Mkataba jengo la UVCCM wazidi kuwakoroga viongozi
*Makamba, Nchimbi wakwepa hoja za Nnauye
*Mwekezaji asogeza vifaa, aanza ujenzi
*Mkataba bado haujasainiwa hadi sasa
*Kamati Kuu kuujadili Julai 29 mwaka huu
Na Kizitto Noya
Mwananchi
SAKATA la utata katika mkataba wa ujenzi wa Jengo la Makao Makuu ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), limechukua sura mpya baada ya kubainika kuwa mwekezaji amekwishaanza kazi, wakati viongozi wa CCM wakidai kwamba mkataba haujasainiwa.
Wakati Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM, Francis Isaac, anasema kuwa vifaa vya ujenzi vimekwishawasili kwenye eneo la ujenzi kama sehemu ya matayarisho, Mwananchi imeshuhudia ujenzi halisi ukiwa umekwishaanza.
Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba, licha ya juzi kusema kwamba, mkataba huo haujasainiwa, jana alishindwa kueleza sababu za mwekezaji huyo kusogeza vifaa eneo la ujenzi akisema kuwa hahusiki na masuala ya ujenzi, ila mkataba ambao ameona kuwa unafaa.
Makamba aliliambia gazeti hili kuwa, mkataba huo una manufaa kwa UVCCM ila hawezi kuzungumzia suala la mwekezaji huyo kusogeza vifaa kabla ya kusainiwa kwa mkataba huo kwani halimhusu.
''Mimi ninachosema, mkataba huo una manufaa kwa UVCCM, kuanza ujenzi ni suala lingine ambalo mimi sihusiki nalo, unaweza kuwapigia wenyewe (UVCCM) waseme kwa nini mwekezaji huyo amesogeza vifaa wakati mkataba haujasainiwa,'' alisema Makamba na kuongeza:
''Ujenzi ni suala la kiufundi, linahitaji vibali na kuthibitishwa na mamlaka mbalimbali siwezi kuzungumzia hilo na ukitaka waulize wenyewe watoe majibu."
Mwenyekiti wa UVCCM anayemaliza muda wake, Dk Emmanuel Nchimbi, alikwepa kuzungumzia utata huo kwa maelezo kuwa, yeye sio mtendaji wa taasisi, bali kiongozi wa vikao vya taasisi hiyo.
Nchimbi alimtaka mwandishi wa habari hii kuwasiliana na watendaji wa UVCCM kwa maelezo zaidi kwa kuwa ndio wasimamizi wa shughuli za kila siku za jumuiya hiyo.
"Mimi sio mtendaji wa taasisi, kazi yangu ni kuongoza vikao uwatafute watendaji watakuwa na majibu ya swali hilo," alisema Nchimbi na kukata simu.
Alipotakiwa kueleza sababu za mwekezaji huyo kusogeza vifaa vyake katika eneo la ujenzi kabla mkataba huo haujasainiwa, Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM, Isaac alisema suala hilo ni la kawaida katika mikataba.
Alisema mwekezaji huyo amefanya hivyo kama sehemu ya maandalizi ya kuanza kazi na jambo hilo ni la kawaida na lipo kwenye hadidu rejea za mkataba huo utakaosainiwa.
"Huwezi kusaini mkataba wakati mwekezaji hajaleta vifaa kwa sababu kuna mambo mengi, moja ni kusaini mkataba na mtu ambaye hana uwezo na suala hilo lipo kwenye Memorandum of Understanding."
Alipoulizwa endapo Jumuiya itakuwa na wajibu gani kama wajumbe wataghairi kuingia mkataba huo, Isaac alisema, kimsingi jumuiya haina gharama yoyote zaidi ya mwekezaji huyo kuondoa vifaa vyake.
"We are very careful (tuko makini sana), tatizo ni watu kutofuatilia data (kumbukumbu) na kutafuta kura kwa njia ambayo sio sahihi," alisema Isaac.
Isaac jana kama ilivyo kwa Makamba, alisema kwamba mwekezaji katika jengo jipya anasubiri kusainiwa kwa mkataba baada ya kikao cha Kamati Kuu mwishoni mwa mwezi huu.
Viongozi hao wakishikilia kwamba mkataba unasubiri kusainiwa, harakati za ujenzi zimepamba moto kinyume cha madai kwamba, mwekezaji anakusanya vifaa vya ujenzi akisubiri kusainiwa kwa mkataba.
Mkataba huo umekwisha kuamsha mvutano mkubwa ndani ya UVCCM na Makamba juzi alizungumza na gazeti la Uhuru akimtuhumu Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Nnape Nnauye, kwamba amewakosea wajumbe wa Bodi ya Wadhamini ya UVCCM kwa kubariki mkataba huo alioueleza kuwa na harufu ya kifisadi.
Nnauye ambaye pia ni mjumbe wa Baraza Kuu la UVCCM, Jumanne iliyopita aliwashambulia Mwenyekiti wa Bodi, Edward Lowassa, Mwenyekiti wa UVCCM, Dk Emmanuel Nchimbi na Kaimu Katibu Mkuu Isaac akiwahusisha na mkataba huo aliouita tata.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kuchukua fomu ya kugombea nafasi ya mwenyekiti wa UVCCM, Nnauye aliwataka viongozi hao kuwajibika kwa kuwa wamehusika moja kwa moja na mkataba huo mbovu.
Alisema, viongozi hao wanapaswa kuwajibika kwani mkataba huo ni tata kwa kuwa moja ya vipengele vyake kinasema, utakuwa wa maisha na mwekezaji atamiliki asilimia 75 ya hisa wakati UVCCM itamiliki asilimia 25 tu.
Nnauye pia alisema utata mwingine katika mkataba huo ni mwekezaji kutumia hati za jengo la UVCCM kuomba fedha za kazi hiyo kutoka benki, badala ya kutumia mtaji wake, jambo alilosema kuwa lingeweza kufanywa hata na jumuiya yenyewe.
Alisema, Lowassa ambaye ni mbunge wa Monduli na Waziri Mkuu Mstaafu, kwa mamlaka yake ya kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya UVCCM na wenzake Nchimbi na Isaac, wangeweza kuzuia suala hilo kwa kuwa ndio wenye jukumu la kusimamia mali za Jumuiya hiyo.
Hata hivyo, hoja ya Nnauye ilipata pingamizi kutoka kwa mgombea mwingine wa nafasi ya mwenyekiti wa UVCCM taifa, Hussein Bashe, ambaye alimlaumu kwa kuwashambulia viongozi hao na kuwahusisha na utata katika mkataba huo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana kabla na baada ya kuchukua fomu ya kugombea nafasi hiyo, Bashe alimtaka Nnauye kuwajibika kwa kujiuzulu nafasi za ujumbe wa Halmashauri Kuu na Baraza Kuu la CCM, badala ya kuwataka viongozi hao kuchukua hatua hiyo kwa kuwa naye alishiriki kwenye maamuzi kwa mujibu wa nafasi yake.
"Kitu kikiamriwa na kamati, kinatakiwa kuwa collective responsibility (uwajibikaji wa pamoja). Iweje, Nnauye aseme hilo leo miezi saba baada ya maamuzi ambayo pia alishiriki?" alihoji Bashe.
Nnauye ambaye baada ya kauli hiyo aliitwa na Katibu Mkuu wa CCM, aliliambia gazeti hili jana kuwa ingawa hapendi kuendeleza malumbano juu ya suala hilo kutokana na heshima aliyonayo kwa Makamba, bado anasisitiza kuwa mkataba huo ni mbovu na viongozi hao wanatakiwa kuwajibika.
Alisema hawezi kujiuzulu nafasi zake za ujumbe wa Halmashauri na Baraza Kuu la CCM kwa kuwa msimamo huo alianza kuuonyesha tangu awali kwa kushawishi Baraza Kuu kuishinikiza kamati ya utendaji irekebishe upungufu huo bila mafanikio.
"Nisengependa kuendeleza malumbano hayo kwani Makamba ni mzee wangu, lakini kwa kuwa watu wananitaka nijiuzulu, nasema siwezi kufanya hivyo kwa kuwa msimamo wangu niliuonyesha kwenye vikao halali bila mafanikio," alisema.
Nnauye jana aliendelea kuhoji sababu za mwekezaji huyo kusogeza vifaa eneo la ujenzi endapo mkataba huo haujasainiwa kama inavyodaiwa na baadhi ya viongozi hao wa CCM akiwamo Makamba.