Na Chuo cha madini kiko Moshi
Monday, 27 September
Na Kizitto Noya
SEKTA ya madini ni miongoni mwa sekta chache zinazokua kwa kasi nchini. Lakini kwa muda mrefu baadhi ya wafanyakazi migodini, wamekuwa wakifanya kazi bila utalaamu wala mikataba maalumu ya ajira.
Tatizo hilo limeifanya serikali kwa kushirikiana na wadau wengine wa sekta ya madini nchini kuanzisha mradi wa kuwaandaa watalaamu wa kufanya kazi migodini unaojulikana kama Integrated Mining Technical Training Project, (IMTT).
Wazo la kuanzisha mradi huo wenye lengo la kuwapata mafundi sanifu, lilianza mwaka 2008 baada ya wadau kubaini hasara kubwa waliyokuwa wakiipata baada ya kuajiri watu wasiokuwa na sifa migodini.
Serikali, Kituo cha Nishati na Madini (TCME), African Barrick Gold (ABG), ambayo zamani ilikuwa ikijulikana kama Barrick na Aglo Ashanti, ndio walikuwa wadau wa kwanza kufikiri na kukubali kuchangia mradi huo.
Wakati serikali ikichangia mradi huo kwa kutoa chuo cha VETA Moshi, kitumike kama kituo cha mafunzo, AGB na Anglo Ashanti wamechanga fedha kwa ajili ya uwekezaji wa awali katika mradi huo.
Meneja Uhusiano wa ABG Teweli Teweli, anasema kabla ya mradi huo, migodi ilikuwa ikiajiri watu na kuwapa mafunzo wakiwa kazini, jambo ambalo sio tu lilikuwa likiwaletea hasara, bali pia lilipoteza muda mwingi wa uzalishaji.
"Utaratibu huo ulionekana kupoteza hela na muda kabla kampuni haijaanza kunufaika na mfanyakazi. Hivyo wadau wakaamua kuchanga fedha kwa ajili ya kuanzisha mradi huo ili kuwaandaa watalaamu.
"Tunaamini IMTT itasaidia kupunguza gharama hiyo kwa kiasi kikubwa,"anasema Teweli na kubainisha kuwa wakufunzi wa mafunzo hayo wanatoka nchini Afrika Kusini.
Mratibu wa mafunzo katika mradi huo, Yan Kleinhans anataja baadhi ya masomo yanayofundishwa chuoni hapo kuwa ni ufundi mitambo, uchomeaji vyuma, ufundi wa magari makubwa, umeme wa viwandani, umeme mdogo na umeme wa magari.
Anasema mafunzo hayo yanatolewa kwa muda wa miaka mitatu na mhitimu ambaye anapata cheti cha kimataifa cha ufundi sanifu, anaweza kufanya kazi migodini katika nchi yoyote duniani.
Kwa mujibu wa Kleinhans baadhi ya kampuni na migodi inayofatoa ufadhili kwa wanachuo hao ni African Barrick Gold (ABG), Mgodi wa dhahabu wa Geita (GGM), Sandvick Mining, Pan African, mgodi wa dhahabu wa North Mara na African Mining Service.
Anaeleza kuwa nchini Tanzania mradi huo umeanza katika kipindi muafaka kwani nchi nyingi duniani zimekuwa zikihangaika kutafuta watalaamu wa ufundi sanifu na kuwalipa fedha nyingi.
Hata hivyo Kleinhans anasema katika kuuendesha mradi huo, anakumbana na changamoto nyingi lakini kubwa ni kubadilisha fikra za wakufunzi wazalendo ambao wengi wao wanachukuliwa kutoka vyuo vya Veta.
"Nimekuwa pia nikikabiliana na changamoto ya walimu kuwawekea alama za ufaulu wanafunzi wakati uwezo wao ni mdogo. Wanafunzi wengi pia wana uelewa mdogo wa lugha ya Kiingereza ambayo ndio inayotumika kufundishia."anasema.
Mmoja wa wakufunzi wa chuo hicho, Michael Kimambo anaeleza changamoto wanazokumbana nazo wakufunzi kuwa ni pamoja na mishahara isiyoendana na ugumu wa kazi yao.
"Mimi nimeingia kwenye mradi wa IMTT nikitokea VETA. Nilichogundua ni kwamba nimeongezewa majukumu lakini mshahara haujabadilika," anasema na kubainisha kuwa sasa analazimika kufika kazini saa 12 asubuhi na kuondoka saa 12 jioni badala ya saa moja asubuhi na saa tisa na nusu jioni.
Mkufunzi mwingine Hassan Mhavile anasema, kazi ni ngumu na malipo ni kidogo. "Hali hii haitii moyo,"anasema na kuongeza kuwa amefanya kazi na VETA kwa takriban miaka 30 sasa, lakini majukumu aliyonayo sasa ni tofauti na magumu zaidi kuliko alivyokuwa VETA
"Mimi nimefika hapa nikitokea Morogoro, kazi ni nzuri lakini malipo hayaridhishi. Hapa ninabanwa na majukumu muda wote," anaeleza.
Henry Peter naye analalamikia kipato akisema ni kidogo na hakidhi mahitaji hivyo kuitaka serikali na wadau walioanzishwa mradi huo kuwafikiria zaidi.
"Kazi kama unavyoiona, ni nzuri na tunaendelea vizuri lakini tunaomba watufikirie kidogo maana hali ya kipato sio nzuri,"anaeleza Peter.
Anasema mbali na kuongeza watalaamu, sababu nyingine ya kuanzishwa mradi huo ni kupunguza majeruhi wanaopatikana kutokana na kazi za migodini.
"Mafunzo haya ni kwa ajili ya kuongeza uzalishaji lakini usalama kazini ni jambo la muhimu zaidi. Tumelenga kupunguza majeruhi watokanao na kazi za migodini,' anasema.
Mwanachuo, Yasin Msangi anaitaka serikali kukiendeleza chuo hicho kwa vifaa na wakufunzi ili mradi huo uwe endelevu na uweze kulisaidia taifa.
"Kwa mafunzo haya, naarajia kuwa mtu makini kazini na kuongeza umaarufu nitafanya kazi kwa nguvu na bidii zangu zote ili nijenge jina na niwe soko la kimataifa,"anasema.
Anaendelea, "Wito wangu kwa serikali na wadau wote wa sekta ya madini ni kuwataka wakiendeleze chuo hicho. Wasiishie kwenye mradi wa majaribio tu kama huo bali mafunzo hayo yasambazwe kwenye vyuo vya VETA nchini ili watanzania wengi waweze kuyapata."
Mkuu wa chuo cha VETA Moshi, Daniel Komba anasema pamoja na changamoto mbalimbali, anaamini mradi wa IMTT umekuja wakati muafaka kutokana na sekta ya madini kukua kwa kasi nchini.
"Zamani tulikuwa tunafundisha tu na mwanafunzi alikuwa anajaribiwa kokote, lakini sasa IMTT inatupa fursa mpya ya kuwapeleka wanafunzi kufanya mazoezi kwa vitendo kwenye makampuni ya madini hasa migodini," anasema.