SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757633010
SEHEMU YA THEMANINI NA TISA
Dokta Yusha aligonga hodi mara tatu mlango wa Dokta Sharifa Juma, alisimama kidogo baada ya kugonga ile mara ya tatu akisikilizia ndipo alisikia kelele za miguu ya mtu ikielekea pale mlangoni ishara kuwa kuna mtu alikuwa anaenda kufungua ule mlango. Dokta Yusha alijipanga vizuri pale mlangoni, tayari kwa lolote kitakachotokea pale mlangoni. Mlango ulifunguliwa, msichana mmoja mdogo mwenye umri kati ya miaka kumi na sita na kumi na nane ndio alienda kufungua ule mlango.
"Shikamoo kaka" Yule msichana alimsalimia Dokta Yusha pale mlangoni.
"Marhaba hujambo binti" Dokta Yusha aliitikia ile salamu huku macho yake yakiangalia moja kwa moja hadi ndani ya nyumba ile.
"Sijambo kaka" Msichana aliitikia kwa sauti yake ya upole.
"Dokta Sharifa nimemkuta?" Dokta Yusha alitupa karata yake kwa kumuulizia adui yake. Alijitahidi kuuliza kwa sauti ya kawaida kuficha hasira zake kwa Dokta huyo.
"Hapana, dada hayupo" Yule msichana alijibu.
"Kaenda wapi?" Dokta Yusha aliendelea kumuhoji yule dada.
"Dada siku ya tatu leo hajarejea nyumbani, na simu yake haipatikani sijui hata yuko wapi?" Yule msichana alielezea kwa kirefu.
Dokta Yusha akajua mambo sasa yameiva. Kwa vyovyote Dokta Sharifa na wanaharam wenzie watakuwa sehemu fulani, wakiwa wanapanga mambo yao, na pengine kuamua kuzima simu kabisa ili kupunguza bugdha toka kwa watu.
Dokta Yusha aliwaza hayo kwa haraka kichwani mwake, huku mdomoni mwake akitoa jibu.
"Sawa binti"
"Akija dada nimwambie alikuja nani?" Msichana yule aliyeonesha dalili ya uwerevu mkubwa aliuliza.
"Mwambie alikuja Dokta makini, Dokta mwadilifu, Dokta mchapakazi, utakumbuka hilo jina?"
"Ndo jina lako hilo? Nitalikumbuka" Msichana alisema huku akitabasamu.
Dokta Yusha alimuaga yule msichana mwerevu anayefanya kazi kwa Dokta katili sana na kuondoka zake. Sasa alielekea nyumbani kwa Dokta mwengine katili, Dokta Zaidi Kilumba. Huko alikutana na kijana wa kiume mlangoni. Mdogo wake na Dokta Zaidi Kilumba, naye alimpa taarifa zilezile kama alizozipata nyumbani kwa Dokta Sharifa Juma, habari za kutoonekana Dokta Zaidi Kilumba nyumbani kwake kwa siku tatu..
ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA