SEHEMU YA 101
Alimdanganya mwanaume huyo, aliyemuona hakuwa shangazi yake bali mwanaume ambaye alitamani sana kulala naye. Akataka kuondoka hapo kumfuata Fareed, Keith alipong’ang’ania akamwambia kwamba huo si muda mzuri wa kumuona shangazi yake kwani hakuwa akijulikana nyumbani na haikuwa mila za kiafrika.
Keith hakuwa na jinsi, kwa kuwa alimpenda sana msichana huyo, akamuacha aendele kwa huyo shangazi yake na yeye angemsubiri ndani ya chumba hicho.
Wakati hayo yote yakiendelea, Fareed alikuwa akiangalia kupitia mlangoni huku akiwa ametokeza jicho tu. Alipomuona Maria akianza kuja kule alipokuwa, kwa haraka sana akapitia mlango mwingine, wakati msichana yule akiingia ndani ya chumba kile, na yeye alikuwa akitoka kutoka katika mlango mwingine.
Alitakiwa kuwa na haraka sana, hakutakiwa kupoteza muda hata mara moja. Akatembea kwa mwendo wa haraka mpaka katika chumba alichokuwemo Keith, akaingia ndani. “Who are you?” (wewe nani?) aliuliza Keith kwani kwa jinsi Fareed alivyoingia ndani ya chumba kile, alionekana kama mtu mwenye haraka nyingi.
“Nobody!” (si mtu yeyote) alijibu Fareed,
Hiyo ndiyo ilikuwa nafasi yake aliyokuwa akiisubiri kwa hamu. Akamsogelea Keith mahali pale, alipomfikia, akamziba mdomo, hakutaka kuchelewa, akamchoma kisu mara tatu tumboni kisha kumlaza chini.
Hakukuwa na mtu aliyeona tukio hilo, kulikuwa na mwanga hafifu na kila mtu alikuwa na mpenzi wake katika vyumba vingine. Fareed alipohakikisha mwanaume huyo amekufa, akatoka ndani ya chumba kile na kuelekea katika chumba alichokuwemo.
“Ulikwenda wapi?” aliuliza Maria huku akimwangalia Fareed.
“Kwani hukuniona?”
“Hapana! Ulijificha?”
“Ndiyo! Nilidhani unakuja na bwana wako!” alisema Fareed.
Akamkumbatia Maria na hapohapo kubadilishana mate. Mwili wa Maria ukasisimka mno, hakuamini kama kweli siku hiyo alikuwa na mwanaume huyo.
Hakutaka kurudi kwa Keith, alikuwa tayari kugombana naye lakini si kumuacha mwanaume huyo ambaye kwake alikuwa mwanaume mzuri, hakuwa radhi kumuacha.
Wakaendelea kuangalia mambo ya historia mpaka walipoitwa ambapo walitakiwa kukusanyika na kuondoka. Maria aliogopa, alijua fika kwamba Keith angemuona na kumkaripia kwa kile alichokuwa amekifanya.