Makapuku Forum

Makapuku Forum

Wanamuita Iron Lady. Alikuwa ni kiongozi wa shoka sana. Alikuwa na urafiki wa karibu na Rais wa Marekani wa wakati huo, Ronald Regan.

Waziri mkuu mpya wa Uingereza ni mwanamke.
Hivyo ni mwanamke wa pili kushika wadhifa huo baada ya Magreth Thatcher
Hii ndio sababu naamini kuwa Trump atakaa USA maana sidhani kama inawezekana na wao wakamuweka Clinton
 
fb5c805386af5403b372cdf5dc3fc53f.jpg
 
NUKUU NO 1# Sote tunajua kwamba Africa si Ufaransa, Uingereza,Marekani au Urusi. Tunajua shabaha ya nchi za magharibi. Jana walitugawa katika ngazi makabila yetu, koo na vijiji kwa kweli wamekuwa wakirenga kutugawa kwa mbinu ya kuibua makundi ya kiuadui miongoni mwetu. Haya yalisemwa na aliyekuwa waziri mkuu wa Congo -Leopoldville(sasa jamuhuli ya kidemokrasia ya Congo DRC),Patrice Emery Lumumba, katika hotuba yake ya Agosti 25,1960, Patrice Lumumba alizaliwa Julai 2,1925 na kuuawawa January 17,1961
Hichi ndicho kilichosababisha nchi za magharibi zikamwondoa kupitia kuku.
 
NUKUU NO 2#; Inawezekana kabisa, nani kweli kwamba jogoo ndiye anayewika, lakini vile vile ni tembe (kuku jike) ndiye anayetaga mayai. Haya yalisemwa na Margaret Hilda Thatcher, aliyezaliwa Oct 13,1925 na kufariki Dunia April 8,2013. Thatcher anatajwa kama kuwa mmoja wa viongozi mashuhuri uingereza akishika wadhifa wa waziri mkuu kuanzia mwaka 1979 hadi mwaka 1990 na kuweka record ya mwanamke pekee kushika wadhifa huo katika nchi hiyo yenye muunganiko wa mataifa manne. Alikuwa kiongozi wa Chama cha conservative mwaka 1975 hadi 1990. Ndiye waziri mkuu aliyekaa kwa muda mrefu zaidi uingereza
Leo ameingia mwanamke mwingine bibi May.
 
SEHEMU YA SITA
OBOBO aliendelea kumfuatilia Cheupe mpaka katika lodge ya Kenya na kumwona akiingia ndani na kijana Yule, akasimama kwa nukta kadhaa kisha akaielekea kaunta na kuagiza kinywaji akijipanga kuendelea kumsubiri hapo nje, ‘nitamkamata tu’ akawaza huku akipokea inywaji chake kutoka kwa mhudumu wa kaunta. Obobo aliapa kumtia mkononi Cheupe ili amfunge mdomo na kujijengea usalama wake katika kazi yake hiyo. Alisubiri pale kaunta kama saa nzima hivi lakini hakumuona Cheupe wala anayefanana naye kutoka ndani ya nyumba ile, ‘atatoka tu,’ akajipa moyo na kuendelea kupiga kinywaji taratibu.
† † †
Jasmine alimwona Kamanda alivyoingia na Cheupe, kama walivyojipanga, aliendelea kutulia palepale alipokuwa ameketi na mara hiyo akamwona mtu mmoja mweusi mwenye tambo kubwa akiingia na kushangaa shngaa nguo aliyovaa ndiyo ile ailyoambiwa na wale jamaa wa bodaboda.
“Shiit” akang’aka peke yake huku akinyanyuka kuelekea ndani maana alijua wazi kuwa akichelewa tu kukamilisha kazi yao basi lazima litatokea timbwili katika eneo hilo. Akainuka na kwenda kaunta ambako alilipia huku akimgonga Yule jamaa makusudi na kugundua kuwa ana bastola upande wake wa kulia. Akatoka na kuelekea ndani ya ile loji na kumwona Kamanda na Cheupe wakipeana mabusu pale mlangoni.
† † †
Obobo akamwona Cheupe akitoka huku akitembea harakaharaka katika maegesho ya magari, akateremka taratibu kutoka pale alipoketi na kuacha noti ya 5000 akapotelea kizani kumsaka mwanadada huyo. Alisimama kwenye nguzo ya umeme na kutazama huku na kule akamwona Cheupe akiivuka barabara kwenda upande wa pili, Obobo naye akavuka n akutembea kando kando ya ile barabara kama mita mia mbili nyuma ya Cheupe hukiu akijaribu kujificha chini ya vibaraza vya nyumba kusudi asionekane na watu kama anamfuatilia binti huyo.
Cheupe aliendelea kutembea haraka haraka huku akiangalia nyuma mara kwa mara, mara moija alipoangalia nyuma akakutana uso na Obobo, akamtambua mtu huyo kwa haraka kiuwa sio mwema kwake, akaanza nusu kukimbia na nusu kutembea. Obobo hakumwacha aliongeza tu ukubwa wa hatua na kumfuata, cheupe alizidi kuongeza kasi huku akitazama nyuma na kuona Yule mtu akizidi kumkaribi. Cheupe akapita mtaa wenye maduka mengi na kutokea ule wa wauza mitumba unaoelekea ofisi za CCM. Watu wakawa wakimshangaa msichana huyo, wengine walimjua na wengine hawakumjua ila kwa mavazi yake walimtumbulia macho.
Muda huo wauza mitumba wengi walikuwa wamekwishafunga biashara zao na wachache walibaki wakimalizia huku vijiwe vya kahawa navyo tayari vilianza kukusanya watu.
“Jamani mwizi! Mwizi huyo!” Cheupe alianza kupi9ga kelele na watu wakaanza kuangaza huku n huku.
“We mwanamke huyo mwizi yuko wapi?” vijana wakaanza kuuliza.
“Huyo nyuma, Yule pale anataka kunipora tangu nilikotoka,” akaeleza.
Obobo alipoona Cheupe anahojiwa na wale vijana akatulia na kujificha nyuma ya gari moja iliyoegeshwa mahala hapo. Mara wale vijana wakamjia na kumzunguka huku wakimwuliza maswali ambayo mwenzao alikuwa hayaelewi. Vurugu ikaanza, Obobo hakuvumilia akachomoa bastola yake na kupiga hewani wale vijana wa katawanyika.
“Ana bundukiii, ana bundukiii, jambazi huyo,” wakapiga kelele.
Mtaa mzima ukawa mshikemshike, Obobo alipopata upenyo akawatoka wale vijana ambao bado walikuwa wakimwandama.
“Paaaaahhh!” risasi moja ilisikika na mmoja wa vijana wale akaanguka vibaya barabarani akivujwa na damu.
“Mamaaaa! kaua huyo, jambazi hilo,” wakaendelea kupiga kelele wakati huo Obobo akapenya hapa na pale na kutokea barabara kubwa karibu na Viwanja vya Nyerere, akaipachika bastola mahala pake kisha akatulia akiangaza macho huku na kule ili amwone Cheupe.
‘Amenipotea,’ akajisemea moyoni huku akijiondoa eneo lile na kuifuata barabara kubwa kuelekea Chako ni Chako. Alivuka barabara mbili tatu za mitaa na kukaribia baa hiyo iliyokuwa imesheheni watu muda huo. Akapunguza mwendo na kusimama mahala Fulani akiangalia kutoka mbali kama atamuona Cheupe lakini hakumwon. Alichokiamua ni kwenda kwenye ile baa, akajipenyeza na kumkamata mhudumu mmoja kumwuliza wapi anapoisshi cheupe.
“Ametoka bado hajarudi, kama una shida naye msubiri,” Yule mhudumu akajibu huku akiondoka na kuendelea na shighuli zake zingine kabisa. Obobo akaketi kitini na kuagiza kinywaji baridi na kulipoza koo lake.
DODOMA CARNIVOLE
SAA NNE usiku ndani ya baa kubwa ya Dodoma Carnivole, muziki mzito ulikuwa ukikita kwenye spika kubwa za kisasa na kufanya watu wa rika tofauti kupata burudani katika eneo hilo. Lakini wale wenye pesa zo kubwakubwa walipewa mahala pao pa ukimya ili kuweza kujadili mambo yao bila kuingiliwa na mtu yeyote.
Ndani ya chumba kimoja kilichobandikwa neno V.I.P kwa maandishi yaliyojinyonganyonga kulikuwamo watu wawili walioketi huku na kule, juu ya meza iliyowatenganisha kulikuwa na makabrasha kadhaa na huku katika vijimeza vidogodogo kila upande kulikuwa na chupa kubwa kubwa za pombe kali ambazo wawili hao walikuwa wakijimiminia matumboni mwao kila mmoja kwa uwezo wake.
“Tumepoteza,” Segereatumbo aliongea mara tu alipoikita bilauri yake iliyokaukiwa kinywaji juu ya ile meza ndogo.
Mheshimiwa Kibanio bado alikuwa akipiga funda lake ambalo ndio kwanza alikuwa akifungua koo baada ya kugonga cheers na swahiba wake huyo.
“Lakini we inakuingia akilini Msesema jinsi alivyokufa?” Kibanio akauliza huku akiitua bilauri yake.
“Ajali haina kinga mheshimiwa, yote yanawezekana,” Segeratumbo akajibu kisha ukimya ukachukua nafasi yake.
“Sikia mimi nina wasiwasi hiki kifo si cha kawaida,” Segeratumbo akaongeza kusema, “Unajua kwa nini nimekuita hapa?”
“Sijui!”
“Usiku huu nimevamiwa, nimevamiwa na lijitu, pande la mwanaume, nikiwa na shemeji yako Mwanahawa. Lile jitu likapora mkoba wangu wa kazini na kutokomea,” akaeleza.
“What? Segeratumbo, ni kweli?” Kibanio akang’aka, kisha akatulia na kufikiria jambo, “Tuna wabaya wengi sana,” akaongea kwa upole.
“Ndiyo, wameshaona wanaumbuka,”
“Segeratumbo!” KIbanio akaongea kwa sauti ya chini.
“Sikiliza Kibanio. Polisi walikuja nikawaelekeza alivyo mtu huyo wakamchora vilevile, na sasa wanashughulikia hiyo ishu. Mkoba wangu baada ya kuona alichokitaka hakipo akautupa nje kwenye maua,” Segeratumbo akaleza.
“Mzee Sege, hapa ni kukaa mkao wa kula bila ulinzi hatuwezi kuishi, hata mimi itabidi nihamishe kabrasha zangu. Kumbeeee!” Kibanio alipigwa na butwaa kwa habari hiyo.
“Na kama kauawa basi muuaji ni profesheno,”
“Ndiyo, lakini tutapataje uhakika wa hili? Inabidi tufuatilie,” Segeratumbo akashauri.
“Sijakuelewa kiongozi,” Kibanio akaonesha shaka.
“Tujiwekee ulinzi, ikiwezekana tufanye juu chini huyu jamaa akamatwe,” Segeratumbo akasema.
“Nimekupata, lakini swala si liko polisi? Atanyooshwa tu,” Kibanio akajibu huku akimimina kinywaji kwenye ile bilauri ambayo sasa ilikwishakauka.
“Kibanio, kumbuka adui yetu atakuwa amekodi mtu makini kufanikisha lengo lake, na sisi tutafute mtu makini katika kuhakikisha ukweli huu unajulikana,” Segeratumbo akaeleza.
“Sawa naungana mkono na wewe”.
Baada ya saa tatu kupita wakiwa palepale wakamaliza mazungumzo yao na kukubaliana kwa sauti moja kuimarisha ngome yao dhidi ya wahujumu uchumi ndani ya serikali. Pamoja na hilo waliona wazi kuwa vita hiyo siyo ndogo ni kubwa hivyo wakaamua kujipanga kwa nguvu zote.
§§§§
Nje ya Kenya lodge Amata alisimama kimya akimwangalia Jasmine akiwapa maelekezo haya nay ale wale askari polisi aliokuwa nao hapo nje, alipomaliza akarudi kwa Amata.
“Vipi mbona umeduwaa?” akamwuliza.
“Nilikuwa nakuangalia Master Plan unavyopanga majeshi,” akamjibu kwa utani.
“Ok, sasa nini kinafuata? Kumbuka mimi kazi yangu nimeimaliza tayari, si ajabu kesho nakuacha sina jipya hapa,” Dkt. Jasmine alimwambia Amata.
“Mh! Ndiyo ndiyo umemaliza, mimi bado inabidi nishughulikie hili swala kwa undani zaidi ili likamilike mapema,” Amata alieleza huku akitoka eneo lile na mkono mmoja kamshika Jasmine.
“Lakini we unalionaje?”
“Haliko sawa kiukweli, kuna watu nitahitaji kuonana nao kwa siri, unajua katika uchunguzi wangu nimegundua kuwa marehemu alikuwa na swahiba zake wengine wawili na hili nimelipata kwenye kumbukumbu zake, ameeleza mambo mengi sana juu ya sakata lao hili, nataka nijue kama ni chanzo kabisa au kuna linguine,” akamwambia Jasmine.
“Sasa usiku huu, tunaenda kuumalizia wapi?” Jasmine akauliza huku akiweka vizuri mkufu wake wa dhahabu uliokuwa ukining’inia shingoni mwake.
“We unataka wapi? Ila kumbuka kazi hii bado mbichi na time is tissue,” akamwambia huku akisimamisha tax na wote wawili wakaingia.
“Chako ni Chako tafadhali,” Amata akamwambia dereva.
“Shiiiiit!” Jasmine akang’aka, “Kuna nini huko Chako ni Chako?” akaongeza swali.
“Nyama, kuna nyama sana pale mpenzi,” akamwambia huku dereva akiondoa ile gari na kukata mitaa kuelekea huko atakako Amata.
“Pale ndo pazuri shemeji!” Yule dereva akadakia mazungumzo.
“Si unasikia!” Amata akaongeza, “Sisi wageni bwana hapa hatujui moja wala mbili, ila mji wenu mtulivu sana,” akaongeza maneno.
“Aaaaa hivo hivo tu braza, tunakomaa kibishi, utulivu zero ijapokuwa ndio makao makuu ya nchi,” akajibu Yule dereva.
“Kwa nini unasema hivyo wakati watu tumekuja kula likizo huku?” Jasmine akaendeleza mazungumzo.
“Jana tu hapa mwenzetu kaibiwa gari yake mpya kabisa, alikuwa kampeleka mteja hoteli ya Bahi kufumba na kufumbua gari haioni,” Yule dereva akaeleza kwa kirefu mkasa huo.
“Kwa hiyo hiyo gari imeokotwa wapi umesema?” Amata akauliza.
“Imeokotwa huko Chuo cha Mipango, ila haijaharibika wala nini, iko safi kabisa, inaonekana aliyeichukua alikuwa na mambo yake tu. Itakuwa ni majambazi,” Yule dereva akaeleza huku akiwa anaegesha gari yake katika baa hiyo maarufu mjini Dodoma.
“Asante sana kijana,” akamshukuru wakati Jasmine akaimlipa Yule kijana pesa yake.
“Vipi niwafwate baade au?” akauliza.
“Ndiyo, nipe namba yako nitakupigia,”
Kamanda Amata akachukua namba ya Yule kijana na kuvuka barabara akiwa kamshika mkono Jasmine na kuingia katika eneo la baa hiyo. Hakukuwa na watu wengi sana siku hiyo lakini hali hiyo ilitokana na muda kuwa umekwenda sana, wakachagua meza moja na kuketi.
“Yule binti anakaa geto moja hapa ndani,” akamwambia Jasmine.
Wakiwa wanaendelea kupata kinywaji hiki na kile, hali isiyo ya kawaida ikaonekana katika eneo lile. Wahudumu wa baa walikuwa wakiingia na kutoka katika mlango wa kuelekea uani ambako kuna mageto ya madada poa.
“Jasmine!” Amata akaita kwa sauti ya upole huku akiinuka taratibu na kuelekea kule wanakoingia wale wahudumu. Baada ya kuuvuka ule mlango alikutana na hali ya taharuki, wale wahudumu wengine walikuwa wakilia na kwenda huku na kule, malngo waliokuwa wakipishaa ulikuwa ni ule wa Cheupe.
“Kuna nini huko?” akamuuliza mmoja wa wahudumu.
“Wamemuua, kaka, wamemuaa,” Yule mhudumu alikuwa akilia huku akimpita Amata bila kumwangalia. Kamanda Amata, akawaondoa wale wahudumu pale mlangoni na kujitoma ndani ya chumba hicho.
Mwili wa Cheupe ulikuwa umetulia kitandani, pochi yake ikiwa pembeni shaghala baghala, akakiendea kitanda na kumtazama Cheupe, akamshika shingoni, shavuni, akaingiza mkono tumboni. Sekunde hiyo hiyo Dkt. Jasmine akaingia ndani ya chumba hicho na kumkuta Kamanda katika hali hiyo.
“Vipi Kamanda?” akauliza na wakati huo tayari akakifikia kile kitanda, akamshika Cheupe shingoni kama vile vile alivyofanya Amata, akageuka na kumtazama Kamanda usoni, wakagongana macho.
“Hajafa!” Jasmine akamwambia Amata, wakati huo akiwa kaukamata mkono wa kushoto wa Cheupe na kauminywa kwa nguvu kwenye kiungo cha kiganja kwa kidole gumba chake.
“Tumwahishe hospitali,” Amata akatoa wazo na wakati huo tayari akamnyanyua Cheupe kwa mikono yake miwili yenye nguvu na kutoka naye nje.
“Jamani kesi hiyo, sasa unampeleka wapi?” mmoja wa wahudumu akaongea kwa sauti.
“Kweli jamani subirini polisi,” mwingine akadakia. Hakuna aliyewasikiliza, Amata na Jasmine wakachukua tax nje ya baa hiyo na moja kwa moja wakamfikisha katika hospitali ya mkoa. Wakafika mapokezi na Jasmine hakuuliza, alimvuta mkono muuguzi aliyemkuta kazubaa maeneo hayo.
“Lete drip na vifaa vyake haraka, haraka sana,” alipompa mari huyo akamkamata mwingine, “Nioneshe wodi ya V.I.P haraka haraka!” Jasmine alitembeza amri kana kwamba yeye ndiye mfawidhi wa hospitali hiyo. Alipooneshwa chumba hicho wakamlaza Cheupe nay eye mwenyewe akaanza kumhudumia kwa hili na lile huku akimkagua kama kuna aina yeyote ya majeruhi ndipo alipogundua kuwa Cheupe alipata pigo baya kwenye maeneo ya nyuma ya shingo na kumpelekea kupoteza fahamu.
“Vipi atapona?” Amata akauliza.
“Yeah! Atapona lakini tunahitaji kufanya kazi ya ziada kwelikweli, inaonekana mshambuliaji alishambulia kichwa kwa madhumuni ya kuua kwa kumvunja shingo upande wa nyuma lakini Mungu mkubwa ila kwa pigo hilo, usipokufa utapoteza fahamu, we mwenyewe unaju,” jasmine akaeleza.
“Ok, nini kinafuata?” akauliza Amata ambaye.
“Hapa ni kupata Philadelphia Collar na anatakiwa asijitikise, alale kwa utulivu kabisa,” Jsmine akaeleza huku akiwa tayari kamweka vizuri Cheupe na sasa walikuwa wanatazamana kwa macho.
“Waoh! Ameamka! Asante Mungu,” Amata akashukuru. Cheupe alionekana kupepesa macho lakini kila mara alikuwa akikunja sura kuonesha maumivu makali ya shingo.
“Lete sindano na diclofenac,” akamwamuru muuguzi aliyekuwa jirani, sekunde kadhaa tu tayari ilikuwa imefika na jasmine aliitumia kumpunguzia maumivu.
Baada ya dakika thelathini za kashi-kashi Cheupe alikuwa tayari katulia kimya na Philadelphia Collar yake shingoni. Jasmine akachukua kadi kubwa iliyoletwa hapo na kuandika kila alilofanya na hali aliyomuacha nayo mgonjwa, pia akaandika matibabu yote anayotakiwa kupata.
“Unaitwa nani?” akamwuliza muuguzi Yule aliyekuwa akimsumbua.
“Kashinde!”
“Ok, sikia Kashinde, sitaki mtu yeyote aingie humu ndani isipokuwa wewe tu, hata akija bosi wako, hata Waziri wa Afya, mwambie ni ‘order’,” Jasmine akamweleza huku akimkazia macho kiasi kwamba Kashinde alikuwa akishindwa kustahimili.
“Samahani, nikiulizwa ninyi ni nani nisemeje? Maana mmekuja tu na kujichukulia majukumu wenyewe,” Kashinde akauliza kwa woga.
“Oh! Nilisahau, jibu hili utampa boss wako tu, mwambie ni amri kutoka kwa daktari maalumu wa Ikulu,” akamwambia huku akimkabidhi ile kadi, akachukua pochi yake na kutoa shilingi elfu thelathini.
“Shika hii, kwa lolote likihitajika na hapa kama hamna, utatumia pesa hiyo, kama kuna shida nipigie,” akamkabidhi na kadi yake ya kibiashara iliyomtambulisha kwa jina la bandia isipokuwa taaluma sahihi.
“Ok, asante,” Kashinde akajibu.
Amata na Jasmine wakaondoka katika lile eneo na kutokomea.
“Wapi sasa?” akauliza Amata.
“Hotelini kwako, sijapumzika, na nimekuja hivi unionavyo,” Jasmine akajibu.
“Ok”.
§§§§
Baada ya kumaliza kazi ile Obobo hakwenda mbali, alirudi kwa wateja na kuendelea kunywa bia yake akisubiri matokeo ajue nini kinajiri. Aliziona heka heka zote mpaka mwisho. Alipomwona Cheupe akitolewa ndani kabebwa na Amata, macho yakamtoka pima. ‘Hajafa au?’ akajiuliza na kushuka pale alipokuwa kisha akaifuatilia ile tax ya akina Amata mpaka kule hospitali. Kabla hajafanya dhara lolote aliichukua simu yake na kuwataarifu wateja wake juu ya hali hiyo.
“Kama unaona ana madhara nyonga tu,” akajibiwa hivyo. Akaiweka simu yake mfukoni na kuelekea mlango wa kuingia ndani ya jengo lile lakini walinzi walimzuia kuwa muda wa kuona wagonjwa ulishapita; hakupenda kuleta vurugu, alitoka na kutazama majengo yale yalivyojipanga. Kwa haraka akazunguka nyuma na kujiweka dirishani akisikiliza mazungumzo yote ya mle ndani mpaka walipoagana na Kashinde na kuondoka. Obobo alisimama kwa muda kisha akaondoka eneo lile baada ya kusikia michakacho ya miguu ya watu. Akafika mbele kabisa ya lile jengo na kuwaona Amata na Jasmine wakiondoka.
“Shiit! Yupi anatakiwa afe kwanza?” akajiuliza kwa sauti kisha akainua simu yake kwa mara nyingine na kuomba kuonana na wateja wake haraka iwezekanavyo.
KIKUYU RESORT
OBOBO alikutana uso kwa nuso na wateja wake lakini mmoja wao hakuwamo. Mheshimiwa Matata alikuwa na Kagosho katika kikao hicho cha dharula.
“Ndiyo Bacteria tupe taarifa,” Matata alianza.
“Maana kutuita huku lazima kuna jambo na sio jepesi,” Kagosho akaongeza.
“Ndiyo kwa sababu tulishapanga tusionane mpaka kazi itakapokamilika, ila imebidi kwa kuwa kuna jambo zito na sio kidogo. Nilikuwa nimepanga kumaliza kazi yenu ndani ya siku tatu hadi tano lakini sasa naona kazi inakuwa ngumu kuliko mpango wa mkataba wetu,” Obobo akaeleza kwa kiingereza safi kabisa cha Uingereza.
“Nini kipya?”
“Kwanza kabisa nimegundua kuwa Yule mwanamke aliyekuwa na Msesema atakuwa mwiba mkali katika mpango huu, nikapanga nimwondoe kimyakimya, lakini bahati mbaya katika shambulio lile la ghafla nimegundua kuna watu wawili mmoja mwanaume na mmoja mwanamke wanafuatilia kwa karibu yendo hizi. Sasa inawezekana serikali yenu imetuma wachunguzi juu ya hili,” akaeleza.
Kagosho na Matata wakatazamana.
“Mh! hatuna taarifa kwa maana zaidi ya polisi wa hapa ambao najua kwa upeo wao hawawezi kujua kinachoendelea sidhani kama kuna wengine,” Matata akajibu.
“Any way, ngoja tulifuatilie usiku huu tutakujulisha. Lakini hawa vijana wa hapa aaaaa wasikusumbue wao watachunguza ajali basi,”
“Ni angalisho maana kama kuna watu wanachunguza hili ujue kazi inaongezeka so na malipo yatabadilika,” Obobo akawaambia.
“Hakuna shaka, sisi tunachotaka hapa ni kupoteza hili swala,” Kagosho akaongeza wakati huo Mheshimiwa Matata alikuwa katulia kimya kama akiwaza jambo, mara akainua uso na kumtazama Obobo.
“Uko sawa,” akamwambia na kumtazama Kagosho, “Kijana yuko sawa, jana nimemwona mtu ambaye nimemtilia wasiwasi. Yeye yuko idara ya Usalama wa Taifa lakini atakuja kuchunguza haya kweli?” akawaeleza na kuuliza.
Ukimya ukachukua nafasi kati yao.
“Wako wawili, hii kazi itakuwa ngumu sana kwa sababu ya hawa sasa sijui nianze na nani?” Obobo alieleza kwa kuwa alijikuta njia panda.
“Kill them all, kwa njia unazoona zinafaa,” Matata akamwambia Obobo. Mara mlango ukafunguliwa bila hodi na kila mtu akashtuka na kujiweka sawa.
“Vipi mbona mnaogopa?” Mheshimiwa Nnandi aliingia na kuwaambia.
“Nnandi nipe taarifa maana upo kitengo muhimu,” Matata akamwambia pindi tu alipojiweka vizuri kwenye kochi hilo la vono.
“Aaa taratibu za kuaga mwili zimebadilika, sasa itakuwa kesho kutwa badala ya kesho,” akawaeleza.
“Kwa nini?”
“Spika amedai tu kuwa kuna mambo ya kifamilia yanapewa nafasi kwanza,” Nnandi akaeleza. Mheshimiwa Matata akamgeukia Obobo.
“Fanya unaloweza kisha kazi ikiisha tukutane Nairobi kama tulivyokubaliana,” alipomaliza kumwambia hayo, Obobo akaondoka ndani ya chumba kile na kuwaacha watafunaji hao wakiendelea na hili na lile.
“Waheshimiwa hapa lazima tuwe makini, tutaumbuka,” Matata akasema.
“Aumbuke nani wewe! Tumejikamilisha, si mnajua hata waziri mwenye zamana ya usalama yuko upande wetu, ni swala la kumwambia tu kama kuna watu wake awaondoshe mara moja,” Nnandi alikuja na wazo jipya kabisa ambalo kwalo kila mtu alihafiki bila ubishi. Wakajipanga kumwona waziri huyo kwani naye ni mmoja wao katikan sakata hilo lakini alikuwa akifanya kwa siri sana kutokana na wadhifa huo.
“Jamani ee kama Yule kijana niliyemwona yupo katika uchunguzi huu naanza kuhisi tumbo la kuhara. Yule kijana ni nyoka mwenye sumu kali,” Matata akawaeleza.
“Hayo yasiwatishe, hawawezi kutufikisha popote kwa mbwembwe zao si tutaendelea kula kuku kwa mrija,” Nnandi aliongeza kusema huku wakati huo mhudumu alikwishamletea pombe kali
 
SEHEMU YA SABA
Siku tatu baadae
KATIBU WA BUNGE alishindwa kuchanganyikiwa baada ya kugundua kuwa nyaraka za mswada wa sakata la Escrow hazionekanai ofisini. Alipekua huku na kule lakini wapi. Niliziweka kwenye droo hii, na nilifunga na funguo nilikuwa nazo mwenyewe, zimepoteaje? Alijiuliza akiwa kaweka mikono yake kiunoni. Kila alipojumlisha moja na moja ilikuja nne na sio mbili. Akashika mkono wa droo na kulivuta kwa kulitikisatikisa lakini halikuwa na kitu ndani yake. Akashusha pumzi ndefu na kuketi kitini huku akihisi macho yake kujaa machozi ya dharula.
Alipoona sasa hana la kufanya, aliinua simu yake na kubofya tarakimu Fulani kisha akaiweka sikioni na kusubiri upande wa pili upokee simu hiyo.
“Hello!”
“Ndiyo mkuu, yaani kabrasha zote za lile sakata hazipo kabisa…”
“Sasa zitakuwa wapi? Au ume-missplace…?”
“Hapana mkuu, naijua kazi yangu, hizi zitakuwa zimeibwa,”
“…Zimeibwa!” ile sauti ya upande wa pili ikahamanika kwa jibu hilo, “…haiwezekani… naomba uje ofisini kwangu mara moja!” ikamwamuru Yule Katibu wa Bunge naye muda huohuo akiwa kajawa na hofu akatoka ofisini. Alipofika nje akasimama kidogo na kisha kama asiyeamini akarudi ndani na kuanza upya kupekua.
Dakika thelathini zilizofuata alikuwa tayari kwa mkuu wake wa kazi, mwili wake ulikuwa umetona kwa jasho ijapokuwa kiyoyozi kilikuwa bize kikifanya kazi ya kupoza hewa.
“Unaniambia zimepoteaje?” Yule mwanamama, mwenye wadhifa mkubwa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akamwuliza katibu wake wa bunge mwenye mamlaka ya kutunza na kujua dondoo zote za mhimili huo.
“Yaani hata sijui, tangu kikao cha mwisho, kabla ya msiba wa Msesema niliziweka kwenye loka namba tatu lakini sizioni pale”.
“Ina maana mtu kaingia kaiba ofisini kwako humohumo?” Yule mwanamama akuliza huku akionekana wazi kushikwa na hasira kali.
“Ataingiaje?” Yule kijana akajikuta anauliza.
“kama hajaiba mtu kutoka nje basi ni wewe na wasaidizi wako mtakuwa mmekula njama, na hili lazima lichukuliwe hatua mara moja. Nenda nitafanya utaratibu mwingine juu ya hili kisha nitakuita pamoja na wasaidizi wako, hii ni aibu kwetu, kabrasha linapotea vipi kwenye kitengo nyeti kama hiki? Ajabu!” mkuu akaagana na huyo katibu na kubaki peke yake ofisini, sura yake ilisawajika kwa mawazo.
§§§§
Taarifa za upotevu wa nyaraka hizo ulilitikisa Bunge, kila aliyesikia habari hiyo hakuamini ama kile anachoambiwa au anachozikia. Maswali yasiyo na majibu ndiyo hasa yaliyotawala vichwa vya walio wengi. Jeshi la polisi nalo lilikuwa likajaribu kadiri ya uwezo wao kuona labda hiki au kile lakini yote ya yote hakuna aliyejua kabrasha hizo zimepoteapotea vipi.
Upande mwingine vijana wa Usalama wa taifa ambao daima huendesha shughuli zao katika eneo hilo nao walikuwa wamekutana kwa siri kujadiliana juu ya upotevu wa kabrasha hizo nyeti.
“Hii ni njama, lazima ifanywe na wenyewe,” mmoja alisema.
“Unataka kutuaminisha kuwa wameiba wenyewe?” mwingine akadakia.
“Ndiyo, sasa funguo unatunza wewe, ofisi ni yako, polisi wanasema hakuna mtu yeyote asiyehusika aliyeingia ndani ya wigo huu usiku wa jana. Sasa hii maana yake ni nini? Inabidi tumchunguze Yule katibu si ajabu kala njama,” mwingine akagongelea msumari ambao karibu jopo zime liliunga mkono.
“Itabidi tufanye hilo ijapokuwa vikao vinaisha leo na watakutana hapa miezi miwili ijayo…”
“Sasa huu ndo muda wa kufuatilia kila kona ili wakirudi bungeni kwenye kikao cha arobaini na nane tuwe na jibu na pia tuwe tumewashughulikia wanaohusika,” alidakia Yule aliyeonekana kama ndiyo mkubwa wa kile kikao. Baada ya majadiliano yaliyochukua muda mrefu muafaka ulifikiwa na kila mmoja alipewa jukumu lake katika kipindi hicho.
Mchana wa siku hiyo kikao kingine kiliendelea katika ofisi Fulani huko walikutana watu wasiozidi wanne; Kamanda wa Polisi mkoa wa Dodoma, mkuu wa Usalama wa Taifa Mkoa wa Dodoma, kiongozi wa askari wa Bunge na Spika. Mjadala uliochukua nafasi ulikuwa ni huo wa kupotea kwa hizo nyaraka nyeti.
Vichwa vilifanya kazi ya kuchambua hiki na kile, lakini jibu la uwazi halikupatikana, polisi walisema kuwa wana uhakika hakuna mtu aliyeingia ndani ya wigo huo kutokana na ulinzi mkali waliokuwa wameuweka kama ilivyo kawaida yao, hata walipohakikisha kwenye kamera za usalama bado hakuna mtu aliyeonekana kuingia ndani ya wigo huo. Baada ya kuchanganua njia zote ambazo kwazo zinaweza kuzaniwa zimetumiwa kuiba nyaraka hizo, bado jibu liligonga kuwa lazima Katibu wa Bunge anahusika kwani nduye ambaye anajua kila kitu jinsi kilivyo na kinavopangwa.
§§§§
Katika kikao cha siku hiyo cha Bunge, Mheshimiwa Kibanio hakuonekana kwenye siti yake, haikuwa kawaida. Kila mmoja alikuwa akimsubiri mtu huyo ambaye alipendwa kwa jinsi anavyojua kujenga hoja ndani ya vikao vya bunge. Mara kwa mara Waheshimiwa walikuwa wakiangalia saa zao lakini hawakumwona kutokea.
Hali hiyo pia ilikuwa kwa Spika wa Bunge, akiwa katika kiti chake alikuwa akitupa jicho mara kwa mara katika kile kiti lakini hakumwona Msesema, huyu leo vipi? Alijiuliza. Kwa siri akaagiza wahudumu wahusika ili kujua kwa nini mtu huyo hajafika bila taarifa na siku hiyo alikuwa na mswada wa kuwasilisha juu ya sakata la Escrow, ilikuwa ni siku aliyoahidi kuwataja wote waliomo kwenye hiyo ‘Orodha ya aibu’.
§§§§
Saa ya ukutani ilipiga muziki wa kuahiria saa kamili imefika, Mheshimiwa Kibanio aliinua uso na kuangalia saa ile, ilikuwa saa tano asubuhi inakimbilia kwenye saa sita huko, akakurupuka lakini alijikuta mwili mzito na kichwa kinamuuma sana. Nini hiki? Alijiuliza pasi na jibu. Akajilazimisha kuamka na harakaharaka akaingia maliwato ili kujiswafi, tayari alikuwa amechelewa kikaoni na ilibaki dakika chache sana kabla hajasimama kulieleza Bunge juu ya wale wote wanaohusika na lile sakata nyeti. Mara akaona simu yake ikiita, alipoinyanyua na kuitazama alimjua anyepiga simu hiyo ni nani.
“Mheshimiwa vipi, tunakungoja kwa hamu!” ile sauti ikamwambia.
“Aaaah! Yaani nashindwa kujielewa asee, ndiyo naamka sijui nini kimetokea,” Mh. Kibanio akajibu huku akivaa shati lake.
“Ok, pole sana, labda jana zilikuwa nyingi sana …”
“Aaaa hapana, jana sijaonja kabisa ila nashangaa nini kimenipata, hata sasa naona kichwa kizito sana na si kawaida,” akaeleza. Alipokwisha kuvaa kila kitu tayari, aliuvuta mkoba wake tayari kuondoka lakini alipounyanyua ukafunguka na kabrasha zote kumwagika, alitupa jicho pale sakafuni zile karatasi zilipozagaa. Hakuamini anachokiona, nani alifungua huu mkoba? Akajiuliza huku akiinama na kuokota yale makabrasha. Badala ya kuyaweka mkobani, akaanza kuyachakura chakura akitazama hili na lile.
“Shiiiit!” akang’aka kwa sauti, akaanza tena kuyachambua yale makabrasha.
“Sasa liko wapi?” akauliza kwa sauti kana kwamba kuna mtu anayeongea naye ndani ya chumba hicho lakini alikuwa peke yake. Akayaacha yale makabrasha na kuanza kupekua kwenye makabati, hakuna kitu. Mheshimiwa Kibanio alijitupa kitandani na kupiga ngolo.
Hakuamini kama kabrasha hizo za muswada muhimu ambao alitakiwa kuuwasilisha mchana huo hazikuwepo, zimekwenda wapi? Lilikuwa ni swali gumu kutegua, akiwa juu ya kile kitanda alijikuta akilia kama mtoto. Akakurupuka na kukusanya yale makaratasi pale chini akayaweka mkobani na kutoka chumbani mle kama mtu aliyechanganyikiwa. Alipoushika mlango akakuta upo wazi, haujafungwa, akasimama na kutazama ndani. Nani kaufungua huu mlango? Nimeibiwa! Akawaza na kujikuta akiishiwa nguvu. Alipokuwa akiuvuta mlango kuufungua akaona karatasi ndogo ikipeperushwa kwa upepo na kuingia sentimeta chache ndani ya chumba hicho. Akaiokota mara moja na kuitazama, ilikuwa na maandishi machache tu.
…Ukitaja hata jina moja tu, yatakukuta yaliyomkuta Msesema…
Kisha mwisho wa maneno hayo kulikuwa na kipicha kidogo cha fuvu la binadamu.
“Shiiit! Ina maana Msesema kauawa? Au ujumbe huu umekosewa?” akajiuliza kwa sauti ndogo. Akiwa anatetemeka, akatoka ndani ya chumba kile na kuteremka ngazi za hoteli hiyo ya Dodoma na kufika chini kabisa kwenye maegesho.
“Mheshimiwa vipi leo? Mbona umekawia sana?” dereva wake akamwuliza.
“Hata sijui kwa kweli nimelala sana, nahisi naumwa maana kichwa chote kizito,” akajibu huku ile gari ikiwa inatoka polepole katika maegesho yale.
§§§§
“Ukimya wetu wa siku tatu umemfanya adui yetu ajitokeze na kufanya mambo yanayoaminika kuwa ni shetani pekee anayeweza,” Madam S alimwambia Amata.
“Ndiyo, ni mbinu nzuri sana uliyotushauri kuitumia, na sasa kama unavyosikia, kabrasha zimeibwa palepale bungeni, inashangaza!” Amata akajibu.
“Yeah, ujue hapa kuna mtu mwenye taaluma kama si ya ujambazi basi sijui tuite ya nini, we kuingia mle ndani ilhali ulinzi mkali na kamera kila kona vyote hivyo vizikubaini. Sasa pale kesi yote inamwangukia Mwambene, katibu wa bunge, lakini hapana, kutokana na wapi tumefikia huyu mtu ni profesheno, lazima tuingie kazini kwa akili zote na nataka apatikane akiwa hai ili tujue nini kipo nyuma ya pazia,” Madam S alimwambia Amata, “Koh! Koh! Koh!” akakohoa kidogo, “Sasa nataka uendelee na kazi, pambana na huyo mtu na umlete mikononi mwangui akiwa na pumzi yake, licha ya hili tu najua atakuwa na mengi sana,” Madam alimalizia kusema, akatoa miwani yake na kuiweka mezani.
“Umesomeka Madam!” Kamanda Amata akajibu huku akinyanyuka, “Nani yuko nyuma yangu?” akauliza.
“Gina, nimeshamuweka tayari”.
“Asante!” Amata akajibu huku akiwa tayari kasimama kwa kuondoka.
“Ofisi yetu imehamia hapa kwa siku chache lakini namnata huyo mtu akiwa hai ili kutoka kwake tujue nani amemtuma,” Madam akasisitiza.
§§§§
Amata akaondoka na kuiacha ofisi hiyo ndogo na kutokomea mjini mpaja hotelini kwake, alipoingia tu jicho lake lilizunguka chumba chote na kugundua kuwa kuna upekuzi wa siri uliofanyika. Wameshajua nilipo, akawaza, kisha kwa hatua za taratibu alikipita kitanda mpaka usawa wa dirisha, alipokaribia kijimeza kidogo kilicho pembeni mwa kitanda ambacho juu yake kuna taa ndogo kwa ajili ya kusomea, saa yake ikapiga ikamfinya na kutoa mlio Fulani mkali. Amata akasimama na kuiinua ile taa akaichunguza na kugundua kuwa kuna kidubwasha kidogo sana kimebandikwa pembeni, alipokiangalia alikijua kidubwasha hicho chenye kazi ya kunasa sauti na kutuma mahala Fulani. Zaidi ya hilo alikitambua kifaa hicho kuwa kina uwezo mdogo wa kurusha mawimbi hayo na si zaidi ya mita 200 za mraba. Adui yangu hayuko mbali kama si yeye basi kibaraka wake, akawaza huku akifungua kabati kubwa la nguo, akachukua kijiredio chake kidogo ambacho hutumia kurekodi sauti mbalimbali, akakibonya na kutafuta sauti aliyoona itamfaa adui yake, akataka kuweka ile ya mtu anakoroma, akaona hiyo sio sawa kwa muda husika, akatafuta nyingine ya kufaa akakiweka katika ile meza kisha akakiwasha, wakati kikiendelea kutoa sauti hizo za mahaba zilizorekodi watu wawili wakifanya mapenzi huku wakiongea maneno ya mahaba, akasogea pembeni na kuvuta meza nyingine akaiweka nyuma ya mlango, akafunga mapazia yote na kuzima taa.
Giza hafifu lilitawala chumba hicho, ile mashine iliendelea kutumbuiza pale mezani. Amata akaketi, bastola yake akaiweka mezani na kisha kujimiminia pombe kali aina ya GIN na kuinywa taratibu akimsubiri mgeni wake kwani alijuwa kwa vyovyote atakuja.
Kutokana na uchovu aliokuwa nao Amata, kijiusingizi kilikuwa kikimnyemelea kwa mbali, lakini mara kwa mara alikuwa akipambana na hali hiyo. Kama alivyodhani ndivyo ikawa, alihisi kitasa cha mlango kikinyongwa taratibu, akageuza shingo na kuangalia kule mlangoni huku bastola yake iliyofungwa kiwambo ikiwa tayari imekaa kinganjani.
Kabla Amata hajamwona mtu huyo aliona kwanza mlango ukisukumwa taratibu na domo la bastola lililofungwa kifaa cha kuzuia sauti likitangulia na kutema risasi nne mfululizo kuelekea kitandani. Alitamani kucheka lakini akajizuia kwa kuwa haikuwa mahala pake.
“Shiit!” sauti kutoka nje ya mlango ikasikika na mara yule mtu akaingia mzima mzima. Alikuwa ni pande la mtu, mwanaume aliyevalia jeans na fulana nzito, usoni mwake alivaa soksi iliyoficha uso wake na kuacha macho tu.
“Karibu katika mikono ya shetani!” Amata aliongea kwa sauti nzito iliyomfanya yule bwana kushtuka na kusimama ghafla, “nilitaka uje na umekuja mwenyewe, ondoa magazine kwenye silaha yako bila kuigeuka,” akamwamuru.
Yule bwana akataka kuuvuta mkono wake wa kushoto kufanya hilo.
“No! tumia mkono huohuo ulioshika bastola,” akamwambia, naye akafyatua ile magazine ikaanguka chini na risasi zake zikatoka ndani yake na kutawanyika, “weka na bastola yako chini,” akamwambia, naye akafanya hivyo.
“Geuka huku mikono yako ikiwa kichwani, ukiniletea ujinga nakumaliza, sina urafiki na viumbe vibaya kama ninyi, mnaotoa roho za watu bila sababu,” akamwambia na Obobo akafanya hivyo, sasa wakatazamana uso kwa uso.
Akainua glass yake na kupiga funda moja la kinywaji, kabla hajamaliza kinywaji kile. Alijikuta bastola yake ikimtoka mkononi mwake ka teke kali alilopigwa na Obobo. Obobo skstus kando kwa miguu yake miwili na kusimama tayari kwa mapigano. Amata akachukua ile chupa na kumimina kinywaji kwenye glass yake bila wasiwasi wowote, huku Obobo akimtumbulia macho kwa kitendo hicho. Akiwa katika kuzubaa huko chupa ile ya pombe ilitua kichwani kwa Obobo na kuvunjika, Amata aliruka kutoka katika kiti alichokaa na kutu mbele ya huyo jamaa kisha konde moja zito likatua shavuni mwa Obobo na kumpeleka chini bila kipingamizi. Obobo akajibetua na kusimama wima kisha akaruka samasoti na mguu wake wa kwanza ukamkosa Amata ule wa pili ukatua begani mwake. Maumivu nakali yakalipenya bega la Amata, hakujali, konde zito la Obobo likaufuata uso wa Amata naye akaepa, la pili akaepa, la tatu akaepa na kuruka ‘beki’, kwa mtindo huo wa sarakasi akampiga mateke mawili mazito chni ya kidevu, Obobo akajibamiza ukutani.
Amata akatua kitandani na bila kuchelewa, akateremka na kupeleka mapigo matatu ya karate yaliyompata Obobo sawasawa na kumsababishia kizunguzungu, Obobo akajitupa chini na kuiwahi bastola ya Amata lakini Amata alilitambua hilo, akavuta teke moja kali lililotua shavuni mpaka karibu na sikio na kumtupa Obobo upande wa pili, Amata akaiokota ile bastola na sekunde hiyo hiyo, Obobo akona hatari iko upande wake, alijikunja na kujikunjua kama samaki akaruka na kujipiga kwenye kioo cha dirisha, akadondokea nje na kupotelea mtaani.
“Shenzi kabisa, hiyo nimekuonjesha, kazi bado inakuja!” Amata alijisemea mwenyewe huku akiwa ameshalifikia lile dirisha na kumwona mtu huyo akipotelea mitaani.
Akaiendea ile bastola ya Obobo pale chini na kuiokota kisha akazipachika zile risasi katika magazine na kuiweka mahala pake, kwa mikono yake miwili, kwa kutumia ule wa kushoto akai-slide kwa upande wa juu na kuruhusu risasi ya kwanza kutumbukia chemba. Bastola la kizamani kweli kweli lo! Akawaza huku akiiangalia angalia, ilikuwa ni Smith and Wesson.
§§§§

Hali ya sintofahamu iliwakumba Wabunge baada ya kukosa kusomwa ile ripoti iliyodaiwa kuwa ina majina ya watu waliokwapua pesa za ESCROW. Spika alipotangaza kuwa swala hilo litajadiliwa kikao kijacho wengine wakazomea na wengine wakakosa ustaarabu hata kuamua kutoka nje.
“Kwa nini isisomwe? Haijaibwa wala nini, wameikalia tu kuficha maovu ya wakubwa, hii nchi hii mpaka tutoke hapa tulipo labda aje kuongoza Yesu au Mtume Muhamad” alilalama mmoja wa waheshimiwa huku akiingia kwenye Shangingi lake tayari kwa kuondoka. Ilikuwa ni vikundi vikundi vya watu watatu au wane; hapa na wengine kule, kila mmoja akilaumu kutosomwa kwa taarifa hiyo toka kwa Mheshimiwa Kibanio.
Watu alijawa na shahuku ya kusikia majina hayo yakitajwa hadharani lakini haikuwa hivyo wakati wengi wao wakiamini kuwa faili hilo halikuibwa bali ni mbinu za wakubwa ni wachache tu walioumiza kichwa kuwa kimtokea nini hata faili hizo zipotee katika mazingira ya kutatanisha.
Katika moja ya vyumba vya mikutano nyeti ndani ya jengo hilo la Bunge kulikuwa na kikao kinachoendelea, kikao cha kamati ya usalama ya Bunge. Agenda kuu ya kikao hicho ilikuwa ni kuona juu ya upotevu wa faili hizo.
Mvutano mkubwa ulikighubika kikao hicho baada ya kusikiliza taarifa ya Katibu wa Bunge.
“Wewe si ndio mwenye funguo itakuwaje hilo faili lipotee?” aliuliza mmoja wa wajumbe. Wakati wakiendelea kubishana mara akaingia Spika ambaye muda wote alikuwa akifunga kikao cha Bunge, akakaribishwa na kupewa taarifa ya wapi kikao kimefikia, alipojiridhisha na taarifa hiyo akawasilisha pia taarifa ya upotevu wa nakala kama hizo ambazo zilikuwa mikononi mwa Mheshimiwa Kibanio na wakati huo taarifa za kuvamiwa kwa Mheshimiwa Segeratumbo nazo zikawasilishwa.
“Yote haya tulikuwa hatujayasema kwa sababu za kiusalama, lakini kumbe tumekosea,” akasema Spika.
“Kwa hiyo kuna mtu au watu ambao wanazisaka kwa udi na uvumba? Basi haina haja ya kuumiza kichwa kwa maana watu hao tunao humuhumu,” mjumbe mmoja akatia neno katika kikao hicho.
“Isiwe tunazugana hapa!”
“Tunazugana vipi? Msesema amekufa kwenye ajali ya ajabu tu, na hizi nyingine ndio zinaleta utata mara mia, tumekwisha.”
Kikao kilichukua muda mrefu, majadiliano yalifikia muafaka kuwa uchunguzi ufanyike na ikiwezekana wanaohusika wachukuliwe hatua.
“Mheshimiwa Msesema alipopata ajali alikuwa na mwanamke mle ndani ya gari hivi haiwezi kuwa ni mmoja wapo?” mjumbe mmoja aliogeza.
Kila mtu alishangaa kwa taarifa hiyo hakuna aliyeijua kwanza ijapokuwa wachache wao waliichukulia ni hali ya kawaida. Jopo hilo likaamua kuwa yule mwanamke akamatwe kwa mahojiano kisha baada ya hapo ndio wajue nini chakufanya. Maamuzi yakaandikwa na kuwekwa katika faili.
“Lakini nitaomba msubiri kwanza kabla sijatoa go ahead ya hili,” Spika aliwaambia.
“Aaaah kikao cha kamati kimeamua!” mwenyekiti wa kamati akaunguruma kwa jazba.
“Nina maana yangu kuwaambia hilo…”
Wakakubaliana na kile kikao kikaisha. Kila mtu akatawanyika.
***
“Kwisha habari yao! Bado kumkomesha mmoja, yule anajifanya mjanja,” Mheshimiwa Nnandi aliwaambia wenzake Kagosho na Matata.
“Tumekodi jabali, mtu anyejua kazi yake,” Matata akaongeza kwa sauti ya kilevi.
“Eti leo walikuwa na kikao cha kamati ya usalama kwa lipi? Hawajui kuwa kati yao kuna mwanetu mle! Hii nchi yetu bwana tutakula tunavyotaka, nani wa kutubabaisha?” Kagosho naye alibwabwaja.
Watatu hawa waliendelea kujipongeza kwa kula na kunywa, kila mmoja kichwani mwake akifikiri tu jinsi gani ya kutumbua pesa hizo ambazo si muda zimetolewa kwenye akaunti hiyo na kuwafikia walengwa kwa mbinu tofauti.
MIAKA MIWILI ILIYOPITA
BENKI KUU YA SERIKALI
GAVANA WA BENKI HIYO alikuwa katika kikao kizito katika moja ya ofisi nyeti za serikali, katika kikao hicho agenda kuu ilikuwa ni jinsi gani ya kifunga hiyo akaunti yenye mabilioni ya pesa yaliyoingia kutokana na mradi hewa wa nishati ya umeme.
“Watu tumefanya kazi kubwa kuhakikisha hili linawezekana, sasa ni wakati wetu kula njasho letu,” mmoja wa wajumbe alikiambia kikao.
“Ni sawa usemalo, lakini unajua kuwa hizi fedha ni za umma?” Gavana aliuliza.
“Za umma! Kivipi? Hivi we unajua tumestrago kiasi gani kufanikisha hii akaunti kunona? Watu tumetengeneza mikataba tumekwenda Thailand tukafanya yetu. Tumerisk kazi zetu ujue, si kwamba hatukuwa na plan bali pesa hizi kuja katika akaunti hii ni kosa moja dogo tulilifanya, na hili lilisababishwa na watu kama wewe,” mjumbe mwingine mwenye ushawishi kwa maneno yake alimwambia yule Gavana.
“Sawa, sasa ninachouliza ni kwa nini hizi pesa zikae hapa?” gavana aliendelea kurusha maswali.
“Swala sio kwa nini, swala ni jinsi gani tutagawa hisa za wenye nazo?” mjumbe mwingine akadakia.
“Hisa! Hisa kivipi?” Gavana akashtuka mpaka akasimama.
“Ndiyo, hisa, watu wamewekeza mapesa kibao katika mradi huu, kwa kuwa tulisema itafika wakati wenye hisa zao wapate gawio lao, na wakati huo ndio sasa,” yule mjumbe wa kwanza akasema.
“Sikilizeni, mambo ya mahesabu hasa ya pesa kama hizi hauendi hivi, wala mgawanyo haufanyiki kama mnavyofikiria ninyi. Kwa kuwa pesa hizi nilizipokea kama gavana kwa maandishi kutoka kwa kiongozi mkubwa basi na zitagawiwa mnavyotaka ninyi kwa utaratibu uleule wa kimaandishi…”
“Unamaanisha nini hapo?” mjumbe yule wa kwanza akadakia.
“…Namaanisha wale waliosaini ili ziletwe hapa na kufunguliwa hii akaunti ya Tegeta Escrow ndio hao hao wasaini kuziondoa,” yule Gavana alifafanua kwa lugha rahisi, “Isitoshe Mkaguzi mkuu wa serikali CAG lazima atakuja kufanya ukaguzi wake kwani Bunge la bajeti limekaribia,” akaongeza.
“Kwa hiyo!”
“Kwa hiyo mniache nifanye mawasiliano na hao watu kisha nitawajulisha nini kimeamriwa,” Gavana akamaliza.
MIEZI MITATU ILIYOFUATA
TAARIFA ya maandishi iliyosainiwa na watu kadhaa wenye vye vikubwa vywenye maamuzi ya juu ilifika katika ofisi ya Gavana wa fedha. Ijapokuwa alitumbua macho lakini hakuwa na la kusema au kuamua. Pamoja na taarifa hiyi iliambatanishwa orodha ya majina ya watu na akaunti zao za benki ili pesa hizo zielekezwe kwenye akaunti hizo kwa viwango vilivyopangwa.
“Come on!” alijiseme hukua kijiegemeza kwa nguvu katika kiti chake cha kunesanesa. Alipoona akili yake haifanyi kazi akainuka na kutaka kutoka ofisini aliposhika kitasa cha mlango simu yake ya mezani ikaita, akasimama kwa hofu na kuiangalia. Kwa masikitiko akairudia na kunyakuwa kutoka pale kwenye kikalio chake.
“Hello…”
“Umepata barua elekezi juu ya zile fedha ulizoziita za umma?” ile sauti ikamwuliza.
“..Ndi-ndi-yo nime-pa-pata!”
“Ok, sasa fanya kama ilivyokuagiza,” ile sauti kaendelea kusema.
“…La-la-ki-n…”
“DO IT NOW, THERE IS NO LAKINI HAPA!” ile sauti ikafoka. Yule Gavana akakaa juu ya kiti chake huku mwili ukitiririkwa na jasho la kutosha, ingawaje kiyoyozi kilikuwa kikijitahidi kuifanya hewa ya humo ndani kuwa tulivu lakini sasa ilikuwa ni mithiri ya tanuru la kuokea mikate. Kila alichokishika kilikuwa cha moto kwake. Akaikamata ile barua kwa mara nyingine, akairudia kuisoma kwa makini na baadae akitafsiri kwa kiingereza ili aone kama maana zinafanana. Mwili wake ulikuwa ukikumbwa na hali mbili mara baridi na mara joto, kipindi Fulani alijipepea kwa gazeti na wakati mwingine akafunga vizuri tai yake, ilikuwa ni sintofahamu ndani ya kichwa chake. Muhuri wa moto uliogongwa na mtu aliyeonekana kuwa na nguvu ulionekana bila shida mwisho wa ile barua na nembo yake tukufu ilikuwa pale.
‘Sina cha kufanya lakini huu ni msala huu!’ akawaza na kuwazua kisha akainua simu yake na kupiga kwenda kwa mtu mwingine. Dakika moja tu alikuja kijana mmoja nadhifu na kupewa maagizo yale, naye bila ajizi maadam ‘mkubwa kasema’ akaenda zake na kufanya uhamisho wa fedha hizo.
Gavana alihisi kichwa kikimuuma, alihisi joto kali kwa mbali aliona kama mwili wake unapoteza nguvu, aliamua kutoka ofisini na kumwomba dereva wake kumfikisha hospitalini haraka kwa uchunguzi.
***
Baada ya zoezi hilo kukamilika watu wengi wakaingiziwa pesa mamilioni kwa mabilioni wakiwamo wafanyabiashara wakubwa, viongozi wa dini, wananchi wa kawaida, viongozi wa serikali na hata watoto wa vigogo waliyakwaa mapesa hayo. Taarifa hiyo iliastua wananchi na wabunge wanaopenda haki na hatima ya Taifa lao.
“Huu ni ufisadi mkubwa, haiwezekani,” mmoja alijisemea hilo.
“Yaani wamegawana!” mwingine alijikuta akitamka.
“Hii nchi inatisha, inabidi tufike wakati tumwogope Mungu!” huyu naye alijikuta akitamka baada ya kusoma habari hiyo gazetini.
“Mamaaaaa we! Hata huyu yumo, mijitu haina aibu,” mwingine alijikuta anapiga kelele.

SEHEMU FULANI FULANI – Siku nyingi tu zilizopita
“Sikiliza! We usiogope, nitatumia akaunti yako ile ya P.O.T Bank, nitaingiza kama Bilioni 19.99 hivi, wewe pale kuna kamisheni yako umesikia kijana!” Mzee Fulani alimwambia kijana mmoja katika ofisi yake mchana huo. Siku hiyo aliwaita watu kama saba hivi ambao alikuwa akiwaamini kuliko anavyojiamini mwenyewe.
“Lakini mzee…”
“Sikiliza wewe: Unataka pesa?”
“Pe-pe-pe-sssa? Ndi-yo, the, kwani kuna asiyependa pesa?” yyle kijana alijibu kwa kuweweseka.
“Sasa katika hizo pesa nitakupa shilingi Milioni mbili na nusu,”
“Hapo sawa! Hamna shida, akaunti yangu ndiyo hiyo hiyo mzee,”
Kila mmoja alijua ni jinsi gani atasafirisha pesa zake kutoka kwenye akaunti hiyo na kufikia akaunti yake binafsi. Hali hiyo wapenda uzalendo hawakuweza kuvumilia, walipigia kelele, wakatangaza maredioni, wakaandika magazetini, wananchi wakakasirika, wakapaza sauti zao dhidi ya dhukuma hiyo ya haki.
Kati ya watu walioibuka katika sakata hilo kama wapenda uzalendo alikuwa Mheshimiwa Msesema, Segeratumbo na Kibanio.
USIKU FULANI
“Pesa tumepata tena nyingi mno ambazo tutakula milele amina, lakini kuna vijitu viko vitatu vinataka kuleta tabu, hivi wanajua tumetoa jasho kiasi gani kutengeneza hii hela?” Mheshimiwa Matata akawauliza wenzake.
“Wajue wapi? Wanataka wapate sifa tu wale,”
“Dawa yao iko jikoni, tena haina haja ya kuwafanyia mbaya ila tuwashawishi tu nao wenyewe wataingia mtegoni,”
“Kwa ngapi?”
“Milioni mia mbili tu kila mmoja akamalize shida zake,” Matata akamaliza huku Nnandi na swahiba wao wakikata kilaji.
***
“Ngriiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiii! Ngriiiiiiiiiiiiiiiiiiii!...” Msesema alishtuliwa na simu iliyo katika kijimeza chake pembeni tu mwa kitanda, akamruka mkewe na kushuka upande wa pilia akinua simu hiyo.
“Unaongea na Mheshimiwa mkubwa sana, Bwana Matata!”
“Ndiyo Comrade!”
“Najua una njaa kama walivyo wanaojiita Wazalendo wenzio, yeyo anayejiita mzalendo huyo ana njaa tu. Najua mbinu zako na wenzio Kibanio pamoja na Segeratumbo. Sasa kuna Milioni mia tisa; tatu kwa kila mmoja, kesho asubuhi kijana wangu atakuletea hundi…”
“Hapana! Siwezi kabisa, hiyo ni rushwa, na rushwa ni adui wa haki, mimi ni Mzalendo hata kama wazalendo ni wenye njaa basi ninyi mabwanyenye mistake wazalendo tufe njaa, tunazitaka pesa za umma zirudi zinufaishe wananchi. Tazama watoto wetu hawana vitabu vya ziada wala kiada, madawati ni shida, madawa hospitalini ni kitendawili, huduma za afya ni dhoofu, vifo vya akinja mama na watoto vinaongezeka ilhali ninyi mnahubiri kupungua kwa asilimia zake. Kuweni na huruma jamani, hizo ni pesa za umma na tutapigana mpaka mwisho. Kumbuka kwamba Mzalendo akichoka damu itaongea…” akakata simu.
“Pumbav sana, limekata simu, linajifanya linajua kumbe linaungua na jua, wacha wafe masikini,” Mheshimiwa Matata akawaambia wenzake.
Ushawishi kwa watu hao watatu ili wakubali kutoufuatilia mpango huo viligonga mwamba. Ndiyo kwanza wakawachochea na wao wakauwasha moto bungeni, mpaka ikapelekea Katibu wa Bunge na Katibu wa Wizara ya Nishati na Madini kumuomba Mkaguzi Mkuu wa Serikali kufanya ukaguzi wa akaunti hiyo. Ukaguzi huo ulilenga kufanya uchunguzi wa kina ambao ungetoa taarifa kamili yenye kuonesha hali halisi kuhusu miamala (transactions) kwenye akaunti maalum ya Tegeta Escrow kisha kutoa taarifa kuhusiana na ukaguzi huo.

MIEZI SITA BAADAE
Ofisi ya Mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali ikauomba umma uvumilivu kwa kuwa ukaguzi huo ulichukua muda mrefu kutokana na hadidu zilizotolewa kuridhiwa na ofisi ya Bunge pamoja na ile ya Wizara ya Nishati na Madini.
Taarifa hiyo kwa umma ilielezea na kufafanua kuwa…
‘ Kwa kuwa Hadidu za Rejea pekee haziwezi kuonesha ukubwa wa kazi bali utekelezaji wa kazi yenyewe ndio unaoweza kutoa taswira halisi, ni vyema umma wa watanzania ukatambua kuwa Ukaguzi huu haujaweza kukamilika kwa kipindi kilichokadiriwa awali hivyo ukaguzi unaendelea kwa kuzingatia Hadidu za Rejea na kifungu cha 29 cha Sheria ya Ukaguzi wa Umma Na. 11 ya mwaka 2008.’
Kwa kuwa wahenga walisema mvumilivu siku zote hula mbivu ndipo ilipofika wakati ambapo ukaguzi huo ulikamilika na hekaheka za huku na huko zikaanza. Watu matumbo yakawa moto, miguu haifanyi kazi wengine mahospitalini. Taarifa hiyo ya ukaguzi ilianisha majina ya watu waliojichotea mifedha hiyo na akaunti zote ziliainishwa wazi wazi.
Waheshimiwa; Msesema, Segeratumbo na Kibanio walizipata taarifa hizo kutokana na vyanzo vyao na kuahidi kutaja majina ambayo hayajaorodheshwa katika orodha hiyo.
“He! Kumbe kuna wengine hapa hawajorodheshwa, tobaaaah!”
 
SEHEMU YA NANE
OBOBO alijifungia ndani ya chumba chake akiwa anajiganga hapa na pale baada ya kupata kichapo kutoka kwa Amata. Mwanaharamu yule kaniumiza, alijisemea kwa sauti ya kusikia mwenyewe. Taya lake lilikuwa na maumivu makali ndipo alipogundu kuwa kapoteza jino moja. Lo! Nilikuwa simjui vizuri yule jamaa, inaonekana yuko vizuri sa kwenye martial arts, nitamtia mkononi, safari hii nitampa mapigo ya kifo, Obobo akajisemea huku akimaliza kujifunga ile clip bandeji katika mkono wake. Akiwa katika kazi hiyo simu yake ikaita, akaiangalia ilikuwa namba tupu isiyo na jina. Akainyakua mara moja na kuipokea baada ya kuona namba ile ni ya Tanzania.
“Hey! Hapa kuna mpango kutoka jeshi la polisi kumpata yule mwanamke aliyekuwa na Msesema ili afanyiwe mahojiano, nafikiri anaweza kutuharibia mpango wetu,” ile sauti kwenye simu ikamwambia Obobo ambaye aliitambua mara moja kuwa ni ya mteja wake.
“Nimekupata, nitalishughulikia mara moja,” akajibu na kukata simu. Akainuka kutoka pale alipoketi na kuuendea mkoba wake, akaufungua na kutoa bastola nyingine baada ya ile ya kwanza kupotelea kule kwa Amata. Hii ilikuwa kidogo sio ya zamani sana. Magnum 22, akaichukua na kuibusu kisha akachukua na kifaa chake cha kuzuia sauti, akaviweka mahala pake katika lile jaketi alilovaa, akachukua moustache wa bandia na kujibandika chini ya pua yake, miwani ya duara kwenye vioo vyake akaipachika machoni kisha akajitupia kofia kubwa yeusi ‘pama’ na kuingia zake mjini, busy day, akawaza.
Jua lilikwishafika Maghalibi, wamachinga walikuwa wakifungafunga bidhaa zao katika mitaa mbalimbali ya Dodoma tayari kurudi kwa wapenzi wao. Obobo alkatisha mitaa miwili mitatu kuelekea hospitali ya mkoa wa Dodoma, nikimmaliza huyu, namsaka Segeratumbo kazi imeisha, akajiwazia wakati akilikaribia lango la hospitali.
***
“Da yule jamaa ana mwili wa chuma asee,” Kamanda akamwambia Gina pindi tu alipoingi ndani ya kile chumba na kukuta kipo vululu vululu.
“Mmepambana muda mrefu sana ee?” Gina akauliza wakati akimganga Amata jeraha lake la mguuni.
“Hapan kidogo tu, ila lo!”
“Nini?”
“Madam kasema nimhakikishe nampata akiwa hai, mtihani mkubwa sana huo!” akamwambia Gina na wakati huo simu yake mfukoni ikaita. Alipoitazama ilijiandika OK, akaiinua na kuiweka sikioni mara moja.
“Nimepata taarifa kuwa Kamati ya Usalama ya Bunge inanza uchunguzi dhidi ya upotevu wa zile nyaraka,” Madam S alizungumza kwa upole.
“Nakusoma bibi…”
“Na uchunguzi wao unataka kuanzi kwa yule msichana Cheupe, polisi wanataka kumkamata kwa mahojiano ya awali, lakini hawajui pa kumpata,” Madam akaendelea.
“Nakusoma bibi…”
“Nimepata taarifa hiyo name kuonesha kuwa sisi hatupo katika sakata hilo nimeruhusu waendelee, sasa tumia akili yako kabla hawajatuaharibia kazi yetu,”
“Message received, work in progress…” kamanda akajibu.
“Waitin for process,” Madam akamalizia na kukata simu. Amata akakurupuka kutoka pale alipo na kusimama wima, akamtazama Gina kisha akaliendea kabati na kutungua fulana moja maridadi, jeans na raba zake zisizofanya kelele kwenye sakafu, akavuta mkoba wake na kuufungua akachukua bastola moja ndogo ‘Beretta’ akaipachika kwenye kijikoti chake, kamba, visu vidogo vidogo vine na silaha nyingine alizoamini kuwa zitamsaidia katika hili au lile.
“Vipi Kamanda!” Gina akashangaa
“Kuna hatari kubwa inataka kutokea, lazima nikamwondoshe Cheupe pale hospitalini. Jeshi la polisi limeanza uchunguzi wa hili sakata la upotevu wa nyaraka, na wanataka kumsaka Cheupe kwa mohjiano sasa wakimpata watatuharibia kazi na ni vipi kama adui yangu naye kapata hiyo taarifa?”
“Ili kupoteza ushahidi lazima atamuua Cheupe,” Gina akajibu.
“Basi kama ni hivo, twende tulkauwahi uhai wake,” kamanda alimwambia Gina na wakati huo alikuwa keishaukaribia mlango, Gina akawahi kutoka nay eye akaufunga nyuma yake. Walipofika kaunta akalielekea dirisha mpaka alipokaa mhudumu wa mapokezi.
“Samahani dada, kuna uharibifu umetokea kule chumbani, naomba utume timu yako ikathaminishe ili nilipe kabla sijaondoka,” alipomaliza tu kusema akaondoka zake lakini hatua tano mbele akasimama kama sekunde tatu hivi akarudi tena pale dirishani. Yule mwanadada mhudumu wa mapokezi akasimama kumsubiri kujua nini tena. Amata alifika dirishani na kutazama dhabibu zilizokuwa kwenye bakuli kubwa, akacukua moja na kutia kinywani kisha akaondoka zake.
Iliwachukua dakika kama tano hivi kufika katika hospitali hiyo, Gina alijifanya kuzubaa nje na Amata akaingia moja kwa moja mpaka kwa yule muuguzi aliyemwachia kazi.
Kashinde alikuwa ameketi katika kijiofisi kidogo akisoma gazeti la siku hiyo, akashtuka aliposikia hodi na kisha mlango ukasukumwa.
“Oh, umenishtua kaka!” akasema huku akinyanyuka.
“Vipi mgonjwa wetu?” akauliza Amata.
“Anaendelea poa, unataka kumwona?”
“Sio kumwona tu, nahitaji kumwondoa hapa haraka,” Kamanda akamjibu Kashinde huku tayari akiongoza njia kuelekea kwenye kile chumba walichomhifadhi.
“Hakuna aliyekuja kukusumbua?” akauliza.
“Wapo. Sema niliwakatalia ka ulivyonieleza,”
“Good!”
Amata alipoukaribia mlango wa kile chumba, akasita kidogo, akasimama.
“Vipi?” Kashinde akauliza.
Amata hakujibu badala yake, taratibu, akamsukuma nyuma Kashinde na kumpa ishara ya kurudi alikotoka huku mkono mmoja ukiwa tayari na bastola nje na ule wa pili ukarudi kuchukua kile kifaa cha kuzuia sauti na kukizungusha pale kwenye domo la bastola. Taratibu akauendea mlango wa kile chumba na kushika kitasa chake, alipojaribu kukikunja ili afungue, hakikukunjika.
“Mh!” akaguna na kujaribu tena, hakikutikisika kabisa, akarudi nyuma hatua tatu na kupiga kwa mguu wake mmoja ule mlango ukavunjika eneo la kitasa na kufunguka huku ukisukuma kiti kilichowekwa kukinga mlango huo usifunguliwe. Cheupe hakuwepo kitandani, kitanda kilikuwa tupu na mashuka yalikuwa yamesukwasukwa kando. Akanyata kwa mwendo wa paka awindaye panya. Matone manne ya damu katika shuka nyeupe za MSD yaliusisimua mwili wa Amata, alipotupa jicho mita mbili hivi ng’ambo alimuona Cheupe kalala kimya, huku linga ikiwa imemwangukia juu yake.
“Cheupe!” akaita na kumuwahi pale chini alipomgeuza, Cheupe alikuwa akiangalia tu bila kufumba macho huku kifuni mwake kukiwa na matundu mawili ya risasi. Amata aliinua shingo na kuangalia dirisha ndipo alipogundua kuwa limevunjwa kioo chake.
“Kashindeeeee!” akaita na sekunde hiyohiyo Kashinde alifika na wauguzi wengine, Amata alimwacha chini Cheupe na kuwahi dirishani, alilichungulia kushoto na kulia na kuona mtu akiishia kwenye kona.
“Shiiiiiit!” akang’aka na kuchumpa kwenye lile dirisha akatua chini na kuruka sarakasi iliyomsidia kukoswa na risasi tatu kutoka kwa Obobo, aliyejibana kwenye kona ya ukuta. Akakamata saa yake na kuizungusha mara mbili kisha akaiminya kitufe cha kati upande wa pembeni.
***
“Piiiiiip! Piiiip!” saa ya Gina ilitoa huo mlio huku ikimfinya mkono wake akajua kuna hatari, akajitoa pale getini alipokuwa akiongea na mlinzi na kuingia upande wa jengo la huduma ya dharura, akapitiliza na kutokea upande wa pili, ndipo alipomwona Amata akijiinua kwenye mchanga, alipogeuka upande wa pili alimwona yule mwanababa aliyevaa kofia kubwa jeusi.
“Freeeze!” alimpigia kelele huku tayari akiitoa bastola yake na kumfyatulia lakini hakuweza kumpata. Amata aliinuka na kuanza kumtimua kwa mbio za mchangani bila kelele ila bastola yake ilining’inia mkononi.
Obobo aliruka wigo wa michongoma kama anayeruka msingi wa nyumba na kutua upande wa pili, na wakati huohuo kamanda Amata aliruka sarakasi maridadi na kuupita wigo ule akatua upande wa pili na hapo alimshuhudia adui yake akiinua bastola kumlenga, akachumpa upande mwingine na zile risasi zikachimba kwenye mnazi. Obobo akaondoka eneo hilo kwa mbio, na Amata akainuka na kuanza kumtimua upya kabisa. Hatua kama mia moja hivi Obobo akasimama baada ya kukutana na ukuta mkubwa unaotenganisha nyumba za shirika la nyumba la taifa na zile za shirika la leri.
Amata hakujiuliza mara mbili, aliruka hewani na kutanguliza miguu yote miwili iliyoenda kutua kifuani kwa Obobo na kumpepesua mpaka chini. Obobo hakuchelewa akajiinua pamoja na kuwa na mwili mkubwa, akasimama wima na kutupa konde zito lililompata Amata sawia, naye akapoteza stamina na alipotaka kujiweka sawa aliuona mguu wa adui yake ukidhamiri kumchota kwa ngwara, akauwahi na kuruka juu ule mguu ukapita peke yake, alipotua chini akajiruvyema na goti lake kulikuja likatua katika kidefu cha Obobo. Akajaribu kujitutumua yule mjinga akakuta network inakata, akasimama kimapigano na kuweka mikono yake kwa mtindo wa mauaji. Amata naye akajiweka sawa, mapigo ya karate yasiyopungua ishirini na nne yalivurumishwa na Obobo, lakini mpaka pigo la mwisho lilimkuta Amata alkiwa kayakinga yote, na mgongo wake ulikuwa umetuna na mikono ikiwa imeweka alama ya x mbele ya kifua chake. Obobo alipojaribu tena, alijikuta akichezea karate tatu za kifua na mbili zikatua usoni, kisha ngwala maridadi ikaichota miguu yake usawa wa magoti akajikuta anashuka na kupiga magoti udongoni. Amata alirusha teke akidhamiria kukiuka maagizo ya boss wake. Adui yake akawa makini kwa kuudaka ule mguu na kuuzungusha kwa nguvu, maumivu makali yalipita kwenye mifupa ya Amata, akawahi kujigeuza na kumfumua teke la upande wa pili shavuni na kuufanya mguu wake kuwa huru lakini alianguka vibaya.\
Obobo alivuta hatua mbila na kukanyaga ukuta wa nyumba kisha akajibenjua na kutua nje ya ule wigo, hakuchelewa mojamojakavuka majumba ya shirika la reli na kuliwahi treni lililokuwa likitoka stesheni kuelekea Singida kwa kuwa pale lilikuwa halina kasi akalidandia na kutokomea nalo.
Gina aliwasili eneo la mapambano wakati Obobo akipotelea, Lijaribu kufyatua risasi lakini ziliuchimba ukuta na kumkosa mshenzi yule padogo sana.
“Mtoto wa Malaya wewe!” akatukana huku akiukamata ule ukuta na kujivuta juu, akamshuhudia Obobo akidandia treni na kutokomea.
Kamanda Amata alishuhudia ufunguo ukitoka katika mfuko wa suruali ya Obobo na kudondoka chini, hivyo alipoanguka alitambaa na kuuchukua akautia mfukoni.
“Pole Kamanda,”
“Usihofu!”
“Tax, mzee Tax!” kijana mmoja alimwambia Amata. Alipoinua sura yake akatabasamu kwa kumwona Scoba keishafika eneo lile, akaingia kwenye hiyo tax na wote wakaondoka eneo lile.
“Pole sana comrade,” Scoba alimwambia Kamanda Amata huku akichukua barabara ya kwenda Dar es salaam.
“Masikini Cheupe!” Amata alisikitika huku akiukunjakunja mguu wake.
‘Isanga Inn 17’ ule ufunguo ulikuwa umeandikwa hivyo kwa maandishi ya kuchoma kwenye kijiplastiki kidogo.
“Scoba, geuza gari,” Amata akatoa amri.
“Uelekeo wapi kamanda?” akauliza Scoba huku tayari akiwa amekwishawasha indiketa ya kushoto na kuiacha hiyo barabara ya Dar es salaam na kupita ofisi za CDA kama anakuja, Nyerere Square.
“Isanga, twende Isanga,” akamwambia Scoba naye bila ajaizi alitekeleza.

ISANGA INN
“Simama hapa!” akamwambia Scoba naye akaegesha gari kama mita mia moja kutoka katika hiyo hoteli, “Nipe dakika kumi na tano hivi, Gina linda mkia wangu,” akatoka na kuondoka. Sekunde ishirini zilimfikia Kamanda Amata kwenye sebule kubwa sana iliyo na viti vichache tu na watu wachache walikuwa wameketi wakijisomea magazeti. Hakuongea na mtu alipita kwenye ujia mrefu huku akisoma namba za vyumba hivyo.
“Kumi na saba!” akauona mlango na kuusoma kwa sauti ndogo. Akapachika ufunguo na kuuzungusha ukafungua, akasukuma mlango taratibu na kujikaribisha ndani kama kwake. Kitanda kikubwa kilionekana kama kimelaliwa muda si mrefu, vitu vilikuwa vimewekwa ovyo ovyo tu. Katika meza moja kulikuwa na mafaili kadhaa yamewekwa hapo, akaiendea na kuyapekua pekua hakuna lile analolitaka.
“Kayaweka wapi mshenzi huyu?” akajiuliza kwa sauti ndogo tu huku akiinua hapa na pale, “Sio kesi!” akasema na kuingiza mkono katika mfuko wa siri wa jaketi lake, akachomoa kitu kama kiberiti hivi, akakipachika chini ya meza kisha taratibu akajivuta kwenye kabati na kuangalia, hakuna jipya.
Akachomoa ile bastola ya kizamani ya Obobo aliyoiacha kule chumbani mwake, akaiweka mezani na risasi zake akazipanga pamoja nayo.
“Hii ni salamu yako, ukiiona ujue mwisho wako u karibu,” akajisemea kwa sauti kama anayeongea na mtu kaisha akaufungua mlango na kuondoka zake akiuacha ufunguo kwa ndani.
§§§§
Kamanda Amata alijiinamia, uso wake ulionesha huzuni hisiyojificha kwa kifo cha Cheupe, bado nilikuwa namhitaji kwa upelelezi, yule hayawani kamkatisha maisha, nitamtia mkononi, safari hii hatoweza kuniponyoka. Nimefanya makosa mara mbili lakini sio mara ya tatu, akawaza huku bado akiwa kajiinamia. Mkono laini ukamgusa begani.
“Kamanda!” Gina akaita kwa sauti ya upole.
Kamanda akageuka taratibu na kumtazama mrembo huyo.
“Basi ameshakufa,” Gina akamweleza huku akimvuta mkono na kumwingiza kwenye gari ambapo Scoba aliiondosha moja kwa moja mpaka katika ofisi yao ya siri ambayo Madam S alikuwa akiwasubiri.
“Karibuni!” akawakaribisha, nao wakaketi vitini lakini Amata bado alikuwa akisikitika sana, “Pole Amata najua lililotokea kule hospitali lakini ndiyo hivyo katuwahi, vipi umepata lolote?”
“Hapana, Madam, yule mshenzi sijui hata kaficha wapi zile faili, nimefika mpaka chumbani kwake sijaziona, lakini nipe saa moja au mbili nitajua kila kitu,” Amata akaeleza.
“Chiba alikuwa anajaribu kuyanasa mazungumzo yake lakini imekuwa ngumu sana, inaonekana jamaa anajua nini anatakiwa kufanya,” Madam alieleza.
“Usiwe na hofu, atakamatika tu, hawezi kuponyoka nchi hii. Lakini huyu bwana hawezi kuja kufanya kazi hii bila kuletwa na mtu, ina maana nyuma yake kuna watu waliomtuma, akina nani?” Amata akaonesha wazi dukuduku lake.
“Ndiyo na sasa nataka uchunguzi ufanyike ndani ya waheshimiwa wenyewe ili tujue kama kuna aliyemkodi huyu jamaa…”
“Siyo ‘kama kuna alaiyemkodi’, nani aliyemkodi, huyo ndiyo ni wa kushughulikia,” Amata almkatiza Madam S na kubadilisha kile alichokuwa akiongea. Mipango na mazungumzo ilifanyika na mitego yote ya kumnasa Obobo ilifanyika. Baada ya kikao hicho cha siri Amata aliondoka akiapa kwa Madam S kuwa siku hiyo hatolala mpaka aujue mwisho.
 
SEHEMU YA TISA
OBOBO ALIINGIA taratibu ndani ya chumba chake, akasimama mlangoni na kukiangalia kwa makini, moyo wake ulipiga chogo chemba baada ya kuiona ile bastola yake a,iyoipoteza kimakosa pale Kenya Lodge. Hakuamini anachokiona, alitazama huku na huku akachomoa bastola yake na kuiweka sawia kiganjani mwake, akapita kona hii na ile akiangalia hapa na pale akidhani labda adui yake yupo ndani. Alipohakikisha hayupo kila kona akaiendea ile bastola, hakuigusa kwanza. Mshenzi huyu alikuja hapa, na kama alikuja keshanijua nilipo, sasa ni kubadilisha mbinu, akajisemea kisha akachukua simu yake na kupiga namba namba Fulani.
“Yes, zile faili bila shaka umezipata…” akaongea na mtu wa pili kwa lugha ya kiingereza.
“Ndio, umefanya kazi nzuri, lakini bado mmoja anazo naye tunazihitaji pia,” ile sauti ikaeleza.
“Sawa, hiyo utaipata usiku huu kwa maana nikikamilisha tu sina budi kuondoka haraka kwani hapa si mahala pazuri kwa sasa,” Obobo akazungumza.
“Ndiyo, ukizipata hizo, nitahakikisha usafiri wako wa kuelekea Dar upo tayari ili kukuondosha hapa na malipo yako utayapata usiku huu huu…”
“Ok! Call you later,” Obobo akakata simu na kukusanya kiilicho chake akatia kwenye begi lake dogo la mgongoni tayari kwa kuondoka. Akafikiria mara mbili tatu akajua akienda kurudisha chumba itakuwa rahisi kwake kujulikana kuwa kaondoka, alichofanya ni kuhesabu pesa za malipo, akaziweka mezani na kuzikandamiza na jagi la maua kisha taratibu akatoka na kupitia mlango wa nyuma na kupotelea mitaani mpaka barabara kubwa na kukodi tax.
“Wapi mzee?” Dreva akauliza
“Uwanja wa ndege!” akajibu, “Ninawahi ndege lakini nikiikosa utanirudisha huku,” akaongeza kusema.
“Sawa hakuna tabu ni elfu kumi tu,” yule dereva alimweleza Obobo naye akampatia noti hiyo, safari ikaendelea mpaka eneo hilo la Uwanja wa ndege/ lengo kubwa la Obobo halikuwa ni kusafiri kama alivyomwambia huyo kijana ila alitaka kufika kukamilisha kazi yake kwa Mheshimiwa Segeratumbo. Akatoa waleti yake kubwa na kuchomoa noti ya shilingi elfu kumi na kumpatia kisha akachikua pakiti la sigara na kuiweka kinywani.
“Una kiberiti?” akamwuliza yule dereva. Naye badala ya kujibu akampatia, Obobo akawasha ile sigara, akavuta pafu moja kubwa na moshi wake kumpulizia usoni yule dereva.
Kizunguzungu cha ghafla kikamvaa yule dereva, akajikuta akiona watu watatuwatatu, mara akahisi kichwa kizito, “umenifanya nini we-we?” akajitahidi kumuuliza Obobo lakini alihisi mtu huyo anazidi kuwa mbali naye, akainua mikono na kujaribu kushika hapa na pale, akajiegemeza kitini na kukufunikwa na kiza kinene. Obobo akateremka na kuzunguka upande wa dereva, akafungua mlango huo na kufyatua kile kiti kikalala kisha akaufunga na kuufungua wa nyuma upande uleule na kumvuta yule dereva mpaka nyuma akamkalisha kitini na kumfunga mkanda kisha akampachika kofia kichwani. Ilikuwa rahisi kwa yeyote anayemwona kujua kuwa mtu huyo yupo kwenye usingizi. Obobo akakamata usukani na kutoka eneo hilo taratibu, akauacha uwanja wa ndege na kuifuata ile hoteli aliyofikia Segeratumbo.
Kabla hajafika maegeshoni, alimwona mheshimiwa huyo akitoka ndani huku wasaidizi wa hoteli hiyo wakiweka mabegi yake mheshimiwa garini. Anaondoka! Akawaza Obobo huku moyoni mwake akiona kuwa mara hii kazi itakuwa ndogo kwani ni kufanya tu kama alivyofanya kwa Msesema. Akasimamisha gari yake na kuendele kumtazama dereva wa Segeratumbo akipanga mabegi ya bosi wake garini na baada ya dakika kumi ile Toyota Prado iliondoka taratibu na kuiacha hoteli hiyo. Obobo aliifuata nyuma kwa umbali kama wa mita mia moja hivi huku kichwani mwake akipiga hesabu za jinsi ya kuupata mkoba wenye nyaraka au kujua nyaraka hizo zilizobaki ziko wapi.
§§§§

Saa kumi na mbili za jioni, Kamanda Amata aliwasili Isanga Inn, kwa kutumia mlango wa nyuma aliingia bila kugundulika na kukifikia chumba cha Obobo, akachomoa bastola yake ndogo na kuiweka sawia kiganjani, akatikisa mlango, uko wazi. Akausukuma taratibu huku kichwani mwake akiwaza kufanyiwa kama kile alichomfanyia adui yake pale Kenya Lodge. Akausukuma mlango kwa nguvu kisha akaruka na kutua mwisho wa chumba, peupe! Hakuna mtu. Kamanda Amata akatahayari, kaondoka? Akajiuliza. Alipotupa jicho mezani, hakuiona ile bastola.
“Shiiit!” Akang’aka na moja kwa moja akaliendea kabati, hakuna kitu, bafuni, hakuna kitu. Akaiendea ile meza na kupapasa mkono wake kwa chini akatoa kile kidubwasha alichokibandika kwa ajili ya kunasa mazungumzo yoyote yatakayoendelea mle ndani. Akakitoa na kukizima kisha akaminya kinobu cha ‘scan’ wakati huo akiwa kapachika vifaa vya kusikilizia.
Kwanza akasikia mlango kuguliwa na kufungwa, ukapita ukimya kisha akasikia mlio wa simu na kusikiliza mazungumzo yale. Kamanda Amata alisikia sauti ya Obobo tu na ile ya pili hakuweza kuisikia. Akakiweka mfukoni kile kidubwasha na kutoka mle chumbani, akatoka kwa mlango ule alioingilia na kuzunguka mbele ya hoteli hiyo akaingia na kufika kaunta, pale akaulizia kama mwenyeji wake yupo, akaambiwa yupo ndani tangu afike hajatoka. Amata akajua kuwa kwa vyovyote Obobo katoroka bila kuaga, kwa maana hata zile pesa amezikuta pale mezani kama zilivyo.
“Mpigieni simu mwambieni kuna mgeni wake hapa kaunta,” akawaambia na mmoja wale wahudumu akachukua simu na kupiga ile namba ya chumba, simu ikaita na kuita haikupokelewa.
“Mh! Haipokelewi labda katoka,”
“Basi nitakuja baadae!” akaaga na kuondoka huku kichwani akijua wazi kuwa Obobo amewacheza shere pale hotelini. Moja kwa moja alifikia katika ofisi yao ya siri na kukutana na Madam S, akampa kile kidubwasha naye akakipachika kwenye ile mashine yake ambayo iliweza kusafirisha sauti hiyo mpaka kwenye mtambo wao kule shamba Dar es salaam ambako Chiba alikuwa huko akifuatili mambo mbalimbali ya kazi zao.
Madam S alikuwa akirudia kusikiliza hiyo kauli ya Obobo
“Yes, zile faili bila shaka umezipata…”
“Kuna mtu tayari anazo hizo faili,” Madam akamwambia Amata.
“Ndiyo!”
“Sawa, hiyo utaipata usiku huu kwa maana nikikamilisha tu sina budi kuondoka haraka kwani hapa si mahala pazuri kwa sasa,”
“Hapa atakuwa anazungumzia nini? Nini hiyo ambayo ataipata?” Madam alihoji.
“Mh!”
“Sawa, hiyo utaipata usiku huu…”
“Sawa, hiyo utaipata usiku huu…”
“Ina maana atampatia usiku huu?” madam akauliza.
“Nini?” Amata akauliza.
“ Labda faili lingine…” Madam akaotea.
“Enheee uko sawa madam, kwani mpaka sasa nani na nani wameripoti kuibiwa faili hizo?” Amata akauliza kwa shauku.
“Katibu wa Bunge na Mheshimiwa Kibanio…” Madam akajibu huku akitikisa kichwa juu chini, “na Segeratumbo naye analo faili linguine japo hajaripoti kama limeibwa au lipo…”
“Sasa hilo ndo litakuwa la tatu ambalo huyu hayawani anataka kulikabidhi usiku huu kwa mteja wake…” Amata akaeleza.
“You are so intelligence Amata!”
“Segeratumbo yuko hatarini, anaishi hoteli gani? Kama una dodoso yoyote,” Amata akamwambia Madam S huku akiiangalia bastola yake kama ipo sawa.
“Niliuliza, wanasema amefikia Air port Resort,”
“Sawa, niko njiani…”
“Ok! Call you later,”
Madam S alisikiliza sentensi hiyo ya mwisho ya Obobo kwa mteja wake.
“Atampigia tena baadae, nafikiri sasa muda huo ni wa kukabidhiana faili hilo,” akamalizia kusema.
“Sasa tunafanyeje, tusubiri tuwakamate hapo wote wawili au mi niende hukohuko Airport Resort?” Amata akahoji.
“Huwezi kujua ujanja wa adui yetu, nenda mi nitakujulisha lolote lile. Gina na Scoba wako patrol, wewe nenda huko na Chiba kule Dar yupo kwenye Cyber Patrol, nina uhakika usiku huu kila siri itadhihirika lakini kumbuka siri sirini,” Madam S akamwambia Amata.
“Yes Mom!” akajibu na kuondoka.
Ngrrrrrrrrrrrrrrr! Ngrrrrrrrrrrrrr! Simu ya mkononi ya Madam S ikaunguruma pale mezani sekunde chache tu baada ya Amata kuondoka, alipotazama kwenye kioo ilisoma ‘TSA 2’ Chiba! Akawaza na kubofya kile kidubwasha cha kijani.
“Mheshimiwa Matata!” Chiba alitamka hilo jina tu na Madam S akaonekana kupigwa bumbuwazi.
“Mheshimiwa Matata? Acha masikhara Chiba, umejuaje?” akauliza.
“Mimi ndio Chiba wa Chiba, nimesikiliza sana hiyo sauti mliyoituma na kabla yake kulikuwa na mlio wa batani za simu iliyokuwa inabonyezwa kuoiga namba hiyo. Kumbuka mpigaji hakuzima button click, na kila button ina mlio tofauti na nyingine, nimeisoma hiyo milio nikaitafsiri kwenye tarakimu ni 0986 777123, nimeipekuwa kwenye mtambo wangu hapa imenipa jina hilo,” Chiba alieleza kitaalam kidogo.
“Ok, Chiba sasa fanya hivi, hakikisha unakamata mawasiliano yake kutoka sasa tunavyoongea na nyuma kidogo ili tuwanase wote usiku huu ikiwezekana,” Madam alieleza.
“Copy and clear!” Chiba akajibu na kukata ile simu.
Shiit! Yaani Mheshimiwa Matata yumo kwenye sakata hili, siamini. Anadiriki kufanya haya, basi hakuna wa kumwamini duniani, Madam akawaza na kujitupa kitini.
§§§§
Kamanda Amata aliegesha gari yake katika maegesho ya hoteli hiyo, na moja kwa moja akaiendea kaunta na kumkuta mhudumu akiwa ametingwa na kuhudumia wateja jioni hiyo.
“Samahani, Mheshimiwa Segeratumbo, mwambie kuna mgeni wake hapa!” Amata akamweleza yule mhudumu lakini akakutana na macho ya mshangao kwa mbali.
“Una miadi naye?”
“Hapana, ila nina shida naye kiofisi,”
“Mheshimiwa amekwishaondoka kama saa moja nyuma hivi,” yule mhudumu akamweleza Amata.
“Aaah! Ameondoka yaani yupo hapa Dodoma au…”
“Kasafiri karudi Dar na chumba keisharudisha,”
“Ok!”
Amata akarudi garini huku kichwa kikimzunguka, akainua simu na kumpigia Madam S.
“Mheshimiwa ameondoka kwenda dar leo!” akamwambia.
“Sawa, njoo hapa haraka kuna habari nyeti sana juu ya hili,” Madam akamwambia Amata kisha simu ikakatika.
Dakika tano zilizofuata Amata alikuwa tayari akipanda ngazi za nyumba hiyo.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom