Kila siku tunaambiwa ni kwa nini CHADEMA walikubali kumpokea Lowassa mtu waliyekuwa wanamtuhumu kwa ufisadi wakati akiwa CCM. Hoja hii ya kukera inayoshabikiwa na kundi la watu ya aina ya
Mzee Mwanakijiji na
Nyani Ngabu siyo tu ni dhaifu bali pia inakera.
Siasa si nasaba ya kiasili (Gene) kwamba ukizaliwa CCM basi ukoo wako milele utakuwa ni CCM ama CHADEMA, bali ni mchezo ambao kanuni yake kubwa ni kufanikisha Agenda inayokubaliwa na chama husika cha siasa. Lowassa alipokuwa CCM alikuwa ni kihimili cha mfumo wa chama hicho, kina Kikwete na wenzake walikuwa anamtumia Lowassa kuunganisha nguvu za wanaopingana ndani ya chama hicho.
Mtu mwenye nguvu kama hiyo ndani ya chama cha siasa unatarajia vipi wapinzani wake wasimshambulie. Halafu CHADEMA walikuwa wanatumia taarifa za Kamati ya Mwakyembe kumshambulia Lowassa na wala si nje ya taarifa hizo. Kusema kwamba kwa kuwa CHADEMA walisema Lowassa ni fisadi basi anakuwa fisadi ni jambo la kustaajabisha kabisa.
Hoja kubwa ya CHADEMA wakati ule na hata sasa ni kuwa kama kina Mwakyembe waliona Lowassa kaitia hasara nchi kwenye Kandarasi ya kufua umeme iliyohusisha Kampuni ya Richmond, kwa nini asifikishwe mahakamani? Kina Mnyika na Lema kwa kutumia mbinu za kisiasa walikuwa wanasema kuwa inakuwaje wezi wa kuku wako magerezani wakati Lowassa yupo mtaani anadunda?
Swali la Msingi kama ufisadi wa Lowassa ulitokana na CHADEMA kusema ni fisadi wao CCM kama chama msimamo wao wakati ule ulikuwaje, walikuwa wanaona kwamba Lowassa ni fisadi ama si fisadi? Ajabu kubwa kuliko yote ni ukiwauliza wana CCM ufisadi wa Lowassa ni upi wanaishia kusema waliosema Lowassa ni fisadi ni CHADEMA!!
Mpaka sasa Lowassa anatuhumiwa tu kwamba ni Fisadi lakini hakuna hoja au ushahidi mahsusi kuonesha kwamba yeye kweli ni Fisadi. Na inawezekana akawa "fisadi" kwa kutumia mbinu na sheria kama za Recep Tayyip Erdogan wa Uturuki na kina siye ndiyo tutakuwa Fethulla Gulen wa zama hizo!!
Hoja kwamba CHADEMA ndiyo "walisema" kuwa Lowassa ni fisadi ni za uwezo wa chini sana katika kujenga hoja. Tunataka mtu aje atuambie yeye anaposema kuwa Lowassa ni fisadi basi na atuambie kuwa ufisadi wake ni upi. Tumechoka kuishi kwa uvumi!!
Anaandika Mtatiro kabla hajanunuliwa na Lowassa
NINI KINAWEZA KUMWANGUSHA?
Mambo matano yanaweza kumwangusha Lowassa. La kwanza ni makundi. Kama nilivyoeleza, yeye ndiye mtu mwenye kundi kubwa kuliko wagombea wote ndani ya CCM, ikiwa chama hicho kitaamua kumpata mtu wa kati ‘neutral’ ili kukifanya chama kisitetereke, yeye ndiye atakayekuwa wa kwanza kuenguliwa.
Lakini jambo la pili ni kashfa ya Richmond. Tangu kashfa hiyo ilipotokea, Lowassa hakuwahi kuiongelea tena na hajawahi kuwaeleza Watanzania alihusikaje na kama yeye hakuhusika ni kina nani waliohusika kwa majina. Ukweli ni jambo muhimu kwa mtu anayehitaji kuongoza nchi. Ukituhumiwa kwa kashfa kubwa kama ya Lowassa halafu unasema tu hukuhusika bila kueleza nani walihusika huku wewe ndiye ulikuwa Waziri Mkuu, inajenga taswira kuwa kuna jambo kubwa unalificha na husemi ukweli kwa jamii yako. Hili linaweza kumhukumu. CCM inaweza kumuondoa Lowassa ili kuondokana na mgombea mwenye madoa hata kama haina uthibitisho na madoa hayo kwa asilimia 100.
Jambo la tatu linaloweza kumchuja Lowassa ni afya yake. Pamoja na kuwa afya ni jambo binafsi na siri ya mtu lakini kwa kiongozi, kila jambo lake ni mali ya umma. Rais Kikwete alipougua tezi dume aliutangazia umma na hakuficha. Kwa kipindi kirefu Lowassa amekuwa akionekana kama mgonjwa na si siri kuwa amekuwa akipata matibabu katika hospitali za kimataifa nje ya nchi.
Anapaswa awaeleze Watanzania nini kinamsibu, la asipofanya hivyo wapinzani wake kisiasa wanaweza kuendelea kulitumia jambo hili ipasavyo na chama chake kikaona lina mantiki na kikalitumia kumsulubu kama “unfit person to lead the nation”. Kila chama kinahitaji mgombea urais wake awe na afya bora, isiyofichwa na inayoeleweka. Anapaswa kujitokeza na kufafanua hili haraka na hasa ikizingatiwa muda umekwenda sana.
Michango ya kujitolea kila kukicha katika taasisi mbalimbali, harambee, nyumba za ibada na maeneo mengine ni jambo jingine linaloweza kumhukumu. Lowassa amejitolea mno katika eneo hili. Chama chake kinaweza kujiuliza kwa nini mtu anayejiandaa kugombea urais ajitolee kwa kiwango hiki kusaidia kuchangisha fedha na hata yeye mwenyewe kuchangia kila panapotokea matukio makubwa?
Je, nia yake ni sahihi? Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kuwa “Ikulu hakuna biashara” na CCM inaweza kujitathmini ikiwa mgombea wa namna hii akiingia Ikulu hataanza kutafuta mbinu ya kujirudishia fedha alizokuwa akichangia. Eneo hili si salama kwa Lowassa.
Jambo la tano ni madai kuwa kuna maelewano hafifu na Rais Kikwete. Jambo hilo hakuna aliyethibitisha, lakini huwezi kulidharau moja kwa moja. Katika siasa, ukishindana na walioshikilia “mpini” unaweza kuanguka mahali usipotarajia. Pamoja na kuwa “hawakukutana barabarani”, ukweli ni kuwa Lowassa na Kikwete wa sasa si wale ‘ma-comrade’ wa 2008 kurudi nyuma. Hawa wa sasa ni watu tofauti na duru za ndani ya Serikali zinaonyesha kuwa haziivi.
Kama hivyo ndivyo basi, karata za Lowassa zinaweza kuingia shakani kwa sababu ya kutoimarisha uhusiano wake na Rais anayeondoka madarakani, maana kwa siasa za kurithishana kwa kujuana katika vyama tawala barani Afrika, lazima tukubali ukweli kuwa, Rais aliyeko madarakani ana mchango na ushawishi mkubwa katika kutengeza rais ajaye.
ASIPOCHAGULIWA (MPANGO B)
Namuona Lowassa akiwa na mipango mitatu ikiwa hatapitishwa kugombea urais:
Mpango wa kwanza ni kuendelea kuihamasisha jamii kimaendeleo katika taasisi za kidini, za kiraia, makundi ya vijana, wazee na wanawake kwa mtindo huuhuu ambao amekuwa akiufanya kati ya 2008 –2015 na hata kutoa michango yake na marafiki zake kwa jamii.
Mpango wa pili ni kuishauri Serikali katika maeneo mbalimbali ya kisera na kiusimamizi. Kwa sababu alipokuwa Waziri Mkuu alionyesha usimamizi mzuri na ufuatiliaji imara katika ofisi za umma, anaweza kuifanya kazi hiyo kiushauri.
Mwisho ni kurudi kwenye biashara. Lowassa ni mfanyabiashara katika sehemu kubwa ya maisha yake. Ikiwa hatagombea urais kwa tiketi ya CCM itakuwa muda muafaka kwake kurejea na kusimamia biashara zake na kuachana na siasa za majitaka kama alivyowahi kutamka mmoja wa marafiki zake.
HITIMISHO
Nguvu ya Lowassa ndani ya CCM haimithiliki na hofu ya chama hicho kuwa kumuacha nje ya ulingo kutakitetemesha haikwepeki. Lakini ukweli ni kuwa ndani ya CCM “kuna minofu mingi” ambayo inawazuia vigogo wakubwa wasiondoke na kuhamia vyama vingine hata kama hawakupitishwa kugombea urais. “There is too much stake to eat in CCM than going out”.
Ndiyo maana bado CCM ina nafasi ya kujichagulia mgombea inayemtaka na vigogo wanaotajwa kuitikisa kama Lowassa wakiogopa kuondoka kwa sababu wamekaa serikalini muda mrefu na sasa hawawezi kumalizia maisha bila mfumo huo waliouzoea.
Kwa hiyo, nadhani Lowassa ataendelea kuwa mwanachama mtiifu kwa CCM akiwa Rais au akiwa raia wa kawaida. Kama kuna vyama vya upinzani vilikuwa “vinamtumbulia” macho kama fisi asubirivyo mkono wa binadamu udondoke, ni vyema vikajipanga kupata wagombea wake imara na vijijenge. Pamoja na yote haya namtakia kila la heri Mzee Edward Lowassa katika safari yake ya kisiasa.
KUHUSU MCHAMBUZI:
Julius Mtatiro ni Mchambuzi wa Masuala ya Kisiasa na Kijamii, ana uzoefu mkubwa wa uongozi wa kisiasa hapa Tanzania. Ana Cheti cha Juu cha Sarufi na Lugha, Shahada ya Sanaa “B.A” katika Elimu (Lugha, Siasa na Utawala), Shahada ya Uzamili ya Utawala na Uongozi (M.A) na ni mwanafunzi wa fani ya sheria (L LB) – Anapatikana kupitia +255787536759,(juliusmtatiro@yahoo.com) Uchambuzi na huu unatokana na utafiti na maoni binafsi ya mwandishi). (Uchambuzi huu umechapishwa na Gazeti la Mwananchi la Jumatatu, 11 Mei 2015).