Tumkumbushe rais wetu aliyetambua taasisi ya urais alipobakiza mwaka mmoja
Kikwete ameigeuza CCM kampuni binafsi
MWANZONI kabla hajaingia kwenye nafasi ya juu ya uongozi wa nchi na hatimaye chama tawala (CCM), Jakaya Mrisho Kikwete, alionekana anaweza kuvivaa viatu vya Mwalim Julius Kambarage Nyerere!
Hii haikuwa, Jakaya Mrisho Kikwete amekuwa mbali na falsafa ya ujenzi wa jamii ya watu walio sawa na huru; badala yake ameifanya CCM kuwa kama kampuni binafsi.
Kabla ya mfumo wa siasa ya demokrasia ya vyama vingi Tanzania ilikuwa nchi ya chama kimoja cha siasa CCM. CCM, kama chama, chama siasa kilivimeza vyama vya TANU na ASP vyama ambavyo vilishiriki katika kuleta sura ya uhuru wa mwanzo wa nchi za Tanganyika (1961) na Zanzibar (1964).
Waliyeasisi TANU na ASP walikuwa na lengo la kuifanya siasa itumikie wananchi kwa maendeleo yao ili kwa siasa safi na uongozi bora waondokane na aina zote za uonevu, unyonyaji, na kupuuzwa kulikotokana na unyonge wa Mwafrika (kama ilivyoainishwa kwenye Azimio la Arusha).
Dhamira ya CCM ilikuwa kuendeleza mapinduzi ya kufuta unyonge wa Mwafrika wa Tanzania! Na ndiyo maana, Mwalimu Nyerere aliasisi Ujamaa na Kujitegemea kama falsafa na njia ya kujenga jamii ya watu waliyo sawa na huru kwa kutumia chama kinachowakilisha matakwa ya wakulima na wafanyakazi wazalendo.
Kwa kipindi chote cha uhai wa muasisi wa Siasa ya Ujamaa wa Tanzania, Mwalimu Julius K. Nyerere, muelekeo wa siasa na uchumi uliyoongozwa na chama (CCM) ulikuwa kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na si maslahi ya watu wachache wenye ubinafsi. Hata hivyo, hali ya siasa iliendelea kubadilika kidogokidogo hadi pale uongozi wa Awamu ya Pili (chini ya uenyekiti wa CCM wa Mzee Ali Hassan Mwinyi) ulipolitelekeza Azimio la Arusha na badala yake kuliasisi na hatimaye kuliweka Azimio la Zanzibar, 1992.
Pamoja na msukumo wa Azimio la Zanzibar (1992) na hatimaye kuanza kwa mfumo wa demokrasia ya vyama vingi (tazama Ibara ya 3(1), Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977 (2005)) sanjari na sera hiyo mpya ya CCM juu ya kuendesha siasa, uchumi na jamii; CCM iliendelea kujiweka kwenye mazingira ya mabadiliko ya kimfumo na kuchukuwa sura tofauti na ile iliyoasisi vuguvugu la Ujamaa na Kujitegemea ambalo ndilo msingi wa siasa ya Tanzania kwa mujibu wa Ibara ya 9 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977 (2005).
Uongozi wa CCM uliendelea kurithi viatu vilivyokuwa vya Mwalimu Nyerere awamu baada ya awamu hadi ilipofika Awamu ya Tatu awamu iliyoshuhudia kupanuka kwa demokrasia ya uwazi na ukweli huku kukiwa na usiri mkubwa wa uendeshaji wa shughuli za Serikali uliyopelekea kuibuka kwa kundi hatari la wafanyabiashara na wajasiriamali wa kisiasa waliyeamua kuwekeza kwenye siasa, huu ulikuwa mwanzo wa CCM kuvamiwa na mtandao wa wafanyabiashara mafisadi.
Benjamin William Mkapa, Rais wa Awamu ya Tatu ndiye aliyeshuhudia kifo cha Mwalimu Julius K. Nyerere na hatimaye kuahidi na kuapa kufuata nyayo za muasisi huyo wa CCM aliyechukia uonevu, unyonyaji na kupuuzwa kulikotokana na unyonge wa Mwafrika.
Hata hivyo, kadri siku zilivyokuwa zinakatika hata miaka mitano ya mwisho ya urais wa Benjamin William Mkapa sehemu kubwa ya athari za CCM kuwa chama kinachowakilisha maslahi ya wakulima na wafanyakazi ilianza kutoweka na kuchukuwa muelekeo wa kuwatumikia watu wachache wenye maslahi ya kibinafsi mwanzo wa ufisadi wa kimfumo na ujambazi wa kiserikali.
Kwa kutambua matumizi ya fedha na rushwa ya uchaguzi kwenye mchakato wa kuingia Ikulu, jambo lililokemewa sana na Mwalimu Nyerere (rejea Hotuba ya Mei Mosi, 1995 aliyoitoa Uwanja wa Sokoine Mbeya), Jakaya Mrisho Kikwete aliunda Mtandao wa Ushindi uliyotumika kuhakikisha anapata nafasi ya kuwa mgombea wa urais wa CCM na hatimaye Rais wa Tanzania!
CCM ilianza kuchukua sura ya kuwa kampuni ambapo wafanyabiashra mtandao waliyopewa nafasi kwenye ubinafsishaji, ambao Mwalimu Nyerere aliuita unyanganyi, walipoanza kuchukuwa nafasi muhimu za kutawala siasa, uchumi na jamii.
Wafanyabiashara matajiri, hususan wenye