Riwaya: Tutarudi na roho zetu?

Riwaya: Tutarudi na roho zetu?

SURA YA NANE

II

Kwa Afrika Kusini ilikuwa kama nafasi ya dhahabu. Vyombo vyote vya habari nchini Afrika Kusini viliandika na kushangilia kwa nguvu kuwasili kwa Joram na Nuru katika nchi yao. Waliipamba habari hiyo kwa maandishi makubwa na kuyatia chumvi nyingi juu ya wizi wa pesa za umma. Walieleza jinsi alivyopokonya pesa hizo, alivyozitumia kwa starehe sehemu mbalimbali ulimwenguni, alivyofaulu kuwalaghai polisi wote duniani, na mwisho alivyoona hana hila tena zaidi ya kukimbilia Afrika Kusini, ili ajisalimishe na kujificha maisha.

"Huu ni mfano hai kwa watu weusi kote ulimwenguni", alieleza mtangaji mmoja wa televisheni. "Hakuna asiyemfahamu huyo Joram Kiango. Alijifanya mpigania haki, usawa na usalama wa watu weusi. Amesababisha vifo vya watu wengi ambao walikuwa na nia njema ya kuzikomboa nchi zao. Ndivyo walivyo watu weusi wote. Wanawalaghai wenzao na kuwafanya wote waote mikia misituni eti wakidai haki na uhuru. Matokeo yake ni kuwafanya, hao wenzao, kuwa vijakazi wakati wao wakitunisha matumbo yao mara baada tu ya kupata madaraka. Natumaini weusi wote mnaodanganywa mtaitumia nafasi hii kuuona ukweli wa mambo. Bila hekima na uongozi wa mtu mweupe Afrika ingekuwa bado gizani, na endapo ataondoka mtu mweupe Afrika giza litarudi...".

Hayo yalisemwa baada ya watu kuwatazama Joram na Nuru wakitoka katika ndege waliyoiteka kuwaleta Afrika Kusini, huku wakiwa wametanguliwa na rubani ambaye walikuwa wamemshikia bastola. Nje ya ndege Joram aliitupa chini bastola yake na kuweka mikono yake juu. Ndipo Polisi wa makaburu waliokuwa wameuzingira uwanja wakiwasubiri, walijitokeza na kuwakamata na kuwakagua haraka haraka. Walipoona hawana silaha nyingine zaidi ya ile iliyotupwa waliwaongoza hadi kwenye gari lililokuwa likiwasubiri. Muda wote huo kamera za waandishi wa televisheni na zile za wapigapicha wa magazeti zilikuwa zikiwaelekea Joram na Nuru kwa ukamilifu. Kama kuna chochote kilichowashangaza watazamaji ni jinsi sura za vijana hawa zilivyoonekana tulivu, nzuri, zisizo na dalili zozote za ugangwe kama walivyotegemea kuwaona.

Msafara wa gari lililowabeba uliishia katika jumba moja kubwa lenye ghorofa kadhaa. Humo baada ya lifti waliyoingia kuwapandisha juu walijikuta katika chumba kilichoelekea kuwa maalum kwa ajili ya kuhoji mateka. Askari waliokuwa nao waliamuru kusubiri, kisha wakatoka zao na kuufunga mlango nyuma yao. Baada ya muda waliletewa chakula na vinywaji. Wakala na kunywa.

Baada ya muda kama walivyotegemea, walianza kutembelewa na maafisa wa upelelezi, ambao waliwauliza maswali kemkem. Maswali yote Joram na Nuru waliyajibu kwa ukamilifu kama walivyojiandaa; kwamba walikuwa wameishiwa na hila za kuwakwepa INTERPOL wakaona hawana njia nyingine zaidi ya kukimbilia Afrika Kusini ambako wangepata hifadhi. Baada ya maswali yalifuata mawaidha na badala ya mawadha ikawa kashfa.

"Wewe kama Joram Kiango ambaye nchi yako na Afrika nzima ilikutegemea huoni aibu kufanya ulivyofanya na kumbilia huku Afrika Kusini?"

"...Utajisikiaje utakapolazimika kufuata matakwa yote ya ubaguzi wa rangi na kulazimika kushuhudia Waafrika wanavyonyanyaswa?", Joram aliulizwa.

"...Unaweza kukiri hadharani kuwa viongozi wote wa Afrika ni wadanganyifu na hawajui watendalo?", lilikuwa swali lingine la maudh kwa Joram.

"...Ukipewa bastola ili umuue mpigania uhuru yeyote atakayematwa utafanyaje?", aliulizwa kwa mara nyingine.

"...Huyu msichana na uzuri wake wote ni malaya?, mbona anakubali kuandamana na mwizi".

Yalisemwa mengi zaidi ya hayo. yapo ambayo Joram aliyajibu kwa namna ambayo alijua kama walitegemea atajibu. Mengine hakuyajibu, akijua kuwa walimtegemea kutojibu. Mengine ilimlazimu kuinama kwa haya wakitarajia kuwa aone aibu. Baadhi ya maswali haya aliyakwepa kijanja akijua ni mitego iliyokusudiwa kumnasa.

Kutoka hapo walipelekwa katika chumba ambacho kilikuwa na mitambo mingi ambao eti ingeonyesha kama walikuwa wakisema ukweli au la. Waliwekwa katika mitambo hiyo na kuanza kuulizwa tena maswali. Yote hayo Joram alikuwa ameyafafanua kwa Nuru kabla hawajaondoka Paris kuelekea Kinsasa Zaire ambako waliiteka nyara ndege ile ya kukodi. Alimweleza kuwa ambacho mtambo kama unaweza kuonyesha ni dalili za moyo kudunda na damu kuchemka mara unapoulizwa swali ambalo litakushitua au utakapobuni uongo. Hivyo endapo utazungumza kwa kujiamini haitaonekana dalili zozote.

Ndivyo ilivyotokea. Saa chache baadaye walikuwa wamechukukuliwa na gari kutoka katika chumba hicho na kupelekwa katikati ya maji ambako waliingizwa katika nyumba moja kubwa na kuelekezwa katika chumba kilichokuwa na vitanda viwili. Humo walikuta mizigo yao yote. Ingawa mizigo yao ilikuwa kama ilivyokuwa, Joram hakusita kugundua kuwa tayari ilikuwa imekaguliwa kwa ukamilifu. Hilo alilithibitisha baada ya kufungua na kukuta kila kitu kimo isipokuwa furushi la pesa zilizokuwa zimesalia. Hilo pia alilitegemea. Hivyo hakubabaika. Akamwendea Nuru na kumvuta mkono akimwelekeza kitandani ambako alimketisha ili ampumzike kidogo.

"Pole", Joram alimwambia Nuru.

"Kwa".

"Usumbufu".

"Mbona bado sijasumbuka. Naamini huu ni mwanzo tu, kuna mengi yanayokuja na nitakuwa tayari kuyakabiri yote...".

"Shii", Joram alimnyamazisha. Usijisikie huru kiasi hicho", alinong'ona. "Bado tuko chini ya ulinzi mkali. Yawezekana wanatutazama na kutusikia. Kiswahili si lugha ngumu kiasi hicho. Endelea kujihadhari".

Moyoni Joram alikuwa na sherehe kubwa. Alikuwa akishangilia mafanikio ya msafara huo ambao ulienda kama alivyokusudia kuelekea kuzaa matunda. Kufika Afrika Kusini na kupata mapokezi yenye hadhi kwa kiwango hiki ilikuwa jambo pekee la pili ambalo alilihitaji sana. Jambo la awali ambalo alihakikisha limefanikiwa kabla hajabandua mguu wakekuiacha dunia huru na kujitosa jehanamu kiasi hiki ilikuwa kulisafirisha sanduku lake ambalo lilikuwa na kila kitu alichohitaji katika jukumu lililokuwa mbele yake. Kati ya vitu vilivyokuwemo ni pamoja na pesa za matumizi muhimu, silaha aina aina, madawa ya kila aina, ramani mbalimbali, ngozi na sura za bandia ambazo zingemfanya aonekane mtu mweupe, na zaidi ya yote ni vile vijigololi maalumu ambavyo alivipata kutoka kwa hayati Chonde.

Ilikuwa imemgharimu uongo mkubwa na pesa kuweza kulifikisha sanduku lile katika nchi hii. Alikuwa ametumia hila za kumwendea mfanyabiashara wa Kimarekani ambaye alikuwa akisafirisha mizigo yake moja kwa moja kutoka Ufaransa. Baada ya kujijenga kwake kwa urafiki bandia alimhadaa kuwa amepata oda ya kuuza madawa ya kulevya nchini Afrika Kusini. Mmarekani huyo alikataa kabisa kujihusisha kwa hali yoyote katika biashara ya aina hiyo. Joram alikazimika kumpigia magoti kwa maneno huku akimpa pesa nyingi na kumwahidi sehemu kubwa ya faida. Ndipo sanduku hilo liliposafiri pamoja na mizigo mingine muhimu ya Joram. Na aliarifiwa kuwa sanduku hilo limefika salama. Ilimpendeza sana Joram kuona kati ya watu wengi waliokuja kiwanjani kushuhudia wateka nyara hao wakitelemka kutoka ndani ya ndege, mmoja wao alikuwa Mmarekani huyo aliyeitwa Moore. Ilimpendeza zaidi kuwa Moore hakuweza kufahamu kuwa mteka nyara huyo ndiye yule aliyekuwa rafiki yake siku tatu zilizopita nchini Ufaransa. Joram akiwa amekariri ramani ya nyumba ya Moore kama anavyovifahamu viganja vyake vya mkono, alikuwa akiisubiri kwa kiu kibwa fursa ya kuweka mikononi mwake mizigo yake.

Kabla ya kuoga kama alivyohitaji kufanya, Joram alijitia shughuli na kufanya kama anayepanga vitu chumbani kwake vizuri. Alichokuwa akifanya hasa ni kitu au vitu fulani na haukupita muda kabla ya kukiona alichokuwa akitafuta. Kipande kidogo sana cha kioo kilichokuwa kimejitokeza sakafuni katika pembe moja ya chumba kama kilichosahauriwa na waashi kwa bahati mbaya. Joram alijua kuwa nyuma yake kipande hicho kulikuwa na nyaya ambazo zilisafiri hadi kwenye mtambo ambao ulikuwa na jukumu la kupeperusha kila wanachoongea au hata kuwaona. Baada ya kuona hayo Joram alilidhika, akijua kuwa alikuwa hana haraka ya kuwa msiri. Alihitaji faragha kwa usiku mmoja tu, na katika usiku huo alijua ambacho angefanya kuufanya mtambo huo ushindwe kuwajibika kwa dakika kadhaa.

Wakaoga.

Wakalala.
 
Nilivyoona m2n tuu nikajua kitu hicho chaja. Kazi njema
 
Joram na nuru ndani ya Africa kusini na tayari kijana ashatambua mtambo wa kuwafuatilia hapo patamu mnoo
 
Sasa nijikumbushe nilipoishia ili niendee kuisoma, natumai M2n ataimalizia week end hii
 
SURA YA NANE
III
Jasho jembamba lilikuwa likiwatoka
maofisa wanne wa Boss ambao walikuwa
katika chumba fulani wakiwashuhudia
Joram na Nuru walipokuwa wakifanya
mapenzi katika chumba chao. Maofisa hao
walikuwa wamekaa katika chumba hicho
kwa muda mrefu, dhamira yao kuu ikiwa
kupata hakika kama kweli Joram alikuwa
hana hila nyingine iliyomleta Afrika Kusini
zaidi ya ukimbizi. Taarifa za maofisa wote
waliotumwa kuwahoji na ambao walikagua
mizigo yao haikuonyesha hila wala ila
yoyote. Hata hivyo upinzani uliokuwepo
uliishia kuamuliwa kuwa wapewe chumba
hiki na kuachiwa uhuru kiasi fulani ili
waendelee kuchunguzwa. Chumba hiki
kilikuwa maalumu na siri kubwa isipokuwa
kwa maofisa wachache wa ngazi za juu.
Ndipo jukumu la kuwatazama Joram na
Nuru likawaangukia kaburu Von Iron na
wenzake.
Ndipo walipolazimika kutokwa na jasho.
Kwani walikuwa wakitazama kwa namna
moja ilikuwa kama picha ya kupendeza
sana, kwa maaana nyingine picha ya
kuchukiza, inayotesa na kuadhibu.
Ilikuwa picha ya kupendeza wakati
walipokuwa wakiwatazama Joram na
mpenzi wake Nuru walipokuwa
wakitazamana kwa mapenzi pindi wakati
wakijiandaa kulala. Ikaanza kuchukiza
walipoanza kuvua mavazi yao na kuketi
kama walivyozaliwa huku wakibusiana. Na
ilianza kutesa walipojibwaga kitandani na
kufanya mapenzi kiroho mbaya bila kujali
au kujua kama wanatazamwa, kana
kwamba walikuwa wakiwaonyesha
watazamani kwa makusudi.
Von Iron aliuzima mtambo huo na kulifuta
jasho lililokuwa katika paji lake la uso.
Hakujiamini kuwatazama wenzake
machoni, akihofu wasije wakasoma kitu
alichokuwa akikisoma akilini. "Tukutane
kesho..." Von aliamuru akianza kutoka nje.
Bila kuinua macho aliweza kuhisi kuwa
wenzake walikuwa wakimhurumia zaidi ya
walivyokuwa wakijihurumia wao. Alijua
vilevile kuwa wenzake hao walijua kama
alivyojua yeye kuwa baada ya kuagana
nao angerudi katika chumba hicho.
Alirudi.
Akiwa peke yake aliwatazama kwa makini
na uhuru zaidi, akisherehekea kila hatua
iliyofuata katika mapenzi yaliyokuwa
yakiendelea mtindo mmoja juu ya kitanda.
Tangu alipokuwa amewaona Nuru na
Joram katika televisheni hajua kuwa
wangeweza kuwa wazuri kiasi hiki.
Kadhalika hakutegemea kuwa Mwafrika
aliyevua nguo angeweza kuwa kiumbe
mzuri kama hawa, aliwategemea kuwa
viumbe wa kutisha sana kama mizimu.
Kumbe sivyo.
Aliendelea kuwatazama. Alijipinda na
kujinyoosha kwa maumivu na tamaa
kubwa huku mkono wake mmoja
akiubembeleza uume wake, mkono wake
wa pili ukiwa umelea kichwa kwa wivu wa
masikitiko. Starehe au mateso yake
yalikoma Joram alipozima taa.
Von alijifariji kwa kuizima mitambo hiyo
na kubonyeza ile ambayo ilimfanya akague
ulinzi na usalama wa ule mtambo wa
nyuklia unaoendesha Satilaiti maalumu
iliyoko angani ikisubiri kufanya kazi
ambayo haitafutika katika kurasa za
historia ya dunia. Aliuona ulinzi
ulivyokuwa makini. Askari wanne wenye
machine guns walikuwa wakipita kwa
zamu kulikagua jengo hilo. Ndani mafunzi
wenye silaha walikuwa machio wakikagua
mwenendo wa mtambo huo kwa umakini
na uangalifu mkubwa. Von aliweza kuona
katika screen kubwa iliyokuwa mbele ya
wanasayansi hao jinsi setileiti hiyo
ilivyokuwa ikielea huku na huko katika
bahari ya Hindi kando ya pwani ya Afrika
Mashariki. Alitabasamu kidogo
alipojikumbusha utaalamu wa hali ya juu
uliotumika katika kuunda chombo hicho
hata kisiweze kuonekana kwa macho ya
kawaida.
Kisha alibonyeza mahali fulani kuondoa
mtambo huo machoni kwake. Badala yake
alibonyeza mahali ambapo palimwezesha
kuona gereza la ardhini ambamo kulikuwa
na mateka au wafungwa ambao walitakiwa
kuteswa hadi kufa. Humo kulikuwa na kila
aina ya mateso. Haikuwepo njia yoyote ya
kuweza kutoka isipokuwa kwa funguo
maalumu ambazo alidhihifadhi yeye
mwenyewe.Von aliwatazama wafungwa au
mateka hao waliokuwa wakikaribia kufa.
Baadhi yao walikuwa weupe, Mmarekani
mmoja ambaye alikuwa mpumbavu kiasi
cha kuamua kuwasaidia wapigania haki wa
Afrika Kusini, pia walikuwepo Warusi
wawili ambao pia tabia zao hazikuwa
tofauti na mzungu huyo pamoja na watu
weusi watatu. Ni hawa watu weusi ambao
walimfanya Von aangue kicheko kwa sauti.
Alijiuliza walikuwa wamepatwa na nini
weusi hawa hata wakathubutu kujileta
wenyewe huku kama wapumbavu. Mtu
atajipeleka jehanamu na kutegemea
atatoka salama?
Zimesikika habari nyingi za watu ambao
waliwahi kufa na baada ya siku kadhaa
kufufuka. Watu hao hudai kuwa
walipokuwa wafu wamefika peponi na
kuwaona malaika. Haijawa kutokea hata
mtu mmoja ambaye aliwahi kwenda
jehanamu na akarudi duniani. Hawa weusi
aliwaona kama watu walipenda sana kufa
vifo vya kikatili. Jambo la kusikitisha kwao
ni kwamba BOSS iliarifiwa tangu
walipoondoka Naijeria na Tanzania na kuja
Botswana. Iliarifiwa pia walipoanza mbibu
za kuvuka mpaka. Hivyo hila zao za
mmoja kujifanya wendawazimu asiyejua
analofanya na mwingine kujitia mkimbizi
anayeishi kambi ya wapigania uhuru
hazikuwa na mafanikio yoyote. Von
hakupenda kuwaona ana kwa ana.
Aliamua wafungiwe katika chumba cha
mauti wasubiri kifo. Hawa walikuwa wawili
tu kati ya wanane ambao walikuwa
wamekamatwa siku mbili zilizopita. Wawili
walikuwa wameuawa kwa mateso wakati
wakihojiwa. Mmoja alikuwa amejiua
mwenyewe kwa sumu baada ya kumvamia
askari aliyekuwa akimhoji na kumjeruhi
vibaya kwa kisu kabla hajameza vidonge
ambavyo vilimuua mwenyewe.
Wapelelezi hawa walikuwa ni matokeo ya
juhudi za kuthibitisha uwezekano wa
kuwepo kwa mtambo maalumu
unaoziadhibu nchi za Kiafrika. Von
alifahamu kuwa bado wangekuja wengi
zaidi, weupe kwa weusi, lakini kamwe
wasingefika popote pa haja. Na kamwe
wasingefika popote kwani zilikuwa
zimesalia siku mbili tu kabla ya Afrika huru
kuipigia magoti Afrika Kusini na kusubiri
vilio na maombolezo yasiyo na mfano. Von
alicheka tena, safari hii kwa kujipongeza
akijua kuwa sifa ndogo kuwa na wadhifa
kama aliokuwa nao sasa. Roho za watu
wengi kuwa mikononi mwako zikisubiri
tamko lako kabla ya kuteketezwa!
Kisha Von aliufunga mtambo huo na
kurudi nyumbani kwake. Akiwa kapera
ambaye hakujua lini angeoa alijikuta
akikosa usingizi alijikuta akimfikiria Nuru
na kumwonea Joram wivu. Bila kufahamu
anachokifanya Von alijikuta akiapa kwa
jina la Mungu kuwa asingekufa kabla
hajamuonja. "Mara moja tu..." alijiambia.
"Nione wana nini wanawake weusi..."
Kesho yake aliamuru Joram na Nuru
waletwe katika ofisi yake. Akiwa
amezungukwa na wasaidizi wake Von
alijitahidi kuwatazama Joram na Nuru kwa
namna tofauti kabisa na ile iliyokuwa
ikipita katika akili yake.
"Sina haja ya kuwahoji chochote", Von
aliwaambia kwa sauti nzito. "Kwa kiasi
mlichohojiwa naamini mmeonyesha kuwa
mmechoshwa na upuuzi wa hawa viongozi
wanaojiita wanamapinduzi katika nchi
zenu. Sivyo?"
"Kwa maana hiyo mngependa kuishi huku
daima. Msimamo wenu ni wa kishujaa.
Nawapenda watu shujaa. Ni hilo ambalo
limenisukuma kuwaacha hai pamoja na
kuwapa heshima ya kuwaita hapa ili
niwape habari njema".
Joram akiwa amesimama mbele yake,
akiwa kamshika Nuru mkono, hakuwa na
haja ya kuambiwa huyu ni nani katika nchi
hii. Alimfahamu mara moja kuwa alikuwa
mkuu wa shirika la kijasusi la utawala huu.
Kwa maana nyingine alikuwa adui yake
namba moja. Mtu ambaye asingeondoka
bila kumpa adhabu ya risasi ya kichwa
kwa hatia ya kusababisha maafa kwa
Waafrika wengi wasio na hatia. Hata hivyo
Joram hakuonyesha dalili yoyote katika
macho yake alipouliza kwa upole, "Habari
njema ipi? Tumeruhusiwa kupewa uhuru
zaidi ya huu tulionao? Tunajiona kama
ndio tuko kifungoni".
"Mko huru kuliko mnavyostahili", Von
alimjibu Joram. "Habari njema niliyotaka
kuwapeni ni juu ya uhalibifu ambao
utazitokea nchi za Kiafrika kesho saa nne
mchana endapo hawatawatuma viongozi
wao hapa leo kuweka saini mikataba ya
kuwa watiifu kwa utawala huu na
kutothubutu kuwasaidia wendawazimu
wanaodai uhuru wa Namibia na haki hapa
Afrika Kusini. Kama hawatafanya hivyo
hadi saa tatu na nusu za mchana. Nyie
mtapewa heshima ya kushuhudia moja
kwa moja Ikulu zinavyoungua, majengo
yanavyoteketea na watu kupoteza maisha.
Mtabahatika kushuhudia jambo la
kupendeza. Jambo la kihistoria".
Macho yake yaliwatazama Joram na Nuru
kwa umakini. Nao wakifahamu kuwa kuna
kitu kilitakiwa kuonekana katika macho
yao, Joram aliruhusu tabasamu kidogo
huku Nuru akifuta machozi.
"Ni habari njema", Joram alisema polepole
baadaye akauliza. "Habari njema...,
tunaweza kuruhusiwa kurudi chumbani
kwetu?".
 
aisee imetulia niliianza jana naskitika imegota hapa. huwa inarushwa muda gani?
 
Hata kama ni mateso haya yamezidi jamani....
 
Back
Top Bottom