KISA CHA 16
LICHA ya kuwa amepokea kipigo kikubwa sana ambacho kilikuwa ni sawa na kuua nyoka, bado John Masele alikataa kata kata kuwa hajawahi kukutana na mwandishi wa habari aitwaye Sam na wala hajui chochote kuhusiana na BvB.
Alipinga licha ya ukweli kuwa waliwahi kukutana na akazungumza naye na kumpatia nyaraka tata.
Masele alipinga kwa sababu alijua hata akisema bado mabaradhuli wale watamuua tu na kisha kumwahi Sam kabla hajatumia zile nyaraka kuwavumbua waovu. Ilikuwa heri afe lakini akiacha harakati zikiendelea nyuma yake.
Kitendo cha mzee Matata kuleta kiburi kilimkera sana raisi. Akaona kuwa ile ni dharau ya hali ya juu, alitambua kuwa anaweza kumpiga risasi na kumuua mara moja, lakini kwake yeye furaha isingekamilika. Badala yake akawasiliana na BvB na kumwomba huduma ya vijana wake kadhaa wanaojua nini maana ya kuua mwanadamu yeyote kwa mateso makali. Akamsihi tena kuwa hakuhitaji afe upesi, alihitaji afe kwa hatua. Ikiwezekana hata ndani ya siku kumi za mateso nd’o aruhusiwe kufa.
____
Raia wa kizungu wanne walipokelewa uwanja wa ndege wa kimataifa wea mwalimu Nyerere. Ugeni huu ulipokelewa na wafanyakazi kutoka ikulu, hivyo baada tu ya kuwasili walipelekwa hoteli ambayo ilikuwa imelipiwa kwa ajili yao.
Waliwasili majira ya saa nne asubuhi!
Muda uleule walipelekwa hotelini na hawakutoka tena hadi ilipotimu saa tisa usiku.
Kazi iliyowaleta kutoka huko walipotoka ni moja tu, kumbana John Masele ili aweze kusema iwapo aliwahi kukutana na Sam ama la!
Na ajieleze zaidi iwapo walikutana ni kitu gani alimpatia!
Hawa wazungu kutoka uholanzi waliaminika kwa kazi yao ya kuadabisha mateka wao. Walikuwa na roho mbaya sana zisizokuwa na huruma hata kidogo. Kuua kwao ilikuwa kama kichekesho tu, ni wazungu hawa ambao mzee Matata alikuwa na video zao na alimuwekea Tina ili kumtisha siku ile. Walikuwa wanatesa na kuua vibaya mno.
Wakiongozwa na dereva waliyekabidhiwa wakiwa kimya kabisa huku wakipuliza sigara kila mmoja. Hatimaye walifika magomeni.
Nyumba ambayo John Masele alikuwa amehifadhiwa.
Walifika na kubisha hodi lakini mfunguaji alichelewa. Wakabisha tena na hapo akafika na kuwafungulia geti haikuwa mara yao ya kwanza kufika katika ngome kadha wa kadha za namna ile.
Wakapita moja kwa moja hadi ndani, dereva akabaki nje na baada ya wao kuingia ndani na yeye akatoweka kwenda mahali alipopajua yeye kwa sababu tayari aliambiwa kuwa hawatatoka mapema. Na wanaweza wasitoke humo ndani kwa siku hiyohiyo. Hakujua hata walichokuwa wakikifuata mle ndani wanne wale.
Walipoingia ndani wakaenda moja kwa moja katika ule ukuta wakataka kupenya lakini wakashtushwa na utofauti wa maelezo waliyopewa awali juu ya mazingira ambayo yapo eneo lile.
Mzungu mmoja akatoa simu yake na kisha kutoka nje ili aweze kupiga.
Alipotoka nje akaenda kwa mlinzi ili aweze kuzungumza kwa lugha ya Kiswahili na wale mabwana wahusika wa ile ngome.
“Hey! Do you speak English?” mzungu akamuuliza mlinzi.
Yule mlinzi akajibu kuwa anaweza.
Yule bwana akabofya namba kadhaa na kutaka kumpatia yule mlinzi simu. Mlinzi akanyoosha mkono wake kuipokea ile simu. Lakini hakuchukua simu pekee.
Akaufyetua ule mkono wa mzungu na kuuvunja huku mkono wake mwingine ukiuziba mdomo wa yule bwana. Kisha akamvutia nyuma ya nyumba.
Akaitoa kofia yake na kuanza kumuhoji yule bwana kwa kiingereza.
“Who the *** are you?” ilikuwa sauti ya Gama iliyo katika ghadhabu kuu.
Yule bwana hakujibu, Gama hakupoteza muda kuzungumza na bubu. Akatoa pigo kali la kareti katika mbavu za yule bwana, hata sauti hakuweza kutoa alibaki kugumia kwa maumivu.
“Who are you bastard!” akamuuliza tena huku akimwonyesha wazi kuwa anataka kutoa pigo jingine.
Mwanga hafifu wa taa ulimmulika mzungu yule ambaye alikuwa mwekundu huku sura ikiwa imemvimba.
“BvB” akatokwa na kauli ile. Kisha akatulia kimya!
Ni aidha alikuwa amepoteza fahamu ama kifo kabisa.
Upesi Gama akaondoka na kuelekea katika kile chumba ambacho walikuwa wamesalia wazungu watatu wakingoja maelekezo zaidi.
“Me, you zea” alizuga kuzungumza kiingereza kibovu Gama, hapa akiwa amevaa tena kofia yake na kufanana na mlinzi.
Mzungu mmoja akatoa kauli kuamriosha mmoja wao aende kutazama mwenzao anasema nini.
Naam! Ramani ya Gama ikaenda kama alivyokuwa anahitaji.
Akamwongoza hadi nje, na kumpeleka nyuma ya nyumba. Akafika na kumwonyesha mwili wa mwenzake.
Hakumpa muda wa kushtuka sana, akamvamia kwa kiwiko akaivunja pua yake.
Mzungu akataharuki na akataka kupiga kelele lakini alichelewa, Gama alifyatua kisu alichokuwanacho kikajikita katika shingo ya yule kaburu.
Kisu kilikuwa na sumu kali. Gama hakugeuka nyuma tena kutazama jinsi atakavyokata roho.
Sasa hakuvaa kofia bali aliingia tena moja kwa moja katika kile chumba.
“You bastard where are you from and who the hell is BvB” aliwauliza huku akiwa anawakabili machoni.
Wakamtazama kwa jicho la hofu wasijue ni kitu gani kinaendelea.
Mmoja akajaribu kumsogelea lakini hakufika mbali ukasikika mlio wa bunduki, alipogeuka alimshuhudia mwenzake akiangukia kichwa huku kisogo kikiwa kinavuja damu.
“Kombolela mzungu..” Sauti ikasikika kisha tena bunduki ikakohoa na kuvunja miguu ya yule bwana aliyebakia.
Na hapo John Masele akajitokeza huku akiwa anajivuta kwa magoti na tabasamu tele mdomoni mwake.
Mchezo walioupanga ukawa umekamilika!
Gama alikuwa amemshirikisha John Masele juu ya kombolela, na pale walikuwa wakilicheza.
“Utajibu maswali yote kwa hiari ama kwa lazima ikibidi?” Gama akamuanza yule mzungu pekee aliyebaki akiwa hai.
Yule mzungu hakujibu kitu Gama. Akatoka nje kisha baada ya dakika zipatazo kumi akarejea tena, mikono yake ikiwa imetapakaa damu na mkononi akiwa na vichwa viwili vya wazungu. Akavirusha mbele ya yule mzungu mbishi.
Hakika alipagawa!
“Do you love hell??” Gama akamuhoji. Na hapo hapo akanyanyua vidole vyake juu, kisha akavishusha katika kichwa kimojawapo katika pigo la ‘finga’ na hapo akachomoka na macho kutoka katika kile kichwa. Akayarusha mbele ya yule mzungu.
“I will chop your eyes while you are alive” akamkoromea huku akimsogelea. Kitete kikamkumbuka yule mzungu.
Mzungu akajibu kila alichoulizwa huku akiwasihi wasimuue kwa sababu yeye ni mjumbe tu.
Akamtaja BvB kuwa ndiye bosi wao na siku iliyokuwa inafuata alitarajiwa kuanza safari ya kuja nchini Tanzania kufuatilia maendeleo ya miradi yake na kubwa zaidi kuitazama ardhi kubwa yenye madini ambayo alipewa zawadi na raisi wa Tanzania kutokana na ukaribu wa kimisaada aliokuwa akimpatia.
Yule mzungu hakusubiri kuambiwa aseme nini maana ya BvB aliitafsiri mwenyewe na kisha akamtaja mzee Matata kama kijakazi wa BvB nchini Tanzania.
Gama alivyotaka kuujua muonekano wa BvB, mzungu yule aliapa kuwa hajawahi kumtia machoni bwana yule hata siku moja katika maisha yake.
“Imelaaniwa ardhi hii” John Masele alijisemea baada ya maelezo ya yule mzungu.
Gama akamkonyeza kwa jicho la kuume. Akatambua nini kinamaanishwa.
Na hapo akafyatua risasi, yule mzungu akabweka na kupoteza uhai. Gama akamchukua John Masele katika mgongo wake kisha akatoka naye nje kwa tahadhari kubwa.
Akampita yule mlinzi mlevi na kutokomea gizani zaidi!
_____
WAKATI Gama Yakubu akihangaika kupenya katika njia ambazo ni salama kwake pasipo kuonekana. Mama lao alikuwa akiichochea moto zaidi ile gari aina ya Noah ambayo aliichukua nyumbani kwa waziri usiku ule.
Wale mateka ambayo walikuwa wanaelekea kuwa huru walikuwa katika maombi mazito kila mmoja akimshukuru Mungu kwa namna yake ya kipekee. Lakini Lili alikuwa mtu wa kulia tu.
Mama lao akiwa ndani ya pensi aliendesha gari kuitafuta Kibaha kama ambavyo walikuwa wamekubaliana na Yakubu ambaye alibaki nyuma kwa ajili ya kuimalizia kombolera yake.
Mitaa ya Kimara na ubungo bado ilikuwa imechangamka changamka licha ya kuwa ulikuwa usiku mnene. Hapo alipita bila wasiwasi wowote.
Lakini shughuli ikawa pevu walipofika mlima wa kibamba kuelekea Kibaha.
Gari ya akina mama lao ilisimamishwa katika namna ya kipekee.
Mawe yalikuwa yamepangwa barabarani!
Watekaji! Mama lao alisema kwa sauti ya kuhamanika, na hapo kila mateka akazidisha maombi yake.
Mama lao alijua kwa namna yoyote ile hawezi kuvuka kikwazo kile na ilikuwa lazima asimame. Aliwaona watekaji wake wakiwa na mapanga na marungu.
Akapunguza mwendo na kusimama!!
Watekaji wakasogea hadi pale garini.
“Mwanamke… tunakupa dakika moja na sekunde mbili.. uwe chini na wote waliomo humu wawe chini na kisha mpotee mbele ya macho yetu… ubakishe funguo pekee humo ndani.” Amri ilitoka.
Mama lao akawageukia mateka wake akatazama namna wanavyomtazama kwa jicho la huruma na wengine wakiwa wamekata tamaa.
“Mnaijua kombolera…. Lili umewahi kucheza kombolera?” aliwauliza na kisha akamgeukia Lilian.
Lili akatikisa kichwa kumaanisha kuwa amewahi kucheza.
“Ili umuokoe mwenzako unatakiwa kufanyaje?”
“Mbona sikuelewi mama…..” alilalamika Lili.
“Sijakuuliza kama unanielewa jibu swali binti…”
“Unabutua….”
“Vizuri sana… unabutua…” mama lao akarudia jibu lile huku anacheka. Kisha akawaambia wasishuke garini anaenda kubutua.
Wakati mama lao anashuka kutoka garini alikuwa anajiona kama yu katika tukio ambalo aliwahi kuwa awali. Lakini tofauti ilikuwa moja tu tukio la awali lilitokea jijini Mwanza, ambapo katika utafutaji wake akiwa bado anatawaliwa na ujana aliangukia katika penzi la kijana mwenye pesa. Naam! Tangu akiwa mdogo alikuwa akitamani kuolewa na mtu mwenye pesa akidhani zile pesa hujileta zenyewe.
Baadaye kabisa penzi likiwa limekolea akajitambua kuwa amezama katika penzi la jambazi aliyekubuhu na hawezi kutoka tena.
Akakubaliana na hali, akafundishwa kushika bunduki na kuitumia, akafundishwa kuwa na roho mbaya inapobidi, akafundishwa kurusha mateke na kupiga ngumi!
Naam! Mama lao akawa mtu mwingine, na hatimaye akaanza kuandamana na mpenzi wake kwenda kuteka magari.
Wao walikuwa wakifanikiwa sana kutokana na mbinu walizokuwa wakizitumia, hii mbinu ya kuweka mawe barabarani mpenzi wake yule ambaye baadaye aliuwawa kwa risasi aliziita mbinu za kishamba. Na aliwahi kumweleza mama lao kwanini mbinu zile ni za kishamba na mama lao akazielewa.
Sasa mama lao naye ametekwa katika mbinu za kishamba hayupo pamoja na marehemu mpenzi wake sasa yu mwenyewe, kwanini asicheke, kwanini asitabasamu wakati anatambua kuwa washamba nd’o wanaojaribu kumteka.
Dhumuni kuu la mama lao kushuka chini peke yake ilikuwa ni kuhakikisha iwapo walimteka wana silaha ama vipi.
Macho yake makali yakapenya katika giza lile jepesi, kwa mbali akamuona mtu mwingine amesimama huku akivuta sigara, hakutazama mara mbili akawa katika marudio akatambua kuwa yule aliyesimama mbali ndiye ambaye huwa anakuwa na bunduki. Na mara zote ndiye huwa kiongozi wa msafara, mama lao akauchuna kama hajamuona lakini kichwani akikiri kuwa marehemu Swebe mpenzi wake alikuwa anajua mambo mengi sana.
Hapa akawa anaishi katika dunia mbili tofauti, kichwani alikuwa makini kuwatazama adui zake lakini kwa nje alionyesha ule uoga wa kike. Akawalaghai wale ‘washamba’ kuwa yeye ni mwanamke wa kawaida.
Wakawa wanamkemea huku wakicheka, walidhani ni mwanamke kweli.
Wakiwa bado wanamdharau mama yule aliyekuwa akiwaomba msamaha. Mara likatokea tukio ambalo huenda watasimulia kwa vizazi vyao vya majambazi ‘washamba’.
Kwa kushtukiza kabisa kama ilivyo katika filamu za mapigano kwa kutumia silaha. Mama lao akaangukia magoti kama anayeomba msamaha, upesi mkono wake mmoja ukaingia kiunoni, na sekunde iliyofuata akawa na bastola mkononi, akafyatua moja kwa moja kumwelekea yule aliye mbali akampata kifuani. Jamaa akarushwa mbali, mama lao hakutaka kujiuliza iwapo amekufa ama la.
Sekunde inayofuata bastola yake ikawa inawatazama wawili wale. Sas ikawa zamu yake kutabasamu na wale jamaa kuanza kubabaika.
“Wee! Thubutu kukimbia na uwe umekimbia milele mbwa nyie…” akawapia mkwara. Kisha akatoa amri upesi.
“Mnayatoa haya mawe kwanza ndani ya dakika moja na sekunde mbili kisha mnapotea machoni kwangu mara moja!! Upesi.”
Mara moja wawili wale wakaanza kuyaondoa mawe kama walivyoamrishwa, huku wakitetemeka. Ndani ya gari Lili ambaye muda wote alikuwa anachungulia kinachoendelea, akajikuta kwa mara ya kwanza akitabasamu.
Barabara ilivyokuwa safi. Mama lao akawatazama wawili wale ambao waliogopa kuondoka bila kuruhusiwa. Kisha akawarushia neno lililowashangaza.
“Kombolela majambazi!”
Akaruka garini na kuitia moto gari. Safari ikaendelea kwa amani kana kwamba hakuna kilichotokea!
Kila mmoja garini alibaki kujiuliza juu ya yule mwanamama.
Hawakupata majibu!!
****
ASUBUHI SANA eneo la magomeni lilijaa umati wa watu, kila mmoja alikuwa akiongea neno ajualo yeye juu ya kile alichokuwa akikiona.
Vichwa vinne vya wazungu vilikuwa nje ya geti la nyumba iliyosadikika kuwa ni ya mheshimiwa waziri wa nishati na madini.
Simu zilipigwa kituo cha polisi cha Usalama magomeni, na punde askari walifika na kujawa na mshangao juu ya jambo lile.
Simu za upepo zikafika makao makuu, na hatimaye mezani kwa Robert Masawe.
Alipigiwa simu na IGP kuelezwa kuhusiana na tukio lile la kutisha tena katika nyumba ya waziri.
Robert Masawe alitamani amweleze IGP juu ya uozo unaoendelea chinichini maana alimuona ni mtu anayetumikia kitu asichokijua. Lakini hakuwa radhi kujaribu kumweleza badala yake alichukua ile taarifa kama taarifa nyingine kisha aingie katika utendaji.
Wakati anakata simu alisimama akapiga saluti huku akiwa peke yake.
Kisha akajisemea “Umelaaniwa mkono wa GAMA….”
Kisha akafanya tabasamu hafifu la matumaini.
WAKATI tukio hili likiendelea, hali ya waziri wa nishati na madini, bwana Mathias Obhare ilikuwa mbaya sana, shinikizo la damu lilikuwa limepanda. Alikuwa amechanganyikiwa kabisa na hakujua ni nani aliyepenya na kuingia katika ngome ile na kufanya yale yote aliyoyafanya.
Taarifa ya maaskari ilitaja kukutwa pia miili ya waafrika wawili ikiwa haina uhai na mbwa aliyepigwa risasi pia akiwa hana uhai.
Si waziri peke yake aliyekuwa amepagawa bali raisi wa nchi alikuwa hajielewi kabisa. Alipiga simu uholanzi kutaka msaada lakini bahati mbaya simu ya Benson van Bronchost haikuwa ikipatikana.
Alisahau kabisa kuwa bwana yule alikuwa safarini kuja Tanzania.
Waandishi wa habari wakaanza kuandika mambo wanayohisi bila kuwa na uhakika nayo.
Wakaandika waziri ameua, wakaandika waziri anajihusisha na umafia na mengineyo mengi huku wengine wakienda mbali zaidi na kutaja kuwa ni vita ya kuelekea ikulu inaondoka na damu za watu.
Tamko la mkuu wa majeshi ya polisi likasubiriwa.
Na hilo lilikuja baada ya siku moja!
Akiwa ameagizwa na raisi kusema hivyo, IGP akazungumza nje kabisa ya utashi wake. Mmoja kati ya watu waliokuwa katika mkutano ule japokuwa kwa siri kubwa alikuwepo Sam ambaye alitoka katika maficho yake baada ya kusikia habari juu ya wazungu wanne na waafrika wawili kuuwawa katika nyumba ya waziri.
“Aliyekuwa waziri wa mambo ya ndani na nje ya nchi, bwana John Masele aliyekamatwa na silaha za moto, ametoroka mikononi mwa polisi wakati akihamishwa gereza la mahabusu. Serikali inamshuku kuhusika na mauaji yaliyotokea katika nyumba ya waziri Obhare. Msako mkali unaendelea dhidi yake.”
Taarifa ile ilipokewa kwa namna tofauti tofauti na waandishi wa habari. Wengi walinung’unika kuwa ilifanana na taarifa ya kupikwa lakini IGP hakujibu swali lolote lile.
Huo haukuwa mwisho wa utata!!
Sam akatabasamu huku akiitazama picha zilizokuwa mkononi mwake akazifananisha na vile vichwa vilivyopigwa picha na kuwekwa magazetini. Picha zilifanana kabisa na zile alizopewa kule kijijini na John Masele ambaye sasa anashutumiwa kuwa ni muuaji.
“Wajinga ndio waliwao… siku zenu zinahesabika!” Sam akasema kwa sauti ya chini huku akiondoka zake.
___