IamBrianLeeSnr
JF-Expert Member
- Nov 10, 2022
- 2,011
- 4,165
Licha ya kuwa nje ya Tanzania kwa miaka mitano na ushei, ushawishi wake katika siasa za upinzani bado ungalipo. Kwa lugha nyingine ni kusema; makovu yake ya kisiasa hayajaondosha mvuto wake wa kisiasa mbele ya wafuasi wa chama chake.
Tundu Lissu alisifika kwa ukosoaji dhidi ya serikali ya hayati Magufuli. Hata kabla ya hapo tayari alikuwa ni mwanasiasa maarufu. Harakati zake za wakati wa Magufuli zilizidi kumuweka mstari wa mbele katika siasa za upinzani.
Wakati akiwa Ubelgiji mara kwa mara alitumia mitandao ya kijamii kuzungumza na Watanzania. Pia amekuwa akishiriki mahojiano katika vyombo vya habari kwa ndani na nje. Haya yote yamesaidia pakubwa kulifanya jina na ushawishi wake yasififie katika siasa za Tanzania.
Ataisaidiaje Chadema kuelekea 2025?
Uwepo wake ni muhimu kupamba na ushawishi wa Chama cha Mapinduzi (CCM), kilichokuwa kikijifaragua peke yake katika uwanja wa siasa, tangu kuanza kwa katazo la mikutano ya hadhara na maandamano mwaka 2016.Zuio la hayati Magufuli lilitaka mikutano ihusishe wabunge na madiwani pekee katika majimbo yao huku wengine wakitakiwa kufanya mikutano ya ndani. Ambayo nayo mara kwa mara ilikuwa ikizuiwa na vyombo vya usalama.
Lissu ikiwa ataamua kuziongoza siasa za Chadema, atakuwa na kazi ya kuhimiza kupatikana kwa katiba mpya kabla ya uchaguzi mkuu 2025. Chadema inaiona katiba mpya ni muhimu mno, kwani italinda kile watakacho kipata katika uchaguzi huo.
Ikiwa Chadema inataka kuendelea kuwa chama kikuu cha upinzani Tanzania Bara, ushawishi wa ACT Wazalendo unaozidi kukuwa kila uchao sio kitu cha kukidharau. Historia ya vyama vya upinzani Tanzania inaonesha, chama kikuu cha upinzani kinapo poromoka hakirudi tena kuwa kikuu.
Lissu ni mtaji na changamoto kwa Rais Samia
Mwishoni mwa mwaka 2018, Bunge La Ulaya lilikuja na dazeni ya maazimio kwa Tanzania, baada ya kile kilichoonekana kukithiri kwa ukandamizaji wa wananchi, kutokana na sheria kali dhidi ya asasi za kiraia, watetezi wa haki za binadamu, vyombo vya habari na vyama vya siasa.Hatua hiyo iliashiria; mambo yanazidi kuharibika panapohusika uhusiano wa Tanzania na nchi nyingine hasa zile za Kimagharibi. Pia, lilikuwa ni shinikizo la kuitaka Tanzania irudi katika mstari, ama hatua kubwa zaidi zitachukuliwa.
Mabadiliko anayoendelea kuyafanya Rais Samia, ikiwemo hili la kuifanya Tanzania kuwa sehemu salama kwa wanasiasa wa upinzani na vyama vyao, yatazidi kumuongezea heshima ya uongozi wake katika majukwaa ya kimataifa.
Tundu Lissu analeta changamoto pia kwa Rais Samia. Kuruhusu mikutano ya hadhara maanake ni kuufanya uwanja wa kufanya siasa kati ya chama tawala na vya upinzani kuwa sawa. Zile zama za Chama cha Mapinduzi kusimama peke yake katika majukwaa na kunadi sera zinakwenda kufa.
Mwezi Juni mwaka 2022, serikali ya Tanzania kupitia Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni, ilitoa kauli kwamba Rais Samia ametengeneza mazingira mazuri ya kisiasa na kuifanya nchi kuwa salama, hivyo hakuna sababu ya viongozi wa kisiasa wakiwemo wa chama cha Chadema, walioko uhamishoni kutorejea nchini.
Kwa hakikisho hilo, Rais Samia atakuwa na wajibu mkubwa wa kuhakikisha usalama wa viongozi wa upinzani na wafuasi wao kama serikali yake ilivyoeleza.
Itakuwa ajabu akiruhusu mikutano ya hadhara na kuahidi usalama, kisha matukio yale yale ya wakati wa hayati John Pombe Magufuli yakianza kujirudia.
Siasa za Tanzania zinachukua sura mpya.
Ni ile sura iliyokuwepo kabla ya mwaka 2016 – siasa za ushindani kupitia mikutano ya hadhara. Ingawa ni mapema sana kutabiri ikiwa mambo yatabaki kuwa shuari kama yanavyoonekana kuanza.