Riwaya: Tutarudi na roho zetu?

Riwaya: Tutarudi na roho zetu?

TUTARUDI NA ROHO ZETU?
SURA YA KUMI
II
Baada ya Nuru kupigwa chenga ya mwili na Joram, kiasi fulani alipagawa, na hali hili iliwafanya makachero wamtilie shaka na kutoa taarifa haraka. "Bado yuko mbele yetu mzee...", haraka taarifa zilimfikia Von Iron ambaye wakati huo alikuwa ametulia ofisini kwake, mara kwa mara alisimama kuangalia saa yake ya mkononi. "...Tufanyeje mzee? Tumuue"... sauti iliendelea kusikika masikioni mwa Von.
"Nimesema mwacheni. msimuue kwanza", Von aliunguruma kupitia walkie volkie iliyokuwa mbele yake. "Mtakapopata nafasi nzuri akamatwe. Tunamtaka akiwa hai", Von aliongeza.
"Huyu msichana inaelekea kuwa anaweza kuleta madhara, mzee. Anaweza kuwa na silaha za hatari...", sauti hiyo iliendelea kushawishi.
"Unataka kuniambia kuwa wanaume wanne mlioshiba mnashindwa kumkamata malaya mmoja tu wa Kiafrika?", Von alihoji kwa sauti nzito.
"Si hivyo mzee. Lakini".
"Lakini nini?, mnachotakiwa kufanya ni kumleta hapa mbele yangu akiwa hai, ili atueleze wapi alikotorokea Joram Kiango. Mkishindwa kufanya hivyo nadhani hamtashangaa kwa lolote litakalowapateni", Von alimaliza na kuzima radio hiyo.
Taarifa za kuonekana kwa Nuru zilikuwa zimemfikia Von nusu saa iliyopita. Fununu zilizosaidia kuonekana kwa msichana huyu zilitokana na mtu aliyefia hospitali baada ya kuruka kupitia dirishani kwa maumivu ya kuchomwa kisu. Kabla ya kukata roho mtu huyo alifanikiwa kutamka kuwa alichomwa kisu hicho na msichana wa Kizungu mwenye lafidhi ya Kiafrika. Wakagundua kuwa mafanikio yote ya Joram yalitokana na hila za kujifanya Mzungu. Ndipo walipoanza upelelezi kwa njia nyingine. Na haukupita muda kabla msichana huyu aliyekuwa akipta mitaani hajatiliwa mashaka kwani haikuwa kawaida kwa wasichana wa kizungu kupita mitaani alfajiri kama hii. Ili kumbaini mtu mmoja alimsogelea ili kumsabahi. Majibu aliyotoa aliutia kasoro uzungu wake kutokana na lafidhi. Mwingine alimkaribia. Ajitia kukosea na kuugonga mkoba wake, kisha akainama mbio mbio kumsaidia kuokota, lakini akashangazwa na wepesi wa msichana huyo katika kuuokoa mboba wake. Alimtazama vizuri zaidi akaona dalili ya Uzungu bandia katika uso na mwili wake. Ndipo akaandamwa, bila ya yeye kufahamu, dakika yoyote akiwa tayari kupigwa risasi, endapo Von angeafiki...
Von hakuwa tayari kuafikiana na makachero hao waliojaa hasira na uchu wa kumwua Nuru. Hakuafiki kwa kuwa yeye pia alikuwa na uchu moyoni. Uchu wa kumpata Nuru akiwa hai. Uchu wa kuonja kile ambacho alikuwa ameambulia kushuhudia kwa macho tu. Ndio, kufa Nuru alikuwa hana budi. Lakini angeweza kufa baadaye. Hakuona sababu yoyote ya kufanya haraka.
"Bosi tayari tumemnasa... yuko mikoni mwetu". taarifa zilimfikia Von.
"Safi sana, mleteni kwangu". Von aliagiza.
Mara zikasikika purukushani katika chombo hicho cha mawasiliano. Zilifuatiwa na milio ya risasi tatu. Moyo wa Von uliodunda kwa hofu. Asingevumilia endapo msafara wa risasi hizo ungeishia katika mwili wa Nuru, kabla.
"Bosi, mchana huyu kamjeruhi mmoja wetu, turuhusu tummalize", alisema kiongozi wa makachero waliomkamata Nuru.
"Nimesema mleteni kwangu akiwa hai", Von aligiza kwa sauti ya msisitizo.
Mara chombo cha mawasiliano kikazimwa. Dakika chache baadaye mlango wa ofisi ya Von ukafunguliwa na kuruhusu msichana aliyekuwa akisukumwa kwa mitutu ya bastola nne, akaingizwa ndani ya ofisi hiyo huku akipepesuka. Alikuwa hai. Lakini jeraha la kisu katika mkono wake wa kulia, michubuko katika sehemu ya shavu, na uvimbe usoni vilidhihilisha kuwa Nuru alipigania uhai wake kwa gharama kubwa lakini hakufanikiwa.
"Ni msichana hatari sana, amemua watu wetu wawili", kiongozi wa msafara huo alieleza.
"Atajuta kuzaliwa...", lilikuwa jibu pekee la Von.
"Ni msicha jeuri mwenye kiburi, amegoma katakata kueleza habari za mwenzake".
"Ataeleza", Von alisema kwa kujiamini.
Makachero wakashangazwa na tabia hiyo mpya ya kiongozi wao Von. Alionekana kama siyo Von Iron waliyemzoea au kumjua. Von Iron wanayemjua angekuwa wa kwanza kutamka kwa ukali "Ua huyo", Na endapo kifo kisingetokea mapema Von Iron waliyemfahamu angekuwa akishuhudia ukali wa hali ya juu ukiendelea katika mwili wa msichana huyo jeuri Nuru. Msichana ambaye zlitisha hasa kwa jinsi ngozi yake bandia ilipoanza kubanduka hapa na pale kutokana na purukushani na kufanya mabaka ya ngozi yake ya asili yajitokeze kwa namna ya kuchekesha na kutisha kiasi.
"Sikilizeni", Von aliamru. "Huyu niachieni mimi. Nitajua la kumfanya. Fanyeni hivi, endeleeni kumsaka Joram Kiango, naamini atapatikana. Mkimpata huyo mtu namtaka vilevile. Hai au maiti. Sawa. Namtaka kumuona mbele yangu akiwa hai.
"Sawa, bosi", makachero waliomkamata Nuru waliafiki na kutoka ofisini kwa Von mmoja mmoja baada ya kutazamana kwa mshangao.
Walipobaki peke yao Von Iron alikiacha kiti chake na kumsogelea Nuru. Akamkazia macho yake makali. Mara akalazimika kuyainamisha macho hayo mara moja baada ya kuona kitu ambacho hakupata kukiona katika macho ya msichana yeyote. Kitu kisichoelezeka kwa ukamilifu. Kitu kama nuru ya aina yake ambacho kilifunua mapazia fulani na kuacha barabara ndefu inayoelekea kusikojulikana. Kilichomfanya Von ayaepuke macho hayo ni zile hisia za kutatanisha ambazo zilimjia ghafla zilimfanya ajihisi kama anayefuata barabara hiyo akielekea huko ambako hakujulikani, katika dunia nyingine inayotatanisha.
"Unazo habari kuwa maisha yako yamo mikononi mwangu?", Von alimuuliza Nuru. Lakini hakupata jibu, jambo ambalo lilimfanya ainue tena macho yake kumtazama Nuru.
Ile nuru ya kutisha, nuru ya ajabu aliyokuwa ameiona awali katika macho hayo haikuwemo tena. Badala yake Von alikutana na macho yale yale aliyoyategemea. Macho ambayo alitamani kuyaona. Macho ya msichana, yenye dalili zote za usichana. Mara Von akawakumbuka marehemu wazazi wake. Akakumbuka kuwa ni kitu fulani katika mambo ya msichana mweusi kama huyu ambacho kiliwafanya waondoke duniani kwa aibu na uchungu. Kitu ambacho yeye Von Iron alikuwa akikitumaini, ili akione na kukionja. Leo ilikuwa fursa ya pekee kwa Von kumtumia msichana huyu. Akaona hii ndio njia pekee kwake kumtumia msichana huyu kujua siri hiyo, kisha angemuua baadaye.
"Unatambua kuwa maisha yako yamo mikononi mwangu?", Von alirusia kuuliza swali.
Bado Nuru hakumjibu. Akaendelea kusimama pale pale alipokuwa amesimama, uchovu ukimsumbua, maumivu yakimtesa. Moyoni hasira kali ilikuwa ikichemka dhidi ya watu hawa. Hakuwa na woga wala shaka kuwa maisha yake yalikuwa ukingoni. Lakini si hilo lililomtia hasira. Hasa alisikitika kuona kuwa amekamatwa kabla ya kazi ya mwisho kukamilika. Japokuwa alikuwa na uhakika kuwa Joram Kiango alikuwa hajakamatwa, lakini aliamini kuwa ingekuwa haki yake kushirikiana na Joram bega kwa bega katika awamu ya mwisho kama walivyofanya ile ya awali. Kiasi vile vile alikuwa akijiuliza kama hakuwa amefanya makosa kwenda kinyume na matakwa ya Joram na kumfuata kwa siri badala ya kumsubiri kama alivyoagizwa. Nuru alijua wazi kuwa ni kitendo hicho ambacho kilikuwa kimemtia mashakani.
Hata hivyo Nuru hakuwa na hofu kubwa sana juu ya maisha yake. Hakuamini kuwa kifo kilikuwa karibu kiasi hicho. Mipango waliyokuwa wameiandaa yeye na Joram ilimpa matumaini kuwa itatokea fursa nzuri ambayo angepata upenyo na kutoroka hadi nchi jirani zilizoko mstari wa mbele. Imani hiyo ilijengeka katika moyo wake, wakati akifikiria hayo, mara akajikuta amezungukwa na makachero wenye silaha lakini wakiwa hawana dalili ya kuzitumia silaha hizo dhidi yake. Hata baada ya yeye kutoa bastola yake na kuua wawili kati yao, wao walifyatua risasi zao kwa dhamula ya kumtisha tu, akajua kuwa wanamtaka akiwa hai, ili wamlazimishe kutoa siri fulani. Hivyo hata alipozidiwa nguvu, baada ya kuvamiwa na kupigwa sana hakuwa na shaka sana.
Na hasa huyu mtu mnene aliyeonekana kama kiongozi wao. Huyu ambaye tamaa ya kimwili ilikuwa wazi katika macho yake. Kosa analofanya huyu la kumtamani lingeweza kabisa kusaidia kuyaokoa maisha yake na Joram Kiango. Nuru alichohitaji ni muda kidogo.
Suala hili la kupendwa na kuhitajiwa kimapenzi halikumshangaza sana Nuru. Maana alilitegemea. Kwani Joram alikuwa amemfafanulia kuhusu umuhimu wa nafasi hiyo pia walipokuwa kwenye maandalizi ya kuingia Afrika Kusini. Joram alikuwa amemwambia kwa lugha ya kishairi akisema kuwa "Katika silaha zote za mwanamke uzuri ni silaha ya kwanza", Akamweleza kinagaubaga nini cha kufanya inapobidi silaha hii kutumika. Hata walipokuwa wakifanya mapenzi kitandani kabla ya kukiharibu kile chombo chao cha kutazamia, Joram alikuwa amemnong'oneza, "Tutafanya kila kitu. Najua wanatutazama usione haya nataka ufanye utundu wake ili wapate homa ili endapo watatukamata, watamani kuyashuhudia waliyoyaona kwa vitendo. Nafasi ambayo natumaini kuwa hutashindwa kuitumia", Haya sasa nafasi hiyo imetokea... Nuru alijiambia kimoyomoyo. Kuwa nafasi ni hiyo aliyofundishwa jinsi ya kutumia silaha ya mapenzi.
Akayainua macho yake, akayalegeza kidogo, akaruhusu tabasamu dogo. "Najua kuwa nitakufa..." Nuru alimjibu Von kwa sauti ndogo ambayo kwenye masikio ya mwanaume ilitosha kuanzisha kongamano fulani baina ya mwili na damu.
Kufa hana budi lazima atakufa! Von alisema moyoni... Utakufa kifo kibaya. Lakini itakuwa baada! Kwa mdomo alisema. "Nimesema maisha yako yamo mikononi mwangu. Vitendo vyenu vilikuwa vya kinyama mno. Pamoja na kupokelewa vizuri katika nchi hii na kuahidiwa kuishi kwa amani na starehe, bado mkadiliki kufanya mambo yasiyoeleweka. Mnapita kuua watu wasiokuwa na hatia tena bila sababu yoyote. Naamini ulikuwa ushauri wa huyu mwendawazimu uliyefuatana naye. Unafahamu alikokimbilia?".
Nuru aliendelea kunyamaza, lakini baada ya sekunde kadhaa aliinua uso na kusema. "Sifahamu".
"Amekutoroka", Von alidakia, "Amekutoroka. Bila shaka wakati huu anajaribu kuitoroka nchi yetu. Hawezi kufika mbali. Bado kidogo atakamatwa na kuletwa hapa akiwa hai au maiti", Von alimaliza huku akiwa ametoa macho yake makali kwa Nuru. Macho yake yalikumbuka alichohitaji. Akazisahau hasira zake dhidi ya Joram na kumnong'oneza Nuru kwa sauti ambayo yeye ilimpa upendo. "Suala lako ni tofauti kabisa bi mdogo. Una nafasi nzuri ya kusamehewa dhambi zako iwapo tu... iwapo...
Von hakujua lipi amwambie Nuru. Hakuwa hodari wa kupambanua mambo, yaani kutongoza. Ingawa alikuwa amesoma riwaya nyingi za hadithi za mapenzi na ilikuwa vigumu sana kwake kujiweka wazi na kila alipotamani kuyaweka wazi aliyoyasoma katika hadithi hizo vitendo vilimshinda. Sababu moja kati ya nyingi zilizomfanya awe hana mke ni kutojua kuwajibika katika suala zima la kuwakabili wasichana. Wote aliowahitaji ilikuwa kama anawadhihaki huku akisubiri watasema nini. Wale ambao hakuwataka ndio walioonekana kumuhitaji na kujileta kwake kwa urahisi. Lakini leo kichwani akiwa hana hata tone moja la pombe hakuona vipi atampata Nuru. Akaduwaa akimtazama.
Nuru akauhisi unyonge huu akaamua kusubiri.
Dakika zilipotea kabla ya Von kuelewa aseme nini. Kisha alikumbuka kuwa alikuwa na akiba nzuri ya vinywaji vikali. Akafungua kabati na kutoa chupa moja ya John Walker ambayo aliimimina katika glasi. Alimkaribisha Nuru ambaye aliikataa. Akaimimina tumboni mwake. Glasi ya pili ilimchangamsha. Akarudisha vifaa hivyo kabati na kumsogelea Nuru akamgusa bega huku akinong'ona kwa sauti ambayo kichwani mwake alihisi kuwa imejaa mahaba. "Wewe ni msichana mzuri sana wa Kiafrika. Sijapata kumwona mwingine wa aina yako". Mkono wake ukagusa mahali ambapo ngozi ya bandia ya Uzungu aliyovaa Nuru ilikuwa imebandukabanduka kwa purukushani. Von akaishika ngozi hiyo na kuanza kuibandua. Gundi nyepesi iliyokuwa imetumiwa kuambatanisha ngozi hiyo ya nailoni na mwili iliacha mabaka meupe. Lakini nyuma ya mabaka hayo ulijitokeza uso mzuri, uso wa asili wa Nuru. "Wewe ni mzuri kama ulivyo. Huhitaji kabisa ngozi hii", Von alisema huku akiendelea kubandua ngozi hiyo sehemu za mapaja ya Nuru.
Sasa aliyekuwa amesimama mbele yake hakuwa tena msichana wa Kizungu. Alikuwa msichana wa Kiafrika. Msichana mzuri ambaye kila muda uzuri wake ulimpumbaza kaburu Von Iron. Kisha tamaa ikaanza kumzidi nguvu mikono yake ikapoteza utulivu na kuanza kutambaa katika mwili wa Nuru, Ulimi wake ukaanza kudai njia katika kinywa cha Nuru. Wakati huo Von alikuwa akitweta kwa nguvu huku akinong'ona maneno ambayo Nuru hakuyaelewa. Von hakutofautiana na sokwe mweupe aliyeonjeshwa asali.
Kile kitendo cha Von kilizidisha hasira katika moyo wa Nuru. Alihisi kama aliyeguswa na kinyaa mikono hiyo ilipoyafikia matiti yake na kuyachezea. Aliona kichefuchefu ulimi ulipokuwa ukibishana na meno yake ukutafuta njia ya kuingia mdomoni mwake. Ambacho Nuru alitamani kufanya ni kuitumia fursa hiyo kuachia pigo ambalo lingeondoa uhai wa Von na kisha kutafuta fursa ya kutoroka. Hata hivyo hakuthubutu kufanya hivyo, kwa kuchelea kuharibu mambo. Hakuwa akikoma kutazama saa kubwa iliyokuwa ukutani. Kila dakika iliyopita alikuwa akiisherehekea kimoyomoyo. Sasa ilikuwa imesalia kama saa moja tu kabla ya mitego waliyotega kuanza kufyatuka. Wakati huo asingekosa mwanya wa kutoroka. Kabla ya hapo Nuru alihitahitaji kuubembeleza muda kwa gharama yoyote: Isingegharimu chochote kuendelea kuliruhusu jitu hili nene liendelee kujipumbaza katika mwili wake. Mara moja mbili Nuru aliguna na kutetemeka kwa namna ya kumfanya aonekane kama aliyeshikwa na ashiki.
Kitendo hicho kiliongeza wazimu kwa Von. Mara akaanza kupambua mavazi ya Nuru. Mikono yake iliyokuwa ikitetemeka iligombana na vifingo vya mavazi hayo huku akinong'ona hili na lile.
"Sikiliza...", Nuru alieleza huku akiushika mkono wa Von na kuutoa mapajani mwake huku akiufinyafinya kwa mahaba. "Hapa ni ofisini. Mtu yeyote anaweza kuingia na kukatisha penzi letu...".
"Hii ni ofisi yangu", Von alikoroma. "Hakuna mtu anayeweza kuingia hapa bila ruhusa yangu".
"Sawa, lakini siyo vizuri".
"Tafadhali", Von alisema kisha akajilaumu kwa kutamka neno hilo. Vipi amtafadhalishe mtu mweusi? Tena mtu ambaye roho yake iko katika mikono yake. Akaupeleka mkono wake wa pili katikati ya mapaja ya Nuru tena safari hii kwa nguvu kidogo. Nuru aliyabana mapaja yake. Ndipo Von alipokumbuka kuwa haitakuwa kazi ndogo kumuingia msichana huyu kwa hiari yake. Hakuwa amezisahau zile picha za sinema ambazo huonyesha jinsi jasho linavyowatoka watu wanaojaribu kunajisi. Wala hakusahau yaliyoandikwa katika kitabu cha mapenzi alichowahi kukisoma zamani, ..."Hicho ni kitu pekee ambacho mwanamke ana mamlaka nacho mwenyewe..., kitu pekee anachoweza kujivunia... ni rasilimali yake pekee...", Hivyo Von akajikuta akilazimika kutumia njia nyingine.
"Una habari kuwa maisha yako yamo mikononi mwangu? Dakika yoyote nikiamua ufe utakuwa marehemu. Najaribu kukuokoa kwa sababu sioni kama unastahili kufa mapema kiasi hiki", Von alimweleza Nuru.
"Nitakuamini vipi kuwa hunidanganyi? Nitajuaje kuwa baada ya kumaliza shida zake hutaniua", Nuru alimwambia Von huku akimlembulia macho yake mazuri.
"Nakuhakikishia kuwa nitakulinda kwa uwezo wangu wote na utakwenda zako kwa amani na furaha tena utasindikizwa kokote utakakotaka kwenda" von alipoona Nuru hajamwamini kikamilifu kwa maneno na ahadi zake alimwacha kwa muda akaiendea kabati baada ya kulifungua alitoa bahasha kubwa. Ndani ya bahasha hiyo kulikuwa na pesa nyingi za mataifa mbalimbali. "Hizi ni pesa zenu. Ni miongoni mwa vitu vyenu mlivyonyang'anywa baada ya kufika hapa Afrika Kusini. Sasa nakukabidhi pesa hizi uwe nazo ili utakapoondoka hapa uweze kuishi nchi yoyote utakayopenda", Von alikabidhi bahasha hiyo kwa Nuru ambaye wakati huo alikuwa akichekelea moyoni, lakini Nuru akaamini kuwa mara baada ya Von kumaliza haja yake angeuawa na pesa hizo kurudi kwenye himaya ya Von.
"Sasa tunaweza kuendelea", Von alisema huku akianza upya kuuchezea mwili ya Nuru. Safari hii Nuru hakumzuia, lakini alikuwa katika mahesabu makali akiwaza na kutafakari atumie hila gani ili aendelee kumchelewesha.
Safari hii kilichomwokoa Nuru ni king'ora kilichotoa mlio wa aina ya paka aliyekabwa koo katika moja ya mitambo ya Von. Sauti hiyo ilimfanya Von aruke hadi kwenye simu na kuichukua kwa ajili ya kusikiliza kwa makini. Sauti nyembamba ilisema kwa wasiwasi.
"Bosi. Inaelekea kuwa tatizo kubwa katika mtambo maalumu. King'ora cha tahadhali kimekuwa kikilia kwa muda mrefu. Simu zote za askari wa zamu hazipokelewi".
"Imposble", Von alifoka. Unataka kunieleza kuwa maafa yanayotokea mjini yanaweza kuhamia huko nje ya mji?", Von aliuliza kwa shauku.
"Inaelekea ndivyo mzee. Kwa sababu huyu mtu anayeitwa Joram haelezeki. Anaweza kuwa yuko huko wakati huu.
"Imposble", Von alifoka tena, "Na kama kweli kaenda huko basi kajipeleka mwenyewe kwenye kifo na kaburi lake litakuwa huko, Von alisita kidogo. Kisha akasema. "Sikia. Andaa helikopita yangu na dereva. Nataka kufika huko mara moja. Nataka kushuhudia kwa macho yangu mwenyewe jinsi mtu huyo anayejiita Joram Kiango anavyosulubishwa.
UTAENDELEA 0784296253
 
Asante kk kwa kutuletea simulizi hii.wadau tupo wengi ila muda kaka tufupishie unatumia muda mrefu kuja kutuwekea simulizi hapa jamvini.samahani kama ntakuwa nimeeleweka vibaya.ila tunashukuru kwa hiki unachokifanya!.
 
asante mkuu, thank you (kwa msisitizo), usikawie tena mkuu.
 
Shukrani sana mkuu kwa kutusogezea tena simulizi hii, natumaini sasa haitakawia tena
 
[h=3]TUTARUDI NA ROHO ZETU
[/h]

SURA YA KUMI


III


Wakiwa angani ndani ya Helikopta, Nuru aliweza kuona vizuri baadhi ya maiti za makachero wa makaburu waliouawa huku wakiwa wamevalia sare pamoja na silaha zao mikononi. Walikuwa wamelazwa sakafuni mbele ya lango kubwa la kuingia katika mojawapo ya vyumba ndani ya jingo hilo lililozungukwa na ua wa seng'enge. Halikopta ililizunguka jumba hilo mara tatu. Von alikuwa akitumia darubuni kuona huku na huko. Aliporidhika na hali ya usalama, alimwamru rubani wa Helikopta hiyo kutua kando ya ua huo karibu na kichaka mahali ambapo mtambo huo ulikuwa kando ya mji.


Ilikuwa safari ya dakika mbili tatu tu, kutoka mjini hadi kufika kwenye mtambo huo. kabla ya kuanza safari hiyo Von alikuwa ametupiana maneno yasiyofaa na msaidizi wake ambaye alikuwa ameshangazwa na maamzi ya Von kuambatana na Nuru ndani ya Helikopta.


"Sikubaliani kabisa na uamzi huo. Nadhani ni wewe ndiye uliyetunga sheria hizi, kumpiga risasi mtu yeyote atakayeonekana akiusogelea mtambo ule, awe raia wa nchi hii ama mgeni. Vipi leo aende huyu mhalifu ambaye bado tunawatuhumu yeye pamoja na mwenzake ambaye yawezekana kuwa yuko huko akifanya mauaji ya siri kwa makachero wetu".


"Huyu ni mateka wangu", Von alimjibu. "Bado nina mengi ya kumsaili. Zaidi ya hayo kama kweli Joram yuko huko tutamtumia huyu kumfanya Joram asithubutu kuendelea na chochote anachowaza kichwani mwake", Von alitetea msimamo wake.


"Bado sikubali", Msaidizi huyo alisimamia hoja yake. "Nimeandaa kikosi cha askari wanne ambao ulipaswa kufuatana nao huko. Kadhalika nilikuwa nikisubiri amri yako ili nitume askari wengine zaidi ya hamsini kwa njia ya magari. Inaonekana yote ninayofanya ni kazi bure".


"Ni bure kabisa", Von alimjibu. "Unajua kabisa kuwa mtambo ule unalindwa katika hali isiyo na shaka kabisa. Hata kama mtu atafanikiwa kuingia ndani hawezi kabisa kufanya uhalibifu wa aina yoyote. Pamoja na juhudi zake zote bado ataambulia kufa tu. Hivyo nakushauri urudi na hao askari wako uliowaandaa. Nitakwenda mimi, huyu mateka na rubani tu. Sawa", Von alieleza kwa msisitizo.


Msaidizi huyo alimtazama Von kwa hasira na mshangao. Von hakuwa na kawaida hiyo. Alikuwa amezithamini sana hekima zake hususan katika masuala yote ya kiusalama katika nchi hii kwa kipindi chote, miaka yote walipokuwa wakifanya kazi ya kuilinda nchi yao. Lakini vitendo vyake masaa machache yaliyopita vilimchanganya kabisa. Vilikuwa vitendo ambavyo havikubaliki. Yeye kama mtu wa pili katika suala zima la usalama wa utawala huo hakuona kama kuna sababu ya kumtii Von hata kwa hilo. Hivyo alimtupia jicho la hasira na kumwambia, "Kwa mara ya kwanza nitafanya kinyume cha matakwa yako".


"Na kwa mara ya kwanza nakwambia kuwa... kuwa... Hufai kufanya kazi chini yangu. Baada ya suala hili nitaangalia suala lako", Von alisema huku akimsukumiza Nuru ndani ya Helikopta akamwamru rubani kuondoka haraka.


Hata hivyo moyoni Von alikuwa na mashaka kuhusu maamzi yake hayo. Alijua kabisa kuwa alikuwa akifanya kosa kubwa sana kufuatana na Nuru huko aendako. Lakini pia aliamini kuwa hiyo ilikuwa nafasi yake ya pekee kufanya mapenzi na msichana huyo na kisha amuue. Ndani ya jumba hilo la mitambo kulikuwa na vyumba kadhaa kikiwepo chumba maalumu kwa ajili ya faragha za wakubwa tu. Chumba hicho kilikuwa na mtambo wa televisheni inayotumia nguvu ya setilaiti iliyoko angani inayotumika kuitazama miji mbalimbali ya Afrika kwa umakini mkubwa. Vilevile kulikuwa na chombo maalumu ambacho kiliwawezesha makaburu kutazama shughuli zote zinazofanyika katika kila chumba ndani ya jumba hilo.


Ilikuwa kawaida kwa Von kujifungia ndani ya chumba hicho mara kwa mara kwa ajili ya kutazama utendaji kazi wa mitambo hiyo na jinsi wahandisi wanavyofanya kazi bila wao kujua. Mhandisi mmoja katika jumba hilo aliwahi kupoteza kazi na uhai wake baada ya kushukiwa na Von kuwa alikuwa na dhamila mbaya ya kuhujumu mtambo huo. Hata hivyo kifo cha mhandisi huyo machoni mwa watu ilionekana kama ajali iliyosababishwa na dereva aliyelewa na kumgonga mtu aliyekuwa akitembea kando ya barabara katikati ya mitaa ya Johannesburg. Leo Von alikusudia kukitumia chumba hicho kujistarehesha na mwili wa Nuru kabla ya kutulia na kuanza kuangalia kwa furaha watu wanavyoteketea kwa moto katika miji ya Dar es Salaam, Lagos, Lusaka, Harare na kwingineko.


Furaha iliyokuwa ikichemka katika fikra za Von iliingia nyongo baada ya Helikopta yake kupita juu ya jengo hilo na kushuhudia jinsi walinzi wa eneo hilo walivyolala hovyo wakiwa maiti baada ya kuuawa. Kutokana na hali hiyo, Von aliingiwa na hofu, akamtupia Nuru jicho la chuki. Tamaa aliyokuwanayo dhidi ya Nuru ikaanza kuyeyuka taratibu na nafasi yake kuchukuliwa na hasira kali. Von alitamani ammalize Nuru papo hapo ili kusahau yote aliyokuwa akihitaji kwake. Wazo jingine likamjia akilini kuwa. Kwa vile Nuru anaonekana katili sana asiyeogopa kifo kama walivyo wanawake wengine anaowafahamu. Hata hivyo Von akajipa moyo kuwa Nuru anaweza kufa baada ya kutaabika sana. Akaamini kuwa hakuna mateso yatakayomtaabisha zaidi ya kushuhudia kifo cha mpenzi wake Joram Kiango. Von akiwa na uhakika asilimia mia kuwa Joram alikuwa mahali fulani katika jengo hilo akilia na kusubiri kifo, Von alitoa bastola yake na kuigongagonga kwenye kisogo cha Nuru. Baada ya Helikopta kutua, Von alimwamru Nuru.


"Twende", Von alisema kwa hasira mara baada ya kushuka kutoka ndani ya Helikopta huku akimwamru rubani awe makini wakati akimsubiri.


Nuru alitelemka na kufuata maelekezo ya Von. Kila walikopita kulikuwa na miili kadhaa ya marehemu waliouawa hovyo, baadhi wakitokwa na damu baada ya kujeruhiwa kwa risasi zilizoingia miilini mwao.


Kiasi fulani ilimshangaza Von kuona jinsi mtu mmoja Joram Kiango peke yake alivyofanikiwa kuwaangamiza askari wengi kiasi kile bila wao kujitetea. Lakini hali hiyo haikumshangaza Nuru hata kidogo. Wala hakuhitaji kusimuliwa. Nuru akiwa mtu anayemfahamu vizuri Joram na hila zake nyingi alijua kuwa Komando huyo alitumia njia moja ama nyingine kuwafikia askari hao wa makaburu na kuwashikisha adabu pamoja na kujiamnini kwa kuwa na silaha za kisasa na bunduki aina ya sub machine gun.


Baada ya kufanya kazi yake ipasavyo Joram, akitoka kona moja kwenda kona nyingine katika ngome ya adui, Joram alifanikiwa kutoa hati zake za bandia na kuwaonyesha askari wa makaburu. Hati ambazo zilifungwa kwa namna fulani kiasi cha kuhifadhi hewa ya sumu ambayo bila shaka iliwafanya askari wa makaburu kulewa ghafla. Hivyo akawa na nafasi nzuri ya kuwaua mmoja baada ya mwingine bila kutumia silaha nzito.


Kilichomshangaza Nuru ni kutokufahamu Joram alikuwa wapi na akifanya nini muda wote huo tana katika eneo la hatari kama hilo. Nuru alikuwa amekadilia kuwa dakika tano zingetosha kabisa kuuteketeza mtambo huo na kutoweka. Na kwa mjibu wa ramani yao ndani ya jumba hilo hakukuwa na ulinzi wowote zaidi. Nuru akajiuliza vipi Joram asitokee na kummalizia Von. Mtu mnene, ambaye hakuwa na uwezo wowote wa kupambana na Joram. Nuru akaamini kuwa ndoto yao unakaribia kuwa kweli, akamuomba Mungu moyoni mwake ili wamalize kazi na kuondoka kurudi Tanzania.


Von hakumpa Nuru nafasi ya kuwaza zaidi. Alikuwa akimsukumasukuma kwa mtutu wa bastola yake haraka haraka. Nuru hakuwa mzito, mara moja alielewa kuwa Von alimtanguliza ili amfanye kuwa ngao yake endapo lolote lingewatokea tofauti na mategemeo yake. Baada ya Von kukagua baadhi ya vyumba vya jengo hilo, akiwa amemtanguliza Nuru kama kawaida, walifika katika chumba maalumu ambacho Von na viongozi wengine hukitumia kwa ajili ya mapumziko.


Ukiondoa makochi na kabati lililojengwa ukutani, chumba hicho hakikutofautiana na maabara au studio ya aina yake katika macho ya Nuru. Mashine na mitambo kadhaa ilikuwa imepangwa kwa tafasiri fulani, kutani kukiwa na screen zilizopangwa katika hali ya kupokea habari mbalimbali. Von aliiendea mashine moja ambayo machoni mwa Nuru ilionekana kama komputa, akaanza kubonyeza swich aina kwa aina mara kioo katika ukuta mmoja kilipata uhai na kuanza kuonyesha mambo ya ajabu. Baada ya hali kutulia Nuru aliweza kuona teknolojia hiyo inavyofanya kazi, waliweza kuona chumba baada ya kingine katika jengo hilo. Kupitia screen hiyo kilionekana chumba kilichokuwa na mitambo ya aina mbalimbali ya kutisha.


Nuru aliweza kuwaona wahandisi watatu waliokuwa makini wakifanyakazi ya kuongoza mitambo hiyo huku wakiwa hawana dalili zozote kuwa mambo yalikuwa yakienda mrama. Kitendo cha wahandisi hao kuwa makini na kazi yao kilimfurahisha sana Von, akaangua kicheko cha furaha. Ni yeye aliyependekeza kuwa ishara ya hatari kwa usalama wa mitambo hiyo zisiwafikie wahandisi hao wasije wakapatwa na hofu na kusababisha setilaiti iliyoko angani kukosa mawasiliano kutoka ardhini, jambo ambalo lingeweza kusababisha maafa na hasara isiyokadiliwa.


Kwa jinsi jengo hilo lilivyoandaliwa Von alikuwa na hakika kabisa kuwa ingemhitaji binadamu mwenye moyo wa malaika kuwafikia wahandisi hao na kufanikiwa kuuharibu mtambo huo. Aliamini kuwa Joram hakuwa na moyo huo. Ni hilo tu lililokuwa likimtia nguvu Von. Sasa akaamini kuwa hakuwa amekosea. Kwa muda aliwatazama tena wahandisi hao wanavyowajibika. Wakiamini kuwa leo ilikuwa siku maalumu ya kazi kubwa hivyo walifanyakazi zao kwa umakini na juhudi ya hali ya juu. Kisha Von alibonyeza kuona sehemu nyingine. Chumba hicho kikahama na vyumba vingine vikaanza kuonekana katika kioo.


"Nataka umuone mpenzi wako atakavyokufa ama mahali alikofia", Von alimwambia Nuru huku akimwelekezea tabasamu la kifedhuli lililoyasindikiza maneno yake, "Keti tafadhali. Keti hapa ili uweze kuona kwa starehe jinsi Afrika inavyoteketezwa kwa mioto ya ajabu".



ITAENDELEA 0784296253

cc. kigongoi, Jimena, Nemesis, Sangomwile, DavidHard, kidi kudi

https://www.jamiiforums.com/member.php?u=41512
 
Asante mkuu ntamaholo, kweli hujakawia, tafadhali usikawie kuleta kipande kinachofuata.
 
Ntamaholo umetisha sana mkuu,endelea kumwaga mambo bwana.
 
Mkuu asante kwa kutuletea simulizi ndani ya muda!na sisi tuenjoy simulizi za joram!
 
Siamini hii week end itaisha bila kupata muendelezo😀😀😀
 
kwa saa za Bongo ni saa 3 usiku, huenda weekend itamalizika bila bila.
 
Najuta kuifatilia hii riwaya.... Mana nimekuwa mtumwa na kila nikichungulia nakuta patupu
 
Back
Top Bottom