SIMULIZI; BALAA
Mwandishi; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010
SEHEMU YA TISINI NA TANO
"Karibu sana kwenye nyumba ya kifo mpelelezi mahiri nchini Tanzania, Daniel Mwaseba!" Jamaa mmoja kati ya wale watu watatu waliokuwa wanatoka kule katika mlango wa ile nyumba ndogo alisema kwa nyodo na dharau kubwa sana.
Daniel Mwaseba hakujibu kitu chochote alikaa kimya huku akitafuta mbinu ya kutoka salama mahali pale, alitafuta kwa haraka namna ya kujiokoa sehemu ile ya hatari, lakini hakuipata!
Ghafla jamaa wale, wote watatu kwa pamoja waliruka juu na huku wakitanguliza mguu wa kulia mbele.
Yalikuwa mateke matatu kwa mpigo! Yaliyorushwa kwa ufundi mkubwa sana.
Mateke matatu yenye uzito tofauti toka kwa watu watatu tofauti yalitua katika kifua cha mtu mmoja, Daniel Mwaseba. Nguvu ya mateke yale yalimsukuma kwa nguvu Daniel Mwaseba katika ukuta na alijibamiza vibaya sana ukutani! Alisota katika ule ukuta na kudondoka chini taratibu.
Kabla hajainuka wale majamaa watatu walisogea kwa kasi pale alipokuwa amedondokea Daniel Mwaseba. Jamaa aliyekuwa amesimama upande wa kulia alirusha teke lengine kwa mguu wake wa kulia, na yule aliyekuwa amesimama upande wa kushoto nae alirusha teke kwa mguu wake wa kushoto, wakati yule wa kati alikuwa amesimama tu akiangalia ujuzi wa wale wenzake. Mashavu yote mawili ya Daniel Mwaseba yalikutana na shurba. Mateke yote mawili yale yalitua katika mashavu ya Daniel Mwaseba. Damu ziliruka toka katika mdomo wa Daniel Mwaseba. Daniel sasa aliona hakuna tofauti, kufa na kuishi vyote ni sawa, akiwa amelegea kidogo kutokana na mapigo ya wale jamaa aliinyanyua bastola yake tayari kwa kufyatua. Alimuelekeza yule mtu aliyesimama katikati ya wenzake, hakuwa na mzaha sasa Daniel, macho yake yalionesha hivyo. Alikuwa tayari kwa lolote!
Kwa bahati mbaya kabisa hakuwahi kufanya alichokuwa anataka kukifanya.
Yule jamaa aliyekuwa kati aliufyatua mguu wake kwa kasi ya haraka sana na kuupiga ule mkono wa Daniel Mwaseba ulioshika bastola. Kwa macho yake yote mawili Daniel Mwaseba aliishuhudia bastola yake ikiruka angani na kutua katika mikono ya yule jamaa wa kati.
E bwanaa wee!
ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA