Michirizi ya Damu

Michirizi ya Damu

SEHEMU YA 75

Hakukuwa na mtu aliyepona, wote waliokuwa wakipelekwa huko, walichomwa sindano ya usingizi na kufanyiwa upasuaji huo ambao uliwapelekea vifo vyao.
Alizoea kazi hiyo, alilipwa kiasi kikubwa cha fedha na hakutaka kuiacha. Mara kwa mara Bilionea Belleck alipokuwa akiwatuma watu, alipigiwa simu na kuambiwa aelekee nyumbani kwa bilionea huyo kisha kufanya kazi hiyo au kama alibanwa sana basi ilikuwa ni lazima mtu huyo apelekwe katika hospitali yake na kumfanyia upasuaji.

Muda huo alipigiwa simu na kijana wa Belleck na kumwambia kwamba kulikuwa na kazi alitakiwa kuifanya. Hakushtuka lakini kwa siku hiyo kulikuwa na ugumu kwani hospitalini hapo alikuwa na wagonjwa ambao walihitaji sana kufanyiwa upasuaji.
“Mleteni lakini nitamfanyia baada ya saa tano,” alisema Dk. Watson.
“Haina shida.”

Hawakutaka kubaki nyumbani hapo, haraka sana akachukuliwa na kupelekwa katika hospitali hiyo. Muda wote huo Fareed alikuwa na hofu moyoni mwake, alihisi kwamba huo ndiyo ulikuwa mwisho wake.

Alikuwa na mzigo mkubwa wa madawa ya kulevya tumboni mwake, wakati mwingine alihisi kwamba kete zile zingeweza kupasuka na madawa hayo kusambaa mwilini mwake na kumuua.

Hakutaka kuona hilo likitokea, alilia kimyakimya, kwake, Belleck alionekana kuwa mwanaume katili aliyeithamini fedha yake kuliko hata uhai wa watu wengine. Huyo hakuwa mwanaume aliyestahili kuwa hai, alitakiwa kuuawa kwani kwa kutumia fedha zake alipata nafasi ya kuwafanyia watu wengine matendo mabaya ya kikatili.

“Mungu nisaidie! Nikitoka katika hili, nitakukabidhi maisha yangu!” alisema Fareed huku gari likiwa safarini kuelekea hospitalini huko.
Hawakuchukua muda mrefu wakafika hospitalini hapo ambapo moja kwa moja akachukuliwa na kupelekwa katika chumba maalumu kwa ajili ya mapumziko.

Hapo alipokuwa, muda wote mwili wake ulikuwa ukimtetemeka, aliogopa, mbele yake alikiona kifo kitu ambacho hakutaka kukiona kikitokea mpaka pale atakapokamilisha ndoto zake.
 
SEHEMU YA 76

“Mbona unakuwa na hofu sana?” aliuliza mwanaume mmoja.
“Hapana! Sina hofu!”
“Usiogope. Ni suala la kuchukua mzigo wetu na wewe tutakuruhusu kuondoka,” alisema mwanaume huyo, japokuwa alijitahidi kumuondoa hofu Fareed lakini hakuonekana kuwa na amani hata kidogo.

Baada ya dakika kadhaa, daktari huyo akafika mahali hapo, akamwangalia fareed, uso wake ulikuwa na maswali mengi juu ya jinsi aliyokuwa nayo mtu aliyeletwa hospitalini kwake siku hiyo.
“Huyu ni mwanamke au mwanaume?” aliuliza Dk. Watson.

“Mwanaume!”
“Hapana! Mbona kama mwanamke?”
“Ni mwanaume tata!”
“Hapo sawa. Tena kwa sababu ana tabia chafu hivyo, nitamfanyia upasuaji bila ganzi,” alisema daktari huyo.

Baada ya dakika kadhaa, akamwambia Fareed aingie katika chumba kingine kabisa. Akasimama na kuelekea katika chumba hicho ambacho kwa kukiangalia tu wala usingejiuliza maswali mengi juu ya kazi iliyokuwa ikifanyika ndani ya chumba hicho.

Kulikuwa na vifaa vingi vya kufanyia upasuaji, kilitisha na kila wakati Fareed alipokuwa akikiangalia mapigo yake ya moyo yalidunda kwa nguvu, aliogopa mno na kuuona mwisho wake ukiwa umekaribia.

“Usiwe na hofu, chukua maji kwanza unywe,” alisema daktari huyo huku akimpa maji ambayo aliyawekea dawa ya usingizi. Fareed hakujua, akayapokea maji hayo na kunywa harakaharaka, baada ya dakika mbili tu, macho yake yakawa mazito na hapohapo kulala kwenye kiti alichokuwepo. Akanyanyuliwa na kulazwa kwenye kitanda cha kufanyia upasuaji tayari kwa kufanya kazi hiyo.

JE, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 77

“Mchungaji! Mimi ni mkosaji! Nimekuja kutubu dhambi zangu! Nimekuwa nikimtumikia shetani kwa kipindi kirefu katika maisha yangu. Nimemtenda Mungu wangu dhambi! Nimekuja kutubu mchungaji,” alisikika mtu mmoja akimwambia padri aliyekuwa kwenye chumba kidogo cha kuungama dhambi.

“Umefanya nini mtoto wa Mungu?” aliuliza padri huyo.
“Nimezini kwa kipindi chote cha maisha yangu, nimekuwa na tamaa ya fedha, nimekuwa nikimtumikia shetani kwa kila aina ya uchafu. Nimechoka, ninataka kuokoka mchungaji, sitaki kumtumikia tena shetani,” alisikika mtu huyo akizungumza na padri huyo ambaye muda wote alikuwa akionyesha ishara ya msalaba.

“Mungu atakusamehe dhambi zako. Amesema kwamba hata kama dhambi zako zinakuwa nyekundu kama damu, atazisafisha na kuwa nyeupe kama theluji,” alisema padri huyo.
****

“What is wrong with her?” (nini kimemtokea?)
“Asthma.” (pumu)
“Where is her inhler?” (kifaa chake cha kuwekea dawa ya pumu kipo wapi?) alisikika mwanamke mmoja akiuliza.
“Here it is but there is nothing in it!” (hiki hapa lakini ndani hakuna kitu) alisikika msichana mmoja akijibu.

“What?” (nini?)
Kila mmoja ndani ya nyumba alichanganyikiwa, mtoto Kyle alikuwa amebanwa na pumu ambayo ilikuwa ikimsumbua kila siku. Mama yake na mfanyakazi wa ndani walichanganyikiwa, walijaribu kuangalia dawa ya kumpa iliyokuwa kwenye kifaa kidogo kinachojulikana kama inhler ambacho alitakiwa kuivuta kwa mdomo dawa hiyo lakini kitu cha kushangaza kabisa, kifaa hicho hakikuwa na dawa yoyote ile.

Waliuona mwisho wa Kyle, alikuwa akilalamika, alikipandisha kifua chake juu kama mtu aliyetaka kukata roho, alipumua juu juu kwa tabu sana kiasi kwamba kila mmoja alikuwa na uhakika kwamba binti yao angekufa usiku huo.
Mama yake hakutaka kuchelewa, haraka sana akachukua simu yake na kumpigia mume wake, Dk. Watson ambaye alikuwa ni daktari kwa lengo la kumwambia kile kilichokuwa kikiendelea kwa mtoto wao, Kyle.

“Unasemaje?” alisikika daktari huyo akiuliza kutoka upande wa pili wa simu.
“Kyle anakufa! Njoo na dawa haraka sana.”
“Dawa zake zipo wapi?”
 
Back
Top Bottom