MakinikiA
JF-Expert Member
- Jun 7, 2017
- 5,011
- 6,542
Rais Joe Biden ameondoa marufuku iliyowekwa na Donald Trump ya kuwapiga marufuku watu waliobadili jinsia kujiunga na jeshi.
Marufuku hiyo ilitangazwa na Bw. Trump mwaka wake wa kwanza akiwa rais wa Marekani.
''Watumishi waliobadili jinsia hawatakabiliwa na uwezekano wa kuondolewa au kutengwa kwa misingi ya utambulisho wao kijinsia,'' Ilisema ikulu ya White House.
Kulikuwa na askari 8,980 mwaka 2019, kwa mujibu wa takwimu za Idara ya Ulinzi zilizochambuliwa na taasisi ya Palm Center.
''Rais Biden anaamini kuwa jinsia haipaswi kuwa kikwazo kwenye utumishi jeshini, na kuwa nguvu ya Marekani iko kwenye utofauti wa wake,'' Taarifa ya Ikulu iliongeza.
Waziri mpya wa Ulinzi Lloyd Austin, generali wa jeshi mstaafu, alisema kwenye taarifa: ''Idara itatumia sera hii kuhakikisha kuwa watu wanaojipambanua kuwa wamebadili jinsia wanapata uhalali wa kuingia na kutumikia jeshi.''
''Vikosi vya kijeshi vya Marekani vina kazi ya kutetea raia wenzetu dhidi ya maadui, wa nje na ndani.
Natumaini tutafanikisha hili vyema ikiwa tutawawakilisha raia wenzetu wote,'' aliongeza.
Bwana Trump alitangaza kupitia ukurasa wa twitter mwaka 2017 kuwa nchi hiyo ''haitakubali au kuruhusu'' kundi hilo la watu kuhudumu kwenye jeshi, akieleza ''gharama kubwa za matibabu na usumbufu''.
Mafufuku hiyo ilianza kufanya kazi mwezi Aprili mwaka 2019. Kundi la watu waliobadili jinsia ambao tayari walikuwa wakilitumikia jeshi waliruhusiwa kuendelea lakini wale waliokuwa wakitaka kujiunga walizuiwa.
Rais Biden mara kwa mara alisema kuwa alipanga kuondoa marufuku hiyo. Kabla ya kuapishwa, ujumbe kutoka kwa Ron Klain, kwa sasa ni Katibu Mkuu Kiongozi ndani ya White House, alisema Bw. Biden alipanga kutumia wiki yake yote ya kwanza ''kuboresha masuala ya usawa na kuunga mkono jumuia mbali mbali za rangi na jumuia nyingine zilizoonekana kutotendewa haki''.
Huu ni mfano wa hivi karibuni wa Bwana Biden kutumia maagizo kubatilisha sera za enzi za Trump.
Tayari amesaini maagizo ya kusimamisha ujenzi wa ukuta wa mpaka wa Mexico, kubatilisha marufuku kwa wasafiri kutoka nchi kadhaa zenye Waislamu, na kuzindua mpango wa kuboresha usawa wa rangi.
Haki za watu waliobadili jinsia zilipigiwa upatu mapema na kampeni ya Biden. Yeye ni rais wa kwanza kuonesha kuunga mkono jamii hiyo katika hotuba yake ya ushindi.
Mwezi Novemba, baada ya ushindi wake, kisha Rais mteule Biden alihutubia jamii ya watu waliobadili jinsia, akiandika kwenye ukurasa wa twitter '' Nitawaona, nitawasikiliza, na kuwapambania si tu kwa ajili ya usalama wenu lakini pia hadhi na haki yenu mliyonyang'anywa''.
Kulikuwa na upinzani wa haraka kwa msimamo wa utawala. Siku yake ya kwanza kazini hashtag #BidenErasedWomen ilishika kasi - ingawa baadaye ilitumiwa zaidi na wafuasi wa haki za jinsia.
Rais alikuwa amepitisha amri ya "Kuzuia na Kupambana na Ubaguzi kwa misingi ya utambulisho cha jinsia", ambayo ilisema kwamba makao ya wanawake, riadha za wanawake na huduma za afya hazipaswi kuwabagua wale wanaojitambulisha kama wanawake.
Makundi ya watu wa mapenzi ya jinsia moja wamefurahia kuwa na mtu ambaye amekuwa mstari wa mbele kutetea haki zao White House.
Utawala wa Trump ulikuwa umesema kwamba marufuku - ya kuondoa sera za Rais Obama - kwa kiasi kikubwa ungehusu kuhusu fedha, sio kuhusu haki za binadamu (ingawa utafiti wa Shirika la Rand la 2016 uliowekwa na idara ya ulinzi ulisema kwamba watu wa jinsia tofauti watakuwa na "kiwango kidogo" athari "kwa gharama za huduma ya afya).