Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania,, Samia Suluhu Hassan na Rais wa Jamhuri ya Uganda Yoweri Kaguta Museveni leo April, 11, 2021 wameshuhudia utiaji saini wa mikataba ya utekelezaji wa bomba mafuta ghafi la Afrika Mashariki ( East Africa Crude Oil Pipeline- EACOP) kati ya Serikali na Kampuni za Uwekezaji uliofanyika katika Ikulu ya Entebbe nchini Uganda
Hafla ya utiaji saini mikataba ya mradi huo imehudhuriwa na Mawaziri na wawakilishi wa kampuni hizo za uwekezaji ambazo ni Total ya nchini Ufaransa na CNOCC ya China.
Marais wameshuhudia utiaji saini wa mkataba wa kwanza ambao ni wa uenyeji wa mradi kati ya Serikali ya Uganda na wawekezaji (Total na CNOCC), mkataba wa pili wa ubia ambapo Serikali za Tanzania na Uganda zimetiliana saini na kampuni hizo (Total na CNOCC) na mkataba wa tatu wa masuala ya kikodi na usafirishaji ambapo Serikali ya Uganda imetiliana saini na kampuni hizo (Total na CNOCC).
Pamoja na kushuhudia utiaji saini wa mikataba hiyo, Marais pia wametia saini tamko la pamoja kuhusiana na utekelezaji wa mradi huo na wameagiza vipengere vilivyobaki katika utekelezaji wa mradi huo vikamilishwe haraka
Mradi huo utahusisha ujenzi wa bomba la mafuta lenye kutumia teknolojia ya joto (heated oil pipeline) lenye urefu wa kilometa 1,445 ambapo kati yake kilometa 1,115 zinapita Tanzania, uwekezaji katika mradi huu unatarajiwa kugharimu Dola za Kimarekani Bilioni 3.5, utazalisha ajira takribani 10,000 wakati wa ujenzi na utasafirisha mapipa Bilioni 6.5 ya mafuta yaliyogundulika katika Bonde la Ziwa Albert nchini Uganda kwenda Bandari ya Tanga nchini Tanzania.