Madhara ya vyombo vya moto ni hatari sana kwa maisha ya watumiaji wake.
Tunasema haya leo tukiitazama ajali mbaya iliyohusisha magari matatu, mabasi mawili na lori iliyotokea katika wilayani Geita jana asubuhi. Hadi jana jioni watu 16 walikuwa wamethibitika kufa na wengine zaidi ya 50 kujeruhiwa katika janga hilo la kusikitisha.
Tunachukua fursa hii kuwapa pole wote waliofiwa na ndugu au jamaa katika ajali hiyo, tunawaomba wawe na moyo wa subira katika kipindi hiki kigumu cha majonzi ya kuondokewa na wapendwa wao.
Kadhalika, tunawapa pole majeruhi wote wa ajali hii, tunawatakia uponaji wa haraka ili wasimame tena na kurejea kwenye shughuli zao za kujiletea maendeleo yao na familia zao, lakini pia katika ujenzi wa taifa.
Kwa hakika wimbi la ajali limekuwa kama ni jambo la kawaida mno katika barabara zetu zote kubwa nchini, mfululizo wa ajali zinazokatiza maisha ya mamia kama si maefu kila mwaka zimekuwa zikiendelea kana kwamba hakuna njia ya kubadili hali hii.
Kwa bahati mbaya sana, kila ajali inapohusisha basi la abiria utasikia kwamba chanzo cha ajali ni uzembe, ama wa dereva au uimara wa chombo anachoendesha, lakini pengine kutokana na shinikizo la abiria au kutimiza hesabu ya siku ya mwenye chombo.
Sehemu nyingine tumesikia kwamba askari wa usalama barabarani wenye wajibu wa kudhibiti vyombo vya usafiri barabarani, nao wamekuwa na sehemu yao katika ongezeko la ajali hizi; ni nadra sana kwa askari hawa kufanya ukaguzi wa kina wa vyombo vya usafiri vilivyoko barabarani, ama kutokana na kazi hiyo kuwa kubwa mno huku idadi ya askari ikiwa ndogo, au kwa sababu tu ya kubweteka.
Kwa habati mbaya sana gari bovu kabisa linaweza kuwa barabarani kwa sababu tu dereva wake amewawezesha trafiki, tumeshuhudia magari mengi yakifia njiani, lakini mengine jinsi yanavyoonekana unajiuliza mara mbili kama trafiki kweli wako barabarani na wako makini katika kutimiza wajibu wao kwa kiwango gani.
Kwa mfano matukio ya malori kujaza mizigo kupita kiasi, kuharibika na kuachwa katikati ya barabara bila ishara yoyote ya hadhari kwa watumiaji wengine wa barabara, ni matukio ambayo yanafanyika mbele ya macho ya trafiki, lakini wanayaacha kana kwamba ndivyo sheria za usalama barabarani zinataka mambo yawe.
Tungependa kusema kwamba katika zama za sasa za mtandao wa kompyuta ni rahisi na inawezekana sana vyombo vyote vya usafiri, hasa vya abiria vikaingizwa kwenye mtandao ambao unaweza kuvifuatilia juu ya mwenendo wao vikiwa barabarani; kwa kufanya hivyo kwa mfano, itakuwa ni rahisi sana kujua nani anakwenda kwa mwendo gani na kisha hatua za hadhari kuchuliliwa kabla ya ajali kutokea.
Tunafikiri wakati sasa umefika wa kutumia maendeleo haya ya tekonolojia kutatua matatizo muhimu ya kijamii kama haya ya ajali za kila siku ambazo zimekuwa zikikatiza maisha ya wapendwa wetu, kusababisha familia hasara kubwa, lakini pia likipunguza nguvu kazi tegemeo kwa taifa hili.
Ni kwa maana hiyo, tunasema sasa tunahitaji ubunifu katika kukabiliana na ongezeko la ajali hizi.