CCM yajimaliza kukumbatia ulaji
Mwandishi Wetu Julai 30, 2008
Raia Mwema~Muungwana ni Vitendo
Imejiweka pabaya 2010
Nape ni ‘moshi' wa moto wa ndani
MGONGANO wa kauli na misimamo ndani ya Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UV CCM) kuhusiana na uwekezaji katika kiwanja cha makao makuu ya umoja huo Dar es Salaam ni matokeo ya chama tawala kuyumbishwa na kujiruhusu kwake kukumbatia fedha katika shughuli zake nyingi, Raia Mwema imeambiwa.
Baadhi ya wanasiasa waliozungumza na Raia Mwema wiki hii, wanasema hulka iliyokithiri ya kupenda fedha kwa njia yoyote ndiyo ambayo sasa inatafuna mzizi mkuu wa UVCCM na jumuiya nyingine za CCM, Umoja wa Wanawake (UWT) na Jumuiya ya Wazazi.
Tokea kuasisiwa kwake, jumuiya zote za CCM zilikuwa ndio nguzo kuu za kisiasa na kiuchumi za chama hicho tawala tokea enzi za TANU na ASP, lakini katika miaka ya karibuni hali imekua kinyume chake na sasa muanguko wa chama hicho unaweza kuchangiwa na jumuiya zake.
Kwa karibu mwezi sasa UVCCM imekuwa katika malumbano yaliyoibuliwa na mmoja wa vijana ambao wamejitokeza kuwania uongozi wa juu wa umoja huo, Nape Nnauye.
Nnauye ambaye anataka kugombea uenyekiti wa umoja huo katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Desemba mwaka huu, amekuwa akisema katika matukio mbalimbali kwamba kuna dalili za ufisadi katika mradi wa ujenzi wa jengo la makao makuu ya UVCCM unaofanywa na kampuni moja ya binafsi.
Kwa mujibu wa Nnauye, mradi huo mkubwa haukupata kuridhiwa na vyombo husika ndani ya UVCCM na hata Kamati Kuu ya CCM na kwamba hata wakati mkataba wenyewe wa ujenzi una utata tayari mjenzi amekwisha kuanza kazi.
Kauli hiyo ya Nnauye imevuta majibu kadhaa kutoka ndani ya CCM yakiwamo ya Katibu Mkuu, Yusuf Makamba, Mwenyekiri wa UVCCM anayemaliza muda wake Emmanuel Nchimbi na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa UVCCM Edward Lowassa, lakini ambayo yamekuwa hayasaidii kueleza ni nini hasa kinachoendelea kuhusiana na mradi huo mkubwa.
Kati ya mambo aliyotaja Nnauye yanayozua utata ni kwamba mwekezaji, kwa mujibu wa hati ya makubaliano ya awali, atamiliki jengo jipya litakalojengwa katika kiwanja hicho kwa asilimia 75 huku UVCCM ikibakiza asilimia 25 milele.
Aidha, Nnauye amesema kwamba mwekezaji huyo ametumia hati ya kiwanja hicho kuombea mkopo benki, jambo ambalo hata UVCCM wangeweza kulifanya na hivyo wao wenyewe kuweza kusimamia ujenzi bila kuhitaji msaada wa mwekezaji.
Lakini wafuatialiaji wa mambo ndani ya CCM wanasema kwamba kuibuka kwa habari hizo kuhusiana na UVCCM kunaeleza tu mambo ambayo yamekuwa yakitokota ndani ya CCM na kwenye jumuiya zake.
Mwaka jana, wanasema kwa mfano, kwamba aliyekuwa Katibu Mkuu wa UWT, Halima Mamuya, aliondoshwa katika wadhifa huo kwa sababu zinazohusiana na mgogoro mwingine wa kiwanja cha UWT, kilichoko Kinondoni, Dar es Salaam, na kilichokuwa na jengo kubwa la umoja huo, ambalo katika miaka ya mwanzo lilitumika kama hosteli ya wasichana.
Kama kilivyo kiwanja cha UVCCM, baadhi ya vigogo ndani ya CCM hawakufurahishwa na hatua ya UWT ya kuingia mkataba wa uwekezaji mkubwa katika kiwanja hicho na wakafanya jitihada za kutaka kina Mamuya wabadili msimamo na ikiwezekana hata kupata mwekezaji ambaye angekuwa ametafutwa na vigogo hao.
Habari zinasema ni mvutano huo ambao hatimaye ulimfanya Mamuya si tu kutupwa nje katika UWT bali pia kumkosesha nafasi ya ukuu wa wilaya aliyokuwa nayo, na habari za yeye na baadhi ya watendaji wengine zikaandikwa sana magazetini zikionyesha kwamba CCM ilikuwa inasafisha safu katika jumuiya zake.
"Ukweli ni kwamba kwa suala la Mamuya na UWT, CCM haikuwa inasafisha safu zake, bali ilikuwa ikiwasukuma nje waliogoma kufuata maelekezo ya vigogo ambao walitarajia kuneemeka kutokana na mikataba ya viwanja vya jumuiya za chama tawala.
"Kuna kundi la vigogo ndani ya CCM ambao biashara yao kubwa ni kamisheni, walikuwa wakihoji ni vipi jumuiya tanzu za CCM ziingie mikataba, tena mikubwa, ambayo dhahiri ingewanemeesha," anasema mwanasiasa mmoja ambaye ni mbunge wa CCM.
Raia Mwema imeaambiwa kwamba mvutano huo wa kiwanja cha UWT uliwalazimisha Mwenyekiti Anna Abdallah na Mwenyekiti wa Bodi ya Udhamini, waziri mkuu msitaafu, Jaji Joseph Warioba, kuja juu wakieleza kwamba UWT ni jumuiya inayojitegemea, ina mali ambazo ziko chini ya usimamizi wa wadhamini na kwa ajili hiyo ina haki ya kuamua kuhusiana na nini kifanyike kuhusu mali hizo.
Hoja ya vigogo ndani ya CCM ilikuwa ni kwamba kama jumuiya tanzu cha CCM, UWT haiwezi kuamua juu ya uwekezaji mkubwa kama unaofanyika katika uwanja wake wa Kinondoni bila baraka za Kamati Kuu.
Sasa inafahamika kwamba tayari vigogo hao walikuwa na wawekezaji kadhaa ambao walikwisha kutayarishwa kwa ajili ya uwekezaji katika kiwanja hicho cha UWT kwa ajili ya maslahi yao badala ya yale ya UWT.
Raia Mwema haikufanikiwa kuwapata Abdallah, Jaji Warioba na Mamuya kuzungumzia suala la kiwanja hicho kinachoendelea kujengwa. Baada ya kuwa nje tangu baada ya sakata hilo la kiwanja, wiki iliyopita, kama ilivyo kwa Nnauye, Mamuya alitangaza kuchukua fomu za kuwania uenyekiti wa UWT akieleza kwamba anakusudia kuendeleza yale mazuri aliyoshindwa kuyahitimisha alipoondoka.
Jumuiya ya Wazazi nayo haikubaki nyuma katika migongano hiyo mingi inayodhihirishwa na ugomvi wa fedha uliosababisha aliyekuwa Mwenyekiti, Abihudi Malegesi kuenguliwa.
Malegesi na viongozi wenzake ndani ya jumuiya hiyo walienguliwa wakituhumiwa kufuja fedha za jumuiya hiyo, tuhuma ambazo yeye alizigeuza kwa kudai kwamba zimetokana na muendelezo wa makundi ndani ya CCM.
Jumuiya hizo tatu sasa ziko katika hatua za awali za kuelekea katika uchaguzi na maoni ya baadhi ya waliozungumza na Raia Mwema ni kwamba kama hapatakuwa na uwazi wa kutosha basi kutashuhudiwa mapambano mengine ya makundi ya kifedha kupigana vikumbo hali ambayo imekuwa kielelezo kikubwa cha uchaguzi ndani ya chama tawala.
Kuyumba kwa CCM ikianzia ndani ya jumuiya zake, ni muendelezo wa kuyumba mfululizo kwa chama hicho tokea serikali ya awamu ya nne iingie madarakani, hali ambayo imeelezwa kuwa si ishara njema kwa chama hicho kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
Kwa zaidi ya miaka mitatu sasa CCM na serikali yake imekua ikikumbana na ‘mazonge' ya kisiasa na kiuchumi ambayo yamekifanya kila uchao kikifanya kazi ya ‘zima moto' na hivyo kuendelea kukidhoofisha machoni mwa wananchi.
Baadhi ya wanasiasa wakiwamo wabunge wa CCM na upinzani wameliambia Raia Mwema kwamba, Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, anapaswa kufanya maamuzi mazito katika kipindi kifupi kilichosalia kabla ya 2010, ikiwa ni pamoja na kuruhusu mageuzi makubwa ndani ya jumuiya za chama hicho na hata ndani ya serikali ili kurudisha imani ya wananchi.