Niliua kwa Kukusudia--31-
ILIPOISHIA KWENYE IJUMAA:
"Ni kweli Inana, sikuwa sawa kwani nina matatizo makubwa mno mdogo wangu."
"Matatizo gani tena dada yangu jamani?" Inana aliuliza huku akinikazia macho kwa shauku kubwa ya kutaka kujua kilichonisibu.
"Elhakimu alinibaka na kunitupa mtaroni."
"Unasemaje wewe?" Inana aliuliza huku machozi yakitengeneza mifereji machoni mwake.
SASA ENDELEA…
Kufumba na kufumbua machozi yakaanza kumtiririka Inana. Nilipoona hivyo, machungu yakanishika nami nikajikuta nikianza kulia. Tulilia kwa uchungu mkubwa huku tukimuuliza Mungu kulikoni aendelee kuruhusu matatizo yazidi kutuandama.
"Kwa nini sisi Mungu, kwa nini jamani?" Inana alilia huku akitamka maneno hayo.
"Hapana usiseme hivyo Inana, huenda Mungu ana mpango wake kwetu," nilimtia moyo mdogo wangu Inana huku nikiendelea kulia kwa uchungu na maumivu makali yasiyokuwa na kipimo wala kusimulika kwa namna yoyote ile.
Moyoni niliendelea kuwachukia mno wanaume. Nikaona si viumbe wema hata kidogo. Wakati tukiendelea kulia, ghafla kuna jambo lilinishitua mno na kujikuta nikisitisha kidogo kulia. Kilichonishitua ni kiwango cha kulia alichokuwa akikionesha Inana. Kwani alilia kwa sauti kubwa na kwa muda mrefu mno. Hakika alionesha uchungu mwingi kuliko hata mimi ambaye nilikuwa nimekumbwa na tatizo hilo.
Ikabidi ninyamaze na kuanza kumbembeleza kwa kumtaka aache kulia kwani kama ni kubakwa tayari nilishabakwa. Na kwa wakati huo nilikuwa nikielekea polisi kudai haki yangu.
"Hapana dada, kuna jambo limeniuma zaidi," alianza kusimulia Inana kwa sauti ya kitetemeshi iliyoambatana na kwikwi ya hasira.
"Jambo gani tena Inana zaidi ya hili la kwangu la kubakwa na Elhakimu?," nilimuuliza nikitaka kujua ni jambo gani lililomuumiza zaidi Inana kama alivyokuwa akidai.
"Samahani kwa kuwa nilikuficha dada, hata mimi huyo Elhakimu alinibaka nyumbani kwa mdogo wake ninapofanya kazi."
Nilikuwa kama niko ndotoni. Maneno ya Inana nikayachukulia kama ndoto ndefu ambayo kwa hakika niliamini kama ingekoma muda si mrefu na kubaki katika hali yangu ya kihalisia.
"Ni kweli kabisa dada, Bosi wako Elhakimu alinibaka mwezi mmoja uliopita sasa, lakini niliogopa kukuambia kwani ni jambo la aibu na udhalilishaji wa hali ya juu mno," alisema Inana huku nikizidi kumshangaa kwani sikuwa tayari kabisa kuyaamini maneno yake.
Kabla sijasonga mbele na simulizi hii, hapa naomba niweke wazi jambo moja muhimu sana.Ukweli ni kwamba hadi sasa nikiwa nasimulia hivi, sijawahi kuisahau siku hiyo kwani ilibadili kabisa mfumo mzima wa maisha yangu. Moyoni nikaanza kujiona kama nimebadilika na kuwa na roho chafu ya kinyama. Nilianza kuhisi harufu ya damu ikinukia kutoka kila pande ya dunia na ulimwengu kwa ujumla.
Basi ngoja niendelee. Inana akanisimulia mkasa mzima kwa jinsi alivyobakwa na Elhakimu kabla hajanibaka mimi. Akasema siku ya tukio Elhakimu alienda nyumbani kwa mdogo wake aitwaye Ashraf mahali ambako mdogo wangu alikuwa akifanya kazi. Kama utakumbuka ni Elhakimu ndiye alinipa wazo la kumtafutia mfanyakazi Ashraf na kulazimika kumfuata Inana huko Chalinze nilikokuwa nimemuacha akihangaika na vibarua vya kujitafutia riziki.
Haya ngoja niendelee. Inana alisema kuwa siku hiyo alikuwa peke yake nyumbani ndipo Elhakimu akafika na kuanza kuzungumza naye. Katika mazungumzo yao, Inana alikuwa akishangaa kuona Elhakimu akimsogelea kila sekunde iliyokuwa ikiondoka.
Inana akaendele kusimulia kuwa, Elhakimu alianza kumshika pasipo ridhaa yake na kuanza kumvua nguo kwa nguvu huku akimwambia maneno ya kimapenzi. Pamoja na kukataa huku akitoa upinzani mkubwa wa kujinasua mikononi mwake, Elhakimua alizidi kutumia nguvu nyingi na hatimaye kufanikisha kumvua nguo zote na kuanza kumwingilia mwilini bila huruma!
Akaweka wazi kuwa, baada ya tukio hilo Elhakimu aliondoka na kumuacha akiwa hajitambui na damu nyingi zikimtoka lakini alipozinduka na kukuta hakuna mtu, aliamua kujikanda kwa kutumia majani ya mtapei yalitokuwa nyuma ya nyumba hiyo ambapo aliyachemsha. Hata alipokuja bosi wake hakuthubutu kumweleza chochote.
Akaendelea kuishi kwa taabu na kujifichaficha hadi alipopona kabisa.
Hadi Inana anamalizia kusimulia mkasa huo wa kubakwa na Elhakimu, sikumbuki vyema machozi yalikuwa yamefika wapi kwani hata macho yalikuwa hayawezi kufumbua vizuri kutokana na kuzidiwa na wingi wa machozi. Haraka nikajikuta nikigairi kwenda kituo cha polisi kuendelea na kesi na kujikuta nikiamua kuchukua uamuzi hatari mno.
Je, ni uamuzi gani huo? Itakuwaje? Kufuatilia leo jioni Usikonde tu