SEHEMU YA 73
Hakushtukiwa na mtu yeyote yule, akatoka na kwenda sehemu ya watu waliokuja kuwasubiri watu wengine, hapo akamuona kijana mmoja akiwa amesimama huku akiwa na bango dogo lililoandikwa jina lake ambapo akamfuata na kujitambulisha kwamba yeye ndiye alikuwa Fareed.
“Are you Fareed?” (wewe ndiye Fareed?) aliuliza jamaa huyo huku akishangaa.
“Yes!” (ndiyo)
“How? Are you a boy or girl?” (Kivipi? Wewe ni mvulana au msichana?)
“Hey! You are wasting my time. Take me where Am suppose to be,” (Hey! Unanipotezea muda.
Nipeleke ninapotakiwa kuwa) alisema Fareed huku akionekana kuanza kukasirika.
Mwanaume huyo hakuongea kitu chochote lakini alionekana kuwa na maswali mengi kichwani mwake. Alikuwa akijiuliza kuhusu mtu aliyekwenda kumpokea, ilikuwa awe na jina la kiume na wakati alikuwa na muonekano wa kike?
Alivalia gauni refu, kichwani alikuwa na wigi, alipaka wanja na lipstic, sasa ilikuwaje awe mwanaume?
Hakutaka kujiuliza maswali zaidi bali ni kukaa kimya na kuendelea kuendesha gari kuelekea katika sehemu ambayo alitakiwa kumpeleka mgeni huyo. Akiwa hapo njiani akamtumia meseji Belleck kwamba mgeni aliyetakiwa kufika, tayari alikuwa ndani ya gari
*** Belleck aliwaanda vijana wake kwa ajili ya kazi ya kuyatoa madawa ya kulevya kutoka tumboni mwa Fareed. Yalikuwa ni madawa yenye thamani kubwa ambayo yangemuingizia kiasi kikubwa cha fedha.
Kete za madawa hayo zilikuwa tumboni mwa Fareed, kwa kawaida alitakiwa kwenda kujisaidia ili kutoa kete hizo lakini Bellck hakutaka kuona hilo likifanyika na badala yake alihitaji mtu huyo apasuliwe tumbo na kutolewa madawa hayo.
Hilo halikuwa tatizo hata kidogo, waliwahi kufanya kazi kama hiyo kipindi cha nyuma kwa watu wengi, kuua, kwa vijana hao lilionekana kuwa jambo dogo sana ambalo lilikuwa ni kama kumuua sisimizi kwa kumkanyaga.
Walijiandaa nyumbani, walimtuma mwenzao kwenda kumpokea Fareed uwanja wa ndege ili atakapofika basi kazi ya kumpasua tumbo ianze mara moja.