Riwaya: Mkono Wa Chuma

Riwaya: Mkono Wa Chuma

RIWAYA : MKONO WA CHUMA

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA ISHIRINI NA NNE.

_______________
ENDELEA.....
_______________

Edward Sambo akapigwa na butwaa, maana mtu aliyeamini amekufa, au mtu ambaye alifanya majaribio mengi ya kumuua, leo hii alikuwa mbele yake wakitazamana uso kwa uso,

"naona vyombo vya habari kila siku vinakuongelea wewe kama shujaa, kwa ushujaa gani uliofanya?" BQ aliuliza huku akiwa amesimama jirani kabisa na Edward Sambo ambaye alikuwa akitetemeka tu,

"sijaja kukupa onyo hapa, nimekuja kujionesha kwako kuwa bado nipo, Mungu amenipa nafasi ya tatu ya kuishi, aliniokoa nilipotaka kulipuliwa na ndege kule katika hifadhi ya wanyama, nikapona. Nafasi ya pili ni ile nilipopigwa risasi baharini, na nafasi ya tatu ni ya wewe kujaribu kuniua kwa sumu, ila bado naishi, nitakufa nikishapata haki yangu" BQ aliongea huku akiiweka bastola yake katika kichwa cha Edward Sambo,

"ondoka, polisi watakuja sasa hivi" Edward Sambo aliongea bila kutegemea,

"Polisi, polisi ndio wakina nani? mimi ni zaidi ya polisi, na uwape ujumbe, waambie kuwa ule unyama nilioufanya hawali, nitauongeza mara mbili, maana wameshindwa kuniua kwa kunitumia mwanajeshi wa kukodi" BQ aliongea huku akiikoki bastola yake, hapo Edward Sambo ushuzi ukamtoka akajikuta anabana miguu bila kutegemea.

Wakati BQ akiendelea kuongea na Edward Sambo, honi za gari zilisikika kutokea getini, BQ akasogea mpaka dirishani na kuchungulia, walikuwa ni polisi, BQ akarudi mpaka aliposimama Edward Sambo,

"ebu ngoja nione kama na wewe unaweza kupewa nafasi ya pili ya kuishi kama mimi, nitafanya jaribio la kukuua" BQ aliongea huku akiiweka bastola yake katika paji la uso wa Edward Sambo,

"nina mengi sana ya kuongea na wewe, ila tutaongea kama utapata nafasi ya kuishi tena" BQ aliongea huku akiikoki bastola yake na wakati huo Edward Sambo alikuwa akiomba polisi waingie ndani tu wamuokoe.

Uko nje polisi waliendelea kupiga honi,

"mbona hatoki?" Dereva wa ile gari ya polisi alimuuliza mwenzake waliyekuwa nae upande wa mbele,

"alafu sio kawaida yake, kila siku uwa tunamkuta getini anatusubiri, leo sijui imekuwaje? au alizidisha kilevi jana?" Yule Polisi mwingine alihoji,

"kwani anakunywaga yule mzee?" Polisi dereva aliuliza huku akicheka,

"anapiga vyombo huyo, tena zile pombe kali kali" Yule polisi mwingine alijibu, kisha akatoa shingo kwa dirishani na kuangalia katika upande wa nyuma wa gari ambao kulikuwa na Askari katika bodi ya gari,

"mmoja ashuke akamuangalie ndani" Askari alipaza sauti kuwaambia wenzake, wakati askari mmoja akishuka ili aingie ndani, walisikia mlio wa risasi, wote wakaruka chini na kulala, walijua kabisa mlio ule umetokea ndani ya nyumba ya Edward Sambo.

Wakiwa bado wanajipanga namna ya kuingia ndani, walisikia mlio mwingine wa risasi, Askari mmoja mwenye nyota mbili, akainua mkono na kutoa ishara watu wawili waingie ndani, kisha yule Askari mwenye nyota akasogea getini na kufungua, Askari wawili wakaingia ndani kwa mtindo wa kutambaa ardhini, kisha wale wa nje wakasubiri sekunde thelathini, hawakusikia shambulio jingine lolote. Askari yule mwenye nyota mbili akatoa ishara kuonesha Askari wengine watatu waingie ndani, Askari watatu wakasogea na kuingia ndani ya geti, kisha yule Askari akaingia na yeye, akatambaa mpaka katika mlango wa kuingilia sebuleni wa nyumba ile, akawaita vijana wake kwa ishara, wakasogea mpaka karibu yake kwa tahadhari kubwa,

"tunavamia sasa, mmoja atafungua mlango, alafu sisi tutaingia kwa kasi ndani na kutawanyika ili kumchanganya adui, sawa?" Askari mwenye nyota mbili aliuliza na wenzake wakajibu kwa kutikisa kichwa kuonesha kukubaliana nae, kisha yule Askari akahesabu kwa vidole mpaka tatu, mmoja wao akafungua mlango kwa kasi, na wengine wakarukia ndani huku silaha zikiwa mkononi, wakamkuta Edward Sambo akiwa amekaa katikati ya dimbwi la mkojo huku akihema haraka haraka,

"mzee Kuna usalama?" Askari mmoja alimuuliza, Edward Sambo akaitikia kwa kichwa kukataa,

"nini tatizo?, maana tumesikia mlio wa risasi" Askari aliuliza,

"BQ" Edward Sambo aliongea,

"ndio nini?" Askari aliuliza,

"sio ndio nini, sema ndio nani?" Edward Sambo aliongea huku akimtazama yule askari usoni,

"sawa, BQ ndio nani?" Askari aliuliza,

"Yule mwanamke muuaji tunayemtafuta" Edward Sambo alijibu na kuwafanya Askari washangae na waweke vizuri silaha zao,

"kafanyaje?" Askari aliuliza,

"ndio aliyepiga zile risasi, alinivamia" Edward Sambo alijibu

"Yupo wapi sasa" Askari aliuliza,

"atakuwa ameshaondoka, alielekea katika chumba changu, kisha kama mlisikia ule mlio wa risasi wa mara ya pili, nadhani alitumia kuvunja kioo cha dirisha, maana alipiga ile risasi akiwa ndani" Edward Sambo aliongea,

"lakini dirishani si Kuna nondo?" Askari aliuliza,

"ndio zipo, kwa hiyo inawezekana bado yupo ndani?" Edward Sambo aliuliza huku akipata nguvu ya kuamka baada ya kugundua kuwa hata kama yule mwanamke amevunja kioo, basi nondo zitamshinda,

"Twendeni" Askari mwenye nyota mbili aliwaambia wenzake huku akiongoza kuelekea katika vyumba, kulikuwa na vyumba viwili tu, kimoja uwa kinafungwa muda wote, kwa hiyo wao walienda moja kwa moja katika chumba cha Edward Sambo, wakapigwa na mshangao mara baada ya kuliona dirisha, ndio kioo kilivunjwa, ila nondo za dirisha hazikukunjwa, ila zilikatwa kabisa, tena sio na machine, inaonesha zilikunjwa kunjwa mpaka zikakatika.

"huyo mwanamke ni mwanaume?! " Askari mmoja aliuliza baada ya kuona hilo tukio,

"acha maswali ya kipumbavu" Mkubwa wake aliongea huku akisogea dirishani.

"ameshaondoka, hakika BQ bado ana uwezo mkubwa sana" Edward Sambo aliongea na kufanya Askari wamtazame,

"unamjua muda mrefu kwani?" Askari alimuuliza,

"sana, tena sana" Edward Sambo alijibu,

"twende ukatoe taarifa ya kuvamiwa kituoni, na hayo maelezo mengine utayatoa mzee wangu" Askari mwenye nyota mbili alimwambia Edward Sambo,

"ngoja nikaoge wadogo zangu, si mnaona hali niliyonayo?" Edward Sambo aliongea huku akiwaonesha eneo la mbele la suruali yake, lilikuwa limelowana mkojo.

Ilibidi polisi wamsubirie Edward Sambo aoge, safari ya msituni haikuwepo tena, maana mtu waliyekuwa wanaenda kumtafuta, waliambiwa ametoka muda sio mrefu.

Baada ya nusu saa, Edward Sambo alikuwa ameshamaliza kuoga, wakatoka pamoja mpaka nje, wakaingia katika gari, safari ya kituoni ikaanza.

Iliwachukua muda mchache tu kufika kituoni, wakatelemka na moja kwa moja walimpeleka Edward Sambo katika ofisi ya mkuu wa polisi, alitakiwa akaeleze alichokutana nacho kutoka kwa BQ.

***************

Baada ya mahojiano kati ya mkuu wa polisi na Edward Sambo kuisha, habari ya kuonekana kwa dada muuaji ilienea kwa haraka sana, safari hii mpaka jina liliwekwa wazi, jina lake halisi, Maria Zyachenko.

Mishale ya saa moja usiku, mkuu wa polisi alipigiwa simu kutoka ikulu, alihitajika na Rais kwa haraka sana.

Mkuu wa polisi alishangaa huo uito, maana tangu alivyoapishwa ndani ya ikulu, hajawahi kufika tena eneo hilo.

Mkuu wa polisi alifika mpaka Ikulu, akakaguliwa mlangoni na kuruhusiwa aingie, akaingiza gari na kuiegesha katika sehemu maalum za maegesho, kisha akatelemka na kuanza kuelekea ndani, ila alisimamishwa na mlinzi mmoja wa Ikulu, akampa heshima yake,

"mheshimiwa Rais yupo upande wa nyuma katika bustani, anakusubiri wewe, naomba nikupeleke" Mlinzi aliongea, kisha mkuu wa polisi akamfuata mpaka nyuma ya nyumba. Walimkuta Rais akiwa amevaa kaptula, laptop ilikuwa mezani, na pembeni ya laptop kulikuwa na chupa kubwa ya mvinyo, na kulikuwa na bilauri mbili, moja ilikuwa na kinywaji, inaelekea Rais alikuwa akinywa, na nyingine ilikuwa tupu.

Mkuu wa polisi alipofika karibu na Rais, alimpigia saluti,

"kaa hapo" Rais alimwambia mkuu wa polisi, na wakati huo yule mlinzi aliyemleta mkuu wa polisi alikuwa akiondoka.

Rais akachukua chupa ya mvinyo na kumimina katika ile bilauri tupu, kisha akamsogezea mkuu wa polisi, mkuu wa polisi akaipokea kwa heshima na kuigida kiasi, kisha akaishusha mezani.

"za siku bwana" Rais alimsalimia mkuu wa polisi,

"nzuri mheshimiwa" Mkuu wa polisi aliitikia kwa uoga,

"nataka kujua haya mambo wewe unayaendeshaje, maana sioni matokeo yoyote mpaka sasa?" Rais aliuliza huku akiifunga laptop yake na kumuangalia mkuu wa polisi,

"mambo gani mheshimiwa?" Mkuu wa polisi aliuliza huku mapigo ya moyo yakiongezeka kasi, maana mpaka Rais akuulize hivyo, ujue kuna jambo hujalifanya kwa ufanisi,

"Habari ya huyo mwanamke muuaji, wewe unaichukuliaje?" Rais aliuliza na kumfanya sasa mkuu wa polisi afikirie kwa muda,

"ni jambo zito kwa kweli, ila kama unavyosikia kupitia vyombo vya habari, huyu mwanamke baada ya ukimya kidogo, aligundulika alikuwa msituni, tena alikuwa na hali mbaya, tukatuma vijana waende wakamkamate uko, ila hatukufanikiwa kumpata mpaka leo tena tulivyosikia ameonekana asubuhi kwa Edward Sambo" Mkuu wa polisi alieleza,

"hii kesi nyie mnaifuatiliaje?" Rais aliuliza,

"samahani mheshimiwa, sijaelewa swali" Mkuu wa polisi aliongea kwa utulivu,

"yaani nyie kama polisi, kuna mtu yoyote mmemteua aifuatilie hii kesi au mnasubiri mletewe taarifa na wasamalia wema tu?" Rais aliuliza kisha akagida kidogo mvinyo,

"Kuna mtu maalum nilimteua aifuatilie hii kesi kwa siri" Mkuu wa polisi alijibu,

"amefikia wapi katika upelelezi wake?" Rais aliuliza,

"mmmh, kwa maelezo ya yule mpelelezi, anadai hili jambo, kuna vita nyingine ya mtu mwingine dhidi ya yule dada, na mtu ambaye anadai alimshuhudia akimpiga yule dada baharini na ikasemekana yule dada amekufa, ni Ray Charles" Mkuu wa polisi aliongea huku akimtazama Rais, Rais akatabasamu,

"huyo kijana wako mpelelezi anaitwa nani?" Rais aliuliza huku akitabasamu,

"anaitwa Joel Minja" Mkuu wa polisi alijibu,

"mwambie awe makini sana" Rais aliongea huku akitabasamu, ila hiyo kauli haikueleweka kwa mkuu wa polisi,

"sawa mheshimiwa" Mkuu wa polisi aliongea,

"au kama vipi, nitakupigia simu, nataka nionane na huyo kijana. Siku mbili hizi nitakupigia simu,. Kingine cha ziada, ongeza ufanisi uhakikishe huyo dada anakamatwa, na ikiwezekana afe kabisa, vinginevyo hiyo nafasi uliyonayo utaiweka mashakani" Rais aliongea kwa umakini mkubwa,

"sawa mkuu" Mkuu wa polisi alijibu kinyenyekevu,

"unaweza kwenda" Rais aliongea na kisha mkuu wa polisi aliamka na kuanza kuondoka, alipopotea tu machoni kwa Rais, alitokea Ray Charles, alikuwa amejificha, hakutaka mkuu wa polisi amuone.

"inaelekea wameshajua uwepo wako katika hii kesi, ila huyu mkuu wa polisi hana uhakika na uwepo wako" Rais aliongea lakini Ray Charles hakujibu kitu.

Wakati mkuu wa polisi akitoka, alipishana na mtu mwingine ambaye alimjua kupitia vyombo vya habari tu, hakuwahi kukutana nae, hivyo walipishana kimya kimya tu.

Yule mtu alielekea moja kwa moja mpaka upande wa nyuma wa Ikulu na kwenda alipo Rais, wakasalimiana kwa bashasha, kwa kukumbatiana, kisha yule mtu akakaa katika kiti, ila yule mtu alipotupa macho nyuma ya Rais, alimuona Ray Charles, yule mtu akashtuka, Rais akaligundua hilo,

"usiogope, kwanini unaogopa?" Rais alimuuliza yule mtu,

"huyu si Ray Charles huyu" Yule mtu aliuliza huku akimuoneshea kidole Ray Charles ambaye aliangalia chini,

"ndiye yeye" Rais alijibu huku akitabasamu,

"imekuwaje kuwaje anaishi wakati alishakufa, familia ilishazika mabaki ya mwili wake?" Yule mtu aliuliza,

"unataka kujua imekuwa Ray anaishi tena?" Rais aliuliza huku akitabasamu,

"ndio, nataka kujua kwa kweli, maana huu ni muujiza" Yule bwana alijibu huku akiwa bado akimtazama Ray Charles,

"lakini hicho sicho nilichokuitia hapa?!" Rais aliongea huku akimimina mvinyo katika bilauri yake,

"ulichoniitia utaniambia baadae, nataka kujua kwanini Ray Charles yupo hai" Yule bwana aliongea,

"sawa, Ray, ebu nenda katembee kidogo" Rais aliongea huku akimgeukia Ray Charles, ambaye taratibu aligeuka na kuondoka eneo hilo, yule bwana alikuwa bado anamuangalia tu Ray Charles, hakuwahi kuamini hata siku moja kuwa Ray Charles anaishi,

"huyo utakuwa unamuona kila siku, hata usijali" Rais aliongea huku akimtazama yule bwana,

"aisee, dunia ina maajabu. Haya nieleze ilikuwaje?" Yule bwana alimuuliza Rais,

"ni story ya kusisimua kidogo'' Rais aliongea huku akiweka sura ya umakini,

"nieleze tu" Yule bwana alionesha kiu yake ya kutaka kuujua ukweli,

"sawa, ngoja nikupe ukweli, ila hakuna anayejua ukweli zaidi yangu na yeye, wewe utakuwa wa Tatu" Rais alianza namna hiyo, kisha akaendelea..

"Huyu Ray Charles sio mzimu wala sio robot " Rais aliongea na kumfanya yule bwana awe makini zaidi..........

**********ITAENDELEA**********

*kwani Kuna mtu hataki kujua habari za Ray Charles humu?

Tutamjua zaidi katika episode inayokuja

the Legend☆
Mm mwenyewe nataka kujua habari za ray charles
 
RIWAYA : MKONO WA CHUMA

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA ISHIRINI NA TANO

_______________
ENDELEA.....
_______________

Rais akaendelea kutoa sababu ya Ray Charles kuwa hai,

"katika ule mchakato wa kuipindua serikali ili Tammy Semmy awe Rais, wale watu ambao walikuwa kama bodyguard wa Tammy Semmy, yaani marehemu Gabby, Jimmy na BQ, walikuwa wakishafanikisha ile kazi, kila mmoja angekuwa tajiri, wasingeendelea na kazi to kumlinda Tammy Semmy, kwa maana nyingine mikataba yao ilikuwa inaisha baada ya Tammy Semmy kuchukua madaraka rasmi. Ila baada ya Tammy Semmy kuchukua madaraka, bado Gabby na Jimmy waliendelea kuwa walinzi binafsi wa Tammy Semmy, kwanini?" Rais aliuliza mwenyewe kisha akaichukua chupa ya mvinyo na kuimimina katika bilauri, ila ilionesha haina kitu, akailaza juu ya meza, kisha akaendelea,

"waliendelea kuwa walinzi wa Tammy Semmy kwa sababu mlinzi aliyetakiwa kuja kuwa anamlinda Tammy Semmy, alikodiwa na jeshi la Somalia kwa ajili ya kwenda kumuua mkuu wa kikosi cha Al shabab, alienda yeye na wenzie watatu, yaani huyo mlinzi ninayemzungumzia ni Ray Charles" Rais aliongea na kumtazama yule bwana,

"kwa hiyo ina maana ile habari iliyotolewa na al shabab juu ya kuwa watu awa walienda kuwachunguza kumbe ilikuwa habari ya kweli?" Yule bwana mwingine aliuliza huku akikaa vizuri zaidi,

"ni habari ya kweli, ila kule walienda bila serikali kujua, walienda kwa makubaliano binafsi baina ya Tommy Semmy na serikali ya Somalia. Kwa hiyo hata walipokamatwa kule, serikali yetu ilikataa kuwatambua, hivyo wale wanamgambo wakaamua kuwaua, ila baadae serikali ilidai kuwatambua ila ikadai haikuwa na taarifa zao. Ila kumbuka kabla Ray Charles hajaenda somalia, tayari aliandaliwa kuwa mlinzi wa Tammy Semmy kutokana na mafunzo maalum aliyokuwa nayo Ray Charles.

Kwa hiyo basi baada ya serikali kuwatambua, viongozi kadhaa wa serikali walienda somalia kuonana na viongozi wa Al shabab, ambapo viongozi hao walikataa kuwapa viongozi wa serikali miili ile mpaka wapewe pesa, serikali ikatoa pesa na viongozi wale wa serikali wakaichukua miili ile na kurudi nayo, ila ilionekana katika ile miili kuna miili miwili ilikuwa bado na uhai ingawa ilikuwa na matundu mengi ya risasi, serikali ikaipeleka ile hospital, ikaonekana ni lazima wafe, kulikuwa hakuna dalili za watu hao kupona, ila madaktari wakashauri labda wapelekwe nje ya nchi, Tammy Semmy akatoa pesa na miili ile ikapelekwa nje, ila mmoja kati ya wale watu alifia njiani, kwa hiyo ukabaki mwili mmoja ambao ni wa Ray Charles.

Mwili ule ulifikishwa China, baada ya kuuchunguza kwa umakini, wakagundua kuwa Ray Charles ataendelea kuishi, ila kama mfu, yaani ataishi ila hatoamka tena, ataendelea kupumua ila ubongo wake na mwili wake havitofanya kazi tena" Rais aliongea kisha akanyamaza, akachukua simu yake na kupiga simu ndani, aliagiza mvinyo mwingine.,

"hii habari inasimumua, lakini mwili wa Ray Charles si tuliuzika kabisa na tuliuaga?" Yule bwana mwingine aliuliza huku akitoa tabasamu la mshangao,

"usiwe na haraka basi, hivi nilikwambia ubongo wake na mwili havitofanya kazi tena?" Rais alimuuliza yule bwana,

"ndio" Yule bwana mwingine alijibu,

"nimekosea, ni kwamba mwili hautofanya kazi tena, ila ubongo ulikuwa ukifanya kazi kwa taratibu sana, unaweza kumuwekea soda mbele, ila akaitambua baada ya wiki.

Sasa wale wachina wakashauri wanaweza kumsaidia kwa njia mbili, ya kwanza ni kummalizia tu, yaani kumuua, na ya pili ni kumuwekea mwili wa bandia, hilo la kwanza, la pili walisema wana uwezo wa kumfunga vifaa vidogo vidogo katika kichwa chake kwa ajili ya kuusaidia mfumo wake wa ubongo kuwa na kasi ya kawaida,

Kwa kuwa Tammy Semmy alikuwa anampenda sana Ray Charles, Tammy Semmy akakubali kumtengeneza Ray Charles, kwa hiyo akakubali kuingia makubaliano ya mkataba wa kuokoa uhai wa Ray Charles, ila gharama za kumfanya Ray Charles aendelee kuwa mtu, zilikuwa kubwa, Tammy Semmy hakuwa na pesa kipindi hicho, pesa zote alizitumia katika mpango wake wa kuingia ikulu. Sasa alichokifanya Tammy Semmy ni kutoa eneo kwa wale wachina, na eneo lenyewe ndio hilo ambalo huyu mwanamke anayetusumbua kwa kuua viongozi, alipewa hilo eneo na Tammy Semmy, tena alipewa kwa mkataba na sahihi za pande mbili, wakiwemo mashahidi, ila na hao wachina tena akawapa hilo eneo, tena kwa mkataba, kwa hiyo basi ikawa Tammy Semmy ameingia mikataba miwili kwa mara moja, ubaya zaidi kuwa hiyo mikataba ililenga sehemu moja. Sasa basi ili kuwa huru, Tammy Semmy aliamua kutumia mbinu za kuua upande mmoja alioingia nao mkataba, na upande alioona utakuwa rahisi, ni upande wa BQ, kwa hiyo akamtengenezea ajali ya ndege, na zoezi likafanikiwa, kila mtu akajua BQ amekufa, mpaka leo wapo wanaoamini BQ amekufa, hata mimi niliamini hivyo, mpaka niliposikia tena habari zake. Je unajua kama BQ amerudi tena?" Rais aliuliza huku akisimama,

"hapana, kwanza mimi ni mmoja wapo ninayeamini BQ amekufa" Yule bwana mwingine alijibu,

"BQ hajafa, yule mwanamke anayeua viongozi wa serikali, ndio BQ" Rais aliongea na kumshangaza zaidi yule bwana,

"bwana wewe, mbona leo unaongea vitu vya kushangaza hivi?" Yule bwana mwingine aliuliza,

"ngoja niende kujisaidia haja ndogo, nikirudi sitoendelea na habari za BQ, nitaendelea na habari za Ray Charles, maana habari zake ndio zimeleta na haya" Rais aliongea huku akiondoka eneo hilo na kumuacha yule bwana akitoa miguno ya mshangao.

***************

Sajenti Minja asubuhi ya leo alikuwa ameamka mapema sana, alikuwa amekaa huku akiona mambo kama yanaenda nyuma na kwenda mbele, yaani mambo yalivyokuwa yanaenda hakujua kabisa, sana sana vitu vilivyomchanganya ni pamoja na watu anaowafuatilia, hawakuwa wakieleweka ni watu au majini? kwa maana akikumbuka lile tukio la kumgonga na gari Ray Charles, kisha akamkanyaga, lakini Ray Charles akaamka na akaendelea kuwashambulia, kitu cha pili kumuhusu Ray Charles ni siku ile Ray Charles alipomvamia, anakumbuka kuwa alimpiga risasi nyingi sana mwilini, lakini Ray Charles hakupata majeraha,

"hapana kwa kweli'' Sajenti Minja aliongea huku akitikisa kichwa kuonesha hakubaliani na utu wa Ray Charles,

"au mzimu? maana kufa alikufa kweli, imekuwaje anaishi?, na yule mwanamke muuaji nae ndio wale wale, yaani nilishuhudia akipigwa risasi ya kichwa, pia akazamishwa na bahari, eti leo hii anaishi? hii ni ngumu kuwezekana" Sajenti Minja aliongea na kutabasamu, yaani alikuwa kama mwendawazimu.

Kilichomtoa katika wimbi la mawazo, ni simu yake ilionesha ikiita, alipoangalia namba ya mpigaji, alikuwa ni mkuu wake wa polisi, akapokea simu haraka.

"upo wapi?" Mkuu wa polisi aliuliza, siku hiyo hakuanza hata na salamu,

"bado nipo hotelini" Sajenti Minja alijibu,

"kazi imekushinda sasa unaamua kulala lala tu, hujui hela ya hoteli unayolipiwa inatoka serikalini?" Mkuu wa polisi aliuliza kwa hasira na kumfanya Sajenti Minja aendelee kuduwaa,

"najua mkuu" Sajenti Minja alijibu kwa sauti ndogo,

"njoo ofisini kwangu, nakupa dakika tano tu, unatakiwa uwe mbele yangu" Mkuu wa polisi aliongea na kukata simu, Sajenti Minja akaangalia kioo cha simu yake na kumshangaa mkubwa wake kwa yale maneno yake,

"sidhani kama Kuna wema" Sajenti Minja aliongea huku akiinuka katika kitanda, aliamua kuvaa nguo moja kwa moja, hakutaka kwenda kuoga kwa maana alipewa dakika chache mno, kwa hali ya kawaida tu, mwendo wa kutoka hapo hotelini mpaka katika kituo cha polisi, ni mwendo wa zaidi ya dakika kumi, sasa leo amepewa dakika tano tu.

Sajenti Minja alitoka mbio mpaka nje, akachukua boda boda iliyomfiksha mpaka kituoni, akamlimpa dereva bodaboda kisha akawa anakimbia kuelekea katika ofisi ya mkuu wa kituo, dakika tano zilishaisha muda tu.

Sajenti Minja alifika mpaka katika mlango wa mkuu wa polisi na kugonga hodi, hakujibiwa, akaamua kusukuma mlango na kuingia, akamkuta mkuu wake akiwa amekaa tu, mezani hakukuwa na kitu kama kawaida, maana Sajenti Minja alishazoea kuwa kila akija hapo ni lazima akute mkuu wake akipitia makabrasha kadhaa yenye kesi za watu.

Sajenti Minja alipokaa, ukimya ukatawala,

"upelelezi wako wa kesi ya huyo dada muuaji umepata kipi kipya?" Mkuu wa polisi aliuliza kwa utulivu,

"kilichoongezeka ni yule mtu tu wa ajabu aliyempiga risasi yule dada kule baharini" Sajenti Minja aliongea kwa utulivu,

"nani huyo?" Mkuu wa polisi aliuliza,

"Yule yule niliyekuambiaga, Ray Charles" Sajenti Minja aliongea na kumfanya mkuu wake akunje sura kwa hasira,

"nilishakuambiga huyo mtu alishakufa, wewe bado unakazania tu, hiyo ni dalili hii kesi inakushinda" Mkuu wa polisi aliongea kwa hasira,

"Mkuu huyu mtu yupo hai na anaishi, kama huamini nenda kaangalie kesi za hapo kaunta, kuna kesi ya mtu kutekwa na mtu huyo" Sajenti Minja aliongea, safari hii alipaza sauti hakuongea kinyonge, mkuu wake akamuangalia, maana hakutegemea ipo siku Sajenti Minja atampandishia sauti,

"sikia Minja, jana niliitwa na Rais, anafuatilia kwa karibu sana hii kesi, na anataka huyo dada auawe, sio akamatwe, vinginevyo mimi nafasi yangu ya kazi itakuwa mashakani" Mkuu wa polisi aliongea kwa huruma, hapo sasa Sajenti Minja akagundua kwanini mkuu wake amechanganyikiwa,

"kwanini auawe, akamatwe afikishwe katika vyombo vya sheria"" Sajenti Minja aliongea,

"haya ni maelezo kutoka juu, hayaitaji kupingwa wala kutiliwa shaka, yanatakiwa yatekelezwe" Mkuu wa polisi aliongea,

"sawa, nitajitahidi mkuu" Sajenti Minja aliongea,

"hakikisha unamtembelea Edward Sambo na unamuhoji kuhusu kitu chochote anachokijua kuhusu dada huyo" Mkuu wa polisi aliongea,

"sawa" Sajenti Minja alijibu,

"unaweza kuondoka, pitia hapo kaunta na uwaambie wanipe jalada la kesi la huyo mtu anayedai kutekwa na Ray Charles" Mkuu wa polisi aliongea, kisha Sajenti Minja akaondoka huku akifurahi kimoyo moyo, aliona lengo lake la kumuaminisha mkuu wa polisi juu ya uwepo wa Ray Charles, lengo linatimia.

Sajenti Minja alifika mpaka kaunta, akamkuta yule Askari aliyeandika maelezo ya Tom,
"wewe peleka kwa mkuu lile jalada la yule dogo niliyemleta wiki iliyopita, hakikisha humwambii mkuu kuwa huyo kijana nilimleta mimi" Sajenti Minja alimwambia yule Askari,

"sawa mkuu" Askari alijibu huku akipekua pekua katika madroo ya meza za pale kaunta.

Sajenti Minja akaondoka zake huku akiwaza kuwa Ikifika usiku, ataenda kuonana na Edward Sambo, sio tu kwa ajili ya kujua habari za BQ, ila pia kumsalimia kwa kuwa ni mshkaji wake wa siku nyingi, ingawa Edward Sambo ana umri mkubwa kidogo kumzidi Sajenti Minja.

****************

Muda wa saa tatu usiku, Edward Sambo akiwa sebuleni, alikuwa ana wasiwasi mwingi sana, ingawa nyumba yake siku hizi ilikuwa na ulinzi wa kutosha, kulikuwa na Askari si chini ya watano na wote wana silaha.

Kawaida muda huo Edward Sambo ni muda wake wa kuingia check chumbai kwa ajili ya kulala, ila tangu BQ amtembelee amekuwa na uoga sana, amekosa kujiamini kabisa.

Edward Sambo alizima runinga na kupiga hatua za kuelekea chumbani, ila mlango wa sebuleni uligongwa, moyo wake ukaripuka kwa hofu,

"nani?" Edward Sambo aliuliza kwa mamlaka,

"mimi Dammy" Sauti ilijibu, Dammy ni mmoja wa Askari aliyezoeana nae sana.

"nini usiku huu?" Edward Sambo aliuliza huku akionekana kutofurahishwa na huo usumbufu,

"nisaidie maji mzee wangu, leo nilisahau kununua dukani, alafu nina kiu sana" Dammy aliongea, Edward Sambo akasogea mlangoni na kufungua, mlango ulipofunguka, Dammy aliingia ndani, ila nyuma yake alikuwa BQ huku akiwa amemuwekea Dammy bastola kichwani, Edward Sambo akahisi jasho likimtoka,.

"asante afande" BQ aliongea na kumpiga na kitako cha bunduki Dammy, alimpiga kisogoni, Dammy akapoteza fahamu na kuanguka chini, yote hayo Edward Sambo alikuwa anayaangalia,

"kaa hapo, naona siku hizi unajifanya bandidu sana, yaani huniogopi kabisa, pamoja na kukutisha sana nilivyokuja hapa mara ya kwanza, lakini bado unatafuta sifa katoka vyombo vya habari kwa kutumia jina langu?" BQ aliuliza huku akimtazama Edward Sambo aliyekuwa ameganda tu,

"hajibu au?" BQ aliuliza huku akiinuka, kitu ambacho hakujua ni kuwa Edward Sambo alikuwa amepoteza fahamu muda mrefu tu tangu alipomuona, kilichokuwa kinamsaidia ni ukuta tu alioegamia,

"wewe mzee" BQ alimuita kwa hasira huku akitaka kumkunja shati, lakini Edward Sambo akaanguka kama mzigo, hapo ndipo BQ akajua mzee tayari amekata moto,

"unajifanya mwamba mbele ya vyombo vya habari, kumbe muoga tu" BQ aliongea peke yake huku akimtazama Edward Sambo aliyekuwa amepoteza fahamu, ila BQ alihisi Kuna mtu amemsimamia nyuma, BQ akageuka kwa haraka na bastola mkononi, ila kwa kasi ya ajabu sana bastola yake ilipigwa teke na kuangukia mbali, BQ akarusha ngumi ya mkono wake mmoja, maana hakuwa na mkono wake wa chuma. Ile ngumi ilidakwa na na kisha BQ alipigwa kichwa katika paji lake la uso, akarudi nyuma huku akipesusuka, kisha akanyooshewa bastola, BQ akabaki anashangaa tu, mbele yake alikuwepo Sajenti Minja huku akiwa hana sura ya mzaha kabisa.

"huyu mwanamke anatakiwa auawe, haya ni maelezo kutoka juu" Sauti ya mkuu wa polisi ilimrudia kichwani Sajenti Minja, Sajenti Minja akaikoki bastola yake, alishaamua kutekeleza maagizo kutoka juu............

********ITAENDELEA*********

the Legend☆
 
RIWAYA : MKONO WA CHUMA

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA ISHIRINI NA SITA.

________________
ENDELEA....
_________________
Ila Sajenti Minja akashusha bastola chini, kuna kitu alikiwaza kichwani mwake, huyu mwanamke ni mara ya pili wanakutana, mara ya kwanza waliwahi kukutana nje ya nyumba ya waziri wa katiba na sheria, anakumbuka mara ya kwanza walivyokutana, yule mwanamke alikuwa na mikono miwili, tena alikuwa na nguvu za ajabu, sasa kwanini safari hii awe na mkono mmoja? Sajenti Minja akairudisha bastola katika sehemu yake, aliamua kujaribu kupigana nae ili aone ni yeye au mwingine, hapo Sajenti Minja alikuwa anacheza kamari,

"ngoja nikupe nafasi ya kujitetea, tupambane" Sajenti Minja aliongea huku akimtazama BQ, BQ akaona huo ndo wakati wa kujitetea, kwanza alidharau uwezo wa Sajenti Minja, kwa maana alishawahi kupambana nae na akamshinda. BQ akafanya kama anageuka anampa mgongo Sajenti Minja, kisha kwa kasi akageuka na teke kali, Sajenti Minja akaudaka mguu wa BQ, tena aliudaka bila kutingishika wala kuumia, kisha akamsukuma BQ, BQ akadondoka chini, Sajenti Minja akapiga piga mikono yake kama anafuta vumbi.

"inuka pambana ili ushinde na ujiokoe" Sajenti Minja aliongea, ila aliona BQ akipeleka mkono sehemu bastola inapokaa, Sajenti Minja akaruka na kutua mbele ya BQ, kisha akapiga teke kali mkono wa BQ uliokuwa unachomoa bastola, basi bastola ikatupwa mbali, BQ akainuka kwa mtindo wa ajabu kabisa, na kwa kasi akamuelekea Sajenti Minja, alipomfikia alipiga ngumi nyingi mfululizo za mkono mmoja, ila zile ngumi Sajenti Minja alikuwa anazipangua kama anajipepea na mkono, yaani ngumi za BQ hazikuwa nzito kabisa, kisha Sajenti Minja akainama na kuichota miguu ya BQ, alafu akamnyanyua juu na kumtupa chini, BQ akapata maumivu,

"ni wewe kweli au mpo wawili?" Sajenti Minja aliuliza huku akimtazama kwa umakini, kipindi BQ alikuwa anavuja damu eneo la kichwani katika kidonda kilichotokana na kupigwa risasi na Ray Charles kipindi cha nyuma, kifupi BQ hakuwa vizuri, yaani aliamua kuingia mitaani kabla hajapona majeraha ya risasi, hicho ndicho kilimfanya akose nguvu na mapigo yake kuzuiwa kirahisi na Sajenti Minja.

BQ akajizoa chini, lakini bado alikuwa katika hali ya kizungu zungu. BQ akamfuata kwa kasi Sajenti Minja, kisha akasimama ghafla, hiyo mbinu ilimchanganya Sajenti Minja, kisha BQ akafanya kama anainama kuivuta miguu ya Sajenti Minja, basi Sajenti Minja yeye alikuwa na kasi mara mbili, yaani kabla BQ hajaigusa miguu ya Sajenti Minja, tayari mikono ya Sajenti Minja ilikuwa imeshafika chini, na hicho ndicho BQ alikuwa anakitaka, basi Sajenti Minja alivyoshika chini tu, BQ aliruka juu ya mgongo wa Sajenti Minja na kutua upande wa pili, kisha akaseleleka mpaka bastola yake ilipoangukia, akainama kuiokota, na kumgeukia Sajenti Minja, akamnyooshea bastola, Sajenti Minja akaanza kuilaumu nafsi yake kwa kumshawishi kupambana na huyo dada, na kipindi BQ alikuwa ameshika bastola kumuelekea Sajenti Minja, ila ile hali ya kizunguzungu ikaongezeka kwa BQ, BQ nguvu zikaanza kumuishia na giza likaanza kuongezeka machoni, BQ akaamua kufyatua risasi kumuelekea Sajenti Minja, lakini kutokana na hali yake, alijikuta shabaha ikipotea na kumkosa Sajenti Minja, kisha BQ akaanguka chini na kuzimia.

Sajenti Minja akabaki anashangaa kwa namna hilo tukio lilivyotokea kwa miujiza, yaani hakuamini kabisa kuwa yule mwanamke muuaji amemuacha.

Sajenti Minja akasogelea sehemu alipokuwa amelala BQ, akamkuta yupo katika usingizi mzito, hakuwa na fahamu, na kipindi hicho Edward Sambo ndio alikuwa anaamka, akashangaa kumkuta Sajenti Minja na pia kuona yule dada akiwa amelala chini,

"Minja vipi?" Edward Sambo aliuliza huku akisogea eneo hilo,

"safi, vipi upo salama?" Sajenti Minja aliuliza,

"nipo salama, mbona umekuja peke yako?" Edward Sambo aliuliza swali ambao Sajenti Minja hakulielewa,

"mbona umeniuliza hivyo?" Sajenti Minja aliuliza na muda huo polisi wengine watano walikuwa wanaingia,

"Kuna kengele ya hatari nimewekewa ukutani na polisi, kwamba chochote kibaya kikitokea niibonyeze hiyo kengele" Edward Sambo aliongea huku akionesha katika eneo ambalo kengele hiyo ipo, na hilo ndio eneo ambalo alisimama sana mpaka akapoteza fahamu kipindi alipovamiwa na BQ,

"sisi ndio tumekuja kwa ajili ya hiyo kengele" Askari mmoja kati ya wale watano, aliongea,

"mbona mmechelewa sana?" Sajenti Minja aliuliza kibabe,

"tulikuwa tunajua huku wapo Askari wengine" Askari alijibu,

"sawa, endeleeni kukariri matukio" Sajenti Minja aliongea huku akimbeba BQ mabegani,

"Mkuu sisi tuna gari, ungetupa tu huyo mtuhumiwa tumpeleke" Askari mmoja aliongea kwa utulivu,

"nyie ndio mmemkamata? mnajua nimeuza roho yangu kiasi gani mpaka huyu dada akawa katika hali?" Sajenti Minja aliuliza huku akiwatazama, lakini wale askari walikuwa kimya, hawakuwa na cha kujibu,

"acheni upumbavu, muwe na akili ya kufikiria" Sajenti Minja aliongea huku akitoka na BQ aliyekuwa amemuweka begani, alitoka nae mpaka nje ambapo kulikuwa na gari walilokuja nalo wale polisi, alimkuta Askari mmoja akiwa amekaa upande wa dereva, Sajenti Minja akazunguka upande wa pili wa mbele na kufungua mlango, kisha akamtupia BQ,

"Mkuu mtuhumiwa hatakiwi kukaa mbele" Askari alizungumza kwa upole, Sajenti Minja hakujibu, alirudi mpaka katika mlango wa dereva,

"toka ndani ya gari" Sajenti Minja aliongea huku akimtazama yule Askari,

"kwanini mkuu? Mimi si ndo dereva niliyekuja na gari hili kumkamata huyu dada muarifu?" Askari alimuuliza Sajenti Minja,

"mmekuja kumkamata ee? mbona mmechelewa? je mngemkuta huyu mzee wa humu ni marehemu tayari?" Sajenti Minja aliuliza,

"isingewezekana, maana kulikuwa na Askari wengine huku" Askari yule alijibu huku akitabasamu,

"bado mnaishi kwa kukariri tu?" Sajenti Minja aliongea huku akifungua mlango na kumvuta nje yule Askari, kisha akaingia ndani ya gari, na kipindi hicho Edward Sambo alikuwa akitoka ndani na Askari wengine ambao walikuwa wakishangaa mambo anayofanya Sajenti Minja,

"hao Askari waliopoteza fahamu wawekeni ndani ya gari" Sajenti Minja aliwaambia Askari,

"wote wamezinduka" Edward Sambo alijibu,

"nitakuja kukuona baadae, ngoja nimfikishe polisi huyu" Sajenti Minja alimwambia Edward Sambo, kisha akawasha gari na kuiondoa na kuwaacha Askari wengine wakimjadili, walihisi wamedhalilishwa.

"Muacheni, huyo ndivyo alivyo, uwa ana maamuzi ya kitata sana" Edward Sambo aliongea huku akirudi ndani na kuwaacha askari nje ya geti.

Sajenti Minja ndani ya gari aliendesha kwa mwendo wa kasi ili kuwahi kumfikisha kituoni BQ, ingawa pia alikuwa na wazo la kumpeleka hospitali, ila alihofia endapo angempeleka hospital na kisha mwanamke huyo akapata fahamu na kutoroka, basi hakuna mtu yoyote ambaye angemuelewa, kwa maana hiyo basi, Sajenti Minja aliona bora amfikishe tu polisi ili wamuone, sasa polisi wenyewe wataamua kama wampeleke hospital au wamuue,

"wao ndio wafanye maamuzi, ila mimi kuua mtuhumiwa siwezi" Sajenti Minja aliongea peke yake na kushika breki ghafla, alifika eneo la darajani na mvua zilikuwa zikinyesha, ikabidi Sajenti Minja apunguze kasi na aendeshe gari kwa umakini sana, kwa maana eneo hilo kukiwa na mvua na giza kama hilo, uwa ni hatari sana.

Sajenti Minja akaweka umakini katika barabara, na muda huo simu yake ilikuwa inaita, akaipuuza, hakutaka kuangalia hata mpigaji ni nani?
Wakati Sajenti Minja akiwa makini namna hiyo, BQ nae alikuwa akifungua macho, fahamu zilikuwa zikimrejea, alifungua macho na kuangalia mazingira aliyopo, akagundua yupo ndani ya gari, tena gari la polisi, alifanya hayo yote kwa umakini mkubwa bila hata kujitingisha. Ila BQ aliona kikwazo ni mkanda wa gari aliokuwa amefungwa, na Sajenti Minja alimfunga makusudi kwa kuwa alikuwa amezimia.

Wakati BQ akiwaza namna ya kumtoka Sajenti, aligundua wapo eneo la darajani, akaona ni eneo zuri sana, ila alihofia kujifungua mkanda kwa maana anaweza kudhibitiwa na Sajenti Minja, kwanza alishakuwa na mashaka kuhusu afya yake na kwa hali aliyonayo hasingeweza kupambana na Sajenti Minja, kingine alichoona ni hatari ni kwamba alihisi jeraha lake la kichwani likivuja damu, ni kweli damu ilikuwa ikitiririka kutoka kichwani na kushukia katika macho.

BQ akafikiria kwa sekunde chache, kisha akatabasamu, alikuwa ameshapata jibu,

"acha nijaribu" BQ aliongea kwa sauti na kumfanya Sajenti Minja ashtuke na kugeuka, hilo lilikuwa kosa, alipigwa ngumi ya shavu, kisha kwa kasi ya hatari BQ akaufungua mkanda wa gari, Sajenti Minja akaona njia nzuri kwa muda ule ni ku-lock milango yote ya gari, akafanya hivyo, kisha akapiga breki za gari, lakini alikuwa amechelewa, maana BQ aliinua miguu yake na kumpiga mateke mengi ya kichwani, Sajenti Minja alijitahidi kuzuia ila alishindwa, kisha BQ alipiga kichwa kioo cha gari, kioo kikapasuka, alafu BQ akajitupa nje ya gari, Sajenti Minja akasimamisha na kutoka huku bastola ikiwa mkononi, ila alichelewa, alikuta BQ akijirusha chini ya daraja na kuangukia katika maji, Sajenti Minja akakimbilia katika zile chuma za daraja na kumuona BQ akipiga mbizi kufuata mkondo wa maji, hapo Sajenti Minja akaona bora apige risasi tu, akalenga na kufyatua risasi nyingi mfululizo, BQ akazama chini ya maji na Sajenti Minja hakumuona tena, akakaza macho kwa dakika kadhaa ila hakumuona, akajishika kichwa huku akijilaumu, kisha akarudi ndani ya gari, na kukumbuka kuwa simu yake ilikuwa ikiita, akaangalia nani alimpigia, akakuta ni mkuu wa polisi, akaiweka simu katika siti ya pembeni, ila simu ikaanza kuita tena, na mpigaji ni yule yule mkuu wa polisi, Sajenti Minja akapokea simu,

"naam mkuu" Sajenti Minja aliongea baada ya kupokea simu,

"hongera sana, nasikia umemkamata yule dada na unakuja nae, tupo kituoni tunakusubiri hapa. Upo maeneo gani?" Mkuu wa polisi aliongea kwa furaha,

"nipo daraja la Dessa" Sajenti Minja alijibu kinyonge,
"sawa, fanya haraka basi, maana mpaka waandishi wa habari wanakusubiri shujaa wetu" Mkuu wa polisi aliongea kwa ucheshi,

"nakuja mkuu" Sajenti Minja alijibu na kisha mkuu wa polisi akakata simu, Sajenti Minja akaitupa simu yake kwa hasira, akawa anajiuliza ataenda kuwaambia nini wakubwa zake? je wataamini kuwa ni kweli yule dada ametoroka? je akiulizwa ni kwanini aliwaacha Askari wengine kwa Edward Sambo na kuondoka peke yake?

Hayo maswali yalianza kumtafuna kichwa Sajenti Minja, akaegemea usukani wa gari, ila alishtuliwa na honi za magari yaliyokuwa nyuma yake, akagundua amesimama katikati ya daraja ambapo ni barabarani, akawasha gari na kuiondoa mpaka mwisho wa daraja na kuisimamisha, bado majibu ya maswali ambayo alihisi ataulizwa, alikuwa hana jibu.

"acha niende, nitapambana uko uko" Sajenti Minja aliongea kisha akawasha gari na kuliondoa kwa mwendo wa kinyonge.

*****************

BQ alipozama wakati Sajenti Minja alipokuwa anapiga risasi, aliibuka baada ya dakika tano, alikuwa akipumua haraka haraka sana, akaendelea kuyakata maji kwa dakika tano nyingine mpaka alipoona Kuna sehemu tulivu kidogo, akaogelea mpaka ukingoni mwa lile bonde na kutoka nje, kwa kuwa ni usiku, hakuweza kulitambua eneo lile haraka haraka, ila lilionekana ni eneo lenye utulivu mkubwa sana, yaani utulivu wake ulitisha, ila BQ aliamua apumzike hapo kwa kuwa alijiamini .

BQ akaanza tena kuhisi kizunguzungu kutokana na kuogelea muda mrefu, pia kuvuja damu katika jeraha lake. BQ akasimama ili aondoke eneo hilo akidhani kuwa huenda akitembea mpaka mbele kidogo anaweza kujua yupo wapi.

BQ alipiga hatua mbili tu, Hali ya kizunguzungu ikaongezeka, akasimama ili apate muda wa kupumzika zaidi, ila alihisi kama kuna hatua za watu zikija kwa mbele yake, akajitahidi kuinua shingo, akawaona watu hao, walikuwa Askari kama wawili hivi, ingawa kulikuwa ni giza na pia BQ alikuwa na hali ya kizunguzungu, ila aliwatambua ni Askari, akili yake ikamwambia afanye kitu, akakusanya nguvu na kutaka kupiga hatua ili akimbie, ila kutokana na hali aliyonayo, na zile nguvu alizikusanya, ubongo ulishindwa kuhimili, akajikuta anapoteza nguvu na kuanguka chini, akajaribu kuinuka ila alishindwa, akajaribu tena, pia akashindwa, akaona hana ujanja, akalala chini chali, ubongo ukawa unalazimisha macho ayafunge, ila mwili ukawa unalazimisha macho yasifunge, na wale watu walikuwa wameshafika, BQ akawaangalia, hakukosea, ni Askari. Macho ya BQ yakakosa nguvu, akayafunga na kisha giza likamtawala.......

**********ITAENDELEA***********

the Legend☆
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom