Makapuku Forum

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amewapa muda wa mwezi mmoja Viongozi wa Mikoa na Halmashauri wawe wamekutana na wafanyabiashara wadogo maarufu kama Wamachinga na kupanga namna bora ya usimamizi wa shughuli za biashara ikiwemo kutenga maeneo ya kufanyia biashara zao.

Hatua hiyo ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa jana wakati akizindua mpango wa uelimishaji na uhamasishaji wa sensa ya watu na makazi wa 2022, ambapo aliwataka Wakuu wa Mikoa wawe makini katika zoezi la kuwapanga Wamachinga nchini na kuepuka vurugu, fujo na uonevu.

Ametoa kauli hiyo leo, Septemba 15, 2021 wakati akizungumza kwa njia ya video na Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu wa Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Waziri wa Viwanda na Biashara, Wakuu wa Mikoa, Wilaya na Uongozi wa Wamachinga.

Waziri Mkuu amewaelekeza viongozi wa Halmashauri za Majiji, Manispaa, Miji na wilaya waone namna ya kutumia baadhi ya barabara za katikati ya majiji na miji kufungwa muda wa alasiri ili kuruhusu Wamachinga kufanya biashara zao katika barabara hizo———“Hii ni fursa nzuri kwa wajasiriamali wetu kufanya shughuli zao”
 
Waziri wa TAMISEMI, Ummy Mwalimu ametoa maelekezo kwa kila Halmashauri nchini kuhakikisha wanawachukulia hatua Watumishi wasiotekeleza majukumu yao na wale wanaojihusisha na vitendo vya ubadhilifu wa fedha.

“Tusipochukua hatua kukomesha ubadhilifu fedha za Halmashauri kila siku zitakuwa zinapigwa na Mimi niwaaambie fedha za Halmashauri zinapigwa sana lazima tuchukue hatua na kuongeza usimamizi”————Ummy

Ummy pia amepiga marufuku Wakurugenzi kuwatumia Walimu kukaimu nafasi za utendaji wa mitaa na kata kutokana na uhaba uliopo, kwani kuna upungufu wa walimu hapa nchini hivyo walimu wanatakiwa kuachwa wafanye kazi yao ya kufundisha.

Amesema hayo mjini Kibaha wakati akiongea na Sekretarieti ya Mkoa wa Pwani, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi, na Makatibu Tawala ambapo pia ameupongeza uongozi wa mkoa kwa kukusanya mapato ya ndani kwa asilimia 99 kwa mwaka wa fedha uliopita.
 
Mkuu wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, (RPC) Ramadhan Kingai amekana kumtesa mshitakiwa Adam Kusekwa kabla na baada ya kuandika maelezo yake ya onyo kama upande wa utetezi unavyodai.

Kingai ameeleza hayo katika Mahakama Kuu Kitengo cha Makosa ya Uhujumu uchumi mbele ya Jaji Mustafa Siyani, wakati wa usikilizwaji wa kesi ndogo ndani ya kesi ya msingi wakipinga kupokelewa kwa maelezo ya onyo ya mshitakiwa huyo.

Hatua hiyo imekuja baada ya Upande wa Utetezi ukiongozwa na Wakili Peter Kibatala kupinga mahakama isipokee maelezo ya onyo ya mshtakiwa wa pili ambayo yalipaswa kutolewa mahakamani hapo kama kielelezo na shahidi wa kwanza wa upande wa mashtaka ambaye ni Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Kinondoni, RPC Ramadhani Kingai.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi kesho Septemba 16, 2021 ambapo Kingai ataendelea kutoa ushahidi akiwa ni shahidi wa 7 katika kesi ndogo baada ya ile ya msingi kusimama.
 
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefanikiwa kupata mkopo nafuu kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa( IMF) wenye thamani ya shilingi trilion 1.3 kwa ajili ya kukabiliana na athari za Covid- 19 katika Sekta ya Uchumi na Kijamii.

Akizungumza Dodoma leo, Waziri wa Fedha na Mipango Dr. Mwigulu Nchemba amesema kuwa fedha hizo zitatumika katika Sekta ziliozoathiriwa na Covid-19 ikiwemo Sekta ya Utalii, Elimu, Afya, Maji pamoja na kusaidia kaya maskini kupitia TASAF.
 
Mwili wa aliyekuwa Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi Simba SC, Zacharia Hans Poppe umezikwa leo nyumbani kwao Kihesa Mkimbizi Mkoani Iringa.
 
Mkuu wa Wilaya ya Morogoro Albert Msando amesema anakatwa Tsh.Milioni 2.8 kila mwezi kutoka kwenye mshahara wake wa Tsh. Milioni 3.1 kama rejesho baada ya kukopa Benki kiasi cha Tsh. Milion 106 ili kutengeneza vibanda vya Wamachinga zaidi ya 700.

Hatua hiyo imekuja baada ya Machinga kutaka kujenga vibanda ila hawakuwa na pesa na walipotaka kukopa Benki ili wajenge wakakosa sifa, ndipo DC Msando akaamua akope yeye ili awajengee mabanda Wamachinga hao.

“Nilikaa na Wamachinga wakaniambia Mmachinga akiingia hapa na deni la Laki 2 la kulipia banda hatochomoka maana hata mtaji wa kuuza hana, Benki wakasema wazo la kwanza lilikuwa kujenga banda ambalo Wamachinga watakopea hilo banda litatumika kama dhamana, nikasema Mmachinga kukopeshwa hela hamtompa kwasabbau hana historia ya kibenki , nikawaza tufanyaje na nataka mabanda yakamilike maana yapo nusu, nikaamua kukopa”

“Nilisema Rais aliona inampendeza kuniteua kuwa DC ili niwatumikie Wananchi nikaiomba Benki naomba nikope wengi waliona ni mwehu wengine wananicheka hadi leo kwamba ‘umekopa sababu ya machinga!?’ nikasema ndio”

“Nikasema badala ya kuchukua pesa kwenda kumpa Mke wangu na Watoto wangu au kupanua biashara zangu, Mimi nitachukua pesa nitamalizia mabanda ili Wamachinga wafanye biashara zao”———Msando
 
Korea Kaskazini leo imefyetua makombora mawili yaliyoelekezwa Baharini ikiwa zimepita siku mbili tangu Serikali ya Korea Kaskazini ilipodai kwamba imefanya majaribo ya makombora mapya ya masafa marefu.

Taarifa iliyotolewa na Jeshi la Nchi jirani ya Korea Kusini, imesema makombora hayo mawili yalifyetuliwa kutoka katikati mwa Korea Kaskazini na kuelekezwa kwenye Bahari ya Mashariki inayofahamika pia kama Bahari ya Japan.

Korea Kusini imesema inashirikiana na mamlaka za ujasusi za Marekani kukusanya taarifa za kina kuhusu majaribio hayo ya silaha na kwamba Jeshi lake lipo kwenye hali ya tahadhari.

Majaribio ya leo ambayo Korea Kaskazini imeyataja kuwa ya "kimkakati" ni ya kwanza kufanywa katika muda wa miezi sita na huenda yatachochea mvutano mpya kwenye rasi ya Korea.

Chini ya maazimio ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Korea Kaskazini inazuiwa kuunda au kufanya majaribio ya makombora ya masafa marefu lakini mara kadhaa Taifa hilo limepuuza marufuku hiyo.
 
“Leo hii Wanawake mmempa Tuzo Rais wenu, Rais Mwanamke kwa bashasha na furaha kubwa lakini nataka niwaambie Wanawake bado hatujaweka Rais Mwanamke, tulichokichangia sisi ni ile kusukuma mpaka Mwanamke akawa Makamu wa Rais, lakini kufika hapa kama isingekuwa kudra ya Mungu ingekuwa ngumu sana”

“Sasa Ndugu zangu Rais Mwanamke tutamuweka Mwaka 2025, Wanawake Oyeee, Tanzania Oyee, Ndugu zangu Mwaka 2025 tukifanya vitu vyetu vizuri, tukishikamana, tukimuweka Rais wetu tutakutana hapa kwa furaha kubwa sana, wameanza kutuchokoza, kuandika kwenye vigazeti ‘Samia hatosimama (kugombea Urais)’ nani kawaambia!?”

“Fadhila za Mungu zikija mikonononi mwako usiziachie, hizi ni fadhila za Mungu, Wanawake tumefanya kazi kubwa kuleta uhuru wa Nchi hizi, kujenga siasa za Nchi hizi, tumebeba sana Wanaume katika siasa ya Nchi hizi, leo Mungu ametupa baraka mikononi tukiiachia Mungu atatulaani”———Rais Samia Suluhu Hassan akiongea leo Dar es salaam kwenye maadhimisho ya siku ya Demokrasia duniani.
 
 
Serikali imesaini mkataba wa ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Msalato Dodoma kwa gharama ya shilingi takribani Bilioni 165.

Ujenzi huo utafanywa kwa ushirikiano wa kampuni tatu kutoka China ambazo ni Sinohydro Coorporation limited, M/s Beijing Sino-Aero Construction Engineering Co. limited pamoja na M/s China Jiangxi International Economic and Technical Cooperation Co. Ltd ambapo unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi 36 kutoka sasa.

Akishuhudia utiaji saini huo, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, amewataka Wakandarasi hao kutekeleza mradi huo kwa viwango vilivyokubaliwa kimkataba na kwa kuzingatia muda ili kuwezesha malengo ya Serikali ya kuifanya Dodoma kuwa Mji Mkuu wa Serikali kufikiwa.
 
Askari wa Vikosi Maalumu vya Wanamaji wa Tanzania na Askari wa Vikosi Maalumu vya Jeshi la Marekani waliohitimu mafunzo ya pamoja ya wiki 6, taarifa ya Ubalozi wa Marekani Tanzania imesema na zina historia ndefu ya ushirikiano wa kijeshi na kushukuru jitihada za Tanzania katika kulinda usalama na amani katika kanda.
 
Zimbabwe imewapiga marufuku kwenda Maofisini Watumishi wa Umma ambao hawajachanja chanjo ya Covid 19.

Waziri wa Habari, Monica Mutsvangwa amesema Baraza la Mawaziri la Nchi hiyo limekubaliana kuwa Wafanyakazi waliochanja pekee ndio wanaruhusiwa kuripoti makazini.

Katika siku zijazo wamepanga kuwa Watu waliochanja pekee ndio wataruhusiwa kuhudhuria kwenye nyumba za Ibada na kwenye Migahawa ya chakula.

Hadi kufikia September 13,2021 Watu Mil 1.9 walikuwa wamechanjwa Zimbabwe, Nchi hiyo ina mpango wa kuwachanja angalau Watu Milioni 10 ili kupunguza maambukizi.
 
Wakati Wasanii wa Tanzania wakisubiria kuanza kulipwa kutokana na kazi zao kutumika sehemu mbalimbali ikiwemo kwenye TV, Radio na maeneo mengine yanayotumia muziki kuanzia December 2021, Afisa TEHAMA wa COSOTA amesema mgao wa pesa Wasanii watapata 70% na Serikali ni 30%.

"Mgao wa pesa ni kwamba Msanii atapata asilimia 70 na COSOTA inapata asilimia thelathini, tutapokua tunakusanya hizi pesa hazitokuwa zinakwenda kwenye masurufu mengine Serikalini ndio maana imekua 70% tunawapa wao na 30% tunatumia sisi kwa matumizi ya kuturahisishia kufikia maeneo mbalimbali kuwakusanyia wao pesa wanayotakiwa kuipata"

“COSOTA tumeandaa mfumo utarahisisha sana zoezi la ukusanyaji mirabaha kwani Msanii atakua na uwezo wa kupata mirabaha yake kwa namna pana zaidi kwasababu Halmashauri zinazokata leseni za biashara zitakuwa na uwezo wa kuwaomba Wafanyabiashara pia kuingia kwenye website na kulipia leseni za biashara zao na kulipia leseni za matumizi ya kazi za muziki moja kwa moja kwenye madawati yao na hawatokua na ulazima wa kuja COSOTA”

"Wataingia kwenye www.hakimiliki.co.tz wataweka taarifa zao za biashara na kupata control number na kulipia leseni yake ya matumizi ya kazi za muziki, tumefanya kikao na kuwaelimisha Maafisa Utamaduni na Maafisa Biashara ili wawape elimu hiyo Wafanyabiashara ili kuondoa usumbufu na mlolongo usiohitajika" ——— asema Afisa TEHAMA Mwandamizi COSOTA Segenge James.
 
Waziri Mkuu wa Haiti Ariel Henry amefukuza kazi Mwendesha Mashtaka aliyekuwa anataka kumfungulia mashtaka kama Mshukiwa katika mauaji ya Rais Jovenel Moise, kitendo hiki kimeiingiza Haiti katika mzozo mpya wa kisiasa.

Wiki iliyopita Mwendesha mashtaka huyo alisema rekodi za simu zinaonyesha kwamba Mtu anayeshukiwa kuwa mpangaji mkuu wa mauaji ya Rais Moise aliwasiliana na Waziri Mkuu Henry usiku ambao uhalifu huo ulifanyika ambapo walizungumza mara mbili kwa kipindi cha dakika saba.

Mshukiwa huyo Joseph Baido ambaye alikuwa Afisa kwenye Wizara ya sheria na ambaye Henry amekuwa akimtetea, anadaiwa kutoroka na hajulikani alipo kwa sasa.

Waziri wa sheria wa Haiti Rockfeller Vincent mwanzoni mwa wiki hii aliiagiza Polisi wa Haiti kumuongezea ulinzi Claude kwasababu alikuwa amepokea vitisho kwa kipindi cha siku tano, vitisho hivyo havijaishia kwake tu bali hata kwa Makarani wa Mahakama wanaripotiwa kwenda mafichoni baada ya kupokea vitisho vya kuuwawa iwapo hawatobadilisha baadhi ya majina na taarifa katika ripoti zao.
 
Polisi Mkoani Manyara wanamshikilia Mwanamke mmoja baada ya kufanya kitendo cha kikatili kwa Mtoto wake wa kumzaa kwa kumchoma kwa moto chanzo kikiwa ni Mtoto huyo kuomba pesa kwa wapita njia.

RPC Mwakyoma wa Manyara amesema "Ilikua Babati Mjini Mtaa wa Mlala Juu Mtoto aitwae Neema Vicent wa miaka mitatu na miezi kumi na moja alichomwa moto na Mama yake sehemu mbalimbali mdomoni, shingoni na usoni, Mama yake aitwae Janeth Vicent alikasirishwa na kitendo cha Mtoto kuomba pesa kwa Wapita njia karibu na kwao"

"Wasamaria wema waliripoti kitendo hicho Polisi na Mama yake akakamatwa, Mtoto alifikishwa Hospitalini na kulazwa, Mama anashikiliwa na Polisi kwa mahojiano zaidi, nitoe wito tusikimbilie kuadhibu Watoto, tukimbilie sana kuelimisha Watoto na kuwajengea Watoto tabia njema" ——— RPC Mwakyoma.
 
Makamu wa Rais wa Tanzania, Dk Philip Mpango leo Jumatano Septemba 15, 2021 amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu , Kassim Majaliwa.

Mazungumzo hayo yamefanyika Ofisini kwa Makamu wa Rais Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma.
 
Kuelekea SIMBADAY Klabu ya Simba imetoa kiasi cha Shilingi Milioni 10,000,000/= kwa hospital ya Rufaa ya Mkoa, Mwananyamala ikiwa ni kurudisha kwa jamii katika Wiki ya Simba.

CEO wa Simba amekabidhi mfano wa hundi ya Shilingi Milioni 10, 000,000/= kwa ajili ya kusaidia wodi ya kinamama na watoto kwenye Hospitali ya Mwananyamala.
 
Tuanzebe Aikataa Man U
.
Beki wa Manchester United Axel Tuanzebe, 23 anayecheza kwa mkopo Aston Villa amewaomba mabosi wa Man United kumruhu kusaini mkataba wa kudumu ili kuendelea kusalia kwenye viunga hivyo kwa muda mrefu.
.
Tuanzebe hakuwa anapata nafasi ya kucheza kwenye kikosi cha kwanza cha Man United tofauti na ilivyo kwa Villa na anaonekana ni mmoja ya wachezaji tegemeo wa kikosi cha kwanza.
 

Similar Discussions

Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…