Hili linathibitisha kwamba mafisadi ndiyo wameshika 'utamu' katika chama cha mafisadi. Hakuna hata mwenye busara huko.
Nape aigawa CCM
na Mwandishi Wetu
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
MGOMBEA wa nafasi ya Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Nape Nnauye, ameigawa CCM kutokana na mkakati uliopo wa kutaka kuliengua jina lake.
Chini ya mkakati huo, kigezo cha umri ndicho kitakachotumika na wabaya wake, na kukipenyeza katika vikao vya juu vya chama katika kuamua hatma yake, kuwania nafasi hiyo nyeti ndani ya umoja huo ambayo pia itamwezesha kuingia katika vikao vya Kamati Kuu ya CCM (CC).
Habari kutoka ndani ya UVCCM zinasema kuwa, mkakati wa kumuengua Nape katika kinyang'anyiro hicho ni wa muda mrefu, lakini umekuja kukolezwa zaidi na hatua yake ya kufichua ufisadi mzito, unaodaiwa kufanywa kupitia mradi wa ujenzi wa jengo la makao makuu la umoja huo, huku akiwataka baadhi ya watendaji wawajibike kwa madai kuwa mkataba huo hauna maslahi kwa umoja wa vijana nchini.
Hivi karibuni, wakati akichukua fomu, Nape alidai kuwapo kwa ufisadi katika mradi wa ujenzi wa jengo la makao makuu ya UVCCM, na kumtaka Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini, Edward Lowassa, Mwenyekiti wa jumuiya hiyo, Dk. Emmanuel Nchimbi pamoja na Katibu wake, kuwajibika.
Kwa mujibu wa vyanzo vya habari kutoka ndani ya UVCCM, baadhi ya viongozi wa juu ndani ya umoja huo, hawataki kuona Nape anachukua nafasi hiyo inayoshikiliwa kwa sasa na Dk. Nchimbi, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.
Nape ambaye hadi siku alipojaza fomu, alikuwa na umri wa miaka 30, lakini itakapofika Novemba mwaka huu, siku chache kabla ya uchaguzi, unaotarajiwa kufanyika Desemba mwaka huu, atakuwa ametimiza miaka 31, hivyo kukosa sifa ya kuwa mwenyekiti wa umoja huo. Umri wa mwisho kwa mgombea wa jumuiya hiyo, unapaswa kuwa miaka 30.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo vya habari, uchaguzi huo awali ulipangwa kufanyika Septemba mwaka huu, lakini ulisogezwa mbele hadi Desemba kwa madai ya kutokuwapo kwa fedha za kutosha kuuendesha.
Hatua ya kuusogeza uchaguzi huo hadi Desemba, imetafsiriwa pia kuwa ni sehemu ya kumwondoa Nape kwenye kinyang'anyiro, kwani msimamo wake wa kuwania tena nafasi hiyo baada ya mara ya mwisho kubwagwa na Dk. Nchimbi, ulishakuwa wazi.
"Wapo viongozi walioapa kuwa Nape hawezi kuchukua nafasi hii, hao wako tayari kufa kuliko kumwona Nape akishika nafasi hiyo, na hawana sababu ya msingi. Kwa hiyo wanataka kumbana kwenye kigezo cha umri na itakapofika Desemba mwaka huu, atakuwa tayari amefikisha umri wa miaka 31, hivyo hatakuwa na sifa," kilisema chanzo chetu cha habari.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa kuchukua fomu, Nape alisema watakaotumia kigezo cha umri kumuengua, watashindwa kwani wakati anajaza fomu, alikuwa na miaka 30 na hadi sasa ana umri huo.
"Hoja hiyo sawa na kuua tembo kwa ubua. Mimi sasa hivi nina miaka 30, niko ndani ya sifa, sasa kama uchaguzi unafanyika Desemba, halafu tayari nina umri wa miaka 31, tena kwa kupitisha mwezi mmoja tu, sijui kama itawezekana kuniengua kwa sababu hiyo, lakini vikao ndivyo vitakavyoamua," alisema Nape.
Baadhi wa wajumbe wa Baraza Kuu la UVCCM, waliozungumza kwa sharti la kutotajwa majina yao kwa nyakati tofauti, walisema suala la Nape huenda likaibua mabadiliko ya sheria katika kuwania nafasi hiyo.
"Nafikiri kuna sababu ya kubadilisha kanuni na sheria zetu za uchaguzi. Ni makosa kusema kijana wa miaka 31 asigombee kwa kigezo cha umri. Yaani taasisi kubwa kama hii, tunataka iongozwe na kijana wa kuanzia miaka 25 hadi 30. Huyo hajakomaa bado," alisema mmoja wa wajumbe wa Baraza Kuu la UVCCM.
Hata hivyo, kigezo cha umri na hoja ya ufisadi, huenda vikawagawa wajumbe wa vikao vya maamuzi, kwani wapo wanaomuunga mkono kwa hatua yake ya kupasua jipu la ufisadi katika mradi huo.
Vyanzo vyetu vya habari vilisema, wapo wazee muhimu ndani ya chama wanaomuunga mkono kijana huyo kwa ujasiri wa kusema ukweli, na kuahidi kumuunga mkono kwenye vikao vya maamuzi.
Hata hivyo, wapo baadhi ya wazee walioeleza waziwazi kukerwa na hatua ya kijana huyo kuwashambulia baadhi ya viongozi na kuwatuhumu kwa ufisadi katika mradi huo.
Nape ambaye ni mtoto wa marehemu Moses Nnauye, ni mgombea pekee aliyopo ndani ya Baraza Kuu na pia ndani ya Halmashauri Kuu ya CCM na amekaa katika nafasi hizo kwa muda mrefu.
Wengine wanaowania nafasi hiyo pamoja na Nape ni Jerry William, Zainabu Kawawa, Hussein Bashe, Beno Malisa, Antony Mtaka, Said Mtanda, Hule Pangisa, Samwel Malelo, Stephen Deya na Gregory Mwankenja.
Wengine ni David Manoti, Mussa Mnyeti, Edson Lubuwa, Mwamini Lusingu, Asma Kalokola, Marco Zablon Alute, Harrod Adamson, Hamad Masauni, Suleiman Muhsin, Issa Haji Ussi, Idila Hillary Vuai, Ashura Ismail, Rashid Msalaka na Raha Ahamada Ali.
Wanaowania nafasi ya Makamu Mwenyekiti ni Happy Mahava, Raha Ahamada, Ali Riziki, Pembe Juma, Michael Bundara, Rabia Hamid, Sadifa Khamis, Shaka Hamedu Shaka, Nuru Muhamed Ahmed na Twaha Ali.