SEHEMU YA MWISHO PART 3
UPANDE WA PILI
Rensho akawakusanya watu wake akiiacha maiti
ya Queen katika jumba lile, Salome alikuwa
amerejewa na fahamu tayari. Rensho akambeba
Eva ubavuni mwake. Safari ya kukitafuta kitovu
cha Kindo na kuusaka mwili wa Rensho!!! Bila
kusahau kuifukua akili ya raisi wa jamuhuri
ambayo ilikuwa imezikwa katika kaburi la mama
yake waziri mkuu mstaafu.
Utata wa mwisho kabisa ukazuka katika harakati
hizi!!
RAISI wa jamuhuri ya muungano alikutana na
waziri mkuu mstaafu katika chumba cha siri
kabisa cha kijeshi.
Alimkuta akiwa amepewa huduma ya kwanza.
Waziri mkuu mstaafu alitamani kudanganya lakini
alipokumbuka kile kitisho kisichokuwa na
masihara kutoka kwa Rensho alilazimika kusema
ukweli mtupu.
Ukweli ambao raisi aliukataa kata kata akidai
kuwa yule bwana amerukwa na akili tu. Hawezi
kuwa amefanya kitu kama kile, eti aliua wabunge
wanne akamuua na mama yake.??
Hapana!! Raisi alikataa katakata. Alikataa huku
akitabasamu akimaanisha kuwa ule ni mzaha
mkubwa kabisa usiotakiwa kutiliwa maanani
kabisa.
“Lakini mkewe anadai kuwa amemuona kwa jicho
lake akiwa uchi?”
“Hapana usikae kuamini maneno ya wanawake
na wewe….hakuna kitu kama hicho….mambo ya
wanawake. Wanafiki wanaota ndoto usiku
wanasema waliona kitu na wanabisha hao.
Wanawake we huwajui wewe, nilikwambia uoe
ona sasa…hujui lolote kuhusu wanawake IGP”
Raisi alizungumza maneno mengi huku akizidi
kuegemea upande wa Waziri mstaafu.
“Hapana mkuu, nimeyafanya hayo yote na mke
wangu ni shahidi wa kweli kabisa, naiomba
serikali yako inihukumu.” Waziri alimsihi raisi wa
jamuhuri.
Kisha IGP naye akakazia.
“Haya mkewe alikuwa anaota, vipi kuhusu maiti
iliyokutwa ndani ya kile chumba mheshimiwa?”
“Waliiweka mahanithi waliomjeruhi, tena hili
jambo nitalisimamia ipasavyo hivi vyama pinzani
vinataka kutudhoofisha kiasi hiki. Na chanzo ni
kwamba anataka kuwania uraisi..shenzi kabisa.
siwezi kuyafumbia macho, kuna vyama
vinatakiwa kufutiwa usajili kabisa, nadhani
unaelewa ninachosema” Raisi alizidi kuwaka.
Kwa asilimia mia akiwa anamtetea waziri
mstaafu.
Siasa bwana!! IGP alijiwazia huku akitazama jinsi
gani waziri mstaafu alikuwa katika hatia ya
waziwazi.
“Waliohusika na tukio hili wanatakiwa wafikishwe
mbele ya sheria mara moja!!” alitoa amri, amiri
jeshi mkuu wa Tanzania.
IGP akatii!!
*****
RENSHO alimruhusu Eva, Anitha na Salome
kuondoka kuelekea nyumbani huku yeye, Kindo
na Getonga wakibaki kwa ajili ya zoezi la mwisho
kabisa.
“Nilisikia unasema kuwa wana kitovu changu,
mbona sielewi?” Kindo alimuuliza Rensho wakiwa
wametulia eneo fulani nje kidogo ya jiji wakisubiri
kigiza kiingine waweze kufukua makaburi mawili.
“Unapozaliwa kitovu kinakuwa kimeungana na
mama. Hivyo lazima kikatwe nd’o unabaki na
hicho kidogo. Basi kilipokatwa kile kitovu huyo
mzee Nshomile alikichukua, lengo lake likiwa
moja tu. Kukutengeneza na kisha kukutumia
katika shughuli zao. Hivyo walitulia kwa muda
mrefu wakiyafanya maisha yako kama yao,
hukuwa na akili darasani Kindo, maisha yako na
ya wazazi wako yamekuwa magumu tu..mwisho
wakaamua wakutumie wewe kunitoa mimi….yaani
kuirudisha tena roho yangu. Wakakuongoza
kufanya mapenzi na Salome kisha kumpa mimba
isiyokuwa mimba. Mimba ya kichawi…. Nia yao
ile mimba kabla haijakomaa waitoe kishirikina na
kisha kuniunganisha na yale mabonge ya damu
nizaliwe upya. Nilitakiwa kupewa cheo.
Waliowaagiza kumuua Salome wakafanya makosa
kwa kumbaka yule binti, na hapa nd’o siku ile
ambayo unakumbuka damu ilianza kuvuja
chumbani nikiwa pamoja na wewe…unakumbuka
?” alimuuliza, Kindo akaikumbuka hiyo siku.
“Basi nd’o mambo yalipowaharibikia hapo na
walikufa wengi, nilibahatika kubaki hai kutoka
katika tukio lile kwa sababu moja tu, sikuwa na
mwili wala roho. Sasa ningekufaje
unadhani….mwili ulizikwa miaka mingi iliyopita na
roho ilikuwa katika mwili wa salome kama mimba
ya ajabu. Hivyo wewe ulikuwa wa muhimu
sana…… wakakutia hofu maradufu. Wauaji wale
wakaishika akili yako ili usiweze kutoa ushahidi
wowote ule juu yao. Mshukuru Mungu wako kuwa
upo hai hadi sasa.” Alimaliza Rensho.
“Na wewe unataka kujua juu ya kitambulisho….h
akina maana tena kile kitambulisho. Nina roho
yangu tayari, kile kitambulisho kilikuwa kwa
sababu moja tu….iwapo mambo yakiwa magumu
kabisa niende kujisalimisha kwa mkuu wetu,
lakini sasa sitajisalimisha bali nitamuangamiza na
popote anaponisikia anajua kuwa nitamuua tu….”
Alisema kwa hasira.
Walizungumza mengi, wakapata chakula na
hatimaye kigiza kikaingia.
Rensho akawashika mikono na kisha wakatoweka
na kutokezea makaburini.
Kindo na Getonga walikuwa wanatetemeka
haswa kujikuta makaburini wakati ule.
“Alikuwa anaitwa Magreth Hossana, tafuta kaburi
lenye jina hilo haraka.” Rensho aliamrisha. Kwa
kihoro Kindo na Getonga wakaanza kuangaza
huku na kule wakilitafuta jina katika makaburi.
“Huyu hapaa…..” Rensho ambaye pia alikuwa
akilitafuta lile kaburi aliwapigia wenzake kelele.
“Hapo hapo mlipo simama kama mlivyo mikono
juu” sauti nzito ya kiume iliamrisha.
Kindo na Getonga wakasimama huku
wakitetemeka. Kutahamaki walikuwa
wamezingirwa mbele ya nyuma na kundi la
wanaume wakiwa wamebeba bunduki mikononi
mwao.
“Nyie ni akina nani?” jamaa mmoja mwenye
ndevu nyingi aliuliza.
Kabla hawajajibu lolote sauti ya Rensho ikasikika.
“Nipo nao kwani vipi?” alitokeza akiwa katika vazi
lake lilelile jepesi kabisa.
“Mnafanya nini hapa wakati huu?”
“Kwani nyinyi mnafanya nini hapa?” na yeye
aliwauliza kwa jeuri. Kisha akaongezea, “Halafu
hamjisikii vibaya wanaume wazima tena sita sijui
mmetushikia bunduki watu tusiokuwa na silaha
na hatuna neno baya na ninyi?” aliwachokonoa
maksudi.
“Kaa kimya mwanamke…tutapasua vichwa vyenu
sasa hivi mkileta dharau wachawi wakubwa
nyie….” Alifoka jamaa mwingine mwenye kipara.
“Ok! Kwani mnataka nini labda…”
“Tunataka kujua nyie ni akina nani?”
“Wachawi tumekuja kuwaroga hizo Bunduki zenu
zigeuke nyoka ikibidi……” Rensho alijibu kwa jeuri
huku akitoa tabasamu hafifu.
Jamaa mwenye kipara akataka kumvamia
Rensho, hapohapo akaifungua mikono yake na
kisha kuifunga.
Mayowe yakatanda pale wale majingili walijikuta
wakiwa wameshikilia nyoka mikononi mwao.
Walipiga mayowe huku kila mmoja akitupa chini
kitu ambacho hapo awali kilikuwa ni bunduki.
“Kuja hapa?” aliamuru walipokuwa wanakimbia.
Wakatii na kurejea huku kila mmoja akipigwa
butwaa tena. Zilikuwa ni bunduki.
Wakaziokota kwa uoga…..
“Sasa mtafanya kazi ndogo tu kisha mtaondoka…
mnifuate haraka” akaamuru wakamfuata.
Wakalifikia kaburi la mama yake waziri mkuu
mstaafu….
“Mtafukua na kutoa jeneza…” alitoa maelezo
mafupi.
“Haraka!!” akaamuru. Wanaume waogopa kufa
wakabaki kushangaa ni kwa namna gani
watafukua kaburi lililojengewa.
“Mnaduwaa….wapuuzi sana nyie…haya nalitoa
jeneza huko chini nikilitoa mmojawenu analifunua
na kutoa hirizi nyekundu katika mwili wa
marehemu.
Rensho hakuwapa nafasi ya kufikiri.
Kindo alikuwa amejikojolea tayari baada ya dada
yule wa ajabu kubadili bunduki kuwa nyoka.
Getonga yeye alikuwa akitokwa jasho kwa fujo.
Haikuwa sinema kweli jeneza likatoka na kuwa
hewani, jambazi mwenye kipara akalivaa jeneza
akafunua. Akaingiza mkono katika mifupa
iliyosalia akatoka na hirizi.
“Wewe ni baba lao….” Rensho akamsifia huku
akiichukua ile hirizi na kisha akaifungua, upepo
ukavuma kidogo, jeneza likatoweka na hirizi nayo
ikatoweka.
“Uwe huru raisi wa watu wema…..” Rensho
akasema hakuna aliyemuelewa moja kwa moja.
“Mnaweza kwenda majambazi nawatakia kazi
njema!” aliwaaga kiutani….
WAKATI HUOHUO!!
Raisi wa jamuhuri ya muungano alikurupuka
kutoka kitandani, akili yake ambayo ilikuwa
ngumu sana kukubali kuwa Waziri mstaafu si mtu
mzuri ilikuwa imefunguka akajiona mjinga sana.
Akampigia simu IGP na kumweleza kuwa waziri
mstaafu hastahili huduma wala uangalizi wowote
ule wa kiafya.
Na sheria ichukue mkondo wake!! Akaagiza.
Walau IGP aliweza kutabasamu.
Akili ya Raisi ilikuwa imefunguka hatimaye.
*****
Makaburi ya CITY katika wilaya ya Temeke,
jeneza la mtoto mdogo lilikuwa juu tayari. Rensho
alilifunua lile jeneza huku machozi yakimtiririka.
“Baba kumzika mwana, kiunafiki kalia
Kaujaza umati sana, mama yangu kazimia
Baba asiye maana, kaidanganya dunia.
Narudi kuangamiza, huruma ka mbali nami.
Waziri si muungwana, ushirikina watumia.
Ikulu wataka sana, bila huruma waua.
Yote sasa ni bayana, wafungwe miaka mia.
Narudi kuangamiza, huruma kaa mbali nami.
Rensho amka tena, Myaka kumi karibia.
U hai si mfu tena, najua unasikia.
Watu hawana maana, ukiwaona kimbia
Narudi kuangamiza, huruma kaa mbali nami.
Rensho aliimba lile shairi huku akibubujikwa na
machozi. Kisha akaingiza mkono wake na kutoka
na hirizi nyeusi. Akaifungua na kuitupa kwa
Kindo. Kindo akajirusha nyuma huku akipiga
kelele.
“Kitovu chako hicho unakikimbia tena….”
Alishangaa Rensho kisha akaingiza tena mkono
katika lile jeneza.
Akatulia kwa muda mrefu kisha akaliachia jeneza
likaanguka mle kaburini.
“Getonga!” alimuita huku akiwa ameinama
bado……Getonga akasogea kwa Rensho.
“Nifungue hirizi kiunoni mwangu…..” alimweleza,
Getonga ambaye uoga ulikuwa umepungua
alimfunua Rensho na kutoka na hirizi kubwa.
“Itupe kaburini, usiniulize niliivaa saa ngapi?”
Getonga akaitupa….
“MWISHO” alisema huku akitabasamu.
“Sasa ninalo joto la kike nina kila kitu cha kuitwa
mwanadamu na sina ulinzi tena wa kishetani.”
Alizungumza huku dhahiri akionekana kuwa na
furaha kubwa.
“Tunalala kwa nani leo..wengine nd’o tunaingia
kuyaanza maisha sasa…..vipi huku duniani
lakini?” aliuliza Rensho huku wakiifuata njia na
kutoka katika makaburi yale.
Getonga akashauri waende nyumbani kwake kwa
sababu sio mbali sana. Wakatembea kwa miguu
kufuata barabara. Kila kitu ambacho Rensho
alikuwa kikiona laikuwa anauliza ni kitu gani.
Kindo na Getonga wakafanya shughuli pevu ya
kumjibu kila swali.
Hakika Rensho alikuwa mpya katika dunia!
Walifika nyumbani kwa Getonga, hawakumkuta
Anitha lakini Salome alikuwepo nje ya nyuma.
Salome akamkimbilia Kindo na kumkumbatia.
“Anitha yupo wapi?”
“Ameenda kwao”
“Na wewe mbona upo hapa nje!!” Getonga
akahoji.
“Mwenyekiti anadai kuwa nyumba hii imefungwa
na serikali…”
“Yupo wapi mjumbe?” aliuliza, Salome
akanyoosha kwa kidole. Getonga akaelekea
nyumbani kwa mjumbe, wakasalimiana kwa
bashasha kubwa huku mjumbe akishangaa jinsi
Getonga alivyokuwa amechafuka.
“Ni simulizi ndefu?” alimjibu.
“Polisi wanakutafuta lakini?”
“Ukweli upo wazi usijali kila kitu kitaenda sawa
naomba unihifadhie hawa wageni wangu. Kwa
usiku wa leo tu, naamini kuwa kesho nyumba
yangu itafunguliwa na maisha yataendelea…”
alimweleza kwa kifupi. Mjumbe akakubali kutoa
msaada huo.
******
KIHITIMISHO!!!
SIKU iliyofuata mambo yalikuwa motomoto,
magazeti yalilipuka kwa habari juu ya waziri
mkuu mstaafu na maamuzi ya raisi juu yake.
Dar es salaam palikuwa na hekaheka, yule
mwandishi aliyetoroka mahabusu kimiujiza
alikuwa mtaani, na yule mshtakiwa mwenza
aliyetoroka pamoja naye alikuwa amepatikana..
Mwanadada anayesadikika kuchuna ngozi za
wanaume wawili alikuwa jijini Dar es salaam.
Mwanadada wa kuitwa Rensho huyu nd’o alitikisa
jiji zaidi. Kila mtu alitaka kujua Rensho ni kimbe
gani hadi akawa anatokea katika miili ya watu
wakifa baada ya kuvuja damu kwa muda mrefu.
Inspekta aliyerukwa akili alikuwa timamu kabisa
akizisikia habari hizi katika redio.
Wanawake waliokuwa wakivuja damu nao
zilikuwa zimekoma kabisa.
Kwa kifupi kila mkazi wa Dar alikuwa na jambo la
kuzungumza.
Maofisini kazi zilikuwa haziendi kila mmoja
alitaka kujua nini hatma ya haya yote.
Mahakama ya hakimu mkazi kisutu, waziri
mstaafu na mzee Nshomile walikiri makosa yao
bila kupinga. Walikubali kuwa nyuma ya majanga
yote yaliyotokea.
BAADA ya siku kadhaa hukumu ya kunyongwa
hadi kufa ilikuwa halali yao.
Rensho na wenzake wakiachwa huru kabisa.
Anitha alirejea kwenye ndoa yake baada ya
wazazi wake kumsihi sana asidai talaka kwani
mumewe alikuwa kazini nd’o maana akajikuta
akiingia katika mkasa huo na hata kama hiyo
haitoshi kwa ushahidi wake mwenyewe ni kwa
kiasi kikubwa alijaribu kuipigania familia yake.
Salome na Kindo wakarejea kuwa wamoja huku
Rensho akiyaanza maisha yake kwa kuishi
nyumbani kwao Getonga.
JIONI moja katika fukwe za coco maeneo flani
nje kidogo ya jiji.
Kindo, Salome, Rensho, Anitha, Getonga na Eva
walikuwa wameamua kukutana kwa ajili ya
kusimuliana mawili matatu. Kila mmoja alisema
lake juu ya mkasa walioupitia.
Getonga ambaye alikuwa amekaa kimya muda
mrefu aliongea wa mwisho.
“Katika mikasa yote niliyowahi kupitia sijawahi
kupitia mkasa wenye kutia HOFU kama huu,
yaani kila nilipogusa ilikuwa ni hofu
tupu….nadhani hata nikiwaandikia makala
wasomaji na wao wataingiwa na hofu wakiwa
wanaisoma… kwa kifupi huu mkasa nitauita
HOFU”
“Amakweli HOFU” Salome alijazia na wengine
wote wakakubali kuwa ule mkasa ulijaa HOFU.
“Ila yote juu ya yote ashukuriwe Mungu maana
maisha yanaendelea!” Anitha alimalizia huku
akimuegemea Getonga begani kimahaba.
“Baba HOFU nd’o nini?” Eva naye akauliza kitoto
toto.
Kila mmoja akacheka kwa sauti ya juu.
Sauti zao za furaha zikamtoa katika hofu
mwandishi wa simulizi hii na kuamua kuitua
kalamu yake chini na kulifunika daftari ambalo
nyuma kabisa liliandikwa neno moja tu…….
“MWISHO”
NB: Tangu riwaya hii iandikwe mwaka 2013
haijawahi kufanyiwa uhakiki.... kumradhi kwa
makosa yoyote yaliyojitokeza.....