Michirizi ya Damu

Michirizi ya Damu

SEHEMU YA 78

“Zimekwisha…” alijibu mwanamke huyo na kukata simu.
Kyle hakuwa kwenye hali nzuri hata mara moja, kadiri dakika zilivyozidi kwenda mbele ndivyo hali yake ilivyozidi kuwa mbaya kiasi kwamba kila mmoja ndani ya nyumba hiyo alijua kwamba siku hiyo ndiyo ilikuwa siku ya mwisho kwa msichana huyo kuishi duniani.

Upande wa pili Dk. Watson ambaye alitakiwa kumpasua Fareed na kutoa kete za madawa ya kulevya alichanganyikiwa kupita kawaida. Alimuandaa mwanaume huyo kitandani, alimnywesha maji yaliyokuwa na dawa ya usingizi na alipotaka kumfanyia upasuaji akapokea simu hiyo kutoka kwa mkewe, simu ambayo ilimtisha kupita kawaida.

Hakutaka kubaki hospitalini hapo, mtoto wake, Kyle alikuwa kila kitu katika maisha yake, alimpenda kuliko kitu chochote kile, kuipuuzia simu ile na kuendelea kufanya mambo yake kwake lilionekana kuwa jambo la kijinga ambalo hakuwahi kulifanya katika maisha yake yote, alichoamua ni kuwaambia vijana waliomleta Fareed kwamba asingeweza kumpasua kwani kulikuwa na simu muhimu aliyokuwa amepigiwa.

“Ila si mara moja tu dokta?” aliuliza kijana mmoja.
“Hapana! Hii kazi inahitaji umakini sana kwani unaweza kumpasua ilimradi tu ukazipasua kete hizo na kupata hasara,” alisema daktari huyo, akawaaga na kuwaambia kwamba angerudi baada ya kumnunulia mtoto wake dawa iliyokuwa ikihitajika.

“Kwa hiyo huyu tumfanyaje?”
“Mwacheni humohumo nitakuja!”
“Sawa.”
Vijana wale hawakuwa na neno lolote lile, walichokijua ni kwamba Fareed alikuwa salama ndani ya chumba kile, wakabaki mahali hapo huku wakipiga stori kwani hawakutakiwa kuondoka mahali hapo mpaka daktari huyo atakaporudi na kufanya kile alichotakiwa kufanya.

Muda ukazidi kwenda mbele, dakika zilikatika lakini Dk. Watson hakuwa amerudi hospitalini hapo kitu kilichowafanya kuwa na wasiwasi kwamba inawezekana daktari huyo aliwakimbia.

Wakampigia simu, akawaambia kwamba angekuja kwani hali ambayo alimkuta nayo mtoto wake haikuwa nzuri, ilikuwa ni lazima akae naye kidogo na kurudi hospitalini hapo kuendelea na kazi.
 
SEHEMU YA 79

Lilipofika saa moja, Fareed akashtuka kutoka katika usingizi aliokuwa nao. Kitu cha kwanza kabisa baada ya kuyafumbua macho yake ni kuangalia mahali alipokuwa.

Aligundua kwamba palikuwa ni hospitalini, hakukumbuka ni kwa namna gani alifika mahali hapo lakini baada ya kukaa na kukumbuka kwa sekunde kadhaa, akakumbuka kila kitu kilichokuwa kimetokea.

Akakurupuka kutoka kitandani pale, ile haikuwa sehemu salama, alijua fika kwamba kama asingeondoka ndani ya chumba hicho ilikuwa ni lazima kupasuliwa tumbo lake na kutolewa kete za madawa ya kulevya zilizokuwa tumboni mwake.

Hakutaka kuona hilo likitokea, ilikuwa ni lazima kuondoka hospitalini hapo, akateremka kutoka kitandani, akaufuata mlango lakini hata kabla hajaufungua, akawasikia watu wakiwa wanaongea kwa nje.

“Mmh!” alijikuta akiguna.
Hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya, akarudi kitandani pale na kutulia, kichwa chake kilimuuma, alitamani hata kupitia katika mlango mwingine lakini kitu kibaya kwake ni kwamba hakukuwa na mlango wowote zaidi ya ule waliokuwa wakiutumia.

Minong’ono ile ya watu bado iliendelea kusikika kutoka nje ya chumba kile, aliogopa, kwa jinsi alivyoona, ilikuwa ni lazima watu hao waingie ndani kumwangalia kwani hakujua daktari alikuwa mahali gani.

Alichokifanya ni kuusogelea mlango na kisha kuufunga kwa ndani, hakutaka mtu yeyoite aingie ndani ya chumba kile na kumkamata, alijua kwamba angekufa, ila hakuwa tayari kuona akifa siku hiyo.

“Ni lazima nifanye kitu!” alisema lakini hata kabla hajafanya kitu hicho, akasikia kitasa cha mlango kikianza kutekenywa kwa ajili ya kufunguliwa lakini haukufunguka kitu kilichowafanya kuanza kuugonga kwa lengo la kuuvunja.
 
Back
Top Bottom