Mwandishi wa Makala

Mwandishi wa Makala

Joined
Aug 12, 2011
Posts
7,150
Reaction score
14,724
SIKUWAHI kabisa kuwaza kwamba ofisi yangu, ambayo mwenyewe nilipenda kuiita studio, ingeweza kuwa na kiza cha kutisha kiasi kile na hata kufikia hatua ya kunifanya kupagawa na kuogopa mno, mpaka lilipotokea la kutokea katika siku moja majira ya saa sita usiku. Ulikuwa ni usiku ambao sitausahau na ndio maana niliamua kuubatiza jina la Usiku wa kizaazaa!

Kwanza nilidhani labda nilikuwa kwenye usingizi wa mang’amung’amu kwa sababu ya pilikapilika nyingi za kutwa nzima ya siku hiyo zilizokuwa zimenichosha na kunifanya kupitiwa na usingizi, na kwamba yote yaliyokuwa yakitokea yalitendeka wakati nikiwa nipo ndotoni, hivyo, jinamizi la ndoto mbaya isiyoeleweka lilikuwa linanisumbua ndotoni.

Hali ile ikasababisha jasho jepesi lianze kunitoka sehemu mbalimbali za mwili wangu, huku nikihisi ubaridi fulani wa woga wa aina yake ukinitambaa mwilini na mapigo ya moyo wangu yakibadili mwendo wake na kwenda mbio isivyo kawaida!

Wakati nikiwa katika hali ile mara hisia zangu zikanitanabaisha kuwa ile haikuwa ndoto bali ni kitu halisi kilikuwa kinatokea muda huo ndani ya studio yangu. Hisia za tukio lile zikasababisha koo langu likauke ghafla huku nywele zangu zikinisimama kichwani kwa hofu.

Hata hivyo, mara hii milango yangu ya fahamu ilikuwa makini zaidi huku nikijaribu kuishirikisha akili yangu kikamilifu katika kuniletea taarifa za kuaminika ili kujaribu kubaini endapo tukio lile lilikuwa katika mlolongo wa yale matukio ya ndotoni au la!

Nilianza kusikia sauti za ajabu ajabu sana zisizoelezeka ambazo zilikuwa zinasikika kwa fujo pasipo mpangilio kutoka katika kila pembe ya chumba kile na kugeuka kero kubwa masikioni mwangu. Hatimaye niliyakodoa macho yangu kwa hofu huku nikiyatembeza mle studio kutazama huku na kule, na hapo nikakutana na ukungu wa giza nene machoni mwangu.

Hali ile ikanifanya niyatulize vizuri mawazo yangu huku nikijaribu kufikiria vizuri kama ni kweli nilikuwa ndani ya studio yangu au nilikuwa sehemu nyingine ambayo ni tofauti kabisa na studio yangu. Kama ningekuwa mlevi ningeweza kusema labda pombe ya siku hiyo ilikuwa imechanganywa na kemikali au ilikuwa kali kupindukia. Lakini wapi!

Swali kubwa lililonijia kichwani mwangu kwa wakati huo ni je, pale nilikuwa wapi? Sikupata jibu la haraka, hivyo nikaamua kupeleka mikono yangu huku na kule nikijaribu kupapasa ili kujipa uhakika wa wapi nilipokuwa, nilijikuta naigusa computer yangu, kisha nikaishika notebook yangu na vitu vingine vilivyokuwa mbele yangu juu ya meza yangu ya kiofisi. Kwa kufanya vile taratibu fahamu zangu zikaanza kurejewa na uhai.

Niligundua kuwa kumbe nilikuwa bado nimeketi kwenye kiti changu kirefu cha ngozi cha kiofisi ndani ya studio yangu na kwamba muda mfupi tu uliopita nilikuwa nafanya kazi kwenye computer yangu iliyokuwa mbele yangu juu ya meza.

Hali ile ikazidi kunichanganya sana! Sasa maswali zaidi yakazidi kuzunguka ndani ya kichwa changu, je, kama nilikuwa ndani ya studio yangu na muda mfupi tu uliopita nilikuwa nafanya kazi, ni nini basi kilikuwa kimenitokea? Je, ni ulikuwa ni mlolongo mrefu wa matukio ya ndotoni? Hapana… hii haikuwa ndoto! Na kama haikuwa ndoto ni nini basi kilikuwa kinaendelea?

“Hivi naota ama ni kweli?” nilijikuta nauliza kwa sauti yenye kitetemeshi kana kwamba kulikuwa na mtu mwingine ndani ya studio yangu niliyekusudia kumuuliza ili anipe uhakika kuwa sikuwa naota. Ili kuhakikisha kama kweli sikuwa naota nikajifinya kidogo kwenye mkono wangu wa kushoto ili nione kama nilikuwa mzima. Finya yangu ya woga ilinifanya nitumie nguvu kubwa na hivyo nilipata maumivu makali sana.

“Ooh shit!” niling’aka kwa sababu ya maumivu makali yaliyochanganyika na hasira.

“Hmm! Kwani saa hizi ni saa ngapi? Mbona…” niliwaza na kuyakatisha mawazo yangu, nikageuza shingo yangu kuangalia ukutani mahali ilipokuwa imetundikwa saa kubwa ndani ya studio lakini sikuweza kuona kitu bali ukungu wa giza nene ulitanda machoni mwangu.

Nikainua mkono wangu wa kulia ambao niliutumia kuvaa saa, nia ilikuwa kuitazama saa yangu ya mkononi aina ya Hublot Big Bang Ferrari King Gold niliyoiagiza kutoka Dubai kwa dola za Marekani 43,600, sikuona kitu badala yake nilishangazwa kuona kuwa bado ukungu wa giza nene ulikuwa umetanda machoni mwangu. Nikachanganyikiwa maana sasa sikujua tatizo lilikuwa ni nini, macho yangu yalikuwa yamepofuka au giza lilikuwa limetanda ndani ya studio!

“Hapa ni kujikakamua, mimi mtoto wa kiume, sitakiwi kupoteza tumaini kipumbafu hivi,” nilijisemea huku nikijaribu kuinuka lakini nguvu fulani kama sumaku ilinirudisha kwenye kiti. Sikukata tamaa nikapapasa juu ya meza na kuchukua simu yangu aina ya Sumsung Galaxy S7 na kuiwasha tochi ili nione, cha ajabu nayo haikutoa mwanga!

“Oh my God! Inamaana nimeshakuwa kipofu!” nilijikuta nasema kwa huzuni huku nikijitahidi kuyakodoa macho yangu yaliyoona ukungu wa giza nene mbele yangu, nikiwa na hofu kubwa…

Naitwa Maximillian Njamba, maarufu kwa jina la ‘Sauti ya Jamii’, jina nililopewa na jamii yangu, hasa kwa sababu ya kazi nzuri niliyokuwa nikiifanya ya kuisemea jamii yangu, kazi ya uandishi wa makala zilizofanyiwa uchunguzi wa kina kwenye gazeti la Rindima. Gazeti la kila siku ambalo pia nilikuwa mhariri wa makala.

Itaendelea…
 
Mwandishi wa Makala - 2

Naitwa Maximillian Njamba, maarufu kwa jina la ‘Sauti ya Jamii’, jina nililopewa na jamii yangu, hasa kwa sababu ya kazi nzuri niliyokuwa nikiifanya ya kuisemea jamii yangu, kazi ya uandishi wa makala zilizofanyiwa uchunguzi wa kina kwenye gazeti la Rindima. Gazeti la kila siku ambalo pia nilikuwa mhariri wa makala.

Uandishi wangu ulijikita zaidi katika kuandika habari za uchambuzi wa masuala mbalimbali yaliyoihusu jamii yangu, habari zilizokuwa zinazingatia zaidi uzalendo kwa nchi yangu na maslahi ya taifa pasipo kumuogopa yeyote.

Sikusita kabisa kufichua uovu uliokuwa ukifanyika wakati wowote na sehemu yoyote bila kujali ulifanywa na mtu gani au kikundi gani cha watu, ilimradi tu maslahi ya taifa yalionekana kuchezewa, na nilijitoa maisha yangu kwa ajili ya jamii yangu kwa hali na mali bila kujali kama kazi hiyo ingeyagharimu maisha yangu au la.

Kwa kifupi, sikuwa mwandishi wa kubahatisha, nikiwa na miaka ishirini na tisa tu tayari nilikuwa nimeshatunukiwa shahada ya kwanza ya sanaa ya habari na mawasiliano ya umma, na nilikuwa katika mwaka wa mwisho nikimalizia shahada yangu ya sheria, kutoka kwenye moja ya vyuo bora kabisa barani Afrika, Chuo Kikuu cha Dar es Salaama.

Kitu kingine kilichonitofautisha sana na wandishi wengine wa makala ni kwamba nilikuwa mdadisi na mfuatiliaji mkubwa niliyependa sana kujikita kila wakati na kazi zangu ambazo kama ingepita siku bila kuzifanya nilikuwa najisikia upungufu mkubwa.

Kazi ya uandishi wa makala mbalimbali yaliyoigusa jamii ilinijengea heshima kubwa sana miongoni mwa jamii yangu na kunifanya nipate tuzo mbalimbali za kitaifa na kimataifa za umahili, na hata kuniongezea idadi kubwa ya marafiki kutoka kila kona ya nchi na hata nje ya nchi.

Baadhi ya rafiki zangu waliokuwa wakifanya kazi katika mashirika ya habari ya kimataifa kama Reuters, BBC, VOA, DW, CCTV n.k, walianza kunishawishi nihamie huko kwani waliamini kuwa kiwango changu cha uandishi hakikuwa cha nchi hii, na kuendelea kubaki katika gazeti la Rindima ningekidumaza kipaji changu.

Nilikuwa naishi eneo la Ilala Sharif Shamba kwenye nyumba niliyoachiwa urithi na walezi wangu, si mbali sana kutoka yalipo majengo ya Baraza la Sanaa la Taifa. Nilikuwa nikiishi peke yangu kwenye nyumba nzima, kwa kuwa kwa wakati huo sikuwa nimeoa na wala sikuwa na ndugu niliyeishi naye, kwa kuwa sikumjua ndugu yeyote.

Historia ya maisha yangu ilikuwa imejaa masaibu ya kila namna, kwani nilizaliwa na kutupwa jalalani na mama yangu, ambaye sikupata bahati ya kujua taarifa zake kama alikuwa hai au mfu, na hadi wakati huo nilikuwa sijui kwanini mama huyo aliamua kunitupa jalalani, tena nikiwa kwenye mfuko wa sandarusi. Huku nikiwa bado sijakata roho msamaria mwema akaniokota na kuamua kunilea.

Ilikuwa ni pale kwenye jalala dogo karibu na makaburi ya Msimbazi Centre, nilipookotwa na msamaria mwema, ambaye alikuwa bibi mzee aliyeishi maisha ya kubangaiza kwenye nyumba moja ndogo iliyokuwa nyuma ya Msimbazi Centre, jirani na Msikiti wa Sharif Shamba. Bibi huyo alijitolea kunilea japo kwa taabu kutokana na hali yake ya uzee.

Niliambiwa kuwa mara baada ya bibi huyo kuniokota kwanza alinifanyia maombi, na alikuwa na kawaida ya kunifanyia maombi mara kwa mara. Bibi huyo alifariki wakati nikiwa na umri wa miaka mitatu na hivyo nikakabidhiwa kwa binti yake pekee, Mariam, aliyekuwa ameolewa na Mzee Maziku Njamba, hivyo ikamlazimu achukue jukumu la kunilea kama mama.

Kwangu Mariam akawa ndiye mama, na mimi nilikuwa mwanaye. Mzee Njamba akawa baba kwangu. Nami nikawa mtoto wao pekee kwa kuwa hawakuwa na mtoto yeyote kwa wakati huo ingawa walishakuwa na watoto mapacha ambao walifariki wakiwa na mwaka mmoja, miezi michache tu kabla mimi sijakuchuliwa kuishi nao.

Miaka miwili baadaye Mzee Njamba alistaafu kazi kutoka serikalini na kulipwa mamilioni yaliyomwezesha kuifanyia ukarabati mkubwa nyumba yake ya Ilala Sharif Shamba, jirani na Baraza la Sanaa la Taifa.

Wote wawili walijitahidi kunilea vizuri na hata siku moja hawakuwahi kunibagua wala kuonesha jambo lolote ambalo lingenifanya nigundue kuwa hawakuwa wazazi wangu wa kunizaa.

Mzee Njamba alifariki dunia miaka michache baadaye kwa ajali ya gari katika eneo la Vingunguti wakati akitokea Gongolamboto alikokwenda kufuatilia miradi yake, na Mariam kwa wakati huo alikuwa na mtoto mwingine wa kike, Rehema, wa miaka miwili tu. Rehema alikuwa alifariki dunia akiwa darasa la pili kwa ugonjwa ambao hadi leo umeendelea kubaki kuwa kitendawili.

Japo ilimuumiza sana Mariam lakini alimshukuru Mungu na maisha yakaendelea, aliendelea kuwa ni mama mkarimu, mwenye roho ya upole na mchapakazi hodari wa aina yake. Wakazi wengi wa eneo lote la Ilala Sharif Shamba walimpenda sana kutokana na roho yake nzuri.

Alijitahidi kunisomesha na hakuacha kunipa usia mara kwa mara akinisisitiza kusoma kwa bidii, pia alinitaka niwe kijana mwema, nimheshimu kila mtu kwani sijui nani angekuja kunisaidia baadaye.

Nilizingatia masomo na kusoma kwa bidii, hatimaye nilichaguliwa kuingia Shule ya Sekondari ya Benjamin Mkapa, ambapo niliendelea kusoma kwa bidii sana.

Nilipoingia kidato cha nne mlezi wangu alifariki dunia baada ya kusumbuliwa na saratani ya shingo ya kizazi ambayo wakati inagundulika ilikuwa tayari imeshasambaa sehemu kubwa ya mwili wake. Na hali ilipokuwa mbaya sana, hasa katika kipindi cha mwisho cha uhai wake hajafikwa na umauti ndipo aliponiita akanieleza siri kuhusu ukweli wa maisha yangu.

Nikiwa na umri wa miaka kumi na saba wakati huo, niliumia sana baada ya kusikia habari hiyo. Nilijihoji sana nikasema, kwanini mama yangu mzazi aliamua kunitupa jalalani baada ya kunizaa? Je, nilimkosea nini mama yangu na Mungu hadi yanikute yaliyonikuta? Na kama Mariam asingekubali kunilea hivi nigeishia wapi?

Sikuwajua wazazi wangu halisi zaidi ya Mariam na Mzee Njamba, wala sikujua nilizaliwa tarehe ngapi zaidi ya kujua umri wangu tangu nilipookotwa jalalani.

Kitendo cha kuujua ukweli kikawa kimeniumiza sana na maisha yangu yote, tangu siku nilipogundua kuwa mimi sikuwa mtoto wa Mariam na Mzee Njamba, bali walijitolea kunilea kwa mapenzi yote kama wazazi nikajikuta nafanya vibaya sana darasani tofauti na wakati huo ambao nilikuwa sijaujua ukweli wa maisha yangu kutoka kwa mlezi wangu niliyemzoea kama mama.

Hali hii ilinisababisha kufanya vibaya kwenye mtihani wangu wa mwisho, na maisha yangu yakabadilika kabisa, sikuwa tena na hamu ya kuendelea kuishi, nikadhani kuwa bora na mimi ningekufa niwafuate walezi wangu nikapumzike kuliko maisha yale.

Isingekuwa juhudi za rafiki na mshauri wangu mkubwa, Costantino Kimwaga, nadhani hali yangu ingekuwa mbaya zaidi. Costantino alikuwa ni zaidi ya rafiki, alikuwa ni zaidi ya kaka au ndugu yeyote, na muda mwingi alikuwa karibu na mimi akinishauri kila alipoona inafaa.

Ndiye aliyenitia moyo baada ya matokeo yangu kuwa mabaya nikaweza kurudia mtihani na baadaye kufanya vizuri, na hata fani ya uandishi ilipata msukumo mkubwa kutoka kwake, kwani yeye alikuwa mmoja wa wandishi mahiri wa makala za kijamii zilizogusa maisha ya wanajamii na aliandikia gazeti la Rindima.

Studio yangu ilikuwa katika chumba kimojawapo ndani ya nyumba niliyoishi hapo Ilala Sharif Shamba. Ilikuwa ni nyumba kubwa yenye vyumba vitatu ikiwa imezungukwa na ua mpana uliojengwa kwa matofali.

Itaendelea…
 
Mwandishi wa Makala – 3

Studio yangu ilikuwa katika chumba kimojawapo ndani ya nyumba niliyoishi hapo Ilala Sharif Shamba. Ilikuwa ni nyumba kubwa yenye vyumba vitatu ikiwa imezungukwa na ua mpana uliojengwa kwa matofali.

Nyumba hiyo ilikuwa na sebule pana yenye seti moja ya makochi ya sofa yaliyopangiliwa vizuri upande wa kulia wa sebule hiyo. Makochi hayo yalikuwa yanatazamana na seti moja ya runinga aina ya Hitachi ya inchi 24 iliyowekwa juu ya kabati maalum la kuwekea runinga na iliunganishwa na decorder ya Startimes yenye chaneli nyingi za kimataifa.

Upande huohuo wa kulia wa sebule kwenye kona kulikuwa na meza fupi ya mapambo na jokofu aina ya Boss. Katikati ya sebule kulikuwa na meza nzuri ya kioo yenye umbo la yai na stuli ndogo nne zilizokuwa zimepangwa kuizunguka meza hiyo.

Ukutani kulikuwa na saa kubwa na picha mbili kubwa, picha moja ikinionesha mimi na ya pili ilikuwa ya mama yangu mlezi. Upande wa kushoto wa sebule kulikuwa na ukumbi mdogo wa chakula wenye meza kubwa ya chakula iliyotengenezwa kwa mti wa mkongo ambayo ilikuwa imezungukwa na viti sita vya mbao ya mkongo vyenye foronya laini.

Jirani na ukumbi huu wa chakula kulikuwa na korido nyembamba iliyokuwa inakwenda vyumbani. Kulikuwa na milango minne, milango miwili ikiwa upande wa kulia na milango mingine miwili ilikuwa upande wa kushoto.

Mlango wa kwanza kulia ulikuwa wa kuingia kwenye maliwato ya wote, mlango wa pili uliingia kwenye studio yangu, na milango iliyokuwa upande wa kushoto ilikuwa ni ya vyumba vya kulala, ambapo mlango wa mwisho kabisa ndio ulikuwa chumba changu cha kulala chenye maliwato ndani (master bedroom).

Studio yangu ilikuwa ni ofisi ya kawaida tu yenye samani chache za kiofisi. Ilikuwa na zulia lenye rangi za bendera ya taifa la Tanzania sakafuni, meza kubwa ya kiofisi ambayo juu yake kulikuwa na kompyuta aina ya Acer i5 na kioo cha flat, kiti kirefu cha ngozi halisi cha kiofisi chenye magurudumu madogo yaliyokiwezesha kusogea, na kilikuwa kinazunguka.

Pembeni ya ile meza kulikuwa na meza ya kioo ya pembe nne na chini ya meza ile kulikuwa na magazeti na majarida kadhaa tofauti ya siku za nyuma. Meza hiyo ilikuwa imewekwa mbele ya kochi moja la sofa lililokuwa likitazamana na ile meza ndani.

Juu ya meza ile ya kioo kulikuwa na vitabu, nakala chache za magazeti ya siku za karibuni na majarida machache yaliyopangwa kwa ustadi, na kulikuwa na kidau cha wino, mhuri na kichupa kidogo chenye wino mweupe wa kufutia maandishi.

Upande wa kushoto wa ofisi ile kulikuwa na picha kubwa ya Rais John Magufuli na nyingine ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere zikiwa zimetundikwa ukutani. Pia kulitundikwa saa kubwa ya ukutani ya mshale na pembeni ya saa ile kulikuwa kalenda moja kubwa.

Upande wa kulia kulikuwa na dirisha pana la kioo lililokuwa limefunikwa kwa mapazia mawili mepesi marefu ya rangi ya kijivu, pia kulikuwa na rafu kubwa ya mbao iliyosanifiwa kwa ustadi wa hali ya juu.

Ndani ya rafu ile kulipangwa vitabu na majarida chungu nzima yaliyoshika vumbi na kupoteza nuru kutokana na kuhifadhiwa kwa muda mrefu ingawaje mazingira ya mle ndani yalikuwa nadhifu na yaliyovutia kwa mpangilio wake. Mbele ya ofisi ile ukutani kulikuwa na ramani kubwa ya Tanzania, yenye kuonesha maeneo yenye vivutio mbalimbali.

Sikuwa nimechacha, kwenye hiyo studio kulikuwa na jokofu dogo aina ya Boss ambalo lilikuwa halikosi vinywaji baridi na juisi vilivyonichangamsha wakati nikiwa nimechoka baada ya kazi ngumu ya kuandika, na kiyoyozi aina ya Singsung kilichokuwa kikisambaza hewa safi.

Katika usiku ule nilioupa jina la usiku wa kizaazaa nilikuwa nimeketi kwenye kiti changu kikubwa cha ngozi cha kiofisi na chenye kuzunguka ndani ya studio yangu, kama kawaida nilikuwa nikiandaa moja ya makala niliyodhani yangewasisimua sana wasomaji wangu. Makala hayo yalihusu maajabu niliyoyaona katika safari yangu ya kutembelea mapango ya Amboni.

Katika safari hiyo nilijifunza mengi ikiwemo neno Amboni ambalo niliambiwa lilikuwa limetokana na maneno mawili, Mama Mboni pamoja na neno Chiramboni. Mapango ya Amboni yako umbali wa kilomita 8 kutoka Tanga mjini kupitia barabara kuu inayoelekea Mombasa.

Unaweza kufika katika hifadhi ya mapango hayo kwa kupitia mojawapo ya njia zinazoelekea huko. Ya kwanza ni barabara ya changarawe iliyo upande wa kushoto meta 200 baada ya kuvuka daraja la hofu, ya pili iko kilometa 1.5 kutoka daraja la utofu katika kituo cha ukaguzi wa mazao ya misitu. Njia zote zinapitia katikati ya kijiji cha kiamoni.

Katika safari yangu nilivutiwa sana na simulizi zilizoelezea njia za mapango zinazoelekea Mombasa, Maweni, Mkoa wa Kilimanjaro n.k. na simulizi za kina Osale Otango (au Samuel Otango) na mwenzake Paulo Hamis.

Watu hawa walikuwa wakitumia kituo namba tatu ndani ya pango kubwa kama sehemu yao ya kujificha kati ya mwaka 1952 na 1956 huku wakiendesha harakati za kupambana na walowezi waliokuwa wamewekeza katika maeneo ya Tanga. Walipora mali na kutishia maisha ya walowezi katika maeneo mbalimbali.

Serikali ya kikoloni iliwatambua kama wahalifu na kujaribu kuwakamata bila mafanikio kwa kipindi kirefu. Mwaka 1957 Paulo Hamis alipigwa risasi maeneo ya Lushoto na kufariki. Wananchi wa kawaida wanawakumbuka kama mashujaa walioendesha harakati za ukombozi wa watu wanyonge kutoka katika mikono ya walowezi na watawala wa kikoloni.

Pia kingine kilichonishangaza sana ndani ya mapango ya Amboni ni taswira kadhaa za kiimani kama sanamu la bikira Mariamu aliye karibu na malaika huku kitabu kikionekana kikiwa kimefunuliwa.

Pia nikaona Kibla ambayo kulingana na utafiti mdogo wa haraka niligundua kuwa kibla hiyo ilikuwa imeelekea upande sawa sawa na ule wa kibla za mkoa wa Tanga, na upande wa kulia wa kibla hiyo palionekana michoro ya neno ‘Allah’ huku pia pakiwa na mchoro wa alama “M” ambayo nadhani ilikuwa inawakilishayo neno Msikiti ama Masjidi ama Mosque…

Nilikuwa nimeketi hapo tangu saa kumi na moja za jioni nikijaribu kuzitazama baadhi ya picha nilizopiga ndani ya mapango ili kukumbuka baadhi ya maajabu, na nilipokuja kushtuka ilikuwa tayari imekwisha timia saa sita kamili usiku, kwa mujibu wa saa iliyokuwa ukutani.

Hadi muda huo sikuwa nimehisi njaa, ila nilijihisi kuchoka sana. Niliinuka na kufungua jokofu dogo lililomo ndani, nikatoa chupa ya soda baridi aina ya Coke na bilauri, kisha nikafungua kizibo cha chupa ile kwa kifaa maalumu cha kufungulia.

Nilipokuwa katika kutaka kujimiminia ile soda ndani ya bilauri mara mwanga ndani ya studio yangu ulitoweka ghafla japo umeme haukuwa umekatika, na papo hapo kuliibuka vivuli vya ajabu vilivyochukua nafasi ya mwanga. Vivuli vile vikasababisha ukungu wa giza nene kutanda machoni mwangu.

Nje ya dirisha la studio yangu, kuliibuka dhoruba kali kana kwamba kimbuka cha Katrina kilitaka kuisomba nyumba yangu kutokana na namna kilivyokuwa kinatishia kubomoa ukuta wa studio, na muda huohuo mawingu mazito yaliyoambatana na muungurumo mkubwa wa radi yakalijaza anga lote nje ya studio na kuyafanya mandhali ya studio yangu kuwa ya kiza chenye kutisha.

Ndani ya studio hakukuwa na mwanga wowote uliopenya kutoka nje, ingawa umeme ulikuwepo na taa za ulinzi nje ya nyumba au zilizokuwa kwenye milingoti ya umeme na kwenye nyumba za jirani zikiendelea kutoa nuru yake kama kawaida. Nilistaajabu sana kwani hili halikuwa jambo la kawaida kabisa!

Mara ikaanza kusikika sauti ya ajabu ya upepo iliyonitisha sana ikajaa ndani ya studio yangu yenye kiza cha mauti, sauti hiyo iliambatana na matawi ya miti iliyopandwa kwenye ua wa nyumba kujibamiza kwa nguvu karibu ya dirisha la studio yangu.

Itaendelea…
 
Mwandishi wa Makala – 4

Mara ikaanza kusikika sauti ya ajabu ya upepo iliyonitisha sana ikajaa ndani ya studio yangu yenye kiza cha mauti, sauti hiyo iliambatana na matawi ya miti iliyopandwa kwenye ua wa nyumba kujibamiza kwa nguvu karibu ya dirisha la studio yangu.

Studio yangu ambayo mara nyingi nilizoea kuiona ni sehemu nzuri na salama haikuwa tena mahala salama kama ilivyokuwa mwanzo. Nikiwa bado nimeketi katika kiti changu cha kiofisi, mbele ya computer yangu, iliniwia vigumu mno kuona kitu chochote kilichokuwa umbali wa hatua moja mbele yangu ndani ya ile studio.

Mara vile vivuli vya ajabu vikaanza kujikusanya na kutua taratibu hadi juu ya kochi la sofa lililokuwa likitazamana na meza ya kioo yenye umbo la yai ndani ya studio. Japo kulikuwa na mwanga mkali wa radi ambao ulikuwa unapenya ndani lakini haukuniwezesha kabisa kumuona vizuri mgeni wangu aliyekuwa amefichwa na vile vivuli na kuketi katika kochi la sofa lililokuwa likitazamana na ile meza.

Mgeni huyo alikuwa wa ajabu sana na alikuwa amekwisha nitokea zaidi ya mara tatu katika wiki hiyo, hasa tangu siku nilipofikiria kuandika makala kuhusu maajabu niliyoyaona katika mapango ya Amboni, wiki moja tu baada ya kurudi kutoka safari ya Amboni. Na katika siku ya kwanza kabisa ya kukutana naye, nilizihisi hasira alizokuwa nazo mgeni huyo.

Huwa spendi kabisa kuzungumza na mtu mwenye chuki na hasira kama huyo. Hata hivyo, aliendelea kunitaka nifanye naye mahojiano. Kila asubuhi nilipoamka, alikuwa akiniita. Kila nilipoketi mezani kwa ajili ya chakula changu alikuwepo pamoja nami kunipa kampani. Kwa ujumla, alikuwa ni mgeni msumbufu mno. Nilianza kuhisi hasira zikinipanda ndani yangu kila nilipomfikiria.

Hivyo, nilikubali kukutana naye japo kwa shingo upande ili nisikie kisa chake alichotaka nikiandike, kwa kuelewa kuwa baada ya kukisikia basi angeweza kwenda zake, mbali nami na asinisumbue tena. Hata hivyo, sikuwa nimetarajia kupata mgeni wa kunielezea kuhusu kisa chake katika muda ule wa usiku wa manane ulioambatana na dhoruba, radi na tashtiti nikiwa katika chumba cha kiza.

Wakati nikikubali kukutana naye sikuwa nimejali! Nilikuwa tayari kumpokea mgeni huyo ili anisimulie kisa chake na kisha aondoke kabisa kwenye maisha yangu. Nilivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu, nikajaribu kuzungumza kwa sauti yangu nzito kwa kujiamini kama vile hakukuwa na kitu kilichoniogofya.

“Haya,” nilianzisha mazungumzo. “Unaweza sasa kunisimulia, ila ni wapi ungependa kuanzia simulizi ya kisa chako?” niliuliza swali huku nikiwa nimekodoa macho yangu kwenye vile vivuli juu ya sofa, mbele ya meza ya kioo.

Mara hali ya kuogofya ndani ya chumba ikaanza kutulia kidogo japo kiza kiliendelea kutawala na ukungu wa giza nene ulikuwa bado umetanda machoni mwangu.

Kwa sauti yake yenye lafudhi Kirundi, mgeni wangu alianza kujieleza kutoka kwenye vile vivuli juu ya sofa.

“Asante sana kwa kuniona. Hakika wewe ni mtu muungwana sana na nimekukubali mno ndani ya moyo wangu…” alimeza mate na kuondelea.

“Kwa muonekano wa magazeti, majarida na vitabu hivi vyote ndani ya ofisi yako, na kutokana na kile nilichokiona, najua kuwa wewe ni msomi wa kada ya juu. Hujui tu bwana mkubwa.

“Laiti ungejua ni kwa muda gani nimekuwa nausubiri kwa hamu wakati huu ungenihurumia badala ya kunikasirikia. Mara tu nilipokuona siku ya kwanza, nilijua kwamba ulikuwa mtu sahihi kwangu. Asante sana kwa kuniona.”

Nilitabasamu kidogo kwa maneno yake.

“Unakaribishwa sana. Na asante kwa sifa zote ulizonimwagia, lakini mimi ni mwandishi wa makala tu ambaye huwa napenda sana kuandika habari zinazogusa maisha ya watu, sina cha zaidi.”

“Ndiyo, wewe ni mwandishi wa makala unayegusa maisha ya watu, hivyo ndivyo ulivyo mheshimiwa, na utaendelea kuwa hivyo. Nilijua tu mara moja kwamba una karama na ustadi mkubwa katika kuandika habari zinazogusa maisha ya watu. Kwa kweli uko vizuri sana kuliko unavyoweza kufikiri!”

Kwenye kiza kile niliweza kuhisi tabasamu pana likichanua usoni kwa mgeni wangu, na hapohapo nikahisi ubaridi mwembamba ukinitambaa kwa kasi kwenye uti wangu wa mgongo ukianzia kwenye shingo yangu na kuishia kwenye mfereji katikati ya makalio yangu na kunisisimua mno. Hali ndani ya studio yangu ilikuwa ni yenye ukimya mno.

Katika muda wote nilioendelea kuzungumza na mgeni wangu wa ajabu katika chumba chenye kiza sikuweza kuona kitu. Ukungu uliendelea kutanda mbele ya macho yangu. Niliisikiliza sauti yake katika giza na kuhisi kwamba mgeni wangu alikuwa ameketi katika sofa.

“Labda siku moja utakuja kuelewa wewe ni mtu wa aina gani na umuhimu wako kwenye jamii! Ila elewa tu kwamba wewe ni mtu muhimu sana kwa wakati huu na mahali hapa, na kwa kisa hiki ninachokwenda kukusimulia, hakuna mtu mwingine yeyote aliyepaswa kukisikia kwanza isipokuwa wewe. Ni wewe tu…

“Ni muhimu sana ukakielewa kisa hiki. Si tu kwamba unalazimika kukisikiliza kwa makini, bali ni lazima pia uwe sehemu ya kisa hiki. Sijui unaelewa ninachomaanisha?” mgeni yule wa ajabu kwenye kiza aliniuliza kwa sauti ya upole lakini yenye amri.

“Ndiyo, nitajaribu,” nilimjibu mgeni wangu wa ajabu ingawa nilikuwa sipendi kuamrishwa.

“Nitafanya kwa kadiri ya uwezo wangu, lakini tafadhali naomba utambue kwamba ninaweza tu kufanya kwa kadiri ya uwezo wangu na si zaidi ya hapo. Mimi sio mtu yeyote maalumu kama alivyo mchungaji, mwanasaikolojia au mshauri nasaha. Kwa kifupi mimi ni mtu wa kawaida sana kama walivyo wengine.”

Yule mgeni wa ajabu aliangua kicheko kikubwa kilichoacha mwangwi uliosambaa hadi upande mwingine chumba kile. Kilikuwa ni kicheko kisichoweza kusahaulika kabisa kwenye akili yangu na kilionekana kupenya hadi ndani ya mifupa yangu. Kicheko chake kiliashiria kabisa kwamba mchekaji alikuwa akinicheka kutokana na namna nilivyoonekana mjinga nisiyetambua hata thamani na karama niliyokuwa nayo ndani yangu. Kicheko kile kilipokoma, alijibu.

“Usijali utakuwa sawa tu, bwana mkubwa.”

“Okay, ni wapi ungependa kuanzia kusimulia kisa chako?” Nilimuuliza tena mgeni wangu, safari hii nilianza kuhisi donge la hasira likinikaba kooni na mwili wangu kuanza kuchemka kwa hasira, lakini sikuwa na namna nyingine yoyote ya kufanya isipokuwa kumvumilia huyo mgeni.

Itaendelea...
 
Mwandishi wa Makala – 5

“Okay, ni wapi ungependa kuanzia kusimulia kisa chako?” Nilimuuliza tena mgeni wangu, safari hii nilianza kuhisi donge la hasira likinikaba kooni na mwili wangu kuanza kuchemka kwa hasira, lakini sikuwa na namna nyingine yoyote ya kufanya isipokuwa kumvumilia huyo mgeni.

“Kuna mambo mengi ya kusema,” yule mgeni wa ajabu alianza. “Sijui wapi pa kuanzia. Ila jambo la muhimu zaidi unalopaswa kulifahamu ni kwamba mimi ni mtu mzuri sana. Nimekuwa naamini kabisa kwamba siku zote ukifanya mambo yaliyo sahihi, wakati mwingine bila kujali ni maumivu gani yatakutokea, utapata tuzo.

“Maisha yangu yote, niliamini kwamba Mungu humzawadia yeyote mwenye kufanya kazi kwa bidii. Ukifanya mambo yaliyo mema na kufanya kazi kwa bidii, basi tarajia kupata tuzo bila shaka yoyote.”

Nilibetua kichwa changu kuonesha kuwa nilikuwa nakubaliana naye. Hii ilikuwa ni falsafa muhimu na yenye nguvu iliyokuwa inaniongoza katika maisha yangu.

“Naam, nataka hili lijulikane mapema kabisa. Mimi sio mtu goigoi kabisa. Na pasipo kujali nilikuwa na njaa ya kiasi gani, nisingeweza kuiba chakula chochote ambacho nilitakiwa kukilinda. Neno langu ndio dhamana yangu. Bwana mkubwa, najua jinsi ambavyo wewe ni mtu muhimu sana kwangu.” Alisema.

Nilibetua tena kichwa changu kukubali. Yule mgeni aliendelea.

“Mimi na wewe tunafanana sana kwa mambo mengi. Hata hivyo, tofauti yetu ipo kwenye tuzo ambazo kila mmoja wetu amepata baada ya kazi ngumu. Juhudi zangu zote na uaminifu wangu havikunisaidia kabisa kunifikisha pale nilipopataraji kufika na katika namna ile niliyotegemea. Siku zote niliamini kwamba kama ukifanya mambo mema, basi lazima utabarikiwa. Lakini mimi nikalaaniwa badala yake.”

“Ukalaaniwa?” Niliuliza kwa mshangao.

“Mimi sio wa nchi hii. Natoka katika jamii ya Watwa, kabila dogo linalopatikana katika nchi za Burundi na Rwanda. Nilizaliwa katika eneo la Cibitoke, mkoa ulio pembezoni nchini Burundi kwenye mpaka wa Burundi na DR Congo (wakati huo ikiitwa Zaire)…

“Wakati huo hatukuwa na fursa kama zilizopo katika nchi hii. Uhasama wa kikabila kati yetu ulituzunguka na hatimaye ukawa sehemu ya maisha yetu. Baba yangu alikuwa mfanyabiashara wa bidhaa katika duka. Kama unakumbuka vizuri historia ya Burundi, tuliuziana kikabila na kila kitu kilifanywa kiukabila. Mwishowe vita viliibuka miongoni mwetu.”

Nilitabasamu tu bila kusema neno japo sijui kama mgeni wangu aliliona tabasamu langu. Muda huohuo nikakumbuka kuwa nilikuwa na chupa ya soda juu ya meza yangu niliyokwisha ifungua muda mfupi tu kabla mwanga ndani ya studio haujatoweka. Nikapapasa na kuichukua kisha nikaanza kujimiminia soda kwenye bilauri yangu. Povu la soda likapanda haraka na kuijaza bilauri huku likimwagika juu ya meza.

Yule mgeni wa ajabu kwenye kiza akaachia kicheko kilichosababisha tena mwangwi uliosambaa hadi upande wa pili wa chumba.

“Mheshimiwa, unaweza kuwa na akili nyingi sana, lakini unatakiwa kujifunza jinsi ya kumimina kinywaji oevu kwenye bilauri. Kwanza ilaze kidogo bilauri yako ikuelekee, na badala ya kumimina kinywaji moja kwa moja kwenye bilauri, jaribu kumimina ukiufuatisha ukuta wa bilauri na ukiache kitiririke taratibu chini kwenye ukuta na kujiunga na kingine. Hapo utakuwa umepunguza matatizo kidogo.”

Nilijitahidi kukodoa macho yangu kumtazama mgeni wangu katika kiza bila kujua hasa jinsi ya kukabiliana na ushauri wake. Hata hivyo, niliamua kujaribu kama alivyosema. Nikailaza kidogo bilauri na kumimina soda kuufuatisha ukuta wa bilauri huku nikiiacha itiririke taratibu kuelekea chini, soda haikutoa povu kama mwanzo. Nikaachia tabasamu na kubetua kichwa.

“Kweli wewe kiboko!” nilisema huku nikiendelea kutabasamu.

“Sasa tunapaswa kwenda haraka kidogo,” yule mgeni wa ajabu alisema. “Sina muda wa kutosha kuendelea kuwepo mahali hapa. Kwa mbali ninaanza kuuhisi upepo mkali ukitaka kuanza kuvuma tena.”

“Sawa, unaweza kuniambia ulikuwa unafanya nini katika nchi ya fursa?” Niliuliza.

“Haha, eti Nchi ya Fursa,” yule mgeni alisema na kuongeza, “ninacheka kusikia neno hilo. Nakumbuka kulisikia mara nyingi mno tangu nilipokuja katika nchi hii, lakini sidhani kama wananchi wenyewe wanazichangamkia fursa zilizopo katika nchi yao!”

“Okay, ni nini kilitokea?” niliuliza tena nikiwa na shauku ya kutaka kujua kuhusu kisa chake.

“Nilikutana na Swedi Kachenje,” yule mgeni alisema. “Huyu Swedi ndie alivumbua dhahabu eneo la Mwendakulima wilayani Kahama na kuanza kumiliki mgodi, baadaye mgodi huu ulichukuliwa na kupewa wawekezaji wazungu, na kuanzia hapo eneo hilo likajulikana kama mgodi wa Buzwagi

“Ni huyu Swedi ndie alinipeleka mkoani Tanga katika mapango ya ajabu ya Amboni. Nadhani unayafahamu, au sio?”

Kauli yake ilifuatiwa na kicheko ambacho kama kawaida kilisababisha mwangwi uliosambaa hadi upande wa pili wa chumba. Nilianza kukizoea kicheko hicho na kuanza kukichukulia kama cha kawaida.

“Ndiyo nayafahamu mapango ya Amboni,” nilijibu kisha nikaongeza. “Kwani uliwahi kufanya kazi katika mapango hayo?”

Niliuliza kwa shauku kwa kuwa nilitegemea sana kusikia habari zaidi kuyahusu mapango ya Amboni, habari ambazo zingeweza hata kuniongezea taarifa muhimu ambazo ningezitumia kwenye makala yangu, kwa kuwa nilikuwa nimerudi wiki chache tu kutoka katika ziara ya kutembelea mapango hayo.

Alipotaja mapango ya Amboni akawa amenikumbusha kuhusu safari yangu huko, nikakumbuka jinsi mapango hayo yalivyohifadhi maajabu makubwa! Pango langu la kwanza kuingia liliitwa ‘Pango la Jinsia’ ambalo ni pango dogo lakini lenye maajabu ya pekee ambalo ni mzizi wa mti wavule uliochora alama ya "V" ama mshale ili kumuelekeza mtumiaji wa njia ya pango hilo kupata urahisi wa kutoka, ingawa utokaji wake si rahisi bila ya kuwa na muongozaji.

Pia nikakumbuka niliona taswira safi ya muundo wa Bara la Afrika likiwa limejichora katika maajabu ya kupendeza zaidi, huku pia nikiona muundo wa mshumaa ulioyeyuka ambao unazidi kufanya mapango hayo kuwa ya kustaajabisha zaidi hasa pale unapoupanda mlima kilimanjaro na kupenya katika njia nyembamba iliyopo ndani ya mapango hayo.

“Ndiyo, nilifanya kazi katika mapango hayo kwa miaka miwili,” Sauti ya mgeni wangu ikayakatisha mawazo yangu, ambayo yalianza kuchukua nafasi kwenye kichwa changu. Kisha sauti ile ikaendelea.

“Swedi Kachenje aliniambia jinsi mapango hayo yalivyo na utajiri mkubwa wa madini ya dhahabu na kwamba watu wengi hawakujua kuhusu mgodi wa dhahabu wa Amboni. Nadhani umewahi kusikia hadithi hizo kupitia waongazaji watalii ndani ya mapango hayo. Naam Swedi Kachenje aliamini kabisa hadithi hizo zilikuwa za kweli…” Yule mgeni alinyamaza kidogo, lakini niliweza kuhisi kulikuwa na huzuni fulani katika sauti yake.

“Habari ya mgodi huu wa dhahabu iliibua ndani yangu kiu yangu ya kufanikiwa maana siku zote nilifanya kazi kwa bidii ili siku moja nije kuwa mmoja wa watu wenye mafanikio makubwa, na Swedi alinishawishi nikubali kuambatana naye na kufanya naye kazi, kwa ahadi kuwa akifanikiwa atanifanya kuwa mshirika wake kibiashara na ndipo ningepata nafasi ya kuwa tajiri kama yeye.”

Kulizuka ukimya fulani ulioanza kunisisimua. Niliweza kuhisi hasira ikijengeka kutoka kwenye kiza upande wa pili wa chumba.

Itaendelea…
 
Mwandishi wa Makala – 6

Kulizuka ukimya fulani ulioanza kunisisimua. Niliweza kuhisi hasira ikijengeka kutoka kwenye kiza upande wa pili wa chumba.

“Lakini tuzo pekee niliyokuja kutunukiwa ilikuwa ni kuporwa kila kitu,” yule mgeni alisema kwa sauti yenye huzuni.

Mazingira ya chumba yaliendelea kuwa ya utulivu mno kwa dakika nzima. Nilibaki kimya bila kusema neno nikisubiri kusikia kauli yake ya pili. Kwa huzuni iliyojionesha kwenye sauti yake nilitarajia kabisa kushuhudia mwako wa hasira.

“Naam kwa miaka miwili, nilifanya kazi kati ya saa kumi na mbili na kumi na nane kwa siku. Nilipata mapumziko siku moja tu ya mwisho wa wiki. Katika muda wangu wa mapumziko, nilipata nafasi ya kukutana na binti mrembo ambaye dunia hii haijapata kumshuhudia, nadhani ni zaidi hata ya yule wa zama za Mfalme Suleiman, yule Cleopatra. Mrembo huyu wa kwangu aliitwa Tunu.”

Nilipapasa juu ya meza yangu na kuchukua notebook yangu pamoja na kalamu, kisha nikaliandika jina la Tunu kwenye notebook yangu. Nilihisi kukereka kidogo kwa kuwa iliniwia vigumu kuona nilichokiandika kwenye notebook yangu katika giza lile. Niliona wazi kwamba huyu Tunu alikuwa ni kiumbe muhimu sana kwa huyo mgeni wangu.

Hata hivyo, nilikuwa na hamu zaidi ya kusikia habari za mgodi wa madini ndani ya mapango ya Amboni na kazi alizofanya hapo Amboni kuliko habari ya Tunu. Kwangu ilikuwa ni habari ya kusisimua mno kupata nafasi ya kuzungumza na mtu aliyekuwa anayajua vizuri mazingira ya Amboni, na ambaye alifanya kazi kama mchimbaji wa dhahabu katika mapango hayo kwa miaka miwili. Habari hii ilizidisha kiu yangu kutaka kuelewa zaidi kuhusu mapango ya Amboni, hivyo niliamua kubaki kimya na kusubiri.

“Tunu wangu alikuwa mwanamke mrembo sana niliyewahi kumuona duniani, ingawa kwa viwango vyako pengine ungeweza kumuona ni wa kawaida mno. Kutoka kwenye utosi wake hadi kwenye unyayo alikuwa na urefu wa futi tano na inchi tisa. Kwangu mimi, alikuwa ni package nzuri ya upendo na furaha.

“Alikuwa msomi wa kiwango chake, mkimya, mpole na mwenye adabu. Siyo siri alijaaliwa uzuri wa sura na umbo akimkopi mama yake mzazi kuanzia sura, sauti, upole na hata utembeaji wao ulishabihiana sana, na alikuwa na kila sifa iliyomstahili msichana mrembo.

“Kila alikopita, watu wa rika zote kuanzia wazee hadi vijana walimbabaikia sana, na hawakuisha kugeuza vichwa vyao ili kuustaajabia mwili wake jinsi ulivyoumbika!

“Tunu wangu alikuwa tofauti sana na wasichana wengine wengi waliojikweza juu ya kila kiumbe duniani wakitaka wafanane na Malaika, lakini Tunu wangu hakujua kabisa kumdharau mtu, awe mchafu ama mtanashati. Alikuwa akimhesabu kila mmoja wao kuwa ni binadamu aliyestahili heshima zake.

“Hadi sasa bado naweza hata kuisikia sauti yake alipokuwa akiimba nyimbo alfajiri. Nilikuwa nikiamka katika kibanda changu kidogo cha nyumba ili tu niisikie sauti yake. Kulikuwa na nyakati ambazo niliweza hata kuchelewa kazini kwa sababu ya kumsikiliza Tunu.”

“Kwa namna unavyomwelezea huyo Tunu wako, ninaweza kuhisi kabisa alikuwa ni msichana mzuri sana!” Nilisema huku nikishusha pumzi ndefu kwa shauku kutaka kujua huyo Tunu alihusika vipi kwenye hicho kisa cha kuchimba dhahabu kwenye mapango ya Amboni.

“Alikuwa mtu pekee muhimu sana kwenye maisha yangu aliyenifanya nisitake kuondoka Kiomoni. Katika nyakati ambazo nilibahatika kumkumbatia kwenye kifua changu na wakati huo kutembeza mikono yangu kwenye nywele zake nyeusi ilikuwa ni furaha mno. Kulikuwa na nyakati za amani na utulivu. Najua unatamani nikuelezee tulivyokutana, lakini elewa tu kwamba tuliunganishwa pamoja kwa njia ambayo siwezi kabisa kuielezea,” alipofika hapo yule mgeni alinyamaza kidogo, kisha akaendelea.

“Tunu alikuwa ndiye malkia wangu, na mimi nilikuwa na mfalme wake, ingawa nilikuwa mhamiaji haramu, kama mnavyotuita siku hizi, na masikini aliyekuwa na kazi ya kutafuta madini mapangoni kwa ajili ya kuhakikisha anajikimu katika maisha lakini Tunu aliendelea kuwa fahari yangu. Alinifanya nijisikie mimi ndiye mfalme wa ulimwengu wake… Mungu wangu, hakika Tunu alijua jinsi ya kunifanya nijihisi vizuri zaidi.”

Hapo nilijikuta nimekenua meno yangu, hasa nilipokumbuka siku nilipotembelea kwenye mapango ya Amboni wakati wa ziara yangu nilibahatika kutembelea vijiji vilivyo pembezoni mwa mapango ya Amboni, hasa kijiji cha Kiomoni ambacho ndicho alikuwa akiishi Tunu. Kumbukumbu hizi zikanipa hamu ya kutaka kumjua zaidi kuhusu mrembo huyu wa shani.

Siku hiyo ndani ya mapango ya Amboni niliona chumba mfano wa ukumbi wa sherehe ambao kwa juu kidogo kinaonekana chumba cha Dj wa sherehe huku upande wa kulia ikionekana njia ya kupanda kilele cha mlima Kilimanjaro.

Pia niliona kituo au pango ambalo limekuwa likitumika na wazee au watu wa kawaida kufanya matambiko au maombi yao ya kawaida na baada ya kumaliza maombi hayo watu hao hutoa sadaka mahali hapo.

Katika upande mwingine wa pango hilo niliona mfano au muundo wa kiti cha enzi ambacho kilikuwa kikitumika zamani kama kiti cha heshima kwa machifu ama watawala wa zamani. Pia nikayaona maficho ya Osale Otango na Paul Hamis.

Na hapo niliweza kuona aina ya popo wajulikanao kama Fruit Bats wakiwa ndani ya pango hilo wakishiriki sana katika kuongeza michoro ya ajabu ya wanyama, na nyayo za binadamu ndani ya pango hilo kwa upande wa juu.

Sauti ya yule mgeni kwenye kiza ikanikatisha kutoka kwenye mawazo yangu. Muda huo sauti yake ikaonesha msisitizo zaidi.

“Upendo wetu ulikua zaidi na zaidi. Kila wakati tulipokuwa pamoja, niliweza kuhisi nguvu fulani kama ya sumaku katikati yetu. Na kila aliponigusa, alinifanya kujisikia mtu maalumu na mwenye bahati kubwa sana. Lakini nilikuwa naogopa kumtamkia kuwa nilikuwa nampenda.

“Ilikuwa ni siku moja katika matembezi ya jioni kijijini Kiomoni, siku hii iliacha kumbukumbu muhimu katika ubongo wangu. Siku hiyo nilimkabili Tunu na kuizungusha mikono yangu kwenye kiuno chake chembamba mithili ya dondola. Naye alijibu mapigo kwa kuzungusha mikono yake kwenye shingo yangu na kunitazama moja kwa moja kwenye macho yangu.”

Alinyamaza kidogo, kisha kilifuata kicheko kilichoacha mwangwi upande wa pili wa chumba. Kilikuwa ni kicheko kama cha kijana aliye kwenye umri wa balehe. Kicheko chake safari hii hakikuweza kunisisimua kama mwanzo.

“Nilimvuta karibu zaidi na mimi, sikujua ni muda gani aligundua kuwa nilikuwa nataka kumbusu. Ila ilitokea tu automatiki. Wakati nakaribia midomo yake, alikiweka vizuri kichwa chake akiuelekeza mdomo wake sambamba na mdomo wangu. Ilikuwa ni wakati ambao nilihisi mbingu zimefunguka…

itaendelea…
 
Mwandishi wa Makala – 7

“Nilimvuta karibu zaidi na mimi, sikujua ni muda gani aligundua kuwa nilikuwa nataka kumbusu. Ila ilitokea tu automatiki. Wakati nakaribia midomo yake, alikiweka vizuri kichwa chake akiuelekeza mdomo wake sambamba na mdomo wangu. Ilikuwa ni wakati ambao nilihisi mbingu zimefunguka…

“Ooh, Tunu wangu alikuwa ana busu la kichawi lililoweza kumloga mtu yeyote hata asiyelogeka. Mwili wangu ulinisisimka mno na nikahisi kuchanganyikiwa. Ulikuwa ni msisimko ambao ulinifanya nijihisi kutaka kurukaruka juu wakati tulipokuwa bado tunabusiana. Hata hivyo, nilijizuia. Sikuwa mjinga kiasi hicho. Lakini nilitamani mabusu hayo yaendelee hata kwa siku nzima.”

“Kwa hiyo mahusiano yenu yaliishiaje, bila shaka ulimuoa?” Niliuliza tena mgeni huyo kwa shauku.

“Aah, sasa wewe unataka kurukia mwisho wa kisa changu,” ile sauti ilinijibu. “Lazima ukisikie kisa changu katika utaratibu mzuri. Niache nimalize.”

“Sawa, nasikiliza,” Nikajibu.

“Naam, usiku uliofuata tulikutana tena kwa ajili ya matembezi mengine. Nilijua tu siku hiyo kuwa kuna kitu ilikuwa lazima kitokee siku hiyo mara tu nilipomuona Tunu. Macho yake yalikuwa yanacheza cheza kwa msisimko na yaliniashiria nitarajie kitu fulani kutoka kwake. Namaanisha yalikuwa yanapepesa na kuwakawaka kama kioo. Sijui kama unaelewa ninachomaanisha?”

“Nakuelewa,” nikamjibu yule mgeni. “Kwa kweli hali ya namna hiyo huwa ni ishara nzuri sana.”

“Kwa Tunu wangu, ilikuwa ishara nzuri kama usemavyo,” yule mgeni kwenye kiza alisema. “Tunu alipenda sana kunichokoza. Hali hiyo ilikuwa ikinifanya kupata msisimko mkubwa ambao uliniashiria kuwa kulikuwa na kitu kizuri kinakuja. Lazima nilikubali kwamba nilikuwa nimeketi kwenye pembe yenye makali nikiwa nashangaa nisijue nini Tunu wangu alikuwa amekusudia kunifanyia…

“Alisubiri kwa saa nzima hadi tulipofika kwenye juu ya kilima, jambo lililoonekana kunimaliza kihisia. Naam ilikuwa ni eneo zuri mno katika kijiji kile cha Kiomoni. Lilikuwa limepakana na bonde lililotokana na msimu wa mvua za masika ambazo zilitengeneza mkondo wa maji lakini maji hayo yakakauka baada ya msimu wamvua kupita.”

Nilibetua kichwa changu kukubali, nilijaribu kukumbuka kama niliona eneo la aina hiyo nilipotembelea katika kijiji cha Kiomoni. Maeneo ya aina hiyo tulizoea kuyaita makorongo.

“Kisha alinisogelea zaidi, na hapo niliweza kunusa harufu nzuri ya manukato. Kwa kweli utakuwa bado hujainjoi maisha mpaka ukutane na manukato kama ya Tunu. Ilikuwa ni kama vile nimelala katikati ya konde lililojaa maua yenye kunukia vizuri wakati wa majira joto. Alikuwa amejichonya kidogo manukato hayo nyuma ya kila sikio na mengine kidogo aliyatonea katikati ya matiti yake kwenye kifua…”

Yule mgeni alinyamaza na kutulia kidogo kwa sekunde kadhaa. Niliamua kuingilia kati ili kumuonesha kuwa nilikuwa nafuatilia kwa makini kisa chake.

“Katikati ya matiti?”

“Ndiyo,” yule mgeni wangu alisema. “Niilipenda sana harufu yake usiku huo. Nilimbusu na yeye akanirudishia busu, kisha alitoa mkebe mdogo kutoka kwenye mkoba wake…” Yule mgeni alipofika hapo alisita kidogo.

Nilisubiri kwa hamu kusikia kuhusu kilichokuwamo katika mkebe huo mdogo. Hata hivyo, alibaki kimya kwa muda. Nikahisi kuwa alikuwa na huzuni na punde tu kingefuata kilio cha kwikwi lakini sikuwa na uhakika wa nini kingetokea. Hata hivyo, niliendelea kusubiri hadi nione mwisho wake.

Hali ndani ya studio ikawa yenye ukimya mkubwa mno kiasi kwamba nikaanza kuhisi labda mgeni yule alikwisha ondoka mle ndani, hali hiyo ikanitia hofu na nywele zangu zikanisimama. Chumba chote kilizizima na kiliendelea kubaki katika hali ya ukimya na kiza chenye kutisha. Baada ya dakika chache, yule mgeni alizungumza.

“Alipoufungulia mkebe wake, Niliona kitu mfano wa utepe wa dhahabu ukiwa na kito kikubwa cha thamani chenye rangi ya zambarau katikati ya utepe huo. Nilipatwa na mshangao mkubwa. Unaweza kuona kuwa hicho hakikuwa kitu cha kawaida sana kwa mwanamke kumvisha mwanaume pete. Angalau katika utamaduni wa nchi yangu, haijawahi kabisa kufanyika. Jiwe la thamani lenye rangi ya zambarau lilikuwa kubwa juu ya pete lakini halikuwa limechongwa kwa staili ya migongo migongo kama ilivyo kwa vito vingine, badala yake lilikuwa laini. Nadhani unajua ninamaanisha nini?”

Kwa mara nyingine tena nilibetua kichwa changu kukubali kana kwamba nilikuwa na uhakika kuwa alikuwa akiniona kwenye kiza kile. Ingawa sikuwahi kufanya kazi sonara na wala sikuwa mtaalamu wa masuala yanayohusu vito lakini nilielewa tofauti kati ya jiwe laini na lisilo laini.

“Naam, baada ya kunipa ile pete, nilimtazama Tunu kwa makini kwa macho yaliyoonesha maswali kibao nikitaka kujua sababu za kunipa pete ile,” yule mgeni aliendelea.

“Tunu aliniambia kuwa alifahamu kuwa kulikuwa na nguvu kubwa ya kiroho iliyokuwapo katikati yetu kila wakati tulipokuwa pamoja. Ndio maana aliamua kunipa ile pete ambayo aliamini ingesaidia kuwa na nguvu zaidi na ingetufanya tushikamane kiroho milele na milele hata kama kimwili tungekuwa mbalimbali.”

“Kwani alikuwa na nguvu ya kichawi?” nilimuuliza yule mgeni huku nikihisi ubaridi wa hofu ukinitambaa kwenye ngozi yangu.

Yule mgeni alicheka kicheko kilichoacha mwangwi upande wa pili wa chumba kwenye kiza.

“Swali lako siwezi kulijibu kwa kuwa sijui. Ninachojua ni kwamba Tunu aliniambia kuwa nikivaa pete hiyo basi ingenisaidia na kujihisi nimo katika hali ya mapenzi ya dhati ambayo sijawahi kuyashuhudia popote. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa baada ya kuivaa.

“Kila siku usiku tulikutana hata kama nilichoka sana na kazi na mchana kwa siku ya mwisho wa wiki ambapo nilikuwa siendi kazini tulikwenda kwenye matembezi pamoja, nikajikuta niko karibu yake zaidi na zaidi. Hatimaye, kila nilipomwona moyo wangu ulipapatika na nilipokuwa mbali naye tumbo langu liliniuma kwa upweke. Ila kumbuka hadi wakati huo sikuwa nimemtamkia kama nampenda wala kufanya chochote zaidi ya kumbusu.”

Nilishusha pumzi na kugeuza shingo yangu kuangalia nje ya studio kupitia ukati msafi wa kioo cha dirisha la studio yangu. Nilishtuka kuona kwa mbali dalili ya dhoruba lililokuwa linaanza kujitokeza, ingalau upepo ulikuwa umepungua na sauti ya muungurumo wake ilisikika kwa chini kidogo.

Matawi ya miti yaliyokuwa yakijipiga kwenye ukuta hayakuwa yakijipiga tena kwenye nyumba, lakini ilikuwa bado kuna giza nene. Yule mgeni wangu alikohoa kidogo kusafisha koo lake.

“Naam, kule kwenye kazi haikuchukua muda mrefu Swedi Kachenje alituambia kwamba alikuwa na tatizo kubwa la kifedha, mgodi haukuwa ukimuingizia fedha yoyote na wataalamu wa miamba walimweleza kuwa hawakuona dalili ya kuwepo madini kwenye mapango hayo…

“Alisema kuwa mkopo aliokuwa amechukua kutoka benki ulianza kumgharimu kwani watu wa benki walipogundua kuwa mgodi hauzalishi walimwita na kutishia kumtaifisha mali zake zote kama angeshindwa kurejesha mkopo aliochukua.” Alinyamaza na kuvuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu. Kisha aliendelea.

itaendelea…
 
Mwandishi wa Makala – 8

“Alisema kuwa mkopo aliokuwa amechukua kutoka benki ulianza kumgharimu kwani watu wa benki walipogundua kuwa mgodi hauzalishi walimwita na kutishia kumtaifisha mali zake zote kama angeshindwa kurejesha mkopo aliochukua.” Alinyamaza na kuvuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu. Kisha aliendelea.

Walisema kuwa walichojua ni kwamba mapango hayo yalikuwa yametokana na mabadiliko ya nguvu za asili zilizobadilisha maumbile ya miamba ya chokaa kipindi cha jurasiki (Jurassic period) takriban miaka zaidi ya milioni 150 iliyopita.

Nilisikia kuwa kulingana na tafiti zilizokwishafanywa, eneo hilo la mapango lilikuwa tena chini ya maji miaka milioni 20 iliyopita na linakadiriwa kuwa na ukubwa wa kilometa za mraba 234 lenye mazingira ya miamba ya chokaa. Ni eneo ambalo linapitiwa na mito na limejaa uoto wa asili.

Miamba ya chokaaa katika mapango hayo imeundwa na madini ya kashiamu kabonate ndio maana miamba hiyo ni migumu kumomonyolewa na maji ya kawaida, lakini ni rahisi kuyeyushwa na maji yenye kiasi kidogo cha tindikali ya kaboni. Tindikali ya kaboni ilibadilisha maumbile ya miamba hiyo… Nikiwa bado nawaza yule mgeni aliongea.

“Naam, nilifanya kazi kwa bidii kwa muda mrefu nikiamini kuwa mwezi ujao mambo yangekuwa mazuri zaidi kama alivyoahidi Swedi. Nakumbuka siku moja Swedi Kachenje aliniita na kuniambia kuhusu mpango wake wa kunifanya mbia katika mgodi huo. Aliniahidi mambo mengi na kuniomba nisimwache. Nilikubali kubaki katika mgodi huo kwa kuona kuwa hiyo ilikuwa ndio nafasi yangu muhimu, na bidii yangu ya kazi ndio ingenifanya kufanikiwa…

“Nilifahamu kuwa kama kampuni ingekuwa katika matatizo, basi hata mimi ningekuwa kwenye matatizo vilevile, hasa endapo nisingechukua hatua kuziba pengo. Hivyo, nilihakikisha kuwa Swedi Kachenje alikuwa anajua kwamba nilikuwa nafanya kazi kwa bidii na kujituma mno ili kunusuru hali mbaya iliyokuwepo…

“Wafanyakazi wengi walionizunguka karibu hawakuwa watu wenye kufanya kazi kwa kujitoa kama nilivyofanya mimi bali walichojali wao ni fedha tu. Walifanya kazi kwa kutegea na muda ulipofika walikwenda zao nyumbani. Wala hawakujali kabisa kama kampuni iliingiza faida au ilipata hasara,” yule mgeni aliongea kwa sauti ya huzuni na kuongeza.

“Kama nilivyojieleza mwanzoni mwa mazungumzo yetu, sikuamini kabisa kuishi kwa njia ya uongo. Sikuamini kuwa mtu hawezi kuishi bila kufanya udanganyifu. Niliamini katika kufanya kazi kwa uaminifu na kwa bidii. Kila muda ulivyosonga mbele, ndivyo nilivyowaona wafanyakazi wenzangu wakizidi kufanya udanganyifu kwenye kampuni wa hapa au pale. Walianza kujifanya kuwa walikuwa wakifanya kazi lakini kwa kweli walikuwa wakichunguza maeneo mengine ya mapango ili kufanya wizi. Unajua kila walivyozidi kufanya ujinga, ndivyo mimi nilivyozidi kufanya kazi kwa bidii.”

“Unadhani hawakukuchukia kutokana na namna ulivyokuwa ukijituma kwenye kazi wakati wao walikuwa wanafanya udanganyifu?” Nimuuliza yule mgeni kwa shauku.

“Mara ya kwanza, hawakuwa na neno, waliona sawa tu. Walikuwa wanapenya katika njia nyembamba iliyopo ndani ya mapango hayo na kupanda wakifuata mlima Kilimanjaro. Naamini hukuiona njia hiyo nyembamba inayoelekea Kilimanjaro ulipokwenda kutembelea mapango hivi karibuni. Ni njia ya kustaajabisha sana. Fanya kila njia wakati mwingine ukitembelea mapango hayo uione.”

“Nitafanya hivyo,” Nilimjibu huku nikishangaa sana na kujiuliza alijuaje kwamba nilitembelea mapango hayo na kitu fulani nilikuwa nimekiona na kitu fulani sikuwa nimekiona katika mapango hayo!

Mara moja nikakumbuka kusikia kutoka kwa waongozaji ndani ya mapango wakieleza kuhusu njia hiyo nyembamba na kuwa zipo habari kuwa kuna wazungu wawili watafiti ambao ni mtu na mke wake waliwahi kuja kwenye mapango hayo, walikuwa wakitaka kuingia ndani ya mapango hayo lakini wenyeji waliwasihi wazungu hao wasiingie bila ya mwenyeji wa kuwaongoza lakini wazungu hao waligoma kutumia muongozaji mwenyeji na hivyo kuingia wenyewe.

Inasemekana kuwa huo ndio ulikuwa mwisho wa wazungu hao kuonekana na hawakutoka tena lakini baada ya mwezi mmoja, mbwa wao alipatikana eneo la Kilimanjaro!

“Naam, kuna siku hali ilizidi, niliona kuwa udanganyifu ulizidi kipimo. Baadhi ya wafanyakazi katika upekupeku wao waligundua baadhi ya mifupa mikuukuu nadhani ilikuwa ya farasi mwitu au kitu kama hicho. Ilikuwa ni mifupa mikuukuu kwelikweli kwani tayari ilikuwa imegeuka kuwa kama vipande vya miamba. Waliacha kufanya kazi na kuanza michezo ya kurushiana huku wakicheka. Jambo hilo lilinikasirisha sana. Wakati huo tulikuwa katika maeneo ya hifadhi ya mapango iliyo pembeni ya ufuko wa bahari.

“Kulikuwa na kanuni iliyotutaka kufanya kazi kwa bidii na kuacha kila kitu pamoja. Kukimbizana huku na kule ndani ya mapango ingeweza kusababisha madhara, lakini hao jamaa walikuwa wakikimbizana na kurushiana mifupa hiyo na kusababisha ivunjike ovyo, na sidhani kama kwa umri wao walipaswa kufanya mambo ya kitoto namna ile. Jambo hilo halikuwa sahihi hata kidogo…”

“Nimewahi kusikia kwamba kuna watu walipata mifupa ya ngamia katika mapango, nadhani itakuwa ndio ile mifupa uliyoiona ambayo jamaa zako walirushiana. Una bahati sana kwa kuwa ulishuhudia jambo hili kwa macho yako?” Nilimkatiza yule mgeni wangu kwa shauku.

itaendelea…
 
Mwandishi wa Makala – 9

“Nimewahi kusikia kwamba kuna watu walipata mifupa ya ngamia katika mapango, nadhani itakuwa ndio ile mifupa uliyoiona ambayo jamaa zako walirushiana. Una bahati sana kwa kuwa ulishuhudia jambo hili kwa macho yako?” Nilimkatiza yule mgeni wangu kwa shauku.

“Ndiyo, nilikuwa na bahati sana,” yule mgeni alijibu na kuongeza. “Kwa mtazamo wangu niliona kwamba wale jamaa hawakuwa wakifanya jambo la haki. Sikuwa na shida kuhusu wao kutegea kazi, lakini sasa sio tu kwamba walikuwa wanategea kazi bali walikuwa wanaharibu hata kazi yetu pia. Hii haikuwa sahihi hata kidogo, na niliazimia kwenda kutoa taarifa kwa Swedi Kachenje. Naam, hawakuwa tayari kuona jambo hilo likifanyika.” Alisema mgeni yule kwa huzuni.

Nilijikuta nahisi ubaridi mwepesi ukiipiga ngozi yangu, na sikujua kabisa kuwa muda huo nilikuwa nimekaa kwenye ukingo wa kiti changu nikiwa nimeyakodoa macho yangu kwenye kiza.

“Kwa hiyo nini kikatokea?” Nilijikuta nauliza kwa shauku.

“Wakati nataka kupanda juu ili nitoke nje ya pango nikatoe taarifa, nilijikuta nikipigwa na kitu kigumu kama bomba au ubao, sikumbuki sawasawa. Pigo la kwanza likanipata sawasawa katika koromeo langu. Nilikamata koo langu na kujaribu kupiga kelele kwa wafanyakazi wenzangu waliokuwa maeneo jirani, lakini sauti haikuweza kutoka nje.

“Pigo lililofuata lilipasua kabisa kifuniko cha goti langu la mguu wa kulia. Wahuni wale wakanipiga miguu yangu tena na tena ili kuhakikisha siwezi kutembea. Walipoacha kunipiga, nilijaribu kutambaa ili kutafuta msaada. Eneo nililokuwepo lilikuwa karibu sana na eneo la kazi na kama ningeweza tu kufika juu, pengine angetokea mtu angeweza kuniona…

“Hata hivyo, wale wahuni walikuwa wamefanya kazi yao vizuri, nilishindwa kuinuka na kulala chini kwenye miguu yao kama mnyoo. Walisimama na kunitazama huku wakinicheka na kunichezea kama vile panya anavyochezewa na paka baada ya kuvunjwa mgongo na kuwa hawezi tena kukimbia.”

“Mungu wangu! Mbona hali ile ilikuwa ya kutisha sana!” Niling’aka kwa uchungu. Kauli yangu haikuwa ya kinafiki.

Nilijaribu kujenga picha kuwa kama ukatili na uovu wa aina ile ningefanyiwa mimi na wale wahuni ningestahimili vipi? Ukweli kwa upande wangu ilikuwa ni mbaya zaidi ya nilivyoweza kufikiria. Ni mbaya sana kufanyiwa mashambulizi ya kimwili, lakini kuteswa na kuumizwa kiasi kile na watu walioonekana kujifurahisha nafsi zao ilikuwa ni jambo lisilofikirika.

“Walikuwa wakatili mno wasio na huruma hata kidogo. Sijui ni jambo gani baya niliwahi kuwafanyia hata waniadhibu kiasi kile. Siwezi kumsahau yule jamaa mfupi jinsi alivyokuwa akimwangalia mwenzake aliyekuwa kibonge cha mtu na kumwambia eti badala ya kuchezea ile mifupa ni bora wangecheza mchezo wa kukamata na kuvuta kende zangu. Wote wawili walicheka…”

“Na hakukuwa na mtu mwingine yeyote jirani na hapo wa kukusaidia?” Nilimkatisha mgeni wangu kwa swali. Safari hii nilihisi donge la hasira na uchungu lilikuwa limenikaba kooni.

“Hapana, kundi kubwa la wafanyakazi lilikuwa tayari limefunga kazi na kuondoka kwenda nyumbani kwa ajili ya mapumziko ya mwishoni mwa wiki. Kumbuka siku hiyo ilikuwa ni Ijumaa. Hao wahuni wawili walibaki hapo kuhakikisha wanaondosha kabisa ushahidi ili madhambi yao yasijulikane.

“Walikuwa na muda wa kutosha kunidhihaki, kunicheka na kunisimanga jinsi nilivyokuwa mnoko na mjinga sana kwa kufuatilia mambo yasiyonihusu. Wakasema kwamba nilistahili kila kitu kilichonipata kwa sababu nilitaka kuifanya jamii iwaone wao ni watu wabaya na wala sikujali kama wangepoteza ajira zao na kuzifanya familia zao zife kwa njaa.”

“Dah… pole sana. Sasa uliwezaje kutoka salama nje ya yale mapango?” Niliuliza tena kwa shauku.

Yule mgeni alikaa kimya kwa muda, chumba chote kikawa kimya mno. Nadhani alikuwa akitafakari jinsi ya kunijibu, kisha akaendelea kusimulia kisa chake kana kwamba hakuwa amelisikia swali langu.

“Baada ya dakika chache ukweli ulianza kuonekana kuwa wale wahuni walianza kuingiwa na hofu kwa walichokifanya. Wakaambiana wao kwa wao na kupanga kutengeneza mazingira ili kifo changu kionekane kama ajali ya kawaida au kitu kilichosababishwa na mimi mwenyewe kwa sababu ya uzembe wangu. Kwa hiyo, wakalisukuma jiwe kubwa hadi juu yangu likanifunika nusu ya mwili wangu sehemu yangu ya chini na kuonekana kama niliangukiwa na mwamba kwa bahati mbaya ama uzembe…

“Maumivu niliyoyahisi wakati huo yalikuwa ni makali mno yasiyopimika na sijapata kuhisi maumivu kama yale katika maisha yangu yote hapa duniani. Sikuweza kupiga kelele, lakini mikono yangu ilijaribu kufinya ardhi kwa maumivu makali. Hadi leo hii, najilaumu kwanini nilifanya vile. Kwa sababu, kila nilipofinya ardhi na kusogeza mkono wangu, pete yangu ilitoa mng’ao na kuwamulika wale wahuni.” Alisema yule mgeni na kutulia kidogo.

Katika ukimya ule niliweza kuhisi uchungu na hasira ndani yake lakini sikuwa na namna yoyote ya kufanya. Nilibaki kimya wakati kisa chake kikianza kufunguka zaidi. Hapa sikujua tena habari za Tunu zimeishia wapi!

“Ulikuwa wakati mgumu sana kwangu kutokana na maumivu makali niliyoyahisi, kiasi kwamba hata akili yangu ilianza kufanya kazi taratibu. Kwa hiyo nilipoona yule kibonge cha mtu ananijia na kuigusa pete yangu, sikuweza hata kutingishika. Nilibaki nimetulia kama mtu aliye katika usingizi mzito nikimwangalia kwa uchungu wakati anaichukua pete yangu…

“Wakati akiichukua pete niliona akichukua kitu muhimu zaidi maishani mwangu, ile pete ilikuwa ni hazina ya moyo wangu, yaani alikuwa anachukua roho yangu. Nilihisi kama moyo wangu unapasuka vipande ndani kwa ndani kwa sababu ile pete ilikuwa imebeba nguvu kubwa ya uhusiano na mawasiliano kati yangu na Tunu. Kupitia ile pete nilimuona Tunu akiwa karibu zaidi na mimi. Baada ya kuipoteza, nilijikuta nimepoteza matumaini yote.”

“Dah! Naweza kuhisi upendo wako ulivyokuwa mwingi kwa Tunu,” niliongea kwa uchungu na kuongeza. “Una bahati sana kumpata mwenzi wa nafsi yako kama Tunu. Unajua baadhi ya watu huishi maisha yao yote bila kupata pendo la dhati kama ilivyotokea kwako.”

“Basi ile pete ilikuwa ni alama ya upendo wangu kwa Tunu, alama ambayo sasa ilikuwa inatoweka na kupotelea katika mikono ya vibaka, macho yangu yakajaa machozi. Nilifumba macho yangu ili kuepuka kuwapa nafasi wale wahuni ya kunifanyia dhihaka zaidi. Nilibaki kuwasikiliza katika hali ya ukimya. Yule kibonge cha mtu alikuwa akijivuna sana jinsi ambavyo pete hiyo ingewapatia pesa nyingi.

“Yule mfupi alionesha wasiwasi kidogo na kumwambia yule kibonge cha mtu kuwa isingekuwa vema kuichukua ile pete kwa kuwa kila mtu pale kijijini alikuwa anajua kwamba ile ilikuwa ni pete ya Tunu, na kwamba kama angejaribu kuiuza kesho yake angejikuta akiwa nyuma ya nondo za jela…

“Hata hivyo, yule kibonge cha mtu aligeuka na kusema kuwa hataichukua lakini alisema hakuwa na uhakika kama hata mimi niliihitaji tena. Nilifungua macho yangu kumtazama yule kibonge jinsi alivyokuwa akiniangalia kwa jicho baya sana.”

Kwa mara nyingine tena yule mgeni wangu kwenye giza alinyamaza. Kikafuata kimya kirefu chenye mzizimo wa majonzi. Niliamua kusubiri tu bila kusema neno.

itaendelea…
 
Mwandishi wa Makala – 10

Kwa mara nyingine tena yule mgeni wangu kwenye giza alinyamaza. Kikafuata kimya kirefu chenye mzizimo wa majonzi. Niliamua kusubiri tu bila kusema neno.

“Yule kibonge aliamua kuiweka ile pete chini ya ardhi ambapo niliweza kuiona, akaikanyaga na kushindilia mabuti yake ardhini zaidi ya mara sita. Lakini alipositisha zoezi lake nilishangaa sana. Utepe wa dhahabu na kito kikubwa cha thamani chenye rangi ya zambarau kwenye ile pete vilikuwa bado imara kabisa! Kila alivyojitahidi kuishindilia ardhini ndivyo alivyojikuta akiilazimisha ile pete kuzama katika udongo.

“Ilionekana wazi kuwa yule kibonge cha mtu aliamua aipoteze ile pete, alisema kuwa kufanya hivyo angeweza kuificha milele isionekane na mtu yeyote. Aliposhindwa kuizamisha kwenye ardhi aliamua kuificha katika giza ili asitokee mtu yeyote wa kuweza kuipata tena. Sikubahatika kuona mahali alipoificha ile pete. Hata hivyo, nilijua kuwa isingekuwa mbali sana na mahala hapo nilipokuwa nimelala huku jiwe kubwa likiwa juu yangu. Hadi leo naamini ipo mahali fulani katika eneo lile.”

“Kwa maana hiyo hujawahi kuiona tena?” Niliuliza swali ambalo hata hivyo jibu lake tayari nilikuwa nalijua kupitia maelezo ya mgeni wangu.

“Bado sijaiona hadi leo,” yule mgeni alinijibu kwa huzuni.

Nilibetua kichwa changu kukubali, wakati yule mgeni katika kile kiza akiendelea kusimulia kisa chake cha kusikitisha.

“Wakati wale wahuni walipokuwa wakijiandaa kuondoka, niliamua kufumba macho yangu na kutulia nikijidai kuwa nimepoteza fahamu ili wasirudi wakanimalizia. Hata hivyo, haikuwa mbali na hali halisi. Nilipata taabu sana kupumua nikiwa na jiwe kubwa lililokuwa limenilalia juu. Washenzi wale walisimama kando wakajadiliana kwa muda wa dakika chache…

“Kisha wakakubaliana kuwa nilikuwa sawa na mfu tayari na kwamba nisingeweza kuumaliza usiku wa siku ile. Kwa hiyo wakasema kwamba hawakuwa na haja ya kunimalizia bali wangeweza kuacha kifo kichuke nafasi yake taratibu. Nakumbuka niliwatazama wakitembea kwa majivuno kutoka eneo lile. Walikuwa wanacheka na kufanyiana utani na niliweza hata kuwasikia wakati wakiungana na kundi jingine la wafanyakazi waliokuwa wakiondoka eneo lile.”

“Mungu wangu!” Nilishindwa tena kuvumilia na kujikuta niking’aka kwa hasira kwa sauti ya chini ambayo hata hivyo ilisikiwa na mgeni wangu.

Nilihisi donge la hasira likizidi kunikaba na kusimama kwenye koo langu kwa muda mrefu huku joto kali la hasira likiibuka ndani yangu, nilijikuta nawachukia wale watu na kusisimkwa kwa hasira kuona kuwa kumbe kulikuwa na watu katika dunia hii waliokuwa na roho ya kinyama kiasi kile bila kujali maumivu waliyoyapata binadamu wenzao. Yule mgeni aliendelea kuongea.

“Basi sehemu iliyofuata baada ya wafanyakazi wote kuondoka ilikuwa ndio mbaya zaidi kwangu. Wale wahuni walifanya kila hila kuzima taa zote zilizotumika kuwaongoza watu katika njia za ndani ya yale mapango, matokeo yake kulikuwa na giza totoro lililotisha mno ndani ya yale mapango. Nilibaki nikiwa nimelala huku nimekandamizwa na jiwe kubwa juu yangu katika pango lenye giza totoro.”

“Hmm! Najaribu kujiweka katika viatu vyako lakini akili yangu inakataa. Kwa vyovyote ulikuwa katika kipindi cha mateso makubwa mno na hali yako ilikuwa ni mbaya,” nilisema kwa huzuni huku nikishusha pumzi ndefu.

“Ilikuwa ni mbaya mno, kwa wakati huo ilikuwa ni sawa na kuzikwa ndani ya kaburi ukiwa hai. Labda nikuulize, hivi umewahi kukaa katika chumba chenye giza totoro na ukiwa huna namna ya kutoka?” yule mgeni akaniuliza.

“Kusema kweli mateso yaliyokukuta yalikuwa ya kutisha mno, sitaki hata kuyafikiria,” nilimjibu yule mgeni huku nikijaribu kuzungusha macho yangu ndani ya studio, giza lilikuwa limetanda na sikujua ni giza gani alilokuwa anamaanisha wakati tayari nilikuwa ndani ya studio yenye giza totoro kwa muda huo!

“Naam, hali ilitisha mno,” yule mgeni alisema na kuongeza, “Unapokuwa umenaswa chini ya jiwe kubwa lenye tani kadhaa ndazni ya pango lenye giza totoro kama ilivyokuwa kwangu, unapoteza kabisa majira. Hujui kama jua lipo juu au limeshatua. Muda unaonekana kusimama, hasa unapokuwa katika kipindi ambacho huwezi hata kujisogeza kutoka sehemu moja kwenda nyingine! Utashangaa kuona dakika moja inaweza kuwa ndefu mno katika kiza hicho.”

Yule mgeni aliponyamaza kidogo, nilijaribu kujenga picha akilini mwangu kuwa mikono na miguu yangu ilikuwa imekandamizwa na mifupa ya mguu wangu imevunjwa. Wakati huohuo nikijitahidi kupambana kuvuta pumzi ndani ya mapafu yangu, bila kujua kama huenda ndiyo ilikuwa pumzi yangu ya mwisho…

Japo nilikuwa ndani ya studio yangu yenye giza totoro lakini niliweza kuhisi msisimko wa ajabu na kujikuta nikimshukuru Mungu wangu kwamba sijawahi kukutana na tukio baya kama lile.

“Muda mrefu niliokuwa nimenaswa chini ya jiwe kubwa katika giza totoro chini ya ile miamba nilinipata muda mwingi wa kufikiri. Nilifikiria sana kuhusu nilivyokutana na Tunu jinsi nilivyompenda sana. Unajua, kosa kubwa nililokuwa nimelifanya ni kwamba pamoja na kumpenda lakini sikuwahi kumtamkia kwamba nampenda. Nilidhani kwamba muda wa kufanya hivyo ulikuwepo mwingi na kwamba ningeweza kufanya hivyo baadaye…

“Nilikuwa bado kijana, na Tunu alikuwa kigoli. Nilifikiria kwamba sikupaswa kufanya haraka, nilitakiwa nisubiri kwa kuwa muda utakuwepo tu. Sasa unatambua kwamba nilitoka katika familia ambayo hawakuwa wakihubiri upendo wala kusema neno nakupenda. Naam ni mara chache sana hata hivyo…

“Wakati nikiwa bado nimelala kwenye pango na jiwe lipo juu yangu, nilijipiga mwenyewe kwa hasira mara kwa mara huku nikijilaumu, nilijiuliza kwanini sikuwahi muda wowote katika maisha yangu kusema tu neno nakupenda. Neno hilo moja tu. Ni neno dogo sana lakini lina nguvu kubwa mno. Kwanini sikulisema wakati nilikuwa na nafasi ya kufanya hivyo?”

Maneno ya mgeni wangu yakanikumbusha kuwa hata mimi nilimpenda kwelikweli kutoka moyoni msichana mmoja aliyekuwa akiishi hapo Ilala Sharif Shamba katika nyumba ya jirani, si mbali sana na ilipo klabu ya usiku ya Galapo, na yeye alijua kuwa nilikuwa nampenda lakini alijifanya haelewi chochote, au labda hakuweza kufanya chochote kwa kuwa alisubiri nimtamkie, na kwa sababu nilikuwa na aibu sana sikuwahi kumtamkia kama nampenda.

Alikuwa ni msichana mzuri na mrembo sana wa daraja la juu ambaye kamwe sikuwahi kumuona msichana wa namna ile katika pitapita zangu. Alikuwa na nywele nyeusi za kibantu alizokuwa anapenda kuzikata vizuri katika mtindo wa Lowcut na hivyo kumfanya aonekane mzuri wa asili.

Macho yake yalikuwa makubwa na meupe yaliyozungukwa na kope ndefu na nyeusi, pua yake ndefu ya kihabeshi, mdomo wake wa kike wenye kingo pana kiasi na vishimo vidogo mashavuni vinavyochomoza haraka kila alipotabasamu vikazidi kuzisulubu vibaya hisia zangu. Huyu msichana aliitwa Vailet Shirima.

Katika kuwaza hayo nilijikuta nayakodoa macho yangu kutazama kwenye giza. Sikujua niseme nini. Nilikubaliana kabisa na yote yaliyosemwa na mgeni wangu. Maisha ni mafupi. Bila kujua nini cha kufanya, nilibetua kichwa changu kukubali.

“Vipi, umeoa?” Yule mgeni wangu kwenye giza akaniuliza.

“Hapana,” nilimjibu.

itaendelea…
 
Mwandishi wa Makala – 11

“Najua, wewe ni kijana bado na una mengi ya kufanya,” yule mgeni kwenye giza alisema. “Lakini najua yupo mtu ambaye unampenda sana. Hakikisha unamweleza jinsi unavyompenda mara tu utakapotambua jinsi alivyo muhimu sana kwako. Sijui unanielewa?”

“Nakuelewa, Bwana mkubwa,” nilijibu na kuendelea. “Hakika leo najifunza mambo mengi sana kutokana na kisa chako. Naamini yatanisaidia.”

Mgeni wangu kwenye giza upande wa pili wa chumba akabaki kimya kwa muda, kisha akaendelea kusimulia kisa chake.

“Basi hawakuweza kuniona mpaka asubuhi ya siku iliyofuata. Nilibaki nimenaswa pale kwenye pango kwa zaidi ya saa kumi na mbili. Walioniona ni watu waliokuwa wanahusika na mambo ya kale ambao walikuwa wakifanya ukaguzi mchana wa siku hiyo…

“Swedi Kachenje aliomba watu wa mambo ya kale wafanye ukaguzi kwa kuwa alitaka kuwa na uhakika kwamba hakukuwa na ukiukaji wowote mkubwa ndani ya mapango hayo ambao ungeweza kuharibu mkataba wake. Baada ya kuniona, sikuweza hata kufungua macho yangu. Walimtaarifu Swedi kachenje ambaye naye aliamua kumwita Tunu haraka kwa kadri alivyoweza. Hata hivyo, nilifariki dunia kabla Tunu hajafika.”

“Ulifanya nini?!” Niliuliza kwa mshtuko mkubwa na kwa sauti yenye kushutumu.

“Nilifariki dunia,” yule mgeni alinijibu bila shaka yoyote.

“Sasa huo utani, hebu kuwa siriasi kidogo. Siamini kabisa masuala ya mizimu na kama unatarajia nitaandika makala kuhusu mzimu, basi utakuwa umekosea sana.”

Muda huohuo nilihisi hasira kali zikiibuka ndani yake, chumba chote kilionekana kimeshuka kama digrii kumi hivi na kuwa kifupi mno. Kutoka kwenye vile vivuli vilivyokuwa juu ya sofa, ikajitokeza sura inayoogofya sana ikiwa imeghadhabika mno kwa hasira zilizolipuka chumba kizima.

Ukungu mfano wa sura ulikijaza chumba kizima chenye futi kumi na kusimama uso kwa uso kukabiliana na mimi. Ilikuwa ni sura mbaya mno na ilitoa pumzi za kutisha na meno yake yalitokeza nje na yalikuwa machafu mno.

Kama hiyo haitoshi, nilianza kuuona mwili wangu ukicharangwa kwa visu vikali na kubanikwa katika moto mkubwa. Nilihisi moto mkali sana ukitambaa kwenye mwili wangu na ngozi yangu ilikuwa inaungua na kunifanya kuhisi maumivu makali mno.

Nilijaribu kuhisi kama nilikuwa ndotoni au lilikuwa ni tukio tukio halisi kama ambavyo lilikuwa linachotokea. Nililia sana kwa uchungu. Mara hali ile ikabadilika. Ghafla, tumbo langu likapasuliwa na mbwa mwitu na kubaki wazi. Sikujua mbwa mwitu hao wametokea wapi. Meno yao yakaanza kuirarua ngozi na kuchanachana nje matumbo yangu. Nilipiga kelele kutokana na maumivu makali niliyoyashuhudia.

“Hivi unataka nifanye nini ili nikushawishi kwamba mimi si mtu hai,” yule mgeni aliniuliza kwa sauti iliyoonesha dhahiri kuwa alikuwa na hasira mno.

“Nakuamini, sasa nakuamini!” Nilisema huku nikilia kwa uchungu.

Ile picha ya mwili wangu kuungua na kushambuliwa na mbwa mwitu ikatoweka kwa haraka kama ilivyotokea. Ile sura ya kutisha pia ikatoweka na kupotelea katika giza, na hali ya chumba ikarudi kama kawaida. Kwa kweli, hali ya chumba ilikuwa ni ya kawaida kabisa, kiasi kwamba nikaanza kufikiri kwamba labda yalikuwa ni mawazo yangu tu lakini hakukuwa na kitu kama hicho.

Mawazo hayo yalidumu kwa sekunde tu kabla sijaamua kwamba ilikuwa inatosha na isingependeza kuendelea kubishana tena na yule mgeni maana kufanya hivyo ilikuwa ni kutafuta matatizo mengine zaidi.

Nilivuta pumzi kwa nguvu kujiweka sawa kwenye kiti changu kirefu cha kuzunguka. Yule mgeni akaendelea kusimulia kisa chake kana kwamba hakuna chochote kilichotokea muda mfupi mle chumbani.

“Mwili wangu ulipokufa, roho yangu ikajawa na hasira kubwa. Niliteseka sana na kuumizwa sana wakati wa ule usiku mrefu wa siku niliyokuwa nimegandamizwa na miamba. Kudumu katika maumivu yasiyoweza kusemeka na adhabu kubwa ya kukaa katika hali hiyo nikiwa hai ilinifanya kuwa na ghadhabu. Niliumia kwa kuwa sikuwa nimepata nafasi ya kusema lile neno moja dogo kwa Tunu wangu. Pamoja na kufanya kazi kwa bidii lakini tuzo niliyoambulia ilikuwa ni kutenganishwa na kuwekwa mbali na mwili wangu!”

Nilibaki kimya nikimsikiliza, hapo sikutia tena neno lolote isipokuwa kusikiliza kwa makini. Aliendelea.

“Wakati Tunu wangu alipowasili mahali pale alikuwa ameumia sana na alikuwa analia kama mtoto mdogo. Wakati huo roho yangu ilikuwa inaelea juu kwenye dari la pango juu ya mwili wangu uliopondwapondwa huku nikiwa naangalia kilichokuwa kinaendelea pale chini. Hasira kali zilinizidia na kuijaza nafsi yangu. Haikuwa haki kabisa.

“Nilikuwa nikifanyiwa hila kwa kila njia niliyofikiria. Nilifanyiwa hila hata kusababisha nishindwe kumwambia Tunu wangu jinsi gani alikuwa muhimu sana kwenye maisha yangu. Wakati nikielea juu huku nikiangalia chini kumtazama Tunu, niliamua kwamba sasa inatosha! Enough is enough. Sitamwacha Abadan. Naweza nisipate nafasi au uwezo wa kuongea naye tena na anaweza asinione tena, lakini sitaondoka nimwache peke yake.”

Nilianza kuhisi kulikuwa na mvutano mkubwa ndani ya sauti ya yule mgeni wangu. Sauti yake ilikuwa ya chini lakini kali zaidi na iliyojaa ghadhabu. Nilizidi kuuhisi ubaridi mwembamba ukizidi kunitambaa mwilini mwangu na kunisisimua zaidi. Sauti yake iliendelea kuongea, lakini safari hii ilikuwa ni kama alitaka kupiga kelele.

“Niliwaambia kwamba sitaondoka kwenda popote nikamwacha Tunu. Abadan. Abadan sitamwacha mpenzi wangu wa milele. Nilitazama chini na kuzungumza maneno ambayo hadi leo bado yamo akilini mwangu. Nilisema; Tunu naapa kwa jina la baba yangu na nafsi ya mama yangu kwamba abadan sitakuacha peke yako. Iwe ni katika maisha haya au ya ulimwengu ujao. Katika kifo au uhai, nitabaki na wewe mpaka nitakapoweza kukwambia neno lile ambalo ninapaswa kulisema kwako. Neno ambalo sitaweza kulisema mpaka tutakapokutana tena.”

Alinyamaza. Nilihisi upepo fulani wenye ubaridi ukikijaza chumba chote na kuzifanya nywele zangu kusimama. Ilikuwa ni hisia tofauti sana ambayo sikuihisi hapo awali lakini ikiwa na nguvu kubwa. Ukimya ulidumu kwa dakika moja, na baada ya dakika moja, niliamua kuuliza swali.

“Naweza kuuliza swali bwana mkubwa? Yuko wapi Tunu kwa sasa?”

Yule mgeni aliendelea kukaa kimya. Jibu lake halikuwa la haraka kama majibu mengine, hili lilikuja baada ya muda mrefu kidogo.

“Tunu alipita kuelekea upande mwingine wa pango. Nasikitika kuwa sikuweza kutimiza kiapo changu japo nilijitahidi sana kuwa karibu naye na kumlinda, lakini sikuweza kabisa kuongea naye.”

“Sijui naweza kukusaidia katika hilo, bwana mkubwa?” Niliuliza na muda huohuo nikakumbuka kitu. “Pia nimejaribu sana kufikiria juu ya maelezo yako kuhusu pete uliyopewa na Tunu. Sijui kwanini hili linanijia akilini mwangu, lakini ninadhani ninayo pete kama hiyo.”

“Ooh rafiki yangu, ni vyema sana kwako kusema hivyo,” yule mgeni alisema na kuongeza. “Hata hivyo, ni muda mrefu sana umepita na nimekwisha kukata tamaa kuwa sitoiona tena hiyo pete.”

Nilivuta droo yangu chini ya meza kuifungua. Nilikuwa na tabia ya kukusanya na kununua vitu mbalimbali vya kihistoria katika maduka ya vitu ya kale kila nilipokuwa kwenye safari zangu mbalimbali. Watu wengi walinishangaa kwanini nilinunua vitu vya kale, wao hupenda kununua vitu vyao kutoka kwenye maeneo yanayouza vitu vya kitalii, huku mimi nikinunua walichoona ni takataka kutoka maduka ya vitu vya kale.

Itaendelea…
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom