Niliua kwa Kukusudia - 29
[h=1]ILIPOISHIA [/h]Wakati nakata kona ya kuelekea nyumbani kwangu, ghafla lilikuja gari moja la kifahari jeusi lililokuwa na vioo vyeusi visivyoonesha ndani na kupaki karibu kabisa na miguu yangu.
SASA ENDELEA…
Nilishituka na kusogea pembeni kidogo ambapo nilianza kuchungulia kwa umakini ili kujua ni nani aliyekuwa ndani ya gari hilo.
Nikiwa naendelea kusumbua ubongo wangu juu ya hilo, ghafla niliona kioo cha upande wa dereva kikianza kushuka taratibu, nikatoa macho nikiwa na hamu ya kujua ni nani aliyekuwa ndani. Bila kutarajia alishuka yule mdogo wake na Elhakimu aliyekuwa akiishi na mdogo wangu Inana.
"Habari za kwako?" alinisabahi huku akionesha uso wa uchangamfu wa hali ya juu. Sikumjibu kwa furaha kama siku zote, hali iliyomlazimu ashuke haraka ndani ya gari na kuja hadi nilipokuwa nimesimama. Akaanza kuniangalia kuanzia miguuni hadi utosini mwa kichwa na kushusha tena macho taratibu huku akionesha dalili zote za kunishangaa.
"Vipi Tunu, kulikoni?"
"Hapana, niko sawa na mdogo wangu anaendeleaje?"
"Anaendelea salama, lakini ni kama una tatizo, naweza kukusaidia tafadhali!"
"Aah, hapana lakini naomba ukifika nyumbani umwambie kuwa namhitaji aje kwangu, sawa?"
"Sawa lakini chukua hii kama nauli maana jua linaanza kuwa la utosi sasa," alisema Ashraf ndipo nikagundua wazi kwamba hakuwa akijua unyama alionitendea kaka yake Elhakimu.
Akaingiza mkono mfukoni na kutoa pochi lake la kutunzia fedha, haraka akatumbukiza mkono na kutoa noti nyekundu kama tano hivi.
Baada ya kunipa akarejea kwenye gari lake akaondoka huku akiniacha nikiwa nimesimama wima.
Japo hapakuwa mbali sana na mahali nilipokuwa nikiishi, Ashraf hakulijua hilo, nikajikongoja kuelekea nyumbani kwangu.
Maumivu yalikuwa ni makali ambapo licha ya kupewa dawa nyingi zikiwemo zile za kuzuia maambukizi lakini niliendelea kupata maumivu makali sehemu zangu za siri na kiunoni.
Kadiri maumivu yalivyozidi kushamiri kila nilipokuwa nikipiga hatua, ndivyo chuki dhidi ya Elhakimu zikazidi kunipanda, kwa mara ya kwanza maishani mwangu nikatamani kulipiza kisasi kwa kuua!
Yalikuwa ni mawazo mabaya mno kwa mtoto wa kike tena binti mdogo kama mimi kuyawaza, lakini sikuwa na jinsi, hakika nikajikuta nikidhamiria kuua japo hadi wakati huu sikujua nitaua kwa njia gani.
"Lakini kwani lazima uue, hakuna njia nyingine ya kulipiza kisasi tofauti na kuua," nilisikia sauti ikijirudia nafsini mwangu. Nikazidi kubaki njia panda.
Wakati nausogelea mlango, ghafla sauti ya marehemu mama yangu ikaanza kusikika moyoni.
"Hakika usilipize baya kwa baya, siku zote epuka maisha ya visasi kwa wakukoseao, kamwe usilipe kisasi kwa yoyote akutendeaye kosa, hata kama ni kubwa namna gani," ilikuwa ni sauti ya mama ikijirudia kwa kasi ya umeme, maneno ambayo alipenda kuniambia mara kwa mara enzi za uhai wake.
"Hapana mama, kwa hili utanisamehe, siwezi kuacha kulipiza kisasi kwa mtu kama Elhakimu, hapana mama, nisamehe mama yangu popote ulipo, lazima nilipe uovu huu, tena kwa sasa natamani kuua, nisamehe mama, hata Allah anisamehe kwa hili.
"Kwani si uliamua kutegemea sheria, subiri akamatwe na haki yako itapatikana ndipo sheria ichukue mkondo wake, kuliko hiyo hatua mbaya ya kuua unayotaka kuichukua," sauti nafsini mwangu ikazidi kuchukua nafasi kubwa. Nilikuwa katika wakati mgumu na mbaya mno.
Kwa hapa naomba niweke wazi kitu kimoja kabla sijaendelea na simulizi hii ya kuumiza.
Maumivi juu ya tukio hilo la kubakwa na Elhakimu yalikuwa ni mara mbili, mosi alikuwa amenivunjia malengo yangu ambayo nilikuwa nimejiwekea kuwa ni lazima mume wangu aikute heshima yake ya ndoa. Lazima awe wa kwanza kukipasua kikombe changu, sasa ndoto na malengo hayo yalikuwa yamefutwa na Elhakimu. Hakika nilimchukia kuliko kiumbe chochote kinachoishi chini ya jua.
Pili, sikuwahi kufikiri kama kuna siku nitadhalilishwa kama alivyonitendea Elhakimu, hakika moyo wangu ulikuwa umejawa na maumivu makali yasiyosimulika kwa maneno wala maandishi.
Mateso, maumivu, simanzi, huzuni na masononeko yalikuwa ni sehemu ya maisha yangu kwa wakati huo, hakika sikujua ni kwa nini Elhakimu ambaye nilimheshimu na kumchukulia kama mzazi wangu alifikia hatua ya kunifanyia unyama ule bila ya chembe ya huruma.
"Lazima niue," nilijikuta nikitamka maneno hayo kwa sauti ya juu.
Je, nini kitaendelea? Fuatilia Usiku mwingi...