Riwaya: Penzi chungu

Riwaya: Penzi chungu

SIMULIZI... PENZI CHUNGU
MWANDISHI.. HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 46

"Ni nini hii afande ?" Veronica Baro aliuliza kwa hamaki.
" nimekwambia ondoka! Au unataka kulala ndani?"
Veronica aliushangaa sana uamuzi ule wa Inspekta Jasmine.
Lakini hakuwa na jinsi, alitoka nje ya kituo kile kikubwa cha Polisi akiwa na wasiwasi mwingi.
Alisogea mbele kidogo ya kituo, alikodi teksi iliyokuwa inampeleka nyumbani kwake.
Ilivyotoka tu ile teksi, na gari nyingine iliyokuwa imepaki pale pembeni kituo cha Polisi nayo iliifuata teksi ile, na kuanza kuifuata ile teksi aliyopanda Veronica Baro. Bila kutambua kama anafuatwa Veronica alitulia katika siti za nyuma za ile teksi.

Dereva wa gari lile likilofuata nyuma ile teksi aliyopanda Veronica Baro alikuwa makini sana. Akihakikisha hatoi nafasi kwa ili gari ya mbele aliyopanda Veronica Baro kujua kama inafuatwa kwa nyuma. Na alifanikiwa kwa hilo.

Teksi aliyopanda Veronica Baro ilipaki katika Mgahawa. Na ile gari ikiyofuata kwa nyuma ilipaki kwa mbali kidogo. Dereva wa gari lile alimshuhudia Veronica Baro akishuka katika ile teksi, na kumuona akimlipa ujira wake dereva wa teksi ile.

Yule jamaa alikuwa ametulia tuli katika sukani ya ile gari. Akiangalia kila hatua aliyokuwa anapiga Veronica Baro. Alimshuhudia Veronica Baro akiingia kwenye ule Mgahawa baada ya kumlipa dereva wa teksi. Veronica Baro alitulia katika meza moja iliyokuwa pembeni ya Mgahawa ule.

Ilichukua muda mfupi, Mhudumu wa ule mgahawa alikuja na Veronica aliagizia kinywaji aina ya red bull, aliletewa na yule Mhudumu kwa kasi ileile, wahudumu walikuwa wanaijua sana kazi yao. Veronica alitulia na kuanza kunywa taratibu ile red bull.

Kule nje, yule jamaa alishuka katika ile gari. Kigiza mwanana cha saa moja kilikuwa kinaanza kuingia, kigiza ambacho kilimsaidia yule jamaa asionekane kabisa na macho ya Veronica Baro. Yule jamaa alichagua kiti kimoja kilichokuwa mbali kidogo na kile kiti alichokaa Veronica, naye akakaa. Mhudumu alienda kumulizia huduma anayoitaka, jamaa aliagiza maji makubwa ya Kilimanjaro. Akawa akayafungua na kuyaacha wazi bila kuyanywa.

Veronica Baro alikuwa hajatulia kabisa. Akiangaza macho Huku na huko, akaona kuna usalama, alitoa simu yake na kuiweka sikioni, aliongea kama dakika tano. Alimaliza na kuiweka simu yake katika mkoba mdogo mweusi. Akaichukua ile red bull yake na kupiga funda refu sana, ilimparia kidogo na nyingine kudondokea katika T-shirt yake nyeupe aliyokuwa ameivaa. Fulana Iliyoandikwa kwa mbele kwa maneno yaliyokolezwa kwa wino mweusi, DUMIZI.

ITAENDELEA
 
SIMULIZI...PENZI CHUNGU
MWANDISHI..HALFANI SUDY
SIMU: 0757 633010

SEHEMU YA 47

Macho ya yule jamaa yalikuwa makini kuangalia katika mlango wa mgahawa ule. Ukimtathmini kila mtu anayeingia ndani ya mgahawa ule.

Kule nje nako pikipiki kubwa aina ya Baja ilipaki katika Mgahawa uleule, waliokuwemo Veronica Baro na yule jamaa. Katika ile pikipiki alishuka kijana mmoja, mrefu wastani, mwenye mwili wa kimazoezi. Alikuwa amevaa T-shirt nyeusi yenye mistari meupe mabegani na suruali ya bluu aina ya jeans.

Kijana huyo aliyeshuka kwenye pikipiki, kwa majina alikuwa anaitwa Daniel Mwaseba.
Kumbe yule dereva teksi aliyopanda Veronica Baro alikuwa shushushu wa jeshi la Polisi. Aliyewekwa kwa lengo maalum.
Wakati anarudi njiani alimpigia simu Daniel na kumuelekeza mahali alipomuacha mwandishi yule wa kike. Moja kwa moja Daniel aliwasha pikipiki lake na kuelekea katika Mgahawa ule. Alishuka katika lile Baja na kuingia katika mgahawa ule. Alielekea upande ule ule alioelekea yule jamaa aliyekuja awali.
Upande ule ulikuwa mzuri zaidi kwa mtu anayetaka kujificha. Yule jamaa na Daniel walikaa sehemu tofauti kwa meza kama tatu.
Ilikuwa inakaribia saa mbili usiku sasa.
Wote wawili wakiwa kwa mbali walimwona Veronica Baro akiangalia saa yake mara kwa mara. Ishara kuwa akitarajia mtu ama watu mahali pale.

Masaa matatu yalipita. Watu wale watatu walikuwa wamekaa vile vile. Hakukuwa na mgeni yeyote wa Veronica Baro aliyewasiri.

Mara, Veronica Baro alisimama na kuelekea nje ya mgahawa, huku akiiangalia simu yake, bila shaka akisoma ujumbe fulani. Daniel na yule jamaa nao waliinuka kwa muda tofauti katika viti vyao, walitoka nje nao. Lakini kule nje hawakumuona Veronica. Kila mmoja alijaribu kuangaza lakini Veronica hakuwepo kabisa.
Veronika Baro alikuwa ametoweka !

ITAENDELEA
 
SIMULIZI.. PENZI CHUNGU
MWANDISHI..HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 48

Daniel ndiye alikuwa wa kwanza kugundua kuwa, walikuwa wanamtafuta mtu mmoja yeye na yule jamaa. Daniel alimsogelea yule jamaa taratibu.

"Habari yako" Daniel alimsalimia yule jamaa huku akimwangalia kwa umakini mkubwa.
"Safi kaka, mambo?"
"Safi, samahani kaka mimi naitwa Daniel, Daniel Mwaseba..." Yule jamaa alimtolea macho Daniel kusikia jina hilo. Bila shaka hakutegemea kulisikia katika maisha yake.
"Mimi naitwa Bruno" Bruno alijitambulisha kwa sauti ya uwoga kidogo.
"Nimekuona umetoka nje kwa kasi, bila shaka ulikuwa unamfuata yule mwanamke?"
"Ndio Daniel, namsaka veronica Baro, namsaka nimuue!" Sasa sauti ya woga toka kwa Bruno ilipotea, aliongea akimaanisha.
"Umuue, kwanini umuue Veronica Baro Bruno?"
"Veronica Baro ni mwandishi wa habari mahiri sana, lakini mahiri pia kuitumia kalamu yake vibaya, ndio! anaitumia vibaya sana kalamu yake, ingawa watu wengi hawajui"
"Kivipi Bruno ? Sijakuelewa kabisa yaani"
"Hapa siyo sehemu nzuri ya kuongelea hili. Ni hadithi ndefu sana, hatuwezi kuiongea tukiwa tumesimama namna hii, turudi mgahawani nikakusimulie"

Daniel na Bruno walirudi tena katika ule mgahawa.

"Ee hebu nambie vizuri unavyomjua mwandishi Veronica Baro" Daniel alichokoza.
"Ni hadithi ndefu sana kama nilivyokwambia awali Daniel. Hapo mwanzo nilikuwa namsikia tu Veronica Baro. Nikimtambua kama mwandishi wa habari mahiri sana Tanzania. Mwandishi wa habari wa kumtolea mfano miongoni mwa waandishi katika fani hiyo. Nilikuwa sijui kabisa upande wa pili wa Veronica Baro. Nilianza kumjua vizuri zaidi Veronica baada ya mpenzi wangu kupata kesi.."
"Anaitwa nani huyo mpenzi wako?" Daniel aliuliza kwa shauku kubwa.
"Anaitwa Suto Sutani" Bruno alilitaja jina hilo akitegemea mstuko toka kwa Daniel, lakini Daniel hakustuka kabisa.
"Eeh" Daniel aliitikia kwa upole, ingawa alistuka kusikia jina la Suto Sutani lakini hakutaka kuuonesha kabisa mstuko wake.
"Mpenzi wangu alikabiliwa na kesi ya mauaji, siyo alikabiliwa, anakabiliwa na kesi ya mauaji mpaka sasa, anatafutwa kwa udi na uvumba usiku na mchana, lakini na uhakika Suto siyo muuaji!, wanamsingizia Suto wangu!" Bruno machozi yalikuwa yanambubujika. Lakini alikuwa analia kimya kimya bila kutoa sauti.
"Unajua sijakuelewa kabisa Bruno, hebu nyoosha maelezo kaka"

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
Habari simulizi za riwaya zipo katika group za WhatsApp, kama upo WhatsApp tuma Niunge kwenda 0757 633010.
Utasoma Riwaya kali sana!
Asubuhi, mchana na jioni.
Mungu awabariki sana !
 
SIMULIZI; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 49

"Suto alikuwa mpenzi wangu Daniel, nilimpenda sana, alinipenda sana, kwa hakika tulipendana !
Lilikuwa penzi tamu sana, utamu wa penzi uliodumu kwa muda mfupi sana.

Siku ya kwanza tu ya Penzi hilo lilipata pingamizi, penzi lilikataliwa na watu wawili muhimu sana katika maisha yangu. Penzi langu na Suto Sutani lilipingwa na baba, lilipingwa na mama, penzi lilikataliwa katakata na wazazi wangu wapendwa.
Lakini mimi sikuwa tayari kumuacha Suto Sutani, mwanamke niliyempenda kuliko kitu chochote duniani, sikuwa tayari kulivunja penzi langu na Suto Sutani.
Kukataa huko kulivunja penzi hilo kulizua jambo, kukataa kwangu kulitengeneza chuki ! Chuki kali sana kati yangu na wazazi wangu wapendwa.
Tulikuwa na mgogoro mkubwa sana na wazazi wangu, mgogoro ulioanza siku yetu ya kwanza tu ya uhusiano wangu na Suto Sutani.
Lakini mimi nilikuwa mbishi, nilikuwa naamini mapenzi ya kweli kati yetu, mapenzi yatokayo moyoni ndio cha kuang'ang'ania penzi hilo. Nilimpenda sana Suto Sutani.

Siku tatu za Penzi lile zilikuwa chungu sana. Chungu, chungu, chungu sana. Chungu kuliko shubiri, chungu kuliko mwarobaini, chungu kuliko kitu chochote kile unachokijua kichungu.
Ndio zilikuwa chungu kwakuwa Suto alisingiziwa amewauwa wanaume watatu nyumbani kwao usiku !
Daniel, inakuingia akilini Suto Sutani kuweza kumuuwa mtu? Nakwambia Suto alikuwa muoga ! Alikuwa anaogopa hata kuuwa mende, kwa mtu mwoga namna hiyo inakuingia akilini Daniel eti Suto Sutani auwe wanaume watatu, tena usiku wenye giza kali. Kwanza Suto mwenyewe hilo giza alikuwa analiogopa. Kama Suto Sutani alikuwa anaogopa kuuwa mende kwa kiatu, ataweza vipi kuuwa mtu kwa shoka?
Hapana ! Walimsingizia Suto Sutani.

Suto alipelekwa Polisi, na hatimaye gerezani, Segerea. Suto aliingizwa kwenye gereza lile linalofanana na kiwanda cha mbu, Suto aliingia kule kwenye watu wenye roho mbaya kabisa. Watu makatili, watu waliyoyashinda maisha, huku maisha yenyewe yakiwa yana hasira na wao...." Bruno aliacha kuongea, alifuta machozi kwa kutumia shati lake lake. Akavuta kamasi nyepesi kwa ndani. Upande wa Daniel alikuwa makini kusikiliza kila kitu akichosema Bruno. Na kurekodi kwa siri bila Bruno kujua.

"Veronica Baro, mwandishi mshenzi kabisa kuwahi kutokea Tanzania, hapana...ni mwandishi mshenzi kuwahi kutokea duniani. Veronica Baro alijitahidi kumwandika vibaya sana Suto Sutani. Alitumia vibaya kalamu yake kuithibitishia dunia kwamba Suto Sutani alikuwa muuaji ! Hivi wewe Veronica ulikuwepo Wakati Suto anauwa? Una hakika Suto Sutani ni muuaji? Uliupata wapi ushahidi?

ITAENDELEA baadae
 
SIMULIZI; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 50

Mwandishi wa habari Veronica Baro ndiye mtu aliyenifanya niamini kuwa Suto ni muuaji ! Aliandika kila siku ubaya kuhusu Suto Sutani, tena kwenye kurasa ya mbele, alimpa Suto sifa zote mbaya unazozijua wewe, Suto jeuri, Suto kiburi, Suto muuaji, nami nikaamini bila kufanya uchunguzi wowote, mbaya zaidi nikaanza kumchukia Suto Sutani, mpenzi wangu.
Nilimwacha Suto akiteseka gerezani, nilimwacha mwanamke niliyempenda zaidi duniani akinyanyasika gerezani, namini nikaingia katika mikono ya mibaya, mikono ya baradhuli, mikono ya shetani!
MANKA.
Nilimsahau kabisa Suto Sutani na kuangukia katika mikono michafu ya Manka. Sikujua, sikujua, sikujua, kumbe Manka hakuwa mwanamke, Manka alikuwa ni nyoka, nyoka mwenye sumu kali sana ! Ninaposema Manka alikuwa shetani namaanisha!.
Wazazi wangu, wakishirikiana na huyo mshenzi aliyetoka hapa, eti mwandishi wa habari mahiri nchini Tanzania, Veronica Baro...... Walinitoa peponi na kunipeleka motoni! Wakati penzi langu na Suto Sutani lilikuwa tamu sana, penzi tamu sawa na zile hadithi nzuri za wale wanawake wa peponi. Penzi langu na Manka lilikuwa chungu sana, chungu mithili ya mwarobaini!
Naweza sema penzi langu na Manka lilikuwa ndio penzi baya zaidi kuwahi kutokea hapa duniani.
Nilifaidi penzi la Manka siku tatu tu za awali, baada ya hapo yalikuwa mateso, yalikuwa manyanyaso" Bruno aliacha kuongea na kumwangalia Daniel usoni. Aliridhika na umakini na utulivu aliokuwa nao Daniel Mwaseba. Utulivu ambao aliusoma sana vitabuni, lakini leo alikutana nao.

"Hivi Daniel unaweza ukaamini ndani ya wiki moja nilimfumania Manka na wanaume watatu tofauti?
Manka alikuwa kahaba, tena kahaba wa kimataifa!
Daniel! Sitaki kuikumbuka juzi, sitaki kuikumbuka, sitaki kabisa....aaah juzi Manka ndio alinionesha yeye ni mnyama kiasi gani...aibu kusema lakini Manka alinifanyia kitu kibaya sana, unastahili kufa Manka. Tena kifo kibaya sana, Manka siyo binadamu kabisa, nakwambia Manka ni mbwa Daniel "
Sauti ya Bruno ilipanda juu, mpaka meza za jirani walikuwa wanakisikia anachosema huku wakigeuka kumuangalia mzungumzaji.
"Juzi alikufanyaje Manka?" Daniel Mwaseba aliuliza kwa sauti ya upole.

Bruno alilia kwa sauti kubwa. Watu wote walishangazwa pale baa. Wengine wakidhani labda pombe imemzidia. Daniel akajua kuna jambo kubwa sana ambalo Bruno alifanyiwa. Nae akazidi kupata kimuhemuhe cha kukitaka kukijua hiko kitu.
"Usilie kaka, ni nini tatizo? Punguza jazba"
Sasa Bruno aliyaacha machozi yambubujike, hakujishughulisha kabisa kuyafuta, Bruno hakuyahofia macho na masikio ya walevi, waliomakinika kwa kumtazama. Kwa sauti ya kwikwi Bruno alisema kitu kilichomshangaza sana Daniel..

ITAENDELEA MCHANA
 
SIMULIZI; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633910

SEHEMU YA 51

"Manka alikuwa ni shetani!
Babaaa...baba naye alikiwa ni ibilisi, ndiyo baba yangu mzazi alikuwa ni ibilisi. Sioni aibu na wala siogopi kusema kuwa baba yangu ni miongoni mwa baba wabaya kabisa duniani!" Bruno aliacha kuongea, aliangalia juu kwa muda. Alikutana na taa nzuri za rangi ya bluu, ziking'inia juu ya mgahawa ule.

"Walifanyaje hao Bruno" Daniel aliuliza akiwa na kihoro kikubwa cha kutaka kujua.
Bruno alitulia kama dakika tano, akilia huku akiiangalia ile taa ya bluu, baadae Bruno alinena kwa utulivu sana.

"Nakumbuka juzi nilitoka Chuo saa kumi na mbili jioni. Niliamua Kupitia kwa mpenzi wangu Manka kabla sijaenda nyumbani. Nilifika nyumbani kwa Manka, lakini nilikaribishwa kwa namna tofauti na niliyoizoea , nilikaribishwa na sauti za malalamiko ya Manka nilipofika tu mlangoni. Manka alikuwa analalamika, Manka alikuwa analiaaaa"
Bruno alianza kulia tena. Daniel alinyanyuka na kwenda kusimama pembeni na alipokaa Bruno. Alimpigapiga mgongoni, na kumshika bega. Alimyanyua na kutoka nae nje ya ule mgahawa. Kule nje waliingia katika gari aliyokuja nayo Bruno. Daniel alikaa kwenye usukani. Wakati Bruno alikaa katika kiti cha pembeni ya dereva. Kabla hajaulizwa Bruno aliendelea kisimulia.
"Nilizunguka nyuma ya dirisha. Ilikuwa ni bahati mbaya kwao hawakukumbuka kushusha panzia...niliwaona....niliwaona Daniel..." Bruno alikuwa anaongea huku anapigapiga mapaja yake kwa mikono yake yote miwili.

"Baba alikuwa juu, mpenzi wangu Manka alikuwa chini. Walikuwa wanafanya mapenzi Daniel !
Baba alikuwa anafanya mapenzi na mkwewe, ilikuwa ni picha mbaya sana kuwahi kuitazama katika maisha yangu, Manka wangu na baba yangu mzazi walikuwa wananisaliti ! Ulinipata uchungu mkali sana Daniel, hakuna uchungu duniani kama uchungu wa penzi, Penzi Chungu sana usiombe Daniel. Machozi yalinitoka siku ile, nililia pale dirishani kama mtoto mdogo. Manka alikuwa analia mle chumbani, mimi nilikuwa nalia pale nje, sote tulikuwa tunalizwa na baba !
Nilijua nitazimia, lakini sikuzimia. Nilishikwa na hasira sana siku ile. Nilitoka kwa kasi pale na kuelekea nyumbani. Nilikoswakoswa kugongwa na magari njiani mara kadhaa. Sikuwa na umakini kabisa. Mapenzi huuwa Daniel, nakwambia mapenzi yanauwa Daniel, unaelewa ninachokwambia? Ushawahi kupenda wewe? Ushawahi kuumizwa na mapenzi wewe? Fikiria unasalitiwa na baba yako mzazi! Fikiria Daniel !
Siku ile nilijua baba ni nguruwe, lakini sikujua kabisa kama mama yangu alikuwa mbango...aaaah kumbe baba yangu ni Nguruwe na alimuoa mwanamke ambaye naye ni Mbango. Siyo kama nawatukana wazazi wangu, hapana!
Siyo kama siwapendi wazazi wangu....hapana! Nawapenda sana wazazi wangu, lakini wacha niwe tu mkweli wazazi wangu ni watu wa ajabu sana. Wazazi wangu ni zaidi ya wanyama Daniel...

ITAENDELEA JIONI M UNGU AKIPENDA
 
Mapengo junior

vip mbona simulizi yako imeanzia sehemu ya 3,nataka mtiriliko ili nianze kuisoma ndugu.
 
Nilizimisplace naziweka soon hapa kwa ajili ya toxic na wengine
 
Mapengo junior

vip mbona simulizi yako imeanzia sehemu ya 3,nataka mtiriliko ili nianze kuisoma ndugu.

SIMULIZI.........PENZI CHUNGU -
SIMULIZI.........PENZI CHUNGU
MWANDISHI... HALFANI SUDY
SEHEMU YA 1

Suto Sutani, alikuwa ni msichana mwenye umri wa miaka 22. Alikuwa msichana mrefu wastani, Suto alikuwa na umbo zuri sana, alikuwa na ngozi nyeupe yenye kupendeza. Katika umri wake wa miaka 22, Suto hakuwa na mpenzi. Hakuwahi kufanya mapenzi, Hakuwahi kupata upendo toka kwa mwanaume yeyote yule duniani. Suto hakupata upendo hata wa baba yake mzazi. Mzee Sutani alimkataa Suto siku ileile aliyozaliwa. Sababu ya kumkataa ilibaki kuwa siri yake.

Bruno Michael, alikuwa kijana mtanashati sana. Alikuwa kijana aliyezaliwa katika familia yenye uwezo kiasi. Alikuwa kijana mwenye uzuri wa umbo na sura, uwepo wa pesa kiasi katika familia yao, vilifanya wanawake wengi sana wamhusudu sana Bruno pale mtaani kwao, Tabata dampo.

Bruno na Suto, walikuwa wanakaa mtaa mmoja, mtaa wa Tabata dampo. Wakati Suto na mama yake walikuwa wamepanga katika nyumba ya mzee Danigo, nyumba yenye vyumba sita na wapangaji sita ndani yake, nyumba ya kiswahili iliyojengwa Kiswahili.
Bruno alikuwa anakaa katika nyumba nzuri ya wazazi wake, nyumba yenye vyumba vitatu, yenye kila kitu ndani, nyumba ya kisasa iliyojengwa kisasa.

Ilikuwa siku ya jumamosi asubuhi, Bruno alikuwa hajaenda chuo siku hiyo. Wazazi wake walikuwa wameenda sokoni kununua mahitaji mbalimbali ya nyumbani kwa gari yao ndogo aina ya Suzuki.
Bruno alikuwa amekaa sebuleni akisoma kitabu cha Riwaya ya Ulaaniwe, riwaya iliyotungwa na Gwiji wa riwaya Tanzania, George Iron Mosenya.
Akili ya Bruno ilikuwa imezama hasa katika riwaya ile yenye kusikitisha sana, huku muziki mwanana wa mwanamziki Ben Pol ukisikika katika spika za redio yake.

Ghafla mlango wa sebuleni uligongwa.
"Karibu" Bruno alisema huku akikiweka juu ya sofa kitabu chake cha riwaya.
"Ahsante " Sauti ya kike ilijibu nje ya mlango ule.
"Sukuma, upo wazi "
Mlango ukafunguliwa.

Aliingia Suto, akiwa amevaa suruali nzuri aina ya jeans na blauzi fupi nyeupe. Mkononi alikuwa ameshika mkanda wa video.
"Kaka Bruno, nimeazima mkanda huu kwa kina Alex, naomba uniwekee niuangalie kidogo" Suto aliomba kwa sauti yake nzuri.
"Sawa, usijari" Bruno aliitikia.

Bruno alikuwa havutiwi kabisa na wasichana, alijiona mzuri, alijiona mtanashati, alikuwa ananata sana pale mtaani. Hakuwapenda wasichana, hakutaka hata kuwa na ukaribu nao. Lakini leo alipatikana, hakuwa na jinsi, walikuwa sebule moja na Suto Sutani.
Bruno aliuchukua ule mkanda mikononi mwa Suto na kwenda kuuweka kwenye deki, na kuzima redio iliyokuwa inaimba. Ulikuwa mkanda wa taarabu . Bruno alirudi sofani na kuendelea kusoma riwaya yake.
Suto akiwa na furaha isiyo na kifani kumuona Mzee Yusuph akiimba kideoni, huku madada wakicheza kwa umahiri mkubwa.

Kidogo kidogo taarabu ikaanza kumuingia kichwani Suto. Mziki wa taarabu ukapenya katika mishipa ya damu yake. Mwili ukamsisimka, Suto alikuwa mpenzi mkubwa sana wa taarabu. Taratibu alianza kutingisha kichwa pale sofani. Bruno alikuwa kazama riwayani, hakumuona Suto alivyokuwa anatingisha kichwa chake.

Taarabu ikachanganya, Suto alijikuta anasimama , akaanza kutingishika mwili wote taratibu. Bruno sasa aliweka kidole kurasa aliyoishia kuisoma, ili isipotee, macho yake yote mawili yapo kwa Suto Sutani.

Suto alikuwa hana habari kabisa. Sasa alikuwa anatingisha nyonga yake barabara. Bruno alibaki kahemewa.
Macho ya Bruno yalipanda kwa wizi, sasa yalitua katika kiuno cha Suto, kilikuwa kiuno kizuri sana. Chenye mviringo unaoeleweka. Bruno alikuwa makini, kiuno kizuri kilikuwa kinafata vizuri ule mdundo wa taarabu. Bruno sasa alikuwa anaangalia dhahiri, sio kiwizi tena.
Kiuno kizuri cha Suto kilikuwa mahiri sana.
Suto alikuwa bize na taarabu, akiwa kasahau kabisa uwepo wa Bruno kwa muda. Bruno alikuwa bize na kiuno cha Suto, akiwa kakisahau kitabu cha riwaya kwa muda.

Bruno naye alisimama taratibu, akawa anamsogelea Suto. Kitabu akikiacha palepale kwenye sofa. Suto alizidi kukatika, na Bruno alizidi kumsogelea. Walikaribiana sana sasa.
Suto kwa mbali alihisi kiuno chake kikishikwa ,

ITAENDELEA
 
Mapengo junior

vip mbona simulizi yako imeanzia sehemu ya 3,nataka mtiriliko ili nianze kuisoma ndugu.

SIMULIZI.........PENZI CHUNGU - SIMULIZI.........PENZI CHUNGU
MWANDISHI... HALFANI SUDY

SEHEMU YA 2

Bruno alikuwa hajielewi. Akili yake ilihama kabisa. Hakuuona kabisa ubaya wa kumshika Suto namna ile. Sasa alikuwa anamuona Suto ni mzuri zaidi ya Cleopatra. Kiuno kilimchanganya sana, alijikuta ghafla amekipenda kiuno cha Suto, hapana, alijikuta anampenda Suto kutokana na kiuno chake kizuri. Sasa waligusana kabisa, Suto akiwa mbele, Bruno akiwa nyuma.
Mikono ya Bruno ilikuwa kifuani kwa Suto, ikichezea maziwa ya Suto, mdomo wa Bruno ulikuwa sikioni kwa Suto. Walikuwa wananesa kutokana na mapigo ya mziki mzuri wa taarabu. Wote wakiwa hoi kwa hamu ya kitu wasichokifahamu. Pale sikioni mdomo wa Bruno ulijikuta ukisema, maneno yalitoka taratibu kwa sauti ya kukatakata mdomoni.

"Dunia mzi-ma ha-ikupe-ndi Suto. Wa-na-ume wote hawa-kup-endi Suto. Ila mi-mi nimegundua wewe ni mwana-mke mzuri sana. Ndio, Dunia nzi-ma inaku-chukia Su-to. Ila mimi naa-hidi ku-kup-enda kua-nz-ia leo, nit-aku-pen-da siku zote za mai-sha ya-ngu Suto,
Ndio, Nakupenda sana Suto !

Ghafla mlango wa sebuleni ulifunguliwa, hakuna aliyeusikia mlango wakati unafunguliwa, hakuna wala aliyesikia mlio wa gari wakati linapaki kule nje. Wote walikuwa wamezama hisiani.
Wazazi wa Bruno walikuwa wamerudi kutoka sokoni.
Baba na mama Bruno walipigwa na butwaa. Kukuta mtoto wao amemkumbatia Suto namna ile. Ilikuwa picha mbaya sana kwao.

" Bruno ! " mama yake aliita kwa ghadhabu.
"Naam "
" Ni nini hiyo ? !"
"Mapenzi mama " Bruno alijibu kwa upole.
"Unasema ! "
"Mapenzi ya kweli Mama"
"Unataka sema, unampenda Suto ?"
"Ndio mama "
"Maajabu haya ! Tangu lini ? "
"Tangu leo Mama "
"Unampenda toka moyoni Suto "
"Nampenda toka moyoni Mama, nataka nimuoe "
"Haiwezekani ! " Baba na mama Bruno walisema kwa pamoja kwa sauti kubwa yenye ghadhabu !

Muda wote huo Suto alikuwa kimya. Alikuwa anasikia kila kitu alichokuwa anasema Bruno. Lakini hakuelewa kabisa. Hakuwahi kumpenda mwanaume tangu azaliwe. Alikuwa anawachukia wanaume wote duniani, sababu kubwa ikiwa ni Simulizi aliyosimuliwa na mama yake, jinsi baba yake akivyomtesa mama yake, kufikia hatua hadi ya kumkataa yeye, mtoto wake. Suto aliwekuwa na kisasi na wanaume wote duniani. Maneno yale ya Bruno yalimtoa Suto machozi.

"Usilie Suto, chozi lako ni la thamani sana kwangu.." Bruno hakumalizia kauli yake.
"Hivi we mtoto umerogwa !" Baba yake alisema kwa sauti ya ukali.
"Nimependa baba " Bruno alisema kwa kujiamini.

Yalikuwa kama maigizo, Bruno mwenyewe hakujua nguvu ya maneno hayo inatoka wapi. Wazazi nao walishikwa na bumbuwazi, Suto alihemewa sana.
Wote hawakujua, mapenzi ni kitu cha ajabu sana, na muda mwengine yanaanza bila sababu maalumu. Bruno hakuwa amerogwa, sasa hakuwa amependa kiuno cha Suto pekee, alimpenda kweli Suto, na dhamira ya dhati toka moyoni mwake alikuwa anataka kumuoa kweli.

ITAENDELEA
 
SIMULIZI; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 52

Nilipofika mlangoni nyumbani, nilisikia kelele za malalamiko, kelele sawa na nilizozisikia nyumbani kwa kina Manka. Sauti, sauti, sautiiii za malalamiko..." Bruno alianza kulia tena. Kwa bahati mbaya Daniel hakuwa mbelezaji mzuri. Alikuwa anamwangalia tu jinsi Bruno akivyolia.
Baada ya kulia na kutosheka, Bruno aliendelea kusimulia.
"Kulwa, Kulwa, kulwa ....ndio neno kuu niliokuwa nalisikia mle ndani. Sauti iliyokuwa inatokea puani kwa mama yangu mzazi. Sauti ilikuwa inamaanisha Mama alikuwa anafanya mapenzi na mwanaume akiyeitwa Kulwa. Nilitamani tena kuzimia lakini nashangaa sikuzimia.
Niliondoka kwa hasira kubwa sana, na kuelekea kwa rafiki yangu Magomeni, rafiki yangu wa siku nyingi sana, alikuwa anaitwa Dotto. Nilisoma nae kidato cha tano na cha sita katika Sekondari ya Benjamini Mkapa. Nilijua huko labda nitapata tulizo.
Niliyoyakuta !

Nilimkuta Dotto amekaa sebuleni, na mwanadada mmoja. Nilipofika tu yule mwanadada aliaga na kuondoka. Baada ya kuondoka yule dada, Dotto aliniuliza kama yule namfahamu, nilimjibu hapana, jibu alilonipa liliniacha hoi sana. Nilitamani nimkimbilie yule dada ili anijibu maswali yangu kadhaa niliyokuwa nayo juu yake, lakini sikuwa na jinsi, Dotto angenielewaje?..umemjuana nae vipi yule dada Dotto?". Nilithubutu kumuuliza.
" Tuna kazi ya kufanya na Veronica Baro. Kazi ambayo ina maslahi makubwa sana"
"Huwezi kunambia Dotto rafiki yangu hiyo kazi?"
"Kuna kazi ndogo sana ya kumuua kidudu mtu, si unajua kazi zetu kaka?"
"Anaitwa nani huyo kidudu mtu Dotto?"
"Anaitwa Suto Sutani !"

Nilibaki mdomo wazi Daniel.

ITAENDELEA baadae
 
Back
Top Bottom