Riwaya: Penzi chungu

Riwaya: Penzi chungu

SIMULIZI; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 53

Dotto alinieleza kila kitu kuhusu mbinu zao chafu, mbinu chafu zilizosababisha Suto Sutani aende jela bila hatia yoyote. Mama yangu mzazi alitumia pesa zake vibaya, Veronica Baro alitumia kalamu yake vibaya, Kulwa, Dotto na Dungu walitumia nguvu zao vibaya. Manka Edward alitumia uzuri wake vibaya. Walitumia vibaya ili kuhakikisha Suto Sutani anafungwa maisha, au Suto Sutani anauwawa!.

Dotto alinisimulia bila kujua kama mimi nilikuwa mhusika mkubwa sana katika mambo yale aliyokuwa ananisimulia. Hapo ndipo nilipoweka kisasi kwa mama yangu mzazi, kisasi kwa baba yangu mzazi, kisasi kwa Kulwa, Dungu na Veronica Baro. Mwandishi niliyetaka kumuua masaa machache yaliyopita.

*****

Huko Mwenge hoteli kwa Suto Sutani, Suto alipumzika vya kutosha, usiku ulovyoingia Suto Sutani alitoka nje kupata mlo wa usiku. Alipotoka nje alipata wazo, alitafuta duka na kununua kanga zingine. Alizivaa kanga palepale dukani. Ile laki mbili ilikuwa inamlinda bado. Alirejea kule hotelini na kuingia Mgahawani, alikaa katika Mgahawa mkubwa wa hoteli ya Ocafona inn, huku akimsubiri Mhudumu amwagizie chakula. Aliangaza watu waliokuwemo katika hoteli ile, alimwona!. Alimwona yule askari polisi aliyemuingiza kwenye gari kwa nguvu siku ile ya kwanza Suto kuingia selo. Yule askari aliyemwangalia kwa jicho la hasira wakati Suto Sutani akiingizwa katika gari la polisi.

Bila kujua kama kaikaribia hatari, askari yule akiwa na mwanamke mmoja pale mezani wakinywa sharubati na vibanzi. Nia ya Suto Sutani ilikuwa ni moja tu, kumfundisha yule askari madhara ya msukumo ule aliomsukuma Suto kwa nguvu kumuingiza ndani ya gari la Polisi. Suto alimuona Mhudumu wa mgahawa ule na kumuita kwa ishara ya mkono. Mhudumu alienda na Suto Sutani alimuagiza mchemsho na maji makubwa. Aliletewa na kuanza kula taratibu. Huku akimwangalia yule askari mara kwa mara. Mara, yule askari alinyanyuka, alikuwa anaelekea maliwatoni. Suto Sutani nae alinyanyuka, alibeba begi lake lenye visu, na kuelekea maliwatoni nae, kulekule alikoelekea yule askari....

ITAENDELEA baada
 
SIMULIZI; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 54

Askari alienda kwa mwendo wa kasi maliwatoni, mwendo ukioashiria alibanwa sana na haja ndogo. Alifanya kosa kubwa sana askari yule, aliingia ndani ya choo bila kufunga mlango. Askari alifungua zipu ya suruali yake, hakumaliza alichotaka kufanya, askari alipatwa na mstuko mkubwa sana, mle maliwato walikuwa watu wawili sasa. Alipata ugeni, ugeni wa Suto mtoto wa Sutani. Askari akiwa kashika zipu ya suruali yake macho yalimtoka!
Hakuamini.
Hakutegemea.
Suto alitabasamu kidogo, kisha alimuuliza yule askari.
"Unanikumbuka?"
Askari hakujibu.
"Naitwa Suto Sutani!"
Kutajiwa jina hilo, mkojo wa yule askari ulitoka kwa kasi, alijikojolea jamaa.
Suto Sutani hakujali ule mkojo, na wala hakujisumbua kuuangalia mkojo ule. Yeye alikuwa makini akiungalia uso wa askari yule. Uso uliotaharuki sana.

"Hivi hujui kumpandisha Mtuhumiwa ndani ya gari kistaarabu? Kwanza unajua maana ya Mtuhumiwa? Au wewe Mtuhumiwa unamchukulia kama mhalifu kamili. Nilikuwa Mtuhumiwa, ukanifanyia vile, ulinisukuma vibaya sana, unakumbuka Askari? Hivi nikikukosea nini mimi?

Swali hilo liliamsha kitu, kwa mara ya pili Askari ulimtoka tena. Sijui kama huu mkojo wa sasa kama ulikuwa umebakia toka ule wa mwanzo au ulikuwa mpya. Lakini Askari alijikojolea tena mbele ya Suto Sutani.
" Kumbe mwoga sana askari, hahaha, acha uwoga askari, sikuuwi, kosa lako halistahili kifo. Nitakupa adhabu ndogo tu Askari, hapana siyo adhabu, hizi ni salamu zangu kwenda kwa Inspekta Jasmine Wahabu. Naomba mkono wako..."
Huku akitetemeka askari alinyoosha mkono wake na kumpa Suto Sutani. Sijui alikitoa muda gani, sijui alikata muda gani, lakini kidole gumba cha mkono wa kulia cha yule askari kilikuwa kinarukaruka katika sakafu chafu za choo, damu zilikuwa zinambubujika Askari mkononi !.

"Hizo ni salamu zangu kwa Inspekta Jasmine"

Suto alisema na kutokomea gizani, akimwacha askari akipiga kelele kule maliwatoni..

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA.
 
Habari wanaJF

Kuna changamoto kuhusu hadithi ya Penzi Chungu... Kuna mfadhili ameitaka kuitolea kitabu.. Na sasa ipo kwa mhariri, jumatatu inaanza kuchapwa.

Changamoto iliyopo mfadhili hataki kuiona hadithi ikiendelea mtandaoni, akihofia soko la kitabu kushuka.
Hivyo kuanzia kesho ntakuwa naiweka moja moja na ntaishia sehemu ya sabini
 
Kama haikuhusu itakuwa inawahusu wanaofatilia funga domo lako pharegy
 
SIMULIZI; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU: 0757 633010

SEHEMU YA 55

Wateja wa Ocafona inn walijaa kule chooni. Wakimwangalia yule askari akibubujikwa damu mkononi. Huku akipiga makelele na kulitaja jina la Suto Sutani.
Ilikuwa hekaheka!

Meneja wa hoteli ya Ocafona inn, alipiga simu kituo cha Polisi kuwajulisha taarifa ile mbaya. Baada ya muda mfupi Polisi waliwasiri pale hotelini, na kuchukua maelezo juu ya taarifa ile. Wote walibaki mdomo wazi, kusikia athari ile ililetwa na Suto Sutani. Askari yule alikimbizwa hospitali, Mwananyamala huku msako mkubwa sana ulianza pale Mwenge na vitongoji vyake. Wakazi wa Mwenge nao waliipata hekaheka ya msako wa Suto Sutani. Lakini Suto Sutani hakuonekana, ilikuwa ni kama hakuwahi kufika Mwenge.

Yule askari aliyejeruhiwa alipelekea hospitali, askari alitibiwa kidonda chake. Kidonda kilifungwa na alipumzishwa kwa muda. Muda wote yule askari alikuwa analia huku akimtaja Suto Sutani.

Taarifa za kukatwa kidole yule askari zilimfikia Inspekta Jasmine akiwa nyumbani kwake. Na aliambiwa kwamba kidole hiko kilikuwa ni salamu zake. Inspekta Jasmine aliipokea taarifa hiyo siyo kwa mstuko mkubwa sana, kwa kuwa alikuwa na sehemu ya kuyahamishia matatizo yale, moja kwa moja alimpigia simu Daniel Mwaseba, na kumwambia salamu zile mbaya zilizotoka kwa Suto Sutani. Kama alidhani atasikia mstuko toka kwa Daniel, alifeli. Daniel hakustuka kabisa. Walipanga kukutana usiku uleule kuweka sawa mipango yao.

Wakati akiwaachia vumbi askari wa Mwenge baada ya kumkata kidole yule askari kama salamu zake kwa Inspekta Jasmine, Suto Sutani sasa alikuwa Tegeta.....

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 56

Suto Sutani alikuwa Tegeta amekaa kwenye kibanda kimoja cha mshona viatu. Suto Sutani ilimshangaza sana kumuona fundi yule akifanya kazi usiku. Ilikuwa ni nadra sana kwa fundi viatu kushona viatu usiku jijini Dar es salaam. Eneo lile kulikuwa na mwanga hafifu ukioangazia sehemu ile. Alitulia kwenye benchi kama anasubiri huduma pale, au anamsubiri mtu pale. Suto Sutani alikaa kimya huku akishuhudia vijana wakicheza mchezo wa draft.
Suto alitulia kimya akiangalia vijana wale wakicheza draft kimajigambo makubwa huku wakitupiana maneno ya kejeri.
Suto aliitathmini sehemu ile na kuona ni sehemu sahihi ya kuupitisha usiku ule. Nyumba ya kulala wageni alikuwa anaziogopa kwa siku ile. Alikuwa anajua walivyo Polisi wa Tanzania. Usiku wa tukio hufanya msako mkubwa sana. Lakini baada ya siku mbili tatu wanaacha. Hilo ndilo lililomfanya Suto Sutani apange kulala pale katika kibanda cha mshona viatu. Huku akichangamshwa na wale vijana wacheza draft.

"Mimi huniwezi Dula"
"Si utaona, nakufunga hili"
"Unajidanganya Dula"
"Hayaaaaaa nimeingia Suto hiyo, mveshe" Kibondo alisema baada ya kete yake moja kuingia king, alitumia neno Suto badala ya king.
Kauli ambayo ilimnyanyua Suto pale. Aliona pale siyo mahali sahihi tena. Alinyanyuka na kuondoka bila kuaga. Baada ya dakika kama kumi na tano Suto kunyanyuka pale kwa fundi viatu, waliingia Polisi kwa gari yao kwa kasi kubwa sana. Ilikuwa mshikemshike!
Polisi walifika palepale kwa fundi viatu...

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU ..0757 633010
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 57

"Habari zenu wazee"
"Salama kaka" Wale jamaa waliitikia huku wakiacha kucheza draft.
"Aisee kuna msichana mmoja tunamtafuta amejifunika kanga za bluu, chini na juu. Mrefu wastani hivi na ana begi mkononi"

Wale vijana walibaki vinywa wazi. Sifa zote walizotajiwa zilikiwa ni sifa za dada aliyekuja pale kwa kuwasalimia vizuri lakini kuondoka bila kuaga.
"Alikaa hapo!" Dula alisema huku akilionesha kwa kidole lile benchi alilokaa Suto Sutani.
"Una hakika alikuwa hapa, Polisi mmoja alisema huku akiwa na uwoga kidogo"
"Alikaa hapo na kaelekea kule muda mfupi uliopita"

Yule Polisi aliongea kwenye radio call kwamba Suto Sutani alikuwa Tegeta. Wale vijana walistuka sana baada ya kusikia Dada waliyekaa nae pale ni Suto Sutani, muuaji hatari sana nchini Tanzania.
Gari kumi za Polisi kutoka kituo kikuu cha Polisi zilikuwa njiani kuelekea Tegeta. Askari walikuwa wamevaa kivita, zana za kivita, na gari zikiwa kasi hasa kumuwahi Suto Sutani !

Askari walijipanga sana. Ilikuwa mithili wanaenda kumkamata jambazi mkubwa sana mwenye silaha za kutisha. Kumbe walikuwa wanaenda kukamata kumbe dhaifu kabisa, mwenye silaha dhaifu sana, visu.

Watu njiani walishangaa sana kasi ya gari zile kumi, zenye wastani wa askari kumi kila moja. Kwa hiyo zaidi ya askari mia moja walikuwa wanaenda Tegeta, Kuhakikisha Suto Sutani anakamatwa.

Taarifa za kuonekana kwa Suto Sutani Tegeta ziliwafikia pia Daniel na Inspekta Jasmine, nao walijipanga vizuri na kuelekea huko. Ilikuwa iwe isiwe, Suto Sutani lazima akamatwe!

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY

SEHEMU YA 58

Zile gari kumi za askari ziliwasiri Tegeta kwa fujo. Askari wote walishuka kabla ya zile gari hazijasimama. Kila mmoja akiwa na bunduki mkononi. Waligawa vizuri, na kila askari akiwa analijua vizuri jukumu lililomleta Tegeta.

"Kumpiga risasi Suto Sutani kisha kumkamata, na kumuuwa siyo mbaya pia" Ilikuwa ni kauli toka kwa Mkuu wa Operesheni ile. Kamanda wa kanda maalum ya Dar es salaam, Elvis Lema.

Askari waliingia kazini, huku maneno ya kamanda wao yakiwa kichwani mwao. Askari walitafuta sana, kwenye hoteli , kwenye mabaa, kwenye nyumba za kulala wageni lakini ilikuwa kazi bure. Hawakufanikiwa kumuona Suto Sutani.
Kwa mara nyingine tena Suto Sutani aliyeyuka!

Polisi sasa waliuhamishia msako wao mtaani, watembeaji usiku walikoma sana siku hiyo. Ilikuwa ni lazima uhojiwe, na ukijibu kisichoeleweka lazima upigwe kidogo na ikiwezekana uwekwe ndani. Ulikuwa usiku mbaya sana kwa walevi.

Inspekta Jasmine na Daniel Mwaseba nao walikuwa wanaenda kwa kasi kubwa sana Tegeta. Kwa lengo moja tu, kumkamata huyo Suto Sutani. Mwanamke aliyekuwa anatafutwa mithili ya gaidi kwa sasa.
Baada ya muda mchache nao walijiunga na wenzao pale Tegeta, walienda kuongeza nguvu, na nguvu iliongezeka hasa. Lakini nguvu hiyo haikusaidia kabisa katika kumkata Suto Sutani.

Wakati Polisi wakiigeuza Tegeta nje ndani, kumsaka Suto Sutani. Suto Sutani mwenyewe alikuwa katika kituo cha kujazia mafuta kama mlinzi Tegeta ileile.

Suto Sutani alivyotoka pale kwa mshona viatu, alitembea huku akiwaza wapi itakuwa sehemu salama kwake. Hakutaka kabisa kulala katika nyumba za kulala wageni, alijua huko atakamatwa haraka sana. Suto Sutani aliongoza barabara akienda asikokujua, mara akaiona sheli pembeni mwa barabara, hapo ndipo alipata fikra mpya, fikra ya kuupitisha usiku ule pale sheli, alihisi ni sehemu salama zaidi.
Alichunguza kwa makini mazingira ya sheli ile. Aligundua kuna mlinzi mmoja tu wa kike. Mlinzi aliyekuwa anasinzia gizani pembeni kabisa mwa sheli ile. Kwa mwendo wa kunyata alimsogelea mlinzi yule wa kike. Pigo moja tu la Suto Sutani aliyebadirika lilimfanya mlinzi yule azimie. Alimburuza hadi kichakani, alimbadirisha nguo, alimvesha nguo zake yake yeye, na Suto Sutani akavaa nguo za kilinzi. Alirudi tena kule sheli na kukaa kiti kile kile cha mlinzi, Suto nae alisinzia.

Inspekta Jasmine na Daniel walizunguka sana mtaani, mafuta ya gari yao yalipungua, wakaiona sheli. Wakawa wanaelekea kujaza mafuta sheli ileile aliyolinda Suto Sutani.

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
Samahani sana wana Jf Nasikitikika kuwaambia Kuwa tumeishia hapo kwani kitabu kimekamilika Kwa anae hitaji apige namba 0757633010
 
SIMULIZI YA KUSISIMUA; PENZI CHUNGU
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

Suto Sutani ni msichana ambaye hakuwahi kupendwa na mvulana yeyote katika maisha yake, kutokana na ubaya wa sura na ngozi yake. Katika hali ya kustaajabisha Suto anajikuta anaangukia katika dimbwi la mapenzi na kijana mtanashati Bruno Michael. Penzi linalopingwa na wazazi wa Bruno siku ya kwanza tu. Penzi linalomshangaza kila mtu pale mtaani.

Penzi kati ya Bruno na Suto linapitia katika visa na mikasa mingi sana ya kutisha na kusikitisha! Mikasa na visa ambavyo vinavyoondoka na roho za watu wengi sana. Mikasa inayomfanya Suto Sutani ageuke mkimbizi ndani ya nchi yake. Inafikia hatua Suto Sutani lazima auwe ili aweze kuishi. Mauaji anayoyafanya Suto Sutani yanamsogeza mpelelezi mahiri nchini Tanzania, Daniel Mwaseba kuingia kazini ili kujua siri iliyojificha juu ya mauaji hayo.

Je nini hatma ya Penzi kati ya Suto Sutani na Bruno Michael? Je mpelelezi Daniel Mwaseba atafanikiwa kujua kiini cha mauaji yanayotokea kila kukicha?

Kitabu kitakuwa mtaani kuanzia jumatano , piga a tuma msg uliza 0757 633010 ili kuweka oda ya nakala yak au kujua bei.
 
Back
Top Bottom