SEHEMU YA 94
Fareed aliumia moyoni mwake, hakujua sababu iliyomfanya Mungu kumpitisha katika maisha aliyokuwa akipitia kipindi hicho. Alidhamiria kubadilisha maisha yake, alidhamiria kumuabudu Mungu katika roho na kweli lakini pale alipokubaliana na moyo wake kwamba alitakiwa kubadilika, tayari tatizo likawa limetokea.
Alilia, alihuzunika, moyo wake ulichoma mno. Alimwamini Padri Luke kwa kuona kwamba angemuombea msamaha kwa Mungu ili maisha yake mapya yaanze rasmi lakini kitu cha ajabu kabisa, mwanaume huyo akaamua kumbaka.
Hakutaka kuendelea kubaki pale alipotupwa, akaondoka na kurudi hotelini, huko akakaa na kulia sana, akahuzunika mno na mwisho wa siku kupanga kurudi nchini Tanzania, alitaka kuanza upya kabisa, kama mtu aliyezaliwa kwa mara ya pili.
Alirudi nchini kimya kimya, hakutaka kumtaarifu Asteria kama alikuwa amerudi, alifanya hivyo kwa sababu alitaka kuyabadilisha maisha yake, aiondoe tamaa iliyokuwa mwilini mwake, asimtamani tena mwanaume ashinde vishawishi vyote na kuwa mtu mpya.
Akamtafuta daktari aliyekuwa akiwahudumia sana wanaume tata, huyo aliitwa Emmanuel Kihampa, daktari maarufu aliyekuwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Alipofika huko, akamfuata katika ofisi yake na kuanza kuzungumza naye.
Hakutakiwa kumficha kitu chochote kile, alitakiwa kumwambia kila kitu kilichokuwa kikiendelea mwilini mwake, alimwambia tabia yake hiyo ambayo ilianza tangu utotoni, alimwambia juu ya tamaa kali aliyokuwa nayo.
Daktari huyo akampa vidonge vya kumeza lakini pia alitakiwa kuchomwa sindano nyumba kwa ajili ya kuua vijidudu ambavyo vilikuwa vikimuingiza katika matamanio makubwa. Hilo halikuwa tatizo, alidhamiria kubadilika, alidhamiria kuyabadilisha maisha yake, hivyo akachomwa sindano hiyo.
Haikutosha, akaambiwa kwamba ilikuwa ni lazima auweke mwili wake kimazoezi, alitakiwa kufanya mazoezi ya kila aina kuhakikisha anakuwa sawa.
Akaanza kukimbia mitaani, akawa anajiunga na vijana wengine kufanya mazoezi huku ikifika usiku, alitumia muda wake mwingi kusoma vitabu, yote hiyo ilikuwa ni harakati za kuachana na tabia chafu alizokuwa nazo kwamba asingeweza kufikiria ngono kama kipindi cha nyuma.