Riwaya: Dili la dola bilioni nne

Riwaya: Dili la dola bilioni nne

NYEMO CHILONGANI
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Kumi na Mbili.

Hakukuwa na muda wa kukaa Mombasa na ndiyo maana Robinson na Robert waliondoka na kuelekea jijini Nairobi. Walikuwa na pesa hivyo walifanya kila liwezekanalo kupata ukumbi mdogo ambao waliifanya kama sehemu yao ambayo wangekuwa wanafanya mahojiano na watu mbalimbali nchini humo.
Walitengeneza logo kubwa ya Wazalendo TV na kuibandika ukutani, walitaka kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha wanafanikiwa kupata pesa kutoka kwa watu waliopanga kuwafanyia umafia na ndio maana hawakuona hatari kutumia pesa.
Humo, wakaweka kamera ndogo za CCTV zilizokuwa katika kila pembe ya chumba hicho kwa juu, hizo ndizo ambazo zingefanikisha zoezi lao na kuingia kwenye akaunti ya WhatsApp ya Jesca na kuchukua picha kutoka katika mafaili yake yaliyokuwa kwenye akaunti hiyo.
Kamera hizo ziliunganishwa mpaka katika kompyuta ya Robinson huku zikiwa na nguvu kubwa ya kuvuta kiasi cha kumvuta nzi kutoka chini kwa mbali alipokuwa na kumuweka karibu kabisa.
Wakanunua masofa mawili, wakayaweka humo na kupanga kila kitu kuwa cha hadhi kubwa. Mwenye nyumba ambaye aliwapangisha sehemu hiyo alishangaa baada ya kugundua kuwa wale waliopanga hapo walikuwa waandishi na walitaka kufanya kazi kabla ya kuelekea nchini Tanzania.
“Mimi nitakaa katika chumba kingine. Kwenye mahojiano yako, zungumza naye kwa kina halafu mtumie kitu kwenye WhatsApp halafu mwambie akisome, akifungua akaunti yake hiyo kwenye simu, nitaivuta kwa kutumia kompyuta yangu kupitia moja ya kamera katika upande atakaokuwa,” alisema Robinson huku akimwangalia Robert.
“Unajua mimi nashindwa kukuelewa, hivi hayo yatafanikiwa vipi?” aliuliza Robert.
“Hivi ushawahi kuiona WhatsApp ya kulipia? Achana na hii ya bure huku Afrika, ile ya kulipia kabisa, ushawahi kuiona?” aliuliza Robinson.
“Hapana!”
“Hiyo inakuwa na vitu vingi, kuna sehemu ya kuhifadhi mafaili yako, kwa mbele kabisa kuna sehemu ya WhatsApp Web, si lazima ubonyeze vile vitufe vitatu, hivyo ndiyo ambayo tutaitumia kuingia kwenye akaunti yake,” alisema Robinson.
Kwa Robert alishindwa kuelewa, hakuwa mtu wa kompyuta, kwake, kila kitu alichokizungumza Robinson kilionekana kama muujiza fulani.
Baada ya kukamilisha kila kitu, wakaanza kuitafuta namba ya mwenyekiti wa vyama vya upinzani, Bwana Timoth Oyoyo ambapo baada ya kuipata tu wakaanza kuzungumza naye.
Walimwambia kwamba walikuwa waandishi wa habari kutoka nchini Tanzania ambao walifika Kenya kwa lengo la kufanya mahojiano na Jesca kwa kile kilichokuwa kikiendelea.
Oyoyo alishtuka, hakuamini alichokisikia, moyo wake ulikuwa na furaha tele, aliamini kwamba endapo Jesca angefanya mahojiano na waandishi wa habari kutoka nchini Tanzania basi ingekuwa kazi nyepesi kulisambaza suala hilo na kupata nguvu kwa kila kitu ambacho wangetaka kupata hapo baadaye.
Walizungumza na kukubaliana, baada ya hapo Oyoyo akazungumza na Jesca ambaye hakuwa na wasiwsi wowote ule.
“Ila kuna umuhimu na kufanya mahojiano na waandishi kutoka Tanzania?” aliuliza Jesca huku akimwangalia Oyoyo.
“Ndiyo! Tena hii ndiyo nafasi nzuri! Jesca, kama kweli tutafanikiwa katika hili, nakuahidi tutashinda hii kesi kwa asilimia mia moja,” alisema Oyoyo.
Ilikuwa ni vigumu kwa Jesca kukubali, ni kama moyo wake ulikuwa na hofu lakini hakuwa na jinsi, akakubaliana naye na hatimaye kumwambia Robert kwamba walikubali kufanya mahojiano.
Siku hiyohiyo majira ya saa nane mchana, wakaonana ndani ya sehemu hiyo ambayo ilitengenezwa na kuonekana kama kituo kidogo cha waandishi wa habari ambapo walikuwa wakipatumia.
Hapo kulikuwa na kamera za kukodi, ilikuwa ni lazima watengeneze sehemu ambayo ingeonekana kwamba kweli ilikuwa ni ya waandishi wa habari kutokana na vifaa vya humo kuwa na gharama kubwa.
“Naitwa Robert kutoka Mzalendo Tv,” alijitambulisha Robert huku kamera ikiwa mbele yao ambapo kulikuwa na vijana wawili waliowakodisha kwa ajili ya kazi hiyo.
Robert alionyesha tabasamu, alimwangalia Jesca, alikuwa msichana mrembo ambaye hakutakiwa kabisa kupitia kile alichopitia. Akazungumza na Oyoyo na kujitambulisha na kumwambia kwamba lengo kubwa la kufanya mahojiano hayo ni kwa sababu walitaka kuisambaza habari hiyo Afrika nzima.
“Ni jambo zuri sana!” alisema Oyoyo.
Baada ya kukubaliana, Robert na Jesca wakakaa kwenye kochi na kuanza kumuhoji maswali kadhaa. Jesca hakuwa na hofu, aliamini kwamba kweli mwanaume huyo alikuwa mwandishi wa habari, kila alichoulizwa, alijibu pasipo kugundua kwamba upande wa pili kulikuwa na mwanaume aliyekuwa akiifanya kazi yake kikamilifu kupitia kamera zilizowekwa ndani ya chumba kile.
Mahojiano yalikuwa yakiendelea, ndani ya chumba hicho kulikuwa na watu wengi kutoka kwenye vyama vya upinzani, kipindi hicho huyo Jesca alikuwa akilindwa kuliko kitu chochote kile kwani walihisi kwamba ndiye angekuwa ushindi wao mkubwa na kumdhoofisha rais wa nchi hiyo, Bwana Kimoni.
“Nataka nikuulize maswali ya siri sana, ila sitokuuliza kwa mdomo, nitakuuliza kwa WhatsApp, kama utaliona linajibika, naomba unijibu kwa mdomo,” alisema Robert huku akimpa kikaratasi aandike namba yake, Jesca akafanya hivyo.
“Haina shida.”
Hiyo ndiyo nafasi iliyokuwa ikisubiriwa, kule alipokuwa, Robinson akaanza kuivuta simu ya msichana huyo, swali lilipoulizwa kwenye WhatsApp na kuifungua tu, haraka sana Robinson akaivuta, akaingiza program yake ya udukuaji na kuanza kwenda kwenye kipengele cha WhatsApp Web ambapo huko kulikuwa na Barcode alizoziscan kwenye kompyuta yake na hatimaye kukubali na kuingia kwenye akaunti ya msichana huyo.
“Bravo figlio,” (safi kijana) alisema Robinson kwa Lugha ya Kilatin.
Hakutaka kuchelewa, hiyo ndiyo ilikuwa nafasi yake pekee. Kitu alichokifanya ni kuingia kwenye mafaili ndani ya akaunti hiyo, humo akakutana na vitu vingi zikiwemo picha na video kuhusu kile kilichokuwa kimetokea.
Alichokifanya ni kuanza kuzikopi harakaharaka. Alizichukua zote ambazo kwa pamoja zilikuwa na ukubwa wa 1.6GB na alipomaliza tu, akaamua kuzifuta kwenye akaunti ya msichana huyo.
Hakuishia hapo, kwa sababu akaunti hiyo iliunganishwa na barua pepe, akaingia huko, akapekua kwenye mafolder yaliyohifadhiwa na kuanza kuzifuta picha na video fupifupi zilizokuwa humo ambazo zingetumika kama ushahidi kwenye kesi hiyo iliyokuwa ikimkabili.
Alipohakikisha amemaliza kila kitu, akazifuta moja kwa moja na kupandikiza kirusi ambacho alikuwa na uhakika kusingekuwa na mtu ambaye angekitoa kwenye akaunti hiyo.
“Nimemaliza mzee baba!” aliandika ujumbe mfupi kwenda kwa Robert ambapo baada ya kuupokea tu, alichokifanya ni kumaliza mahojiano harakahara na kuwashukuru wote kwa ushirikiano waliowapa.
“Tunashukuru sana!” alisema mwanaume huyo, watu hao hawakutaka kupoteza muda, wakaondoka zao mahali hapo huku wakiwa na uhakika kwamba habari hiyo ingesambazwa zaidi na uozo wa Kimeta ungejulikana kila sehemu.
***
Jesca alishtuka, hakuamini kile kilichokuwa kikiendelea, aliangalia simu yake kwenye Mtandao wa Kijamii wa WhatsApp kwa lengo la kuangalia kama kulikuwa na zile picha na video alizokuwa ameziweka kwenye faili lake, alipopekua hakuona kitu jambo lililomfanya kushtuka.
Hakuangalia mara moja, aliangalia zaidi ya mara tatu, alifungua huku na kule lakini hakubahatika kuziona. Hilo likamchanganya, alichanganyikiwa, akaingia kwenye barua pepe ambapo huko pia alizihifadhi, alipofungua, akazikosa na mbaya zaidi akakutana na vitu ambavyo hakuvielewa.
Haraka sana akampigia simu Oyoyo na kumwambia kwamba alitaka kuonana naye, kwa jinsi alivyoongea tu mwanaume huyo akajua kabisa kulikuwa na kitu kilichoendelea hvyo haraka sana akaonana naye na kuanza kuzungumza.
Kwa jinsi msichana huyo alivyoongea na machozi kumtoka aliamini kabisa kulikuwa na jambo kubwa na zito. Alipomwambia tu kwamba zile picha na video hazikuwa zikionekana, akahisi mwili wake ukinyong’onyea na kukaa kwenye kochi.
“Unasemaje?” aliuliza mzee Oyoyo.
“Zimefutwa, kuna mtu aliingia kwenye akaunti na kuzifuta,” alisema Jesca.
Oyoyo alimwangalia Jesca, hakuamini alichokuwa akiambiwa, alihisi kama alitaniwa kwani miongoni mwa vitu ambavyo walitakiwa kuwa makini navyo ni hizo picha na video.
Aliambiwa kwamba zilifutwa kwenye simu yake na barua pepe, zilifutwaje? Nani aliingia na kufanya kazi hiyo? Alimuuliza kama simu yake aliwahi kumgawia mtu yeyote yule na kuitumia, alimwambia kwamba hakufanya hivyo, sasa kama simu hiyo haikuchukuliwa na mtu yeyote, ni nani alifanya kazi hiyo?
Hawakutaka kumwambia mtu yeyote yule, ilikuwa ni lazima wajue kilichotokea mpaka vitu hivyo kupotea katika mazingira ya kutatanisha.
Waliendelea na uchunguzi wa kimyakimya kwamba iilikuwa ni lazima mtu huyo agundulike kwani walikuwa na hofu kwamba inawezekana katika hoteli ambayo walimlaza kulikuwa na mtu aliyeingia na kuiiba simu hiyo.
“Jesca! Inawezekana vipi?” aliuliza Oyoyo huku kijasho kikimtoka.
“Hata mimi nashangaa!”
“Hawa watakuwa watu wa serikali! Ni lazima tufanye kila liwezekanalo kuhakikisha vitu hivyo vinarudishwa,” alisema Oyoyo.
Hicho ndicho walichokifanya, haraka sana wakawasiliana na vijana wao wa IT na kuwaambia kulikuwa na kazi iliyotakiwa kufanyika haraka sana na kama iliwezekana basi waonane kwenye hoteli hiyo.
Ni ndani ya nusu saa tu vijana hao wakafika hotelini hapo, wakachukuliwa na kupelekwa katika chumba hicho na Jesca kuanza kuelezea kilichokuwa kimetokea.
Vijana hao walimsikiliza kwa makini, tatizo walilokutana nalo siku hiyo lilikuwa kubwa, mbaya zaidi hata kuwahi kuitumia WhatsApp ya kulipia hawakuwahi hivyo walivyoambiwa kuhusu mambo hayo walibaki wakishangaa tu.
“Hakuna mtu anayeweza kudukua akaunti ya WhatsApp, labda kuna mtu alichukua simu yako,” alisema kijana mmoja, kila kitu alichombiwa aliona kabisa haikuwezekana hata kidogo.
“Ila hakuna mtu aliyeichukua!”
“Hata mtu aliyekutaka ufungue akaunti yako?”
“Hakuna...sijawah....hebu subiri! Nafikiri ni wale waandishi wa habari!” alisema Jesca.
“Waandishi gani?”
Jesca akaanza kuwaambia kuhusu watu hao, hapo ndiyo Oyoyo akakumbuka kila kitu, naye akahisi kwamba inawezekana waandishi wale wa habari ndiyo waliohusika katika kungia kwenye akaunti ya Jesca na kuzifuta picha hizo.
Haraka sana Oyoyo akachukua simu yake na kupiga nchini Tanzania katika Televisheni ya Wazalendo na kuomba kuzungumza na meneja mkuu. Hilo halikuwa tatizo, simu ikaunganishwa mpaka huko na kuzungumza naye.
Kwanza alimuelezea kila kitu, jinsi walivyokuwa wakipambana lakini mwishi wa siku waandishi kutoka nchini humo waliondoka na kuelekea Kenya ambapo walifanya mahojiano na Jesca, walihisi kulikuwa na kitu walichokifanya.
“Waandishi kutoka kwetu?” aliuliza mwanaume huyo huku akionekana kushangaa.
“Ndiyo!”
“Hapana! Hatukutuma mwandishi yeyote yule,” alisema meneja kwenye simu.
“Hamkutuma mwandishi yeyote?”
“Ndiyo! Hao ni waandishi gani?” aliuliza meneja.
Kwa kusema maneno hayo tu kukampa uhakika Oyoyo kwamba wale wanaume wawili ndiyo waliokuwa wamehusika katika jambo hilo hivyo ilikuwa ni lazima wapambane kuhakikisha wanawapata na kuchukua picha na video zile.
Hawakujua ni kwa jinsi gani wangeweza kuwapata, waliwaambia wenzao kuhusu watu hao na hivyo kuanza kuwatafuta kimyakimya, kwa kile kilichokuwa kimetokea, ilikuwa ni lazima iwe siri kwani kama isingekuwa hivyo, wangekosa kila kitu kwa sababu kama wangeulizwa kuhusu ushahidi wa picha na video hizo, wasingekuwa na lolote la kuionyeshea mahakama.
“Jamani naomba tupambane! Wale vijana ni muhimu sana, si mnawakumbuka?” aliuliza Oyoyo.
“Mimi nawakumbuka sana! Ila wamefanya nini bosi?” aliuliza kijana mmoja, hakukuwa na mtu aliyekuwa akifahamu zaidi ya Oyoyo na Jesca.
“Wamefanya jambo moja kubwa sana, kwanza tuwatafuteni, tukiwapata nadhani itakuwa fudisho kwa watu wengine,” alisema Oyoyo huku akijitahidi kila kitu kilichoendelea kuwa siri kubwa pasipo watu wengine kufahamu lolote lile.
 
NYEMO CHILONGANI
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Kumi na tatu

Mara baada ya kuzipata picha ambazo Oyoyo na watu wake walikuwa wakilingia nazo, Robinson na Robert wakarudi mjini Mombasa na kukaa katika hoteli ya kawaida ambapo huko wakaanza kupanga mipango yao.
Ilikuwa ni lazima wazitumie picha hizo kupata pesa nyingi kutoka kwa watu hao, ilikuwa ni lazima waionyeshe Afrika kwamba wao walikuwa watu hatari, waliopaswa kuogopwa, watu ambao walikuwa na uwezo wa kufanya mambo magumu ambayo yalishindikana kabisa.
Kitu cha kwanza kilikuwa ni kutafuta namba ya Rais Kimoni kwa lengo la kuzungumza naye na kumwambia kuhusu picha hizo.
Haikuwa kazi nyepesi kuipata namba ya mwanaume huyo hivyo walichotakiwa kufanya ni kutafuta namba za watu wengine ambao waliamini kabisa kupitia wao wangeweza kufanikiwa kuipata namba yake.
Hilo halikuwa tatizo, wakapewa namba ya Waziri wa Fedha, Bwana Machali na kuanza kuzungumza naye. Walimwambia kwamba walikuwa na ishu walitaka kuzungumza na rais.
Waziri huyo hakutaka kuwapa, alihisi kabisa kulikuwa na jambo la hatari na hata hivyo halikuwa jambo jepesi kumpa mtu asiyemjua namba ya rais wake, hivyo akawaambia kwamba hakuwa nayo.
“Unajua sisi tuna jambo muhimu sana tunataka kuzungumza naye, hebu mpigie simu, mwambie kijana mwenye zile picha za Kimeta na yule Jesca anataka kuzungumza na wewe,” alisema Robinson kwenye simu.
Machali hakujua Robinson alimaanisha nini lakini hakuwa na jinsi, alipokata simu tu, akampigia Rais Kimoni na kuanza kuzungumza naye. Alimwambia kama alivyoambiwa kwamba kulikuwa na kijana ambaye alikuwa na picha za rafiki yake, Kimeta ambaye alipiga na msichana Jesca wakati wakiwa hotelini akimbaka.
Rais alivyoambiwa hivyo hakutaka kuchelewa, haraka sana akaomba hiyo namba, akapewa na kumpigia Robinson, alihitaji kuzungumza naye kuhusu jambo hilo kwa kuwa alichokiamini ni kwamba picha hizo zilikuwa kwa Oyoyo na Jesca, sasa ilikuwaje ziwe kwa mtu mwingine?
Akampigia na kuanza kuzungumza naye. Robinson alimwambia ukweli kwamba picha alizichukua kimazingaombwe tu kutoka katika simu ya Jesca ambapo zilikuwa zimefichwa na kusingekuwa na mtu yeyote ambaye angeziona tofauti na yeye.
“Kwa maana hiyo wao hawana picha hizo ama?” aliuliza rais huku akionekana kuchanganyikiwa kwa furaha.
“Pigia mstari mzee baba! Yaani mimi ndiye mwenye picha hizo na si mwingine,” alijibu Robinson kwa sauti ya kujiamini sana.
Rais hakutaka kuamini, alihitaji kuziona hizo picha, hilo halikuwa na tatizo, Robinson akamtumia picha moja. Rais alipoipata, akashtuka, hakuamini alichokuwa akikiona.
Ni kweli ilikuwa picha ikimuonyesha rafiki yake, Kimeta akimbaka Jesca chumbani. Yeye mwenyewe ndiyo kwanza ilikuwa mara ya kwanza kuziona picha hizo, hakuamini alichokuwa akikiona.
Akampigia simu Robinson na kumwambia kwamba alikuwa tayari kumlipa kiasi chochote cha pesa lakini alihitaji picha hizo zifutwe na zisionekane tena kwenye dunia hii.
“Sawa! Ninahitaji dola milioni mbili, fanya haraka,” alisema Robinson kiasi ambacho kilimshtua mno rais.
“Unasemaje?”
“Nadhani umenisikia, utanipa ama?” aliuliza Robinson.
“Naomba nijifikirie!”
“Dau linaongezeka zaidi kila baada ya saa moja, ukizidi kuchelewa ndivyo ambavyo pesa itaongezeka zaidi,” alisema Robinson.
Ukimya ukasikika kwa sekunde kadhaa, kiasi alichokitaja kilikuwa ni milioni mia mbili kwa shilingi ya Kikenya na bilioni nne kwa shilingi ya Kitanzania.
Kilikuwa ni kikubwa mno lakini ili kumsaidia rafiki yake kuepuka kifungo ilikuwa ni lazima akilipe kiasi hicho cha pesa kwa sababu bila kufanya hivyo basi mtu wake wa karibu afungwe gerezani.
Akazungumza naye na kumwambia kwamba angempigia muda si mrefu kwani alihitaji kujifikiria zaidi kuhusu malipo hayo.
Mtu ambaye alikuja kichwani mwake alikuwa ni jaji, Ibrahim Kifathi ambaye ndiye aliyechaguliwa kuisimamia kesi hiyo mpaka siku ya hukumu. Akampigia simu na kumwambia kuhusu kilichokuwa kikiendelea, kulikuwa na watu waliokuwa na picha za ushahidi, kama lingekuwa jambo jema basi wazinunue ili kesi hiyo washinde pasipo tatizo lolote lile kwa sababu ushahidi ungekuwa umepotea.
Alichokisema Kifathi ni kwamba hawakutakiwa kuzinunua picha hizo kwa sababu yeye mwenyewe tayari aliseti mipango yake ili kuonekane hakuna kesi yoyote ile hivyo piga ua ilikuwa ni lazima huyo kimoni ashinde kesi hiyo.
“Kwa hiyo nisinunue hizo picha?” aliuliza rais.
“Wala usinunue! Kimeta anashinda kesi bila tatizo,” alisema Kifathi kwenye simu.
Hiyo ikaonekana kuwa nafuu kwa rais, hakutakiwa kununua picha hizo kwa kuwa alihakikishiwa kwamba kesi wangeshinda hata kama picha zilikuwepo. Hakutaka kumwambia Robinson, akaamua kumpotezea kwa kuwa aliamini jaji Kifathi alikuwa na uwezo wa kufanya jambo lolote lile.
***
Kitendo cha rais kumpigia simu Robinson lilikuwa kosa kubwa, simu ilipokatwa, alichokifanya Robinson ni kuanza kuidukua simu hiyo ili aanze kufuatilia kila simu iliyokuwa ikiingia na kutoka, siyo hiyo tu bali hata meseji ambazo zilikuwa zikiingia na kutoka.
Hilo alifanikiwa pasipo rais wala usalama wa taifa wa Kenya kuligundua. Mpaka kipindi ambacho Rais Kimoni anampigia simu Kifathi na kuanza kuzungumza naye, Robinson na Robert walikuwa wakisikia mazungumzo yao, alikasirika kwa kuwa aliamini kwamba ni kweli Kifathi alikuwa na uwezo wa kufanya jambo lolote lile.
“Tumefeli,” alisema Robert huku akionekana kukata tamaa, mazungumzo aliyokuwa ameyasikia, yalimvunja nguvu.
“Sijawahi kufeli tangu nizaliwe, na sitoweza kufeli! Hapa bado tutafanikiwa na kupata kiasi hicho ch pesa,” alisema Robinson.
Kitu ambacho kilikuja kichwani mwake ni kuhusu huyo Jaji Kifathi, alichokiamini ni kwamba kulikuwa na mambo mengi ambayo majaji walikuwa wakiyafanya ili kuwanyanyasa watu fulani mahakamani na hata kutoa hukumu ambazo hazikuwa sawa.
Aliamini hilo kwa sababu ndiyo ilikuwa hulka ya baadhi ya majaji barani Afrika. Alitaka kuzijua siri hizo na kwa sababu aliipata namba ya Kifathi, aliamini kuwa iliunganishwa na akaunti yake ya barua pepe hivyo alihitaji kuingia huko.
Kwa uwezo wake mkubwa wa kudukua, akafanikiwa kuingia kwenye barua pepe ya Kifathi na kuanza kuangalia zile zilizokuwa zimeingia na kutoka. Humo hakukutana na yoyote mbaya, zilikuwa ni zile za kawaida.
Hakutaka kuishia hapo, alichokigundua ni kwamba hakukuwa na mtu aliyeiacha barua pepe mbaya sehemu ya wazi, kama kulikuwa na mchezo aliucheza na kushirikishwa humo, ilikuwa ni lazima aifute.
Alichokifanya ni kwenda kwenye sehemu ya kufutwa barua pepe, huko alikutana na baadhi, hakuridhika, kwa kutumia programu yake ya Undelete email, aliyoiweka kwenye kompyuta zake, akaanza kuzitafuta zile barua pepe zote ambazo zilikuwa zimefutwa kabisa na hazikuwepo, ilikuwa ni sawa na kurestore vitu ambavyo vilipotea.
Hapohapo barua pepe nyingi zikaanza kujirudisha huku nyingine zikiwa na picha nyingi. Alizirudisha barua pepe zaidi ya mia moja na kuanza kuzipitia.
Huko ndipo alipokutana na vitu alivyokuwa akivitaka mno, aliweza kuziona barua pepe ambazo mwanaume huyo aliwasiliana na watu wengi waliokuwa na kesi mbalimbali na kuambiwa kwamba angepewa kiasi kikubwa cha pesa kama tu angewasaidia kushinda kesi zao.
Mwanaume wa kwanza ambaye aliwasiliana naye aliitwa Brown Williams. Huyo alikuwa mwekezaji kutoka nchini Uongereza ambaye alifika Kenya mwaka 1990 na kuwekeza katika kilimo cha kahawa.
Alipofika hapo, kutokana na matendo yake ya udhalilishaji wa wanawake waliokuwa wakimfanyia kazi ikiwemo kuwabaka na kuwapiga, akafikishwa mahakamani na jaji ambaye alisimamia kesi hiyo alikuwa Kifathi.
Baada ya kuona kwamba angeshindwa kesi hiyo na kufungwa miaka mingi, akawasiliana na mwanaume huyo na kumwambia kuhusu lile lililokuwa likiendelea.
Kwanza akamwambia angemlipa dola milioni moja na nusu kama tu angemsaidia kushinda kesi hiyo.
Walizungumza mengi kwenye barua pepe na huyo Kifathi kumwambia awamalize mashahidi wote watatu ili kusiwe na kesi yoyote na barua pepe ambayo ilifuata kutoka kwa Brown ilimwambia Kifathi kwamba tayari mashahidi waliuawa na hivyo kushinda kesi iliyomalizika mwaka 2011.
Ukiachana na hiyo pia kulikuwa na mambo mengine mengi. Robinson mwenyewe alipokuwa akiyaona, alishindwa kuamini kama kweli yule Kifathi alikuwa mtu muovu kiasi hicho.
Alizichukua zote hizo, alikuwa na ushahidi wa barua pepe na hivyo kupanga kumtafuta Kifathi ili amwambie kuhusu kile kilichokuwa kikiendelea.
“Kumbe kuna watu waovu sana. Aisee yule mzee ukimwangalia unaweza kupiga magoti akuongoze sala ya toba, kumbe mshenzi tu,” alisema Robert.
“Hii ndiyo dunia! Ngoja nimtafute,” alisema Robinson na hapohapo kumpigia simu Kifathi.
Simu haikuita kwa muda mrefu, ikapokelewa na kuanza kuzungumza naye. Alijitambulisha kwa jina la The Ghost ambaye alikuwa akijua mambo mengi kwenye dunia hii ambayo yalijificha, hata yale yaliyokuwa chini ya kapeti aliyafahamu vilivyo kabisa.
“Sijajua unamaanisha nini! Unataka nikusaidie nini wewe The Ghost?” aliuliza Kifathi, kwa jinsi alivyomsikiliza Robinson, aliona kama mwanaume aliyejisifu sana.
“Unamkumbuka Brown Williams?” aliuliza Robinson.
Baada ya kulisikia jina hilo, moyo wa Kifathi ukapiga paa! Hakutarajia kulisikia, lilimshtua kupita kawaida. Robinson akabaki kimya huku akiendelea kumsikilizia mwanaume huyo, alihitaji kusikia kama angezungumza kitu chochote kile.
Alipoona amebaki kimya, akaanza kumwambia kuhusu kilichotokea kati yake na Muingereza hiyo, jinsi alivyopokea rushwa kutoka kwake, alivyomsaidia kushinda kesi yake na kuwamaliza mashahidi watatu ambao waliwekwa kwa ajili ya kesi hiyo.
Hakuishia hapo tu, alimwambia mambo mengi, kesi nyingine ambazo alizisimamia na kujifanya mtuhumiwa kushinda na wakati ushahidi ulionyesha wazi kwamba alishindwa kesi hiyo.
Kwa jinsi alivyokuwa akiambiwa kwa data, Kifathi akabaki akitetemeka, mwili ukaanza kutoa jasho jingi, hakuamini kama siri zake zingejulikana. Hakujua huyo ghost alizijuaje na wakati hata kuwasiliana na Brown alifanya kwa barua pepe tu kwa kuamini mawasiliano ya simu yangeweza kudakwa.
“How do you know all of this?” (umejuaje yote haya?) aliuliza Kifathi swali ambalo alijua wazi kabisa hakutakiwa kuuliza.
“I told you...I am the Ghost...” (nilikwambia...mimi ni mzimu) alisema Robinson na kukata simu.
 
NYEMO CHILONGANI.
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Kumi na Nne.

Kifathi alichanganyikiwa, simu ilikatwa lakini bado alikuwa na hamu ya kuzungumza na mwanaume aliyempigia, hakutaka kupoteza muda, haraka sana akampigia na simu kupokelewa.
Alichanganyikiwa, kijasho chembamba hakikuacha kumtoka, alitetemeka huku akiona kabisa huo ndiyo ulikuwa mwisho wake, yaani kila kitu kilichokuwa kimetokea, kingewekwa wazi, watu wangempuuzia na kumuona mjinga ila kubwa kuliko yote ni kwamba angeshtakiwa na kuhukumiwa kifo kwa kuwa alishiriki kwenye mauaji.
Alimwambia Robinson kwamba ni kweli alifanya hayo yote yaliyotokea lakini alihitaji amtunzie siri kwani vinginevyo maisha yake yangeharibika na kuonekana kutokuwa na thamani hata kidogo.
Hakuishia hapo tu bali alimwambia kwamba alikuwa tayari kufanya kitu chochote kile, hata kama angehitaji pesa, kwa mambo aliyokuwa ameyafanya alikuwa tayari kutoa kiasi chochote kile.
Robinson akaanza kucheka kwa dharau, hilo ndilo alilolitaka, akamwambia Kifathi kwamba ishu ile ilikuwa kubwa na hakuwa na mpango wowote ule wa kuchukua pesa kutoka kwake.
Kauli hiyo ikamchanganya zaidi Kifathi, kwenye simu hiyohiyo akaanza kulia kama mtoto mdogo huku akiomba msamaha kwa nguvu kubwa.
Muda wote huo ambao Robinson alikuwa akizungumza na Kifathi, Robert alikuwa pembeni, alikuwa akicheka sana, hakuamini kama kungekuwa na mwanaume aliyekuwa akiogopa kuchafuliwa kama huyo.
“Ninahitaji kiasi cha dola milioni moja kutoka kwako,” alisema Robinson kwenye simu.
Kifathi akashtuka, kiasi alichoombwa kilikuwa kikubwa sana, hakuwa na pesa hiyo, alimwambia Robinson kwamba hakuwa na kiasi hicho cha pesa kwani kilikuwa kikubwa mno.
Alichokisema Robinson ni kwamba kama alishindwa kumpa kiasi hicho basi angetoa siri hizo kwani wakati akifanya mambo yake yote, alichukua pesa kutoka kwa watu hao zaidi ya dola milioni hamsini na nane, sasa ilikuwaje ashindwe kutoa dola milioni moja?
“Kama hauna! Basi sawa. Kwa heri...” alisema Robinson.
“Hapana! Naomba usikate simu, nipo tayari kukupa hizo pesa,” alisema Kifathi huku akitamani hata Robinson awe mbele yake na azungumze naye.
“Hiyo haitoshi! Wewe ndiye unayesimamia kesi ya Kimeta, sasa tunataka kesi hiyo ashindwe kwa kuwa ushahidi wa picha upo. Mwambie rais anunue hizo picha, akishindwa, tutaziweka hadharani na pia na wewe mambo yako yatakuwa hadharani pia,” alisema Robinson.
Hapo ndipo alipogundua kwamba mwanaume huyo inawezekana alikuwa yule aliyezungumza na Rais kimoni. Alichanganyikiwa, hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya, alimwambia rais kwamba kesi ile angeshinda bila tatizo lolote lile, alimpa uhakika huo lakini ghafla tu aliambiwa na mtu mwingine kwamba alitakiwa kumshawishi rais huyo anunue picha hizo vinginevyo ushahidi ungewekwa wazi.
Hakujua afanye nini lakini kwa sababu mwanaume huyo alikuwa na maovu yake, hapohapo akampigia simu rais na kumwambia kile kilichotokea.
Rais alishangaa, akagundua kwamba walikuwa wakidili na watu hatari sana, waliokuwa na uwezo wa kufanya jambo lolote lile. Aliogopa, kama aliambiwa na Kifathi kwamba alitakiwa kununua hizo picha vinginevyo maovu yake yote yangewekwa wazi, hakuwa na jinsi, akakubaliana naye.
Akamwambia Kifathi kwamba ni lazima wapambane kuhakikisha watu hao wanauawa na kitu chepesi alichomwambia Robinson baada ya kumpigia simu ni kumwambia kuhusu malipo ya pesa hizo, yaani azifuate ikulu.
“Unanifanya mimi mtoto sana! Tangu tumewasiliana zimepita saa tatu, na kila saa iliyozidi utalipia dola laki moja,” alisema Robinson.
“Hakuna shida,” alijibu rais kwani alijua kwa namna moja ama nyingine ilikuwa ni lazima afanye kila liwezekanalo kuhakikisha hizo pesa atakazompa Robinson mwisho wa siku zinarudi kwake.
Wakakubaliana malipo kufanyika katika benki, yaani yeye rais azitume kwa namba alizopewa. Kabla ya kufanya hivyo, kitu cha kwanza alichokifanya ni kuwasiliana na uongozi wa benki na kuwaambia kwamba kulikuwa na kiasi ambacho atakiweka kwenye akaunti fulani, kikiingia, hawakutakiwa kukiruhusu kitoke chote mpaka mtu huyo aende benki kwa ajili ya kufanya uhamisho huo, na pindi atakapokuwa huko, awapigie simu polisi na kwenda kumkamata.
“Hakuna tatizo mkuu!”
Hicho ndicho alichokifanya, akawasiliana na Robinson, akamwambia kwamba angemtumia kiasi cha dola milioni tatu na laki tatu, yaani milioni moja ni ya Kifathi, milioni mbili ni zake na laki tatu ni za ile ambazo ziliongezeka kila baada ya saa moja.
Baada ya kuelewana, haraka sana akamtumia kwenye akaunti yake, kwa Robinson pesa ilisoma kwamba iliingia lakini hakujua kama benki hiyo iliizuia pesa hiyo isitoke yote ili akitaka itoke yote basi aende na kuihamisha hukohuko benki.
***
Penzi la Richard lilimchanganya Upendo, hakuamini kama mwisho wa siku angefanikiwa kuwa na mwanaume huyo. Kila kona chuoni hapo alikuwa naye, alimpa pesa na kumpa mapenzi motomoto.
Alimthamini na kumuonyeshea mapenzi ya njiwa, ambayo mwanaume yeyote alitakiwa kuonyeshwa na mpenzi wake.
Kwake, Richard alichukia mno, hakutamani kabisa kuona msichana huyo akimpenda namna ile. Alimchukia lakini kwa kuwa kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea nyuma ya pazia, hakuwa na jinsi.
Aliwasiliana na marafiki zake nchini Kenya, walimwambia jinsi walivyofanikiwa kwa kila kitu walichokuwa wakikipanga, walimwambia kwamba mara baada ya kumaliza mipango yote wangeondoka na kuelekea nchi nyingine lakini mwisho wa siku wafanikiwe kwa kile walichokuwa wakikihitaji.
Alifurahi, kiasi ambacho watu hao wangetoa kingekuwa kikubwa sana ambacho kingewapa utajiri mkubwa kabla ya kuondoka na kwenda katika nchi nyingine.
Aliendelea kukaa nchini Tanzania na Upendo, ili msichana huyo aone jinsi alivyokuwa akimpena Richard, kwenye kila sehemu mitandaoni aliweka picha za mwanaume huyo na wakati mwingine akiziposti ili kuwaringia mashoga zake.
Kila msichana aliyeziona picha za Richard alichanganyikiwa, kijana huyo alikuwa mzuri wa sura, watu walizipakua picha hizo na kuziweka kwenye akaunti zao na kumsifia mwanaume huyo kwa jinsi alivyokuwa mzuri.
“Jamani! Ndoto yangu kubwa ni kulala na mwanaume kama huyu. Ana sura nzuri, macho yanaita, angalia mwili wake ulivyojijenga, jamaniiiiii! Natangaza kabisa mwenye mwanaume huyu tutapambana na sisi tunamtaka pia,” aliandika msichana mmoja mrembo mno.
Picha hizo zilichukuliwa na kuwekwa sehemu mbalimbali na hatimaye Richard kupigiwa kura na akaunti nyingi kwamba ndiye mwanaume mzuri kuliko wanaume wote barani Afrika.
Jina lake likaanza kuwa kubwa, kila msichana aliyemuona, alidiriki kusema kwamba kwenye maisha yake yote, japo kwa mara moja alifanikiwa kumuona mwanaume mzuri kama alivyokuwa Richard.
Wanawake hawakuishia hapo, waliposema kwamba walitaka vita walimaanisha na hivyo kuanza kumtafuta Richard. Kumpata haikuwa vigumu, wakafanikiwa na hivyo kuanza kuomba nafasi ya kuzungumza naye au hata kupiga picha.
Kwa Upendo yalikuwa ni maumivu makali, kila alipokaa na Richard, wanawake walimfuata na kutaka kupiga picha pamoja naye. Aliumia lakini hakuwa na jinsi, aliamini kwamba Richard asingeweza kumuacha kwa sababu kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea.
“Nitaua mtu!” alisema Upendo.
Aliyasema hayo kama utani lakini moyoni mwake alimaanisha, alikuwa na hasira sana, alikuwa tayari kuchezewa yeye lakini si Richard ambaye kwake alikuwa kama malaika.
Msichana aliyeitwa Manka ambaye alitumia jina la baby_manka kwenye mitandao ya kijamii aliyekuwa na wafuasi zaidi ya laki tisa akaanza kuziweka picha hizo huku akiahidi kiasi cha shilingi milioni moja kwa yeyote ambaye angafanikisha kupatikana kwa namba ya Richard.
Tangazo hilo likawafanya watu wengi kuchangamkia fursa, Manka aliitaka sana namba ya Richard kwa kuwa alikuwa mwanaume aliyempenda kwa moyo wote.
Baada ya siku mbili tu, msichana huyo akaipata namba ya Richard na hivyo kuanza kuwasiliana naye. Hakutaka kujificha, alimwambia ukweli kwamba alimpenda sana na moyoni mwake alikuwa mtu wa thamani mno kuliko yeyote yule.
Richard alikataa lakini Manka hakutaka kukubali, kwake, alikuwa tayari kukosa kila kitu katika maisha yake lakini si kuona akimkosa mwanaume huyo.
Wakati Manka akiendelea kumtongoza Richard, Upendo akaambiwa hila za mwanamke huyo kwamba ilikuwa ni kumuachanisha na Richard ili awe naye.
Kwa Upendo yalikuwa kama matusi, hakutaka kukubali, aliikumbuka gharama aliyoingia mpaka kumpata mwanaume huyo, hivyo kwa moyo mmoja akaridhia amuue huyo manka ili awe na amani moyoni mwake.
Alipanga mipango, hakukuwa na mtu aliyekuwa akijua lolote lile, huko kwenye mitandao Manka alizidi kutamba kwamba angempata Richard ambaye alikuwa usingizi wake pasipo kugundua kama upande wa pili Upendo alikuwa akijipanga kwa ajili ya kummaliza.
Siku ziliendelea kukatika, watu waliendelea kumpongeza Manka na kumwambia aendelee kumfuatilia Richard kwani angeweza kumpata mwanaume huyo na kuanza kuwarusha roho wanawake wengine waliokuwa na majina makubwa nchini Tanzania.
Baada ya wiki moja, maiti ya Manka ikakutwa katika Ufukwe wa Coco, ilikatwakatwa mapanga, ilibakwa na kisha kuchomwa visu mfululizo na kwenda kuitupa katika ufukwe huo huku ikiwa kwenye kiroba.
Watu walioiona, walishtuka, hawakujua maiti ile ilikuwa ni ya nani mpaka pale ambapo polisi waliichukua na kuipeleka hospitali, kusafishwa na kuonyeshwa kwamba alikuwa ni Manka, yule mwanamke aliyekuwa na jina kubwa katika mitandao, mwanamke aliyependwa kwa stori za udaku, kula bata na mambo mengine, ndiye huyo ambaye maiti yake ilikutwa ufukweni. Nani aliyefanya mauaji hayo? Hakukuwa na mtu aliyejua.
 
hahahhaah, nimepapenda hapa,

"Hilo halina tatizo,” alisema Robinson huku akimwangalia Upendo.
“Unasemaje wewe?” aliuliza Richard huku akionekana kupaniki, jicho alilomkata Robinson halikuwa la nchi hii.
 
NYEMO CHILONGANI.
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Kumi na Tano

Moyo wa Upendo ulikuwa kwenye maumivu makali, hakuamini kilichokuwa kikiendelea. Kila alipopita kwenye mitandao ya kijamii ni Manka tu ndiye aliyekuwa akitamba. Aliwaambia wafuasi wake kwamba alitaka kutembea na Richard na kwa sababu hata yeye mwenyewe alikuwa mzuri wa sura, hakuona kama mwanaume huyo angekataa kuwa naye.
Upendo alikuwa kwenye wakati mgumu, aliujua uzuri wa mpenzi wake, alikuwa mwanaume wa kipekee aliyekuwa na sura yenye mvuto mkubwa, aliamini kwamba endapo Manka angepambana kwa lengo la kumchukua mwanaume huyo, basi mbali na mkataba waliokuwa wamewekeana ilikuwa ni lazima aachane naye.
Hakutaka kuona hilo likitokea katika maisha yake, alimthamini mwanaume huyo, alimpenda na kumuonyeshea mapenzi ya dhati. Hata siku moja katika maisha yake hakufikiria kumuacha na ndiyo maana alikuwa radhi kufanya jambo lolote lile lakini si kuona Richard akiondoka mikononi mwake.
Kelele za msichana huyo zikawa chukizo masikioni mwake, aliogopa na hivyo alichopanga ni kummaliza tu kwa kuamini kwamba angekuwa na furaha maisha yake yote.
Akawatafuta watu ambao aliwaahidi kuwapa kiasi kikubwa cha pesa kwa ajili ya kazi hiyo. Vijana hao waliokuwa wakikaa Kinondoni hawakuwa na tatizo, kama walipewa kazi na kwa malipo makubwa na mazuri, walikuwa radhi kufanya mauaji hayo lakini si kuziacha pesa hizo.
Kumfahamu Manka hakukuwa na tatizo, alikuwa msichana maarufu, alijulikana kila kona kwa sababu ya ukurasa wake katika Mtandao wa Instagram kuwa na wafuasi wengi, hivyo wakafanya mipango ya kumteka.
Walichokijua ni kwamba Manka alipenda sana kwenda katika Klabu ya Laspinho ambapo huko alikuwa akienda na kampani yake ambapo walicheza muziki, kunywa pombe na hata kufanya mambo mengi yakiwemo ya kutafuta mabwana.
Akawaambia waende huko na walipofika, wakakutana na msichana huyo aliyekuwa na marafiki zake huku akionekana kuwa na furaha mno.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake, alikuwa ni malaya wa mitandaoni, aliyaendesha maisha yake kwa kuweka picha alizozipiga studio na kuwavutia wanaume, wengi walimchukua na kufanya naye mapenzi kwa malipo kidogo na kuendelea na mambo yake.
Kijana mmoja miongoni mwa wale watatu waliotumwa, mara baada ya kumuona alipokaa kwenye sofa moja na marafiki zake, akaenda na kukaa hapo, akamuita mhudumu na kuanza kuongea naye.
“Kuna ombe kali ipi hapo?” aliuliza jamaa huyo aliyependa sana kujiita Killer.
“Zote zipo, kali na zile lainiiiiiii...”
“Naomba kali! Nichanganyie,” alisema Killer, akachukua sigara yake na kuanza kuvuta.
Ni ndani ya dakika kadhaa, mezani kulikuwa na chupa saba za pombe kali na za gharama. Manka na wenzake ambao walikuwa pembeni walimshangaa, kwa jinsi alivyokuwa ameagiza pombe nyingi namna ile wakahisi kabisa mwanaume huyo alikuwa na pesa nyingi hivyo wakaanza kujivuta.
“Umependeza...” alisema Manka kwa sauti ya juu kutokana na sauti ya muziki iliyokuwa kubwa humo, alihisi kabisa asingeweza kusikika.
“Ahsante! Unataka kunisaidia?” aliuliza Killer.
“Kama itawezekana! Ila si unaona nina kampani!” alisema Manka.
“Hiyo si tatizo! Subiri,” alisema Killer na kumuita mhudumu.
Pombe zilizowekwa juu ya meza zilikuwa nyingi mno lakini akamwambia mhudumu kwamba alihitaji pombe nyingine. Hilo halikuwa tatizo, haraka sana zikaletwa, akalipia na kuanza kunywa.
Hakuwa mnywaji sana, alikuwa kazini, alijua kabisa kwamba hakuruhusiwa kulewa kwa kuwa alitakiwa kufanya kazi hiyo kwa asilimia mia moja hivyo akaawaachia wanawake hao wanywe kadiri walivyoweza.
Ilipofika majira ya saa tisa usiku, akawaambia kwamba alikuwa akienda kulala na lingekuwa jambo jema kama angeondoka na Manka kwani alitokea kumpenda mno.
“Una hela?” aliuliza Manka kwa sauti ya kilevi.
“Nyingi tu na ndiyo maana nimewanywesha mpaka mnashangaa,” alisema Killer na kumshika kiuno Manka, akamvutia kwake.
Wakanyanyuka na kuanza kuondoka. Manka akawaaga wenzake, aliona amepata buzi kumbe ndiyo alikuwa akienda kufa. Walipofika nje, jamaa akalifuata gari lake, wakaingia na kuondoka mahali hapo.
Manka hakuonekana kuwa na hofu hata kidogo, alichoamini ni kwamba mwanaume huyo alikuwa bwana wake ambaye alijitoa kumgharamia kila kitu kumbe upande wa pili alikuwa muuaji mkubwa.
Wakaondoka! Walipofika maeneo ya Kinondoni, gari likakata kuna ya Manyanya iliyokuwa ikielekea Kinondoni Makaburini, mbele kidogo ikakata kona kulia na kuelekea kwenye njia ya vumbi.
Gari liliendeshwa, Manka alijihisi kuwa salama kabisa, alimuamini mwanaume huyo na alikuwa tayari kufanya lolote lile katika maisha yake lakini si kuona akizikosa pesa ambazo aliamini kwamba mtu huyo alikuwa nazo.
Baada ya dakika kadhaa, gari likasimama nje ya geti moja, kutokana na pombe alizokuwanazo kichwani hakujua alikuwa mahali gani, geti likafunguliwa na gari kuingizwa ndani.
Wanaume wawili wakalifuata gari hilo, wakafungua mlango na kumteremsha Manka kwa mapenzi ya dhati huku wakimuita shemeji na kuelekea naye ndani.
Manka akajisikia huru, kwa sababu alikunywa pombe nyingi, hakuwa na hofu hata kidogo. Akaingizwa mpaka sebuleni, akapitishwa na kuelekea chumbani ambapo akavuliwa nguo zote na kuanza kubakwa mfululizo na wanaume hao watatu.
Hilo ndilo walilolitaka, ilikuwa ni lazima wafanye hivyo kwanza, walizoea kumuona msichana huyo kwenye mitandao ya kijamii, aliringa, alijifanya kuwa na maisha mazuri kwa kupiga picha kwenye majengo ya watu na magari ya kifahari kumbe maisha yake hayakuwa kama yale yaliyoonekana kwenye mitandao.
Kwa sababu alibakwa mfululizo, pombe zilimuisha na kuanza kulia kama mtoto mdogo lakini hakukuwa na mtu aliyemuachia, waliendelea kumbaka zaidi na zaidi.
Walipomaliza, wakaamua kumkatakata na mapanga kisha kumchukua na kumuweka kwenye kiroba na kwenda kumtupa katika Ufukwe wa Coco usiku huohuo na kuondoka zao.
Huo ndiyo ulikuwa mwisho wake, Manka akafa katika kifo kibaya mno, watu walihuzunika, picha zake zilipostiwa kwenye mitandao ya kijamii huku wananchi wakiwasisitiza polisi kufuatilia suala hilo kwa undani kabisa kwani walijua dhahiri kwamba nyuma ya tukio hilo kulikuwa na mtu fulani.
Tetesi zikaanza kusikika kwamba aliuawa na mwanamke mmoja aliyewatuma watu kwa sababu aliibiwa mume wake, mwingine alisema kwamba alifumaniwa, wengine walisema kwamba alitapeli mzigo wa madawa ya kulevya, kwa kipindi hicho hakukuwa na mtu aliyejua undani wa kifo chake, watu wengi walisema kile ambacho walihisi kwamba ilikuwa kweli, hakukuwa na mtu aliyejua kama kilichokuwa kimesababisha kifo chake ni kitendo chake cha kutaka kumchukua Richard kutoka mikononi mwa Upendo.
***
Hakukuwa na kitu ambacho Robinson alikuwanacho makini kama masuala ya pesa, alijua kabisa kulikuwa na mchezo, pesa ziliingia kwenye akaunti aliyokuwa amempa Rais Kimoni lakini alichokishtukia ni kwamba pesa hizo hazikuruhusiwa kutoka.
Ni kweli zilikuwa kwenye akaunti yake lakini alishangaa mno kuona pesa hizo hazichukuliki japokuwa zilikuwa kwenye akaunti hiyo.
Robinson kichwa kilimuuma, alimwambia Robert jinsi kulivyokuwa na mtihani mkubwa kuchukua zile pesa, alimuelezea mambo ambayo hakuyaelewa kwani alizungumza kama mwanaume aliyesoma sana masuala ya IT.
Alitakiwa kupambana! Watu wa benki walikuwa na uwezo mkubwa wa kuingiza codes, kufanya kila kitu walichokiweza lakini kichwa chake kilimwambia hakukuwa na mtu aliyeweza kutengeneza kitu duniani ambacho hakikuwa na uwezekano wa kuvumbuliwa.
Alichezewa mchezo na yeye alichokifanya ni kuingiza codes. Halikuwa jambo jepesi, ili kuingia kwenye database ya benki ilikuwa ni lazima awasiliane na kijana wa IT wa huko na kuzungumza naye, amwambie kuhusu suala lake na hatimaye afanikiwe.
Hiyo ilikuwa kazi ya Robert, yeye ndiye aliyetakiwa kusafiri kuelekea jijini Nairobi kwa ajili ya kuonana na kijana mmoja aliyekuwa akihusika na masuala ya IT ambaye angemwambia kile alichohitaji kukifanya, kama inawezekana amwambie kuhusu codes za kuingia kwenye database ya benki hiyo.
Robert akaenda mpaka Nairobi, ndani ya Benki ya Avatar na kuanza kusubiri na kuangalia mazingira ya humo. Alihitaji kuonana na mmoja wa vijana hao ambao angezungumza nao na kumwambia ukweli kwamba alichokuwa akikihitaji kilikuwa ni codes za kuingilia kwenye database na angemlipa kiasi kikubwa cha pesa.
Alisubiri kuanzia asubuhi mpaka mchana. Akaona angekaa sana hivyo akaelekea mapokezi na kuomba kuonana na meneja masoko ambaye aliamini kwamba angeweza kumsaidia.
Alipoulizia, hilo halikuwa tatizo, kwa kuwa alisema alikuwa na biashara yake alihitaji sana kuiunganisha na benki hiyo kama walivyokuwa wafanyabiashara wengine, dada yule akampeleka mpaka katika ofisi ya bosi huyo kwa lengo la kuongea naye.
Nyuma ya meza alikaa msichana mrembo aliyeitwa kwa jina la Rachel, alizungumza naye na kumwambia kile alichokuwa akikitaka kwamba kulikuwa na biashara yake ya mtandaoni aliyotaka kuifanya hivyo kama ingewezekana basi ingekuwa ni vizuri kama angeonana na kijana mmoja wa IT kwa lengo la kuzungumza naye.
Kwa jinsi Rachel alivyoonekana, alivyokuwa na nyodo, alimwangalia Robert na kumshusha, alimshangaa, suala kama hilo kwa benki yao hawakuwa wakihusika nalo mpaka mtu alipotakiwa kwenda benki kuu ambapo huko ndipo angeulizwa mambo mengi kuhusu biashara hiyo ya mtandaoni na hivyo kuifanya.
“Hatufanyi jambo kama hilo kwenye benki yetu,” alisema Rachel, si kwamba kweli hawakuwa wakifanya, walifanya ila kwa siri kubwa na hakutakiwa mtu mwingine afahamu.
“Dada! Najua biashara inaweza kufanyika lakini sijajua kwa nini unanikatalia,” alisema Robert.
“Hatufanyi! Naomba unielewe!”
Huo ndiyo ulikuwa msimamo wa meneja masoko, Rachel. Hakutaka kumwamini Robert kwa kuwa hakumfahamu, hakujua hasa biashara yake ilikuwa nini.
Robert alimuomba sana lakini msimamo wa Rachel hakubadilika hivyo akaondoka, alipofika nje akampigia simu Robert na kumwambia kilichotokea.
“Unahisi hiyo biashara inafanyika ila hajataka tu kukwambia?” aliuliza Robinson kwenye simu.
“Ndiyo! Nahisi wanaifanya ila kwa siri!”
“Umesema aliyekuwa huko ni msichana?”
“Ndiyo! Tena mzuri, demu wa Kikuyu! Jamani yule demu mkaliiiiiiii...” alisema Robert.
“Basi sawa. Dawa yake ipo. Mpigie simu Richard mwambie aje Kenya haraka sana, hii kazi inabidi ifanyike,” alisema Robinson.
 
NYEMO CHILONGANI.
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Kumi na Sita

Hilo ndilo lililotakiwa kufanyika, codes za kuingilia kwenye database ya benki zilitakiwa kupatikana haraka iwezekanavyo. Akampigia simu Richard na kumwambia kwamba kulikuwa na kazi kubwa hivyo alitakiwa kupanda ndege haraka sana na kuelekea nchini Kenya katika Jiji la Nairobi.
Ili aaminike, naye Upendo akapewa simu na kuzungumza na Robert na kuambiwa kuhusu Richard kwamba kulikuwa na kazi ilitakiwa kufanyika haraka sana. Akakubaliana naye na siku iliyofuata tu mwanaume huyo akasafiri mpaka nchini Kenya.
Alipofika huko, akakutana na wenzake wawili na kuanza kuongea. Kwanza akaambiwa kuhusu pesa zilizokuwa zimeingizwa kwenye akaunti, zilikuwa nyingi mno kiasi kwamba hata Richard mwenyewe alionekana kushangaa.
“Kwa hiyo?” aliuliza.
Wakamwambia kuhusu msichana aliyekuwa na cheo cha Umeneja Masoko, alikuwa msichana mrembo na mwenye msimamo hivyo walimpigia simu yeye na kumuhitaji kwa sababu walihitaji kwa udi na uvumba kuchukua pesa zile.
Walimpa maelekezo yote na hivyo siku iliyofuata Richard akaondoka na kuelekea huko benki huku akiwa amevalia shati jeupe, tai nyeusi na suruali nyeusi huku miwani ikiwa machoni mwake.
Alipoingia benki tu, wasichana wote wakageuka na kumwangalia. Walichokiona, hawakuamini, uzuri wake ulinogeshwa na miwani aliyovaa, kila aliyemuona alidiriki kusema kwamba Mungu alijua kuumba, walihisi siku ambayo Mungu alimuumba Richard alisema kwamba alihitaji kutengeneza mwanaume mwenye sura nzuri kuliko wote katika dunia hii.
Richard alitembea na kwenda kukaa kwenye kiti na wateja wengine. Wasichana hawakuyatoa macho kwake, walibaki wakiduwaa kwa kumwangalia, wale waliokuwa mapokezi walitamani kumfuata na kumuhudumia, wasichana wengine waliokuwa wakifanya kazi hapo wakawaita wenzao kwa lengo la kumwangalia Richard tu.
Msichana mmoja wa hapo alishindwa kuvumilia, kila alipomwagalia Richard alihisi moyo wake ukiwa na kimuemue cha kutaka kuzungumza na Richard, akaanza kumsogelea na kuongea naye.
“Samahani! Sijui unahitaji huduma gani ya kibenki?” aliuliza msichana huyo huku akimwangalia Richard aliyekuwa akitabasamu tu.
“Nahitaji kuonana na Meneja Masoko!” alijibu.
“Oh! Njoo huku,” alisema msichana huyo.
Richard akasimama na kuanza kumfuata msichana huyo, kwa jinsi alivyokuwa akitembea, kila mmoja alitamani sana kuongozana naye, wafanyakazi wengine wakamuonea wivu mwenzao kwa kuona kwamba alifanikiwa kumchukua Richard, hata kama hakufanikiwa siku hiyo basi angepewa hata namba ya simu.
Walipofika kwenye mlango wa ofisi ya Rachel, kwanza akaingia na kuanza kuongea naye, alimwambia kuwa kulikuwa na mgeni mlangoni, alikuwa mzuri wa sura kupita kawaida, alimtaka hivyo Rachel alitakiwa kutulia asilete mapepe hata kidogo.
“Ni mzuri! Ana uzuri gani?” aliuliza Rachel.
“Wewe acha tu bosi! Huko chini nimeacha balaa, kila msichana anamtaka!” alisema msichana huyo.
“Mmh! Hebu mwambie aingie,” alisema Rachel.
Msichana huyo akatoka na kumwambia Richard aingie. Mwanaume huyo akafanya hivyo, alivyoufungua mlango tu na macho ya Rachel kugongana naye, hapohapo akahisi kama moyo wake ukilegea, akaanza kutetemeka kwa hofu huku kijasho chembamba kikianza kumtoka, mwanaume aliyekuwa akimwangalia alikuwa kama vile alivyoambiwa kwamba ni mmoja wa watu waliokuwa na sura nzuri mno.
“Karibu sana,” alisema Rachel huku akimpa mkono.
Walipogusana tu, Rachel akahisi akipigwa shoti iliyosambaa mwili mzima na kumpa hali ambayo hakuwahi kuihisi hapo kabla.
“Asante sana!” aliitikia Richard na kukaa, alichompagawisha zaidi msichana huyo ni pale alipoanza kumwangalia kwa jicho la mahaba ambalo lilianza kueleza hisia zake kwa msichana huyo.
“Siwezi kuvumilia...” alijisemea Rachel.
***
Rais Kimoni alikuwa kimya, alihitaji kujua kile kilichokuwa kikiendelea. Aliwaambia watu wa benki wazizuie pesa zile kwa kuamini kwamba mtu ambaye alimwambia kuwa alikuwa na picha hizo amtumie na yeye mwenyewe kuzifuta katika simu yake.
Aliambiwa kazi ingefanyika kikamilifu hivyo kitu alichokisubiria kilikuwa ni picha hizo kutumiwa tu. Ilichukua zaidi ya saa moja, hakukuwa na kitu kilichofanyika na alipojaribu kumpigia simu Robinson, haukuwa ikipatikana.
Hakutaka kuwa na hofu, aliamini kwamba picha angetumiwa tu kwa kuwa tayari alimtumia mwanaume huyo pesa na asingeweza kutoa kiasi chote hicho, na kama kweli alihitaji kuzitoa zote alitakiwa kwenda benki ambapo huko angetuma watu na kwenda kumkamata.
Siku hiyo alisikilizia, siku ya pili ilipoingia, alipoona kimya ndipo akajaribu kumpigia simu Robinson kwa lengo la kuzungumza naye lakini simu haikuwa ikipatikana.
Alijua kulikuwa na kitu, akawasiliana na benki, wakamwambia kwamba pesa zilikuwepo kwenye akaunti na haikuchukuliwa hata shilingi moja.
Alichokifanya ni kumtumia ujumbe mfupi Robinson na kumwambia kwamba kila kitu alikamilisha hivyo alitakiwa kumtumia picha hizo na kuzifuta kwa kuwa tu aliheshimu kile alichomwambia.
Baada ya kutuma ujumbe huo, alisubiri mpaka saa moja jingine ndipo akaona ujumbe ukiwa umepokelewa kitu kilichoonyesha kwamba mwanaume huyo aliwasha simu, hapohapo simu yake ikaanza kuita.
Aliyekuwa akipiga alikuwa Robinson, moyo wake ukashtuka, alianza kumuogopa mtu huyo kwani aliamini kwamba angemfanyia jambo moja baya sana kama tu angeruhusu picha zile zibaki kwa wapinzani. Akaipokea harakaharaka.
“Niambie! Umeziona hizo pesa?” aliuliza rais.
“Niliziona tangu jana! Nashukuru sana! Nimeshazichukua, nakutumia picha sasa hivi,” alisema Robinson kutoka upande wa pili.
“Umezkwishazichukua?” alijikuta akiuliza rais huku akipigwa na mshtuko.
“Kwani si zangu! Sasa kwa nini nisizichukue?”
“Basi naomba nitumie hizo picha na uzifute kabisa kwako!” alisema rais.
“Usijali! Nipe dakika kadhaa!”
Rais Kimoni alichanganyikiwa, hakuamini kilichokuwa kikiendelea, Robinson alimwambia kwamba pesa hizo alizichukua, sasa ilikuwaje watu wa benki kumwambia kwamba pesa hizo bado zilikuwa kwenye akaunti hiyo.
Haraka sana akawapigia na kuanza kuongea nao. Walichomwambia ni kwamba pesa hizo bado zilikuwepo kwenye akaunti ile na kile alichoambiwa kwamba zilitolewa ulikuwa ni uongo mtupu.
“Kwa hiyo walionidanganya ni nyie au yeye?” aliuliza.
“Yeye!”
“Basi zirudisheni kwenye akaunti yangu,” alisema rais na kukata simu.
Kichwa chake kilikuwa na mawazo tele, hakujua ni kitu gani hasa kilichokuwa kikiendelea. Alikaa kwa dakika kadhaa, ujumbe wa WhatsApp ukaingia kumaanisha kulikuwa na picha alizokuwa ametumiwa, alipozifungua, zilikuwa picha za Kimeta alizokuwa na msichana Jesca.
Moyo wake ukatulia japokuwa hakuwa na uhakika kama mtu huyo hakubaki na picha, alichokuwa akikisikilizia kilikuwa ni kutoka kule benki na kuambiwa kuhusu pesa hizo.
Baada ya kuona kuna ukimya sana kwa zaidi ya nusu saa, akaamua kupiga simu na kuwauliza. Meneja ambaye alikuwa akizungumza naye alionekana kutetemeka, aliogopa, ni kama alikuwa na kitu alichotaka kumwambia rais lakini aliogopa kufanya hivyo.
“Kuna nini?’ aliuliza rais kwa sauti ya kibabe.
“Mkuu, ni kwamba....”
“Pesa hazipo au?”
“Mkuu! Yaani hatujui nini kimetokea,” alisema mwanaume huyo wa upande wa pili.
“Niambie chochote kile,” alisema.
Jamaa huyo akaanza kumwambia kwamba pesa zilionekana kwenye akaunti hiyo lakini walipoingia kwa lengo la kuzihamisha, hazikuwepo, kulikuwa na mtu aliyezichukua na kuwaachia kivuli cha pesa hizo.
Rais hakujua chochote kile, kwake, taarifa hiyo ilimchanganya kupita kawaida. Ilikuwaje pesa aitume humo, ikae halafu wamwambie kwamba kulikuwa na kivuli, pesa hiyo haikuwepo.
Hakutaka kukubali, ikulu hakukukalika, akaondoka na kuelekea huko benki yeye mwenyewe. Wafanyakazi walijua kilichokuwa kikiendelea, kitendo cha kumuona rais huyo mahali hapo wakajua tu nini kilikuwa kikienda kutokea.
Hakuonana na meneja, alionana na mkurugenzi na kuanza kuongea naye. Kila alichoambiwa, hakikuingia akilini, ilikuwaje pesa hizo ziwe humo na baada ya muda zisionekane? Kwake, lilikuwa jambo lisilowezekana kabisa.
“Atakuwa ni yule mwanaume, yaani amechukua hizo pesa bila benki kujua, kivipi? Alizihamishaje?” alijiuliza rais huku pale kitini alipokuwa akionekana kuchoka mno.
***
Rachel alibaki akimwangalia Richard, hakuamini kama angeweza kukutana na mwanaume aliyekuwa na sura nzuri kama huyo ambaye alikaa mbele yake.
Aliambiwa kwamba alikuwa na shida, kwake, alikuwa tayari kumsaidia kwa kila kitu kwa kuamini kwamba shukrani kubwa na ya kipekee ambayo angempa ingekuwa ni kulala naye.
Kwa jinsi Richard alivyokuwa akiongea, alijiamini kupita kawaida, alimwangalia msichana huyo huku akijifanya kuwa na pesa ya kumiliki kampuni ya Google, alizungumza naye na kitu pekee alichomwambia ni kutaka kufanya biashara na beki hiyo.
Alimwambia mipango yake, japokuwa haikuwa imekamilika lakini Rachel aliona kama imekamilika na kuamini kwamba benki hiyo ingekwenda kufanikiwa sana kama tu wangeungana na biashara ya mwanaume huyo aliyekuwa mbele yake.
“Yaani mtatengeneza mamilioni! Ningependa nionane na mkuu wa kitengo cha IT, manake kwenye biashara hii lazima na wao wahusike,” alisema Richard.
Haraka sana Rachel akanyanyua mkonga wa simu na kupiga upande wa pili ambapo baada ya sekunde kadhaa alikuwa akiongea na mwanamke mmoja, alimuhitaji kwenda ofisini kwake ambapo baada ya kumuona Richard, naye akashtuka.
“Rebecca...karibu sana!” alisema Rachel.
Huyo mkuu wa kitengo cha IT alikuwa msichana mrembo mweupe, mfupi, mwenye wowowo la kuwaiba wanaume za watu, aliyenona miguu na kiuno kilichomegeka.
Alikuwa msichana mzuri ambaye naye aliwatingisha sana wanaume waliokuwa wakifanya kazi humo. Aliitwa ofisini humo, kitendo cha kumuona Richard alishindwa kuamini kama kungekuwa na mwanaume mzuri kama alivyokuwa.
Akaambiwa kuhusu Richard na mwanaume huyo kuanza kumwambia kuhusu biashara yake. Alikubaliwa kwa haraka sana kwa kuwa alikuwa na sura nzuri na ya kuwavutia wanawake.
Walizungumza mengi na baada ya hapo akamuaga Rachel na kuomba kwenda katika chumba cha IT kwa lengo la kuzungumza na wengine.
Kila alichokisema, kilikubaliwa na hivyo kwenda huko. Lengo lake halikuwa kwenda kweli ila alihitaji muda wa kukaa chemba na Rebecca ili azungumze naye.
“Yaani nimeona wanawake wengi katika dunia hii, ila sijaona msichana mrembo kama wewe,” alisema Richard huku akimwangalia msichana huyo usoni.
“Jamani! Kweli?”
“Ndiyo! Unaonekana kuwa msichana wa kipekee sana, mwerevu, mwenye mafanikio makubwa mno. Nimeamua kuja kufanya biashara na nyie ila kuna kitu nataka sana unisaidie, kama ukinisaidia, nakupa elfu hamsini,” alisema Richard huku akimwangalia msichana huyo.
“Kitu gani?”
“Namba ya siri ya database ya hapa kwenu,” alisema Richard maneno yaliyoonekana kumshtua mno Rebecca.
“Namba ya siri ya database?”
“Ndiyo!”
Rebecca akakaa kimya, alimwangalia mwanaume huyo huku akionekana kutokuamini kile alichokisikia. Aliijua namba ya siri ila kila alipojaribu kufikiria kazi ambayo ingefanyika kupitia namba hiyo hakupata jibu zaidi ya kuhisi kulikuwa na mchezo mbaya.
Hakutaka kumwambia, alimkatalia katakata. Alichokifanya Richard ni kukatisha mazungumzo kuhusu database na kumwambia kwamba alihitaji kuonana naye chemba na kuzungumza.
Rebecca alivyoambiwa hivyo akachanganyikiwa, kutoka na mwanaume kama Richard kwake ingekuwa bahati ya mtende kwa marafiki zake na wakatu wengine. Akakubaliana naye na hatimaye wakatoka na kwenda kwenye Mgahawa wa Oswardo ambao ulikuwa maarufu hapo Nairobi na kuanza kuzungumza huko.
Richard akajifanya kumpenda mno Rebecca, alimsifia vya kutosha, alimpamba kwa maneno matamu mno kiasi kwamba msichana huyo akajiona yeye ndiye mwanamke mrembo kuliko wote katika dunia hii.
Walizungumza kwa dakika arobaini na tano huku wakinywa juisi, wasichana mbalimbali waliokuwa wakiingia katika mgahawa huo walipomuona Richard, walichanganyikiwa mno kwani uzuri wake ulionekana kwa kila aliyekuwa akimwangalia.
“Ningefurahi kama ningepata nafasi ya kuwa nawe chumbani leo hii,” alisema Richard kwa kuamini msichana huyo asingeweza kukataa hata kidogo.
Ni kama Rebecca alisikia vibaya, akauliza kile alichoambiwa huku akionekana kutokuamini. Richard alimwambia zaidi kwamba alihitaji kuwa naye usiku wa siku hiyo kwa kuwa alimpenda sana.
Kumkataa mtu kama Richard ulionekana kuwa ujinga wa hali ya juu, kwa kutumia pesa zake mwenyewe, akakubali na kuchukua chumba.
Hicho ndicho alichokitaka Richard, alifanikiwa kulala naye, alimuonyeshea mapenzi ya usiku mmoja kiasi kwamba msichana huyo alichanganyikiwa. Hakuishia hapo, akaahidi kumuoa kama tu angekuwa tayari kumwambia kila kitu alichotaka kuambiwa na kumuonyeshea uaminifu wote.
Rebecca alikubali kwa asilimia mia moja na hata alipoulizwa kuhusu namba ya siri, hakuwa na jinsi, akakubaliana na mwanaume huyo kwamba iwe siri na asimwambie mtu yeyote yule kama alimwambia kuhusu jambo hilo la siri.
Alichokiamini Rebecca ni kwamba mwanaume huyo angemuoa na kuishi naye kwa raha kabisa kumbe mwenzake alimfuata kwa sababu tu kulikuwa na namba za siri alizokuwa akizihitaji.
Usiku huo wakaonyesheana mapenzi motomoto na walipoachana tu, Richard akamtumia namba Robinson ambaye akaanza kufanya kazi ya kuingia katika database ya benki hiyo.
“Hureeeeee....” Robinson alipiga uyowe mkubwa.

JE, nini kitaendelea?
 
NYEMO CHILONGANI.
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Kumi na Saba

Hakukuwa na muda wa kuchelewa, haraka sana Robinson akaingiza codes zake na kufanikiwa kuingia ndani ya database hiyo kwa kutumia namba za siri alizokuwa amepewa na Richard. Kazi hiyo ndiyo ilikuwa ngumu kuliko zote, kitendo cha kupata namba hizo zilimaanisha kwamba alikuwa na uwezo wa kufanya kitu chochote kile.
Kwenye database hiyo akatafuta akaunti yao, alipoiona, akaziona pesa hizo ila hazikuwa na uwezo wa kutoka hata kidogo. Hiyo ilikuwa kazi ndogo, alikuwa mtundu kupitiliza hivyo alichokifanya kilikuwa ni kuweka virusi vyake kwa ajili ya kuuharibu mfumo mzima kwa dakika kadhaa, azitoe pesa hizo na kuziweka katika akaunti yao iliyokuwa nchini Tanzania.
Hicho ndicho alichokifanya, haraka sana wakati virusi wakiwa wameanza kushambulia mfumo huo, huku akawa anafanya kazi yake ya kuhamisha pesa hizo.
Robert alikuwa pembeni yake, alibaki akishangaa tu, aliiangalia kompyuta ya Robinson na kazi iliyokuwa ikifanyika lakini hakuweza kupata kitu chochote kile, kwake vilionekana vitu ambavyo havikueleweka hata kidogo.
Alifanikiw akuhamisha pesa hizo ila hakutaka kuondoa kivuli, alihitaji watu wa benki watakapoangalia waone kuna pesa lakini baada ya kuingia kwa ndani wakute kukiwa na shilini 0.00.
“Huu ulikuwa mchezo mdogo sana,” alisema Robinson.
Kwa kuwa aliamini kwamba pesa hizo zingeweza kuonekana mahali zilipokwenda, akapata kazi nyingine ya kuharibu mawasiliano na baadaye kuufanya mfumo mzima wa kuhamisha pesa usomeke kwamba pesa zilitumwa kuelekea kwenye akaunti ya chama tawala cha nchi hiyo.
“Nimemaliza. Pesa zimekwishaingia,” alisema Robinson huku akionekana kuwa na furaha.
“Zimekwenda wapi sasa?” aliuliza Robert.
“Kwenye akaunti yetu!”
Hiyo haikutosha, kiasi ambacho alikituma huko kilikuwa kikubwa sana, watu wa benki wangeweza kuhoji kuhusu pesa hizo kitu ambacho alihisi kingewaweka matatani.
Mchezo alioucheza ulikuwa mdogo tu, akaziacha pesa hizo lakini akaweka loki kwamba watu wa benki kama wangeingia kwenye akaunti yao, kiasi cha pesa ambacho wangekikuta kingekuwa kilekile kumbe kulikuwa na pesa nyingine ambazo hazikuweza kuonekana mpaka pale ambapo wangeanza kufanya yao.
“Kwa hiyo hizo tuzifanyaje?” aliuliza Robert.
“Tutatakiwa kusafiri kuelekea nchini Marekani, huko tutafungua akaunti na tutaziingiza hizi pesa, hata tukizutuma huku kutakuwa hakuna maswali yoyote yale, tena kule kuna mambo mengi tutayafanya nitawaambia tukifika huko,” alisema Robinson.
Robert akabaki kimya akimwangalia rafiki yake huyo, alimshangaa lakini alimshukuru Mungu kwa kumkutanisha na mtu kama huyo. Alikuwa na akili kubwa mno, kitendo cha kuhamisha pesa hizo na kwenda kwenye akaunti yao huku akiwaambia kwamba hata benki wenyewe wasingejua kilimshangaza sana.
Baada ya saa moja, Richard akarudi na kuuliza kuhusu kilichoendelea. Akaambiwa kila kitu kwamba mchezo ulikamilika na pesa hizo zilikuwa mahali salama kabisa.
“Kwa hiyo mkwanja wote umeingia?” aliuliza Richard huku akionekana kushangaa.
“Ndiyo! Naomba simu nimpigie Oyoyo,” alisema Robinson na kupewa simu yake.
Hawakwenda nchini Kenya kuuza sura bali walikwenda huko kwa ajili ya kutengeneza pesa na kurudi nchini Tanzania. Robinson akawasiliana na Oyoyo na kumwambia kwamba picha walizokuwa wakizihitaji walikuwanazo hivyo kama walitaka basi walitakiwa kuwapa dola laki mbili kwa ajili ya kuwaachia picha hizo.
Kilikuwa kiasi kikubwa sana, si kwamba asingekipata, alikuwa na uhakika wa kukipata kwa muda mfupi lakini kiasi chote hicho kukitoa kwa mtu mmoja lilionekana kuwa jambo gumu.
Hakumficha, alimwambia ukweli, naye Robinson akamwambia kwamba kama suala hilo lilikuwa gumu basi wangekwenda kwenye kesi hiyo bila kuwa na ushahidi na hivyo Bwana Kimeta angeachwa huru kwa kuwa ushahidi ulikosekana.
“I will call you,” (nitakupigia) alisema Oyoyo na kukata simu.
Kichwa chake kilichanganyikiwa, mwanaume aliyeongea naye alionekana kuwa mtu hatari ambaye hakuonekana kuwa na masihara hata kidogo. Alichokigundua ni kwamba mwanaume huyo alikuwa Mtanzania kutokana na lafudhi yake ilivyokuwa katika kutamka baadhi ya maneno ya Kiswahili vizuri kabisa.
Akawaambia wenzake, nao walichanganyikiwa kama alivyochanganyikiwa. Walijadili suala hilo huku wakimshirikisha Jesca na mwisho wa siku kukubaliana kwamba wamtumie pesa mwanaume huyo kwa ajili ya kutumiwa picha hizo.
“Lakini kweli hatuwezi kuzipata pasipo kumtumia pesa?” aliuliza mwanaume mmoja.
Walikaa na kujadili kwa kipindi kirefu mno na mwisho wa siku wakakubaliana kwamba wachukue begi lililokuwa na pesa hivyo na kuondoka nalo kuelekea katika maduka ya Westgate Shoppig Mall yaliyokuwa hapo Nairobi.
Maduka hayo yalikuwa ni kama Mlimani City, ndiyo ambayo Jumamosi ya tarehe 21 mwaka 2013 yalivamiwa na wanamgambo wa kigaidi wa Al Shabaab na kuwaua baadhi ya watu na kutoroka.
Humo ndipo ambapo Oyoyo na wenzake walijadiliana kwamba ni lazima makabidhiano yafanyike huko ili kama itawezekana basi waweze kumkamata mtu huyo na kumfungulia mashtaka.
Baada ya kukubaliana, Oyoyo akampigia simu Robinson na kumwambia kuhusu jambo hilo. Kwanza akashtuka, kitendo cha kuambiwa kwamba makabidhiano yakafanyie huko Westgate Shoppig Mall kukamtia hofu kwa kuhisi kulikuwa na jambo moja kubwa lilitakiwa kutokea huko.
Alimwambia Oyoyo kuhusu jambo hilo, hofu aliyokuwanayo kwamba inawezekana mwanaume huyo alipanga mikakati ya kuhakikisha wanamkamata lakini Oyoyo alimwambia kwa sababu kiasi alichokihitaji kilikuwa ni kikubwa mno basi ilikuwa ni lazima waende huko na kukabidhiana.
“Mkileta polisi?”
“Hatuwezi kufanya hivyo kwa sababu mna picha za ushahidi! Naomba tuonane huko, sisi wenyewe hatukuamini, tukionana sehemu ambayo ni tofauti na huko unaweza kutuma watu wamteke mletaji halafu useme hukuzipata,” alijitetea Oyoyo.
“Sawa. Iwe kesho, majira ya saa kumi jioni, nitakwambia mahali pa kuziweka humo ndani,” alisema Robinson na kukata simu.
Aliwaambia wenzake kile alichoambiwa, wote wakacheka, waliambiwa jambo la kitoto sana, walihisi kwamba kulikuwa na mtego mkubwa ambao mwanaume huyo alitaka kuutumia lakini kwa sababu waliamini kwamba wao walikuwa na akili kubwa, wakakubali na hivyo kujipanga tayari kwa kwenda kuchukua pesa huko.
Walitakiwa kwenda Westgate, wakaone jinsi mazingira yalivyokuwa. Kwa kuwa ilikuwa ni mchana, wakaelekea huko na kuanza kuangalia huku na kule jinsi mambo yalivyokuwa humo ndani. Watu walikuwa wengi humo, ilikuwa ni Ijumaa ambayo kulikuwa na watu ambao waliamua kufanya manunuzi ili wikiendi wasitokea.
Walizunguka huku na kule na kuona sehemu ambayo waliamini kwamba kama pesa zingewekwa hapo na wao kwenda kuzichukua, basi ilikuwa ni lazima waonekane na kukamatwa.
“Nadhani pesa ziwekwe pale karibu na ule mlango ulioandikwa emergency,” alisema Robert.
“Halafu?”
“Nina wazo moja, kama kuna mwingine mwenye wazo jingine aseme tuone lipi zuri,” alisema Robert.
Akaanza kuwaambia kuhusu mpango wake. Alichokifikiria ni kwamba wafanye kila liwezekanalo kuhakikisha wanamtafuta mtu anayehusika na umeme ndani ya jengo hilo, kwa maana ya kwamba walitakiwa kuzima umeme wa jengo zima na kwa sababu humo hakukuwa na madirisha, kulikuwa na milango tu kama Mlimani City basi ingekuwa rahisi kuwa na giza kubwa na hivyo kuchukua pesa hizo na kuondoka nazo,” alisema Robert huku akiwaangalia wenzake.
“Ila napo kuna tatizo katika hilo,” alisema Robinson.
“Lipi?”
“Nje kuna mwanga. Huoni kama mtu ukiondoka na hilo begi utaonekana ukifika kwenye mwanga hata kama ndani kuna giza?” aliuliza.
“Atakayechukua begi hilo hatopitia mlango wa mbele, atapitia ule wa emergence,” alijibu Robert.
“Napo huko kuna mwanga. Nahisi tuangalieni jingine, yaani nataka hizi pesa zichukuliwe kitaalamu mpaka washangae,” alisema Robinson.
“Mimi nina wazo!” alisema Richard.
“Lipi?”
“Tufanyeni kila liwezekanalo tukarekodi milio ya risasi halafu tuje na flashi ambapo kwa ndani kutakuwa na sauti hizo za risasi,” alisema Richard huku wenzake wakimwangalia.
“Halafu!”
“Tukifika humu, kwa sababu kuna sauti ya muziki inasikika, bila shaka kuna sehemu ambapo hii miziki inabadilishwa, tujue ni sehemu gani, humo ndipo ambapo mmoja wetu atakwenda na kuweka hii flashi na kuanza kusikika hiyo milio ya risasi,” alisema Richard.
“Mh!”
“Ni wazo langu.”
“Halafu watu wakisikia milio ya risasi inakuwaje?” aliuliza Robinson.
“Yaani cha kwanza tutazima taa, kutakuwa na giza, watu si watajua ni kawaida umeme umekatika, halafu ghafla tunapiga kelele kwamba kuna mtu ana bunduki, watu wakitaharuki, yule aliyekuwa kwenye chumba cha kubadilishia muziki ataweka flashi na kuanza kupiga kelele za risasi. Hebu fikiria, mtu anasema kuna watu wa bunduki, ghafla umeme unazima na milio ya risasi kusikika huku kukiwa na giza, kuna mtu atabaki kweli ndani?” aliuliza Richard.
“Mh! Hakuna!”
“Na kwa sababu bado Wakenya wanaogopa uvamizi wa Al Shabaab ni lazima watakimbia kuelekea nje. Wakati watu wakikimbia, tunachukua begi letu, tunapita mlango huo wa dharura na kuondoka huku ndani kukiwa na varangati,” alisema Richard.
“Mh! Hilo wazo lako kiboko,” alisema Robert.
“Naomba tufanye hivyo! Tukifanikiwa katika hilo, basi pesa tumechukua na kusepa zetu,” alisema Richard.
“Sawa.”
Wakati hayo yote yakiendelea kupangwa, walikuwa wamekaa kwenye viti vyao wakiendelea kuyajenga. Kila mtu aliyekuwa akipita hapo aliwaangalia, kitu kilichowafanya watu kuangalia sana ni uzuri aliokuwanao Richard.
Wasichana wengine hawakutaka kupita, walisimama pembeni na kuanza kumwangalia Richard, alikuwa mzuri wa sura kiasi kwamba walihisi kuchanganyikiwa. Walitamani japo mwanaume huyo awasalimie tu lakini hakutaka kujirahisisha namna hiyo.
Baada ya kukubaliana, kitu cha kwanza kilikuwa ni kuonana na mtu ambaye alihusika katika kubadilisha nyimbo zilizokuwa zikisikika humo na kuongea naye. Waliulizia na kuambiwa mahali alipokuwa. Wakaondoka na kumfuata, walipoonana naye wakamuita pembeni na kuzungumza naye.
Walijua jinsi Waafrika tulivyokuwa, kwenye mambo ya pesa walikuwa tayari kufanya jambo lolote lile. Walimwambia kuhusu kubadilisha sauti za muziki kwa sekunde kumi tu, yaani wanabadilisha muziki na kurudisha kama zamani.
Hawakutaka kumwambia ukweli kwa kuhisi kwamba angekataa. Walimdanganya kwa kumwambia kwamba mmoja kati yao mpenzi wake alikuwa akitimiza miaka ishirini na walitaka kumfanyia sapraizi mahali hapo, yaani watoe sauti za muziki wa kawaida na waupige muziki wa siku ya kuzaliwa ambao ulikuwa kwenye flashi yao.
Hilo halikuonekana kuwa tatizo hata kidogo, lilikuwa jambo dogo mno kwani haikuwa mara ya kwanza, Wakenya walikuwa wakifanya mambo hayo mara kwa mara humo hivyo akakubaliana nao na hivyo kumlipa kiasi cha shilingi elfu ishirini na kuondoka zao huku wakimwambia kwamba kesho wangerudi. “Hakuna tatizo!” alisema.
“Sawa. Nitakuja kesho,” alisema Robonson.
Baada ya kumaliza hilo, wakaondoka na kuanza kutafuta sehemu ya kuzima umeme jengo zima. Kwanza walitaka kujua kama jengo lingezimika, jenereta lingechukua muda gani mpaka kujiwasha.
Hilo walitakiwa kulifanya wenyewe, walimuuliza dada mmoja aliyekuwa na duka humo na kumwambia kwamba walikuwa mafundi umeme na hivyo walitaka kuona swichi ya kuzima jengo zima ilikuwa wapi, kwa kuwa alijua ilipokuwa, akawaonyeshea na hivyo kwenda huko.
Ilikuwa katika njia ya kuelekea chooni, kwa pembeni karibu kabisa na ofisi ya meneja mkuu wa hilo jengo. Walichokifanya, pasipo kuogopa kitu chochote kile, Robinson akaizima na kukimbia kuelekea chooni huku wakiangalia saa zao.
Ni ndani ya sekunde kumi tu, jenereta likawaka na hivyo kujua kwamba mara umeme unapokatika, huchukua sekunde kuanzia tano mpaka saba kwa jenereta kujiwasha, hivyo walitakiwa kufanya haraka sana.
“Tuna sekunde tano za kurekebisha kila kitu, twendeni tukajipange na kesho turudi kikazi. Ni lazima hizi pesa tuondoke nazo, cha msingi tuwaambie wazipeleke karibu na duka la Tecno, umeme ukizimika na milio ya risasi kusikika, mmoja anakwenda kulichukua, anatokea mlango wa dharura na kuondoka nalo, sawa?” alisema Robinson na kuuliza.
“Sawa.”

Je, nini kitaendelea?
Mpango utakamilika?
 
NYEMO CHILONGANI.
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Kumi na Nane.

Walipofika hotelini, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuanza kurekodi sauti za milio ya risasi, hilo halikuwa tatizo, ilikuwepo nyingi sana kwenye mitandao na hivyo kuichukua na kuiweka kwenye flashi na hivyo kupanga mikakati ya kukamilisha jambo lao siku ya kesho ambayo ilikuwa ni Jumamosi iliyokuwa na watu wengi mno hapo Westgate Shopping Mall.
Asubuhi ya siku hiyo ilipofika, kitu cha kwanza kilikuwa ni kuzungumza na Oyoyo, Robinson alimwambia mahali pesa hizo zilipotakiwa kuwekwa, hilo halikuwa na tatizo, mwanaume huyo akawapanga watu wake na kuwaambia kila kitu na hivyo ilivyofika majira ya saa tisa kuanza kuelekea huko.
Robinson na wenzake walikwishafika humo. Walikaa kwa kutengana huku macho yao yakiwa mahali pale walipotaka pesa hizo ziwekwe. Walimuona mwanaume mmoja akielekea pale, akaangalia huku na kule na kuziweka pesa zile zilizokuwa kwenye begi na kuondoka.
Waliangalia huku na kule, waliwaona baadhi ya vijana wakisogea karibu na kule, walijua kabisa kwamba hao walikuwa miongoni mwa watu waliotaka kuona ni nani ambaye angekwenda kuchukua lile begi, wamkamate na kuondoka naye.
Ulikuwa ni mchezo wa kitoto sana, wakaacha na Robinson kuanza kuelekea kule kwa jamaa anayebadilisha nyimbo huku akiwa na flashi yake. Alitembea kwa kujiamini huku akiwa na kofia yake kichwani kwa ajili ya kujizuia na kamera za CCTV zilizokuwa mahali hapo.
Alipofika huko katika chumba cha kubadilishia miziki, akakutana na kijana yule aliyeonana naye jana na kuanza kuzungumza. Alimchangamkia kana kwamba walifahamiana miaka mingi iliyopita.
Wakaanza kuongea na Robinson kuchukua simu yake na kumwambia kijana yule alihitaji kuzungumza na mtu ambaye alikuwa humo na mpenzi wake ili ajiandae kumfanyia sapraizi hiyo.
Simu ikapokelewa na Robert na kuanza kuzungumza naye. Iliunganishwa mpaka katika simu ya Richard na hivyo watatu kuanza kuwasiliana.
Robinson alikwenda pembeni kidogo ili mazungumzo yake naye yasisikike na jamaa huyo. Alimwambia Robert kuwa alitakiwa kusogea kule kulipokuwa na begi lakini pia Richard alitakiwa kujifanya akienda chooni, yeye ndiye ambaye alitakiwa kuzima taa baada ya kusikia Robert akipiga kelele kwamba kulikuwa na mtu aliyekuwa na bunduki humo ndani.
“Haina shida! Weka flashi kabisa,” alisema Robert.
Baada ya kumaliza, hakukata simu, alimwambia jamaa kwamba alihitaji kuweka hiyo flashi, baada ya kuruhusiwa na kuiweka, akamwambia Robert aanze kupiga kelele kwa kudai kwamba kulikuwa na mtu aliyekuwa na bunduki ndani ya jengo hilo.
“Somebody got gun....somebody got gun....” (kuna mtu ana bunduki...kuna mtu ana bunduki...) alipiga kelele Robert, sauti ambayo ilisikika na kila mtu mahali hapo.
Watu wakaogopa, kumbukumbu za mwaka 2013 zikaanza kuwajia vichwani mwao, walichohisi ni kwamba wanamgambo wa Al Shabaab walivamia tena hivyo kujianza kukimbia.
Wakati wakiwa wametajaruki huku wakiangalia kila upande na Robert akiendelea kupiga kelele, mara ghafla milio ya risasi ikaanza kusikika kutoka kwenye spika zilizokuwa humo, hakukuwa na mtu aliyejua mahali zilipotoka, kwa kuwa hilo lilikuwa duka kubwa watu wakaanza kukimbia hovyo.
Wakati wakikimbia kuokoa maisha yao, ghafla umeme ukazimika kitu kilichowachanganya zaidi watu na kuhisi kwamba kweli kulikuwa na ugaidi humo na ndiyo maana baada ya milio ya risasi kusikika kwa wingi, umeme ukakatika.
Hakukuwa na mtu aliyegundua kwamba zilikuwa ni spika, Robert aliposema kwamba alimuona mtu akiwa na bunduki, na milio ya risasi kusikika na ghafla umeme kukatika, hakukuwa na mtu aliyebaki, kila mmoja akaanza kukimbia huku kukiwa na giza.
Wale waliokuwa kwenye maduka ya bidhaa wakatoka na kuanza kukimbia, wengi waliumia kwa kujigonga, watoto walianza kulia na hakukuwa na mtu aliyebaki mahali hapo, mpaka wauzaji wenyewe walianza kukimbia hovyo.
Hiyo ndiyo ilikuwa nafasi yenyewe, kulikuwa na giza lakini macho ya Robert yalikuwa makini mno, haraka sana akalisogelea lile begi, akalichukua, akaufungua mlango wa dharura na kutoka huku akiwa na begi lile.
Wanaume wale ambao walikuwa ndani humo kwa lengo la kumuona mtu ambaye angechukua begi hilo nao walitimua mbio, waliogopa kufa, walichanganyikiwa, walijua ni kweli kwamba kulikuwa na mtu aliyekuwa na bunduki ambaye alianza kushambulia.
Haraka sana kwa kutumia mwanga wa simu yake Robinson akatoka katika kile chumba na kukimbia, akaungana na Richard na kutoka nje ambapo wakaunganisha mpaka nyuma, wakakutana na Robert aliyekuwa na begi lenye pesa, wakachukua teksi moja na kuondoka huku wakiwa wamefanikiwa kwa kile walichokitaka.
Polisi walikusanyika nje ya maduka hayo huku wakiwa na bunduki, nao wenyewe waliogopa kuingia ndani, waliambiwa kulikuwa na magaidi humo ndani, walijua wanamgambo wa Al Shabaab walivamia tena na kufanya mashambulizi.
Hakukuwa na mtu aliyeingia, kila mmoja alibaki nje huku akiogopa, walisimama mbali kabisa kwa kuamini kwamba kweli mule ndani kulikuwa na magaidi kumbe hakukuwa na kitu.
Hapo nje walikuwa wakisikilizia, hawakutaka kuingia, walihitaji wanajeshi wafike kwani wao ndiyo waliokuwa wazoefu zaidi, baada ya dakika ishirini, wakafika makomandoo ambao wakaanza kuingia ndani kikomandoo huku wakiwa na magwanda yao na bunduki nzito na kali mikononi mwao.
Walitembea kwa machale huku wakiangalia kila upande, hawakufanikiwa kuona mtu yeyote wala maganda ya risasi, kama kweli risasi zilipigwa mfululizo ilimaanisha kwamba wangekutana na maganda lakini kitu cha ajabu kabisa kulikuwa peupe.
“Mbona hakuna mtu, hata damu?” aliuliza mwanajeshi mmoja huku akiangalia kila upande.
“Hata mimi nashangaa! Walisema kwamba kulisikika milio ya risasi, mbona hata maganda hakuna?” aliuliza mwingine.
Siku hiyo ilikuwa ni habari kuhusu uvamizi huo tu, kwenye vyombo vya habari kulikuwa na taarifa kuhusu tukio hilo kiasi kwamba hata Al Shabaab wenyewe waliposikia, walitoa taarifa na kusema kwamba hawakuhusika katika shambulio hilo.
Wakati hayo yote yakiendelea, Oyoyo alijaribu kuzungumza na vijana wale waliokwenda huko Westgate Shopping Mall na kuwauliza kuhusu kile kilichotokea. Vijana hao walimwambia kila kitu kwamba walikwenda kuweka begi lile lililokuwa na pesa na baada ya dakika kadhaa wakaanza kumsikia mwanaume mmoja akipiga kelele kwamba kulikuwa na mtu aliyekuwa na risasi, ghafla umeme ukakatika na milio ya risasi kuanza kusikika.
“Kwa hiyo?” aliuliza Oyoyo.
“Tukakimbia.”
“Mlirudi?”
“Ndiyo! Ila begi halikuwepo,” alisema Oyoyo.
Huko alipokuwa akashika kichwa, tayari akili yake ilimwambia kwamba pesa hizo zilichukuliwa na mwanaume huyo na iliwezekana kabisa kuhusu suala la uvamizi, hakukuwa na uvamizi wowote ule.
Akafuatilia taarifa ya habari, alihitaji kujua kila kitu kilichotokea kama kulikuwa na maganda ya risasi yalipatikana, alipouliza, aliambiwa hakukuwa na kitu chochote kile, yaani hakukuwa na dalili zozote zile za uvamizi ndani ya jengo hilo.
Akawapigia simu wenzake na kukutana, wakaanza kuzungumza suala hilo, hakuwaficha, aliwaambia ukweli kwamba hawakufanikiwa kumkamata kijana huyo kwa sababu alisababisha vurumai ndani ya jengo hilo na kuchukua pesa hizo.
“Mmh! Sijaelewa, yaani kivipi?” aliuliza mwanaume mmoja.
“Humo hakukuwa na uvamizi wowote ule.”
“Lakini wanasema kwamba milio ya risasi ilisikika!”
“Hakuna kitu!”
“Sasa hiyo milio ni ya nini?”
“Hebu subiri! Nahisi kuna kitu.”
Kichwa cha Oyoyo kilichanganyikiwa, alifikiria mambo mengi mno, akawachukua watu wake na kuelekea kwenye duka hilo, walisema kwamba kulisikika milio ya risasi, kama kweli hakukuwa na maganda ya risasi yaliyopatikana inamaana kulikuwa na njia nyingine ambayo ilitumika.
Akili yake ilimwambia mtu aliyekuwa akihusika na kubadilisha miziki ndani ya jengo hilo alikuwa akihusika hivyo kuonana naye na kuanza kuzungumza.
Kijana huyo alimwambia ukweli kwamba kulikuwa na mtu alimfuata akiwa na wenzake, alimwambia kwamba kulikuwa na msichana alikuwa na sherehe ya siku ya kuzaliwa hivyo walitaka kumfanyia sapraizi.
Alimwambia kila kitu, hakutaka kumficha. Oyoyo na wenzake walibaki wakimsikiliza tu na mwisho wa siku wakakubaliana kwamba walishindwa kumpata kijana huyo kwa kuwa aliwatoka katika hatua ya mwisho kabisa.
“Watanzania! Watanzania! Watanzania!” alisema Oyoyo huku akionekana kuchanganyikiwa. Pesa nyingi ambazo hakutaka kabisa kuona zikiondoka, zilichukuliwa katika mazingira ya kutatanisha na kubaki mikono mitupu.
***
Vijana watatu hatari, wazee wa mipango, vijana wasioshindwa na kitu chochote kile walikuwa ndani ya teksi wakirudi hotelini. Hawakuzungumza kitu chochote kile, walikuwa kimya huku wakiangalia nje ya gari hiyo.
Ilikwenda mpaka walipofika hotelini ambapo wakateremka na kumlipa pesa yake dereva teksi na kuingia ndani. Kila mmoja alikuwa na furaha, hakukuwa na mtu ambaye aliamini kwamba wangeweza kupata kiasi kikubwa cha pesa.
Hizo dola laki tano zilikuwa pesa nyingi mno, ni zaidi ya bilioni moja kwa pesa za Kitanzania. Walitakiwa kuondoka na kuiweka pesa ile kwenye benki, lakini haikutakiwa kuwa ya Tanzania, walitakiwa kuzibadilisha kwa mfumo wa dola na kuziweka katika akaunti yao.
Chumbani, begi likafunguliwa, walikuwa na mpango wa kuzibadilisha kuwa kwenye pesa ya Kimarekani lakini kitu kizuri kabisa tayari pesa hizo zilibadilishwa na hivyo kuwa na kazi nyepesi mno kwao.
Wakakumbatiana na kupongezana kwamba kazi kubwa waliyotakiwa kuifanya nchini Kenya ilikamilika na hivyo walitakiwa kuondoka kurudi Tanzania.
“Ila bado Kimeta!”
“Achana naye. Kwa hizi pesa tulizozipata, nadhani tumefanikiwa. Tuondokeni. Ngoja niwatumie hizi picha, kwa ishu ya Kimeta kumbaka yule msichana, acha apelekwe jela tu, sisi hatutoshughulika na ishu yake,” alisema Robinson na kumtumia Oyoyo zile picha huku akimshukuru sana kwa pesa alizoziweka kwenye begi kwani zilifika mikononi mwao salama kabisa.
“Ni kweli nyie ndiyo mliosababisha vurumai ndani ya Westgate?” aliuliza Oyoyo.
“Inawezekana! Ila pesa tamu sana. Siku nyingine kukitokea tatizo, usisite kuwasiliana nami,” alisema Robinson na kukata simu. Siku hiyohiyo wakaanza safari ya kurudi nchini Tanzania huku wakiwa wamepiga pesa za kutosha huko Kenya.
 
NYEMO CHILONGANI.
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Kumi na Tisa.

Upendo aliridhika, kitendo cha kuwa na Richard kilimpa moyo kwamba hatimaye alifanikiwa kupata alichokipata. Chuo kizima kilijua kwamba wawili hao walikuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi, alimpenda mwanaume huyo kiasi kwamba hakutaka kuona mtu yeyote yule akienda na kulivunja penzi lao.
Alikuwa radhi kufanya kitu chochote kile lakini si kuona akimkosa mwanaume huyo. Kulikuwa na wanawake wengi waliomfuata Richard na alijua kupambana naye, si kwa kuwafuata bali hata kuwatumia watu waliokwenda na kuwapiga mikwara mingi.
Kwa penzi la Richard alikuwa radhi kufanya chochote kile, kuua kwake halikuwa jambo gumu, ilimradi alijua kwamba alipambana kuhakikisha penzi lake na Richard linadumu, hakujali kitu chochote kile.
Aliagwa na Richard kwamba alikuwa akienda nchini kenya, aliambiwa na Robinson kuhusu kuhitaji kwa mwanaume huyo lakini moyo wake haukuwa na amani hata kidogo, alihisi kabisa kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea katika maisha ya watu hao.
Iliwezekana kabisa kwamba walikuwa wakimtumia mpenzi wake kwa ajili ya mambo ya kipumbavu na ndiyo maana alitamani kuwaambia ukweli kuhusu kumuacha mpenzi huyo ili aendelee kumfaidia.
Siku zikakatika mpaka ile ambayo Richard na wenzake wakarudi nchini tanzania na kuomba kukutana naye. Alijua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea kutokea huko, alikuwa na uhakika kwamba watu hao walipata pesa zake hivyo alitakiwa kuachana na Richard.
Hakukubali hata kidogo, ilikuwa ni lazima apambane kuhakikisha jambo hilo halikubaliki hata kidogo. Kwake, pesa hazikuwa na umuhimu wowote ule, alichokuwa akitaka kuwa nacho maisha yake yote ni Richard tu na si mtu mwingine.
Vijana hao walitaka kukutana na Upendo kwa kuwa Richard alichoka, hakuwa huru, Upendo alikuwa king’ang’anizi mno, kila wakati alitamani kuona akiwa na mwanaume huyo lakini si kuona akiondoka mikononi mwake.
“Najua mnajua jinsi yule demu alivyokuwa mbaya,” alisema Richard huku akiwaangalia wenzake.
“Ndiyo maana tukasema tukamlipe pesa zake ili akuache kwa sababu hatuna muda wa kuendelea kubaki nchini Tanzania, ni lazima tuondoke kuelekea Marekani mwezi huu,” alisema Robinson.
“Naomba kitu cha kwanza tumuite, tumlipe pesa zake na mimi niendelee na maisha yangu,” alisema Richard.
Hiyo ndiyo ilikuwa sababu ya kuwasiliana na Upendo kwa lengo la kuonana naye. Hilo halikuwa tatizo, wakaonana katika Mgahawa wa Samaki Samaki na kuanza kuzungumza naye.
Walimwambia ukweli, maneno yao yalikuwa kama msumali wa moto moyoni mwa Upendo, hakuamini alichokisikia, wakati mwingine alitamani sana kuona kila kitu kilichokuwa kikiendelea kuwa kama ndoto.
Moyo wake uliuma mno, alimwangalia Richard, hakutaka kumuacha, alitamani kuona akiendelea kuwa naye. Aliamini kwamba kiasi cha pesa ambacho aliwaazima watu hao kilikuwa kikubwa kiasi kwamba wasingeweza kukipata ndani ya muda mfupi namna ile.
Hilo lilimpa maswali mengi kichwani mwake, kama kweli watu hao walipata kiasi hicho kikubwa ndani ya mwezi tu, je, walikuwa wakifanya biashara gani ya siri kiasi cha kuwaingizia pesa hizo.
“Kwa hiyo sasa tunataka uachane na Richard, tunakulipa pesa yako sasa hivi,” alisema Robinson huku akimwangalia Upendo aliyeonekana kutia huruma mno.
“Ila mbona mnanikatili hivi?”
“Tunakukatili? Kivipi?”
“Kwa sababu tulikubaliana ni baada ya miaka mitano,” alisema Upendo.
“Hapana! Tulikubaliana ndani ya miaka mitano. Hata mwezi huu mmoja pia upo ndani ya miaka hiyo mitano,” alisema Robinson.
Kwa Upendo lilikuwa sula gumu kumuingia kichwani, katika vitu ambavyo hakutaka kabisa kuona vikitokea ni kuachana na mwanaume huyo.
Alizungumza nao lakini hawakutaka kumuelewa, walimwambia kuhusu mpango wao wa kusafiri na kuelekea nje ya nchi, hawakutaka kubaki nchini Tanzania kwa sababu kulikuwa na mambo walihitaji kuyafanya kwa ajili ya kuingiza pesa zaidi.
Japokuwa hakupenda lakini hakuwa na jinsi, mwisho kabisa Upendo akakubaliana nao lakini alihitaji kuzungumza na Richard kwa sababu kulikuwa na kitu muhimu sana alihitaji kumwambia.
Richard hakujua kilikuwa kitu gani, akakubali na hivyo kwenda pembeni na kuanza kuzungumza. Alichomwambia ni kwamba alikuwa na mimba yake, alihisi dalili zote na alifurahi sana kuona akiwa amepata mimba hiyo kwa kuwa yeye ndiye alikuwa mwanaume aliyempenda kuliko wote katika dunia hii.
“Una mimba yangu?” aliuliza Richard huku akimwangalia Upendo.
“Ndiyo!”
“Unamaanisha nini? Yaani unajua sijaelewa?” aliuliza Richard huku akimwangalia msichana huyo.
“Kwani mtu akiwa na mimba yako huwa anamaanisha nini?” aliuliza Upendo,
“Kwa sababu tulikuwa tunatumia kinga kila siku!”
“Lakini unakumbuka siku ambayo kinga ilipasukia ndani?” aliuliza Upendo.
“Nakumbuka! Lakini pia....”
“Richard! Nina mimba yako,” alisema Upendo na kuondoka mahali hapo.
Richard alibaki akiwa amesimama, hakuamini kilichokuwa kikiendelea, alikumbuka kabisa kwamba siku ambayo kinga ilipasukia ndani hakumwaga mbegu zake ndani ya mwanamke huyo, sasa ilikuwaje amwambie kwamba alikuwa na mimba?
Alijifikiria mengi, alijiuliza maswali ambayo hayakuwa na majibu yoyote yale. Upendo akawaambia wamtumie pesa hizo hivyo Robinson kumwambia kwamba siku inayofuata angekwenda benki na kumuhamishia kiasi hicho cha pesa, hivyo akaondoka zake.
Robinson na Robert walimwangalia Richard, kwa jinsi alivyoonekana ilionyesha kulikuwa na tatizo lililotokea, wakamuuliza na yeye kuwaambia kila kitu alichoambiwa na msichana huyo kwamba alikuwa na mimba yake.
Hakuwaficha kitu chochote kile, aliwaambia kuhusu kinga, kama alivyoshangaa yeye hata watu hao nao walishangaa, ilikuwa ni vigumu kwa msichana kupata mimba na wakati hakukuwa na mbegu zilizoingia katika mfumo wake wa uzazi.
Walichomwambia ni kwamba kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea, iliwezekana kabisa msichana huyo alikuwa akimdanganya kwa kuwa aliamini kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wao baada ya kulipwa pesa hizo.
“Kwa hiyo ananidanganya?” aliuliza Richard.
“Nadhani! Hebu kwanza wasiliana naye na umwambie ishu ya kwenda kupima,” alisema Robert.
Hilo ndilo alilolifanya, haraka sana akawasiliana na Upendo na kumwambia suala la kwenda kupima ili kujua kama alikuwa na mimba kweli ama la.
Upendo hakutaka kuona hilo likitokea ila alichokifanya ni kuanza kumzungusha kwa kumwambia wangekwenda lakini hilo halikutokea kabisa.
Richard akapata uhakika kwamba huo ulikuwa mpango uliochezwa na msichana huyo na ukweli ni kwamba hakuwa na mimba kama alivyokuwa amemwambia hivyo kuachana naye na kuendelea kufanya mambo yake mengine.
Siku zilikatika, baada ya siku mbili, Richard akaja kushtuka akiwa nje ya nyumba yake aliyopanga akiwa amelala kibarazani. Hakujua ni kitu gani kilitokea, alishangaa mno kwani kitu alichokikumbuka ni kwamba mara ya mwisho alikuwa klabu akinywa na marafiki zake na baada ya hapo, hakukumbuka ni kitu gani kilikuwa kimetokea.
Haraka sana akampigia simu Robinson na kuanza kuongea naye, alihitaji kukumbushwa mahali alipokuwa, ni kitu gani kilitokea mpaka asubuhi kujikuta akiwa kibarazani nyumbani kwake.
“Jana ulilewa sana, ulikunywa mpaka tukashangaa,” alisema Robinson kwenye simu.
“Nililewa sana?”
“Ndiyo! Wanawake walikufuata kutaka kuondoka nawe, ukakataa, yaani hukumbuki lolote lile?” aliuliza Robinson kwenye simu kitu kilichomfanya Richard kuanza kukumbuka.
“Halafu ikawaje?”
“Uliondoka mapema sana kwenda nyumbani. Nadhani ulipofika, hata kuingia ndani ukashindwa ndiyo maana ukalala kibarazani. Kichwa chako cha panzi, acha pombe chalii angu,” alisema Robinson na kuanza kucheka.
Richard akakata simu, hakutaka kuishia hapo tu, akampigia simu Robert na kuanza kumuuliza kilichokuwa kimetokea usiku wa jana. Kama alivyoambiwa na Robinson ndivyo alivyoambiwa na Robert pia kwamba alilewa sana na kuondoka kurudi nyumbani, hakukumbuka kilichotokea njiani mpaka asubuhi hiyo ambapo alijikuta akiwa amelala kibarazani.
“Mh! Pombe siyo ishu kabisa,” alisema Richard na kuingia ndani.
Hakutaka kuwasiliana na Upendo, bado alikuwa na mambo mengi ya kufanya, kulikuwa na mipango mingi mbele yao ambayo walitakiwa kuhakikisha mpaka wanaipatia muafaka na kufanikiwa zaidi.
Walipanga kwa pamoja kwamba ni lazima wasafiri waelekee nchini Marekani ambapo huko waliamini wangepata pesa nyingi na kufanikiwa kuliko walivyokuwa barani Afrika.
Hawakuacha kukutana, kila siku walionana na kuzungumza mambo mengi mno. Walikumbuka kwamba walipanga kwenda nchini Misri baada ya kutoka Kenya lakini huko waliona kama wangejichelewesha, kwenda Marekani kungewafanya wapate mabilioni ya pesa.
Wakati wenzake wakiendelea kufikiria kuhusu kuelekea nchini Marekani kichwa cha Richard kilimfikiria zaidi Upendo. Alihisi kulikuwa na kitu kilitokea na ndiyo maana aliambiwa na msichana huyo kwamba alikuwa na mimba.
Alifikiria mambo mengi lakini kubwa zaidi ni kitendo cha kumpa mimba msichana huyo. Alikuwa mbaya wa sura, alichukiwa na wanaume wote chuoni lakini jambo la ajabu kabisa, eti mwisho wa siku alimpa mimba na kutarajia kupata mtoto pamoja naye.
“Hivi nizae na msichana mbaya namna ile! Mungu kwa nini umenipiga kwa pigo hili?” aliuliza Richard alipokuwa chumbani akifikiria kuhusu msichana huyo.
Kwa kuwa Upendo alijua Richard kuwa na mimba yake basi muda mwingi akawa anampigia, aliendelea kumwambia kwamba alimpenda kuliko mtu yeyote yule na ndiyo maana aliamua kupata ujauzito wake kama njia mojawapo ya kumuonyeshea ni kwa jinsi gani alimthamini.
Kwa Richard moyo wake ulikuwa na hasira mno, wakati mwingine alitamani kumwambia ukweli kwamba hakumpenda lakini kitendo cha kubeba mimba yake tu kikamfanya kuogopa na kuhisi kwamba angeharibu kila kitu.
“Ila simpendi! Huo ndiyo ukweli, yaani simpendi mno,” alisema Richard kila alipokuwa akimfikiria msichana huyo.
Siku ziliendelea kukatika, bado Richard aliendelea kuwaza kama kweli Upendo alikuwa na mimba au alikuwa akimtega. Moyo wake ukagawanyika, alihisi kabisa kwamba inawezekana msichana huyo alimdanganya ili tu baadaye afanye juu chini na azae hata mtoto kwa mwanaume mwingine ili ionekane kama yeye ndiye aliyekuwa baba wa mtoto huyo.
Hilo likampa hofu na hatimaye kuamua kumpigia simu na kuzungumza naye. Kwanza walizungumza mambo mengine kabisa na mwisho kabisa Richard akaingizia suala lake kwamba alihitaji kuamini kama msichana huyo alikuwa na mimba kweli au alimdanganya kwani kipindi cha nyuma kila alipokuwa akimwambia waende hospitali msichana huyo alikataa kwa kuleta visingizo vingi.
“Basi twende hospitali tukapime,” alise aRichard.
“Hakuna shida. Twende.”
Hilo ndilo lililotokea, siku iliyofuata wawili hao wakaondoka na kuelekea hospitalini. Huko, kila mtu aliyekuwa akiwaona alishangaa. Kilichowashangaza ni uzuri wa Richard na ubaya wa Upendo.
Walikuwa watu wawili wasioendana, wasichana wengi walitokea kuvutiwa na Richard lakini kwa jinsi alivyoamua kuwa na msichana mbaya kama Upendo, wengi walishangaa.
“Jamani yule kaka mzuriiiiiii....kama malaika,” alisema msichana mmoja aliyekuwa amekaa na wenzake kwenye benchi hospitalini hapo.
“Kweli shoga’angu...ila yule msichana aliyekuwa naye! Mh! Mbona anatisha hivyo?” aliuliza msichana mwingine huku naye akionekana kushangaa.
Muda wote Richard alikuwa akijishtukia, hakuamini kama kweli yeye leo hii alikuwa akitembea na Upendo ambaye alikuwa na mimba yake. Walikwenda moja kwa moja mpaka kwa daktari ambapo akampima Upendo na kukuta akiwa na mimba ya wiki mbili.
“Ni kweli una mimba ya wiki mbili,” alisema daktari huku akiwaangalia wawili hao walioonekana kuwa tofauti, kwa Upendo alikuwa na tabasamu pana ulioufanya ubaya wake uongezeka lakini kwa Richard alikuwa na hasira kali zilizomfanya kuonekana mzuri zaidi.

Je, nini kitaendelea?
 
NYEMO CHILONGANI.
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Ishirini

Ni kama Upendo alijua kila kitu kilichokuwa kikienda kutokea, kitendo cha Richard kutokuwa na furaha baada ya kuwa naye aliamini kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wao na hivyo kuachana. Hakutaka kuona hilo likitokea katika vitu ambavyo hakutamani kabisa kuona vikitokea basi kilikuwa ni kuachana na mwanaume huyo.
Alimpenda, tena kutoka moyoni mwake, alijua kabisa kila kitu kati yake na Richard kilikuwa kikienda mwisho kwa kuwa tu mwanaume huyo hakuonekana kumpenda hata kidogo.
Alihitaji sana kuwa na mtoto na Richard, hakujua angefanya nini kwani mwanaume huyo naye alikuwa makini sana kila walipokuwa wakifanya mapenzi. Hilo lilimsumbua sana kichwani mwake, hakutaka kuona akiendelea kusononeka, aliamua kuanza kuulizia kama kungekuwa na uwezekano wowote wa kufanya ili ashike mimba yake.
Akampigia simu rafiki yake aliyekuwa nchini Marekani na kumuuliza kuhusu jambo hilo. Rafiki yake huyo akamwambia kama kweli alihitaji kushika mimba kutoka kwa Richard ilikuwa ni lazima azichukue mbegu zake na kuzipandikiza kwenye mayai yake.
“Kivipi?” aliuliza Upendo.
Rafiki yake huyo aliyeitwa kwa jina la Manka akaanza kumwambia kuhusu vitu hivyo ambavyo alitakiwa kufanya. Kulikuwa na mambo mawili ambapo yeye alitakiwa kuchagua mojawapo kwa ajili ya kulifanya kushika mimba ya mwanaume huyo.
Kitu cha kwanza kiliitwa IVF yaani In Vitro Fertilization. Hii ni njia inayotumika kwa wanawake ambao wanakuwa na mirija iliyoziba, wanaume wenye mbegu chache, wanawake waliokuwa na uvimbe katika ovari na matatizo mengine mengi.
Hii hufanyika kwa kuchukua mbegu za mwanaume na mwanamke na kuziweka katika chupa maalumu iliyokuwa na hali ya joto ambapo pale hukaa kwa kipindi kirefu na mtoto kuanza kutengenezwa.
Hatua ya kutengeneza mtoto kwa kutumia mbegu za mwanaume na mwanamke ilianza mwaka 1978 katika Mji wa Oldham nchini Uingereza ambapo Louise Joy Brown alitengenezwa katika chupa na kuwa mkubwa kabisa huko maabara.
Yalikuwa ni mafanikio makubwa mno kufanyika na hivyo watoto kuendelea kutengenezwa kwenye chupa mpaka leo hii.
Ukiachana na IVF pia kulikuwa na ile ya kufanya Surrogation. Hiyo ni ile hatua ambayo mwanaume anatolewa mbegu zake na kupandikizwa kwa mwanamke pasipo kufanya mapenzi.
Mbegu za mwanaume zinapokutana na yai la mwanamke, hupata mimba na kuanza kukua mpaka kufikia hatua ya kujifungua.
Hii njia hutumika zaidi kwa matajiri ambao wanakuwa hawana watoto hivyo huchukua wanawake wengine na kuwapandikizia mbegu na kujifungua.
Hii ilionekana kuwa njia sahihi kwa Upendo, alihitaji kuwa na mbegu za Richard ili azichukue na kuzipandikiza katika mfuko wake wa uzazi ili ashike ujauzito wa mwanaume huyo na mwisho wa siku kujifungua.
“Hiyo njia ya pili nimeipenda. Ninaweza kuonana na watalaamu hao?” aliuliza Upendo.
“Si tatizo!”
Haraka sana akaunganishwa na madaktari hao na kuanza kuwasiliana nao kwa barua pepe. Aliwaambia ukweli kwamba kulikuwa na mwanaume ambaye alihitaji sana kuchukua mbegu zake na kuzipandikiza katika mayai yake.
Hilo halikuwa tatizo hata kidogo, madaktari hao wakakubaliana naye na kumwambia alipie kiasi cha dola laki mbili kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.
Kwake, pesa hazikuwa na tatizo lolote lile, kitu pekee alichokuwa akikitaka wakati huo ni kupata mtoto ambaye angezaa kutokana na mbegu za Richard.
Upendo aliwaambia kuhusu Richard, aliwaambia kila kitu na hivyo madaktari hao kumwambia kwamba wangefanya kila liwezekanalo kumsaidia kwa hali na mali.
Baada ya siku kadhaa, madaktari hao wakasafiri mpaka nchini Tanzania ambapo wakaonana na Upendo huku wakiwa na vifaa vyote na hivyo kuanza kumsubiri Richard aliyekuwa amekwenda nchini Kenya.
Baada ya kurudi ndipo akamwambia kuhusu suala la mimba. Alihitaji kumtengeneza kwanza, ajue kwamba alikuwa na mimba yake. Richard alipoambiwa na hivyo kutaka kwenda kupima na msichana huyo alikataa katakata na alifanya hivyo kwa sababu bado mbegu hazikuwa zimepandikizwa.
“Hivi tutaweza kuzipata mbegu zake kweli pasipo kufahamu?” aliuliza Upendo.
“Zitapatikana!”
Alichomwambia daktari ni kumnywesha dawa ya usingizi mwanaume huyo na kisha apelekwe sehemu ambapo huko angetolewa mbegu zake kitaalamu na kupandikizwa kwenye mayai yake.
Hilo likamfanya Upendo kuwashirikisha wasichana wawili ambao walitakiwa kumfuatilia Richard kila kona na siku ile ambayo alikwenda klabu na wenzake na kunywa, miongoni mwa wasichana waliokuwa wamekaa nao walikuwa hao wawili.
Wakamuwekea dawa ya usingizi mzito kwenye kinywaji chake na alipokunywa tu, akahisi uchovu mwingi, akaaga n kuondoka humo ila alipofika ndani ya gari tu, akapitiwa na usingizi mzito.
Wasichana hao wakaingia ndani ya gari hilo na kuondoka naye ambapo wakaonana na Upendo aliyekuwa amewaandaa madaktari wake hivyo kumchukua Richard na kumpeleka kwenye chumba fulani walichokuwa wameandaa.
Macho yao yalipotua kwa mwanaume huyo, wakapata sababu ya Upendo kutamani mno kuzaa naye, alikuwa mwanaume mzuri wa sura, alivutia kiasi kwamba ingekuwa ni vigumu kwa msichana yeyote yule kukataa kuzaa naye.
Humo ndani wakaanza kuushtua mwili wake, kuifanya damu yake izunguke kwa kasi kubwa. Walimshika sehemu muhimu, hasa kwenye nyonga na magotini kwa nyuma na kuanza kuzitekenya sehemu hizo.
Ulikuwa ni utaalamu mkubwa, mambo hayo yote yalifanyika huku akiwa amepitiwa na usingizi mzito. Madaktari hao walikuwa wazoefu na kazi zao, mara kiungo cha Richard kikasimama na kuendelea kufanya kazi yao kwa kutumia mafuta maalumu laini waliyokuwanayo.
Walifanikiwa kwa asilimia mia moja, mbegu zake zikatolewa, zikawekwa kwenye chombo maalumu na kisha Upendo kuchomwa sindano ya usingizi, kifaa kingine kikachukuliwa na kuanza kuingizwa kwenye mayai yake kupitia sehemu za siri.
Mbegu hizo ziliingizwa, walizifuatilia kwa kutumia mashine maalumu, zikaenda katika yao la uzazi la Upendo na hivyo kuanza kutengeneza mtoto taratibu pasipo wawili hao kukutana kimwili.
Baada ya kumaliza hatua hiyo iliyochukua saa mbili, Richard akachukuliwa na kupelekwa ndni ya gari ambapo liliendeshwa, na alipofikishwa kwake, akatolewa na kulazwa kibarazani huku akiwa hajui ni kitu gani kilitokea.
***
Vijana hao watatu hawakutaka kuendelea kubaki nchini Tanzania, ili wapate pesa zaidi ilikuwa ni lazima kuondoka na kuelekea nchini Marekani. Huko walikuwa na uhakika wa kuingiza pesa nyingi sana kama tu wangekuwa na uwezo wa kufanya madili makubwa na mengi.
Njiani, wakiwa ndani ya ndege vichwa vyao havikutulia hata kidogo, walikuwa wakifuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea wakati huo nchini humo. Kulikuwa na mambo mengi mno kiasi kwamba walichanganyikiwa ni lipi ambalo walitakiwa kuanza nalo.
Walitaka kudili na watu wakubwa kiasi cha serikali kushtuka lakini pia wakahisi kitendo cha kutafutwa na serikali ya Marekani ingekuwa kitu kikubwa na kibaya mno kiasi kwamba ingewafanya kutokuishi kwa raha kama walivyotakiwa kuishi na wakati walikuwa na pesa.
“Kuna taarifa nimeiona hapa,” alisema Robert huku akiwaoyeshea wenzake simu iliyokuwa imeunganishwa na huduma ya intaneti.
“Habari ipi?”
“Mshawahi kumsikia mtu anaitwa Kamacho?” aliuliza.
“Hapana! Ndiye nani?”
Robert akaanza kuwaelezea kuhusu mtu huyo. Alikuwa ni mmoja wa watu waliokuwa wakitafutwa sana na serikali ya Marekani. Alikuwa mtu wa Mexico ambaye alisafirisha sana madawa ya kulevya kuelekea nchini humo.
Katika orodha ndefu ya CIA, mtu wa kwanza kabisa ambaye alikuwa juu ni huyo mwanaume. Kazi yake kubwa ilikuwa ni kusafirisha madawa ya kulevya kutoka Mexico na kuingia Marekani.
CIA walipambana naye, walijitahidi kuizuia biashara hiyo lakini walishindwa kabisa kitu kilichowafanya kumteka kaka yake aliyeitwa kwa jina la Hernandez na kumfunga gerezani kwa kumsingizia kuhusika na uuzaji wa madawa ya kulevya kama ilivyokuwa kwa ndugu yake.
Walichomwambia ambacho kilikuwa cha siri sana ni kutakiwa kujisalimisha, kama kweli alihitaji ndugu yake atoke gerezani, na kama alimpenda basi alitakiwa kuelekea nchini Marekani na kujipeleka mwenyewe katika kituo cha polisi.
“Oh! Sasa hapo kuna nini? Yaani kuna uhusiano upi wa sisi na huyo Kamacho?” aliuliza Richard huku akimwangalia Robert.
“Yaap! Hivi hatuwezi kumtorosha jela huyo Hernandez halafu tukapiga pesa ndefu kwa Kamacho?” aliuliza Robert.
Swali lake hilo likamfanya Richard kuanza kuangaliana na Robinson, kwao lilikuwa jambo moja gumu sana ambalo walihisi kabisa wasingeliweza hata kama wangetumia ujanja gani.
“Haiwezekani!” alisema Robinson.
“Hahah! Hakuna kitu kama hicho. Unakumbuka kwamba hakuna kisichowezekana chini ya jua? Basi hili nalo linawezekana kabisa kufanyika, tumtorosheni huyu mtu,” alisema Robert huku akiwaangalia wenzake.
“Tutafanya vipi? Yaani itakuwaje mpaka tumtoroshe mwanaume huyu?” aliuliza Robinson.
Robert akaanza kuwaambia mipango yake, kile alichokuwa amekifikiria ambacho aliamini kwamba kama wangekifanya basi ingekuwa kazi nyepesi kwao kumtoa gerezani Hernandez.
Kwa jinsi alivyokuwa akiielezea mipango yake, ule ugumu ambao ulikuwa vichwani mwa marafiki zake ukaanza kutoweka na hatimaye hata nao kuhisi kwamba kitu hicho kilikuwa chepesi sana kama tu wangethubutu kufanya hivyo.
Aliwaambia mipango yote na baada ya hapo akawaambia kuwa kama wangefanikiwa basi wangechukua kiasi cha dola milioni mia moja kutoka kwa Kamacho.
“Atatoa hizo pesa?” aliuliza Richard.
“Atatoa tu. Damu nzito kuliko maji, hizo pesa atatoa. Kama kweli mtu ana utajiri wa dola bilioni kumi, tena kila siku anaingia mamilioni ya pesa, atashindwaje kutoa pesa hizi, cha msingi ni kuonana naye kwanza,” alisema Robert huku akiwaangalia wenzake.
Dola milioni mia moja zilikuwa ni zaidi shilingi bilioni mia mbili, walitakiwa kupambana mpaka wanazipata pesa hizo kutoka kwa Kamacho.
Ndege ilichukua saa ishirini na mbili ndipo ikaanza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa JFK jijini New York.
Kabla ya kuteremka wakaanza kuangalia mandhari ya jiji hilo. Walikumbuka kwamba waliambiwa mengi kuhusu Marekani na siku hiyo walikuwa ndani ya ndege wakiteremka tayari kwa kukanyaga ardhi ya nchi hiyo.
Kipindi cha nyuma, miezi michache iliyopita hawakuwa na uhakika wa kufika nchini humo kwa haraka kipindi hicho lakini siku hiyo, ni ndani ya miezi michache tu walikuwa wakikanyaga huku wakiwa matajiri wakubwa.
Walipoikanyaga tu, kila mtu akashusha pumzi kwa nguvu, moja ya ndoto zao zilikuwa zimekamilika kitu kilichowafurahisha mno.
Wao na abiria wengine wakaanza kutembea kuelekea lilipokuwa jengo la uwanja huo. Walipofika, wakachukua mabegi yao na kutoka nje ambapo walikuta gari la Hoteli ya King Lear likiwasubiri nje, wakaingia na kuanza kuelekea katika hoteli hiyo huku kila mmoja akiwa na uhakika wa kufanikiwa.
“Jamani kama tutafanikiwa, tutakuwa tumepiga bonge moja la bao,” alisema Robinson huku akiwaangalia wenzake.
“Kweli kabisa. Ila tutafanikiwa, hata kama CIA watatutafuta, bado tutafanikiwa tu,” alisema Richard huku akiwa na uhakika kufanikiwa kwa mipango yao yote waliyokuwa wameipanga ndani ya ndege. Kitu cha kwanza kilikuwa ni kumtafuta huyo Kamacho
 
NYEMO CHILONGANI.
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Ishirini na Moja

Robinson, Richard na Robert walikuwa nchini Marekani katika hoteli ya King Lear wakiendelea na mambo yao kama kawaida. Siku hiyo walitakiwa kupanga mipango yao, kikubwa zaidi kulikuwa na kitu ambacho walitakiwa kufanya, kitu ambacho waliamini kwamba kama wangefanikiwa basi wangefanikiwa kuwa na pesa nyingi zaidi.
Ilikuwa ni lazima wasafiri kutoka hapo Marekani na kuelekea Mexico kuonana na mwanaume aliyejulikana kwa jina la Kamacho. Walijua kwamba ni vigumu kupatikana kwa mwanaume huyo ila ilikuwa ni lazima wahakikishe wanakwenda na kuonana naye.
Hawakutakiwa kwenda wote watatu, kwa sababu kulikuwa na mambo mengi ya kufanya, huko akatumwa Richard, yeye ndiye ambaye alitakiwa kwenda Mexico na kuhakikisha mwanaume huyo anapatikana haraka iwezekanavyo.
Huku nyuma Robinson na Robert walitakiwa kubaki, wao ndiyo wangekuwa wanampa maelekezo juu ya kitu gani alitakiwa kufanya. Hilo halikuwa tatizo, kwa sababu hapo New York mpaka Texas hakukuwa mbali sana, wakaanza kufanya harakati za kupata kibali cha kuingia nchini humo.
Walikuwa na pesa, hakukuwa na tatizo lolote lile, Richard akafanikiwa kupata kibali cha kwenda Mexico na hivyo siku hiyohiyo kupanda ndege na kuelekea jijini Texas. Walipanga mipango yao, hawakutaka atumie ndege, walihitaji atumie gari kwa sababu huko mpakani ambapo ndipo alipotakiwa kupita kulikuwa na michezo mingi ya uingizaji wa madawa ya kulevya iliyokuwa ikichezwa.
Safari hiyo kutoka hapo Texas mjini mpaka El Paso, mpaka wa Mexico na Marekani alitumia saa kadhaa akafika huko ambapo kulikuwa na bango kubwa lililoandikwa ‘Welcome Mexico’ ambalo lilisomeka vizuri kabisa.
Kulikuwa na msururu mrefu wa magari, kila mtu mahali hapo alionekana kuwa bize mno, hakukuwa na mtu aliyekuwa na mpango na mwenzake, kila mmoja alifuatilia kile kilichomfanya kuwa mahali hapo.
Zamu yake ya kuangaliwa hati ya kusafiria, ikaangalia, ilipoonekana kufaa, ikapigwa mhuri na kuingia nchini Mexico. Hakujua ni kwa namna gani angeweza kumpata huyo Kamacho, alisoma kwenye mitandao kwamba alikuwa mtu katili ambaye hakuwa na huruma hata kidogo.
Kwake, hakuogopa kwa kuwa alikuwa na kitu ambacho aliamini kabisa mwanaume huyo angemuhitaji kuliko mtu yeyote yule.
Akaondoka mpakani na kuelekea katika hoteli ya El Pablo iliyokuwa umbali wa kilometa sita kutoka El Paso, alipofika huko akachukua chumba na kutulia chumbani.
Aliwasiliana na wenzake, aliwaambia tayari alifika na alichokihitaji kilikuwa ni kuonana na mwanaume huyo ili ampe taarifa kwamba alikuwa na mpango kabambe wa kumtoa ndugu yake, Hernandez katika gereza kubwa nchini Marekani, kama kweli alihitaji msaada wake, basi alitakiwa kumsikiliza.
“Nitampataje?” alijiuliza.
Aliwasiliana na wenzake na kuwaambia ugumu ulivyo, walijua ni kwa jinsi gani wangesumbuka sana kuonana na mwanaume huyo lakini kwa sababu alikuwa muuzaji wa madawa mkubwa, waliamini alikuwa na watu wengi waliokuwa wakimpelekea taarifa, hasa huko mpakani.
Alichokifanya ni kusubiri, kulala na asubuhi ilipofika tu, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumfuata dada wa mapokezi na kuanza kuzungumza naye.
Siku iliyopita mtu aliyekuwa hapo alikuwa mwanaume, huyu wa sasa hivi, msichana mrembo ndiyo kwanza alikuwa amemuona, macho yake yalivyotua kwa Richard akashtuka mno.
Ni kweli aliwaona wanaume weusi wengi, wenye sura nzuri lakini huyu aliyekuja leo alionekana kuwa tofauti mno, alipendeza, alikuwa na sura nzuri kiasi kwamba hata yeye mwenyewe alihisi kabisa hakukuwa na mwanaume aliyekuwa na sura nzuri kama huyo.
“Hi!” alimsalimia, msichana huyo alimkodelea macho, hata salamu ile hakuisikia.
“Haloooooo....” aliita huku akimchezea mkono wake mbele ya macho yake, msichana huyo akashtuka.
“Oh! Welcome...” (Oh! Karibu..) alisema msichana huyo huku uso wake ukiwa na tabasamu pana.
Alishindwa kuvumilia, tabasamu lake lilikuwa usoni mwake, alitokea kumpenda mwanaume huyo kwa kuwa alikuwa mzuri wa sura. Alitamani amwambie kitu chochote kile kizuri ili akae naye kwa muda mrefu na kuzungumza.
“I need your help,” (nahitaji msaada wako) alisema Richard huku naye uso wake akiuwekea tabasamu pana lililomchanga kabisa msichana huyo.
“No problem! What can I help you?” (hakuna tatizo! Nikusaidie nini?) aliuliza msichana huyo.
Richard alianza kuzungumza naye, alimwambia kwamba alifika nchini Mexico kwa lengo la kuonana na mwanaume aliyeitwa kwa jina la Kamacho.
Hakujua alipokuwa akiishi ila alitamani sana kuonana naye kuliko mtu yeyote yule. Msichana huyo aliposikia hivyo, hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, kwake haikumuingia akilini kwa mwanaume mzuri kama alivyokuwa Richard kumuulizia Kamacho, mwanaume aliyekuwa na roho mbaya mno.
“Kamacho?” aliuliza huku akimwangalia.
“Ndiyo! Ninahitaji kuonana naye,” alisema Richard.
Msichana huyo alichomwambia ni kwamba hajawahi kumuona hata siku moja. Ni kweli alimsikia sehemu mbalimbali akitafutwa au hata kuwatuma watu wake kufanya utekaji na mauaji lakini hakuwahi kumuona hata siku moja zaidi ya kwenye magazeti tu ambayo yalikuwa yakimzungumzia yeye.
“Hujawahu kumuona hata kidogo?”
“Kweli! Na simjui kabisa,” alisema msichana huyo.
Richard hakutaka kuzungumza zaidi, akatoka na kuelekea matembezini, kichwa chake kilikuwa na mawazo tele, hakujua namna ya kumpata Kamacho kwani ingekuwa ni rahisi kuambiwa mahali alipokuwa akipatikana na kwenda yeye mwenyewe.
Alizunguka huko kwa saa zima kwa kuhisi kwamba inawezekana angeweza kuonana na mtu yeyote ambaye angeweza hata kumwambia kuhusu mwanaume huyo lakini hilo halikuwezekana.
Baada ya kutembeatembea kwa saa mbili akaamua kurudi hotelini na kuingia chumbani. Kitu cha kwanza kilikuwa ni kuwasiliana na wenzake na kuwaambia kuhusu ugumu wa kile alichokuwa amekutana nacho.
“Kwa hiyo hujampata kabisa?” aliuliza Robinson.
“Ndiyo! Nimejitahidi mno kuulizia,” alisema Richard.
Alichokisema Robert ni kwamba Richard alitakiwa kuhakikisha anafanya kila liwezekanalo kuhakikisha anampata mwanaume huyo na njia pekee ya kumpata ilikuwa ni kumuulizia kila mtu kuhusu mwanaume huyo.
Ulikuwa ni mtihani mkubwa lakini hakuwa na jinsi, alitakiwa kufanya kama alivyoambiwa hivyo kuondoka na kwenda chini kulipokuwa na mgahawa.
Alipofika huko, akaanza kuwauliza wahudumu kuhusu Kamacho. Kila mtu alibaki akishangaa, haikuwa kawaida kwa mtu kumuulizia mwanaume huyo kama ambavyo yeye alimuulizia.
Kila mmoja alimuuliza maswali juu ya sababu iliyomfanya kutaka kuonana na mwanaume huyo lakini hakutaka kuwaambia ukweli, msimamo wake ulikuwa uleule kwamba alihitaji kuonana na mwanaume huyo tu.
Hakusaidiwa kwa lolote lile, akaondoka na kurudi chumbani. Bado alikuwa na shaka kubwa kuhusu kumpata Kamacho, hakujua ni kitu gani kingetokea huko mbele kwani hakuweza kumpata na mbaya zaidi kila mtu aliyemuuliza kuhusu mwanaume huyo alibaki akimshangaa tu.
Siku ziliendelea kukatika, siku ya pili, na ya tatu ikaingia lakini hakuwa amefanikiwa kwa lolote lile. Siku hiyo alilala chumbani kwake, alisikia mlango unagongwa, haraka sana akaiangalia saa yake, ilikuwa ni saa tano usiku.
Hakujua ni nani alikuwa akipiga hodi, akausogelea mlango, kabla ya kuufungua, akachungulia kwenye kitundu kidogo cha mlango, hakuona mtu lakini bado alisikia mlango ukigongwa kumaanisha mgongaji alikuwa pembeni, alijificha, hakutaka kuonekana na mtu huyo.
“Who is it?” (nani?) aliuliza huku akiwa ndani.
“Linda!”
“Who the hell is Linda?” (Linda ndiye nani?) aliuliza.
Msichana huyo akamwambia kwamba alikuwa mhudumu, kulikuwa na jambo alihitaji kuzungumza naye. Alichanganyikiwa, hakujua kulikuwa na jambo lipi msichana huyo alihitaji kuzungumza naye.
Akamuuliza, akamjibu kuhusu mwanaume aliyekuwa akimtafuta, Kamacho, alipata taarifa kwamba alikuwa sehemu fulani, hivyo alihitaji kumwambia.
“Mh!” aliguna.
Kwa sababu alikuwa na hamu na Kamacho, akaufungua mlango kwa lengo la kumsikiliza huyo Linda. Mlango ulipofunguka, wanaume watatu waliokuwa wamejificha kwa pembeni ambao walikuwa na bastola mikononi huku miili yao ikiwa imechorwa tatuu, wakaingia ndani, wakamsukuma na kumlaza kitandani.
“Ukipiga kelele tu, ubongo utasambaa kitandani,” alisema mwanaume mmoja kwa sauti iliyokuwa nzito.
Hata kabla hajajibu kitu, hapohapo akapigwa na kitu kizito, akaanza kuona giza, ni ndani ya sekunde kadhaa tu, akapoteza fahamu.
Richard alikuja kupata fahamu baada ya saa mbili, akayafumbua macho yake, akajikuta akiwa ndani ya chumba kimoja kilichokuwa na mwanga hafifu, alikalishwa kwenye kiti huku akiwa amefungwa kamba miguu na mikono.
Hakujua ni kwa namna gani alikuwa ndani ya chumba hicho, akaanza kuangalia huku na kule kwa macho yake yaliyokosa nguvu. Akajitahidi kuyafumbua na kuangalia huku na kule, akaanza kukukuruka ili ajitoe kwenye kamba zile lakini alishindwa.
“Halooooo!” aliita kwa sauti ili kuona kama kungekuwa na mtu yeyote yule ambaye angefika mahali hapo.
Aliendelea kupiga kelele kwa dakika kadhaa, mara mlango ukafunguliwa na mwanaume mmoja kuingia huku akiwa amevalia pensi na shati lililofunguliwa vifungo vyote.
Alimwangalia Richard pale alipokuwa, hakuzungumza kitu ila kwa jinsi alivyomwangalia, macho yake tu yalitosha kumwambia kwamba hakutaka kusikia akipiga kelele tena.
Richard akaogopa, hakujua alikuwa mahali gani na watu waliomteka walikuwa akina nani. Alitulia kwa nusu saa, mlango ukafunguliwa tena na wanaume sita kuingia huku mmoja akiwa amevalia kofia ya Marlboro na suti nyeupe.
Watu wengine wakasimama nyumba kabisa na mwanaume aliyevalia suti akamsogelea pale alipokuwa kwa lengo la kuongea naye. Richard hakujua mwanaume huyo alikuwa nani, aliogopa, hakuona kama kungekuwa na dalili za kutoka ndani ya chumba kile akiwa mzima kabisa.
“Wewe ni nani?” aliuliza mwanaume huyo.
“Richard!”
“Umetoka wapi?” aliuliza mwanaume huyo.
“Nimetoka Afrika,” alijibu.
Mwanaume huyo akacheka sana, alichokifikiria ni kwamba alidanganywa. Akawaambia vijana wake wamchukue Richard na kutoka naye.
Wakafanya hivyo na kumpeleka kwenye chumba kingine kilichokuwa na mashine kubwa huku pembeni kukiwa na watu wengine wakiwa wamefungwa kamba.
Mashine moja ikawashwa, mwanaume mmoja miongoni mwa wale waliokuwa wamefungwa kamba akachukuliwa, akaanza kupiga kelele za kuomba msamaha lakini jamaa mwenye suti hakutaka kujali kabisa.
Akachukuliwa na kuingizwa kwenye mashine ile ambapo ikaanza kumvuta na kumsagasaga huku nyama yake ikienda kuangukia sehemu nyingine iliyokuwa na ndoo.
Richard akaogopa mno, aliona kabisa kwamba huyo ndiyo ulikuwa mwisho wake. Jamaa yule mwenye suti akamsogelea na kumuuliza tena alitoka wapi kwani halikuwa jambo jepesi mtu kutoka barani Afrika na kumuulizia Kamacho.
“Yule aliyetumbukizwa, alitapeli madawa ya kulevya yenye thamani ya dola milioni mbili. Alitukimbia lakini tukamakamata, hiyo ndiyo adhabu yake. Huwa hatuoni shida kuua, kwanza ndiyo tunasikia burudani kabisa mioyoni mwetu. Una nafasi ya mwisho, umetoka wapi?” alisema mwanaume huyo na kumuuliza.
“Nimetoka Afrika! Naomba unielewe, huo ndiyo ukweli wangu, nimetoka Afrika,” alijibu Richard huku akitetemeka.
“Nuno! Mtumbukizeni kwenye mashine,” alisema jamaa huyo, hapohapo Richard akabebwa mzimamzima na kuanza kupelekwa kwenye mashine ile kama ilivyokuwa kwa mwanaume yule mwingine
 
NYEMO CHILONGANI.
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Ishirini na Mbili.

Wakati vijana wa Kamacho wakiwa wamemshika Richard kwa lengo la kumtumbukiza kwenye ile mashine ili asagwe ndipo akaanza kulitaja jina la Hernandez, aliwaambia alikuwa hapo kwa ajili ya mwanaume huyo aliyekuwa amekamatwa na kufungwa gerezani nchini Marekani.
“Nimekuja kuzungumza nawe kuhusu Hernandez,” alisema Richard kwa sauti, kila mtu aliposikia hivyo, akashangaa, si wao tu bali hata Kamacho naye alishtuka hivyo kuwaambia vijana wake wamuachie ili amsikie vizuri alichokuwa akikijua kuhusu Hernandez.
Wakamchukua na kumpeleka kwenye chumba kingine ambapo huko kulikuwa na meza na kumwambia akae kwenye kiti kwa ajili ya kuzungumza. Hakumfahamu mwanaume huyo lakini kwa jinsi alivyomtaja ndugu yake, akahisi kabisa kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea.
Kwanza akapewa maji na kuanza kunywa, baada ya dakika kadhaa, Kamacho akatoka katika chumba kimoja na kuingia mule na kuanza kumuuliza maswali kuhusu ndugu yake huyo na sababu iliyomfanya mpaka kumtaja.
“Umemjuaje ndugu yangu?” aliuliza Kamacho.
“Nilimfuatilia kwenye mitandao pamoja na wenzangu,” alijibu Richard.
“Kwa sababu gani?”
“Tunataka kumtoa gerezani,” alisema Richard huku akimwangalia Kamacho.
Mwanaume huyo aliposikia hivyo, akaangaliana na wenzake, kwake, kile alichoambiwa kilikuwa ni kitu kigumu sana kufanyika. Aliwahi kuwatumia polisi wa nchini Marekani kwa kuwapa kiasi kikubwa cha pesa lakini hawakufanikiwa kumtoa mtu huyo gerezani.
Hilo lilimpa mawazo mengi, kitendo cha Richard kumwambia kwamba alikuwa na mpango huo, moyo wake ukaridhika na kuanza kuhisi kuwa kijana huyo angefanikisha mpango huo, alichotakiwa ni kumwamini tu.
“Ndugu yakoana thamani gani?” aliuliza Richard, sasa akaanza kujiamini kwani Kamacho pamoja na ubabe wake, akawa mdogo tu.
“Unamaanisha nini?”
“Utatoa kiasi gani kwa ajili ya kumleta mpaka mikononi mwako!” alisema Richard.
“Dola milioni moja!”
“Unahisi inatosha hiyo?”
“Wewe unataka kiasi gani?”
“Kumbuka tupo watatu, itakuwa jambo zuri sana kama tutapata dola milioni sita ili tukuletee mpaka mlangoni,” alisema Richard.
Kamacho akanyamaza, kiasi alichoambiwa atoe kilikuwa kikubwa mno, hakuwahi kufikiria hata siku moja angatoa kiasi kikubwa namna hiyo tena ndani ya muda mfupi tu.
Lakini mbali na kufikiria kiasi hicho cha pesa akaanza kuufikiria ukaribu wake na Hernandez, alimpenda mno, kwake, huyo alikuwa karibu naye, ni zaidi ya upendo, yaani ni zaidi ya kitu chochote kile.
Walizungumza lakini Richard hakutaka kushusha bei, alimwambia ugumu wa kazi hiyo, kama kweli alijitahidi kumtoa mwanaume huyo gerezani na kushindwa, ilimaanisha kazi hiyo ilikuwa ngumu mno.
Hakuwa na jinsi, alikubaliana naye na hivyo kumsindikiza Richard mpaka mpakani El Paso na kuahidi kumtumia siku inayofuata ili kazi ibaki kwake na hao wenzake.
Huku nyuma Kamacho hakutaka kumwambia kitu chochote kile, aliambiwa kwamba hakutakiwa kuamini habari yoyote ile ambayo ingeonekana mbele yake kwa sababu dili walilokuwa wakienda kulifanya ili ndugu yake atolewe gerezani lilikuwa kubwa mno, hivyo hakutakiwa kuwa na hofu hata kidogo.
Richard akaondoka mpaka jijini Texas ambapo hapo akapanda ndege na kuelekea jijini New York kuonana na wenzake. Aliwaambia kila kitu kilichotokea kwamba Kamacho alikubaliana naye na alikuwa tayari kutoa kiasi hicho cha pesa kwa ajili yao.
“Safi sana! Hebu tufanyeni kazi ya kiume sasa,” alisema Robinson, akayapeleka macho yake kwa Robert ambaye kazi yake kubwa ilikuwa ni kutumia kichwa chake kuuelezea mpango jinsi ulivyotakiwa kufanywa.
“Kitu cha kwanza ni lazima tumtafute daktari ambaye anafanya kazi ndani ya gereza hilo. Huyo tutaongea naye kirafiki kwamba aende katika gereza hilo kwa lengo la kumchoma sindano Hernandez, hiyo sindano itakuwa na kazi moja, kuyasimamisha mapigo yake ya moyo kwa muda wa saa sabini na mbili,” alisema Robert na kuendelea:
“Daktari akimpima, atasema kwamba mwanaume huyo amekufa, hivyo atatakiwa kwenda kuzikwa kwenye makaburi yaliyopo nje ya gereza hilo,” alisema.
“Kwa hiyo atazikwa?”
“Hapana! Hawezi kuzikwa kwa sababu tutakwenda na maiti yetu hapo ambayo ndiyo tutaizika,” alisema Robert.
“Tutaizika? Kivipi?”
“Taarifa zitatolewa kwamba Hernandez amekufa, daktari atakwenda kumpima na kugundulika kwamba amekufa kwa sababu mapigo yake ya moyo yamesimama, kumbuka kwamba huyu daktari ni wetu, yaani yeye atacheza dili kuhakikisha mchezo unachezwa vizuri kabisa.
“Sasa ikishaonekana Hernandez amekufa, watapigiwa simu watu wa kitengo cha kuzika, bado sijawajua, ila tutatafuta namba zao, wewe utazidukua, simu ikipigwa kwao kwa lengo la kwenda huko kuzika, simu itakuja kwetu, kwa hiyo sisi ndiyo tutakwenda na mwili wetu ndani ya gari,” alisema Robert, wenzake walikuwa kimya tu wakisikiliza mipango yake.
“Halafu?”
“Kwenye kuzika tutauzika mwili mwingine, halafu mwili wa Hernandez tutauingiza ndani ya gari na kuondoka zetu,” alisema Robert.
“Bado kutakuwa na tatizo hapo! Najua tutakapokuwa tunazika, polisi wa magereza watakuwa wanatuangalia, sasa tutabadilishaje mwili? Halafu kwani ni lazima twende na mwili? Hatuwezi kuzika mdoli?”
“Ni kazi nyepesi sana. Huyo daktari tutampa baruti, tutamwambia ampe kijana mmoja na kumdanganya kwamba ni mabomu ambayo yatafanya ukuta ubomoke na kutoroka. Hapo ni lazima atuhusishe sisi, yaani amwambie kwamba kuna watu watakuja kumzika Hernandez, kwa sababu polisi watakuwa bize kutuangalia sisi, basi wao watumie nafasi hiyohiyo kupiga baruti hizo, ukuta ubomoke na watoroke, sasa wakati baruti hizo zitalia kwa sauti kubwa, hawa polisi waliokuwa huku kwetu hawatoweza kubaki, ni lazima watakimbilia gerezani, hiyo itakuwa nafasi yetu ya kumtoa Hernandez na kuuweka huo mdoli kaburini kisha kuondoka,” alisema Robert.
“Mimi ndiyo maana napenda kufanya kazi na Wachaga,” alisema Richard na kuanza kucheka.
Mipango ilipangwa, ilikuwa kabambe lakini suala moja tu ndiyo lilikuwa gumu ambalo Richard hakuwa amelifafanua, nalo lilikuwa ni kuhusu huyo daktari, kama wangempa pesa, alitakiwa kupewa kiasi gani ili afanye kazi hiyo.
“Na daktari tutamlipa kiasi gani?” aliuliza Robinson.
“Dola 0.00,” alijibu Robert.
“Unanichanganya kidogo!”
“Namaanisha hatolipwa!”
“Kwa nini?”
“Guys! Hivi mnajua kwa nini nilisema Vonso aende akasome katika Chuo Kikuu cha Tallahassee hukohuko Florida?” aliuliza.
“Hapana! Ndiyo utuambie”
“Basi hii ndiyo sababu! Hiki kitu nilikipanga kabla, nilijua tu kuna siku tutakuja kuchukua pesa nyingi kizembe kabisa,” alisema.
“Kivipi?” aliuliza Richard, Robert akabaki akitabasamu tu.
***
Maisha yalikuwa yakiendelea vizuri kabisa chuoni. Vonso alikuwa mwanaume mkimya ambaye alipenda sana kujifunza mambo mbalimbali. Alihitaji kuwa mkali kwenye sheria kwa sababu alijua kulikuwa na watu waliolipia kiasi kikubwa cha pesa kwa ajili yake.
Hakutaka kuwaangusha, alipambana usiku na mchana, alijisomea vitabu vingi, alipitia kesi nyingi za zamani, jinsi watu walivyokuwa wakitumia vifungu mbalimbali katika kushinda kesi zao.
Ilikuwa ni lazima ajue mambo mengi kuhusu sheria, alihitaji kuwa mtu muhimu katika dunia hii. Hapo chuo, kutokana na kujifunza mambo mengi na kuwa mkali, wanafunzi wengi wakaanza kumzoea na kuhitaji kujifunza mengi kupitia mtu huyo.
Miongoni mwa watu ambao walikuwa wakipenda sana kupiga naye stori alikuwa msichana Vivian James, msichana mrembo ambaye baba yake alikuwa daktari mkubwa katika Hospitali ya St. Joseph iliyokuwa Florida hapohapo nchini Marekani.
Alikuwa msichana mrembo mno, alipenda pombe, alipenda starehe, kwenye kila sherehe ambayo iliandaliwa chuoni hapo, hakukosa, alitamani kwenda kwenye kila sherehe kiasi kwamba wenzake walimzoea na hata siku alipokosa, walikuwa wakiulizana kama alikuwa akiumwa ama la.
Vivian hakuwa na leseni ya udereva, alipokonywa baada ya kukamatwa mara kadhaa akiwa anaendesha gari huku amelewa. Hilo kwake halikuwa tatizo, alichohitaji ni kwenda kwenye kila sherehe kwa sababu tu alipenda kufanya hivyo.
Wanaume nao hawakuwa nyuma, kupitia ulevi wake, walipambana mpaka kulionja penzi lake. Kwake, hilo halikuwa tatizo, hakuwa msichana mgumu, kila mwanaume aliyekuja na mipango yake, alifanikiwa kumchukua na kumfanya chochote kile.
Baada ya kukaa kwa miezi kadhaa, huku akipewa taarifa na vijana watatu waliokuwa wakimlipia ada kwamba walikuwa nchini Marekani, akaambiwa aandae sherehe ya kuzaliwa kwake ambayo ingekwenda kufanyika mwezi huo na wao wangesimamia kila kitu.
Hilo halikuwa tatizo, kwa kuwa watu hao walimwambia wangelipia kila kitu, wakakubaliana naye na hivyo kuwaambia marafiki zake kuhusu sherehe hiyo.
Kwa Vivian, aliposikia, alichanganyikiwa, kwake, sherehe ilikuwa kila kitu hivyo akaanza kujipanga na marafiki zake na hatimaye kusubiri siku ya sherehe hiyo kufanyika.
Siku zilikwenda kama kawaida na baada ya siku kadhaa, hatimaye siku husika ikafika na hivyo watu kujiandaa usiku kwenda huko kusherehekea na Vonso katika siku yake ya kuzaliwa.
Sherehe ilifanyikia katika nyumba moja kubwa ya kukodi iliyokuwa ufukweni, watu walicheza na kufurahi pamoja. Waliokuwa wanywaji, walikunywa sana, waliokuwa wakitaka kufanya mapenzi, hakukuwa na mtu aliyezuiliwa.
Vivian alikuwa amekaa na marafiki zake, walikuwa wakipiga stori kwa sauti kubwa kwani walikuwa wamelewa mno kwani hata sauti zao tu zilionyesha ni kwa jinsi gani pombe ziliwaingia vichwani mwao.
Baada ya dakika kadhaa, akafika mwanaume mmoja pale walipokuwa, alikuwa Richard. Alipowafikia, akaanza kuwaangalia kwa macho ya kuvutia huku mkononi akiwa na chupa ya Heinekenn ambayo ndani yake kulikuwa na vidonge vya usingizi.
“Hey girls! You look stunning...” Hey warembo! Mmependeza) aliwaangalia na kuwasifia.
Wasichana hao wakaangalia na kuanza kucheka, kwa kuwa walilewa, hakuona kama kungekuwa na ugumu wowote ule. Richard akakaa kabisa karibu na Vivian na kumwangalia.
“I just need your company miss,” (nahitaji kampani yako mrembo) alisema Richard.
“Me?” (mimi?)
“Yaap! I was looking for you,” (ndio! Nilikuwa nakutafuta?)
“Why? Do we know each other?” (kwa nini? Tunafahamiana?) aliuliza Vivian kwa sauti ya kilevi.
Richard hakutaka kuzungumza kitu, alichokifanya ni kuchukua glasi iliyokuwa chini na kumuwekea ile pombe aliyokuwa akinywa na kumtaka kunywa.
Hilo halikuwa tatizo, Vivian akaichukua na kuanza kunywa, si yeye tu bali hata wenzake nao wakaanza kunywa mfululizo pasipo kugundua kama pombe ile iliwekewa madawa ya usingizi.
Ni ndani ya dakika tano tu, wote wakapitiwa na usingizi, alichokifanya Richard ni kumuinua na kuanza kuondoka naye kwenye gari. Hakukuwa na mtu aliyekuwa na hofu yoyote ile, walijua ni mtu ambaye alilewa hivyo alikuwa akipelekwa kwenye gari.
“Oya washikaji! Mtu wenu huyu hapa,” alisema Richard huku akimuingiza Vivian ndani ya gari hilo.
“Safi sana!” alisema Robinson, akawasha gari na kuondoka mahali hapo kwa mwendo wa kawaida tu.
 
NYEMO CHILONGANI.
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Ishirini na Tatu

Vivian alikuja kurudiwa na fahamu akiwa ndani ya chumba kidogo kilichokuwa na mwanaga hafifu. Alishangaa, hakujua ni kwa namna gani alifika ndani ya chumba kile. Alikalishwa kwenye kiti na mikono yake ikiwa imefungwa kwenye kiti kile.
Alijaribu kujitoa lakini alishindwa, hakuishia hapo tu bali akajaribu hata kuitoa miguu yake, akashtuka kuona nayo ikiwa imefungwa kama ilivyokuwa mikono ile. Aliumia, alijaribu kufikiria ni kwa jinsi gani alifika mahali pale.
Alikumbuka mara ya mwisho alikuwa kwenye sherehe ya mmoja wa wanachuo wenzake, Vonso, huko alikula na kunywa na mwisho wa siku hakukumbuka kilichokuwa kimeendelea baada ya hapo.
Akaanza kuita kuomba msaada, alikuwa akilia, moyo wake ulikuwa na hofu tele, alihisi kabisa huo ndiyo ungekuwa mwisho wake, asingeweza kutoka, asingeweza kuwasiliana na mtu yeyote pale na mwisho wa siku angekufa ndani ya chumba hicho kitu ambacho hakutaka kabisa kuona kikitokea.
Wakati akipiga kelele, mara mlango wa chumba kile ukafunguliwa na Robinson kuingia, hakumfahamu mtu huyo kwani hata uso wake ulifichwa na nguo iliyotengenezwa kwa staili ya kininja. Akaanza kumuomba msamaha japokuwa alikuwa na uhakika hakuwa amefanya kosa lolote lile.
Robinson alimwangalia, msichana huyo ndiye ambaye angewafanya wapate pesa nyingi, kwa kumtumia huyo ndiye ambaye wangewafanya kuendelea kutafuta dola bilioni nne. Vivian alipoona Robinson hamsaidii kwa lolote lile zaidi ya kusimama na kumwangalia tu, akaanza kupiga kelele za kuomba msaada kitu kilichomfanya Robinson kuchukua gundi ya plastiki na kumfumba mdomo.
Baada ya sekunde chache mlango ukafunguliwa na Richard kuingia, kama alivyokuwa Robinson naye alivalia kininja, alibaki akimwangalia msichana yule, alikuwa dili kubwa mno ambapo baada ya kuzungumza na baba yake basi wangejua ni kitu gani kilitakiwa kufanywa.
Walizungumza kwa dakika moja na kutoka ndani ya chumba kile huku wakiwa na simu ya Vivian, huko walipokwenda, wakachukua namba ya mzee James na kumpigia kwa lengo la kumpa taarifa kwamba binti yao alikuwa kwao, walimtaka kufanya jambo moja tu, vinginevyo basi wangemuua kama walivyowaua watu wengine.
Kwa jinsi mzee huyo alivyosikika kwenye simu, alionekana kuogopa, alijawa na hofu na mpaka simu inakatwa walijua dhahiri kwamba angefanya kile walichotaka akifanye.
“Ila si wanaweza kudukua simu yake na kujua alipo?” aliuliza Richard na Robinson kuanza kucheka.
“Yaani waidukue simu ambayo ipo mikononi mwangu! Basi nitakuwa nimeshuka kiwango kwa kiwango kikubwa sana,” alisema Robinson huku akicheka, kwa kile alichoambiwa, kilimfanya kutoa tabasamu pana.
***
Dokta James alichanganyikiwa, kilichotokea kilimtisha mno, aliogopa, alihisi kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa maisha ya binti yake. Hakumuona binti yake usiku uliopita, alimpa ruhusa ya kwenda kwenye sherehe ya rafiki yake lakini mpaka asubuhi ya siku hiyo hakuwa amerudi nyumbani.
Alimpigia simu lakini haikupokelewa na baada ya dakika kadhaa haikuwa ikipatikana kabisa. Hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea huko, alichanganyikiwa, mke wake hakuwa na amani hata kidogo, alikuwa mtu wa kulia tu, moyo wake ulimwambia kwamba kulikuwa na jambo baya lililokuwa limetokea hivyo walitakiwa kuhakikisha wanawasiliana na polisi ili kuanza kufuatilia kila kitu.
Hawakutaka kuchelewa, simu ikapigwa mpaka katika kituo cha polisi ambapo wakafika hapo na kuanza kuzungumza nao. Waliwaambia kila kitu, ni kwamba binti yao aliaga usiku uliopita lakini kitu cha ajabu kabisa mpaka muda huo hakuwa amerudi nyumbani.
Polisi walichukua maelezo yao, wakachukua namba ya simu na kuanza kumtafuta. Kwa sababu waliambiwa na wazazi hao kuhusu uwezekano wa kutekwa, wakawasiliana na maofisa wa FBI (Federal Bureau of Investigation) na kuwaambia kila kitu, yaani kwa sababu wao ndiyo walikuwa na uwezo zaidi yao wa kuwatafuta watu waliotekwa, wakaamua kuwaachia hao.
Maofisa wa FBI wakawasiliana na wazazi wa Vivian na kuanza kuongea nao, walihitaji kupata maelezo kidogo kuhusu binti huyo, kama ilivyotokea ndivyo walivyowaambia hivyo watu hao kuanza kazi ya kumtafuta msichana huyo.
Kitu cha kwanza kabisa ambacho walikuwa na uhakika ni kuipata simu yake. Walijua ni lazima huko alipokuwa alikuwa na simu hivyo lingekuwa jambo zuri kama wangeidukua na kujua kila kitu. Wakafanya hivyo, kitu kilichowashangaza ni kwamba simu ilionekana lakini cha ajabu haikujulikana mahali ilipokuwa.
Hilo likawashtua kidogo, wakahisi kulikuwa na jibu, wakaendelea kuitafuta, ilishindikana kabisa kitu kilichowafanya kuhisi kuwa msichana huyo alitekwa na mtu ambaye alikuwa na utalaamu mkubwa wa kucheza na network.
Maofisa wa FBI hawakutaka kukata tamaa, walihitaji kufuatilia kamera, michoro yao na kila kitu lakini bado hawakupata kitu. Hawakuishia hapo, kitu ambacho walikuwa na uhakika ungekuwa mwanzo mzuri ni kuzungumza na marafiki zake ambao walikuwa katika sherehe hiyo.
Wakawasiliana nao na kuonana, wakawauliza maswali mengi kuhusu usiku huo ambao Vivian alitekwa na watu wasiojulikana.
“Alikuwa amelewa sana, yeye na watu wengine, alikuwa na kijana mmoja hivi, akamchukua na kumpeleka ndani ya gari,” alisema msichana mmoja.
“Ilikuwa ni majira ya saa ngapi?”
“Ni kama saa nane usiku hivi!”
“Aina ya hiyo gari?”
“BMW nyekundu,” alisema.
“Ulibahatika hata kuona namba?”
“Hapana! Niliona ubavu ubavu tu,” alijibu.
“Na ndani ya hilo gari kulikuwa na watu wengine?”
“Nahisi hilo kwani mlango ulipofunguliwa, nilimuona kama mtu mwingine hivi, ila sikumfahamu hata kidogo,” alijibu.
“Na huyo mtu aliyemchukua alikuwa Mzungu ama mweusi?”
“Mweusi!”
“Tunashukuru!”
Hivyo ndivyo vitu ambavyo walihitaji kusikia kutoka kwa watu hao, waliwahoji wote mpaka Vonso ambaye ndiye aliyekuwa amewaalika watu hao, kwenye mahojiano hayo aliwaambia kwamba hakufahamu kitu chochote kile.
Ni kweli hakufahamu, mpango uliokuwa umefanyika ulimficha, walimuandalia sherehe pasipo kujua kama watu hao walikuwa na mpango wao kwenye hilo.
Maofisa wakaendelea na kazi yao, waliamini kwa kile walichokuwa wamekipata kingewasaidia lakini mpaka siku tatu baadaye hawakuwa wamefanikiwa kumpata msichana huyo kitu kilichowafanya kuhisi walikuwa wakipambana na watu waliokuwa hatari sana.
“Mambo yamekuwa magumu sana, taa za barabarani zinaonyesha matukio, ila ikifika majira ya saa 8:23 usiku, kamera zinaonekana kuzima na baada ya dakika kadhaa kuwaka. Nadhani hawa watu waliofanya huu mchezo ni hatari sana kwenye mambo ya teknolojia na hata kuzidukua kamera za barabarani,” alisema ofisa mmoja ambaye alilifuatilia jambo hilo kwa siku tatu mfululizo lakini hakuwa na majibu juu ya kile kilichokuwa kimetokea.
***
Dokta James na mkewe walikuwa kwenye majonzi makubwa, hawakuwa na raha, muda wote walihisi kabisa binti yao alikuwa ameuawa mahali fulani na mwili wake kufukiwa sehemu.
Walikata tamaa, walimuomba Mungu kwamba kama binti yao huyo hajauawa basi Mungu amlinde mpaka siku ambayo wangemtia mikononi mwao. Waliwategemea maofisa wa FBI na polisi kwamba wangefanikiwa kumpata binti huyo lakini kitu cha kushangaza mpaka siku tatu zinakatika hakukuwa na mategemeo yoyote yale.
Baada ya kutimia siku ya nne, mzee James akapokea simu kutoka kwa namba ambayo haikuonekana kwenye kioo cha simu yake, mtu aliyepiga alimwambia kwamba kulikuwa na mazungumzo walitakiwa kuongea ambayo kama yangekwenda vizuri basi angempata binti yake akiwa salama kabisa.
“Nataka kwanza nisikie sauti yake,” alisema mzee James, hilo halikuwa tatizo, Vivian akapewa simu na kuisikia sauti yake akilia huku akiomba msaada.
“Nadhani umeridhika,” alisema Robinson.
“Niambie unataka nini!”
“Tunataka kitu chepesi sana ambacho utaweza kutupatia haraka sana,” alisema Robinson.
“Kitu gani?”
“Tunataka ukamtoe Hernandez gerezani,” alisema Robinson.
Mzee James alishtuka, hakujua mwanaume huyo alimaanisha nini, hakuhusika na gereza, hakukuwa na jambo lolote lile kuhusu yeye na mfungwa huyo. Alijua alifungwa katika gereza lililokuwa na ulinzi mzito, isingekuwa kazi nyepesi kumtoa lakini watu hao walimwambia kwamba ingewezekana kama tu wangeshirikiana.
“Hivi unalijua lile gereza lilivyokuwa na ulinzi mkubwa?” aliuliza mzee James.
“Najua sana! Lakini huwezi kuamini, mbali na ulinzi huo lakini bado unaweza kumtoa mtu huyo gerezani,” alisema Robinson.
Kwa kuliangalia lilikuwa jambo gumu sana kwake lakini Robinson aliendelea kumsisitiza kwamba lingekuwa jambo jepesi mno.
Robert akapewa simu na kuanza kuzungumza na mzee huyo, alimwambia mpango wao, kitu cha kwanza alitakiwa kutafuta dawa zilizokuwa na nguvu ya kusimamisha mapigo ya moyo kwa saa sabini na mbili lakini pia walitakiwa kuwa na baruti ambazo angepewa kijana mmoja huko gerezani, jinsi ya kuonana na kijana huyo ni yule ambaye angekuja ofisini mwake kutibiwa na kumpa hizo baruti na kiasi cha dola elfu moja na kumwambia aende akazipige ndani ya gereza hilo majira ya saa kumi jioni, muda ambao vijana hao watatu watakuwa nje na daktari huyo kwa lengo la kumzika Hernandez.
Aliambiwa kila kitu na mwisho kabisa akaambiwa kwamba kama mpango huo usingekamilika basi ndiyo ungekuwa mwisho wa maisha ya binti yake.
Maneno hayo yalimshtua na kumfanya kuhisi kwamba alitakiwa kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha mpango huo unafanyika. Baada ya kumalizia kila kitu, akaambiwa aende katika park ya Santana iliyokuwa hapohapo New York ambapo huko angekutana na baruti, kiasi cha pesa na hivyo kutakiwa kuanza kazi hiyo siku inayofuatia.
“Haina shida.”
Hiyo ndiyo kazi aliyopewa, kwa jinsi maelekezo juu ya kile alichotakiwa kufanya alivyopewa aligundua kabisa kwamba watu hao hawakuwa na masihara hata kidogo, walikuwa ni watu wenye akili kubwa ambao walikuwa na uwezo wa kufanya jambo lolote lile.
Kwa kile alichoambiwa, hakuwahi kufikiria hata kidogo kama kuna mtu angemwambia hivyo, mbinu hizo zilikuwa kubwa, za kisasa ambazo zilimpa uhakika kwamba kusingekuwa na mtu yeyote yule ambaye angegundua kama mtu huyo alitoroshwa.
“Nitafanya hivyo! Nitapambana kwa ajili ya mtoto wangu,” alijisemea mzee huyo huku akiwa na uhakika wa kufanikiwa kwa kile alichoambiwa.

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumamosi.
 
NYEMO CHILONGANI.
DILI LA DOLA BILIONI 4

Sehemu ya Ishirini na Tatu

Vivian alikuja kurudiwa na fahamu akiwa ndani ya chumba kidogo kilichokuwa na mwanaga hafifu. Alishangaa, hakujua ni kwa namna gani alifika ndani ya chumba kile. Alikalishwa kwenye kiti na mikono yake ikiwa imefungwa kwenye kiti kile.
Alijaribu kujitoa lakini alishindwa, hakuishia hapo tu bali akajaribu hata kuitoa miguu yake, akashtuka kuona nayo ikiwa imefungwa kama ilivyokuwa mikono ile. Aliumia, alijaribu kufikiria ni kwa jinsi gani alifika mahali pale.
Alikumbuka mara ya mwisho alikuwa kwenye sherehe ya mmoja wa wanachuo wenzake, Vonso, huko alikula na kunywa na mwisho wa siku hakukumbuka kilichokuwa kimeendelea baada ya hapo.
Akaanza kuita kuomba msaada, alikuwa akilia, moyo wake ulikuwa na hofu tele, alihisi kabisa huo ndiyo ungekuwa mwisho wake, asingeweza kutoka, asingeweza kuwasiliana na mtu yeyote pale na mwisho wa siku angekufa ndani ya chumba hicho kitu ambacho hakutaka kabisa kuona kikitokea.
Wakati akipiga kelele, mara mlango wa chumba kile ukafunguliwa na Robinson kuingia, hakumfahamu mtu huyo kwani hata uso wake ulifichwa na nguo iliyotengenezwa kwa staili ya kininja. Akaanza kumuomba msamaha japokuwa alikuwa na uhakika hakuwa amefanya kosa lolote lile.
Robinson alimwangalia, msichana huyo ndiye ambaye angewafanya wapate pesa nyingi, kwa kumtumia huyo ndiye ambaye wangewafanya kuendelea kutafuta dola bilioni nne. Vivian alipoona Robinson hamsaidii kwa lolote lile zaidi ya kusimama na kumwangalia tu, akaanza kupiga kelele za kuomba msaada kitu kilichomfanya Robinson kuchukua gundi ya plastiki na kumfumba mdomo.
Baada ya sekunde chache mlango ukafunguliwa na Richard kuingia, kama alivyokuwa Robinson naye alivalia kininja, alibaki akimwangalia msichana yule, alikuwa dili kubwa mno ambapo baada ya kuzungumza na baba yake basi wangejua ni kitu gani kilitakiwa kufanywa.
Walizungumza kwa dakika moja na kutoka ndani ya chumba kile huku wakiwa na simu ya Vivian, huko walipokwenda, wakachukua namba ya mzee James na kumpigia kwa lengo la kumpa taarifa kwamba binti yao alikuwa kwao, walimtaka kufanya jambo moja tu, vinginevyo basi wangemuua kama walivyowaua watu wengine.
Kwa jinsi mzee huyo alivyosikika kwenye simu, alionekana kuogopa, alijawa na hofu na mpaka simu inakatwa walijua dhahiri kwamba angefanya kile walichotaka akifanye.
“Ila si wanaweza kudukua simu yake na kujua alipo?” aliuliza Richard na Robinson kuanza kucheka.
“Yaani waidukue simu ambayo ipo mikononi mwangu! Basi nitakuwa nimeshuka kiwango kwa kiwango kikubwa sana,” alisema Robinson huku akicheka, kwa kile alichoambiwa, kilimfanya kutoa tabasamu pana.
***
Dokta James alichanganyikiwa, kilichotokea kilimtisha mno, aliogopa, alihisi kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa maisha ya binti yake. Hakumuona binti yake usiku uliopita, alimpa ruhusa ya kwenda kwenye sherehe ya rafiki yake lakini mpaka asubuhi ya siku hiyo hakuwa amerudi nyumbani.
Alimpigia simu lakini haikupokelewa na baada ya dakika kadhaa haikuwa ikipatikana kabisa. Hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea huko, alichanganyikiwa, mke wake hakuwa na amani hata kidogo, alikuwa mtu wa kulia tu, moyo wake ulimwambia kwamba kulikuwa na jambo baya lililokuwa limetokea hivyo walitakiwa kuhakikisha wanawasiliana na polisi ili kuanza kufuatilia kila kitu.
Hawakutaka kuchelewa, simu ikapigwa mpaka katika kituo cha polisi ambapo wakafika hapo na kuanza kuzungumza nao. Waliwaambia kila kitu, ni kwamba binti yao aliaga usiku uliopita lakini kitu cha ajabu kabisa mpaka muda huo hakuwa amerudi nyumbani.
Polisi walichukua maelezo yao, wakachukua namba ya simu na kuanza kumtafuta. Kwa sababu waliambiwa na wazazi hao kuhusu uwezekano wa kutekwa, wakawasiliana na maofisa wa FBI (Federal Bureau of Investigation) na kuwaambia kila kitu, yaani kwa sababu wao ndiyo walikuwa na uwezo zaidi yao wa kuwatafuta watu waliotekwa, wakaamua kuwaachia hao.
Maofisa wa FBI wakawasiliana na wazazi wa Vivian na kuanza kuongea nao, walihitaji kupata maelezo kidogo kuhusu binti huyo, kama ilivyotokea ndivyo walivyowaambia hivyo watu hao kuanza kazi ya kumtafuta msichana huyo.
Kitu cha kwanza kabisa ambacho walikuwa na uhakika ni kuipata simu yake. Walijua ni lazima huko alipokuwa alikuwa na simu hivyo lingekuwa jambo zuri kama wangeidukua na kujua kila kitu. Wakafanya hivyo, kitu kilichowashangaza ni kwamba simu ilionekana lakini cha ajabu haikujulikana mahali ilipokuwa.
Hilo likawashtua kidogo, wakahisi kulikuwa na jibu, wakaendelea kuitafuta, ilishindikana kabisa kitu kilichowafanya kuhisi kuwa msichana huyo alitekwa na mtu ambaye alikuwa na utalaamu mkubwa wa kucheza na network.
Maofisa wa FBI hawakutaka kukata tamaa, walihitaji kufuatilia kamera, michoro yao na kila kitu lakini bado hawakupata kitu. Hawakuishia hapo, kitu ambacho walikuwa na uhakika ungekuwa mwanzo mzuri ni kuzungumza na marafiki zake ambao walikuwa katika sherehe hiyo.
Wakawasiliana nao na kuonana, wakawauliza maswali mengi kuhusu usiku huo ambao Vivian alitekwa na watu wasiojulikana.
“Alikuwa amelewa sana, yeye na watu wengine, alikuwa na kijana mmoja hivi, akamchukua na kumpeleka ndani ya gari,” alisema msichana mmoja.
“Ilikuwa ni majira ya saa ngapi?”
“Ni kama saa nane usiku hivi!”
“Aina ya hiyo gari?”
“BMW nyekundu,” alisema.
“Ulibahatika hata kuona namba?”
“Hapana! Niliona ubavu ubavu tu,” alijibu.
“Na ndani ya hilo gari kulikuwa na watu wengine?”
“Nahisi hilo kwani mlango ulipofunguliwa, nilimuona kama mtu mwingine hivi, ila sikumfahamu hata kidogo,” alijibu.
“Na huyo mtu aliyemchukua alikuwa Mzungu ama mweusi?”
“Mweusi!”
“Tunashukuru!”
Hivyo ndivyo vitu ambavyo walihitaji kusikia kutoka kwa watu hao, waliwahoji wote mpaka Vonso ambaye ndiye aliyekuwa amewaalika watu hao, kwenye mahojiano hayo aliwaambia kwamba hakufahamu kitu chochote kile.
Ni kweli hakufahamu, mpango uliokuwa umefanyika ulimficha, walimuandalia sherehe pasipo kujua kama watu hao walikuwa na mpango wao kwenye hilo.
Maofisa wakaendelea na kazi yao, waliamini kwa kile walichokuwa wamekipata kingewasaidia lakini mpaka siku tatu baadaye hawakuwa wamefanikiwa kumpata msichana huyo kitu kilichowafanya kuhisi walikuwa wakipambana na watu waliokuwa hatari sana.
“Mambo yamekuwa magumu sana, taa za barabarani zinaonyesha matukio, ila ikifika majira ya saa 8:23 usiku, kamera zinaonekana kuzima na baada ya dakika kadhaa kuwaka. Nadhani hawa watu waliofanya huu mchezo ni hatari sana kwenye mambo ya teknolojia na hata kuzidukua kamera za barabarani,” alisema ofisa mmoja ambaye alilifuatilia jambo hilo kwa siku tatu mfululizo lakini hakuwa na majibu juu ya kile kilichokuwa kimetokea.
***
Dokta James na mkewe walikuwa kwenye majonzi makubwa, hawakuwa na raha, muda wote walihisi kabisa binti yao alikuwa ameuawa mahali fulani na mwili wake kufukiwa sehemu.
Walikata tamaa, walimuomba Mungu kwamba kama binti yao huyo hajauawa basi Mungu amlinde mpaka siku ambayo wangemtia mikononi mwao. Waliwategemea maofisa wa FBI na polisi kwamba wangefanikiwa kumpata binti huyo lakini kitu cha kushangaza mpaka siku tatu zinakatika hakukuwa na mategemeo yoyote yale.
Baada ya kutimia siku ya nne, mzee James akapokea simu kutoka kwa namba ambayo haikuonekana kwenye kioo cha simu yake, mtu aliyepiga alimwambia kwamba kulikuwa na mazungumzo walitakiwa kuongea ambayo kama yangekwenda vizuri basi angempata binti yake akiwa salama kabisa.
“Nataka kwanza nisikie sauti yake,” alisema mzee James, hilo halikuwa tatizo, Vivian akapewa simu na kuisikia sauti yake akilia huku akiomba msaada.
“Nadhani umeridhika,” alisema Robinson.
“Niambie unataka nini!”
“Tunataka kitu chepesi sana ambacho utaweza kutupatia haraka sana,” alisema Robinson.
“Kitu gani?”
“Tunataka ukamtoe Hernandez gerezani,” alisema Robinson.
Mzee James alishtuka, hakujua mwanaume huyo alimaanisha nini, hakuhusika na gereza, hakukuwa na jambo lolote lile kuhusu yeye na mfungwa huyo. Alijua alifungwa katika gereza lililokuwa na ulinzi mzito, isingekuwa kazi nyepesi kumtoa lakini watu hao walimwambia kwamba ingewezekana kama tu wangeshirikiana.
“Hivi unalijua lile gereza lilivyokuwa na ulinzi mkubwa?” aliuliza mzee James.
“Najua sana! Lakini huwezi kuamini, mbali na ulinzi huo lakini bado unaweza kumtoa mtu huyo gerezani,” alisema Robinson.
Kwa kuliangalia lilikuwa jambo gumu sana kwake lakini Robinson aliendelea kumsisitiza kwamba lingekuwa jambo jepesi mno.
Robert akapewa simu na kuanza kuzungumza na mzee huyo, alimwambia mpango wao, kitu cha kwanza alitakiwa kutafuta dawa zilizokuwa na nguvu ya kusimamisha mapigo ya moyo kwa saa sabini na mbili lakini pia walitakiwa kuwa na baruti ambazo angepewa kijana mmoja huko gerezani, jinsi ya kuonana na kijana huyo ni yule ambaye angekuja ofisini mwake kutibiwa na kumpa hizo baruti na kiasi cha dola elfu moja na kumwambia aende akazipige ndani ya gereza hilo majira ya saa kumi jioni, muda ambao vijana hao watatu watakuwa nje na daktari huyo kwa lengo la kumzika Hernandez.
Aliambiwa kila kitu na mwisho kabisa akaambiwa kwamba kama mpango huo usingekamilika basi ndiyo ungekuwa mwisho wa maisha ya binti yake.
Maneno hayo yalimshtua na kumfanya kuhisi kwamba alitakiwa kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha mpango huo unafanyika. Baada ya kumalizia kila kitu, akaambiwa aende katika park ya Santana iliyokuwa hapohapo New York ambapo huko angekutana na baruti, kiasi cha pesa na hivyo kutakiwa kuanza kazi hiyo siku inayofuatia.
“Haina shida.”
Hiyo ndiyo kazi aliyopewa, kwa jinsi maelekezo juu ya kile alichotakiwa kufanya alivyopewa aligundua kabisa kwamba watu hao hawakuwa na masihara hata kidogo, walikuwa ni watu wenye akili kubwa ambao walikuwa na uwezo wa kufanya jambo lolote lile.
Kwa kile alichoambiwa, hakuwahi kufikiria hata kidogo kama kuna mtu angemwambia hivyo, mbinu hizo zilikuwa kubwa, za kisasa ambazo zilimpa uhakika kwamba kusingekuwa na mtu yeyote yule ambaye angegundua kama mtu huyo alitoroshwa.
“Nitafanya hivyo! Nitapambana kwa ajili ya mtoto wangu,” alijisemea mzee huyo huku akiwa na uhakika wa kufanikiwa kwa kile alichoambiwa.

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumamosi.

Imekaa Poa sana
 
Wewe jamaa unajaza SERVER za JamiiForums. Hebu rudi Facebook au Insta huko (Au kama una kipaji cha uandishi nenda kaandike vitabu).

Huu uwanja haukufai. Hatupo JF kwaajili ya kuhadithiwa hadithi, tupo kwaajili ya kujadiliana mambo ya msingi.

Mpaka nimeshtuka kuona NOVEL nzima umeshusha hapo.[emoji47] [emoji47] [emoji47]
Hujitambui wewe, vitu gani vya msingi sasa,
Hakuna kipya kazi kujadiliana masuala ya kipuuzi tu ya akina bashite,
Hujui maisha yanahitaji burudani?
Kila siku ni ngonjera tuu tuu tuu hakuna maana.
Sasa kama umeona hii riwaya haikuhusu kaa pembeni au nenda kwenye majukwaa ya siasa siyo kutuletea kiwingu hapa.
Huu ni uendawazimu.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom