NJAMA
SURA YA NNE
FUNUNU III
"Mimi naona tukapate chakula cha mchana
kwanza", Sherriff alishauri.
"Sawa", walijibu kwa pamoja. Sherriff alikaa nyuma
pamoja na Margret na wakati huo mimi naendesha
nikiwa katika mafikara mengi, Sherriff alichukua
jukumu la kumtuliza Margret akimweleza mambo
mengi juu ya matatizo ya binadamu na kumwambia
kuwa asihuzunike sana maana ndiyo binadamu.
Kadiri Sherriff alivyozidi kusema ndivyo Margret uso
wake ulizidi kutokwa na huzuni kwani mimi
nilikuwa nawaangalia katika kioo cha kuendeshea.
Hata Sherriff alipofika kusema yeye huwa anaamini
kuwa kwa kila linalotendeka linatendeka kwa ajili
ya uzuri, nilimwona Margret anamwemwesa kwa
mara ya kwanza, na ndipo sura yake ilionyesha
uzuri aliokuwa nao. Niliona hata Sherriff aligundua
uzuri huo, kwani uso wake ulibadilika kiasi cha
kwamba moyo wake uliguswa.
Tulifika New Afrika Hoteli, nikaegesha gari wote
tukatoka nje. Basi, moja kwa moja tulifuliza
kwenda kwenye lifti ya kutupeleka orofa ya kwanza
ambapo ndipo Bandari Grill ilipo. Mbele yangu
nilimwona Eddy anavuka sehemu ya mapokezi,
halafu akazungusha kichwa akaingia kwenye choo
kilichopo hapa chini. Hii ilikuwa ishara kuwa alitaka
kuniona.
"Samahani jamani nasikia nimebanwa haja ndogo,
tangulieni nakuja sasa hivi. Margret, we ndiye
mwenyeji washughulikie wagaeni".
"Bila wasiwasi", alijibu akiwa anaanza kupona
kutoka katika mshituko alioupata.
Niliingia maliwatoni nikamkuta Eddy ananisubiri.
"Mpaka dakika hii hakuna chochote", aliniambia
bila kuniangalia.
"Sawa, nendeni mkale halafu nenda ofisini
nitakukuta huko kiasi cha saa kumi hivi".
"Oke", alisema huku akielekea kwenye mlango wa
kutokea.
Mimi nilimaliZa haja yangu ya uongo na kweli
nikaondoka kujiunga na wenzangu. Tulipata muro
safi sana hapa Bandari Grill, na kwa sababu kila
mtu alikuwa na njaa tulikula kimya kimya.
"Nasikia kichwa kinaniuma", Veronika alilalamika.
"Nafikiri kwa ajili ya hali ya hewa. Joto jingi sana
kuliko ulilozoea", nilimjibu.
"Kama ni hivyo afadhali ukameze dawa upumzike,
sisi tutakwenda kumwona Kiki halafu tutakuja
kukuona", Sherriff alishauri.
"Naona hivyo ni sawa", alijibu.
Basi tulikubaliana Veronika apumzike sisi tuendelee
na shughuli. Tuliondoka New Afrika na
kumtelemsha Veronika Kilimanajaro.
"Vero mpenzi, kuna gari lile pale unaweza kulitumia
wakati wowote. swichi iko chini ya zulia",
nilimuonyesha gari ambalo Eddy alikuwa ameliacha
hapo. Sisi tuliondoka na kuendelea na safari yetu
ya Kinondoni.
"Twende kupitia barabara ya Upanga moja kwa
moja, halafu tukivuka Salendar briji mbele kuna
barabara ya Kinondoni hivyo tutaingia kushoto.
Sehemu iko mbele ya makaburi. Baada ya
makaburi kuna barabara la vumbi, linakatisha
barabara hii. Tukiacha hilo na kuendelea mbele
tukakuta barabara nyingine ya vumbi inaingia
kushoto na kuna kibao kimeandikwa Bamboo Baa
and Restauranti, basi hapo ndipo tutakapoingia",
alieleza Margret kwa ufasaha kabisa.
Mimi hupenda maelezo ya namna hii, siyo mtu
amefika mahali pa kukata kona ndipo anasema,
kata hapa kushoto. Maelekezo hayo ni ya kihuni na
ndiyo anayosababisha ajali nyingi.
Nilifuata maelezo ya Margret vizuri kabisa,
nilipotaka kuingia kushoto pale kwenye bao la
tangazo la Bamboo Baa and Restauranti, Margret
alisema, 'Njia hapa si nzuri twende pole pole,
halafu mbele kidogo utakata kushoto tena tuelekee
kwenye nyumba hizo pale", alinielekeza na
kuonyesha kwa kidole.
Niliendesha pole pole nikaikuta njia na kuifuata
kuelekea kwenye nyumba hizi za shirika la nyumba.
"Baada ya nyumba hiyo yenye bendera ya CCM,
ambayo ndiyo ya mjumbe, ya pili yake".
"Hapa?".
"Ndio, mlango huu huu".
Nyumba hizi zinakaa familia mbili mbili, lakini
zimetengwa katikati kiasi kwamba kila familia ina
sehemu yake kamili. Tulitoka ndani ya gari,
Margret akatangulia na kibisha hodi. Lakini
hatukupata jibu. Nilisikia moyo wangu unapiga
haraka haraka, hii ni sirika niliyozaliwa nayo, na
ilikuwa ni ishara kuwa kuna hatari.
"Hebu ngoja Margret", nilimwambia nikimrudisha
nyuma.
Niliujaribu mlango ukafunguka nikamwita Sherriff
na kumwambia hakuna mtu, tulifungua mlango
mwingine uliokuwa unaelekea jikoni, bafuni na
chumba cha kulala. Tukiwa wote na wasiwasi
tukibisha hodi kwenye mlango wa chumba cha
kulala. Lakini hatukupata jibu. Nilitoa Bastola
yangu, na kusukuma mlango wazi.
Tulimkuta mtu ambaye tuliamini ni Kiki
amechomwa kisu kifuani!, nilipomshika nikajua
alikuwa amekwisha kufa saa nyingi sana. Kisu
kilikuwa kimeachwa pale kifuani. Kilikuwa kisu
kikubwa na mpini wake mwekundu. Tulimwita
Margret aje atuhakikishie.
Akiwa anatetemeka kwa woga alikuja na kusema,
"Ndiye yeye masikini", akaanza kulia tena
tulimbembeleza na kumvuta na kuondoka haraka
haraka ndani ya nyumba hiyo. Tuliingia katika gari
langu na kuelekea mjini. Sasa nilianza kuongeza
hesabu kwamba mbili na mbili na kupata nne. Na
vile vile majahiri hawa walianza kunitisha kwani
mbinu zao zilikuwa kubwa. Lakini hata hivyo mbinu
za Willy ni kubwa zaidi.
"Mapambano yameanza Sherriff", nilisema kwa
sauti ambayo sikuamini ilikuwa yangu.
"Na kweli yameanza", Sherriff alijibu.
Wakati huo tulikuwa tumesimama kwenye taa za
usalama barabarani za salendar briji tukuelekea
New Afrika. Saa yangu ilisema ni saa kumi na
dakika mbili.
"Naona mimi mnifikishe nyumbani", Margret
aliomba.
"Unakaa wapi".
"Ninakaa kwenye orofa pale nyuma ya Rex Hoteli".
"Nazijua orofa hizo, uko orofa ya ngapi, maana
tunaweza kukuhitaji ama kikazi ama katika hali ya
kustarehe, unasemaje?".
"Karibu mimi niko orofa ya pili chumba namba
kumi na nane. Simu yangu ni 22221".
Basi wakati huo tulikuwa tumefika Posta ya
Azikiwe, tulipofika kwenye sanamu ya Bisimini,
tukaingia Independent Evenue.
"Unajua", Margret alitugutusha.
"Ehee", nilijibu na kumwangalia ndani ya kioo cha
kuendeshea, maana yeye alikuwa amekaa nyuma.
"Sijui ni mafikara yangu, ila tu limekuja kama wazo
la kunishangaza, maana baada ya kutokea mambo
haya kila kitu nakiona si cha kawaida
kinanigutusha".
"Nini kimekugutuusha?", Sherriff aliuliza akionesha
msisimko.
"Unajua pale kwenye lango la kuingia ndani ya ofisi
yetu kumekuwa na mwendawazimu ambaye
amekaa pale zaidi ya mwezi mzima. Amekuwa
amevaa matambalatambala tu na amebeba
makopo mengi, sijui mmemuona?".
"Mimi nilimwona", Sherriff alijibu.
"Mimi sikumwona".
"Polisi walikuja kumchukua siku moja, na
kumpeleka kunakohusika lakini hazikupita saa tatu
akarudi. Alikuwa hatoki pale hata dakika moja,
usiku na mchana kutokana na walinzi wa usiku
wanavyosema. Leo mlipokuja alikuwepo maana
mimi niliona gari lenu linaingia wakati natoka
kunywa chai. Gari lenu lilipoingia na yeye alivuka
lango akaingia ndani. Hii ni kawaida yake, kwani
huwa anaombaomba kwa kila mgeni anayefika pale
ofisini na ndio sababu aliitiwa polisi kwa sababu
anawafadhaisha wageni wetu. Gari lenu mliliegesha
mbele kabisa ya mlango wa kuingia mapokezi na
kutoka ndani ya gari haraka hivyo hakuwahi. Mimi
nilipoingia pale mapokezi nilikuta nyinyi
mmekwisha kwenda ofisini kwa Mantare ila
nilimkuta yule kichaa anamuuliza yule msichana
wa mapokezi. Hawa watu wanasema wanatoka
katika gazeti la Afrika. Yule msichana wa mapokezi
alikasirika na kumfokea, Toka hapa! kama
wanatoka gazeti la Afrika watakufaa nini wewe?,
wana kazi ya maana kuliko kuonana na
mwendawazimu kama wewe. Toka!".
"Kitu cha kushangaza ni kwamba wakati
tunaondoka pale ofisini kwetu nakumbuka
sikumuona wala makopo yake na kilago chake
hakikuwepo, sijui jambo hili lina maana yoyote au
mnaonaje nyinyi wenyewe?", alimalizia Margret.
"Unasema alikuja hajawahi kutoka pale hata dakika
moja, ila tu siku ile aliyochukuliwa na polisi kwa
muda wa masaa matatu?", nilimuuliza.
"Nina uhakika kabisa maana mimi damu yangu
ilikuwa haipatani na yule mtu kabisa, na ni mimi
niliyefanya kampeni ya kumuitia polisi lakini
aliporudi alionekana kuwa maafisa wote walidharau
kumchukulia hatua tena".
"Ukimwangalia alikuwa anaonekana kichaa au
unafikiri anajifanya tu?", nilimuuliza.
"Kitu kilichonikosanisha naye ni kwa sababu siku
moja aliniambia yeye si kichaa ila anajifanya tu ili
kujipatia pesa bila jasho. maana ilikuwa
ukimwangalia sana wakati yeye hana habari
anakuwa kama si mtu kichaa, ila huwa anapoona
watu anakuwa kichaa kabisa".
"Asante sana, kumbuka jambo hili linaweza likawa
na msingi tutaliangalia".
"Asante".
Niliegesha gari mbele ya Rex Hoteli.
"Wakati wowote tutegemee", nilimweleza huku
akitelemka.
"Mnakaribishwa", akiwa zaidi anamwangalia
Sherriff. Sherriff alitoa mkono wake wakapeana
mikono. Tayari kulikuwa na kitu kinapita kati yao,
maana nyuso zilikuwa wakati wanapeana mikono,
mimi ndiye najua, maana hata mimi hali hii
inanitokea. Walikuwa wameanguka katika penzi.
"Mimi naona turudi pale ofisi ya kamati
tukahakikishe kama kweli hayupo pale yule kichaa",
nikimwambia Sherriff.
"Sawa".
Tulikwenda kimya kimya kila mtu akichambua
mambo, tuliyokuwa tumeyapata na kuyaona,
tulipofika pale ofisini tulimkuta mlinzi wa jioni
anayeingia kazini saa tisa wanapofunga kazi mpaka
saa kumi na mbili asubuhi, ilionekana alikuwa
anafanyakazi masaa mengi sana, lakini yeye
alipenda kazi yake na kuridhika na kipato
alichokuwa anakipata, baada ya kutusalimia na
kutueleza hizo saa zake za kazi, nilimuuliza.
"Unajua kulikuwa na mzee mmoja kichaa hapa sijui
amehamia wapi?'.
"Hata mimi nashangaa, kichaa huyu alikuwa hatoki
hapa hata dakika moja. Hata haja zake alikuwa
akiifanya hapa hapa karibu. Polisi walimchukua
hapa akawachenga akarudi mwishowe
wakamwachia akae tu. sasa leo nafika nakuta
kiisha ondoka na wala harufu yake hakuna.
Nimeshangaa sana. Amekaa karibu mwezi mzima".
"Ulikuwa unapata fursa ya kuzungumza nae?".
"Si mara nyingi, ila tu siku moja nilikuja
na ..........akasita kusema.
"Sema tu usiogope, hata kama ni siri, sisi
tutakufichia".
"Lakini nyinyi ni akina nani?".
"Sisi tunashughulikia wagonjwa wa akili, tumepata
habari toka polisi kuwa kuna mwendawazimu hapa,
hivyo unaweza kutueleza tabia yake ili tuweze
kumtafuta. Kwa hiyo usisite kutueleza",
nilidanganya.
Baada ya kutafakari mambo haya aliendelea, "Siku
moja kulikuwa na tafrija hapa ofisini jioni. Mimi
niliweza kwa mbinu zangu kujipatia mzinga mzima
wa whiski aina ya 'Dimple' nikauficha wagaeni
wote walipoondoka, nilitoka nje ya lango na kuanza
kunywa huu mzinga wa whiski. yeye alipoona
ninakunywa hii whiski alikuja na kopo lake
akaniomba kwa vile nilikuwa najuwa siwezi
kumaliza chupa nzima nilimgawia nusu basi
alikunywa ile pombe kama maji. Basi ilipomkolea
akaanza kuzungumza Kiingereza ila mara kwa
mara alisema neno sijui 'Sazafrika' neno hili
alilirudia mara nyingi. Na nyinyi mnajua vichaa
mimi niliachana nae nikaendelea na shughuli zangu.
Sasa sielewi kama kilikuwa Kiingereza sawa sawa.
Lakini kitu kilichonivutia ni kule kutamka hicho
Kiingereza chake kama mzungu. Lakini husema
kichaa ana mashetani saba, anaweza kuzungumza
lugha saba tofauti."
"Asante sana, na samahani sana kwa
kukubugudhi", Sherriff alitoa mfukoni shilingi
arobaini akampa. Yule Mzee alifurahi sana.
"Mungu awaongezee wanangu".
Tuliingia ndani ya gari tukaondoka zetu.
"Unaona mambo yalivyo Sherriff?, hii inaonyesha
wazi kuwa George Kiki alikuwa ni jasusi
aliyepachikwa hapa na mabeberu na wakafanikiwa.
Mimi simulaumu mtu yeyote, hata mimi huenda
ningemsaidia kupata kazi. Baada ya mabeberu
kujua mkataba wa silaha kati ya PLF na Urusi
miezi sita iliyopita walichukua hatua ya kuhakikisha
hizo silaha haziwafikii wapigania uhuru wa PLF
maana inasemekana ni silaha za kisasa kabisa.
Tutakapoonana na kiongozi wa PLF atatueleza
zaidi, kuajiliwa kwa kiki miezi sita iliyopita
kunaoana kabisa na nyakati za mkataba huo.
Inaonekana kazi ya jasusi huyo ni kujua mambo
yote yanayotendeka juu ya huo ili mwishowe aweze
kuiba hizo karatasi za kuchukulia silaha, jambo hili
amefanikiwa", nilinyamazi kidogo.
"Kwanini wamwue?", Sherriff aliuliza.
"Kwa sababu hawakuwa na haja nae tena, asije
akashikwa na kutoa siri. Hii inanionyesha jinsi watu
hawa walivyo wajuzi katika kazi yao, hawataki
kufanya makosa".
Wakati huu tukizungumza tulikuwa tukielekea mjini.
"Juu ya huyu kichaa unasemaje?".
"Huyu kichaa nae ni jasusi. Ninavyoona mimi huyu
aliwekwa pale ofisini kusudi aweze kuona nini
kitatokea hapo ofisini baada ya silaha kuibwa.
Aliwekwa mwezi mmoja ili kuondoa mashaka.
Hivyo alikuwa anangoja kuona baada ya polisi na
maofisa wa usalama ni nani mwingine aliyekuwa
na dukuduku juu ya jambo hili. Aliposikia waandishi
wa habari wa gazeti la Afrika nao wamejiingiza
akawa amemaliza kazi, akaondoka kwenda
kupeleka ujumbe, ni wazi kabisa wao walijuwa
polisi na maofisa wa usalama watalishughulikia
jambo hili na ninafikiri walishapima uzito na kuona
wanaweza kukabiliana nao. Hivyo walingoja wajue
kama kuna kundi jingine litakalojiingiza katika
katika upelelezi wa tukio hili. Sasa wamejua; kwa
hivyo waandishi wa gazeti lazima muwe macho.
Tokea sasa kaeni katika tahadhari; lolote linaweza
kutokea. Unaonaje maoni yangu?'.
"Lo Willy, ndio maana wewe ni mpelelezi maarufu
katika Afrika. Maelezo yako yanaeleza hali halisi
kabisa. Na swali ulilomuuliza Margret kama kuna
mtu mwingine aliyeweza kuona akiweka karatasi
ndani ya mkoba, mimi nilikuwa silifikilii kabisa na
ndilo swali lililotupa mwanga. Kweli kila mtu na
kazi yake", alisifu Sherriff.
"Lakini maswali mliyouliza ninyi vile vile ni ya
maana sana, nafikiri kuliko waliyoulizwa na Polisi.
Sidhani Polisi wameishafikia hii tuliyofikia kwa
muda huu mfupi".
Mara wazo likanijia.
"Lile jambo lililokuwa linakutatanisha nimepata jibu
lake. Swali la nani aliyepiga simu kwa Mlingi akiiga
sauti ya Mantare na maneno ya Mantare aliyozoea
kuzungumza na Mlingi".
"George kiki", alijibu Sharriff.
"Kabisa, unajuwa Kiki alikuwa anaingia ndani ya
kila ofisi ya ofisa akiwa kama tarishi. Swali hili
nilimuuliza Mantare akakubali. Hivyo Kiki akiwa
jasusi aliyefundishwa, ninavyofikilia, haikuwa kazi
kumsiliza Mantare katika simu zake nyingi na
ninafikiri alifanya kila njia kusikiliza simu kati ya
Mantare na Mlingi. Hii inaonekana wazi kabisa".
"Lo tunaanza kuona mwanga sasa", Sherriff
alisema.
"Kweli tumeona mwanga, lakini ni mwanga
unaotufikisha kwenye giza nene. Maana Kiki
ambaye angetupa fununu ya watu hawa amekufa,
yule kichaa lazima ameshapotea hewani, gtumerudi
pale pale".
"Watu hawa ni akina nani na silaha hizi ziko
wapi?", niliuliza swali hili wakati naegesha gari
New Afrika.
"Hilo ndio swali gumu lakini afadhali tunajua Afrika
Kusini inahusika, maana Kiki katokea huko. Na yule
kichaa alipolewa alizungumzia Sozafrika ambayo
nasadiki ni South Afrika".
"Sawa kabisa, lazima tujuwe tunapambana na
South Afrika na haikosi shirika lao la ujasusi
'BOSS', linasaidiwa na mashirika mengine ya
ujasusi ya nchi za kibeberu. Hivyo tutakuwa na
kazi ngumu maana watu hawa nimewahi
kupambana nao ni watu hatari kabisa".
"Tumwombe Mungu atasaidia".
"Na wewe ukijisaidia", nilijibu.
Wote tukacheka na kutoka ndani ya gari. Ilikuwa
saa kumi na moja. Hivyo kabla hatujavuka
barabara nilionelea nifike ofisini kidogo halafu
niende nyumbani.
"Sherriff mimi nafika nyumbani kidogo, nitakuona
saa kumi na mbili kamili".
"Sawa nitakusubiri hapa duka la kahawa".
oke basi saa kumi na mbili".
Niliingia ndani ya gari na kuondoka. Nilipofika
ofisini nilimkuta Eddy na vijana wengine. Linda
alikuwa ameshaondoka.
"Eddy kuna mtu mmoja anaitwa George Kiki,
alikuwa akifanyakazi kwenye ofisi ya Kamati ya
ukombozi kama tarishi?, hapa aliingia kama
mkimbizi baada ya kutoroka Afrika Kusini. Alifika
ofisi za chama cha SANP, ambao walimpeleka
kwenye Kamati ya Ukombozi waweze kumsaidia
angalau kazi yoyote. Inawezekana hana kisomo cha
kutosha. Nataka ukague habari hii kwa kutumia njia
zetu za kawaida. Unaweza kuwajulisha makomredi
wetu kule Soweto, nadhani watakuwa na maelezo
kamili. Habari hizi nazitaka haraka. Kila kitu,
aliingiaje hapa alikwendaje kwenye ofisi za SANP
alikuwa anaishi namna gani, nani walikuwa rafiki
zake nk. wewe unajua".
Eddy aliyekuwa anachuku maelezo haya alijibu.
"Atashughulikiwa bosi, usiwe na wasiwasi".
"Chifu yuko?".
"Kaondoka".
"Haya asante, usitoke mpaka nitakapokujulisha
tena".
"Mimi nipo".
Ndio sababu nilimpenda mtoto huyu. Nidhamu yake
kwangu ilizidi ya mdogo wangu ambaye tumetoka
ndani ya tumbo la Mama Willy. Niliingia ndani ya
gari nikaelekea zangu Upanga.
Niliposimamisha gari mbele ya mlango, moja kwa
moja macho yangu macho yangu yakaangukia
kwenye kitu kilichokuwa kwenye ubao wa juu ya
mlango mkubwa wa kutokea nje. Nilitoka nje ya
gari haraka haraka nikiwa tayari kwa mapambano.
Nilikuta ni kisu chenye mpini mwekundu kama kile
tulichokikuta kwenye kifua cha maiti Kiki; ncha
yake ilitumiwa kama kipini cha kubandika kipande
cha karatasi pale mlangoni.
Niliking'oa nikachukua karatasi na kusoma
yaliyobandikwa hapo yalisema.
Willy Gamba, kama unathamini maisha yako
achana na hao watu wa gazeti la Afrika. na kama
ni rafiki zako waambie waondoke hapa mjini
tunawapa mpaka saa kumi na mbili jioni wawe
uwanja wa ndege. Vinginevyo yaliyompata Kamara
Frank yatawapata na nyinyi. Hili ni onyo kali na si
mchezo. Shughulika na mambo yako usishughulike
na mambo ya watu wengine. Wapo wenyewe
wanaohusika waachie. Nasema tena saa kumi na
mbili jioni leo wawe uwanja wa ndege na wewe
baada ya kuwafikishia habari hizi tusikuone
unashughulika zaidi ya kazi yako ya kawaida ya
AIA Subiani.
Kwanza nilicheka maana niliona kazi sasa inaanza.
Hii inaonyesha upelelezi wetu ulikuwa umewashitua
kuliko wa Polisi. Nilijua yule kichaa alifanya kazi
yake vizuri sana, maana ni yeye tu
aliyetufahamisha kwa majahiri wenzake. Hiki kisu
chenye mpini mwekundu ilimaanisha damu. Nami
niljua damu imeanza kunuka.
Nilifungua mlango nikaingia ndani, nikakoga haraka
haraka kisha nikabadilisha nguo nilifungua sanduku
langu la silaha na kuchukua bastola zingine mbili
kwa madhumuni ya kuwapa Sharriff na Verokika
kwani hakukuwa na mchezo tena, maana upatapo
onyo toka kwa watu kama hawa huwa hawatanii.
Kisha niliinua simu na kupiga kituo cha Polisi cha
Salendar Bridge.
"Hallo kituo cha Polisi hapa".
"Sikiliza, nenda Kinondoni Hananasifu, Estate
kwenye nyumba ndogo ndogo za shirika la Nyumba
nambari IIC utakuta kuna maiti ambayo ina zaidi
ya masaa ishirini na nne", kabla hajatamka neno
nilikata simu. Niliangalia saa yangu muda ulikuwa
umekimbia na ilikuwa saa kumi na mbili kamili.
Niliingia ndani ya gari nikakimbilia New Afrika.
Nilipoingia duka la kahawa sikumwona Sherriff
nikapata wasiwasi. Nikaenda mapokezi kuuliza
wakaniambia aliacha habari kuwa amekwenda
dukani mara moja nimsubiri. Nilirudi nikasimama
nje pale magari yanapoleta watu New Afrika
yanapozungukia. Niliangaza huku na huku na mara
nikamwona Sharriff anakuja akiwa anavuka tawi la
Benki ya nyumba. ghafla alipokuwa anataka kuvuka
barabara ilitokea gari sijui wapi ikapiga breki,
wakatoka watu wawili haraka kama umeme,
wakamvuta Sharriff ndani ya kiti cha nyuma cha
gari, na gari hilo likaondoka tena kama umeme.
Kitendo hiki hakikuchukua hata nukta tano.
Watu wote waliduwaa wasijue cha kufanya, lakini
mimi Willy nilijua la kufanya. Nilikimbia kwenye gari
Eddy alilokuwa amekodi na kuliacha New Afrika.
Kwa vile alikuwa ameliegesha vizuri niliingia na
kuondoka kama umeme. Nilikuwa nimeona lile gari
linakata kulia kutoka barabara ya Azikiwe kuingia
Azania Front. Nilipoingia Azania Front niliona gari
lao linafika kwenye ofisi za NASACO nikacheka.
ITAENDELEA