SEHEMU YA KUMI NA SABA
SEHEMU YA KUMI NA SABA
“Acha simba!!!” ikaamrisha sauti kali. Nikapepesa macho ili nijionee ni nani huyo!!
Na hapo akatokea MAMA LAO akiwa na tabasamu usoni na rungu kubwa mkononi!!
Alikuwa anatokwa damu mdomoni lakini hakuwa na kitu kinachoitwa wasiwasi tena, akaanza kutembea zaidi.
Alikuwa anachechemea!!
“Mama lao…” nikajikuta natokwa na sauti yenye kitetemeshi.
“Tuondoke hapa Sam. Wajinga wana mtandao mpana sana hawa. Simama Sam jikaze simama tupotee hapa.” Alinisihi Mama lao, lile jibwa lilibaki kutikisa mkia, bila shaka lilimjua vyema Jojina na mbwa akojuaye….
Hakuna kilichoharibika.
Nikajikaza nikasimama wima, mbwa huyu hakuwa na madhara tena kwangu ilhali Jojina alikuwa amemkaripia tayari.
Nikajikongoja huku nikiyasikia maumivu ya kiuno bado. Lakini ilikuwa heri maumivu haya kuliko kuuwawa kabla sijatimiza azma yangu.
Sikujua kama mwendo wangu ulikuwa mdogo kiasi cha kumkwaza Jojina, hakusema na hata angesema isingesaidia kuniongezea mwendo mgongo ulikuwa unauma sana, na si hivyo tu hata nilipojaribu kukimbia yale maumivu ya kinywa kilichopasuka yalisababisha kichwa kiwe katika maumivu makali sana. Jojina alinitazama kwa huruma huku akizidi kukaza mwendo.
Mara akasimama ghafla kisha akachuchumaa, nikamfikia nikiwa nashangaa.
“Panda mgongoni Sam… panda upesi” aliniamuru, ni kitu ambacho sikukitarajia hata kidogo lakini hakuwa na masihara hata kidogo, akarudia kauli yake safari hii kwa kuamrisha.
Nikajiweka mgongoni, Jojina akasimama kama kifaru akaanza kutimua mbio mimi nikiwa mgongoni. Usiku wa giza tukielekea anapopajua yeye. Niliyafumba macho yangu kukabiliana na uchungu niliokuwa nikiusikia. Kichwa kilikuwa kinauma haswa!! Lakini haukuwa wakati muafaka wa kulalamika.
Mama lao akaendelea kutimua mbio.
“Taksiii….Taksiiii msaada tafadhali mgonjwaaa!!” aliita kwa nguvu baada ya kuziona taksi kadhaa zikiwa zimeegeshwa.
Dereva moja akawahi upesi akaufungua mlango wa teksi yake. Hapo sasa nilikuwa nimefumbua macho nikishuhudia filamu hii ya aina yake.
“Tupeleke Stendi ya mabasi…” aliamuru Jojina na hapo nilikuwa siti ya nyuma na yeye akiwa pembeni yangu.
Dereva alibaki kuduwaa ni kama hakuwa akiamini kama tulikuwa na pesa ya kumlipa, Jojina akaling’amua hilo, upesi akajipekua na kutona na noti nyekundu akamlipa dereva.
Akatia gari moto tukatoweka…njia haikuwa mbaya sana hivyo wakati huu nilipata fursa ya kutambua kuwa kinywa kilipasuka japo si vibaya sana lakini shingo ilikuwa inauma sana bila shaka yule bwana aliyenipiga mateke.
Stendi haikuwa mbali, tukapewa pesa yetu iliyosalia na kutelemka, wakati huu nikijikongoja mwenyewe. Kila kitu katika suala la maamuzi nikamuachia Jojina maana walau yeye alikuwa na unafuu.
Sikujua alikuwa na maana gani usiku mnene kama ule kuamua safari ya kuja stendi lakini hakuniacha niumie akili kutafakari sana, mara akaita teksi nyingine.
“Tupeleke Gangilonga” akatajiwa bei akalipa.
Ukimya ukatawala kwa takribani dakika kumi na tano. Tukatelemka mahali ambao Jojina aliamua yeye.
Teksi ilipoondoka tukatembea kwa mwendo wa miguu hadi katika nyumba kubwa kiasi iliyozungukwa na majani mengi, bila shaka ni kutokana na watu kutoishi eneo lile kwa muda mrefu.
Jojina alivyofika pale geti lilikuwa limefungwa na hakushtuka ni kama kitu alichokitarajia.
Akachumpa ukutani akatua upande wa pili. Kisha akafungua geti dogo na kuniruhusu niingie ndani.
“Miezi sita sijakanyaga hapa aisee.” Alisema neno la kwanza tangu tufike pale. Sikuchangia chochote.
Akaniongoza hadi ndani, uzuri wa Iringa hakuna vumbi kali sana, badala yake vipindi vya baridi huchukua nafasi kubwa zaidi hivyo hapakuwa na madhara ya vumbi.
“Hapa hakuna umeme wala nini Sam.” Alizungumza tena, nikamuunga mkono kwa kumweleza kuwa hilo si tatizo cha muhimu usalama wetu.
Akapapasa huku na kule akaibuka na mshumaa, kisha akavuta kumbukumbu na kupapasa sehemu nyingine akaibuka na kiberiti na kisha kutengeneza mwanga hatimaye.
Nikaketi naye akaketi katika makochi chakavu yaliyokuwa pale ndani.
“Baba yangu alikufa maskini lakini walau alijenga kibanda hiki kwa taabu.” Akaanzia hapo, hili halikunigusa sana. Nilitamani kusikia juu ya namna tulivyoweza kuokoka.
Nikaamua kumuuliza.
Akatabasamu kidogo kisha akaketi vyema!!
“Sam, yaani japokuwa huwa siendi katika nyumba za ibada hata miezi sita ama mwaka lakini nimeamini kuwa Mungu huwa hamtupi mja wake…. Lakini najiuliza iwapo nami ama sisi ni waja wake. Maana nikiwa katika kile chumba changu nikaisikia sauti ya baba mwenye nyumba ikilalamika, na kuna watu walikuwa wakitoa karipio. Nikasitisha nilichokuwa nafanya, simu yangu nilikuwa nimeweka katika chaji. Nikainyofoa kwanza nikaiweka katika mkoba wangu. Nikatuliza akili, mara nikaona mwanga wa gari. Mwenye nyumba wangu hana gari, nikajishtukia na kuheshimu machale yangu kuwa hapa mambo yanaanza kuharibika, nikapitia dirishani mbiombio nikakimbia hadi nyuma ya nyumba ambapo sauti hizo zilikuwa zinatokea. Nikasikia wakimuuliza juu yangu iwapo nimerudi, kisha wakamuuliza iwapo amewahi kuniona na mgeni. Nikasikia wakimuuliza iwapo anaifahamu sura fulani katika picha ambayo najua tu ni yako hakuna mwingine. Mwenye nyumba akakiri kuwa nilikuwa nimerejea tayari. Lakini hakukubali kiwepesiwepesi badala yake walimpa kipigo kwanza nd’o akalainika.
Alipokubali kuwaongoza kuja upande wa kile chumba changu na stoo pia ndipo nikashtuka na kuja mbiombio upande ule, nikakuita hukuitika, nikawasha tochi nd’o pale ukanipa ile bahasha!!! Wajinga wakavamia pale mimi haraka nikadidimia chini.
Sam niliumia sana nilipowashuhudia wakikupa kipigo kiasi kile, bahati nzuri ndani ya chumba changu tofauti na simu nilichukua pia kile kirungu changu cha mgambo si nilikwambia nilipita huko, kiukweli hicho kirungu niliwadhulumu.
Nikajiuliza sasa mimi na kirungu nitakusaidia kitu gani mie. Wakakutukana matusi mazito, nikatamani kukimbia lakini ningeweza vipi kukuacha ufe hivihivi.
Nikatamani kupiga kelele lalini mwenzangu we, sisi wahehe ni waoga sio siri, yaani unaweza kupiga kelele asitokee hata mtu mmoja sasa hapo ni kipi kama si kujitafutia kufa burebure.
Nikataka kuwakabili kwa kirungu lakini kweli wanaume wanne kwa kirungu kimoja, si matusi hayo!!
Nikajikuta naketi chini, na hapo nikakumbuka jambo la muhimu kupita yote na siajui tu niliwaza vipi kuhusu mbwa wa kufugwa wa baba mwenye nyumba. Yule mbwa huwa hana masihara, baba mwenye nyumba alipewa na wazungu fulani hivi rafiki zake. Nikavamia banda nikalifungua, uzuri ananitambua yule mbwa!!
Nikamvuta hadi nyuma ya nyuma, ghafla nakutana na wanaume wawili kati ya wanne nikatambua kuwa kazi sasa imeanza.
Nikamwachia mbwa akala sahani moja na bwana mmoja halafu mimi na kirungu dhidi ya mwanaume asiyekuwa na silaha, Sam nilimrukia, akanipiga teke mbavuni yule bwege, nikajikaza nikafyatuka na rungu nikalituliza hapa (akagusa utosi wake) jamaa akalainika bila kupiga kelele, chini!!. Ile nageuka namkuta mwenzake akitapatapa pale chini damu inamruka, nikammulika nikahisia kuwa uhai ulikuwa unafanya urafiki naye. Nikamrukia kwa ghadhabu, kabla sijamfikia nikajikwaa nikaanguka chini, nilipoamka hasira zote kwa yule bwana, na yeye nikamtandika rungu kwenye paji la uso. Bila shaka kajifia yule we tungoje taarifa ya habari tu. Kuja kusimama wima tena simwoni mbwa. Nikataka kumwita kwa sauti ya juu lakini nikahofia usalama maana nilitambua fika kuwa wale wanaume wawili wapo bado kule mbele. Nikaanza kunyata taratibu gizani ili nitambua kulikoni, nd’o hapo nikaisikia sauti ya baba mwenye nyumba ikimwamrisha mbwa kushambulia!! Walau amani ikarejea japo niliendelea kunyata, hadi wakati nafanikiwa kufika ndipo namuona yule mbwa akitaka kukushambulia nikamzuia…Sam Mungu ametupangia jambo fulani amini!! Hili tukio halikuwa la kuokoka kirahisi namna hiyo hata kidogo.” Jojina alimaliza na kushusha pumzi kwa nguvu, nami nikashusha pia kama tuliambizana kufanya vile kwa pamoja.
“Sam nadhani tunatakiwa kupumzika halafu kesho twende Makanyagio. Lazima tuanzie huko.”
“Makanyagio? Nd’o wapi huko??”
“Kweli wewe mgeni Iringa nimeamini. Huko ni sehemu maarufu sana kuna makaburi kule, kama unakisikia chuo cha Mkwawa basi ndo kuelekea hukohuko.” Alimaliza kisha akasimama, lakini mimi sikuwa na usingizi. Jojina akaleta godoro la pamba ambalo lilikuwa linatoa harufu ya uvundo akalitandika pale sebuleni.
“Tutalala hapa maana huko chumbani hapalaliki kuna harufu sana.”
“Popote tunalala Jojina.” Nilimuunga mkono.
Akajitupa na baada ya muda alikuwa anakoroma, nilijaribu kujilazimisha kulala lakini hata usingizi haukujileta jirani nami.
Nikapata wazo la kujishughulisha na bahasha na yaliyomo.
Maana swali juu ya hawa watu walikuwa wanatafuta nini na mbona wameacha ile bahasha lilikuwa linanisumbua.
Nikaichukua bahasha kutoka katika kiti alichokuwa ameketi Jojina.
Nikashtuka na mapigo yangu ya moyo yakaongeza mwendo kasi. Bahasha ilikuwa nyepesi sana tofauti na ilivyokuwa awali wakati inabeba picha na makorokoro mengineyo.
Nikaanza kutetemeka nikiamini kuwa ule ushahidi nilioupigania kwa muda mrefu umetoweka, nikaingiza kwa uoga mkono ndani ya ile bahasha. Hapakuwa na makaratasi mengi sana.bali karatasi moja tu!!
Nikalichomoa upesi. Lilikuwa karatasi tofauti kabisa na yale ambayo yalikuwa ndani ya bahasha ile awali.
Nilianza kumwamsha Jojina awe shahidi lakini bahati mbaya hakunisikia hata kidogoa alikuwa amezama katika dimbwi la usingizi.
Nilijaribu kuiweka akili sawa labda si bahasha ninayoitazamia, lakini ilikuwa ni ile na sasa haikuwa na kitu ndani yake.
Nikafungua ile karatasi kwa makini nitambue kama nayo ni moja kati ya zile za awali lakini hapana hii ilikuwa tofauti.
Nikajongea katika mshumaa, nikaanza kuisoma.
Hofu ikatanda maradufu, ulikuwa mwandiko wa kike.
“Sam kama huu ujumbe utakufikia sam, fanya kila uwezalo uniokoe Sam. Nimefanya kila jitihada nijitoe katika mikono ya watu hawa lakini jitihada zimegonga mwamba. Nakuandikia ujumbe huu nikiwa nimekata tamaa kabisa ya maisha na sina uhakika kama utaupata ujumbe huu, Sam yanayotokea huku hayasimuliki hata kidogo kwa maandishi, ninayoyashuhudia huku nilipo ni mazito mimi na wewe hatuyawezi bila msaada wa watu wengine, lakini hao watu wengine ambao nawasema wote wapo katika upande wa watu hawa. Sam kama ukiona ni ngumu sana kuniokoa, amini kuwa nimeridhia kufa. Wewe funga safari ondoka katika nchi hii, nenda mbali Sam maana ukiingia huku hautatoka Sam. Jiondokee uende mbali labda utapata msaada kutoka kwa watu wengine huko wasiokuwa wenyeji wa ardhi hii.
Natamani sana walau ningejua huku nilipo ni wapi lakini bahati mbaya sina hata kitu kimoja cha kufananisha ene3o hili. Na bora ningekuwa natulia sehemu moja, hawa jamaa wananihamisha kila leo. Nimeuza utu wangu Sam na nimeshiriki penzi na huyu bwana ambaye kama ni mkweli atakufikishia ujumbe huu, ameshindwa kabisa kunivujishia siri za humu lakini amesema kuwa hapendezwi na mambo ya humo na atakushirikisha. Nimeamua kumwamini kwa sababu sina namna na hata nisipomwamini mimi ni wa kufa tu Sam wangu!!! Sama kama itakuwa sawa naomba umsikilize huyu bwana, macho yake hayadanganyi hata kidogo, na laiti kama pasingekuwa na vifaa vya kurekodia humu ndani angeweza kunieleza jambo nami nikakuandikia.
Samahani kwa mwandiko huu mbaya, nimeyaandika haya nikiwa katika giza, narudia tena kama huyu bwana ni mkweli basi alifanya hila ya kuzima taa na kuzuia kamera kuweza kunirekodi, nikafanikiwa kukuandikia haya.
Sam, kama sitafanikiwa kupona nifikishie salamu hizi kwa mama yangu mwambie nampenda sana, pia mwambie mzee Matata katika maisha yake ajifunze kumsikiliztu kabla hyajaamua kumuhukumu. Hii itasaidia kuokoa wengi.
Akupendaye!!!