Mahakama Kuu ya Malawi imetupilia mbali matakwa ya kuhesabu upya kura. Akitoa hukumu, saa 3 usiku jana, kwa saa za Malawi, Jaji Kenyata Nyirenda, alisema kwamba kifungu cha 99 cha sheria ya Uchaguzi wa Rais, kinaeleza kwamba matokeo hayana budi kutangazwa ndani ya siku nane, ambazo mwisho wake ulikuwa jana 30.5.14, na kwamba sheria haitoi nafasi ya kuongezwa muda huo. Hivyo akaiagiza Tume ya Uchaguzi, kutangaza mara moja matokeo rasmi ya Uchaguzi. Muda mfupi baadaye, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi (MEC), Jaji Maxon Mbendera, alimtangaza rasmi, Profesa Peter Mutharika wa chama cha Upinzani cha DPP, kuwa mshindi kwa kupata 36.4% za kura. Aliyefuatia, ni Mchungaji Lazarous Chakwera wa chama cha MCP, aliyepata 27.8%. Aliyekuwa Rais, Joyce Banda, amekuwa wa tatu kwa kupata 20.2%, na wa nne, ni Atupele Muluzi wa UDF, aliyepata 13.7%. Baada ya kutangazwa matokeo hayo, maelfu ya wafuasi wa DPP walijimwaga mitaani kusherehekea ushindi, na muda mfupi baadaye, Joyce Banda aliyakubali matokeo. Profesa Peter Mutharika ataapishwa kuwa Rais, saa 4.30 asubuhi hii, kwa saa za Tanzania, katika viunga vya Mahakama Kuu ya Malawi.