* CCM hawaoni waliyoyaacha ndani ya chama hicho? Mlata It is true that you may fool all the people some of the time; you can even fool some of the people all the time; but you can't fool all of the people all the time.
Monday, 16 May 2011 08:27 newsroom
* Asema kauli za Mbowe zimejaa vituko, njozi
* Awaonya waache kubaka demokrasia nchini
* Mlata: Chadema wamekuwa kero kwa jamii
NA BASHIR NKOROMO, MANYONI
KATIBU wa Halmashauri Kuu Taifa (NEC) CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, amesema madai ya CHADEMA kwamba watafanya nchi isitawalike ni ndoto za mchana na kuwatukana Watanzania. Amesema Watanzania wamefanya uchaguzi kwa amani na kuipa ridhaa CCM kuongoza dola, hivyo kauli za Chadema ni kupingana na maamuzi ya walio wengi na kuwaona hawana busara. Pia, amesema Tanzania ni nchi ya kidemkrasia na ambayo viongozi wake wanapatikana kikatiba, hivyo vitendo na kauli za viongozi wa Chadema ni kubaka demokrasia. Aliongeza jambo hilo kamwe halitavumiliwa na serikali ya CCM na Watanzania kwa jumla litokee, kwani inahatarisha amani na mustakabali wa nchi. Nape aliyasema hayo mjini hapa juzi, wakati akihutubia mamia ya wananchi na wanachama wa CCM wakati wa kuitambulisha Sekretarieti mpya ya Chama. "Sasa Watanzania wanapokuwa wamefikia maamuzi kwa hekima zao halafu mtu mzima kwa kukosa busara anakuja kuwaambia eti anataka nchi isitawalike, watamwelewaje?" alihoji Nape Alisema mara baada ya uchaguzi mkuu kumalizika viongozi wa Chadema chini ya Freeman Mbowe, wamekuwa wakifanya vituko mbalimbali, huku wakitamba kuwa watahakikisha nchi haitawaliki. "Ndani ya Chadema hakuna demokrasia na Mbowe hilo ameshindwa, sasa anataka kuvuruga nchi nzima. Hili haliwezekani hata kidogo, kwani Watanzania si wajinga na wanafahamu baya na zuri na manufaa ya demokrasia," aliongeza Nape. Pia, alitumia fursa hiyo kuwaasa Watanzania kupuuza kauli za Mbowe na wenzake, kwani zinaweza kuliingiza taifa hatarini na kuathiri wasio na hatia kwa manufaa ya wachache. "Tazameni Kenya, baada ya uchaguzi viongozi walizusha malumbano kila mmoja
alirusha maneno akiwa ndani ya nyumba yenye kiyoyozi na ulinzi, lakini mwisho wa siku wananchi ndio wakaingia kwenye maandamano na mauaji kutokea. "Leo wamepatana wanagonganisha glasi za mvinyo katika sherehe mbalimbali, ila maisha ya watu yalipotea na wengine kupata ulemavu mpaka sasa hawajapona. Chadema ndiyo wanataka nchi kwenda huko,haiwezekani," alisema Nape.
Kuhusu Chadema kutumia maandamano ili kupata uongozi wa nchi, Katibu wa NEC ya CCM, Uchumi na Fedha, Mwigulu Nchemba,
alisema hizo ni ndoto, kwani Tanzania ni nchi ya kidemokrasia. Alisema Tanzania ina utaratibu wake wa kufanya uchaguzi kila baada ya miaka mitano na kwamba, wananchi bado wanaipenda na wana imani na CCM, kwani ndiyo maana wameipa nafasi ya kuongoza tena. "Jamani hawa watu vipi, hapa Tanzania kila baada ya miaka mitano tunafanya uchaguzi kupata viongozi, waache kuota ndoto za mchana, kwani Watanzania wamewakataa kupitia uchaguzi sasa maandamano ya nini. Wanataka kuonewa huruma ili waangamize watu?" alihoji Nchemba. Mbunge wa Viti Maalumu, Martha Mlata, alisema maandamano ya Chadema ni kero kwa wananchi na wanarudisha nyuma maendeleo, kutokana na wananchi kujihusisha na uzalishaji mali. Alisema Chadema wameshindwa kwenye uchaguzi halali, na kwamba kama wana uchungu na maisha ya Watanzania wanapaswa kuwahamasisha kufanya kazi na si kuandamana kila kukicha. "Hawa vigogo wanaandamana kwa sababu jioni wanagawana posho na kujipongeza,
lakini wananchi wanarudi nyumbani na kuwaza familia itakula nini. Hawana nia njema hata kidogo, tusikubali kupotoshwa na kikundi
cha watu wachache wenye uchu wa madaraka," alisema Martha. Mkutano huo wa Manyoni, ulitanguliwa na mikutano katika mji mdogo wa Puma na baadaye Itigi, ambapo Naibu Katibu Mkuu wa CCM, John Chiligati alipokea wanachama wapya 70 na baadaye kupokea wengine wapya kwenye mkutano uliofanyika Manyoni. Mapema, Chiligati akifungua shina la wakereketwa wa CCM la Baghdad mjini Itigi, Wajumbe wa Sekretarieti ya CCM Taifa, Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Singida na Kaimu Mkuu wa mkoa huo, Paschal Mabiti walifanya harambee ya papo hapo na kuchangia shina hilo sh. 700,000 kuanzisha mradi.