Michirizi ya Damu

Michirizi ya Damu

SEHEMU YA 70

“Hapana!”
“Hahaha! Unakosa utamu mkubwa sana. Ni pombe nzuri yenye kulewesha kidogo,” alisema Belleck huku akiifuata chupa moja iliyokuwa mezani ambayo iliandikwa Kemical Boom ambayo ilikuwa na kilevi cha 70%.

“Mmh! Nitaiweza?”
“Kwa nini uishindwe mpenzi! Ni tamu sana,” alisema Belleck huku akichukua glasi na kuimimina pombe ile katika glasi ile aliyokuwa nayo.
Ilikuwa vigumu kwa Fareed kugundua kwamba mwanaume huyo alikuwa mtu mbaya katika maisha yake, alichokiona, kilikuwa ni mapenzi ya dhati, kila alichokuwa akifanyiwa, kwake kilionekana kuwa sahihi kwa kuwa tu alipewa fedha nyingi na mwanaume huyo.

Akaifakamia pombe hiyo na kuanza kunywa kwa kasi. Hakuchukua dakika nyingi, akahisi viungo vya mwili wake vikianza kuuma, akaanza kusikia kizunguzungu, ilikuwa pombe kali na hakutakiwa kunywa nyingi kiasi hicho. Wakati akiwa kwenye hali hiyo, ndiyo kwanza Belleck alikuwa akicheka tu.
“Nimelewa…..” alisema Fareed. Hakukaa kwenye hali hiyo kwa muda mrefu, akaona giza, akajilaza kitandani, alionekana kama mtu aliyepoteza fahamu.

“Safi sana! Ngoja niwaite vijana,” alisema Belleck, hapohapo akachukua simu na kuwapigia vijana wake wa kazi.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 71

Ndani ya dakika kadhaa wanaume watatu wakafika mahali hapo, walikuwa wamejiandaa vilivyo, kwa jinsi walivyoonekana, walikuwa tayari kufanya kazi muda wowote ule. Belleck akawakaribisha huku akionekana kuwa na furaha tele, katika maisha yake yote, hakukuwa na kitu kilichokuwa kikimuingizia fedha kama biashara ya madawa ya kulevya.

Alitaka kumtumia Fareed katika biashara zake, alitaka kumpa mzigo wa madawa ya kulevya na kuyasafirisha maka nchini Ufaransa. Hilo kwake halikuwa tatizo, usiku huohuo wakamnywesha kete kumi na mbili za madawa ya kulevya na kumsubiri aamke ndipo wamwambie kuhusu safari hiyo kwani tayari walimuandalia tiketi yake.

Fareed aliamka baada ya saa moja kupita. Alijisikia uchovu, hakujua alikuwa mahali gani. Pale alipokuwa kulikuwa na kitanda kikubwa, chumba kizuri, akaamka na kuanza kuangalia huku na kule na ndipo kumbukumbu zake zikaanza kurudi na kukumbuka kwamba mara ya mwisho alikunywa pombe kali na baada ya hapo hakujua ni kitu gani kiliendelea.

“Nipo wapi? Belleck kanileta wapi?’ alijiuliza huku akisimama kutoka pale alipokuwa.
Akaelekea dirishani, akachungulia, alikuwa kwenye ghorofa ya nne, aliogopa, ile haikuwa hoteli aliyokuwa amefikia, ilikuwa nyingine kabisa. Alipoangalia kwenye kimeza kidogo akakutana na kitabu kidogo kilichoandikwa ‘King Caspian Hotel’.

“Nimefikaje King Caspian?” alijiuliza.
Aliijua hoteli hiyo, ilikuwa hapohapo Kuwait, haikuwa hoteli ile aliyofikia, alijiuliza sana lakini mwisho wa siku akajua kwamba Belleck ndiye aliyekuwa akifahamu kila kitu kilichokuwa kimetokea.

Alijaribu kutoka ndani ya chumba hicho, mlango ulikuwa umefungwa kwa nje, moyo wake ukajawa na hofu kwa kuhisi kwamba Belleck alikuwa mmoja wa wafanyakazi wa Keith ambao walijua kwamba hakuwa amekufa baharini hivyo kutaka kumuua tena.

“Mungu! Huyu Keith ananitakia nini lakini?” alijiuliza huku akionekana kuwa na hasira kali.
Akaliangalia begi lake lililokuwa pembeni, zipu ilikuwa wazi kuonyesha kwamba kulikuwa na mtu alilifungua, alipoangalia ndani, akakuta kukiwa kumepekuliwa, hakukuwa na vitambulisho vyake, hakukuwa na hati ya kusafiria.
 
SEHEMU YA 72

Alichanganyikiwa, hakujua ni kitu gani kilikuwa kimetokea. Moyo wake ukaingiwa na hofu kwa kuona kwamba alipoteza kila kitu, akakifuata kitanda, akakaa na kuanza kulia.

Wakati akiendelea kulia, mara mlango ukafunguliwa na wanaume watatu kuingia ndani ya chumba hicho. Hawakuzungumza kitu, walibaki wakimwangalia. Harakaharaka Fareed akasimama na kuwaangalia, akajua kwamba watu hao ndiyo waliokuwa wamefungua begi lake na kupekua.

“Naomba mnisamehe! Hivi kwa nini Keith anataka kuniua? Nimemfanya nini? Kama ni gharama za pesa yake nitamrudishia,” alisema Fareed huku akiendelea kulia.

“Keith ndiye nani?”
“Bosi wenu aliyewatuma!”
“Hatumfahamu huyo. Tumekuja kukupa ujumbe mmoja.”
“Upi?”

“Unatakiwa kusafiri leo kuelekea Ufaransa,” alisema mwanaume mmoja.
“Kuelekea Ufaransa?”
“Ndiyo!”
“Kufanya nini?”
“Una mzigo wetu tumboni mwako, utatakiwa kufika nchini humo.

Utakapofika katika Jiji la Marseille, ukitoka nje utakuta kuna mtu anakusubiri huku akiwa na bango lililokuwa na jina lako, mfuate huyo, ukipinga na kufanya kitu cha tofauti, tutakuua!” alisema mwanaume huyo huku akimwangalia Fareed kwa macho yaliyomaanisha kile alichokuwa akikisema.

“Sawa,” alijibu Fareed huku akitetemeka.
Muda ulipofika, akakabidhiwa kila kitu na kuanza kuelekea uwanja wa ndege. Moyo wake ulijuta, wakati mwingine alijiapiza kutokurudia kufanya ukahaba kwa Wazungu kwani wao ndiyo waliokuwa wakimuingiza kwenye matatizo tofauti na Waarabu ambao wao walichokuwa wakikihitaji ni mapenzi tu.

Njia nzima alilia, hakunyamaza, mpaka alipoingia ndani ya ndege bado aliendelea kulia kama kawaida. Moyo wake ukaanza kuifikiria safari hiyo, hakujua kama angevuka salama uwanja wa ndege kwani kwa nchi za Ulaya na Marekani kulikuwa na ulinzi mkali viwanjani kuliko hata katika nchi za Afrika na Asia.

Alitumia saa thelathini kwenye ndege, tena kwa kubadilishabadilisha mpaka alipofika nchini Ufaransa katika Jiji la Marseille. Akateremka na abiria wengine, mabegi yakapita sehemu ya uchunguzi na wao kuruhusiwa.
 
Shunie
shemeji yangu ukipost muendelezo naomba unitag pleas.
hii hua inanikosa kwa wakati sjui kwanin.
but nisaidie please
 
Back
Top Bottom