Natoa tamko la kumuomba radhi Abdulrahman Kinana, ikumbukwe nilikuwa na kesi katika Mahakama Kuu ya Tanzania iliyofunguliwa na Kinana kutokana na matamshi niliyowahi kuyatoa kumuhusisha na ujangili. Ninakiri tuhuma hizo hazikuwa za kweli wala ushahidi wowote, bali zilikuwa na malengo potofu ya kisiasa na kizandiki.
============
FULL TEXT:
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
TAMKO LA KUOMBA RADHI LA MHE PETER SIMON MSIGWA (MB)
Ndugu Wanahabari,
Leo nimewaita kwa ajili ya jambo moja tu; kutoa tamko la kuomba radhi kwa ndugu yangu Abdulrahman Kinana.
Itakumbukwa kwamba nilikuwa na kesi katika Mahakama Kuu ya Tanzania iliyofunguliwa na ndugu Kinana dhidi yangu kwa sababu ya matamshi niliyowahi kuyatoa dhidi yake –ndani na Bunge, nikimhusisha na biashara ya ujangili na uuzaji wa nyara za serikali.
Katika hotuba yagu nikiwa Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni nikiwasilisha maoni yetu wakati wa mjadala wa makadirio ya matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii ya mwaka 2013/2014, nilitoa maelezo marefu ya kumhusisha ndugu Kinana na biashara hizo.
Kutokana na tuhuma zangu hizo kwake, Ndugu Kinana alinifungulia mashitaka katika Mahakama Kuu ya Tanzania kwa shauri namba 108 ya mwaka 2013. Katika kesi hiyo iliyosikiliwa na kuhukumiwa na Jaji Zainab Muruke, nilikutwa na hatia baada ya kushindwa kuthibitisha tuhuma zangu hizo mbele ya Mahakama.
Leo, nakiri mbele yenu na kupitia ninyi, mbele ya Watanzania, kwamba tuhuma hizo nilizozitoa mara kadhaa dhidi ya Kinana hazikuwa na ukweli wala ushahidi wowote. Taarifa nilizopewa na kuzitumia hazikuwa na ukweli bali zilikuwa na malengo potofu ya kisiasa na kizandiki. Nasikitika kwamba taarifa hizo nilipewa na watu waliokuwa na malengo maovu.
Mambo kama haya hutokea katika jamii na maishani. Nasi kama binadamu inapotokea kuwakosea wenzetu busara hututuma kuomba radhi na kwa waliokosewa kuwa tayari kusamehe.
Ni dhahiri kwamba kupitia kauli zangu za huko nyuma dhidi yake, nimemkosea, nimemdhalilisha na kumkashifu ndugu yangu Kinana. Nafurahi kuwaambia hapa kwamba nimekutana na kaka yangu Kinana na kumuomba radhi yeye binafsi na amekubali kunisamehe.
Nimekuja hapa hadharani kuomba radhi kwa sababu nafahamu aliyeumizwa si Kinana peke yake, bali familia yake, ndugu zake na marafiki zake.
Mtakubaliana nami kwamba Ndugu Kinana ni mzalendo, mtu muungwana na mstaarabu ambaye kwa kweli hastahili kuzushiwa, kukashifiwa wala kudhalilishwa. Ninamshukuru na kwa kweli nitaendelea kumheshimu kama alivyodhihirisha undugu, ustaarabu na uungwana wake kwangu na kwa familia yangu.
Baada ya msamaha huo wa Kinana, sasa shauri hili la kimahakama sasa litakuwa limemalizika rasmi.
Nawashukuru sana kwa kuhudhuria na kunisikiliza. Ahsanteni.
Mhe Mchungaji Peter Simon Msigwa
Mbunge, Jimbo la Iringa Mjini
Aprili 19, 2020
Dar es Salaam.
============
Pia soma:
1) HOTUBA ya Kambi ya Upinzani Bungeni, Maliasili na Utalii na Peter Msigwa (FULL TEXT)
2) Kinana kupitia Wanasheria amuandikia Msigwa kumtaka amuombe radhi
3) Mchungaji Msigwa (CHADEMA) amtaka Kinana awahi kortini
4) Kinana amburuza Msigwa kortini
5) Msigwa amuomba mzee Mtei akaongee na Kinana ili wayamalize!
6) Mahakama kuamua kesi ya Kinana leo
Umemkosea Mungu umemkosea kinana