NITAKUPATA TU
SEHEMU YA 052
Teddy akasimama akiwa ameduwaa akiutizama mwili wa mwanaume yule wa kizungu uliolala katikati ya dimbwi la damu. Nani amemuua mwanaume huyu? Nani anawaua watu hawa? Anawaua kwa sababu gani? Je wanaficha ushahidi? Yalikuwa maswali tata kichwani kwa teddy. Bado bastola ilikuwa mkononi akiinyoosha kuelekea kule ulipo lala mwili. Sasa akaamua kusogea akiwa makini kwa kila hatua. Akauruka mwili ule kisha kuingia ndani kabisa ya chumba cha mwanaume yule. Kuingia huko macho yake yakainasa vurugu, vurugu iliyofanywa kabla ya mwanaume yule kuuawa. Kila kitu kilikuwa chini ama kimevunjika ama kusambaa. Damu ilianzia ndani kabla ya sebuleni. Muonekano wa mtu yule aliyeuawa ilionyesha kuwa aliuawa akiwa kule sebuleni. Lakini kuvurugika kwa vitu sambamba na matone ya damu yalikivuruga kichwa cha teddy. Ilionyesha waliouawa walikuwa wawili. Ilionyesha aliyeuawa chumbani alikuwa mwingine. Ni hapo alipoipata hamu, hamu ya kumtafuta ama kumuona mtu mwingine aliyeuawa. Lakini angemtafutia wapi ikiwa hapakuwa na sehemu nyingine ya kutokea? Hapo ndipo alipoifanya akili yake kufanya kazi. Akatambua lazima kuna sehemu kuna mlango wa kupitia. Mlango ambao ndio uliotumiwa na watu kumficha huyu marehemu wa pili. Umakini ukaongezeka. Teddy akaangalia kila upande kama angeweza kugundua chochote. Lakini haikuwa rahisi. Haikuwa rahisi kwa kuwa hakuuona mlango wala alama yoyote iliomuonyesha kama kuna sehemu ya kupitia. Bado hakuamini alitaka kuhakikisha ukweli, mawazo yake yalimwambia ipo sehemu. Ni hapo wakati akiwaza hilo alipouona ufa ukutani. Lakini kilichomgutusha, huu haukuwa ufa wa kuonyesha dalili ya kubomoka kwa ukuta. Bali huu ulikuwa ufa wenye kunyooka kuonyesha kwamba ulitengenezwa maalum. Teddy akasogea huku umakini ukiwa katika kiwango cha juu. Alipoufikia ule ufa akafanya kama anaugusa ukuta, punde akashangaa ukuta ukijifungua. Akatupa macho ndani kwa chati, damu tena ilionekana mle ndani. Sasa akaamua kuingia kabisa kwenye chumba kile cha siri akiifuatilia ile damu. Damu iliyotapakaa katika chumba kile cha siri. Kuingia kwake ndani kukafuatiwa na tukio la kujifunga kwa ule ukuta. Punde akajikuta akitizamana na wanaume wanne walioshiba kama wacheza mieleka. Ni katika kasi ile ile teddy akataka kunyoosha bastola afyatue risasi. Lakini hakuwahi kulifanya hivyo. Kwani kwa wepesi wa unyoya, akajikuta akipokea mateke matatu mfululizo kutoka kwa mmoja kati ya wale wanaume wanne. bastola yake ilikuwa pembeni sasa alikuwa amesimama akiwa mikono mitupu. Wanaume wale wakamtizama kwa dhihaki. Wakamtizama wakimdharau. Muda mfupi wakaanza kumfuata wote kwa pamoja. Teddy akawa anarudi nyuma. Ni kipindi akigota ukutani ndipo alipouona ukuta ukifunguka tena. Akamuona mwanamume akiingia katika namna itiayo burudani Moyoni na Hata machoni. Mwanaume aliyeingia mfano wa kivuli. Teddy akataka kwenda kumkumbatia, lakini hakuweza kufanya hivyo. Hakuweza kwa kuwa uingiaji ule ulimpa kihoro. Kwanza hakuamini kama mtu huyu anaweza kuwa pale. Akamuangalia alivyokuwa akitembea, akahisi labda alikuwa akumtizama Joram kiango, akahisi huyu labda ni willy gamba.
Hata wanaume wale wanne walikuwa wameduwaa wakimwangalia kijana huyu aliyekuwa akiingia. Sio kwamba hawakumjua, sio kwamba hawakumuona, bali hawakutarajia hilo. Hawakutarajia ujaji wa mwanaume yule. Yule ambaye waliambiwa yupo tanga kwenye msiba wa mama yake. Lakini leo hii alikuwa mbele yao akitembea kama dume. Dume ambalo halikuonyesha hofu. Hata wao wakalishangaa na kuduwaa. Hawakumuangalia Teddy tena, wakamuache Teddy akinata na kuzunguka. Masimba akampita Teddy kisha kwenda kusimama mbele ya wanaume wale. Haikuchua hata sekunde katika tendo lile lililotendeka. Tendo lililowaacha wanaume wawili kati ya wanne wakianguka chini. Kila mmoja alikuwa akitoka damu kooni. Kisu kilikuwa kimepita kwenye shingo zao. Hili liliwashtua wanaume wawili waliobaki. Wakaamua Kujaribu bahati yao. Mmoja akatupa teke ambalo lilimpata Masimba na kusababisha bastola yake kuanguka. akabaki mikono mitupu. Ngumi zikapigwa katika aina fulani inayovutia. Licha ya kuwa na miili mikubwa lakini wanaume wale walikuwa wakiziweza ngumi. Yalikuwa mapambano yaliyodumu kwa Dakika Sita. Mapigano ambayo yalimfanya teddy ajisikie Hamu. Sio hamu ya tendo bali ilikuwa hamu ya kupambana. Lakini alipokuja kutizama Chini akaiona miili ya wanaume wale ikiwa sakafuni wakivuja damu. Baada ya kuwamaliza wale, masimba akamshika teddy na kumuongoza. "Hatutakiwi kuwa hapa, kuna mtu anatembea na sisi. Kuna mtu anaufuta ushahidi. Lazima tumjue." Aliongea masimba huku wakitokea mlango wa nyuma wa jengo lile kuelekea Nje. Wakatoka nje kabisa ya jumba lile. Ilikuwa safari ya kumtafuta mtu anayewazidi kwa kuwaua wale watu muhimu. Ni lazima wafanye hivyo. Safari hii ikaishia mpaka katika ile nyumba ya siri. Humo ndani wakapokewa na France sambamba na Salha. Hilo likaonyesha kumshtua Teddy. Hakutegemea kukutana na lile. Hakutegemea kumuona Salha sambamba na france pale ndani. Hapo akahisi kitu kikiupenya Moyo wake na kujikuta akitamani kuongea kitu. Sio kwamba alimuogopa Salha bali kitendo cha kumkuta pale akiwa na france ambaye alikuwa mikononi mwake ilimfedhehesha sana. Masimba aliligundua hilo mapema. Masimba aliugundua wivu katika uso wa teddy. Wivu sambamba na kutokuamini ni moja ya vitu vilivyomchanganya. Akamsogelea Teddy na kumkumbatia, "usihofu mama huyu ni mmoja kati yetu.. alichokifanya kumchukua France ilikuwa ni usalama wa mtoto sambamba na Familia. Watu hawa wangegundua hili tungempoteza Vicky sambamba na familia nzima.." aliongea Masimba. Teddy akanyamaza kwa muda, kisha akasogea na kumkumbatia france.
*******
Ulikuwa usiku wa manane pale Masimba alipokuwa mezani akikagua nyaraka alizopewa na yule mama wa ofisi ya waziri mkuu. Alikuwa akipekua moja baada ya nyingine. Akaisoma kwa makini na kupitia kila neno. Mawasiliano ya waziri mkuu na baadhi ya watu. Nyaraka muhimu za uingizaji na usambazaji wa biashara ya madawa ya kulevya. Biashara ya pembe za ndofu ni kitu ambacho kilikuwa kikifanywa na Ofisi ya waziri mkuu. Mikakati na mipango ya biashara hiyo ilisukwa kwa ustadi na watu wazito ndani ya serikali. Tembo, twiga na hata meno ya tembo vilisafirishwa kwenda china na watu wanaonekana kama Watalii. Kila mstari aliokuwa akiusoma alijikuta mwili ukimsisimka kutokana ya kile kilichomo ndani ya nyaraka zile. Waziri mkuu alikuwa ametengeneza genge la uharifu kwa kutumia cheo chake. Lasilimali za Nchi zilikuwa zikisafirishwa kila uchwao kwa kupitia mipakani na hata kwenye viwanja vya ndege. Hakikuwa kitu cha kawaida. Akainuka pale na kurudi chumbani. Moja kwa moja akaiendea simu yake, alipoichukua akatafuta namba ya chief. Sekunde mbili simu ilikuwa hewani. "Kuna tatizo kijana?" Aliongea chief kwa sauti ya usingizini. "Nipo kazini mkuu na unaitambua hii kazi. Nakuja muda mfupi hapo nataka unipeleke Ikulu." Akajibu masimba. "Ikulu muda huu? Hujui kuwa kuna sheria na taratibu zake za kuingia. Unadhani usalama wa ikulu wataturuhusu? Alijibu chief kwa aina ya swali. "Wewe ni nani hapa nchini? Mimi ni nani hapa nchini? Ongea na rais muda huu kuwa tunakwenda hapo." Alipomaliza kuongea hayo akakata simu bila kusubiri jibu la Mkurugenzi. Kisha akageuka kitandani kumuangalia Teddy Harry aliyekuwa amejiegemeza kitandani. Akakutana na macho ya teddy yakimtizama. Haya kuwa macho ya kawaida. Yalikuwa macho yanayohitaji kukijua kitu. Teddy alihitaji kuambiwa kitu. Masimba akamtizama sana.. punde walikuwa wamekumbatiana. "Naenda Ikulu mpenzi..Kuna kitu ambacho siwezi kubaki nacho hapa. Naomba uwe mlinzi wangu kwa nyuma yangu. Nataka umuangalie yule ambaye anatembea nasi. Hakikisha huonekani na wana usalama wengine." Aliongea huku akimuachia teddy na kuifuata bastola yake. Akatoka mle ndani akifuatana na Teddy tayari kwa safari ya kupeleka nyaraka Ikulu.