NJAMA
MAPAMBANO NI VIBARAKA
III
"Ohuu. Bosi umetokea wapi?". Linda aliuliza huku
akitoa pumzi ndefu ya kuonyesha wasi wasi
aliokuwa nao umemtoka.
"Nimetoka mahabusu".
"Pole sana bosi".
"Usinipe pole sasa hivi, mapambano bado kabisa
yanaendelea, utanipa pole nikiweza kumaliza
mapambano haya kwa usalama. Eddy yuko wapi?".
"Yuko katika shughuli za kujaribu kukutafuta apate
kujua uliko. Lakini kila baada ya muda mchache
anauliza hapa".
"Akipiga tena simu mwambie arudi haraka. Je
Sherriff yuko wapi?".
"Wote wako pamoja".
"Haya kaniletee Sandwich za nyama ya kuku na
niwekee glasi ya whiski ofisini kwangu. ninakwenda
kunawa kidogo".
Baada ya kumaliza kunawa niliingia ofisini kwangu
na kuanza kunywa whiski na Sandwich alizokuwa
ameleta Linda.
"Chifu yuko?", niliuliza.
"Amesema muonane saa moja bila kukosa", Linda
alijibu.
Mara simu ililia ofisini kwa Linda. Linda akashika
simu yangu iliyokuwa imeunganishwa na yake.
Alibonyeza kidude kimoja baada ya kuinua mkono
wa simu.
"Hello nani hapo?", Linda aliuliza".
"Oh Eddy, rudi hapa haraka Bosi yuko hapa. Yuko
hai kabisa ameketi kwenye kiti chake anakunywa
whiski"....
"Haya asanhte", Linda aliweka simu huku akicheka.
"Nakwambia bosi ungesikia sauti ya Eddy
niliposema uko hapa. utafikiri mtu aliyekwamwa na
mwiba wa samaki".
Simu iliita tena ofisini kwa Linda na Linda
akachukua simu.
"Hello nani hapo?", Linda aliuliza. "Ehe Unasemaje
Issack... Eddy bado hajafika hapa, lakini atafika
muda si mrefu, na kama una habari muhimu Bosi
yuko hapa". "Oke, njoo haraka sana", Linda alijibu
na kukata simu.
"Vijana wa Eddy aliokuwa amewasambaza, huyu
Issack na mwenziwe ndio walikuwa na jukumu la
kuangalia mienendo ya Sikazwe", alisema Linda.
"Ghafla mlango wa ofisi yangu ulifunguliwa,
Sherriff, Eddy na Zabibu wakaingia ndani.
"Pole sana Bosi, sisi tulijua kwa uhakika kuwa
utakuwa msambweni", Eddy alitoa pole.
Linda na Zabibu waliangaliana kwa jicho baya.
Inaonekana Linda hakunda Zabibu kuja ofisini kwa
bosi wake.
"Huyu anakuja kufanya nini, si afadhali angalikaa
nyumbani, akawaachia wanaume hawa kazi hii.
Mara nyingine kutembea na wanawake katika
mapambano kama haya kunaweza kuleta mkosi".
"Mimi sina mkosi. Pilipili usiyokuwa inakuwashia
nini?. Shughulika na mambo yako dada na mimi
nitashughulika na yangu, usinijue kabisa", alijibu
Zabibu kwa hasira.
"Haya basi yaacheni hayo mambo ya kitoto hapa
tuko kazini. Sitaki kusikia uchafu mwingine
wowote", niliwaonya.
Nilianza kuwaeleza yaliyonipata toka mwanzo
mpaka mwisho. Nilipomaliza kuzungumza tu Issack
akaingia.
"Ehe tupe maelezo", Eddy alimdai.
"Nitaanza toka jana usiku kwa faida ya wale
ambao hawakupata habari hizo toka mwanzo.
Sikazwe tulianza kumwona mnamo saa tisa za
usiku akitokea barabara ya Bagamoyo. Alielekea
moja kwa moja nyumbani kwake na hakutoka tena
mpaka saa sita za mchana. Mnamo saa sita hivi
aliondoka akaenda kula chakula cha mchana.
Aliporudi mnamo saa saba hivi alikuja na lori dogo
tani tatu likimfuata nyuma. Alifungua mlango na
kuanza kutoa mizigo iliyofungwa kama mtu
anayehama. Baada ya kujaza gari hili, liliondoka na
nikamwambia Ismail alifuate. Ismail aliporudi
alisema mizigo hiyo imetelemshwa kwenye bandari
ndogo yaani pale ngalawa na meli ndogo ndogo
zinapopakia mizigo yao.
"Yaani mizigo hiyo ilikuwa imefungwa kisafari?'.
"Ndio".
"Haya endelea".
"Kiasi cha saa tisa hivi walikuja watu wawili ndani
ya gari, mmoja Mzungu mwingine mwafrika.
Walikaa kama dakika tano tu wakaondoka.
Nilimwambia Ismail awafuate. Walielekea barabara
ya Bagamoyo, Ismail aliporudi alisema watu hawa
waliingia barabara ya Kilimani na kuingia nyumba
moja inayotazamana na Hosteli ya Tazara. Sikazwe
hakutoka. Mnamo saa kumi na moja hivi alikuja
mtu mwingine na gari akazungumza nae mlangoni.
Maneno aliyosema yalionyesha kumkasirisha
Sikazwe maana alimsukuma, na yule mtu haraka
haraka akaingia ndani ya gari na kuondoka....
"Ismail alimfuata huyu mtu lakini mtu huyu aliingia
Estiennes Hoteli na kuanza kunywa pombe, hivyo
akamwacha akarudi. Wakati natoka Sikazwe
alikuwa bado yuko ndani lakini nafikiri atatoka
maana alichukua debe la mafuta ya petrol akajaza
gari lake".
"Kazi nzuri umefanya".
"Asante", alijibu kwa furaha sana.
"Eddy nitayarishie gari, hapana Issack nitatumia
gari lako mimi na wewe tutakwenda kumfuata
Sikazwe, popote atakapokwenda. Sherriff Eddy na
wengine mnisubiri hapa hapa nitarudi ila
mjitayarishe kwa usiku wa kazi", niliwaeleza lakini
niliona wanashangaa.
Kabla hawajaanza kusema mengi nilimwambia
Linda. "Mwambie Chifu anisubiri kidogo nikichelewa
kufika saa moja".
Nikatoka nje pamoja na Issack nikawaacha
wamepigwa na butaa.
Niliangalia saa yangu ilikuwa saa kumi na mbili na
dakika tano na kwa majira ya wakati huu ya Dar es
Salaam giza lilikuwa limeingia. Tulipofika kwa
Sikazwe tu tulimwona naye anafungua mlango wa
gari akaweka mkoba wake ndani, kisha akaingia na
kuwasha gari moto. Sisi tuliegesha gari letu kama
watu wanaopunga hewa pwani saa za jioni kwani
vile vile kulikuwa na magari mengine. Alipoondoka
tu Sikazwe sisi taratibu tulimfuata.
Mimi ninapomfuata mtu hata awe na ujuzi wa
namna gani hawezi kunitambua. Sikazwe
alituongoza mpaka kwenye nyumba hii ambayo
Issack alisema ilikuwa karibu na Hosteli ya tazara.
Alipiga honi mbele ya lango kubwa. Tukaona askari
anakuja kumfungulia akaingia ndani. Majibwa
mawili makubwa yaliandamana na askari huyu. Sisi
tulienda na kuegesha gari letu mbele ya baa ya
Hosteli ya Tazara. Mtu yeyote angedhani tuko
humo katika baa, tunakunywa.
"Unayo bastola yenye seilensa?", nilimwuliza
Issack.
"Ndiyo".
"Nipe. Wewe ningoje hapa lakini uwe katika
tahadhari kitu chochote kikitokea njoo haraka,
umenielewa.
"Hamna wasiwasi bosi".
"Kazi ninayokwenda kuifanya ni ndogo ila majibu
ndio yananipa wasiwasi".
"Nakutakia kheri, bosi".
"Nafikiri nitaihitaji".
Nakutakia kheri, bosi".
"Nafikiri nitaihitaji".
Niliondoka na kwenda kwenye nyumba ile. Mbwa
walikuwa wanabweka kila gari linapopita mbele ya
ile nyumba. Niliona hii itanisaidia maana hata
wakibweka halitakuwa jambo la ajabu. Niliangalia
wapi upepe unatoka nikaona ulikuwa unatoka
mashariki kwenda magharibi, hivi nikaamua kuingia
nyumba hii kutoka magharibi kuzuia mbwa wasije
wakaninusa. Nyumba ilikuwa imezungushiwa ua
wenye seng'eng'e zenye miba upatao urefu wa futi
sita kwenda juu. Kati ya mafunzo yangu makubwa
kuruka ilikuwa mojawapo. Nilikuwa naweza kuruka
futi saba wakati mwingine nane. Hivyo nilirudi
nyuma nikaruka juu ya seng'eng'e na kutumbukia
ndani ya ua bila kishindo maana nilitanguliza
mabega.
Nilikumbuka kuwa kibao nje la lango kubwa
kilikuwa kimeandikwa jina la Tony Harrison, hivi
nilijua huyu ndiye mwakilishi wa Euro-Afro. Zabibu
aliwahi kunieleza habari hizi. Walivyokuwa
wanahusiana na Sikazwe ndicho nilikuwa nimekuja
kutafuta. Kwanza ilinibidi nitoe kikwazo kimoja
yaani askari mlinzi na mbwa. Nilisikia mbwa
wanabweka mbele ya nyumba, hivyo nilijibanza
kwenye ukuta wa upande huu wa magharibi halafu
nikanyata pole pole mpaka kwenye kona ya ukuta
na mbele. Nilichungulia nikaona askari mlinzi
pamoja na mbwa wake wawili. Nilikohoa yule
askari akastuka akaangaza huku na huko asione
kitu maana mimi nilikuwa nimeganda kama kupe
kwenye ukuta. Ili kuridhisha mashaka yake alikuja
upande niliokuwa akifuatana na mbwa. Alikuwa na
bunduki mkononi, kwa umbo lake nikajua ni 'SAR'.
Alipofika karibu kabisa na mimi niliona mbwa
wanainua mikia nikajua tayari wameninusa.
Nililenga bastola yangu nikawaua wale mbwa kwa
kuwapiga katikati ya vichwa kwa upesi sana
kwamba yule askari alishangaa kuona mbwa
wanaanguka hata bila kubweka. Alipogeuka na
kuniona tayari alikuwa amechelewa, nilimrukia
nikamkaba kabali taratibu mpaka alipokufa bila
kutoa sauti. Nilivuta mizoga ya majibwa haya na
maiti ya yule askari na kuyaweka kando ya ua
upande wa magharibi kwenye seng'eng'e. Nikiwa
nimeridhika na hatua yangu ya kwanza. Sasa
nilichukua hatua ya pili.
Nilianza kuzunguka nyumba kwa nyuma nikielekea
mashariki. Sikwenda mwendo mrefu kabla sijafika
mahali nilipokuwa ninapahitaji. Nilikuwa nimefika
nje ya sebule na dirisha la nyumba lilikuwa wazi,
na nikasikia mazungumzo ya huko ndani kama
nami niko pale pale. Hivyo nilibana tena kwenye
ukuta nikaanza kusikiliza mazungumzo.
"Lakini Tonny, mimi nimrjitshidi sana lakini huyu
mdudu Gamba na kundi lake amewaua watu wangu
wengi sana. Fikiria Shuta na Mlambo wameuawa.
Nadhani nisingejitahidi zaidi ya hapo. Lakini hata
hivyo bado nina watu wa kutosha kutekeleza kazi
hii. Usiku huu huu itakwisha, usiwe na shaka.
Hii ilikuwa sauti ya Sikazwe.
"Sawa Ray, lakini naona ungejitahidi zaidi ya hapo
maana lazima ile meli ndogo iondoke saa tisa za
usiku ili kuwahi meli yetu ya Euro-Afro Mtwara
usiku wa kesho. Tayari rubani wa meli hiyo ana
habari na mpango wa kutoa mizigo ndani ya meli
ndogo (scooner) na kuingiza katika meli hiyo huko
Mtwara haina uangalizi sana kama bandari ya Dar
es Salaam", Tonny alisema.
"Vizuri mimi nitajitahidi, tayari mizigo yote
imefungwa vizuri, imebaki kusafirisha tu kwenda
kwenye bandari ya meli ndogo".
"Nimepata habari kuwa unangojewa kwa shangwe
na wakuu wa serikali ya Afrika Kusini. Nimewaeleza
mipango yote, na wao wako tayari kuzungumza na
chama chako ili damu isimwagike Nchini.
Wamefurahi sana kwa kazi yetu ya kuweza kuziiba
silaha za hatari ambazo zingeua wananchi wa
Afrika Kusini bure, kumbe mnaweza kufikia
maafikiano ya kubadilisha siasa ya Serikali ya
Afrika Kusini kwa mazungumzo", Tonny Harrison
alieleza.
"Na mimi nimeona ni wenda wazimu kuendeleza
vita dhidi ya Afrika Kusini kwa njia ya
mapambano.Lakini bado chama cha PLF
kitaendeleza mapambano. Chimalamo ni mtu
mwenye nia ya kuuza ubaguzi wa rangi kwa
mapambano na mtutu". Sikazwe alionya.
"Si wewe unajua vitu vyao vyote na namba ya
askari wao na mafunzo waliyopata askari wao
pamoja na silaha walizonazo.
"Ndiyo, najua kila mbinu ya jeshi lake maana
mwaka jana Kamati ya Ukombozi ya OAU ilitaka
kutuunganisha. Hivyo tulipewa fursa ya kuelezana
kikamilifu hali ya mali ya kila Chama kwa
mwenzake. Tulikuwa wote tumekubali kuungana
tukaelezana siri zote za vyama vyetu. Ni wakati tu
tulipokuja na maoni ya namna ya kuweza kufikia
hali ya kubadili siasa ya ubaguzi bila kumwaga
damu, ndipo nilipokataa tena mpango huo wa
kuunganisha vyama. Nilidai kuwa siasa ya Chama
cha PLF na chama changu zilikuwa na tofauti za
kimsingi ambazo hatukuweza kukubaliana. Huu
ulikuwa uongo lakini ulikubalika ikaonekana
tuendelee hivi tulivyo ili mradi wote tuna nia moja
kwa hivyo siri zote za PLF ninazo.
"Kwa hiyo siri zote za PLF unazijua na kwa sababu
wewe umejiunga na serikali ya Afrika Kusini
itakuwa rahisi sana kuwateketeza wapigania uhuru
wa PLF wasijaribu tena. Yaani litakuwa pigo kubwa
kiasi kuwa kuweza kuimarisha chama chao kianze
mapambano tena, lazima itawachukua muda mrefu,
na wakati huo Ray utakuwa uanatawala pamoja na
wazungu huko Afrika Kusini". Sikazwe alitoa
kicheko.
"Msiwe na wasiwasi mimi nitakuwa nao bega kwa
bega kuleta hali nzuri katika Afrika Kusini na
nitakuwa mstari wa mbele kupinga harakati za
ukombozi ambazo wakati huo zitakuwa hazina
maana".
"Kesho ndiyo siku kubwa kwako utakapoingia
Pretoria na kuwekewa zulia jekundu", Tonny
alisema kwa sauti ya kejeli.
Bila kutambua ile kejeli Sikazwe alijibu. "Ninaisubiri
kwa hamu sana. Magari yale yaliyofanya kazi
tayari yamebadilishwa rangi za jeshi la Tanzania.
Kwa hiyo saa nne inaweza kupitia Intercontinental
Motors na kuyachukua ili kubeba ile mizigo toka
bohari mpaka bandari ndogo".
"Tayari Max ameisha waarifu, au siyo ?', Tonny
aliuliza.
Niliinuka taratibu kumwangalia huyu Max
nikamtambua; ni yule aliyetukimbia kule kwenye
uwanja wa Saba Saba.
"Mara hii nitakupata", nilijisemea moyoni maana
mara moja alinikumbusha Veronika.
"Ndiyo, gari ziko tayari", Max alijibu.
"Oke mimi ninakwenda kijitayarisha saa tatu unusu
ndipo nitatoka nyumbani kwangu kuelekea kwenye
shughuli.
"Je kuna wasiwasi wowote?", aliuliza Tonny.
"Hamna taabu, tayari watu wa Forodha wanajua
tunapeleka spea za magari Mtwara na tumeisha
zungumza nao vizuri hamna taabu".
"Lakini usimsahau Gamba na wenzake", Tonny
alikumbusha.
"Usiwe na wasiwasi nina askari zaidi ya mia
ambao wamefundishwa mafunzo ya juu hapa hapa
Tanzania. Kama Gamba na wenzake wanataka kifo
vema, na waje watuingilie watakiona kilichomtoa
kanga manyoya shingoni".
"Oke nakutakia upakuzi mwema".
"Max, kwa sababu wewe ndiye kiongozi wa meli hii
ndogo uwe macho kusije kukatokea kosa", Tonny
alimwonya.
"Wewe unanijua sifanyi kosa mara mbili",
alijigamba Max.
"Haya Sikazwe nafikiri saa tisa na nusu tutaonana
hapa sitalala nitakusubiri".
"Usiwe na shaka", alijibu Sikazwe huku akisimama.
"Lo, nipe tiketi yangu ya ndege kabisa".
"Chukua hii hapa imelipiwa na serikali yako
unakokwenda kuwa kati ya watu wakubwa
watakaoongoza nchi yenye nguvu kuzidi zote katika
Afrika".
Sikazwe na Max walimwaga wakafungua mlango
wakatoka nje. Tonny Harrison alibaki ameketi
kwenye kiti. Kwa vile nilikuwa na wasiwasi kuwa
wangeshangaa kutomwona askari mlinzi na mbwa
wake, nilitoka pale dirishani nikazunguka mbele.
Kwa bahati nzuri hawakushughulika kumwita
askari, ila Max alikwenda akafungua mlango,
Sikazwe akapitisha gari langoni, halafu Max
akarudisha mlango na kuingia ndani ya gari
wakaondoka.
Mimi nikaona nimepata wakati mzuri wa
kuzungumza na Tonny Harrison. Nilipoangalia saa
yangu nikaona ni saa moja na nusu. Saa mbili
zilikuwa zinatosha kumaliza shughuli zangu na
Tonny Harrison kabla sijamfuata Sikazwe hapo saa
tatu na nusu. Nilifungua mlango taratibu maana
ulikuwa umerudishiwa tu bila kufungwa kwa
ufunguo. Nikiwa na bastola mkononi niliingia
sebuleni na kumkuta Tonny Harrison ameinamia
meza anasoma faili.
"Habari za kazi Tonny Harrison?".
Harrison aligeuka na kujikuta anaangalia katikati
ya mdomo wa mtutu wa bastola. Pale pale
aligeuka sura. Kwanza ikawa ya manjano kisha
ikageuka ikawa nyekundu kama mtu aliyechapwa
kofi usoni. Unajua hawa wenzetu weupe akichapwa
kofi muruwa uso hugeuka na kuwa mwekundu.
Alitaka kutamka neno akashindwa. Niliona alikuwa
hategemei kabisa maisha mwake kukutana na
wakati kama huu ambao alijikuta anatazama
mdomo wa kifo.
"Habari gani?. Au umekuwa bubu?".
Nilisogea taratibu huku bastola yangu ikiwa
imemlenga katikati ya uso wake. Kwa kigugumizi
alijibu. "Nzuri....".
"Telemka hapo kwenye meza njoo tukae hapa
kwenye makochi nina mazungumzo ya maana na
wewe kabla sijaondoka".
Bila kusita aliinuka kwenye kiti na kwenda kukaa
kwenye kochi. Wakati wote huu mdomo wa bastola
haukumwachia hata chembe ya nafasi. Nilikwenda
pale mezani alipokuwa ameacha faili nikalichukua.
Nilikaa upande mwingine wa makochi tukawa
tunaangaliana ana kwa ana.
"Bwana Harrison natumaini tumewahi kuonana?".
"Ndiyo, nafikiri tulionana kwenye tafrija
iliyoandaliwa na Lion Club Hotelini Kilimanjaro".
Nikaweka bastola yangu kwenye paja huku macho
yangu yakiwa yanamwangalia kwa makini.
"Na si mara moja au mbili?".
"Nafikiri ni mara nyingi".
"Nasikitika kusema kwamba leo sikuja kwenye
tafrija ila nimekuja kuzungumza nawe kwa ajili ya
suala la hatari ambalo wewe unalijua vizuri zaidi.
Faili niliyoichukua kwenye meza ilikuwa
imeandikwa "SIRI" halafu kichwa cha faili kiliitwa
"OPERESHENI HUJUMA". Mara moja nikajua katika
faili hili ndimo kulikuwa na maelezo yote ya jinsi
tukio hili lilivyofanywa na hawa majahiri. Ule
ulikuwa ni ushindi thabiti hivyo niliweka faili kwenye
mapaja yangu.
"Sina haja ya kujitambulisha kwako kuwa sasa hivi
nimekuja kukuona kama nani, kwa sababu
natambua unaelewa, au sivyo".
Ndiyo".
"Bila kupoteza muda ningependa kujua, bwana
Harrison, wazo la kuziiba silaha za wapigania
uhuru mkiwatumia wapigania uhuru wenyewe
limetoka kwa Makaburu au kwa mataifa ya
Magharibi?".
"Kwanza kabla sijajibu swali lako nataka kutoa
mshangao wangu kwako jinsi ambavyo umeweza
kupeleleza na kugundua jambo hili ambalo
lilitayarishwa kwa mbinu za hali ya juu. Mimi
ningependa unieleze kwanza jinsi ulivyoweza
kupeleleza mpaka kunifikia mimi kitu ambacho
sikutegemea kabisa. Nafikiri baada ya hapo
unaweza kunifanya unavyotaka kwani hili faili
uliloshika lina kila kitu. Sina hata haya ya
kukueleza mengi; yote utayakuta humo".
Mpaka sasa nilishatambua kuwa Harrison hakuwa
mtu mwenye ujuzi wowote katika mambo ya
kijasusi ila alikuwa ametumiwa tu kwa sababu
ndiye mtu pekee ambaye angeweza kutekeleza
jambo hili bila kushukiwa, na kweli kwa muda wa
miezi sita alikuwa amefaulu kutotambulikana.
"Sawa, bwana Harrison. Nafikiri nitaanzia toka
mwanzo ninavyofikiri ndivyo mambo yalivyokuwa
mpaka kufikia hali hii.
"Mnamo miezi sita iliyopita Rais wa Chama cha
wapigania uhuru kiitwacho PLF, Ndugu Cicil
Chimalamo, alitembelea Urusi kwa nia ya kutafuta
msaada wa kijeshi; yaani silaha kwa ajili ya
mapambano yaliyokuwa yameanza dhidi ya serikali
ya Afrika Kusini.
"Kwa vile Ndugu Chimalamo alikuwa na habari zote
kuhusu nguvu za kijeshi za serikali ya Afrika Kusini
ilizonazo alitoa maombi yake kwa serikali ya Urusi
ili aweze kupatiwa msaada wa silaha za kisasa
walizonazo Makaburu. Ombi hili la Ndugu
Chimalamo lilikubaliwa na serikali ya Urusi na
akaahidiwa kupatiwa silaha hizi katika muda wa
miezi sita. Na kwamba katika muda huo silaha hizi
zitakuwa zimewasili Dar es Salaam".
Akiniangalia kwa makini, nilitoa pakiti yangu ya
sigara ya aina ya Tropicana, nikatoa sigara mbili,
moja nikampa na nyingine nikavuta mwenyewe,
kisha nikaendelea.
"Kwa kutokana na mbinu za kisasa za kijasusi za
mashirika ya kijasusi ya nchi za Magharibi habari
hizi zilinaswa. Ziliponaswa habari hizi ndipo nchi
za Magharibi zilipopasha habari serikali ya
Makaburu tishio lililokuwa linakuja dhidi yao. Hapo
ndipo serikali ya Makaburu ilipokaa chini na kufikiri
nini la kufanya. Uamuzi wa Makaburu ukawa wa
kufanya ujahiri huu ndilo lilikuwa tatizo. Lakini
baada ya kulishughulikia suala hili ambalo nafikiri
walitupiwa wakuu wa shirika la ujasusi, yaani
"BOSI", walifikiria mbinu za hali ya juu na kuamua
kuwa kwa kutumia mbinu hizi wangeweza kufaulu
kuziteka silaha hizi kabla hazijafika mikononi mwa
wapigania uhuru. Bashiri yangu ni sawa na vipi?'.
"Mpaka sasa hujakosea kitu", alijibu.
"Makaburu ni wajanja sana na wanawajua wakuu
wa vyama vya wapigania uhuru vizuri sana. Hivyo
waliamua kumtumia mkuu mmoja wa wapigania
uhuru ambaye walikuwa wanajua kuwa hakuwa na
msimamo kamili, kwa vile walimjua alikuwa
hapiganii hasa ukombozi wa waafrika wanaoonewa
huko Afrika Kusini bali alikuwa akipigana ili apate
cheo. Ukubwa na kujaza tumbo lake ndio ilikuwa
nia yake. Hivyo waliamua kumtumia bwana Ray
Sikazwe wa Chama cha SANP, ambaye ndiye
alipatikana na sifa hizi walizozitaka. Walipofikia
hapa kilichokuwa kimebaki ni namna gani
watamwingia na kuweza kumridhisha kweli
akisaidiana nao katika kuhujumu vyama vingine
angepata kila alichokitaka. Hapa ndipo walipohitaji
msaada wa nchi za Magharibi na hapo ndipo wewe
Harrison ulipoingizwa katika njama hizi".
Nilinyamaza kidogo kiasi chs kupitisha mate.
"Kampuni yenu ya Euro-Afro ni kampuni kubwa
sana, na ina rasilimali nyingi katika Afrika Kusini.
Inamiliki madini ya maangamizi, chromiumu na
platinumu katika Afrika Kusini. Na Afrika Kusini
ndiyo nchi pekee isiyo ya kikomunisti inayotoa
madini haya ambayo yanahitajika sana katika
viwanda vya nchi za Magharibi. Hivyo serikali ya
Makaburu ilizungumza na nchi za Magharibi
zizungumze na kampuni yenu ikiwa na kisingizio
kuwa kama wapigania uhuru hawa wakipata silaha
hizi si serikali ya makaburu tu itaangamia, bali nchi
za Magharibi zilizo na rasilimali zao nchini humo
nazo zitapoteza mali zao. Kwa hivyo swala hili
lilikuwa muhimu kwa nchi za Magharibi kama ilivyo
kwa serikali ya Makaburu.
"Kwa vile Kampuni yenu inamiliki makampuni mengi
katika nchi mbalimbali za kiafrika na mojawapo
ikiwa ni Tanzania, hivyo ilionekana ndiyo kampuni
pekee ambayo ingeweza kusaidia katika suala hili.
Hivyo wakubwa wako waliarifiwa juu ya suala hili
na hatari zake kama halitaweza kushughulikiwa
haraka na kwa kikamilifu. Kwani hatari hii
isingekuwa kwa Afrika Kusini tu ila pia Kampuni hii
ya Kibepari ingeweza kupoteza mali zake zote ikiwa
wazalendo watashinda vita vya ukombozi.
Kutokana na sababu hizi wakubwa zako
walikubaliana na Makaburu kuwa kulikuwa na haja
ya kushirikiana ili kulinda maslahi ya Makaburu na
nchi za Magharibi. Hapo ndipo ulipopashwa habari
namna utakavyoshughulikia suala hili. Mpaka hapo
maelezo yangu ni sawa au vipi?'.
"Sijui ulijuaje?, endelea maana nashangaa sana
jinsi Afrika huru ilivyoendelea katika upelelezi".
"Habari zilipokufikia pamoja na plani yote ndipo
ulipomwita bwana Ray Sikazwe na kumweleza
kama ulivyoelekezwa. Ndipo ulipomdanganya kuwa
serikali ya Makaburu iko tayari kufanya
mazungumzo na chama chake ili wafikie uhuru wa
walio wengi kwa mazungumzo bila mapambano, ila
kwanza atimize sharti moja. Sharti hilo ni
kusaidiana kati ya majasusi wa "BOSI" ambao
wataingia Tanzania kama wanachama wa chama
chake na kundi lake la wapigania uhuru lililokwisha
kufundishwa mbinu za vita katika kuziteka silaha
za chama cha PLF ambazo zilikuwa zikitegemewa
kuwasili mjini Dar es Salaam mnamo miezi sita
hivi".
"Kwani unadhani Makaburu hawawezi kutafuta
suluhisho la namna hii, baada ya kutambua kuwa
umefika sasa wakati wa kuanza kuwachukulia
waafrika kama binadamu wenzao?", Harrison
aliuliza.
"Mimi najibu kuwa baso, kwani kama nia yao
ingekuwa hiyo wasingetaka suluhisho na chama
kimoja tu na kwa siri, wangeliutangazia ulimwengu
na kuomba vyama vyote vinavyohusika na tatizo la
Afrika kusini vishiriki vyote kwa ujumla bila sharti
lolote, la hasha, Harrison. Hizi zilikuwa mbinu tu za
kuhujumu harakati za mapambano ya chama cha
PLF ambacho kinaendelea na mapambano makali
dhidi ya serikali ya Makaburu".
"Sawa nafikiri umenipa msingi wa mambo kama
yalivyopangwa na serikali ya Afrika Kusini
ikisaidiwa na nchi za Magharibi ambao ndio sisi.
Lakini tulifaulu katika kuziteka nyara silaha hizi bila
tatizo, je umekuja kugundua ni nani wanahusika?,
ingawaje juzi tulipata habari kuwa wewe ni
mpelelezi hatari lakini hatukuamini ungeweza
kugundua kitu".
"Nitakueleza sasa. Nilipoanza upelelezi wangu siku
ya kwanza tu niliona mwanga kwani mlikuwa
mmefanya kosa. Kosa lenyewe lilikuwa ni kumwua
kiki. Nilipokuta Kiki amekufa, tulianza kuchunguza
habari zake tukakuta mambo yote aliyokuwa
ameeleza juu yake si kweli, hivyo tukagundua
alikuwa jasusi wa Makaburu waliokuwa wamefaulu
kumweka katika ofisi ya za kamati ya Ukombozi ya
OAU, na ni yeye aliyeweza kufanikisha jambo hili".
"Na mlijuaje kuwa mimi na sikazwe tunahusika?".
"Kosa jingine. Sikazwe nilipomwuliza kama
anamfahamu Kiki alisema aliwahi kumwona mara
moja tu wakati alipofika ofisini kwake na
kumpeleka kwenye kamati ya Ukombozi ya OAU ili
wamsaidie kazi. Sasa tulipofahamu kuwa Kiki
alikuwa na rafiki msichana aitwae Zabibu
nilimtafuta.
"Nilipofika kwake wakati mmemtuma mtu wa
kwenda kumwua nikamkomboa. Yeye huyu binti
alinieleza kuwa Sikazwe alikuwa rafiki mpenzi wa
Kiki pamoja na wewe. Hii ilidhihilisha kuwa Sikazwe
alisema uongo hivyo mara moja nikaanza kumhisi
kuwa yumo katika mpango huu. Nilipojua kuwa kati
ya makampuni yaliyo chini ya Euro-Afro ni pamoja
na Intercontinental Motors ambao ni wakala wa
magari ya "Benzi" nchini hapa nikawa na uhakika
kabisa wewe unahusika. Maana magari
yaliyotumiwa yalikuwa maloli makubwa ya aina ya
Benzi ambayo ni sawa na yanayotumiwa na jeshi
letu. Na magari yote ya jeshi kwa siku ile
yameweza kufahamika yalikuwa wapi. Hivyo
ikaacha sababu moja tu magari yaliyobeba zile
silaha yalitoka kwenye kampuni yenu ya
Intercontenental Motors ya jeshi pamoja na
kuyaweka namba za bandia. Juu ya mavazi ya
kijeshi wapigania uhuru wengi wanayo hivyo, hilo
halikuwa tatizo kwenu. Una swali jingine?".
"Nafikiri umenielewesha vya kutosha na ninakupa
hongera kwani kweli wewe ni mpelelezi maarufu si
Afrika tu ila Ulimwengu mzima. Maswali mengine
niliyokuwa nayo nimekwishajua majibu yake baada
ya kuzungumza na wewe na kuamini mimi
mwenyewe kuwa wewe huwezekani".
Ghafla mlango ulifunguliwa na Issack akaingia
bastola mkononi.
"Karibu Issack samahani kwa kuchelewa nilikuwa
na Bwana Tonny Harrison hapa ambaye ni
mwakilishi wa kampuni ya Euro-Afro ambaye ndiye
alikuwa kiongozi wa tukio la bandarini".
Niliangalia saa yangu nikaona ni saa mbili.
"SWali na mwisho Harrison, silaha mmezificha
wapi?".
"Sikazwe ndiye anajua, na kama umeweza kufikia
hapa sidhani utashindwa hatua ya mwisho".
"Haya simama twende zetu. Issack kalete gari
hapo mbele ya mlango".
Issack alitoka na Harrison bila matatizo alisimama
na kuangalia sebule na vitu vilivyokuwemo kwa
huzuni. Alitangulia mimi nikafuata nyuma. Nilipofika
mlangoni nilizima taa, nikawa na faili kwapani na
bastola ikiwa imemlenga Harrison. Nilirudisha
mlango na kuelekea kwenye lango.
"Askari na mbwa wangu wako wapi?", Harrison
aliuliza tulipofika kwenye lango.
"Sasa hivi wako sehemu ambayo mimi na wewe
hatujafika lakini siku moja tutafika".
Issack alikuwa ameegesha gari mbele ya lango,
Harrison alifunga mlango wa nyuma mimi
nikamfuata na kukaa naye.
"Kwa usalama wako usijaribu kitu chochote",
nilimweleza huku Issack anaondoa gari.
"Mimi hata bastola sijui kuinua, watu hawa
waliniahidi ulinzi mkali na kwamba ingekuwa
vigumu operesheni hii kushindwa. Kumbe
wameniuza. Usiwe na wasiwasi na mimi, sijui
mbinu yoyote mbele ya bastola".
Nikajua wakati wake wa kusema ukweli umefika.
"Vipi bosi?", Issack aliuliza.
"Kituo cha usalama kwa watu kama hawa".
Issack kwa sababu alielewa ni kituo gani cha
usalama alikwenda moja kwa moja na kupiga honi
tulipofika kwenye lango. Mlinzi alikuja akafungua
lango sisi wote wawili tukatoa vitambulisho vyetu.
Akastuka mara moja na kuturuhusu kuingia.
Nilimwongoza Harrison mpaka kwenye ofisi ya
kituo hiki cha usalama.
Nilipofika nilimkuta afisa wa zamu nikatoa
kitambulisho changu, naye akastuka.
"Ndio Mzee".
"Huyu mtu awekwe chini ya ulinzi mkali mpaka
utakapopata maelezo tena".
Niliomba kitambulisho chake nikachukua jina,
namba na cheo chake.
Alikuwa na cheo kikubwa. Kisha nilirudi ndani ya
gari.
"Moja kwa moja ofisini, maana saa tatu na nusu
ndipo kazi kubwa ya kukata na shoka inaanza".
ITAENDELEA