RIWAYA : MKONO WA CHUMA.
MTUNZI : ALEX KILEO.
SEHEMU YA ISHIRINI.
_________
TEMBEA...
_____________
Yule bwana akajitupa chini kabisa, nguvu zilikuwa kama zinataka kumuishia, mara akainuka na kutoka nje, akamkuta Dokta Smith akiwa amekaa huku akilia,
"naona umetimiza hadhma yako" Dokta Smith aliongea huku akijifuta machozi, ila yule bwana mswahili alishindwa kujibu, alikuwa akilia tu.
Dokta Smith akainuka taratibu na kuingia ndani ya hema, huku machozi yakiendelea kumtoka, baada ya kuingia ndani, alifungua sanduku lake na kutoa kichupa kidogo sana kilichokuwa na dawa ya maji iliyokuwa na rangi ya ugoro pembeni iliandikwa antibiotic, kisha akamkamulia BQ mdomoni maji ya kile kichupa, alafu akamuondoa shuka mwilini na kumuacha akiwa amelala mtupu.
Alafu akachukua chupa ya maji safi, akaijaza maji aliyoyachanganya na mizizi iliyotwangwa, akamtundikia kama drip, kisha Dokta Smith akatoka nje huku akijifuta machozi, akaenda kukaa na yule mswahili,
"kile kichupa cha sumu ulichotumia kumuua huyo mwanamke umekiweka wapi?" Dokta Smith aliuliza huku akiwa na hasira,
"nisamehe sana rafiki yangu, roho inaniuma sana kufanya kitendo hiki" Mswahili aliongea huku akifuta kamasi kutokana na kilio,
"Ile sumu upo wapi?" Dokta Smith aliuliza kwa kufoka kiasi kwamba mate yakamtoka, lakini yule bwana mswahili hakujibu kitu aliendelea kulia tu.
Dokta Smith akaona kama anadharauliwa vile, akampiga yule bwana mswahili ngumi kali ya kichwani,
"Ile sumu ipo wapi?" Dokta Smith aliuliza kwa hasira huku akimkwida shati,, yule bwana Mswahili akaona ni vyema aitoe ile chupa ya sumu, akaitoa mfukoni na kumpatia Dokta Smith,
"mpumbavu wewe" Dokta Smith aliongea huku akiikwapua ile chupa, kisha akamsukuma yule Bwana Mswahili, kisha Dokta Smith akakifungua kile kichupa, akamkata jicho kali yule Mswahili, kisha akaigida dawa yote iliyokuwa katika kile kichupa. Kuona hivyo yule Mswahili akahamaki, akabaki amepigwa na bumbuwazi,
"unafanya nini wewe?" Mswahili aliuliza huku akijaribu kumpora ile dawa, ila alikuwa amechelewa, alifanikiwa kumpora ila chupa ilikuwa tupu, tayari dawa yote aliinywa Dokta Smith.
Mswahili akapiga hatua moja nyuma na kubaki akishangaa, ghafla Dokta Smith akaanza kupapalika kwa kurusha miguu huku na uko kama anakata roho, kisha akanyooka na kutulia.
Mswahili akajishika kichwa na hasiamini anachokiona, kulia alishindwa, kucheka alishindwa, alibaki mdomo wazi huku nguvu zikimuishia mwilini.
*******************
Sajenti Minja alikuwa yupo kitandani muda huo akimsubiri Tom, bado kichwa chake kilikuwa kikimuwaza yule kijana aitwaye Ray Charles, yaani alikuwa hajielewi kabisa, yaani kwanza alikuwa ahamini maelezo ya habari aliyoisoma mtandaoni kuhusu mtu yule kufa, na pia aliilalazimisha akili yake ijaribu kutofautisha kati ya picha ya mtu yule aliyesoma habari zake kwenye gazeti na mtu yule aliyemvamia siku chache zilizopita, lakini ilishindikana, kwa maana mtu ndiye yule yule mmoja.
Wakati akiwa katika tafakari nzito, alisikia mlango ukigongwa kwa nguvu, akainuka na kuchukua bastola yake, hakuwa akijiamini kabisa, alishamuogopa Ray Charles baada ya kusoma habari zake, alihisi ni mzimu au mtu hasiye wa kawaida.
Sajenti Minja alisogea mlangoni kwa umakini mkubwa, huku nako mgongaji alizidisha nguvu ya kugonga mlango. Sajenti Minja aliufikia mlango na kufungua kwa nguvu, kisha akaelekeza bastola mlangoni,
"we we we bastola hiyo!" Tom aliongea kwa uoga huku akijiziba uso wake kwa mikono, Sajenti Minja akacheka,
"we lazy kweli, yaani unaizuia risasi kwa mkono?" Sajenti Minja aliongea huku akiendelea kucheka,
"mambo gani hayo ya kutishiana bastola hivyo?" Tom aliongea kwa kulalamika huku akiingia ndani,
"sio nakutishia, najihami tu kutokana na kitu nilichokigundua leo" Sajenti Minja aliongea huku akikaa katika kochi,
"ni nini tena?" Tom aliuliza,
"si unakumbuka ule mchoro niliokuonesha siku iliyopita?" Sajenti Minja aliuliza huku akiiweka bastola yake pembeni,
"ndio, si ya yule jamaa aliyekuvamia?" Tom alijibu kwa mtindo wa kuuliza,
"swadakta, ndio huyo huyo" Sajenti Minja alijibu,
"amefanyaje sasa?" Tom aliuliza,
"Yule bwana, ni mtu aliyekufa. Yaani inasemekana amekufa muda mrefu tu" Sajenti Minja aliongea na kumtazama Tom usoni, uso wa Tom ulionekana kutaharuki kabisa,
"sijakuelewa bro" Tom aliongea huku akiwa bado kataharuki,
"ni somo gumu sana kulielewa, ila shika hii simu na uangalie hii habari" Sajenti Minja aliongea huku akimpatia Tom simu yake.
Tom akaanza kuipitia ile habari, alisoma mpaka akaimaliza, akarudia tena, akaisoma mpaka akaimaliza.
"tayari nimeimaliza, sasa hii habari inahusiana vipi na yule jamaa aliyekuvamia?" Tom aliuliza huku akitaka kumrejeshea Sajenti Minja simu,
"umeangalia na picha ya huyo mwanajeshi uliyesoma habari zake?" Sajenti Minja alimuuliza Tom huku akiwa hataki kupokea simu,
"picha zipo kwa wapi?" Tom aliuliza,
"chini kabisa ya hiyo habari" Sajenti Minja alijibu, kisha Tom akashuka mpaka chini katika ile habari, hapo ndipo alipopigwa na butwaa, ni kweli kabisa, picha ya mtu ambaye habari zake inasemekana alikufa, ndiye yule yule Tom aliyemshuhudia nyumbani kwa Sajenti Minja siku chache nyuma.
"hii haiwezekani" Tom aliongea kwa kupaniki,
"ndio imeshawezekana sasa" Sajenti Minja aliongea,
"haya mambo mbona kama ya Sudy Bakari? au amerudi?" Tom aliuliza huku akimuangalia Sajenti Minja,
"sijui, ebu chekecha kichwa ili tupate kitu" Sajenti Minja aliongea kivivu,
"Sasa mimi nitachekechaje kichwa? sijui pa kuanzia" Tom aliongea huku akiitupia kitandani simu ya Sajenti Minja,
"lazy sana wewe, hivi taaluma yako ni nini?" Sajenti Minja aliuliza huku akiinua kichwa chake kumtazama Tom,
"mimi ni muandishi wa habari" Tom alijibu huku akimtazama Sajenti Minja,
"tumia taaluma yako kupata ukweli, usikae kizembe" Sajenti Minja aliongea,
"Sasa mbona sina ajira, nitatumiaje taaluma yangu kupata ukweli? si bora Ningekuwa naandika gazeti au natangaza " Tom alijibu,
"unajua ulimwengu ni kama kijiji? Ebu tafuta maneno ya kujaribu kuchimbua hii habari ya huyu mtu, ukiyapata you jaribu kupost mtandaoni ili tuone ni nini kitafuata" Sajenti Minja alimuelekeza Tom,
"bro hukumbuki kipindi kile nilifanya hivyo kwa lile tukio la waziri wa ulinzi? nilikutana na kashkash nyingi sana. Kwa hiyo bro hilo wazo lako siliungi mikono, naogopa" Tom aliongea,
"wewe fanya kama inawezekana, nakuhakikishia, mimi na vyombo vya usalama tutakuwa nyuma yako" Sajenti Minja aliongea,
"bro usiseme hivyo, mimi najua kwa namna nilivyoteseka" Tom aliongea kwa huruma,
"mbona huniamini wewe, amini mimi nipo nyuma yako" Sajenti Minja alijaribu kumshawishi Tom,
"ujue bro wasiwasi wangu ni kama huyo mtu atajua na mimi nafuatilia mambo yao, ndo hatari itapoanzia, nadhani sasa hivi hana mpango na mimi kwa kuwa anajua simfuatilii" Tom aliongea,
"unakuwa kama mtoto wa kike bwana, watoto wa kiume uwa hatuogopi kupambana Tom" Sajenti Minja aliongea kwa kusihi,
"sawa bro, ngoja nifikirie cha kuandika" Tom aliongea kiunyonge huku akisikitika,
"huo ndio uanaume sasa, basi wewe endelea kufikiria, ngoja nikalete chakula nje" Sajenti Minja aliongea huku akiinuka kitandani na kuvaa shati yake, kisha akaelekea nje na kumuacha Tom akiwa peke yake ndani.
Tom baada ya kufikiri kwa muda mchache kidogo, akaitoa simu yake mfukoni na kuingia "Facebook" akaenda katika account yake na kuandika "UNAMJUA RAYMOND CHARLES? ASKARI WA TANZANIA ALIYEKUFA MIAKA MITATU ILIYOPITA, ILA AMEONEKANA TENA AKIWA HAI. BAADA YA SIKU MBILI NITAKUJA NA HABARI KAMILI" Tom alindika na kurudia kusoma alichoandika, kisha akapost ule ujumbe, akatoka Facebook.
Baada ya dakika mbili, Sajenti Minja alirudi ndani akiwa na chipsi na soda,
"dogo umeshapata cha kuandika au bado unafikiria?" Sajenti Minja alimuuliza Tom,
"nimeshaandika na kutupia Facebook kama dakika mbili zilizopita" Tom alijibu,
"safi, safi sana, tusubiri majibu" Sajenti Minja aliongea kwa furaha huku akimpa Tom mfukn mmoja uliokuwa na chipsi na soda,
"sasa bro mimi niache niende, hizi chipsi nitaenda kula na shemeji yako" Tom aliongea huku akiinuka katika kiti,
"sawa, we wahi, chukua hii utapanda bajaj" Sajenti Minja aliongea huku akimpa Tom noti ya shilingi elfu kumi, Tom akaipokea na kuiweka mfukoni,
"ngoja nikutoe basi" Sajenti Minja aliongea huku akisimama,
"hapana, hapana, we endelea kula tu" Tom aliongea,
"sio vizuri bwana, ngoja nikufikishe hata hapo mapokezi" Sajenti Minja aliongea kwa kusihi,
"we kula bwana, kwani mimi mgeni bwana?!" Tom aliuliza na Sajenti akabaki anatabasamu,
"usiku mwema basi" Sajenti Minja alimuaga Tom,
"poa bro, na kwako pia" Tom aliongea kisha akaondoka, akatoka nje ya geti la hotel, na kuingia barabarani, safari ya kurudi kwake ilianza usiku ule, hakuchukua bajaj, aliamua atembee tu kwa kuwa hakuwa na haraka ya kuwahi kurudi.
***************
Mida Ile ile ya usiku, anaonekana Ray Charles akiwa ameegesha gari yake nyeusi pembezoni mwa barabara, na upande wa pili wa barabara kulikuwa na nyumba nzuri ya Kisasa yenye geti jeusi.
Ray Charles alikuwa akiitazama ile nyumba huku akionekana ana huzuni, alipeleka mkono wake katika picha ndogo aliyoibandika katika kioo cha gari yake, akaipapasa ile picha ambayo alionekana yeye akiwa na mwanamke mrembo, pamoja na mtoto wa kiume wa miaka minne.
Ray aliipapasa ile picha huku akiuma meno yake kwa hisia kali, wakati akiendelea kuwa katika hali hiyo, alishuhudia gari ikasimama mbele ya ile nyumba, kisha akatelemka yule mwanamke mrembo aliyekuwa katika picha ya Ray Charles, baada ya hapo yule mwanamke akasogea mlango wa nyuma na kumchukua mtoto, ambaye huyo mtoto nae yupo katika picha ya Ray Charles. Kisha ile gari ikaondoka, yule mwanamke akagonga geti, mlango ukafunguliwa, yule mwanamke akaingia ndani, Ray Charles akatabasamu, ila tabasamu halikubeba furaha.
Simu yake ikaanza kuita, akaiangalia na kupokea,.
"naam mheshimiwa" Ray Charles aliongea baada ya kupokea simu,
"wewe umeona habari zinazozagaa mitandaoni muda huu?" Rais aliuliza kwa ukali,
"hapana mheshimiwa" Ray Charles alijibu huku akijiuliza ni habari gani?
"Kuna mpumbavu mmoja amepost habari zako Facebook, na watu wengi wameonekana kuvutiwa na habari, ile, ebu ingia uitafute hiyo habari, aliyepost anaitwa Thomas Anthony" Rais aliongea na kukata simu, Ray Charles akaingia mtandaoni na kutafuta jina aliloambiwa, kweli akaikuta ile habari, akaipitia muda mfupi tu, kisha akabonyeza katika jina la huyo aliyeandika habari, shida yake ilikuwa kuiona picha tu ya huyo aliyeandika hiyo habari. Alipofungua picha, akakutana na picha za Tom, Ray Charles akatabasamu kwa hasira, maana huyu mtu anamjua, na kipindi hicho simu yake ilikuwa ikiita, aliyepiga alikuwa Rais.
"umeshaiona hiyo habari?" Rais aliuliza baada ya ray Charles kupokea simu,.
"ndio mkuu" Ray Charles alijibu,
"huyo mtu mtafute siku mbili kabla hajapost habari kamili, na umuue" Rais aliongea kwa mamlaka,
"sawa mkuu, huyu atapatikana leo hii hii" Ray charles alijibu,
"unamjua?! " Rais aliuliza,
"ndio, ni rafiki yake na yule Askari amayefuatilia kesi ya yule dada niliyemuua baharini" Ray Charles alijibu,
"basi uwa, uwa wote" Rais aliongea na kukata simu.
***********
Tom aliendelea kukata mitaa usiku ule. Akaona kama ataendelea kufuata barabara atachelewa vile, alichoamua ni kuingia njia za vichororoni. Alipita kichochoro cha kwanza, kikafuata cha pili, ila kichochoro cha tatu alipofika, alihisi kuna mtu alikuwa akija huku akikimbia, Tom akataka kujikaza asimame, ila akakumbuka mkaa huo una vibaka sana, Tom akaamua akimbie tu. Tom alipoanza kukimbia, yule mtu akaongeza kasi, Tom akakunja kona, yule mtu nae akamfuata huko huko, Tom alikimbia dakika tano tu, akachoka, akaamua asimame huku akihema kwa nguvu, vichomi vilimshika,
"sina hela, nina simu tu, hii hapa" Tom aliongea huku akihema, alishaamini huyo anayemkimbiza ni kibaka. Yule mtu akaichukua ile simu, kisha akaiwasha huku sura yake ikiwa karibu na kile kioo, hapo Tom ndipo aliiona vizuri sura ya yule mtu, alikuwa ni Ray Charles, Tom akashtuka, akaanza kukimbia tena, ila alishangaa akipigwa risasi ya bega na kutupwa chini, Tom akaanguka chali huku akihisi maumivu makali sana begani,
"wewe ndiye unayejifanya unanijua sana?" Ray Charles aliuliza huku akiwa ameelekeza mdomo wa bastola katika kichwa cha Tom,
"nisamehe, mimi nilitumwa tu" Tom aliongea huku akilia, na pembeni ya kichwa chake kulikuwa na mfuko chipsi uliopasuka baada ya kuutupa chini,
"msamaha utasaidia nini kwa jambo ambalo limeshasambaa nchi nzima?" Ray Charles aliuliza huku akiikoki bastola yake, Tom mkojo ukamtoka, Ray Charles akaruhusu risasi usawa wa kichwa cha Tom, Tom akakumbwa na giza nene kichwani, hakuona kitu tena, hisia zake hazikuwa tena duniani, mwili wake ulilegea na hakutambua tena kitu chochote kinachoendelea duniani......
**********ITAENDELEA**********
the Legend☆