa mtoto wake tu ambaye mwili wake ulipata joto kali mno na kila alipomwangalia, alikuwa na uhakika kwamba usiku huo ndiyo ulikuwa wa mwisho kumuona mtoto wake akiwa hai.

“Niue Mungu!” alisema huku akikimbia kama mtu aliyechanganyikiwa. Kwa jinsi alivyokuwa, kila mtu aliyemuona alifikiri kwamba mwanamke huyo alikuwa chizi, wengi wakaanza kumpiga picha na kuchukua video, yeye hakutaka kujali, alikuwa akikimbia kuelekea katika Hospitali ya Mwananyamala huku tayari ikiwa imefika saa nane kasoro usiku.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 34...

David hakutaka kukumbuka kuhusu Sarafina, kwake, msichana huyo alikuwa kama wengine tu, kutembea nao na kufanya mapenzi kisha kuwaacha wakiwa na maumivu makali, na mbaya zaidi kuwaacha na mimba huku akikataa kwamba haikuwa yake.

Alipotoka kwa Sarafina, moyo wake ukavutika kwa msichana mwingine, huyo aliitwa Paulina. Alikuwa ni miongoni mwa wasichana warembo chuoni hapo. Alimpenda, alimvutia kwani mapaja yake manene na kalio lake kubwa lilimpagawisha kupita kawaida.

Kama kawaida yake akajitosa, alitaka kutembea na msichana huyo, amuonyeshee mapenzi ya dhati kama alivyomuonyeshea Sarafina, amfanye ajione kuwa mwanamke mwenye thamani, anayependwa zaidi ya mwanamke yeyote katika dunia hii, lakini akishamaliza kazi yake, amuache na kuendelea na maisha yake.

David aliingia kwa gia ya kumsifia, kwamba alikuwa mwanamke mrembo, mwenye sifa za kuitwa mrembo ambaye alikuwa na umbo kali hata Agnes Masogange hakuwa akiingia. Moyo wa Paulina ukafurahi, akapenda kusifiwa, akapewa sifa kemkem na kuambiwa kwamba sura yake ilikuwa ya kitoto, iliyokuwa na mvuto kama video vixen, Baby Annaiyah kitu kilichomfanya kumpenda mwanaume huyo.

Alipenda kuonana naye kwa kuwa tu kila walipokutana alikuwa akisifiwa. David akautumia udhaifu huohuo kummaliza Paulina, akawa haoni wala asikii, yeye ndiye aliyekuwa akimpigia sana simu David na kuzungumza naye kwani aliamini kwamba kila alipofanya hivyo ilikuwa ni lazima kusifiwa.

“Eti kama Jenifer Lopez,” alisema Paulina huku akitoa kicheko cha kike.
“Ndiyo hivyo Paulina. U msichana mzuri sana mpaka Jini Maimuna anakuonea wivu. Mtoto unajua kucheka, unajua kutembea. Na huko nyuma ulivyoumbika. Mtoto mashallah! Yaani ungekuwa

Mombasa, sasa hivi unamiliki ndege yako, biashara kubwa kutoka Dubai,” alisema David, jinsi alivyoongea alionekana kumaanisha japokuwa ukweli ni kwamba alitaka kupata nafasi ya kukiona kitovu cha msichana huyo na baadaye kushuka chini kidogo.

“Wala mimi siyo mzuri!” alisema Paulina huku akitaka kusikia david angempa sifa zipi nyingine.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 35...

“Unajidanganya! Nilipokuona mara ya kwanza, nilidhani nimekutana na jini. Nilipokusalimia, hakika mtoto una sauti nzuri sana, hivi ushawahi kuimba kwaya?” aliuliza David.
“Hapana!”

“Kwa sisi tuliowahi kuimba, sauti yako ni sauti ya kwanza, ile inayowafanya wenye mapepo walipuke, ni sauti ambayo ukiimba kwa muda mrefu, Mungu atasimama kwenye kiti chake cha enzi na kujivunia uumbaji wake, kujivunia kumpa msichana mmoja sauti nzuri ya kumsifu na kumuabudu,” alisema David.

Kila mstari aliomwambia Paulina, alilainika, akamuona david kuwa mwanaume mzuri, ambaye alistahili kuwa maishani mwake. Akasimama kutoka kitandani, akakisogelea kioo na kuanza kujiangalia. Sifa za mwanaume huyo zikaanza kujirudia kichwani mwake, kweli, kile alichokisema David ndicho alichokiona, akalitingisha kidogo kalio lake.

“Ahsante Mungu kwa kunipa hii silaha matata!” alisema Paulina kisha kutoa tabasamu.
Paulina alianza kubana, akabana na kubana lakini akashindwa kuvumilia. Katika siku ambayo hakuitarajia, akajikuta akilala kwenye kitanda cha David, akaipanua miguu yake na kuvunja amri ya sita na mwanaume huyo.

Hilo likawa kosa, damu zikakutana, akajiona kama amemalizwa kila kitu, hakuwa na ujanja tena, mwanaume huyo aliitumia nafasi hiyohiyo kukutana naye kimwili, hata kama alikuwa hataki, alikumbushwa namna alivyokuwa fundi kitandani, akakumbushwa jinsi alivyokuwa akiguna juu ya sita kwa sita na mwisho wa siku kumkubalia tena.

Wakabanjuka na kubanjuka, starehe zikaongezeka, baada ya miezi miwili, msichana Paulina akaanza kujisikia tofauti, hakutaka kuchelewa, akaenda kupima, majibu yakatoka na kuambiwa kwamba alikuwa na mimba.

Alijuta, alimtafuta David na kumwambia kuhusu ujauzito huo, kama ilivyokuwa kwa Sarafina, akamkatalia, akamwambia kwamba haikuwa yake, na kama alikuwa na mchezo wa kupata mimba sehemu nyingine kisha kumsingizia, basi wasijuane.

Paulina akaumia lakini hakuwa na jinsi, akakubaliana na mwanaume huyo, alichokifanya ni kutoa mimba na maisha yake kuendelea huku akijiahidi kwamba asingeweza kuuruhusu mwili wake uchezewe na mwanaume mwingine kama ilivyokuwa kwa David.

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 36...

Hiyo ilikuwa ndiyo tabia yake, David hakuridhika, akaendelea kuwafunua wasichana wengi na kila alipokutana na marafiki zake akaanza kuwaambia kuhusu sifa za wanawake mbalimbali, alijua wanene walikuwa na mbwembwe gani kitandani, alijua wembamba walikuwaje, weupe na weusi, wote alijua wanafananaje.

Baada ya kutembea nao sana, mwisho wa siku akakutana na msichana mmoja, binti aliyetoka katika familia bora, huyu aliitwa Gloria, msichana mrembo, mwenye figa matata ambaye alikutana naye katika Ufukwe wa Mbalamwezi.

Alimfuata na kuzungumza naye, kwa kuwa alikuwa muongeaji sana, ndani ya dakika kadhaa wakawa kama watu waliofahamiana miaka mingi iliyopita hivyo kubadilishana namba za simu.

“Basi nitakucheki!” alisema David.
“Usijali! Nitasubiri simu yako,” alisema Gloria huku akiingia ndani ya gari lake la kifahari kisha kuondoka mahali hapo huku David akiwa amesimama akiliangalia linavyoondoka.

“Hawa ndiyo wanawake sasa. Huyu naoa,” alijisema huku akiachia tabasamu pana.
**** Sarafina alionekana kama kituko, watu wachache waliokuwa wakimwangalia walibaki wakimshangaa, hawakuamini kumuona mwanamke aliyekuwa kwenye hali ile kama alivyokuwa Sarafina.

Alikuwa akiendelea kukimbia kuelekea katika Hospitali ya Mwananyamala, hakufahamu kama Magomeni kulikuwa na hospitali, hospitali alizokuwa akizifahamu zilikuwa mbili tu, Muhimbili na hiyo aliyokuwa akiifuata.

Kama kulia, alilia sana lakini hakukuwa na kitu kilichobadilika, mtoto Malaika aliendelea kuwa kwenye hali ileile, mboni nyeusi haikurudi, macho yake yaliendelea kuwa meupe huku mwili ukimtetemeka.

Huku akiwa njiani akikimbia na tayari akiwa amefika Kinondoni Studio, ghafla akapigiwa honi, akayapeleka macho yake pembeni kuliangalia gari lililompigia honi, macho yake yakatua katika gari moja ndogo.

“Dada unakwenda wapi?” aliuliza mwanaume aliyekuwa ndani ya gari hilo, harakaharaka Sarafina akamkimbilia huku akilia.

“Naomba unisaidie! Mtoto wangu anakufa! Malaika wangu anakufa,” alisema Sarafina huku akimwangalia mwanaume huyo ambapo baada ya kupeleka macho kwa Malaika, yeye mwenyewe alishangaa.

“Mungu wangu!” alisema, hapohapo akaufungua mlango, akamuingiza ndani na kuanza kuelekea hospitali.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 37...

Njiani, dereva aliendesha gari kwa mwendo wa kasi. Hakuchukua muda mrefu akafika hospitalini hapo ambapo akamfungulia Sarafina mlango na kisha kumteremsha.

“Nesi! Nesi msaada jamani!” alipiga kelele mwanaume huyo. Manesi wawili wakasogea, walipomwangalia Malaika, wao wenyewe wakashangaa, wakamchukua na kumpeleka katika chumba cha matibabu kisha kumuwekea dripu ya maji yaliyochanganywa na dawa.

Sarafina alibaki kwenye benchi akilia, alimwangalia mwanaume yule, alishindwa ni kwa jinsi gani alitakiwa kumshukuru kwani alikuwa amemsaidia kwa kiasi kikubwa na inawezekana pasipo yeye basi mtoto wake, Malaika angeweza kufa njiani.

“Nashukuru sana,” alisema Sarafina huku akilia.
“Usijali mama!”
Matibabu yaliendelea, mwanaume yule hakuondoka, alibaki hapohapo hospitali akitaka kuona ni kitu gani ambacho kingetokea. Kila alipomwangalia Sarafina, hakujua alikuwa na nini ndani yake, alikuwa akiendesha kuelekea klabu lakini ghafla, huku akiwa na haraka akamuona mwanamke huyo, hakuwa na lengo la kusimama, hakuwa na lengo la kuzungumza naye lakini alishtukia gari lake likisimama na yeye mwenyewe kuzungumza kitu ambacho hakukitaka kabisa.

“Ni Mungu ndiye aliyesimamisha gari langu! Kwa nini alitaka nimsaidie mwanamke huyu?” alijiuliza lakini alikosa jibu.
Akasahau kuhusu klabu, hakutaka kwenda tena huko, alibaki hospitalini hapo na Sarafina huku akimfariji kwamba mtoto wake angepona na kusingekuwa na kitu chochote kibaya ambacho kingetokea.

Baada ya saa moja, mlango wa chumba alichokuwemo mtoto wake ukafunguliwa, nesi mmoja akatoka kutoka humo, harakaharaka Sarafina akasimama na kumfuata nesi, alitaka kujua ni kitu gani kiliendelea, alitaka kujua hali ya mtoto wake.

“Mtoto wangu anaendeleaje?” aliuliza Sarafina huku akimwangalia nesi yule machoni, akashindwa kujibu swali hilo, ghafla machozi yakaanza kumlenga na mwisho wa siku kutiririka mashavuni mwake.

“Nini kinaendelea?” aliuliza Sarafina, machozi ya nesi yalimjibu swali alilokuwa ameuliza, huku akiwa na presha kubwa moyoni mwake, ghafla nesi yule akaanza kulia kwa sauti, Sarafina akashtuka, naye akaanza kulia, sauti ndogo ikaanza kusikika moyoni mwake kwamba mtoto wake, Malaika alikuwa amefariki dunia.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom