WIZI FEDHA ZA UMMA:
:: Ni ile iliyohusishwa na ufisadi BoT :: Msimamo wa CAG wamkaanga Balali
:: Asema hakuwahi kukagua hesabu zake :: Mbunge ahoji ni ya umma au binafsi
Na Godfrey Dilunga, wa Mtanzania
WAKATI Bunge likianza Mkutano wake ujao, keshokutwa, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh, amekana kuitambua wala kukagua hesabu za kampuni tata ya Meremeta, inayohusishwa na ufisadi wa mabilioni Benki Kuu ya Tanzania (BoT).
Taarifa iliyowahi kutolewa na Serikali ilieleza kuwa, kampuni hiyo ilikuwa ikimilikiwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kwa ajili ya mradi wake wa Nyumbu, Kibaha, Mkoa wa Pwani.
Hata hivyo, Utouh anasisitiza kuwa, haimo katika orodha ya kampuni 158 za umma, zilizomo katika orodha ya ukaguzi.
CAG aliikana Meremeta Ltd jana jijini Dar es Salaam, katika semina kati ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mashirika ya Umma (POC), na wenyeviti na watendaji wa mashirika ya umma.
Alifikia hatua hiyo baada ya Mbunge wa Musoma Vijijini, Nimrod Mkono, kutaka Msajili wa Mashirika ya Umma kueleza kampuni hiyo ni ya binafsi au umma. Kama ni ya umma, alitaka CAG aeleze kama aliwahi kukagua hesabu zake.
Kwa mujibu wa Mkono, waliowahi kuwa wafanyakazi wa kampuni hiyo wamekuwa katika hali ngumu ya kufuatilia mafao yao na wamekuwa wakitaka kujua hatima yao kutoka kwake, kama mbunge.
"Ndugu mwenyekiti (wa Kamati ya Bunge, Kabwe Zitto) siijui Meremeta na si kati ya mashirika na taasisi za umma 158 ambazo nimekagua hesabu zake," alisema CAG.
Kampuni ya Meremeta inadaiwa kuwahi kuendesha shughuli za uchimbaji dhahabu, Musoma Vijijini.Hata hivyo, baadaye kampuni hiyo inadaiwa kuchotewa mabilioni ya fedha kutoka BoT katika mazingira yenye utata.
Ni miongoni mwa kampuni zilizowahi kutamkwa bungeni mwaka jana, zikihusishwa na ufisadi wa mabilioni katika Benki Kuu.
Inadaiwa kwamba, aliyewahi kuwa Gavana wa Benki Kuu, Dk. Daudi Balali aliidhinisha au kuruhusu au kunyamazia malipo ya dola za Marekani 118,396,460.36 zinazodaiwa kupelekwa katika akaunti isiyojulikana ya Benki ya Nedbank Ltd. ya Afrika Kusini.
Fedha hizo zinadaiwa kupelekwa huko kama malipo ya madeni ya kampuni muflisi ya Meremeta Ltd, iliyokuwa inachimba dhahabu katika eneo la Buhemba Wilaya ya Musoma, mkoani Mara.
Tangu kuanzwa kutajwa kwa kampuni ya Meremeta bungeni, Serikali imekuwa ikitoa taarifa mbalimbali.
Taarifa hizo ni pamoja na inayodai kuwa Meremeta Ltd, ilikuwa kampuni ya Kitanzania iliyokuwa ikimilikiwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kwa ajili ya mradi wake wa Nyumbu, Kibaha, Mkoa wa Pwani.Hata hivyo, habari zilizowahi kuandikwa na vyombo vya habari nchini, zilidai kuwa nakala ya usajili iliyotolewa na Msajili wa kampuni Uingereza na Wales, inaonyesha kampuni hiyo iliandikishwa nchini Uingereza.
Iliandikishwa Uingereza, Agosti 19, mwaka 1997 na ilifilisiwa huko huko Uingereza, Januari 10, 2006.
Hapa nchini, inadaiwa kuwa taarifa ya Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) ya Mei 31, mwaka 2005 inaonyesha Meremeta Ltd ni tawi la kampuni ya kigeni iliyosajiliwa Tanzania kama tawi, Oktoba 3, 1997.
Vile vile taarifa hiyo inaonyesha kwamba hisa 50 za Meremeta Ltd.
zilikuwa zinamilikiwa na Kampuni ya Triennex (Pty) Ltd. ya Afrika Kusini na hisa 50 zilizobaki zilikuwa zinamilikiwa na Serikali ya Tanzania kwa kupitia kwa Msajili wa Hazina katika Wizara ya Fedha.
Inadaiwa kuwa, Gavana Balali aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Meremeta Ltd. kati ya mwaka 2004 na 2005.
Hata hivyo, kuna utata mkubwa juu ya nani ni mmiliki hasa wa Meremeta Ltd. kwa kuwa taarifa ya BRELA inaonyesha pia kwamba kampuni mbili za Kiingereza – London Law Services Ltd. na London Law Secretarial Ltd. zinamiliki hisa moja moja za Meremeta Ltd.Kampuni hizo zinadaiwa kutumia anwani moja iliyoko 84 Temple Chambers, Temple Avenue, jijini London.
Baadhi ya hoja zinazogonga vichwa vya wafuatiliaji wa masuala ya kitaifa, ni kwamba, hajulikani ni kwa nini Gavana Balali aliruhusu fedha za umma kutumika kulipia madeni yote ya kampuni ambayo Serikali ilikuwa inamiliki hisa 50 tu, wakati kampuni nyingine za kigeni zilikuwa zikimiliki hisa 52.