CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimemshukia Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, John Tendwa, kikisema kuwa ameanza propaganda za kukibeba Chama cha Mapinduzi (CCM) katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Arumeru Mashariki.
Tendwa alikaririwa na vyombo vya habari akimtahadharisha Mbunge wa CHADEMA katika Jimbo la Arusha Mjini, Godbless Lema, kutokanyaga kwenye kampeni za uchaguzi huo kwa tishio la kuuawa na viongozi wa kimila (Washiri).
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CHADEMA, John Mnyika, alisema kauli ya Tendwa ni ishara ya kutumia madaraka vibaya kujaribu kuibeba CCM kwenye uchaguzi huo mdogo baada ya wananchi wa Arumeru kuonyesha wanakipenda CHADEMA na kutaka mabadiliko.
Tendwa akae pembeni aache uchaguzi kwa vyama vya CHADEMA na CCM. Alikwenda kufanya tathmini na amelizungumzia jambo moja ambalo amelifanya propaganda, mbona hazungumzii rushwa iliyofanywa na CCM kwenye kura za maoni? alihoji Mnyika.
Alisema wadau mbalimbali wamelalamikia vitendo vya rushwa vilivyojitokeza CCM na kwamba yeye kama msajili kuna sheria tatu ambazo zinampa mamlaka ya kuzungumzia hayo.
Alisema kuna sheria ya vyama vya siasa ambayo moja kwa moja inampa wajibu wa kuzungumzia rushwa kadhalika ile ya gharama za uchaguzi ambayo inampa mamlaka ya kufuatilia vitendo hivyo.
Kama ana nia njema, vitendo vya rushwa ambavyo pia vinazungumzwa na wana-CCM wenyewe angevitolea kauli, kuacha hayo ni kutumia madaraka vibaya. Kuyaacha mambo ya msingi na kulizungumzia moja tu ni propaganda za kuibeba CCM, alisema
Katika hilo, Mnyika alimtaka Tendwa afanye mambo mawili; kwanza atoe ripoti ya kina ya tathmini aliyokwenda kufanya Arumeru na ijulikane wazi na pili, kwa sababu ameitaja CHADEMA awakabidhi nakala ya ripoti kamili aliyoifanya, vinginevyo watachukua hatua.
Mnyika aliwatahadharisha wananchi wa Arumeru Mashariki, kukumbuka kuwa wakati wa kampeni, viongozi wa serikali wamekuwa na kawaida ya kutumika propaganda kusaka ushindi.
Wanataka wananchi wa Arumeru, wajifunze kilichotokea Tarime mwaka 2008, waliamua kuwa na mshikamano, wakapuuzia propaganda wakaamua kuchagua CHADEMA, alisema Mnyika.
Kwa mujibu wa Mnyika, Machi 3-4 watafanya uteuzi na si kuangalia propaganda kama za Tendwa. Hivyo kuwataka wazee wa Arumeru Mashariki kuwaunga mkono ili kazi waliyoianza mwaka 2010 ilete manufaa.
Source:Tanzania Daima