Riwaya: Penzi chungu

Riwaya: Penzi chungu

SIMULIZI... PENZI CHUNGU - SIMULIZI... PENZI CHUNGU
MWANDISHI.. HALFANI SUDY

SEHEMU YA 17

Inspekta Jasmine tangu alipopewa tu jukumu la kupeleleza kesi hii, hakuwa amepiga hatua yoyote.
Alishawahoji mama Suto, Suto na majirani wawili. Alijumuisha maelezo yao na kujikuta yupo palepale.
Pamoja ya kuwa majirani walikuwa hawampendi Suto lakini hawakusita kutaja sifa nzuri za Suto, mbele ya inspekta Jasmine.

Jumatatu ya leo ilimkuta Inspekta Jasmine mlangoni kwa jirani wa tatu wakina Suto.
Alikuwa anaitwa mama Siyawezi.
"Habari mama" inspekta Jasmine alisalimia.
"Nzuri mwanangu" mama Siyawezi alijibu huku akimwangalia Inspekta Jasmine kwa macho ya udadi.
"Mimi ni afisa wa jeshi la Polisi" Inspekta Jasmine alisema huku akionyesha kitambulisho.
"Nimefanya nini tena jamani ?" Mama Siyawezi alisema kwa sauti ya woga.
"Usiwe na wasiwasi mama, kuna vitu vya kawaida tu nataka kukuliza"
"Mwenzenu mimi nikisikia Polisi tu roho inaniruka, nawaogopa sana Polisi"
"Walikufanya nini Polisi hadi uwaogope kiasi hicho ?"
"Wala hawajanifanya kitu, mimi nikiona mavazi yenu tu yale yaani nachanganyikiwa, bora wewe hujayavaa, ningekukimbia hapa" Mama Siyawezi alisema huku akicheka.
"Hahaha tuendelee na kilichonileta mama"
"Sawa, nakusikiliza " Mama Siyawezi alitulia sasa.
"Unaitwa nani mama?"
"Jina nililopewa nyumbani ni Asha Msigeze, ila sahivi wananiita Mama Siyawezi, kwa kuwa nini mtoto wa kike anaitwa Siyawezi, lakini yupo Kisiju kwa bibi yake"
"Sawa mama, ulikuwa unamfahamu Suto?"
"Nisimfahamu Suto mimi, kazaliwa hapa hapa, kakulia hapa hapa, na kaulia hapa hapa!"
"Kamuua nani Suto?"
"Yaani, we askari halafu huna habari, Suto kawaua vijana watatu hapa, mwezi uliopita. Wawili kwa kisu, na mmoja kwa panga. Yule wa panga alikatwa vibaya sana. Ile picha inajirudia Kila mara nikilala, kumbe Suto alikuwa katili sana yule"
"Una hakika Suto aliwauwa wale vijana wale?"
"Nakubali sikusoma, ila picha nazielewa vizuri sana, ukiangalia mazingira tu ya siku ile, unapata jibu....Suto anahusika katika mauaji....au anawajua vizuri sana wauaji !" Mama Siyawezi alipigia msumari wa mwisho katika kaburi la Suto.
"Sawa mama Siyawezi, hivi ni nani aliyekuwa rafiki mkubwa wa Suto?"
"Mama yake" mama Siyawezi alijibu bila kufikiria.
"Hakuwa na rafiki mwengine?"
"Rafiki wa Suto ni mama yake mzazi......aaaaah lakini juzijuzi alipata rafiki mpya wa kiume"
"Ni nani?"
"Kwa jina sijui, lakini ukienda kumuuliza mama Suto atakwambia."
"Nashukuru mama, ahsante kwa ushirikiano wako"

Inspekta Jasmine alitoka nyumbani kwa mama Siyawezi na kuelekea kwa mama Suto. Nia ni kumjua huyo rafiki mpya wa Suto.
Angejua kitakachotokea, ni bora asingetoka ndani ya nyumba ile.

Alivyotoka Inspekta Jasmine, mgeni mpya wa kiume aligonga hodi katika nyumba ya mama Siyawezi, Mama Siyawezi alidhani Inspekta Jasmine amerudi tena. Alifungua mlango kwa haraka, kumbe alikuwa anaharakia kifo. Alipofungua tu mlango, alitazamana na kisu !

Itaendelea......badae
 
SIMULIZI.... PENZI CHUNGU - SIMULIZI.... PENZI CHUNGU
MWANDISHI.. HALFANI SUDY

SEHEMU YA 18

Jicho la kwanza la mama Siyawezi alikitazama kisu, tazamo la pili alijiangalia upande wake wa kushoto wa kifua chake. Pale unapokaa moyo. Nusu ya kile kisu kirefu alichokitazama mara ya kwanza kilikuwa kimezamishwa katika upande wake wa kushoto wa kifua na mkono imara wa mwanaume. Mama Siyawezi, alianguka chini huku akijiangalia kifuani. Akishuhudia damu nyingi zikibubujika katika kifua chake, ilikuwa ni kama bomba linalopitisha maji yenye kasi kali limekatika ghafla, ilikuwa ni picha mbaya na ya kutisha sana, mama Siyawezi alikata roho pale chini, bila kuijua sababu sahihi ya kuchomwa kisu kile, alikufa na kisu kifuani.
kwa mwendo wa kasi, mgeni yule wa kiume mwenye roho inayopaswa kuitwa mbaya, alitokemea mtaani.

Kwa kutumia gari yake ndogo, aina ya Rav 4 nyeusi, Inspekta Jasmine alifika nyumbani kwa mama Suto. Alikuwa anagonga hodi katika mlango wa nyumba ya kina Suto Sutani mara ya tatu sasa, lakini hakujibiwa.
Alijaribu kuusukuma ule mlango,
ukafunguka!
Aliingia sebuleni kwa tahadhari kubwa sana, macho ya Inspekta Jasmine yalikutana na majimaji ya ajabu katika kapeti zuri la pale sebuleni, maji maji mekundu, damu!
Damu ile ilikuwa inaelekea au kutokea chumbani. Inspekta Jasmine aliifata, huku akiwa kaishikilia bastola yake mkononi, tayari kwa kukipiga kiumbe chochote kibaya kitakachotokea mbele yake.
Michirizi ya damu ilimfikisha Inspekta Jasmine hadi chumba cha mama Suto,
Alipigwa na butwaa !
Alikuwa anatazamana na mwili usio na roho wa mama Suto! huku ukiwa na jeraha baya sana kifuani, juu kidogo ya ziwa lake la kushoto. Damu nyingi zilikuwa zimetapaa sakafuni. Bila shaka mama Suto aliuwawa sebuleni na kuburuzwa mpaka chumbani. Inspekta Jasmine aliichunguza nyumba yote kwa umakini mkubwa, hakukuwa na mtu yeyote ndani ya nyumba ile, watu wote waliikimbia nyumba ile baada ya tukio la siku ile usiku, tukio lililompeleka Suto Sutani Segerea.
Inspekta Jasmine alipiga simu Polisi, walifika pale kwa gari yao baada ya dakika kumi. Baada ya taratibu za kipolisi mwili wa mama Suto ulipakiwa na kupelekwa hospitali ya Amana. Baada ya Inspekta Jasmine kuchunguza mazingira ya ile nyumba, akihusianisha na tukio lile, hakupata jibu sahihi.
Alitoka nje ya nyumba ile. Alipofika nje, alipigwa na butwaa !
Alikutana na waandishi wa habari wameshafika eneo lile, wakiongozwa na mwandishi wa habari mahiri wa gazeti la Dumizi, Veronica Raymond Baro.
Waandishi wale walimvamia Inspekta Jasmine, kila mmoja na swali lake lake.
Inspekta Jasmine hakujibu swali hata moja, haukuwa muda wa kujibu maswali, ulikuwa ni muda wa kutafuta majibu ya maswali lukuki yanayotokana na visa vya ajabu tena mfululizo vya kesi ile, aliwaangalia tu waandishi wale kwa macho yake madogo. Alipenya kwa nguvu katika kundi lile kubwa la waandishi wa habari, aliingia kwenye gari yake, akaling'oa kwa kasi kubwa sana, akiwa hajui anaelekea wapi ?

Baada ya kuzunguka kwa muda mrefu na gari bila uelekeo maalumu. Sasa alipata mawazo mawili yakiyokinzana. Aende hospitali ulipopelekwa mwili wa mama Suto, au arudi Tabata kwa mama Siyawezi.
Inspekta Jasmine hakujua kwanini nafsi ilimwambia arudi Tabata, kwa mama Siyawezi, nafsi ilishinda aliamua kwenda huko.

Alipaki gari yake vizuri barazani kwenye nyumba ya mama Siyawezi. Akawa anaelekea mlangoni kugonga mlango. Inspekta Jasmine aligonga sana mlango ule, lakini haukufunguliwa. Alijaribu kuusukuma, ilikuwa kama mlango wa mama Suto, nao ulifunguka bila kizuizi chochote, Alichokiona pale chini ya sakafu Inspekta Jasmine kilimstua sana. Aliukuta mwili wa mama Siyawezi umelala katika dimbwi dogo la damu.
Alichoka sana !
Alishusha pumzi ndefu, sasa, Inspekta Jasmine aliona maji yamezidi unga.
Sasa alijua kwamba anapambana na watu wanaozijua nyendo zake zote. Bila shaka walimwona wakati kaja kwa mama Siyawezi, na walijua pia ataenda kwa mama Suto.
Inspekta Jasmini aliwapigia tena askari Polisi. Waliwasiri baada ya muda mchache, waliuchukua mwili wa marehemu mama Siyawezi na kuupeleka hospitali nao, Inspekta Jasmine nae alielekea huko kwa gari yake...
KESHO
 
SIMULIZI....... PENZI CHUNGU - SIMULIZI....... PENZI CHUNGU
MWANDISHI..HALFANI SUDY

SEHEMU YA 19

Walifika katika hospitali ya Amana. Mwili wa mama Suto uliingizwa katika chumba maalumu cha kufanyia uchunguzi. Daktari Boniface Mperu ndiye alikuwa na jukumu la kuuchunguza mwili wa mama Suto, na daktari huyohuyo ndiye aliyehusika katika uchunguzi wa maiti ya mama Siyawezi muda mfupi uliopita.
Inspekta Jasmine na askari wengine wawili walikaa nje ya chumba ambacho Dokta Boniface akifanyia uchunguzi wakimsubiri Dokta Boniface amalize, ili wajue watapata nini katika uchunguzi huo kitakachowasaidia katika upelelezi wao.

Katika benchi moja la wagonjwa la pale hospitali ya Amana, lilikaliwa na watu wengi sana, wagonjwa pamoja na waliokuja kuwaona wagonjwa wao. Miongoni mwa watu hao, kulikuwa na kijana mmoja asiyetulia. Akipepesa macho huko na kule, akiwa makini na nyendo za Inspekta Jasmine na wale askari wawili.

Kijana huyu ndiye yuleyule aliyekuwa mgeni wa mama Suto muda mfupi uliopita.
Alimuua kinyama sana kwa kutumia kisu chake kikali, alimuuwa mama Suto kwa sababu akizozijua yeye .

***********

Kule gerezani Suto Sutani, alipewa taarifa za kifo cha mama yake mzazi kwa dharau kubwa sana. Beji na Zura walionesha dharau kubwa sana. Hawakuonesh kujari kabisa kifo cha mama Suto. Hawakujari kabisa hisia za Suto Sutani juu ya msiba wa mama yake mzazi.
"Nyang'au mwenzio kashakufa huko!"
Beji alimwita Mama Suto Nyang'au, bila kujua Suto ana hisia gani juu ya mama yake, Suto anampenda vipi mama yake.
Neno nyang'au lilibadirisha hisia za Suto. Kuuwawa kwa mama yake kulimbadirisha kabisa Suto!
Sasa alihama, alihama rasmi toka kuitwa Suto Sutani hadi kuuitwa Suto muuaji kweli! Kama mwandishi wa habari mahiri wa gazeti la Dumizi, Veronica Baro alivyomwita.
Kifo cha Mama yake kilimtoa Suto kutoka katika hali ya u binadamu, na kumpeleka kwa kasi katika hali ya unyama. Suto sasa hakuwa na cha kupoteza Duniani. Mtu pekee aliyekuwa anamjari na kumthamini hapa duniani alikuwa kauwawa. Suto alikuwa anatamani kufa na yeye, lakini atakufa vipi ilihali watu waliomsababishia matatizo makubwa katika maisha yake walikuwa bado wanaishi?

"Nitawauwa mmoja baada ya mwengine!!!!!!!!"

Suto alitoa kauli hiyo akiwa peke yake, chozi la uchungu likitiririka katika mashavu yake, na kudondoka chini, katika sakafu mbovu ya jela, kwa kauli hiyo Suto Sutani alikuwa anamaanisha. Na alikuwa amepania kuuwa kweki ili kulipa kisasi cha mama yake mzazi !

**************

Baada ya saa moja, Dokta Boniface alitoka katika chumba cha uchunguzi. Akawanyooshea mkono kina Inspekta Jasmine ili wamfate ofisini kwake. Bila kusema neno, askari wale watatu walimfata daktari yule kijana, lakini hawakuwa watatu walioitikia wito ule wa Daktari kama waliyokuwa wanajiona, walikuwa wanne, na yule kijana alinyanyuka taratibu pale kwenye benchi nae alifata kwa nyuma kusikiliza walichoitiwa askari wale...

ITAENDELEA
 
SIMULIZI.. PENZI CHUNGU
MWANDISHI.. HALFANI SUDY

SEHEMU YA 20

Wakati wakina Inspekta Jasmine wakiingia ofisini kwa dokta Boniface, yule kijana alikaa katika benchi, nje ya ofisi ya dokta Boniface. Alitega kwa umakini masikio yake yote mawili na kusikiliza maongezi ya kule ndani kwa umakini.
"Eeh dokta Boniface, tupe ripoti ya uchunguzi wako ulioufanya" Inspekta Jasmine alianzisha mazungumzo walipoingia tu ndani.
"Mambo yote nimeandika katika faili, ila la msingi ninalotaka mjue, marehemu hawa wamekufa muda mmoja, wamepishana sekunde chache sana. Alianza yule mwanamke aliyeletwa mara ya kwanza, akafatiwa na huyu mlimleta sasa. Wauaji inaonesha ni wazoefu na makini sana, hawajaacha alama zozote katika miili ya maiti zile, lakini habari zaidi zipo humo katika ripoti zao za uchunguzi"
"Inawezekana muuaji akawa mmoja daktari?"
" Hiyo kazi yenu Afande, kupeleleza kwa umakini chanzo cha vifo vyao, na kuwajua wauaji halisi. Sisi kwa vipimo vyetu hatujaligundua hilo, mengine mengi yameelezwa kwenye hizo ripoti za uchunguzi wa vifo vyao." Dokta Boniface alisema huku akiionesha kwa kidole ile ripoti aliyoishika Inspekta Jasmine.
"Sawa, tunashukuru sana dokta"
"Karibuni sana Afande"
Walipeana mikono.

Inspekta Jasmine na wale askari wawili walitoka nje ya ofisi ya Dokta Boniface, wakimpita pale yule kijana bila hata ya kumwangalia usoni. Hawakuwa na tahadhari yoyote. Walitembea katika ile korido ndefu na kutoka nje ya hospitali, hawakujua kabisa kama kuna kijana anayewafata, nia ya kijana yule ni kuzipata zile ripoti kwa njia yoyote ile. Ripoti zilizokuwa katika bahasha mbili kubwa, mikononi mwa Inspekta Jasmine.

Waliingia ndani ya gari ya Inspekta Jasmine na kuondoka. Yule kijana alichukua pikipiki na kuanza kuwafata kwa nyuma. Wakiwa ndani ya gari walikuwa hawana hili wala lile. Walikuwa hawajui kabisa kama wanafatwa.

Inspekta Jasmine hakuzipa uzito uliostahili ripoti zile ripoti za uchunguzi toka kwa Dokta Boniface, wao walikuwa wameridhika na maneno ya dokta Boniface. Lakini kwa upande wa yule kijana, pamoja na kusikia baadhi ya maneno ya Dokta Boniface, lakini nia ya kuzipata ripoti zile ilikuwa palepale, alijua dokta Boniface alikuwa anaficha baadhi ya vitu, ndio maana aliwasisitizia sana wale askari wakazisome zile ripoti za uchunguzi.

Kule hospitali, ndugu wa mama Siyawezi waliruhusiwa kuichukua mwili wa ndugu yao, tayari kwa maandalizi ya kwenda kuzika.
Hakukuwa na zuio lolote la kuzuia miili ile, maana kama uchunguzi ulikuwa umishafanyika.
Mwili ule muhimu sana kwa mustkabali wa kesi hii ulichukuliwa.
Huku mwili wa mama Suto ukichukuliwa na wasamaria wema, waliojitolea kwenda kuuhifadhi katika makazi yake ya milele. Mazishi ya mama Suto yalienda kufanyika, bila uwepo wa mtoto wake kipenzi Suto Sutani....

YA KESHO SIYO YA KUKOSA.
 
Dah inspector jasmine atakosea sana kama hatasoma ile repory,dahh,iimefika patamu
 
Yeah itamsumbua sana...hii ni moja ya sheeda ya mapolice wetu...usikose muendelezo wake
 
SIMULIZI.... PENZI CHUNGU
MWANDISHI.. HALFANI SUDY

SEHEMU YA 21

Inspekta Jasmine na wale askari wawili walikuwa wanaelekea kituo cha Polisi cha kati. Hawakujihangaisha kabisa kufungua zile ripoti za uchunguzi.

Walipofika kwenye mataa walisimama ili kusubiri taa ziruhusu gari yao kuendelea na safari.
Inspekta Jasmine alikuwa ametulia kwenye usukani, akiwa ameshusha kioo mpaka chini, ili kupambana na joto la Jiji la Dar es salaam. Askari mmoja alikaa pembeni yake, na yule askari mwengine alikuwa amekaa nyuma ya Inspekta Jasmine. Ile bahasha yenye ripoti za uchunguzi za vifo za mama Suto na mama Siyawezi, zikiwa katikati ya mapaja ya Inspekta Jasmine. Askari wote kwenye gari walikuwa kimya. Kila mmoja akitafakari lake.

Ghafla mkono mwembamba ulipenya katika dirisha la dereva, na kutua katika mapaja ya Inspekta Jasmine, na kuitwaa ile bahasha yenye ripoti muhimu sana. Mkono ule ulirudishwa kwa haraka sana ukiwa na bahasha. Kilikuwa kitendo cha haraka sana, mithili ya kufumba macho na kufumbua.
Yule kijana mwenye pikipiki alifanikiwa kuichukua ile bahasha muhimu sana mbele ya askari watatu na kuondoka nayo.
Askari wote walibaki wameduwaa. Kwanza hawakuelewa kilichotokea, na baada ya kuelewa hawakuamini kabisa kilichotokea. Walikuwa wanaangaliana tu wakati pikipiki ile ikipenya katikati ya magari na kutokomea kusikojulikana.

Askari wale walihemewa, sasa wakawa wanatafuta jinsi ya kugeuza gari ili wakaangalie uwezekano wa kupata ripoti nyingine za uchunguzi kwa Dokta Boniface.

************
Kule gerezani, Suto Sutani alikuwa na mambo mengi kichwani, sasa alikomaa, alikomazwa na maswahibu na madhila makubwa yaliyomkuta.
Suto sasa alibadirika !
Akawa kiburi, haogopi, hajari, na mtukutu hasa. Matatizo yaliibadiri tabia nzuri ya Suto Sasa akatawaliwa na wazo moja tu kichwani mwake, kutoroka gerezani na kwenda nje kulipa kisasi !

***********

Inspekta Jasmine na askari wenzake walifika katika hospitali ya Amana, na moja kwa moja walienda kwenye ofisi ya Dokta Boniface, Dokta hakuwepo. Walikaa nje kwenye benchi kumsubiri. Benchi lilelile alilokaa yule kijana aliyewapora bahasha yenye ripoti muhimu za uchunguzi.

Baada ya robo saa, Dokta Boniface alirejea. Alishangaa kukutana tena na wale askari pale. Kabla ya salamu, Inspekta Jasmine alisema;
"Dr we lost a report!"
"Whaaat?"
"Ndio hivyo dokta, kuna dereva bodaboda mmoja katupora aisee, sijui alidhani kuna hela mle"
"Kaichukua, yule kijana itakuwa kaichukua "
" Mbona sikuelewi Dokta"
Dokta Boniface alitulia, akameza funda kubwa la mate, kisha aliwakaribisha ofisini na kuanza kuwaelezea habari nzito kuhusu yule kijana mwendesha pikipiki....

TUKUTANE BAADAE HAPAHAPA
 
SIMULIZI...PENZI CHUNGU
MWANDISHI.. HALFANI SUDY

SSEHEMU YA 22

Dr Boniface aliongea maneno yaliyowaacha hoi kina Inspekta Jasmine na wale askari wengine.

"Leo asubuhi, ilivyokuja ile maiti ya kwanza kabla sijaifanyia uchunguzi kuna kijana alikuja ofisini kwangu. Alidai yeye ni ndugu wa marehemu mama Suto na alitaka nimpe ripoti ya uchunguzi ya kifo cha mama Suto kwa siri. Aliniahidi pesa nyingi sana.
Alisema anataka kumshughulikia mtu aliyemuua dada yake. Nilimkatilia katakata, nilimwambia huo sio utaratibu wetu hapa hospitali. Aliondoka kwa ghadhabu, huku akiniahidi atahakikisha anaipata ripoti ya uchunguzi kwa njia yoyote ile . Mimi nilimpuuza lakini
tangu muda ule nilikuwa makini sana kwa kila hatua niliyokuwa ninapitia, nikijiahidi kutunza ripoti kwa hali yoyote ile.

" kwani ripoti ilikuwa ina lipi la maana Dokta, si yaleyale uliyotueleza?"
"Hapana Inspekta!" Dokta Boniface alisema kwa sauti kubwa huku akigonga meza kwa kiganja chake.
"Kuna nini sasa?"
"Alama ya macho ya muuaji!"
"Unasema?"
"Ndio, pamoja na muuaji kuvaa gloves mikononi, lakini alijisahau, taswira yake ilionekana dhahiri katika macho ya marehemu mama Suto. Na na na marehemu wote wawili ilitokea taswira moja!"
"Sasa kwanini hukutuambia kabla maneno hayo, ili tuwe makini kuilinda ile ripoti, na hayo yaliwezekana vipi kwa muda mfupi kama ule ?"
"Ilikuwa kwa ajiri kwa usalama Inspekta, niliamua kutosema pale, ili kama kuna mtu anatusikiliza kwa siri aidharau ripoti ile, kuhusu muda mfupi aliotumia muuaji, hata mimi inanishangaza Afande "
"Sasa tushaipoteza ripoti muhimu za uchunguzi, zenye macho ya muuaji, tunaomba ukafanye tena uchunguzi, nitalipia mimi gharama zote."
"Mmechelewa Inspekta, ndugu wa marehemu washachukua maiti zao"
"Afanalekiii !"

Miguu ya Inspekta Jasmine iliishiwa nguvu, akawa anadondoka chini taratibu, wale askari wawili wakamdaka na kumketisha kitini.
Kama maji yalikuwa yamepita shingoni, sasa yalikuwa yanamzamisha kabisa Inspekta Jasmine, hakutegemea kabisa kama atapata vikwazo katika kesi hii. Kesi aliyoiona nyepesi sana, sasa ilimkalia shingoni.

*************

Usiku wa siku ile ulivyoingia ulikuja na janbo. Saa sita ya usiku, Suto akiwa amelala usingizi mzito. Mlango wa geti lake ulikuwa unafunguliwa taratibu.
Aliyekuwa anafungua mlango ni Zura akishirikiana na yule kijana aliwaibia bahasha kina Inspekta Jasmine mchana uliopita, alikuwa anaitwa Ndula wa Ndulani.

Lakini Zura na Ndula walikuwa hawajui. Suto hakuwa Suto yule, sasa alikuwa Suto mpya, Suto mwenye hisia. Akiwa usingizini alisikia kwa mbali ukelele wa mlango ukifunguliwa.
Aliamka kimyakimya.
Taratibu Suto alijisogeza mpaka nyuma ya mlango. Kulikuwa Giza la kutisha. Akiwa pale nyuma ya mlango Suto alimuona vizuri mtu akiingia kwa mwendo wa kunyata na kisu chake mkononi. Alikuwa anakifata kirago alicholalia Suto muda mfupi uliopita.
Ndula ananyata na kisu chake bila kujua kuwa nyuma nae alikuwa ananyatiwa na mtu, Suto Sutani aliyebadirika !

ITAENDELEA .
Kwa mara ya pili Suto anataka kuuwawa, je Ndula wa Ndulani atafanikiwa?
Soma kisha, tafakari kimyakimya.......
 
SIMULIZI... PENZI CHUNGU
MWANDISHI.. HALFANI SUDY

SEHEMU YA 23

Zura alikuwa amerudi kule getini. Akisubiri Ndula amalize kazi kule ndani, kazi ya kumuua Suto. Ni yeye aliyewabadirishia lindo askari wenzie ili apate nafasi ya kumuingiza Ndula gerezani, na alifanikiwa.

Akiwa kwa nyuma akisaidiwa na giza, Suto alimrukia yule jamaa, kwa nguvu zake zote Suto alimkaba Ndula shingoni. Kutokana na hofu na nguvu ya ile kabali, kisu cha Ndula kilidondoka chini. Suto akazidisha kubana mikono yake. Ndula alijaribu kujitoa bila mafanikio.
Suto alikuwa na nguvu mithili ya mwanamme. Ndula macho yalimtoka, kabari ile ilinasa barabara shingoni mwake.
Ndula hakufurukuta. Mara alianza kuishiwa nguvu, alidondoka chini taratibu.
Alikuwa amezimia.
Suto alimwangalia usoni yule mtu. Alikuwa amevaa soksi kubwa iliyoziba kabisa sura yake. Aliivuta ile soksi na kuivua. Alimwangalia yule mtu usoni. Lakini hakumtambua. Hakuwahi kukutana na yule mtu kabla.
Suto alimvua yule mtu ile fulana nyeusi na suruali nyeusi alizovaa. Alizivaa yeye. Kichwani alivaa ile soksi nyeusi nayo. Alifanana kabisa na Ndula wa Ndulani.
Alitoka nje kwa mwendo wa kunyata, mlangoni alimkuta Zura, alimfungulia mlango Suto bila kumhoji chochote. Akidhani yule ni yule jamaa waliyemtuma, kashafanya walichomtuma.

Suto Sutani sasa akawa huru tena.
Lakini Suto alijua utapita msako mkali juu yake, na labda atakamatwa, lakini alidhamiria kulipa kisasi kwanza kwa watu waliomsababishia madhila yale, kabla hajakamatwa.
Alipofika mbele kidogo, alivua ile soksi usoni na kuitupa. Aliipekuwa mifuko ya ile nguo aliyovaa, katika mfuko wa mbele wa kulia wa suruali ile, alikutana na kitu akichokihitaji sana muda ule.
pesa. Zilikuwa shilingi laki mbili taslimu ndani ya mfuko wa suruali ile. Katika mfuko mwingine alikutana na kisu kirefu.
Sasa alifikiria aende wapi, akajifiche mkoani, ama abakie jijini Dar es salaam.
Mwishowe aliamua kubaki Dar es salaam, Mbagala ndio lilikuwa chaguo lake la kujihifadhi kwa muda, akisubiri sakata la kutafutwa litulie. Alijua kutokana na Mbagala kuwa na mchanganyiko wa watu wengi sana, itakuwa ngumu sana kukamatwa. Usiku wa manane alipanda daladala na kuelekea Mbagala.

**************

Mzee Sutani, alikuwa ni mfanya biashara maarufu wa viatu, katika soko la Karume.
Miaka 22 ilikuwa imepita tangu amtelekeze mama Suto kule Tabata, na mwanae kichanga.
Hadi sasa alikuwa hajui habari za mama Suto, wala mtoto wake Suto. Sasa alikuwa ameoa mke mwengine, na kuzaa nae watoto watatu.
Itaendelea badae
 
SIMULIZI.... PENZI CHUNGU
MWANDISHI.. HALFANI SUDY

SEHEMU YA 24

Siku ya ijumaa, ilikuwa siku yenye pilikapilika nyingi sana kwa Mzee Sutani.
Jana yake siku ya alhamisi, alikuwa ametoka jijini Mbeya, kununua mzigo mkubwa wa viatu. Siku ile ya ijumaa asubuhi alikuwa na kazi ya kuusafirisha mzigo ule toka Mbagala Charambe hadi sokoni Karume. Kwa kuwa alikuwa na mzigo mpya, alifanya biashara nzuri sana siku ile.
Kutokana na kupanga vizuri mzigo wake, ili kesho yake aanze kuuza tu, alijikuta anarudi nyumbani kwake usiku wa manane, alipanda daladala iliyokuwa inaelekea Mbagala. Wakati anapanda daladala ile kuna mfanyabiashara mmoja alimwita kwa sauti kubwa
"Mzee Sutani, naona Leo biashara imefanyika kweli"
"Hamna Mzee Ngonyani.........."
Maneno mengine waliyoendelea kuongea wazee wale. Hayakusikiwa vizuri na abiria mmoja wa kike, aliyekaa siti moja na Mzee aliyeitwa kwa jina la Sutani. Neno Mzee Sutani lilirindima katika kichwa chake.
"Baba" alijisemea kimoyomoyo.
Suto Sutani, alikuwa katika daladala ile aliyopanda mtu aliyeamini kuwa ni baba yake, Mzee Sutani.
Hasira zikampanda Suto, aliamini baba yake ndio chanzo cha madhila yote yaliyomkuta. Suto alidhamiria kumuua baba yake usiku ule.

***********

Kule jela ilikuwa patashika, alfajiri iligundulika kwamba Mfungwa mmoja ametoroka, huku mwili wa mtu asiyetambulika, lakini amefariki ukikutwa katika selo ya Mfungwa aliyetoroka, Suto Sutani. Wakati Suto aliamini yule mvamizi alikuwa amezimia, kumbe la, Ndula alifariki kwa ile kabali ya nguvu aliyompiga usiku.
Lakini hakuna aliyeweza kukitegua kitendawili kile, Suto ametorokaje, na yule mtu ameingiaje, kitendawi walikuwa wanaweza kukitegua Beji na Zura. Lakini nao walijifanya hawaelewi kitu. Patashika ikawakumba askari wote waliokuwa zamu usiku wa siku ile. Mkuu wa Gereza la Segerea alikuwa mkali mithili ya mbogo. Lakini haikusaidia kitu, ukweli ulibaki palepale, Suto Sutani alikuwa ametoroka, na yule kijana alikuwa ameuwawa.

Asubuhi ya siku ile msako maalum ulianza, viliwekwa vizuizi katika njia zote kuu za kutoka nje ya Jiji la Dar es salaam, huku askari wote waliokuwepo katika vizuizi hivyo walikuwa na picha ya Suto mkononi. Kuhakikisha Suto hatoki nje ya mkoa wa Dar es salaam, lengo ni kumkamata akiwa hai au amekufa.

Beji na Zura, wao walikuwa hawaelewi kabisa nini kilitokea usiku ule, Zura ndio alibaki katika mshangao mkuu, hakuamini kabisa kama yule mtu aliyemruhusu kutoka ndani ya Gereza alikuwa Suto. Vibarua vyao sasa vilikuwa mashakani, pamoja na msako wa Polisi, nao waliweka msako wao wa siri wa kumsaka Suto, waliapa lazima wamkamate Suto na kumuua !

Wakati Polisi na kina Beji wakipanga hayo, Suto Sutani, sasa alikuwa katika gari pamoja na mtu aliyeamini ni baba yake wakielekea Mbagala. Mahali alipopachagua Suto kuweka maficho yake ya muda.
Bila Mzee Sutani kujua kama binti aliyekaa nae siti moja ni mwanae wa kumzaa mwenyewe, lakini sasa alikuwa ni kama mtoa roho kwake...

ITAENDELEA KESHO
 
SIMULIZI..... PENZI CHUNGU
MWANDISHI.. HALFANI SUDY

SEHEMU YA 25

Gari ilipofika Mbagala rangi tatu, Mzee Sutani alishuka kwenye gari, kwa nyuma akifuatwa na Suto Sutani. Alikuwa sasa akielekea stendi yanakopaki magari ya Mbagala Charambe.
Hakukuwa na gari hata moja, wala abiria pale stendi. Ulikuwa ni usiku mwingi sana. Magari yanayoelekea Charambe, ni tofauti na magari yanayofika katikati ya Jiji, yanayotembea saa ishirini na nne.

Suto alimfata baba yake kimya kimya. Akisubiri wafike sehemu muafaka ili atekeleze alichotaka kutekeleza.
Walipofika stendi, Suto akaona pale ndio mahali muafaka kwake. Mzee Sutani aligeuka nyuma, alishangaa kumuona mtu. Alijua yupo peke yake mahali pale. Kwa usiri mkubwa, Suto alikichomoa kile kisu toka katika zile nguo nyeusi alizovaa, na kumfata Mzee Sutani kwa mwendo wa taratibu, bila wasiwasi wowote.
Alimkaribia kabisa, Suto alimshika mkono yule Mzee kwa nguvu na kumgeuza kwa nyuma. Maana Mzee Sutani alikuwa amegeuza kichwa tu, kiwiliwili kilikuwa bado kinaangalia mbele.

"Naitwa Suto "
"Suto !"
"Unanikumbuka kumbe"
"Suto mwanangu, Suto Sutani ?"
"Nilikuwa mwanao, sasa siyo mwanao tena, ni adui yako, tusiongee sana kwa kifupi nimekuja kuitoa roho yako mbaya !"

Mzee Sutani alifadhaika sana, hakutegemea wala hakuamini kilichotokea. Ilikuwa ni kama yuko ndotoni, kukutana na mwanae usiku kama ule. Tena akiwa anatisha, na anatoa vitisho.
Mzee Sutani alikiona kile kisu kirefu alichokishika Suto. Mzee wa watu alianza kutetemeka.

"Kwanini ulimkataa mama yangu ?, kwanini ulinitelekeza nikiwa mdogo sana?"
Suto aliporomosha maswali mfululzo, lakini Mzee Sutani hakujibu hata swali moja.

"Baba"
"Nisamehe sana Suto" Alisema huku machozi yakimtoka.
"Nimekusamehe baba"

Suto alisema kwa kejeri.
Maana alisema maneno hayo huku akichomeka kile kisu kwa nguvu sana katika kifua cha baba yake mzazi, Mzee Sutani. Alimwacha yule Mzee akigaragara pale chini stendi, huku akiwa ameushikilia mpini wa kisu, kilichozama vizuri sana kifuani kwake.
Kwa haraka Suto alitokomea anakokujua yeye.

Asubuhi, Tanzania iliamka na habari kubwa mbili. Habari ya kwanza ni kutoroka kwa mahabusu hatari sana, na mtuhumiwa wa mauaji gerezani, na habari ya pili ni kuuwawa kwa Mzee mmoja kwa kisu huko Mbagala rangi tatu. Hakuna aliyehusianisha matukio hayo mawili, wote walihisi ni matukio mawili yasiyo na uhusiano wowote. Jeshi la Polisi, chini ya Inspekta Jasmine, likaingia katika michakamichaka mengine mipya.
Mchakamchaka wa kumsaka Suto Sutani, na mchakachaka wa kumsaka muuaji wa mzee huko Mbagala rangi tatu.

Asubuhi ya siku hiyo ilimkuta Veronica Baro, mwandishi mahiri wa gazeti pendwa la Dumizi, Mbagala. Alienda kupeleleza undani wa kifo cha yule Mzee Mbagala. Ili aandike habari yenye uhakika au hata kupata picha mnato za kuweka katika gazeti lake, ili kuwepo na uhalisia na kuvutia wasomaji.
Ni mwandishi Veronica Baro, ndiye aliyeitambulisha jamii ya Tanzania kwamba yule Mzee aliyeuwawa Mbagala rangi tatu alikuwa ni baba mzazi wa mahabusu aliyetoroka usiku wa siku ile. Huku akiweka wazi maoni yake kuwa kifo cha yule Mzee kinahusiana na mahabusu huyo moja kwa moja.
Akimaanisha Suto ndio muuaji !. Msako wa Suto sasa ulipamba moto maradufu....

ITAENDELEA BAADAE
 
SIMULIZI... PENZI CHUNGU
MWANDISHI.. HALFANI SUDY

SEHEMU YA 26

Suto Sutani alikuwa Gongo la mboto. Alishaona Mbagala siyo sehemu salama tena. Alirudi tena stendi na kupanda gari linaloelekea Mbagala usiku uleule, na sasa alikuwa kwenye nyumba ya kulala wageni huko Gongo la mboto.
Akiwaza jinsi maisha yake yaliyobadirika ghafla, toka Suto mwema, Suto mstaarabu, Suto mwenye tabia njema mpaka kuwa Suto katili, Suto asiyeogopa chochote, Suto muuaji !
Aliiumalizia usiku ule wenye kumbukumbu mbaya kwake akiwa pale, usiku wa kwanza uliofanya aue mtu, tena baba yake mzazi. Alilala huku masikio yake yakiwa nje, Alikuwa makini sana. Hakutaka kabisa kukamatwa na Polisi kabla hajalipa kisasi kwa watu waliomkosea na kumletea matatizo makubwa hapa duniani.

************

Kwa upande wa Polisi ilikuwa shughuri pevu. Walisaka sana, walipekua sana lakini walikuwa hawajagundua kabisa Suto kaelekea wapi, walitafuta hasa huko Mbagala, Wananchi wa Mbagala waliteseka sana kutokana na msako huo, kila nyumba ilipekuliwa kumsaka Suto Sutani lakini hawakufanikiwa kumwona Suto. Ilikuwa kama wanamtafuta mtu ambayo hakuwahi kuwepo kabisa katika sura ya dunia.

Inspekta Jasmine kichwa kilikuwa kinamuuma. Sasa hakujua kabisa nani mwema na nani mbaya katika mkasa huu. Mkasa alioupa jina la 'Mkasa wa. Suto'.
Mkasa ambao ulisababishwa na penzi, penzi kati ya Suto Sutani na Bruno. Penzi lililoanza kama mas'hara, likashamiri ghafla kama uyoga, sasa penzi hilo lililokuwa na ndoto nyingi sana, ndoto za kuishi pamoja kama mke na mme. Penzi lililopigwa sana vita na wazazi wa Bruno siku ya kwanza tu lilipoanza, na sasa penzi hilo limegeuka kuwa chungu. Penzi Chungu kwa Suto Sutani.

Inspekta Jasmine alikubari, alikubari kushindwa kutatua utata wa mkasa huu, mkasa uliosababishwa na penzi. Aliamua asubuhi aende kwa mkuu wake wa kazi kuomba atolewe katika kuipeleleza kesi hii, na apewe mtu mwengine. kwa mara ya kwanza Inspekta Jasmine alishindwa kumtia mikononi mhalifu, kwa mara ya kwanza Inspekta Jasmine alikubari kushindwa. Maana aliona tangu kapewa kazi ile, hajapiga hatua yoyote ya kuitatua kesi ile, huku watu wakiendelea kuuwawa. Bila kumjua adui halisi ni nani.
Alijua atakumbana na maswali mengi toka kwa mkuu wake wa kazi, na pengine angedharauliwa sana na kukaripiwa, lakini uamuzi wake ulibaki palepale, aliamini kuwa kesi hii ilikuwa imemshinda!

**************

Asubuhi na mapema Suto Sutani aliamka kule nyumba ya kulala wageni, Gongo la mboto. Alioga vizuri na kutoka nje ya nyumba ile ya kulala wageni iliyokuwepo mtaa wa uswahilini sana. Kama bahati alikutana na kijana mmoja karibu tu na 'guest' ile akiuza visu. Alinunua visu kadhaa, maalum kwa ajili ya kazi iliyokuwa mbele yake.

Baada ya kununua visu, alitembea akielekea ilipo barabara kuu. Alikuwa anatafuta sehemu wanakouza magazeti.
Aliyapata.
Aliwakuta watu wengi sana walikuwa wamejaa kwenye meza moja ndogo ya magazeti iliyokuwa kandokando ya barabara. Alijipenyeza katikati ya kundi lile dogo la wanaume, macho yake yalitua gazetini.

"Suto muuaji auwa tena Mbagala !"

Hayo yalikuwa maneno yaliokozwa kwa wino mwekundu, mbele kabisa katika gazeti pendwa la Dumizi....

ITAENDELEA KESHO
 
SIMULIZI.... PENZI CHUNGU
MWANDISHI.. HALFANI SUDY
SIMU......... 0757633010

SEHEMU YA 27

Suto alistuka sana kuona kichwa kile katika gazeti la Dumizi, alilinunua gazeti lile na kurudi nalo katika guest yake aliyofikia kwa mwendo wa haraka sana. Huku akiwaacha watu wakimjadiri muuaji hatari Suto Sutani pale katika meza ya magazeti, bila kujua kwamba Suto mwenyewe walikuwa nae pale muda mfupi uliopita.

Suto alifika chumbani kwake, alikuwa amevaa miwani na kofia. Alivua miwani kisha akavua kofia kubwa aliyovaa kichwani. Akakaa kitandani na kuanza kuisoma ile habari iliyoandikwa kwa usanii mkubwa na mwandishi Veronica Baro.
Aliisoma habari ile mpaka mwisho, alisoma jinsi mwandishi alivyomhusisha katika mauaji yale ya mwanzo, ya watu watatu kule Tabata. Pia mwandishi akimhusisha na mauaji mapya yaliyotokea Mbagala rangi tatu alfajiri. Kwanza suto alishangaa sana uweledi wa mwandishi yule, kuandika habari ya upande mmoja tu kwa uhakika mkubwa bila kutoka kujua ukweli toka upande wa Mtuhumiwa. Pia Suto alishangaa sana uharaka wa kuchapa habari wa gazeti lile. Alifanya mauaji saa kumi alfajiri, saa mbili asubuhi alijisoma katika kurasa ya mbele.

"Eti Veronica Baro, una uhakika mimi niliwauwa wale vijana, una hakika ndugu mwandishi? Nitakutafuta Veronica unijibu maswali yangu, wewe ulikuwepo usiku ule? Ulinishuhudia mimi nikishika lile shoka na kulizamisha kifuani kwa yule kijana? Lazima unijibu hayo maswali Veronica, ukishindwa kujibu nitakuuwa Veronica, mimi umeninadi kama Suto muuaji, nitakuthibitishia sasa uuaji wangu!" Suto alikuwa anaongea na lile gazeti kama linamsikia vile. Au unaweza sema gazeti lile lilikuwa ndiye Veronica Baro mwenyewe.

Suto alilichukua lile gazeti la Dumizi. Akalishika kwa mikono yake yote miwili, na kulichana kwa hasira vipande vidogovidogo sana. Akavitawanya kwa fujo mle chumbani.

"Veronica Baro, umejiongeza mwenyewe katika orodha ya watu wangu niliopanga kuwauwa, orodha ya kifo, nitakuua Veronica !" Suto alikuwa anaongea na vile vipande vya gazeti sasa.

Suto alijiliza kitandani chali, akiliangalia bati chakavu la gesti ile ndogo.

"Maisha yamenibadirikia ghafla sana, leo hii nimekuwa natafutw....." Hakumalizia kauli yake.
Mlango wa chumba chake uligongwa kwa nguvu sana. Suto moyo ulimpiga kwa nguvu. Akainuka pale kitandani.

Ngo...Ngo.. Ngo...
Mlango uligongwa tena kwa nguvu zaidi.

"Askari" alijisemea mwenyewe kimoyomoyo.

Suto alikuwa anatetemeka mle chumbani kama kulikuwa kuna baridi kali. Aliona mwisho wake umefika, umefika bila ya kutimiza kisasi chake kwa watu walimsababishia madhila yale makubwa hapa duniani.

"Siendi kufungua mlango" alijisemea tena kimoyomoyo.
Ngo....Ngo....Ngo !
Mlango uligongwa tena kwa sauti kubwa zaidi.
Suto alilivuta begi lake lililokuwa uvunguni mwa kitanda.
Alitoa kisu !
Alikishika imara kwa mkono wake kushoto, alielekea taratibu kwa tahadhari kubwa sana pale mlangoni !
Kilikuwa ni miongoni mwa vipindi vigumu sana kwa Suto. Aliufikia mlango, alishika funguo kwa mkono wa kulia, akaanza kuuzungusha kuelekea kulia, mlango ulianza kufunguka taratibu, Ghafla ukasukumwa kwa nguvu...

ITAENDELEA BAADAE
 
Back
Top Bottom