SEHEMU YA 115
Hawakujua mwanaume huyo alikuwa akifanya nini mahali hapo kwani haikuwa rahisi kumuona mtu mweusi akiwa katika ufukwe huo.
Wakamuuliza alichokuwa akikihitaji, hakuwaficha, akawaambia kwamba alitaka kuzamia kuelekea barani Ulaya, alikuwa amesafiri kwa umbali mrefu, lengo kubwa likiwa ni kufika huko.
“Umetokea nchi gani?” aliuliza mwanaume mmoja.
“Nigeria!”
“Ooh! Sawa. Kwenda Ulaya si tatizo. Ila una pesa?” aliuliza kijana mmoja.
“Kiasi gani?”
“Kukufanyia mpango ni paundi mia tano. Ukiingia ndani ya meli, mwenyewe utatakiwa kumlipa,” alisema kijana mmoja.
“Kiasi gani?”
“Huwa anahitaji paundi elfu moja!”
“Hilo si tatizo!”
“Una passipoti?”
“Ndiyo!”
“Umegongewa viza?”
“Yeah! Ya hapa ila nilikuwa mpitaji tu!”
“Sawa.”
Hiyo ndiyo ilikuwa kazi yao kubwa, walikuwa wakiwasafirisha watu wengi katika Mfereji wa Suezi kuelekea nchini Uturuki, Hispania au Ugiriki. Walikuwa wakilipwa kiasi kikubwa cha fedha ambacho waligawana na watu wa ulinzi na kuwaruhusu watu hao kupita bila tatizo lolote lile.
Fareed alipowapa kiasi hicho, wakachukua mtumbwi mmoja na kuanza safari ya kufuata meli moja kubwa ya mizigo. Kabla ya kuifikia, wakawasiliana na nahodha aliyekuwa akihusika katika meli hiyo, walimwambia kwamba walikuwa na mtu aliyetaka kuingia nchini Uturuki.
Hilo halikuwa tatizo, walipofika katika meli hiyo, wakakaribishwa kinyemela, nahodha, Mzee Ahmed akakabidhiwa kiasi chake cha dola elfu moja na kumpeleka Fareed ndani ya chumba kimoja cha siri kilichokuwa na mizigo mingi na kumwambia akae huko.
Moyo wa Fareed ukaridhika, akahisi kwamba hiyo ndiyo njia salama ya kuepuka mkono wa sheria nchini Misri. Alijifungia ndani ya chumba hicho, baada ya saa kadhaa, meli ikatoa nanga mahali hapo na kuanza safari ya kuelekea Cyprus kabla ya kuingia nchini Uturuki.