JanguKamaJangu
JF-Expert Member
- Feb 7, 2022
- 2,308
- 5,460
“Mvua za Juu ya Wastani hadi Wastani zinatarajiwa katika maeneo ya Kusini mwa Mkoa wa Morogoro, mikoa ya Iringa, Lindi, Mtwara, Singida, Dodoma, kaskazini mwa mkoa wa Katavi, Kigoma na Tabora.
Aidha, mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani zinatarajiwa Kusini mwa Mkoa wa Katavi, mikoa ya Njombe, Rukwa, Songwe, Mbeya na Ruvuma”.
Dkt. Ladislaus Chang’a, Kaimu Mkurugenzi Mkuu TMA na Makamu Mwenyekiti Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabia Nchi (IPCC) amesema athari zinazoweza kujitokeza ni vipindi vya unyevu wa kuzidi kiasi pamoja na mafuriko vinaweza kujitokeza na kuathiri ukuaji wa mazao na miundombinu ya kilimo, vilevile, kina cha maji katika mito na mabwawa kinatarajiwa kuongezeka.
Pia, Dkt. Chang’a ametoa ushauri kwa wadau mbalimbali kuzingatia matumizi endelevu ya uhifadhi wa rasimali maji.
Dkt. Chang’a amefafanua kuwa Msimu wa Vuli kwa miezi ya Oktoba hadi Disemba, 2023 katika maeneo yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka (Mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu, Mara, Manyara, Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Dar es Salaam, Kaskazini mwa Mkoa wa Morogoro, Pwani (ikijumuisha kisiwa cha Mafia) pamoja na Zanzibar (visiwa vya Unguja na Pemba) utabiri wake ulitolewa tarehe 24 Agosti, 2023.
Mvua hizo zimeshaanza katika maeneo ya Ukanda wa Ziwa Victoria, Pwani ya Kaskazini na baadhi ya maeneo ya nyanda za juu Kaskazini mashariki kama ilivyotabiriwa.
Ongezeko la mvua linatarajiwa katika miezi ya Novemba na Disemba, 2023. Vilevile, mvua za nje ya msimu zinatarajiwa katika mwezi Januari na Februari, 2024.