Msije mkanilisha maneno baadaye. Nasema hapa hapa mwanzoni, si Rais Magufuli wala Kikwete ambaye anawaogopa au aliwaogopa wafanyabiashara. Wafanyabiashara ni watu muhimu kwa uchumi wa kitaifa. Lakini, natumai wote mnajua kama nijuavyo mimi, Rais Magufuli naye ameshajifananisha na Kikwete katika mambo yawahusuyo wafanyabishara.
Ulipotokea wizi wa mabilioni ya shilingi za kitanzania, yaliyochotwa isivyo halali BOT, Rais Mstaafu Kikwete aliwaamuru wafanyabiashara waliohusika 'kurudisha' fedha hizo. Ni kama Rais mstaafu aliwaambia wezi warudishe pesa walizoiba. Wananchi wakasema na kuhema hadi wakalala. Mambo yakapita. Hadi sasa, haijulikani kama zilirudishwa au la na kwa kiwango gani. Maisha yanasonga.
Jana, Rais Magufuli amewapa siku saba wafanyabiashara, waliohusika na kupitisha makontena yao Bandarini bila kulipa kodi, walipe kodi waliyokwepa. Wengi wetu tunajua kuwa kukwepa kodi ni kosa la jinai.
Adhabu ya kukwepa kulipa kodi stahiki ni kubwa tu mhusika anapokutwa na hatia Mahakamani. Ni Rais Magufuli na Serikali yake ndiyo waliogundua ukwepaji kodi wa makontena pale Bandarini. Uchunguzi na kusimamishwa kazi watumishi ukafuata. Rais yuko serious juu ya kadhia hii.
Wakati watumishi wamepoteza na wengine kusimamishwa kazi, wafanyabiashara wahusika wametakiwa kulipa kodi walizokwepa ndani ya siku saba. Is it fair? Wafanyabiashara, jana, walimpigia makofi sana Rais Magufuli wakati akisema hivyo.
Wafanyabiashara hao wakubwa nchini walishusha pumzi na kushukuru kuepukwa na dhahama ya kisheria. Lakini, makontena husika yatajulikana yalikuwa na nini na hata kujua usahihi wa kodi ambayo wafanyabishara walikwepa?
Hakika, katika hili la wafanyabishara watenda jinai, Rais Magufuli amefanana na Rais Mstaafu Kikwete!
Mzee Tupatupa wa Lumumba, Dar es Salaam