SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
Simu; 0757 633010
SEHEMU YA MIA NA TISA
Bosi wa Six killers, Don Genge alikuwa anayaangalia yote hayo kwa umakini mkubwa sana, huku akitabasamu. Aliuhusudu sana uwezo uliokuwa unaoneshwa na vijana wake.
Mbili alivyotua chini alijipanga imara, huku akimkuta Daniel Mwaseba akiwa imara zaidi yake. Wanaume wawili walikuwa tayari kwa kazi! Mmoja kutetea kazi haramu, mwengine kupinga kazi haramu.
Mbili alirusha teke la nguvu kwa mguu wake wa kulia, teke lililokuwa linaenda katika sura ya Daniel Mwaseba, lakini Daniel aliliona. Alifanya mambo mawili kwa kasi ya haraka sana. Daniel alibonyea kwa chini kidogo huku akiufyatua ule mguu wa kushoto wa Mbili uliobaki chini. Kwa mara ya kwanza tangu waanze kupambana Daniel Mwaseba alikuwa amemuweza Mbili. Jamaa alidondoka chini vibaya sana. Ilikuwa mithili ya gunia la viazi limerushwa toka kwenye fuso. Daniel Mwaseba hakutaka kabisa kushangaa, aliruka juu kiasi na kutua kwa nguvu tena kwa miguu yake yote miwili katika tumbo la Mbili wa six killers.
Mbili aliipatapata!
Mkanyago ule ulimwingia barabara Mbili. Alitema majimaji mekundu mdomoni bila kupenda, Ilikuwa ni damu!. Daniel Mwaseba hakuzubaa, aliruka tena juu huku goti lake la mguu wa kulia likielekea shingoni kwa Mbili. Hili sasa lilikuwa pigo la kifo!
Lakini cha ajabu goti lile la Daniel Mwaseba halikufika katika shingo ya Mbili. Ndio halikufika kabisa!
Tano wa six killers aliingilia kati kumuokoa jamaa yake, maana bila hivyo, Daniel Mwaseba alikuwa ameshageuka mbogo!
Tano aliruka juu nae na kumvaa Daniel Mwaseba hukohuko angani.... .
Nini mwisho wa Daniel Mwaseba katika kambi hatari...Je kina Mwanasheria na Dokta Yusha watafanyaje ili kutimiza lengo lao?
ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA