NITAKUPATA TU
SEHEMU YA 054
Mwili wa mhudumu aliyemuacha sekunde dakika moja iliyopita, alimkuta akiwa mfu amelala katikati ya dimbwi la damu huku kisu kubwa imesimama katikati ya tumbo. Utumbo ulikuwa nje ukining'inia kwa pembeni. Bado mwili ulikuwa wa moto na damu ilikuwa ndio kwanza inatembea. Kengele za hatari zikagonga kichwani kwa masimba. Aliujua uhatari wa kupambana na mtu wa aina hii. Mtu aliyetumia sekunde kufanya mauaji ya aina hii. Hilo pekee lilimpa ujumbe kuwa ndani ya hoteli ile kulikuwa na mtu hatari sana. Mtu ambaye hatakiwi kuachwa. Akarudi nyuma na kuuacha mwili wa mhudumu yule ukiwa bado umelala katikati ya damu. Akairuhusu miguu yake itembee katika namna ya utayari , mikono ilikuwa tayari hata pale alipokuwa akipanda ngazi. Akanyoosha kuelekea pale kwenye chumba alichokisoma kwenye daftari la wateja. Chumba alichohisi kuwa atakuwa ameingia Salha na mwanaume Yule aitwaye marlon. Masikio yakinasa huku pua zikiinusa harufu ya damu. Harufu ambayo bado ilikuwa ikisumbua katika matundu ya puA zake. Hatua ishirini mbele akauona mlango wa chumba kile. Mlango ambao hakuonyesha kufungwa bali kuegeshwa tu. Akaongeza umakini mkono wake ukiwa umenyooshwa kwa mbele kuilekeza bastola pale. Hata alipoangalia chini matone ya damu kutoka ndani ya chumba kile yalimrejesha katika utambuzi yakinifu katika medani ile. Sasa alikuwa ameuweka mwili katika aina yoyote ya mapambano. Akageuka na kuelekea pale. Masikio yakinasa kushoto, kulia na hata kisogoni kusikia chochote kitu. Bado damu ilikuwa ikitembea taratibu. Mlango uko wazi na kisha damu. Kuna nini? Ama ni mtego? Lilikuwa swali lisiliteguliwa kwa wakati ule. Mguu wake wa kushoto ukausukuma mlango huku bastola imetangulia. Baada ya mlango kumpa nafasi ya kuangalia ndani, akatupa macho kwa haraka.. hakukiona kitu zaidi ya damu.. Hilo likamfanya aingie ndani kabisa.. Kuingia ndani akajikuta akitizama na kitu ambacho hakukitegemea, tukio ambalo lilimfanya ahisi kwanba anaitizama picha za video zisizopendeza machoni mwake. Alihisi kile anachokitizama hakikuwa kitu cha kweli. Ni punde alikuwa akimtizama akiingia akiwa hai. Lakini sasa alikuwa akimtizama akiwa maiti. Akimtizama akiwa amechinjwa shingo na kutenganishwa. Hakuwa anamtizama mtu mwingine, hakuwa akimtizama mnyama ama picha za video. Bali alikuwa akimtizama Salha akiwa uchi wa mnyama huku kichwa na kiwiliwili vikiwa vimetenganishwa. Hakukiamini kitu hicho, hakuamini kama Salha ameuawa katika namna ile. Akarudi nyuma na kuiacha ile hoteli akiwa amechanganyikiwa. Akiwa amefura kwa Hasira. Aliamua kuwarudia vijana wale kule kigogo. Akatembea katika namna ya kuonyesha kutokuwa makini. Hakupita hatua hata nne akaisikia sauti ikitokea nyuma yake.. sauti ya mwanaume asiye na utani.. mwanaume shupavu. "Tupa Bastola yako chini na usigeuke." Masimba akatii akijiona mpumbavu. Akauona mwisho wake, akajua kwanza safari hii hawezi kupona. Akaituma bastola chini kisha kuinyanyua mikono juu. Akakisikia kidole cha mtu wa nyuma yake kikiitoa risasi katika chemba cha usalama. Sasa alikuwa akilipuliwa. Lakini kabla ya hilo akahisi umajimaji ukimmwagikia katika mavazi yake. Maji maji ambayo yalimfanya ageuke kuangalia nyuma. Hapo akakutana na tukio jingine la kushangaza. Maiti ya mtu ilikuwa nyuma yake, maiti ya mtu ikiwa haitazamiki kwa Risasi. Kichwa kikiwa kimefumuliwa. Yalikuwa matukio yaliyotokea katika kipindi kifupi sana. Ndani ya sekunde thelathini. Nani amemuokoa katika hili? Nani amemuua huyu mtu..? Akiwa anajiuliza akamuona mtu akitokea, mtu ambaye aliiduwaza akili yake kwa sekunde tano. Teddy Harry alikuwa akitokea taratibu akitembea kuelekea pale aliposimama yeye. Teddy mwanamke wa maisha yake. Teddy mzuri na hata teddy mtamu. Mkononi alikuwa ameishikilia bastola ya kirusi Special colt 38. Alikuwa akitembea kwa madaha yote. Alikuwa akinataka katika mwendo wake wa twiga.
Alifanana na Nuru wa Joram kiango, akifanana na Yule Veronica wa Willy gamba. Alikuwa mfano wa Regina wa Sudi. Alinata na kunata. Alipofika aliposimama Masimba teddy akajitupa kifuani huku akimgonga Masimba Mgongoni. "Kuwa makini Baba ningekupoteza mpenzi wangu. Aliongea teddy akiendelea kujilaza kifuani kwa masimba. Kwa mara ya kwanza masimba akaamini Teddy alikuwa amebadilika. Teddy alikuwa amerudi katika uaminifu wale. "Nimeamini mpenzi, nimekuamini kutoka moyoni. Huu niwakati wa kuondoka." Aliongea masimba wakitoka Ndani ya Hotel. Walitoka kama kawaida pasipokutiliwa shaka. Wakatoweka katika namna ambayo hakukuwa na mtu aliyewaona au kuwatilia shaka
*******
Wakati Masimba akielekea masaki nyumbani kwa mkurugenzi wa idara ya ujasusi, teddy alikuwa akielekea kigogo baada ya kupewa maelezo na Masimba kuhusu kushuka kwa vijana wale ambao anahisi watakuwa na maelezo kuhusu aliyemuua Salha. Alisaidiwa na giza usiku ule kutembea bila kuonekana mpaka kigogo. Akapokelewa na sauti za mbwa waliokuwa wakibweka. Teddy akatulia gizani kwa muda akiichunguza nyumba aliyoambiwa. Ilikuwa nyumba nzuri pekee katika Nyumba zote zilizolizunguka eneo lile. Licha ya uzuri huo lakini pia ilizungushiwa miti ya michongoma ambayo iliifanya nyumba hiyo ionekane kama kichaka. Upande wa nyuma wa nyumba ile kulikuwa na migomba mingi ambayo ndani yake palionekana uwepo wa kinjia kilichopita katikati ya migomba. Teddy akahama pale nakuzunguka upande mwingine wa Jengo lile. Akakutana hata upande ulijengwa na kupandwa migomba kama Upande aliopita. Akaangaza macho huku na huko alipoona kuna utulivu wa kutosha Teddy alijibunua na kuchupa kisha kutua ndani katika sekunde ile ile. Utuaji wake ulikuwa mfano wa paka anayenyatia panya. Baada ya kutua hapo akapokewa na giza nene na totoro. Taa zisizo na mwanga ndizo zilizokuwa zikiwaka ndani ya Nyumba ile. Wimbo wa Shania Twain still the one ndio pekee uliosikika ukihanikiza katika nyumba ile. Wimbo ulioonyesha uburudishaji wa miili ya mtu kutoka mahala fulani. Akaachana na hilo sasa akawa anatafuta nafasi ya kuingilia ndani ya nyumba ile. Hakutaka kufanya haraka kutokana na kutokiamini sehemu ile. Aliogopa na kuogopa kugutukiwa mapema. Aliamini kwa mazingira yale hapakosi mtu anayetizama usalama. Kutoka pale alipo akaokota kupo ambalo lilikuwa pembeni yake na kulitupa upande mwingine tofauti na alipo, nia ikiwa ni kujua kama kuna mtu au lah.
Hazikupita hata dakika akamuona mtu akitokea katikati ya migomba. Mtu huyu alikuwa amevaa mavazi meusi ambayo yalifanana kabisa na giza la sehemu ile. Mtu yule mkononi alikuwa amekamatia bunduki aina ya Sub Machine Gun. Akazunguka akiutizama kila upande. Teddy akaanza kutambaa mfano wa nyoka kuelekea pale aliposimama yule mlinzi. Alikuwa mfano wa kiza na mfano wa kivuli cha migomba. Hata alimfikia karibu mlinzi yule hakumuona. Teddy akafyatuka mfano wa mshale na kumtia kabari na kuanguka naye chini. Kufika chini akamshika shingo na kuivunja. Yule mtu akakata roho pale pale. Baada ya kummaliza akamburuza mpaka katikati ya Migomba. Akamuacha hapo yeye akaanza kusonga kuelekea ndani ya Nyumba ile. Alitembea kwa umakini wa hali ya juu. Alitembea kwa umakini mpaka pembozini mwa nyumba. Hapo akatulia kusikiliza sauti. Bado sauti ya wimbo wa shania ilikuwa ikipenya masikioni mwake. Akaongeza hatua nyingine mpaka mlangoni. Akausukuma kidogo, akauona mlango ukifunguka. Akagundua haukuwa umefungwa.. Akausukuma tena kidogo, akajikuta yupo ndani ya korido moja ndefu. Akasogea haraka ili kuipita ile korido. Akiwa anakaribia kuimaliza, mlango wa mbele yake Ukafunguliwa...