nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,860
- 5,803
*Wadai anakwenda kuvuna fedha
*Wakumbusha yaliyomtokea Temeke
Na Gladness Mboma
SIKU moja baada ya Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa CCM kumpitisha Rais Mstaafu Bw. Benjamin Mkapa kwenda kuzindua kampeni za chama hicho katika jimbo la Igunga, viongozi wa vyama vya upinzani vinavyoshiriki kinyang'anyiro hicho wamesema kiongozi huyo mstaafu anakwenda jimboni humo kuvuna aibu na yatampata kama yale yaliyompata Jimbo la Temeke kwenda kumnadi Bw.Cisco Mtiro mwaka 1996.
"Mkapa hana ubavu wowote wa kufanya aende Igunga kuzindua kampeni za CCM, kwa kuwa mikataba yote mibovu ya madini imesainiwa chini ya uongozi wake wakati mgombea anayeenda kumnadi Dkt. Dalaly Kafumu ambaye ni Kamishna wa Madini wa Wizara ya Nishati na Madini alikuwepo pia katika kipindi hicho.
"Mwaka 1996 Bw. Mkapa alienda Temeke wakati wa uchaguzi mdogo kumpigia debe Bw.Mtiro aliyekuwa anagombea na Bw. Augustino Mrema, lakini aliishia kuzomewa huku Mrema akiitwa ndiye Rais," alisema msemaji wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bw. Erasto Tumbo.
Katika uchaguzi huo Bw. Mrema aliibuka kuwa mshindi kupitia tiketi ya Chama cha NCCR-Mageuzi.
Naibu Katibu Mkuu Bara wa CUF, Bw. Julius Mtatiro na Msemaji wa CHADEMA, Bw. Erasto Tumbo wakizungumza kwa nyakati tofauti walisema kuwa Bw. Mkapa ushawishi wake uko kwa watu wa kimataifa na si kwa watu wa kawaida.
"Kwenda kwake Igunga ni kwenda kusafisha aibu ya CCM, lakini ningekuwa ni mimi ningekataa kupokea zigo ilo kwa vile wanakwenda kujitia aibu na kwa nini aende maali CCM hawatakiwi haoni kama anaenda kuaibika,"alihoji, Bw. Tumbo.
Alisisitiza kwamba kama Bw. Mkapa amekubali kwenda Igunga anatakiwa awe tayari kukabiliana na aibu atakayoikuta kuanzia yeye na serikali yake ya CCM.
"Leo Mkapa analetwa kuja kumnadi Dkt. Kafumu. Kafumu yuko Wizara ya Nishati na Madini kwa hiyo hawezi kukwepa lawama za kuua sekta ya madini na kuwafanya Watanzania wawe masikini ndani ya nchi yenye rasilimali nyingi," alisema.
Alisema Dkt. Kafumu kashindwa kutetea hata wafanyakazi wa Tanzania wanaofanya kazi kwenye makampuni ya madini huku wakilipwa sh. 600,000 wakati wafanyakazi wa kigeni wakilipwa mamilioni ya fedha kwa kutumia dola.
Bw. Mtatiro alisisitiza kwamba Bw. Mkapa kama alivyo Kafumu wote ni sehemu ya uongozi uliofikisha sekta hiyo ya madini maali pabaya kwa muda mrefu na wamechangia kudhoofisha uchumi wa nchi, hivyo hawawezi kuwadanganya wana Igunga.
Bw. Mtatiro alimtupia tuhuma nyingine kwa kudai kuwa wakati wa uongozi wake hakuchukua hatua dhidi ya biashara zisizo salama na hatari kwa usalama wa urais Ikulu na nchi, ambapo alitolea mfano kashfa kama ya Meremeta, TANGOLD na Kiwira na kusisitza kwamba siyo msafi.
Alisema kuwa CCM ni wanafiki walimshinikiza Bw. Rostam Azizi ajiuzulu ati kwa sababu anahusishwa na ufisadi, baada ya Bw. Rostam kujiuzulu wanampeleka Bw. Mkapa kujenga heshima ya CCM.
Juzi Kamati Kuu y CCM ilimteua Dkt.Kafumu kupeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi mdogo wa ubunge jimbo hilo la Igunga katika kikao kilichofanyika chini ya Mwenyekiti Rais Jakaya Kikwete, ambapo kamati hiyo ilimteua Mwenyekiti Mstaafu wa CCM, Bw. Benjamini Mkapa kuzindua kampeni za uchaguzi huo.