Riwaya: Penzi chungu

Riwaya: Penzi chungu

SIMULIZI.....PENZI CHUNGU
MWANDISHI ... HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 38

Suto alijipongeza sana kwa kupanda daladala ile. Daladala iliyomkutanisha na mmoja wa maadui zake!
Daladala ilienda huku ikishusha abiria na kupandisha wengine kama ilivyo kawaida. Hatimaye Suto Sutani naye alipata siti ya kukaa, katikakati ya daladala ile. Alikaa huku akiwa amepakata mkoba wake wenye vitendea kazi, visu vya kutosha kwa kazi maalum. Daladala ilipokaribia kariakoo yule abiria aliyekaa dirishani katika ile siti aliyokaa Suto alinyanyuka. Suto akasogea ile siti ya dirishani sasa, akajifanya amelala usingizi mzito.
Daladala ilifika mwisho, abiria wote walishuka, alibaki Suto Sutani pekee amelala ndani ya daladala.

Kondakta Banda aliangalia siti za gari yake, alimuona abiria mmoja amesalia, bila shaka amelala, alienda kwa mwendo wa haraka huku akipiga kelele za kumuamsha Suto.

"Huyo utalipa na hela ya kitanda hapa!"

Suto alijifanya kama hasikii, kumbe maneno yote yalipenya vizuri sana katika masikio yake. Banda alimkaribia sasa, taratibu Suto alichomoa kisu katika begi lake, alikishika imara kile kisu kwa mkono wake wa kulia. Banda alimuinamia Suto, kwa lengo la kumtikisa ili amuamshe, alimpigia kelele kali huku akiwa anamtikisa bega kumuamsha, lilikuwa kosa kubwa sana alilolifanya Banda kondakta. Ghafla! Kwa nguvu zake zote Suto alizamisha kile kisu katika tumbo la Banda. Lilikuwa ni tendo la haraka ambalo Banda hakulitarajia, na atalirarajia vipi wakati hakuwa anamjua kwamba yule ndiye Mfungwa aliyetumwa kwenda kumuua! Alitumwa kazi usiku, alienda kuitekeleza usiku. Banda alitoa mguno hafifu wa maumivu, alijaribu kupeleka mkono katika tumbo lake, lakini haukufika, akajitupa pale kwenye kiti, huku akiruhusu damu nyingi sana zichafue siti za daladala ile. Macho yaliangalia juu ya kipaa cha gari, yamemtoka pima mithili kaiona ndoto ya jaha. Wakati dereva wake akiwa nje ya ile gari, ndani ya gari konda aliuwawa ndani ya gari.
Ndio, Banda aliuwawa!
Taratibu Suto alinyanyuka, na begi lake lenye kisu, na kushuka nje daladala, bila wasiwasi wowote, kama abiria wengine. Alijichanganya kwenye kundi kubwa la watu pale sokoni Kariakoo. Huku akiacha dhahma kubwa ndani ya ile daladala....

"Suto amebadirika!"

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA.
 
SIMULIZI......PENZI CHUNGU
MWANDISHI..HALFANI SUDY
SIMU: 0757 633010

SEHEMU YA 39

Kule gerezani Segerea kwa Beji hali ilikuwa ya taharuki kubwa sana!. Askari wengi walikuwa wamemzunguka Beji, wakiwa hawaelewi ni kitu gani kilichomtokea. Beji alikuwa ametapakaa damu mwili mzima, kasoro kichwa tu. Hata sehemu sahihi iliyopata jeraha ilikuwa haijulikani. Ilikuwa damu tupu!

Ni mkuu wa Gereza mwenyewe ndiye aliyekuwa wa kwanza kuuona mwili wa Beji pale chini. Alikuwa anatoka ofisini kwake ili kwenda haja ndogo, alishangaa sana kuuona mwili wa askari wake wa zamani ukiwa umelala hoi huku umeegemea ukuta. Aliusogelea taratibu.
Aliona Damu !
Aliushangaa mwili ule ulivyotapakaa damu, hakuelewa kabisa Beji amekumbwa na nini. Alipiga simu polisi kuwataarifu juu ya tukio lile la kutisha sana, kuwahi kutokea katika Gereza la Segerea. Wakati wanawasubiri askari Polisi ndipo askari wengine walijaa katika eneo lile. Wote walipigwa na butwaa, hawakuelewa kabisa kilichomkumba askari wa zamani Beji.

Baada ya nusu saa askari Polisi waliwasiri, wakiwa pamoja na daktari. Baada ya uchunguzi wa daktari uliochukua nusu saa, mwili wa Beji ulichukuliwa na kukimbizwa haraka hospitali. Kwa bahati nzuri Daktari aligundua kuwa Beji alikuwa hajafa, ila mapigo yake ya moyo yalikuwa chini sana.

Wakati hayo yanatokea huko Segerea, Inspekta Jana alikuwa ameketi ofisini kwake, akitafakari mwenendo wa kesi ya Suto Sutani, hakuelewa kabisa Suto anaupata wapi uwezo wa akili wa kuwakimbia Polisi waliopitia mafunzo namna ile. Historia yake ilionesha kwamba Suto hakumaliza hata darasa la saba, Siyo! Suto hakuanza hata darasa la kwanza. Historia hiyo ilizidi kumtia hasira Jasmine, askari msomi, anayeheshimika sana na viongozi wa juu Serikali na wananchi wa Tanzania kwa ujumla kwa weledi wake, kwa umakini na uchapakazi wake, leo hii anazidiwa ujanja na Suto? Ilikuwa ni dharau kubwa sana.

Wakati Akiwaza hayo simu yake ya mezani iliita, simu ilitoka kwa yule askari Polisi aliyeenda kule Segerea, alimpa taarifa ya kuchomwa kisu kwa Beji!
Inspekta Jasmine alihamanika sana!
Dakika tano baadae alipokea tena simu, ilikuwa inatoka sokoni Kariakoo, simu yenye taarifa ya kuchomwa kisu kondakta wa daladala na kuuwawa!
Inspekta Jasmine hakuelewa, aende Kariakoo ama Amana hospitali ulikopelekwa mwili wa Beji?
Hakika alichanganyikiwa sana !

"Ngoma nzito kwa Inspekta Jasmine! "

ITAENDELEA
 
SIMULIZI....PENZI CHUNGU
MWANDISHI...HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 40

Inspekta Jasmine alitoka nje ya ofisi yake. Alichukua pikipiki yake, aliiondosha kwa kasi kubwa lakini akiwa hana uelekeo maalum, hajui aende Amana hospitali ama Kariakoo sokoni. Lakini akiwa juu ya pikipiki alipata maamuzi, aliamua kwenda Amana hospitali, alijua mwili wa huyo mtu aliyeuwawa Kariakoo nao utapelekwa Amana tu.

Baada ya kufanya mauaji yale ya kikatili, Suto Sutani aliona Kariakoo siyo mahali salama tena kwake, alijua muda mchache ujao kariakoo itajaa maaskari wakimsaka muuaji wa kondakta yule. Hakutaka kabisa kukutana na Polisi wakati bado hajamaliza alichopanga kufanya, Suto Sutani alipanda daladala inayoelekea Mwenge kutokea Kariakoo.
Suto bado alikuwa na hela za kutosha, zile shilingi laki mbili za yule mvamizi kule gerezani bado zilimlinda. Alijua askari sasa itakuwa wameacha kumtafuta Hotelini. Alifika Mwenge na kuchukua chumba katika hoteli iitwayo Ocafona inn, chumba namba 41. Kuingia tu ndani alilala usingizi mzito sana sofani, maana alikuwa hajalala vizuri kwa siku mbili mfululizo.

Wakati Suto Sutani akilala katika hoteli Ocafona inn. Inspekta Jasmine alikuwa anateremka katika pikipiki yake, aliwasiri katika hospitali ya Amana, iliyopo Ilala. Moja kwa moja Inspekta Jasmine alienda ofisini kwa dokta Boniface, kujua hali ya mgonjwa mpya aliyeletwa, Beji.

"Za siku nyingi dokta"
"Safi, vipi za kazi?"
"Kazi imekuwa kazi kweli, vipi huyo mtu aliyepigwa kisu anaendeleaje?"
"Mgonjwa yuko ICU, kile kisu kiliingia sana shingoni, na kapoteza damu nyingi sana"
"Umeongea na mgonjwa hata kidogo dokta, anasema nini kilitokea dokta?" Inspekta Jasmine aliuliza kwa wahka mkubwa.
"Mgonjwa hajibu chochote anachoulizwa, yeye anasema neno moja tu tena kwa sauti dhaifu, Suto Suto Suto basi, nadhani anamzungumzia yule mwanamke muuaji.
Taarifa hizo zilimchosha kabisa Inspekta Jasmine, kabla hawajaamua wafanye nini simu ya dokta Boniface iliita.

" Nakuja sasa hivi" Dokta Boniface alijibu baada ya kuisikiliza simu, alitoka mbio huku akimwacha Inspekta Jasmine kapigwa na butwaa. Naye alitoka nje kinyonge. Alivyotoka nje aliona mwili wa mtu mwengine ukiwa umebebwa katika machela, na kupelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti, baada ya kuuliza, Inspekta Jasmine aliambiwa ulikuwa mwili wa kondakta aliyeuwawa Kariakoo, Inspekta Jasmine akajua sasa mambo yamekuwa mambo.

Akiwa kasimama palepale ghafla alishikwa bega, Inspekta Jasmine alistuka sana. Aligeuka nyuma kwa haraka, mkono wake wa kulia ukiwa umeshafika kiunoni kuitoa bastola yake.....

ITAENDELEA baadae kidogo samahani jana cm ilizima chaji
 
SIMULIZI.....PENZI CHUNGU
MWANDISHI..HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 41

Alikuwa anatazamana na Dokta Boniface.
"Beji amefariki !"
"Unasema.."
"Alipoteza damu nyingi sana, amefariki Afande"
Chozi la hasira lilimtoka Inspekta Jasmine. Alikuwa anatumaini atapata kila kitu kutoka kwa Beji.
"Siku ya kukukamata Suto utajuta, utalipa damu ya watu hawa, nakwambia utalipa Suto, na nitakukamata tu Suto, hakuna marefu yasiyo na ncha, hakuna Suto, wewe ua, nami nitakipasua vibaya sana kifua chako kwa bastola hii Suto. Nitakuuwa baada ya kukupa mateso makali sana, chozi hili utalilipa Suto....."

"Vipi Inspekta mbona unalia?" Inspekta Jasmine alikatisha anachoongea na kumwangalia aliyemuita, alistuka sana, alikuwa ni Daniel Mwaseba !
Mpelelezi namba moja nchini Tanzania, kijana shupavu, jasiri, mwerevu, anayetumia akili nyingi sana katika kukamata wahalifu. Kijana asiyeogopa misukosuko katika kukamata wahalifu. Ni nani asiyemjua Daniel Mwaseba nchini Tanzania. Kijana aliyelisaidia Taifa katika mipango mingi mibaya iliyopangwa na maadui wa Taifa hili. Daniel Mwaseba alikuwa anatabasamu mbele ya chozi mwanana la Inspekta Jasmine.

"Hatukufunzwa kulia kutokana na matatizo, tulifunzwa kutatatua matatizo, iweje akulize Mhalifu afande, ni udhaifu na aibu pia" Daniel Mwaseba alimwambia Inspekta Jasmine.
"Afadhali umekuja Daniel, afadhali" Inspekta Jasmine ilikuwa kama hajayasikia maelezo ya Daniel, alikumbwa na furaha iliyoambatana na fadhaa, kumuona Daniel kwake ilikuwa ni kuisha kabisa kwa kesi anayoifatilia.

"Eeh nambie Inspekta, tatizo hasa nini?"
"Suto Sutani! "
"Suto" Daniel aliuliza kwa sauti kubwa.
"Unamjua Inspekta?"
"Anyway, tutafute sehemu nzuri tuongee"
"Twendeni mukaongelee ofisini kwangu" Dokta Boniface alitoa ushauri wake.
"Sawa dokta" Walikubaliana nae.

Askari wale wawili walienda ofisini kwa dokta Boniface. Waliketi vizuri vitini na kuanza kuongea.

"Eeh Daniel unamjua Suto?"
"Mmh simjui sana, lakini nipo hapa kwa ajiri ya kumjua Suto, na kujua vitu zaidi kuhusu Suto Sutani"
"Unataka kujua nini zaidi ya kukwambia Suto Sutani ni muuaji hatari zaidi kuwahi kutokea hapa Tanzania" Inspekta Jasmine aliongea kwa msisitizo.
"Ngoja nikwambie kwanini nimemfata Suto hapa"
Inspekta Jasmine alitulia tuli, na Kumsikiliza Daniel ambaye alimsimulia mambo mapya kabisa yanayoihusu kesi ile....

ITAENDELEA
 
SIMULIZI....PENZI CHUNGU
MWANDISHI..HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 42

"Nimewasiri jana toka Ujerumani. Baada ya kuwasiri tu katika ardhi ya Tanzania, IGP aliniita. Nilitoka uwanja wa ndege wa kimataifa wa Juliuas Nyerere moja moja kwa moja nilienda kituo kikuu cha Polisi. Niliwakuta watu watatu ofisini, wote wamekaa wameshika tama. Wakiwa wamezongwa na mawazo.
Nilimkuta Waziri wa mambo ya ndani ya nchi, nilimkuta mkuu wa majeshi, pamoja na mkuu wa Polisi Tanzania.
Kwa jinsi nilivyowakuta wamekaa nikajua kuna tatizo kubwa sana lililokuwa linawakabiri.
Mkuu wa Polisi, kamanda John Rondo ndiye aliyenikaribisha na kuniamuru nikae kwenye kiti, nilikaa nikiwa na hofu sana. Sikujua ni kitu gani kilichowakutanisha wakuu wale wakubwa wa nchi, tena wakiwa katika hali ya wasiwasi namna ile, IGP John Rondo alianza kuongea, kabla hata ya kusubiri nitulie vizuri kitini.
Alinambia mambo makubwa sana, mambo ambayo yalikuwa rahisi sana kuingia katika masikio yangu, lakini yalikuwa magumu sana kuyaelewa. Hata John Rondo mwenyewe hakuwa na uhakika sana na alichokuwa anakieleza, lakini mwishoni alinielekeza kwa mtu ambaye anaweza kunifafanulia mambo hayo, alinambia niende kwa usiri mkubwa sana, na nitumie ushawishi mkubwa sana ili aweze kunambia mambo hayo. Ni yeye aloyeyashuhudia mambo hayo, huku akionywa kutotoa siri ya mambo hayo, kutoa siri ni kuweka rehani maisha yake. Mtu huyo ni mwanamke, anaitwa Magdalena Zomba, lakini watu wengi wanamtambua kama mama Suto. Nilitoka pale kituo cha Polisi na kuelekea Tabata, nyumba akiyoishi mama Suto, niliwakuta majirani wachache, walionieleza kuwa mama Suto amefariki siku kadhaa, sasa nikajua kazi imeanza. Ndio nimekuja hapa moja kwa moja kuulizia ripoti ya uchunguzi wa kifo cha mama Suto iko wapi, nami nianze kazi yangu"

Inspekta Jasmine mwili wote ulikuwa unamtetemeka, alikumbuka alivyoidharau na kuipoteza ripoti zile za daktari kizembe, kumbe ripoti zile hasa ya Mama Suto ilikuwa na umuhimu mkubwa sana, ripoti ambayo ingetoa njia kwa kukamatwa kwa hao watu, wenye nia mbaya lakini isiyoeleweka wazi kwa wakuu wale wa Polisi na mkuu wa jeshi.

"Ripoti zilipotea Daniel" Inspekta Jasmine aliingea kwa sauti yenye kitetemezi.
"Zimepotea vipi Inspekta?"
"Kuna kibaka aliiba tukiwa katika foleni, na kufanikiwa kukimbia nazo"
"Come on Inspekta, hatufanyi mambo kiurahisi namna hiyo, alikukimbia vipi kibaka Inspekta ?."

Inspekta Jasmine hakuwa na la kusema, alimuomba radhi Daniel, huku akimuomba taarifa ya kupotea kwa ripoti asiipeleke kwa IGP.
"Sasa insp...." Daniel hakumalizia alichotaka kusema, simu ya Inspekta Jasmine ilikuwa inaita.
Akaipokea.
"Mnafanya kazi gani Inspekta, raia wenye hatia wanaendelea kuuwawa, au unataka tuandike kwamba jeshi la polisi ni wazembe kuliko taasisi yoyote Tanzania" Bila salamu Veronika Baro aliwaka kwenye simu.
"Come down mwandishi, tunalifanyia kazi"
"Hadi lini Afande, tuandikaje sasa kwenye magazeti, tuandike nini zaidi ya uzembe wa jeshi la Polisi ?." Inspekta Jasmine hakutaka kuendelea Kumsikiliza mwandishi yule alikata simu.
Mara, simu yake ilianza kuita tena, hakuipokea, alikuwa anaitazama tu mithili ya mtoto akiungalia kwa makini mdoli wake...

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA.
 
SIMULIZI....PENZI CHUNGU
MWANDISHI...HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 43

Daniel alimwangalia kwa huruma askari mwenzie, akajua kesi imemshinda, kwa mkanganyiko uliokuwepo katika kesi ile. Inspekta Jasmine aliendelea kuiangalia tu simu yake iliyokuwa inaita.

"Lete simu" Daniel alimwambia Inspekta Jasmine.
Bila kipingamizi wala ubishi wowote Inspekta alimpa simu yake Daniel Mwaseba.
Daniel aliipokea ile simu na kuongea kwa kujiamini.

"Naitwa Daniel Mwaseba, unahitajika leo katika kituo cha Polisi cha kati saa kumi jioni" Lengo la Daniel kusema hivyo ilikuwa ni kumfanya Veronica aiogope na kuiheshimu dola, lakini kauli ile ilipokelewa tofauti sana na Veronica.
"Daniel Mwaseba, umerudi?"
"Ndio, na nakuhitaji kwa mahojiano saa kumi jioni kituo cha Polisi kati" Daniel alisema bila kubabaika. Ghafla! Simu ya upande wa pili ilikatwa!
"Kuna kitu itakuwa anakijua huyu mwandish wa habari " Daniel alisema huku akimwangalia Inspekta Jasmine usoni.
"Sikuelewi Daniel"
"Hujaisikia sauti ya huyu mwandishi, baada ya kujua tu anaongea na mimi ameingiwa na woga, woga huo unajidhihirisha pia katika sauti yake, kwa nini aniogope, kama yeye ni mwandishi wa habari mzuri mwenye lengo la kupata habari tu ?"
Inspekta Jasmine alianza kuelewa sasa.
"Huyu mwandishi anaitwa nani?" Daniel aliuliza.
"Veronica, Veronica Baro"
"Sawa, mweke kwenye orodha yetu ya watu wa kutupeleka kwenye lengo"
"Sawa Daniel"
"Hapa hamna cha kusubiri, twende kituoni tuone kama Veronica Baro atakakuja, akija tutajua mbivu na mbichi baada ya kufanya nae mahojiano, asipokuja tutajiridhisha na tunachokihisi"
"Sawa Daniel"

Inspekta Jasmine alianza kuuhusudu uwezo wa Daniel Mwaseba. Siku ya kwanza tu kuingia Daniel katika kesi hii walianza kupiga hatua muhimu sana...

ITAENDELEA
 
SIMULIZI: PENZI CHUNGU
MTUNZI: HALFANI SUDY.
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 44

Kule upande wa pili kwa mwandishi wa habari nguli wa gazeti la Dumizi hali ilikuwa mbaya. Veronica Baro alikuwa anatetemeka, hajui lipi afanye, hajui lipi aache.
Mara nyingi sana alikuwa anamsifia Daniel Mwaseba katika makala zake mbalimbali gazetini. Alikuwa anaufahamu sana uwezo wa Daniel Mwaseba, kwa kuusikia uwezo wake na yeye kuuandika kwenye gazeti kwa umahiri mkubwa sana. Sasa leo hii alikuwa anaitwa kituo cha Polisi ili akahojiwe na Daniel Mwaseba.
Aliikumbuka vizuri sana makala yake moja aliyoiandika katika gazeti la Dumizi, miaka mitatu iliyopita. Makala yenye kichwa cha habari.
" Daniel, Mwanaume Hatari Zaidi Duniani" Makala hiyo ilimpa heshima sana Veronica Baro na kwa kiasi kikubwa ilichangia kupata tuzo ya mwandishi bora wa kike kwa mwaka huo. Tangu mwaka huo, Veronica aliendelea kuitwaa tuzo hiyo.
Veronica alikumbuka kuwa tamaa ya pesa ndiyo iliyomponza. Pesa za mama Bruno zilifanya Veronica Baro aitumie kalamu yake vibaya. Amkandamize Suto Sutani, ashindwe kabisa kuweka uwiano katika habari zake kuhusu Suto Sutani.
Sasa maji yalikuwa shingoni kwake.

Saa kumi kasoro dakika kumi na tano, Veronica Baro aliwasiri kituo cha Polisi cha kati. Alipokelewa na askari mmoja aliyemkuta kaunta. Baada ya kujieleza kuwa alikuwa na miadi na Daniel Mwaseba, alikaribishwa katika kiti kilichokuwepo pale mapokezi. Veronica Baro alionesha uwoga dhahiri usoni mwake, sura yake ilikuwa mithili ya mwanafunzi aliyekuwa anasubiri adhabu ya bakora toka kwa mwalimu anayemuogopa sana. Moyoni sasa roho ilimpwitapwita, miguu ilimtetema, alikuwa na hofu, hofu ya kukutana na Daniel Mwaseba!.
Saa kumi kamili ilifika, Veronica akiwa amekaa palepale, lakini Daniel Mwaseba alikuwa hajawasiri bado pale Polisi.
Saa kumi na nusu, Veronica ilimkuta amekaa palepale kitini,

Mara alinyanyuka kwenye kiti, muda huohuo Inspekta Jasmine aliingia akiwa katika sare zake safi za jeshi la Polisi. Kwa ishara ya mkono alimuashiria Veronica akae, bila kutafakari Veronica Baro alijipweteka tena kitini. Inspekta Jasmine alisalimiana na yule askari aliyekuwepo pale kaunta na kuingia ndani. Woga wa Veronica ulirejea kwa kasi zaidi safari hii. Kutosalimiwa na Inspekta Jasmine ilionesha kuna tatizo ndani yake. Sasa tumbo lilianza kumuunguruma. Ishara mbaya zaidi kwa mtu mwenye woga.
Inspekta Jasmine alirudi tena. Kwa mwendo wake wa madaha, kofia yake ya kipolisi ikiwa kaishika mkononi. Alimkaribia kabisa Veronica Baro, kisha akamuonesha ishara kuwa asimame, Veronica alisimama. Inspekta Jasmine alitoka nje akimwacha Veronica amesimama vile vile....

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI: PENZI CHUNGU
MWANDISHI: HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA 45

"Hivi ndivyo anavyopaswa kufanyiwa mwandishi wa habari?" Veronica Baro alimuuliza kwa hasira askari aliyekuwepo pale kaunta.
"Hapana....Hiyo ni namna sahihi ya kuwafanyia wahalifu!" Inspekta Jasmine alikuwa anaongea kumjibu Veronica huku alikuwa anaingia tena ndani.
Veronica Baro alistuka sana, lakini akajivisha ujasiri wa bandia.
"Nani mhalifu Inspekta Jasmine, kauli zitakuponza" Veronica Baro alimtisha kidogo Inspekta Jasmine.
"Kama wewe zilivyokuponza pesa" Inspekta Jasmine alimjibu bila kumwangalia usoni.
Kusikia kauli hiyo, moyo wa Veronica ulipiga kwa nguvu, akajua ameshajulikana, alihisi kama kavuliwa nguo zote, tena akiwa katikati ya soko.

Inspekta Jasmine alipatia, ni kweli pesa zilimponza Veronica, ingawa yeye ilimtoka tu hiyo kauli, hakukusudia.
"Nifate" Inspekta Jasmine aliongea huku akiiondoka, huku Veronica Baro akisimama na kumfata Inspekta Jasmine mithili ya mkia. Wakaingia katika ofisi moja pale kituoni. Kwa haraka Veronica Baro alifanikiwa kusoma kilichoandikwa juu ya mlango ule. Maneno makubwa yaliyonakshiwa kwa rangi nyeusi yalisomeka.

OFISI YA UPELELEZI WA MAKOSA YA JINAI.

Alipoingia ndani alimkuta Inspekta Jasmine ameshakaa tayari, kwenye kiti kilichokuwepo nyuma ya meza pekee iliyokuwemo mle ofisini. Meza iliyojaa mafaili na makaratasi mbalimbali.

"Karibu mwandishi bora nchini Tanzania"
Veronica Baro hakujibu, ajibu nini wakati mambo yalimuendea kombo kwa haraka sana. Hata hela zake alizopewa alikuwa hajazitumia vizuri. Leo hii anaingia matatani.

Veronica alikaa kitini, macho yake makubwa akiyainamisha chini kwa aibu.

Mara simu ya Inspekta Jasmine iliingia ujumbe, ujumbe toka kwa Daniel Mwaseba.

"Usimhoji chochote huyo Mwandishi, mruhusu tu aondoke"

Inspekta Jasmine aliushangaa sana ujumbe ule, alitamani kumuhoji Veronica kwa sababu aliona kila dalili kuwa Veronica Baro kuna vitu anavijua katika sakata lile. Hiyo ndio sababu iliyomfanya atamani kuupinga ujumbe wa Daniel lakini hakuweza. Kumpinga Daniel Mwaseba ni kumpinga Raisi wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania, aliyempa dhima hiyo Daniel Mwaseba.
Veronica Baro aliruhusiwa kuondoka bila ya kuhojiwa chochote pale kituoni.....

"Nini lengo la Daniel Mwaseba? Tuwemo wote katika sehemu ya 46"

ITAENDELEA
 
Back
Top Bottom